Search This Blog

UNA NINI LAKINI MELISSA - 5

 

    Simulizi : Una Nini Lakini Melissa

    Sehemu Ya Tano (5)





    Baada ya hapo sauti ya dada haikusikika tena bali mtoto akiwa analia tu. Darren akaendelea kumbembeleza mwanaye akimsihi anyamaze kwani usiku umekuwa mkubwa na yeye amechoka sana. Kwa kama lisaa limoja, mtoto akaendelea kulia tu, akipunguza sauti na kurudi tena upya.



    Darren akachoka sana kumbembeleza, mikono ikawa inamuuma, macho yanamsaliti kwa kuwa mazito, kichwa nacho kinachoshwa na sauti kali ya mtoto.



    Mlango ukagongwa tena.



    “Nani?” akauliza kwa sauti ya uchovu.



    “Dada wa kazi!” sauti ikamjibu toka mlangoni.



    “Unataka nini?”



    “Mtoto ana shida gani?”



    “Amekurupuka tu toka usingizini, usijali. Unaweza kulala.”



    “Naweza kukusaidia?”



    “Hapana! Usijali, nitambembeleza mwenyewe mpaka alale.”



    Basi baada ya hapo sauti ya dada wa kazi haikusikika tena, Darren akaendelea kumbembeleza mtoto. Kwa kama nusu saa akawa anafanya zoezi hilohilo tu. Kila alipojaribu kumweka mtoto kitandani ambembelezee hapo, ikawa tabu zaidi, mtoto aliongeza kilio.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hakujua sasa cha kufanya. Kila mtindo alitumia lakini haikusaidia. Ilifikia kipindi akawa anapitiwa na usingizi ingali amesimama. Alimweka mtoto kitandani kwa kulazimisha akaendelea kumbembeleza hapohapo, kidogo akapitiwa na usingizi.



    Kama baada ya dakika mbili akakurupushwa na hodi ya tatu mlangoni mwake. Akauliza, “Nani?”



    “Dada wa kazi!”



    “Unataka nini?”



    “Mtoto anasumbuliwa na nini?” dada akauliza.



    “Si nilishakwambia!” Darren akafoka kidogo.



    “Naomba nimbembeleze,” sauti ya dada ikaomba.



    “Nimesema nambembeleza mwenyewe. Hukunielewa?”



    Kukawa kimya kidogo.



    Punde sauti ya dada ikasema tokea mlangoni, “Utanipa nimbembeleze ama nije nimchukue mwenyewe?” mara hii sauti ilikuwa na amri ndani yake.

    .



    Darren akajawa na hofu. Akamnyakua upesi mtoto wake na kumfichama kwenye mikono yake akiwa anatazama mlango kwa hofu. Punde mlango ukaanza kubamizwa kwa nguvu na kwanguvu! Darren akajaribu kuteka simu yake atoe taarifa polisi lakini hakuiona. Kwa muda alikuwa kama mtu aliyechanganyikiwa. Hakujua cha kufanya.



    Mlango ukaendelea kubamizwa na kubamizwa. Mwishowe ukaanza kudhoofu na kubomoka. Vipande vyake viliruka huku na huko. Ilikuwa ni ajabu mbomoaji alikuwa anatumia nyenzo gani kufanyia zoezi lake hilo.



    Darren alichofanya ni kutwaa kipande kidogo cha mbao ya mlango na kubebelea kama silaha. Ni ajabu kama mtu ameweza kubomoa mlango atamzuiaje kwa kipande cha mbao, lakini alikuwa na imani.



    Mkono wake uliobebelea kipande hicho cha mbao ulikuwa unatetemeka. Macho yamemtoka na paji lake la uso linatiririsha jasho.



    “Ni nani wewe?” Darren akauliza kwa sauti yenye kusita. Hakujibiwa. Kilichokuwa kinafanyika ni mlango kubamizwa tu! Tena kubamizwa kwanguvu mno.



    Kidogo, kwasababu ya hofu na kukurupushwa usingizini, mtoto naye akaanza kulia. Alikuwa analia kwanguvu haswa kiasi cha kumchanganya Darren. Ingawa Darren alimsihi anyamaze, haikusaidia kitu.



    Mwisho wa siku mlango wote ukawa upo chini na mlangoni akiwa amesimama mwaname anayechuruza damu mikononi. Mwanamke huyo si mwingine bali dada wa kazi. Mikono yake ilikuwa imejeruhiwa vibaya mno kwa kubamiza mlango hata kuvunjika. Macho yake yalikuwa makubwa yanayong’aa, uso wake umepauka kuwa mweupe.



    Alimtazama Darren kisha akainamisha shingo yake kwenda kushoto na kulia, kisha kulia na kushoto. Akamnyooshea kidole Darren pasipo kusema jambo. Alafu kama mtu aliyegandishwa na barafu, akaanza kupiga hatua kumwendea Darren.



    Darren akamtisha na kipande chake cha mbao, “Kaa mbali!” akafoka. “Kaa mbali na mimi!” lakini mwanamke yule hakuwa anasikia wala kujali, akaendelea kusonga kumfuata Darren, na alipomkaribia akanyoosha mikono yake yote miwili na kisha akasimama.



    Kukawa kimya kidogo. Darren akamtazama mwanamke huyo kwa hofu na maulizo. Naye mwanamke huyo akawa anamtazama Darren kwa macho ya kumpembua. Kidogo akashusha macho yake kwa mtoto na kumtazama kwa sekunde kadhaa, alafu akasema kwa sauti ya kukoroma, sauti ya chini, “namtaka huyo mtoto.” alafu akahema kwanguvu na kusema kwa sauti ya hewa, “Nipatie, nami nitaenda nisirudi nyuma!”



    “Wewe ni nani?” Darren akauliza akiwa anamshikilia vema mwanaye. Alikuwa amejiminyia kwenye kona akitamani kutoboa ukuta atokee nje.



    Yule kiumbe akamtazama Darren alafu akapindishia shingo yake kushoto. Aliporejesha shingo yake kulia, akasema, “Mimi Melissa.”



    “Melissa!” Darren akastaajabu. Hakujua alipata wapi nguvu ila alijikuta akisimama huku akitusi na kulaani. “nimekwambia kaa mbali na mimi Melissa!” punde akazabwa kofi lililomtupia ukutani yeye na mwanaye. Kwa muda kidogo akashindwa kuelewa kinachoendelea. Kwa mbali alisikia sauti ya mwanae ikilia sana lakini hakuwa anaweza kufanya kitu.



    Kama baada ya dakika tano, akiwa ameanza kupata nguvu, akasikia sauti yaita,



    “Hey! Helloooow!” kidogo mwanga ukatua kwenye macho yake yalofumba, akayafinya na kuyafumbua akiwa anajikinga na mkono wake wa kuume.



    “Upo sawa?” alisikia sauti inauliza. Kidogo akabaini sauti hiyo inatokea dirishani. Walikuwa ni majirani, wanaume wawili. Mmoja alikuwa amebebelea bunduki kubwa na mwingine amebebelea gongo kubwa na kurunzi. Walikuwa wamesikia zile kelele na walikuja kutazama jirani yao amepatwa na nini.



    Kabla Darren hajajibu kitu, alitazama kwanza kando yake kumtafuta mwanaye. Akamwona akiwa amelala kama hatua tatu tokea alipo. Alikuwa kwenye ukimya wa mbao. Na dada wa kazi alikuwa amelala kwa pembeni yake naye akiwa kimya.



    Upesi akamfuata mwanaye na kumtazama. Hakuwa na dalili ya uhai. Alimwita na kumwita lakini ikiwa bure, mtoto hakuitika kwa kucheka wala kulia. Darren akapatwa na hofu kubwa sana ya kumpoteza mwanaye. Alimtikisatikisa aone kama ataamka lakini napo haikusaidia. Mtoto alikuwa amenyamaza. Alikuwa amenyazama milele.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Darren akapiga magoti na kugugumia kwa kilio. Alipata hasira sana. Alinyanyuka kama mbogo akamwendea dada wake wa kazi na kumvuta kwanguvu akimuuliza amemfanya nini mtoto wake, lakini dada naye alikuwa kimya. Hakuweza kuongea wala kujitetea kwa njia yoyote ile.



    Darren asijali, akaanza kumuadhibu dada huyo kwa kumkandika mateke. “Shetani! Shetani! Shetani mkubwa wewe! Nitakuua!”



    Kama si majirani kuvunja mlango na kuja kumshika, sijui hatma ilikuwa ni nini. Waligundua dada wa kazi alikuwa yu mzima, ila kama mtu aliyekuwa kwenye ‘coma’, hali mfu ya kupoteza fahamu, ila mtoto alikuwa amekwishafariki.



    Basi dada wa kazi akawahishwa hospitali kwa matibabu zaidi. Mtoto naye akapelekwa huko kuhifadhiwa kwa ajili ya mazishi, na Darren pia, kwakuwa alihisiwa anaweza akawa si mzima, naye akapelekwa hospitali.





    **



    Baada ya juma moja …



    Darren alikuwa ameketi kwenye kingo ya bahari. Alikuwa amevalia bukta na miguu yake ikiwa tupu pasi na viatu.



    Upepo ukimpuliza taratibu, alikuwa anatazama bahari kwa umakini. Kuna kitu alikuwa anawaza kichwani ingawa macho yake yalikuwa yanatazama mawimbi ya bahari. Mkono wake wa kuume ulikuwa umebebelea mchanga, ila akiwa ameuminya kana kwamba anataka kuukosesha hewa.



    Macho yake mekundu yalitazama mbali na karibu ya bahari. Yalitazama kushoto na kisha kulia ya bahari alafu akashusha pumzi ndefu. Akanyanyuka na kuanza kurandaranda.



    Alitembea akiwa anawaza na kuwazua kichwani mwake. Kila alipofunga macho alimwona mwanae, alimwona mkewe. Ilikuwa ni ajabu na ghafla kwake. Kuna muda hakuwa anaamini kama Josephine hakuwapo naye, wala mtoto wao. Ilikuwa inamuwia ugumu sana kuamini kuwa yu mwenyewe hatimaye.



    Alihisi maisha yake yanaparanganyika kama kioo kilichobondwa na jabali. Alikuwa anahisi hana umuhimu wowote maishani hivi sasa. Alikuwa anajihisi mfu anayetembea.



    Alikunja ngumi yake akiendelea kutembea. Aling’ata meno yake na kutazama bahari tena, alafu punde akasema, “Melissa!” kwa sauti ya kufifia. Akarudia tena, “Melissa. Melissa. Melissa!” alafu akaapa, “Nitakumaliza kwa mkono wangu mwenyewe. Nitakumaliza Melissa!” alipomaliza kusema maneno hayo macho yake yakawa yanamwaga machozi. Alishindwa kujizuia kuumia. Moyo wake ulikuwa unavuja damu.



    Jua likiwa linaanza kuwa kali kumaliza asubuhi, Darren akajirejesha kwenye gari lake na kutimka kuelekea upande wa magharibi. Alitembea kwenye gari kwa takribani masaa matatu kabla ya kuja kukomea kwenye nyumba kubwa namba 4089 kibaoni. Nyumba ya mwanamke yule aliyemwona mtandaoni kwa swala la mtoto wake kuwa na chapa mwilini.



    Kabla hajashuka na kuzama humo, akalipekua kwanza jengo hilo kwa macho yake mepesi, kisha akashuka na kuliendea. Alipogonga kidogo akafunguliwa na mlinzi, akajitambulisha na mlinzi akamruhusu kuingia ndani maana alikuwa na miadi na mwenye nyumba.





    “Nilipata shida sana. Nilitafuta kila namna lakini haikusaidia. Na nakumbuka vema ikiwa ni usiku wa manane, nikampoteza mwanangu wa pekee!”



    Darren akataka kujua zaidi kumhusu mwanamke huyo. Mbali na mtoto je yeye alishawahi kukumbwa na kadhia yoyote ile? Basi mwanamke yule akaeleza kuwa kwa kitambo kifupi baada ya mama na baba yake kufariki, ndipo alipoanza kuona mambo fulani ya ajabu ndani ya mji wao. Mwanzoni alikuwa anadhani anawehuka na labda ana laana na ule mji, hivyo akafanya kuhama aende mbali.



    Alipoenda huko, akatuama na kuanzisha familia ambayo iliishi kwa amani mpaka pale mambo yalipokuja kuibukia katika namna ambayo hakuwa anaweza kuelewa vema.



    “Ninachokumbuka ni kwamba, baada ya tetemeko kubwa la ardhi lilitokea miaka mitano nyuma, maisha yangu yakaanza kubadilika kwa wepesi sana. Sikuwa tena mtu wa amani bali kuona vituko na viroja. Mtu wa kuona mambo ya ajabu yasiyokuwa na mithili. Ajabu ni kwamba, baada ya mtoto wangu kufariki, mambo hayo yalipotea mpaka sasa.”



    “Na vipi kuhusu mume wako?” Darren akadadisi. Charlie akatabasamu kwanza ila macho yake yakiwa kinyume. Alitazama chini kwa sekunde chache kabla hajabinua kinywa chake na kusema, “Alikuwa mwanaume niliyekuwa namhitaji. Mwenye kujali na kujua kupenda. Nilijihisi nimekamilika nilipokuwa naye. Alinifanya nisahau kifo cha wazazi wangu kwa muda kwani alikalia sehemu tupu ambayo iliachwa wazi.”



    Akadondosha chozi. Akalifuta kwa kidole chake onyeshi kabla hajaendelea kuongea, “nilimpoteza kwenye ajali!” akapandisha mabega yake akisema, “sijui nini kilitokea lakini aliacga daraja na kutumbukia baharini. Waokozi walipokuja kumtazama, hakuwa hai tena.”



    “Gari lake lilipata hitilafu?” Darren akauliza.



    “Sidhani,” Charlie akajibu. “Gari lake lilikuwa sawa kabisa isipokuwa tu sehemu ambayo iligonga daraja. Sijajua kumhusu yeye. Sijajua alikuwa kwenye hali gani. Ila kwa mujibu wa shuhuda wa tukio, mume wangu alibamiza kioo chake cha pembeni kwanguvu kabla gari halijapoteza mwelekeo na kudumbukia.”



    Kwa namna moja Darren akaona simulizi ya huyo mwanamke inawiana na ya kwake. Kwa kutaka kuhakikisha zaidi, akamuuliza Charlie, “Kuna mtu yeyote ambaye ulikuwa naye kwenye mahusiano kabla ya mumeo? Namaanisha mpenzi wako wa kwanza?”



    Charlie akafikiri kidogo kabla hajasema, “Niliwahi kuwa naye. Ila ni kipindi cha zamani za utotoni. Sichukulii mahusiano yale kama yalikuwa serious.”



    “Je haujawahi kumwona mwanaume huyo uliyewahi kuwa naye kwenye mahusiano? Yaani baada ya kuoana na mumeo? Au kipindi chochote kwa namna yoyote?”



    “Hapana,” Charlie akakataa. “Sijawahi kuonana naye tangu kipindi hicho.”



    Hapa kidogo Darren akajiona ni wa tofauti na Charlie. Mbona yeye anasumbuliwa na Melissa? Basi akaamua naye kumshirikisha Charlie kuhusu habari zake. Alipomaliza kumweleza kila kitu, Charlie akamuuliza Darren, “Unapajua anapokaa huyo Melissa?”



    “Ndio, napajua,” Charlie akajibu.



    “Naweza nikaonana naye?” Charlie akauliza akiwa ametoa macho kidogo.



    “Unahitaji kuonana naye?”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ndio, kama itawezekana.”



    Darren akanyamaza kidogo kisha akasema, “Si mtu mzuri kama unavyoweza kudhani.”



    “Najua,” Charlie akamkatiza. “Sitegemei awe mtu mzuri, ila ningependa kuonana naye.”



    “Kwanini? Huoni utakuwa umejiweka kwenye hatari?”



    “Hatari ipi, Darren? Nimepoteza mume na mtoto wangu, kuna hatari nyingine zaidi ya hiyo?”



    Kimya kidogo. Charlie akaendelea kuzungumza, “Nadhani kuna maswali yangu atakuwa na majibu nayo.”



    “Yapi hayo?”



    Hapa Charlie akamweleza Darren kuwa anahisi mama yake alikuwa ni mtu mwenye agano tokea nyuma. Mara kwa mara mama yake alikuwa anamwambia kuwa maisha yake hayatakuwa ya furaha kwakuwa yeye ni kizazi cha shetani. Damu yake inachembechembe za majini. Alipotaka kujua zaidi, mama yake hakumweleza kwa kumwambia muda bado mpaka pale utakapowadia na basi atajua.



    “Una picha ya mama yako?” Darren akauliza. Charlie akafungua simu yake na kumwonyesha Darren picha ya mama yake, “huyu hapa wa kwanza upande wa kulia.” darren alipotazama vema, akagundua sura ya mama huyo haikuwa ngeni. Ilikuwa ni sura anayoijua. Aliionea wapi? Akajiuliza akirusha macho huku na kule.



    “Vipi, Darren?” Charlie akamuuliza.



    “Nahisi namjua huyu mtu,” Darren akajibu akiendelea kufikiri na punde akakumbuka. Sura hiyo aliionea kwenye ile picha ambayo aliipata kwenye jengo la bibi yake! Akamweleza Charlie habari hiyo.



    “Kweli?” Charlie akastaajabu.



    “Ndio, ni kweli!” Darren akaapa. Basi Charlie akafikiria kwa udogo na kusema, “Darren, nadhani sasa utakuwa unaona kuna haja gani ya kuonana na Melissa. Yeye anaweza kutueleza mambo haya kwa undani.”



    Darren akashika kichwa, “Lakini Melissa si mtu mzuri hata kidogo. Ameyfanya maisha yangu yawe magumu kupita kiasi. Sikutaka kabisa kuhusiana naye.”



    Charlie akauweka mkono wake begani mwa Darren, “sikia, Darren. Hatuna machaguzi hapa. Na kati ya wewe na mimi, hakuna mwenye maelezo ya kumtosha mwenzake isipokuwa huyo Melissa. Hima twende tukamwone!”



    Darren akafikiri kidogo kabla hajanyanyuka na kumpakia Charlie kwenye gari yake, safari ikaanza. Walitembea kwa muda wa kama nusu saa pasipo kuzungumza. Charlie ndiye alikuja kuuvunja ukimya kwa kumuuliza Darren, “Ulimpenda Melissa?”



    Darren akanyamaza kwanza kama mtu anayepangilia jibu kichwani kisha akasema kwa ufupi, “Ndio.”



    “Na yeye alikupenda?” Charlie akauliza akimtazama Darren anayatazama mbele.



    “Sidhani,” Darren akajibu.



    “Haudhani?”



    “Ndio. Kama angekuwa ananipenda basi angeniweka bayana kila kitu,”



    “Kila kitu kama kipi Darren? Kuwa yeye ni jini aliyeishi na bibi zetu tuokea huko nyuma? … ungemwelewa? Ungeendelea kuwa naye?”



    “Charlie, sijui haya mambo yaendavyo. Ila nisingeweza kuishi na Melissa zaidi. Unawezaje kufanya hivyo punde unapohisi kuwa uliyenaye si binadamu?”



    Charlie akanyamaza asinene tena. Wakaumaliza huo mjadala. Kwenye majira ya saa tano za usiku wakawa wamewasili kwenye makazi ya Robson. Hapo waliposhuka, Charlie akauliza, “Hapa ndipo kwake?”



    “Hapana, bali kwa mpenzi wake! Nadhani atakuwapo hapa,” Darren akaji bu wakisonga.



    “Na vipi kama hatokuwapo?” Charlie akauliza.



    “Basi mpenzi wake atakuwa anajua alipo,” Darren akamalizia kauli na kubisha hodi mara tatu. Punde akafunguliwa na Robson ambaye alishangaa kumwona Darren hapo wakati huo.



    “Vipi, Darren?”



    “Naweza kuonana na Melissa?” Darren akaenda moja kwa moja kwenye lengo lililomleta.



    “Vipi, kuna tatizo?” Robson akauliza.



    “Ndio, lipo,” Darren akajibu na kisha akarudia tena kauli yake, “Naweza kuonana na Melissa?”



    Robson akawafungulia mlango wakaingia ndani. Ila walipoketi, simu ya Darren ikaingiwa na ujumbe. Alipoutazama kuusoma, ulikuwa unatokea kwa Melissa.



    “Sipo hapo. Nikuteni fukweni,” ujumbe ulisoma.



    Upesi Darren na Charlie wakaelekea huko ufukweni ambapo Melissa alikuwapo, na kweli wakamkuta akiwa ameketi mchangani akitazama maji ya bahari. Mbali na hivyo kulikuwa kimya sana isipokuwa upepo.



    Darren akamwita Melissa akiwa anamtazama, naye Melissa akamtazama na kumkaribisha, “Nadhani hapa ni eneo zuri la kufanyia maongezi.” Darren na Charlie wakaketi wakimweka Melissa katikati yao.



    “Ulimwambia Robson kama nipo huku?” Melissa akauliza.



    “Hapana, hajui hilo,” Darren akajibu kisha akamuuliza Melissa kama anamjua mwanamke yule aliyekuja naye, yaani Charlie. Pasi na kumtazama, Melissa akasema anamfahamu hata kabla hajaja hapo.



    Aliposema hayo akamtazama Darren. Macho yake yalikuwa tayari yameelekea kuwa mekundu. Akamshika mkono na kumuuliza kwa upole, “Darren, utasadiki nitakayokuambia?”



    Darren alipojibu swali hilo, Melissa akamuuliza na Charlie swali hilohilo. Alipolijbiwa ndipo akaanza kunena. Darren na Charlie wakawa wametega masikio yao vema kabisa. Japokuwa upepo ulikuwa unapuliza, bado sauti ya Melissa ilisikika vema.



    “Pengine mimi naweza nikawa mtu mbaya sana kwenye vichwa vyenu. Hamtaki kuniona na sifai kuwa hai wala kuwa mbele yenu hapa nilipo. Ila …” alipokomea hapo akamtazama Darren, “Kama si upendo wangu kwako, Darren. Basi usingalikuwa hai mpaka sasa. Haujui ni makovu mangapi umenisababishia kwa maneno yako lakini sikuwahi kuacha kukupenda.”



    Aliweka kituo na kutazama bahari kwa sekunde kama sita akiwa kimya. Kuna kitu alikuwa anawaza kichwani mwake. Na basi alipojiona yu tayari ndipo akaendelea kunena ya kuwa hapo zamani kabisa ya miaka takribani mia tatu iliyopita, walikuwa kwenye familia kubwa ya bwana Roddeth. Bwana huyo alikuwa ni mtu mwenye nguvu kubwa na mwenye kuhofiwa sana.



    Alikuwa na nguvu za ajabu. Watu wangekusanyika kwake awasaidie matatizo mbalimbali lakini kwa sharti la kutoa sadaka. Alikuwa si mtu wa kawaida bali jini, lakini alistahimili kuishi miongoni mwa binadamu. Na kwa uzao wake basi akapata watoto watano wa kike ambao kwa mujibu wa maelezo ya Melissa, mmoja wa hao watoto alikuwa ni yeye, na wengine ni pamoja na bibi yake Darren na Charlie na wengineo wawili.



    Walikuwa ni watu wapendanao mpaka pale siku moja baba yao alipokufa na kugawa mali zao pasi na usawa. Walichukiana na kila mmoja akaelekea upande wake. Lakini kwasababu Melissa alikuwa ni kipenzi kikubwa wa baba yao basi ingali baba yupo kwenye kitanda chake cha kifo alimkabidhi mwanaye huyo kito cha moja ya mkufu wake akimwambia, “Utaishi milele, mimi safari yangu naona ikomee hapa.”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Alificha kito hicho kwa namna zote ili ndugu zake wasije kukiona na kumpokonya. Na kwake haikuwa ngumu sana kwani walikuwa tayari wameshatengana na kila mmoja akaenda njia yake binafsi.



    Basi miaka ikapita kila mmoja akiwa na chuki na mwenzake na uadui pia. Kila mmoja akapata kuishi kwa namna ajuavyo huko mbali. Wengine wakafikia kuanzisha maisha kwa kuwa na mahusiano na binadamu.



    “Halikuwa jambo jema. Baba yetu wakati yu hai alikuwa akitusisitiza juu ya hilo. Endapo tutakapokuwa kwenye mahusiano na binadamu basi si kwamba tutawafanya watoto waingie kwenye damu yetu isiyo ya kawaida, bali damu hiyo itawawinda na kuwaangusha,” alisema Melissa.



    Lakini kwasababu za mapenzi, wenzao wawili walizaa na binadamu. Na kama ilivyokuwa neno la baba yao, watoto hao wakawa wanasumbuliwa kwa kutokewa na mambo ya ajabu wasiyoweza kuyaeleza. Mengine hata yakitishia uhai wao.



    Kutokana na hayo ndipo binadamu hao wakawa wanatafuta tiba ya kujikinga dhidi ya maajabu waliyokumbana nayo. Na kila tiba walipoipata wakaifungia kwenye vitabu walivyovihifadhi maeneo ya mbali kabisa na makazi yao. Maeneo salama ambayo hayafikiwi na binadamu.



    Vitabu hivyo vilikuwa ni vifungo vya kufunga yale yote yaliyokuwa yanawasumbua, na wakafanikiwa kufanya vivyo kwa muda.



    “Shida ni kwamba, vitabu hivyo vinakuwa si vifungo tu bali hubeba roho za wale vinavyowalinda. Hivyo pale vinapopata madhara, basi na wale waliokuwa wanavimiliki hufa kwa aina hiyohiyo ya kifo,” maneno hayo ya Melissa ndiyo yakamkumbusha Darren kifo cha mama yake kilivyorandana na moto wa msitu. Akamuuliza naye Charlie akasema kuwa mama yake alikufa kwa kuzama maji ingali alikuwa chumbani mwake! Ikiwa ni muda mfupi baada ya tetemeko la ardhi kutokea.



    “Baada ya hapo basi ndipo matatizo yenu yakaanza upya,” Melissa akaendelea soga, “Kwakuwa vifungo vilikuwa vimeenda basi ndiyo maana mambo ya ajabu yakaanza kuwatokea upya kwenye familia zenu, na itakuwa vivyo mpaka pale damu mliyobeba itakapotulizwa.”



    Darren akamuuliza Melissa, “Mbona maisha yangu yalikuwa yametulia kabla ya kuja kukutana na wewe? Mbona kila mara ninapoonana na wewe huwa nakutana na jambo baya?”



    Melissa akamtazama Darren akiwa anadondosha chozi, “Darren kamwe hautokuja kuelewa ni mangapi nilikuwa nayapitia kwasababu yako. Maisha yako kutuama kabla ya kuja kukutana na mimi haikuwa inamaanisha kuwa utakuwa sawa, lah! Na hilo halikuwa kwako peke yako bali pia kwa Charlie.



    Mambo yalianza kubadilika si kwasababu ulikutana na mimi bali kwasababu ulikuwa umepata mtoto. Kama vilevile ilivyokuwa kwa Charlie. Mlikuwa mmefufua upya agano lenu, Darren,” Melissa alisema kwa sauti ya chini alafu akatazama chini kabla hajaendelea kunena, “Kila ulipokuwa unakutana na baya lolote, nami nilikuwapo pembeni, na ndiyo maana ulikuwa unatoka ama kushinda hai. Isingalikuwa hivyo, ungeshakufa muda mrefu Darren.”



    “Na vipi kuhusu ile siku nilipoenda kwenye ile nyumba iliyotangazwa kwenye gazeti? Ilikuwa ni kweli ama ndoto kukuona pembeni ya gari yangu?” Darren akauliza. Melissa, bado akiwa anamtazama mwanaume huyo, akamjibu, “Yote yalikuwa ni uhalisia, Darren. Na ni mimi ndiye nilikurudisha pale kwenye gari lako upesi baada ya kuzidiwa na wale wadhalimu. Lakini uliponiona pembeni yako haukunipa muda nikajitetea, bali ukanijaza shutma na kunifukuza!”



    “Kwanini hukuniambia yote hayo, Melissa?” Darren akauliza.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kwasababu haukunipa muda huo Darren. Maisha yako yote umekuwa ukinichukulia kama adui yako. Mtu ninayekusababishia mabaya na nuksi,” Melissa akieleza hayo machozi yakamtiririka zaidi. Na Charlie akagundua kuwa mwanamke huyo alikuwa akimomonyoka miguu yake kuwa udongo.



    Akamshtua Darren atazame. Darren akapayuka kuuliza, “Melissa, nini kinatokea?” akiwa amemshika mkono mwanamke huyo. Melissa akatazama miguu yake inayomomonyoka na kisha akamtazama Darren na kusema, “Hii ndiyo gharama yangu kwa kusema haya. Yanipasa niende Darren. Maisha yangu yamekwisha hapa duniani.”



    “Hapana Melissa, si una kito cha kuishi milele?” Darren akauliza.



    “Sina kitu chochote Darren,” Melissa akasema akilaza kichwa chake kifuani mwa Darren, “Yote nimeyatoa kwa ndugu zangu kama sadaka ya kukubakiza wewe hai.” kisha akamtazama Darren na kumwambia, “lakini haikusaidia na wamenigeuka. Wanataka maisha yako, wanataka maisha yenu. Wanataka kila ambacho bibi yako alikuwa anamiliki. Siwezi kuwazuia tena, Darren. Sina nguvu hiyo.”



    Melissa alipomaliza kauli hiyo, mwili wake ukawa umeshapukutika mpaka kufikia tumboni. Mwili uwake ulikuwa kichuguu cha mchanga. Akamwaga Darren, “Kwaheri, mpenzi”



    “Melissa!” Darren akaita akimshika Melissa vema. “Usiondoke, Melissa! Tutawezaje kupambana wenyewe? Tafadhali usituache!” Lakini tayari sasa mwili wa Melissa ulikuwa umepukutika zaidi mpaka kifuani. Maneno pekee ambayo aliyasema kabla hajamalizika kabisa ni haya,



    “Kuna kitu kwenye jeneza la bibi yako,” alipotaka kunena zaidi, kichwa chake kikamomonyoka na hatimaye akawa mchanga kabisa. Darren na Charlie wasiamini macho yao wakautazama mchanga ule wa bahari.



    “Amejitoa sadaka kwa ajili yetu,” akasema Charlie akimtazama Darren kisha akauliza, “sasa tunafanyaje?” Darren alipohakikisha kuwa kweli Melissa ameenda, akamwambia Charlie waende kule kwa bibi yake. Lakini muda ulikuwa umeenda sana.



    “Vipi tukadamka asubuhi?” Charlie akapendekeza.



    “Hapana,” Darren akatikisa kichwa. “Huoni ni hatari zaidi tukiendelea kungoja?” kweli Charlie akaafiki, lakini sasa wangefanyaje na muda ulikuwa umewatupa mkono?



    Wakiwa wanafikiri namna ya kufanya, simu ya Darren ikaita, alikuwa ni Isabel. Alipokea na kumjulia hali mwanamke huyo.



    “Upo wapi, Darren?” Isabel akauliza. Darren akamtazama Charlie na kujibu, “Nipo mbali.”



    “Wapi? Tafadhali waweza kuniambia?” Isabel akasisitiza, lakini kabla Darren hajajibu akamtazama kwanza Charlie, mwanamke huyo akamtikisia kichwa. Darren akakata simu.



    “Darren, usimwamini mtu yeyote kwa sasa hivi,” Charlie akamwambia akiwa amemkazia macho.



    “Kwanini? Huyu nafahamiana na--”



    “Hapana!”



    Punde simu ikaita tena, Darren akamtazama Charlie. Ajabu mwanamke huyo akampoka simu hiyo na kisha akaikata na kuizima. “Tuondoke, Darren!”



    Basi upesi wakalifuata gari lao na kujikwea. Charlie akamwambia Darren waelekee kwake alafu ndiyo waende huko waendako, Darren akatii. Walipofika kwa Charlie wakapakia silaha kadhaa ndani ya gari, Charlie akabeba na pesa, wakaanza safari ya kwenda kwenye nyumba ya marehemu bibi yake Darren.



    Wakatembea kwa muda mrefu sana mpaka pale ambapo usiku sasa ukawa mkubwa. Wakiwa kwenye majira ya saa tano usiku, wamebakiza kama kilomita ishirini kuwasili wanapoelekea, Charlie akahisi kuna gari linawafuatilia. Alimshtua Darren na kumtaka aongeze mwendokasi.



    Darren alipojaribu kutazama kwa kutumia vioo akaliona gari hilo wanalolishukia. Halikuwa ngeni machoni mwake. Alipoenda mbele zaidi na kulitazama vema, akagundua kitu,



    “Isabel!” alijikuta akinena mwenyewe.



    “Unamaanisha yule mwanamke?” Charlie akauliza. “Yule aliyekuwa anakupigia simu?”



    “Ndio!” Darren akajibu. “Ndiye yeye!”



    Charlie akatazama nyuma kuliangazia gari hilo. Lilikuwa linakuja kwa kasi. Alihofia sana.



    “Darren, sasa tunafanya nini?”



    “Sijui!” Darren akatikisa kichwa akiwa ametoa macho kukodolea kioo cha juu ya kichwa chake. Alikanyaga pedeli ya mafuta zaidi, gari likakimbia. Punde lile gari linalowafuata likatokomea wasijue limeenda wapi!



    “Unaliona?” Darren akamuuliza Charlie.



    “Hapana, silioni!” Charlie akajibu akiwa anaendelea kukagua. Kwa muda kidogo akaendelea kutazama asilione tena gari lile linalowafukuza, basi wakaendelea na safari yao mpaka waelekeapo. Walipofika wakajitua toka kwenye gari na kabla hawajaenda mbali sana, wakatupa macho yao kukagua.



    Ilikuwa ni nyumba iliyomezwa na kiza. Kulikuwa kimya sana. Kwa namna moja ama nyingine kulikuwa kunatisha.



    Wakiwa wanaendelea kutazama, Charlie akagundua kitu. Akamwita Darren na kumuuliza, “Nini kile? Ni gari ama macho yangu?” Darren alipotazama akaona gari kwa mbali upande wao wa kulia. Gari hilo lilikuwa limeegeshwa kwa ukimya. Lilikuwa ni lile gari waliloliacha barabarani. Gari ambalo Darren hudhania ni la Isabel.



    “Umeliona likiingia muda huu?” Darren akauliza.



    “Hapana,” Charlie akajibu na kuongezea, “Nimeliona likiwa tayari limeegeshwa.” kisha akauliza, “atakuwa amefika kabla yetu?”



    Darren hakuwa na majibu, upesi akamwamuru Charlie wachukue kila kinachohitajika kwenye gari na waelekee eneo la kaburi upesi. Walipofanya hivyo, mara gari lile likawasha taa zote kwa pamoja, pap! likawamulika na kuwaumiza macho!



    Upesi wakakimbia kule kaburini na kuanza kuchimba kwa maelezo ya Darren. Wakiwa wanaendelea kuchimba, Charlie akamwona mtu kwa mbali akija kwenye mwelekeo wao. Hakuweza kumwona vema maana alikuwa yu mbali, kitu pekee alichoweza kubaini ni kuwa mtu huyo ni mwanamke kutokana na umbo lake na mwendo pia.



    Mikono yake iliyokuwa tupu ilikuwa ikienda mbele na kurudi nyuma sababu ya mwendo.



    “Chimba, Charlie! Chimba!” Darren akabweka. Wakafukua kana kwamba sungura udongoni na mtu yule alipokaribia, Darren akamsihi Charlie aendelee na zoezi ilhali yeye akamkabili mtu huyo anayekuja.



    “Darren, una uhakika?” Charlie akauliza kwa mashaka.



    “Usijali, endelea,” Darren akasema akitoka shimoni na kupiga hatua kadhaa kusonga mbele. Alipomfikia mtu yule ndipo akabaini kweli alikuwa ni Isabel.



    “Isabel,” Darren akaita na kuuliza, “Ni nini unataka hapa?”



    Isabel akatabasamu na kuuliza, “Darren mbona haupokei simu yangu?” kabla Darren hajajibu, akauliza tena, “Kwani kuna tatizo lolote baina yetu?”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Darren akamtazama kwanza Isabel kwa namna ya kumtilia mashaka. Alikuwa anahisi kuna kitu hakipo sawa.



    “Isabel, unataka nini hapa?”



    Isabel akatazama nyumba kubwa iliyokuwa kando yao, “Ni nyumba kubwa. Nimeipenda sana Darren. Vipi ile ofa yangu, waweza kuniuzia?”



    “Siuzi tena!” Darren akajibu.



    “Kwanini? Auhitaji pesa tena?”



    “Sihitaji pesa zako, Isabel.”



    Isabel akamtazama Darren na kumsogelea karibu zaidi.



    “Tangu lini umeanza kukataa pesa zangu, Darren?”



    “Kuanzia leo. Sihitaji tena. Na pia sihitaji kukuona pia!”



    Isabel akakunja shingo yake kutazama kule shimoni. “Naona umepata mwanamke mpya.”



    “Hayakuhusu, Isabel. Hicho ndicho kimekuleta?”



    “Hapana, Darren,” Isabel akajibu akiweka mkono wake begani mwa Darren. “Kilichonileta hapa ni kuchukua kilicho changu tu.”



    “Kipi chako hapa?” Darren akauliza.



    “Vyote unavyoviona hapa,” Isabel akajibu na kuongezea, “Vyote ni urithi wangu. Na kwakuwa haukutaka niuchukue kwa amani, basi nitatumia nguvu!”



    “Ebu tumia nione!” Darren akasema akimkazia Isabel macho.



    “Una uhakika?” Isabel akauliza akipandisha nyusi yake moja. Punde Darren akaanza kuhisi maumivu makali ya kichwa.



    “Darren nisingependa nitumie nguvu dhidi yako. Nitakumaliza. Kwahiyo kwa kunusuru maisha yako, songa kando nifanye kilichonileta.”



    Japo Darren alikuwa anasikia maumivu makali bado hakuwa radhi kumruhusu Isabel atende kile alichokuwa amekusudia. Basi akamvamia akimtupia maneno makali lakini alichoambulia hakikuwa kinasimulika vema. Alitupiwa mbali tena kwa mkono mmoja tu. Akaangukia tumbo na kulalama kwa maumivu makali!



    Isabel akapiga hatua nzito kumfuata Charlie. Alipomfikia akanyoosha mkono wake kumnyaka mwanamke huyo, ila upesi Charlie akatumia kifaa alichokuwa anachimbia kumwadhibia Isabel! Alimchana na kumvujisha damu!



    Isabel akautazama mkono wake unaovuja damu kisha akakunja ndita akimtazama Charlie. “Umekwisha!” akafoka na kujitupia ndani ya shimo. Charlie alipotaka kumwadhibu tena Isabel, nyenzo yake ikadakwa na mkono wa Isabel wenye nguvu.



    “Kamwe usijaribu!”



    Isabel akampokonya Charlie dhana hiyo na kisha akataka kumbamiza nayo kichwa. Kheri kabla hajatimiza adhma yake hiyo, nyenzo ikadakwa na mtu nyuma. Isabel alipogeuka kutazama, alikuwa ni Darren. Na kabla hajafanya jambo, mwanaume huyo akamwadhibu kwa kumzamishia ncha za reki usoni mwake! Kilikuwa ni kitendo cha kinyama ambacho Darren amewahi kufanya tangu azaliwe.



    Hata wakati Isabel anaanguka chini, Darreb alikuwa ameachana asiamini kama amelitenda hilo. Basi upesi, wakishirikiana, wakamtoa Isabel ndani ya shimo na Darren akamburuza kwa hatua kadhaa mbali na shimo kisha wakaendelea kuchimba kaburi.



    Walipofanya hivyo kwa takribani dakika sita, mara Isabel akanyanyuka akiwa na reki lake usoni. Si Darren wala Charlie aliyemwona. Mwanamke huyo akachomoa reki usoni na kulitupia kando. Alikuwa anachuruza damu lakini hakuwa anajali. Upande wake wa kushoto ulikuwa umefunikwa na damu inayotiririka kama bomba.



    Alipotupia reki kando ndipo Darren na Charlie wakasikia na kuhisi. Darren alipotazama na kubaini hilo akahofia sana. Hata Charlie vilevile. Ni mtu wa aina gani angenyanyuka baada ya kadhia ile? Lakini kwa ujasiri Darren akatoka ndani ya shimo baada ya kumwambia Charlie aendelee kufukua.



    “Darren!” Charlie akaita kwa hofu. Aliogopa. Aliona Darren angeenda kufa. Lakini Darren asijali akajiendea kifua mbele. Alipomfikia Isabel akasema, “Nitakuua!” naye Isabel akamwambia, “Karibu tena!” kisha akamnyaka shingo yake kwa nguvu na kumnyanyua juu juu!



    “Ndiyo kwanza tupo kwenye moja, Darren. Unadhani binadamu kama wewe anaweza kuniua?” Darren akarusharusha miguu akijitahisi kujinasua toka kwenye mikono ya Isabel. Hakika asingeweza kwani mikono ya mwanamke huyo ilikuwa imeshiba nguvu haswa. Ilikuwa inaminya uhai toka kwenye mwili wa Darren.



    Darren akapapatika sana pasipo mafanikio. Akarusha na mateke ambayo mengine yalikwenda hewa na mengine kumkita Isabel lakini haikusaidia, mwanamke huyo alikuwa mithili ya gogo kavu!



    Basi Darren aliyekuwa anaelekea kufa alipoona amefanya kila jambo pasipo mafanikio na sasa anaelekea kufa, akamtazama Isabela akilenga kumtusi ama kumlaani. Ni kheri katika hilo akabaini jeraha alilokuwa nalo Isabel mkononi, lile jeraha ambalo Charlie alimsababishia. Basi kama simba aliye na njaa, Darren akadaka kwa mikono yote jeraha hilo na kuliparua sana. Isabel akashindwa kuvumilia na hatimaye akamwachia Darren aliyejidondokea chini akikohoa.



    Darren alikuwa anahisi kifua kinambana, shingo nayo imeziba. Alikuwa anahema kwa tabu. Koo lake bado halikuachia. Alikohoa mara kadhaa akiwa anahangaika kumeza mate.



    Hakukaa sana akamwona Isabel akimfuata kwa hasira. Alipotaka kuamka akimbie, Isabel akamwendea kwa kasi sana na kumdaka. Darren akajitahidi kurusha ngumi na kutumia nguvu zake za kibinadamu lakini akashindwa kabisa! Isabel alikuwa ana nguvu mno!



    Mwanamke huyo pasipo kujiuliza mara mbilimbili, akadidimizia kucha za mkono wake wa kushoto kwenye tumbo la Darren, na hakufanya vivyo mara moja bali mara tatu! Darren akalalamika sana kwa maumivu. Isabel akamtupia mbali akiwa amemalizana naye.



    Darren, akiwa amelala kama mtu anayengoja kifo akiwa ameshika tumbo lake linalovuja, akamtazama Isabel. Akamwona mwanamke huyo akiwa anaenda kumfuata Charlie kule shimoni. Basi akapaza sauti kuu kumwita Isabel. Halikuwa zoezi rahisi, alikuwa anahisi maumivu makali sana lakini alifanikisha adhma yake hiyo.



    Isabel alipogeuka kumtazama, Darren akapaza sauti kumtusi na kumkebehi mwanamke huyo. Kitendo hicho kikamkasirisha sana Isabel, akaamua kuachana na Charlie akammalize mwanaume huyo kabisa. Basi akamjongea kwa madaha akiwa anamwambia ni kwa namna gani atakapofurahi akiona roho yake inaenda.



    “Kama bibi na mama yako, nawe utaenda hukohuko!” akasema Isabel. “Mwana usiwe na haya ukatembea na bibi yako. Hujui Melissa ni sawa na bibi yako, ati Darren?”



    “Na mbona na wewe ulikuwa unanitaka?” Darren akaguguma kuuliza. Saa hii kinywa chake kilikuwa kinachuruza damu pia. Isabel akacheka akiwa anazidi kujongea, “Mimi? Darren mpenzi nilikuwa nataka tu kukumaliza na si kingine. Unadhani mimi ni kama yule mpofu Melissa? Mjinga kama yule?”



    “Ni wewe ndiye mjinga, si Melissa!” Darren akafoka.



    “Pole sana, Daren,” Isabel akasema akiwa anamalizia hatua yake moja kumfikia Darren. “Mpumbavu wako ameenda, nani atakulinda sasa?” akauliza na kucheka. “Kwa akili yake amejitoa uhai kwa ajili yako. Wewe binadamu. Kwa sababu tu ya kukwambia yote yale ambayo hupaswi kuyajua. Shenzi kabisa!”



    Alipomaliza kusema hayo akamnyakua Darren na kisha anyanyue mkono wake ili apate kumkita tena tumboni kama alivyofanya hapo awali. Lakini mara hii kabla hajafanya vivyo, akastaajabu kuona mpini wa reki ukitokezea tumboni mwake! Hamaki alikuwa ni Charlie nyuma yake!

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Basi akamwacha Darren na kisha akapiga magoti akiwa anatazama chuma kile kilichomtoboa tokea mgongoni mpaka tumboni na kisha akadondoka puh! Na kutulia tuli,



    Charlie akamjulia hali Darren.



    “Niko sawa,” Darren akamjibu na kisha akamuuliza, “Umefanikiwa?”



    “Bado kidogo!” Charlie akajibu. Akatazama tumboni mwa Darren, kulikuwa kunamwaga damu sana. Akashikwa na imani, “Darren, nikuwahishe hospitali!” alisema akitaka kunyanyuka akaendee gari lakini Darren akamdaka mkono na kumwambia, “Hapana, Charlie. Nenda kamalizie kwanza ile kazi!”



    “Darren, nitaendeleaje na upo kwenye hali hii?” Charlie akauliza.



    “Hapana! Hapana! Nenda kwanza, tafadhali nenda!” Darren alisisitiza na basi kwa shingo upande, Charlie akaenda zake. Akazama shimoni na kufukua zaidi na zaidi, ndani ya dakika tano akawa amefikia jeneza, akafunua na humo ndani akakuta maiti ya bibi yake Darren ikiwa mifupa.



    Alipotazama vema akabaini kulikuwa na kito rangi ya asamawati, basi akakibeba na kupaza sauti, “Darren, nimekipataaaa!”



    Haraka akatoka ndani ya shimo na kumkimbilia Darren. Lakini alipofika akabaini Darren hakuwa anasogea wala kuashiria kama mzima. Alipotazama vema akabaini pia mwili wa Isabel ulikuwa umesogea kidogo toka pale alipouacha, na kama haitoshi, reki halikuwa tumboni, bali kwenye kichwa likiwa limemtoboa!



    Hapo Charlie akabaini ya kuwa Darren na Isabel walipambana kwa mara nyingine. Akapata hofu zaidi juu ya uhai wa Darren. Akamwita sana na kumtikisa, kwa mbali Darren akafungua macho yake kumtazama. Alikuwa ana mjeraha kooni na kifuani. Karibia mwili wake wote ulijawa damu.



    “Umepata?” Darren akauliza kwa kunong’ona.



    “Ndio, nimepata!” Charlie akajibu kwa kitete. Macho yake yalikuwa mekundu yakitaka kumwaga machozi. “Twende nyumbani, sasa!” akasema akijaribu kumnyanyua Darren.



    “Hapana, Charlie,” Charlie akasema na kuongezea, “Hapa ndiyo nyumbani kwangu, sina pengine. We nenda mimi utaniacha hapa.”



    “Nitakuachaje Darren? Tumekuja wote hapa! Nyanyuka tafadhali twende!”



    Charlie alipoona ni ngumu kumnyanyua Darren basi akaenda zake asogeze gari karibu. Alipojipaki kwenye gari, akaendesha upesi sana kumrudia Darren. Alipoliweka gari tenge akashuka na kumwendea Darren, ila kwa muda huo hakuwa Darren tena bali mwili tu.



    Akapambana kumweka kwenye gari, lakini kabla hajawasha gari Isabel akanyanyuka na reki lake kichwani! Mwanamke huyo akakaa mbele ya gari akimtazama Charlie kwa macho ya kukodoa.



    Charlie akastajabu sana. Akahangaika kuwasha gari, kabla hajafanikiwa, Isabel akawa tayari amezama ndani na kumkaba shingo kwanguvu! Charlie akaweweseka sana kujiokoa.



    Ajabu wakiwa kwenye zoezi hilo, wakasikia mtu akigonga kwenye kioo cha dirisha. Isabel alipotazama, akabaini ni Melissa! Akastaajabu akiwa ameachama mdomo!



    “Ina -- inawezekanaje?”



    “Unadhani nilikuwa mjinga, sio?” Melissa akauliza.



    Kufumba na kufumbua akafungua mlango wa gari na kumnyaka Isabel. Kwa mikono yake akamnyofoa mwanamke huyo koo na kisha akamtupia mbali kana kwamba kitenesi!



    “Melissa!” Charlie akaita kwa kustaajabu. Akamkumbatia Melissa kwanguvu na kisha akamwambia kumhusu Darren. Walipomtazama wakabaini mwanaume huyo alikuwa amekwisha kufa.



    Basi Melissa akachukua kile kito ambacho Charlie alikipata kwenye jeneza la bibi yake Darren kisha akakitazama na kusema, “Nilikuwa nayajua yaliyo mbele yangu hata kuhifadhi sehemu ya maisha yangu kwenye jeneza lile.” aliposema hayo, akamtazama Charlie na kumwambia, “Utakapokutana na Darren mwambie nampenda sana. Hatimaye amekuwa huru. Hatimaye mmekuwa huru.”



    Aliposema hayo akaingiza kile kito kinywani mwa Darren na kisha kumfumba mdomo. Charlie akamuuliza, “vipi kuhusu yule Isabel, hatarejea tena?”



    Melissa akamjibu hatorejea tena kwa roho zake zimekwisha. Ndani yake alikuwa na roho kadhaa na kadiri walivyokuwa wanamuua ndivyo walivyozimaliza mpaka kubakia moja aliyoimaliza yeye muda si mrefu.



    “Umejuaje?” Charlie akamuuliza.



    “Kwasababu isingekuwa rahisi kummaliza kama nilivyofanya,” Melissa akamjibu na kisha akamuaga. Moja kwa moja akaenda kwenye shimo la kaburi na kudmbukia humo. Punde, Darren akaamka. Alikuwa mzima wa afya kabisa asiye na jeraha.



    Charlie alipomweleza kila lililotokea, upesi akakimbilia kwenye kaburi kumtazama Melissa. Akamkuta mwanamke huyo akiwa ana uhai amekwishakufa. Akamwita na kumwita pasipo mafanikio, Melissa alikuwa ameenda.



    Melissa hakuwapo tena.



    Basi wakamfukia kwenye kaburi hilo na kwenda zao.





    MWISHO

UNA NINI LAKINI MELISSA - 4

 

    Simulizi : Una Nini Lakini Melissa

    Sehemu Ya Nne (4)







    Darren akashtushwa na kauli hiyo. “Una maana gani, Madam Isabel?”



    Isabel akatabasamu. “Nini ambacho hujaelewa, Darren? Anyway, hii nyumba unayokaa sasa, sijapendezwa nayo. Umeona nyumba ya mwenzio Roby?”



    Kabla Darren hajajibu, Isabel akaendeleza maneno, “Nataka na wewe uwe na nyumba kama ile. Kubwa na ina nafasi kidogo. Sawa?”



    “Lakini sina tatizo na nyumba yangu hii,” Darren akajitetea.



    “Najua, najua, Darren. Hauna tatizo kabisa na nyumba yako hii, lakini nimekuomba tu uhame hapa. Tafuta nyumba kubwa zaidi. Usijali, nitasimamia kila kitu. Sawa?”



    Darren hakujibu, badala yake akatazama chini. Hakuwa ameafiki wazo hilo. Isabel akafungua pochi yake ndogo na kutoa kipande cha gazeti lenye picha kisha akamkabidhi Darren. Ilikuwa ni picha ya jengo la bibi yake kule kijijini.



    Akamuuliza, “Unajua nyumba hiyo?”



    “Ndio,” Darren akawahi kujibu. “Ni nyumba ya marehemu bibi yangu.”



    “Roby aliniambia hivyo,” Isabel akamhusia na kumuuliza, “Je, naweza nikaiununua?”



    “Nani alikwambia inauzwa?” Darren akauliza.



    “Kwenye gazeti ilikuwa inasema hivyo. Wamekosea?”



    Darren akafikiri. Pengine wazazi wake waliweka matangazo hayo wakiwa hai. Sasa vipi? Akawaza. Aibakize ile nyumba ama aiuze tu?

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ngoja ntakujibu,” akamwambia Isabel.



    “Sawa. Utakapokuwa tayari utaniambia,” Isabel akasema akifunga pochi yake. “Nitakulipa pesa taslimu, Darren.”



    “Sawa.”



    “Kwaheri. Nitakuja kukuona siku nyingine.”



    Kabla Darren hajatoka ndani ya gari, Isabel akambusu shavuni na kumuaga kwa kumnong’oneza, “Kwaheri, Darren.”



    Darren hakusema kitu akatoka zake na kwenda ndani. Alipoketi sebuleni, mkewe akatokea chumbani akiwa amembebelea mtoto. Macho yake yalikuwa yanatiririsha machozi.



    “Darren,” Josephine akaita na kuuliza, “Unaniletea mwanamke wako nyumbani kwangu. Kweli?”



    Darren akakodoa.



    Kidogo mkewe akajigeuza na kwenda zake ndani pasipo hata kuaga na huku akiwa anamwaga machozi. Hali hiyo ikamfanya Darren ajisikie vibaya sana. Moyo ukamnyong’onyea akiwa anajiuliza nini kimemsibu mkewe?



    Hakuwa anajua kwamba mkewe alimwona wakati Isabel akimbusu kwenye gari, kioo cha gari kilikuwa chini hivyo ikapeleka kuonekana kwa urahisi na mkewe akiwa chumbani.



    Akaketi pale sebuleni kwa kama sekunde tano kabla hajanyanyuka na kumfuata mkewe ndani kumjulia hali lakini kumuuliza nini shida. Alipofika, akamkuta mkewe akiwa amejilaza kitandani analia. Mtoto alikuwa amelala kwenye kitanda chake.



    Akamwita, “Josephine!” mwanamke hakuitika. Akarudia kuita tena na tena lakini bado kukiwa kimya. Akaketi kitandani na kumshika bega.



    “Mke wangu,” akaita kwa upole. Mwanamke bado akawa kimya. Ni sauti ya mafua tu ndiyo ilikuwa inasikika na miguno ya kilio.



    “Nimekufanya nini?” Darren akauliza. “Niambie basi nini tatizo?” Darren akahisi huenda mkewe aliumizwa na kile kitendo cha mkewe kwenda kuonana na Isabel kando, basi akaomba msamaha huku akimhakikishia kuwa hakufanya jambo baya, lakini bado tu. Josephine aliendelea kulia asiseme jambo.



    Zikapita kama dakika tano … sita … saba … bado Josephine kimya. Mwishowe Darren akaona ni staha akimwacha mwanamke huyo yeye aende sebuleni kutulia alafu baadae mwanamke huyo atakapokuwa sawa, aongee naye.



    Akaketi sebuleni kwa kama lisaa. Kimya. Akawasha runinga na kutazama lakini akili yake yote ikiwa kwa mkewe. Akaitazama kwa kama nusu saa, bado kimya. He! Akashangazwa na hali hiyo. Akapatwa pia na mkanganyiko wa nafsi, je aende tena kumbembeleza mkewe au atulie hapo mpaka atakapokuja mwenyewe?



    Akiwa anawaza, mara akasikia mlango ukifunguliwa na kisha vishindo vya mtu. Kidogo akamwona mkewe akifika sebuleni lakini akipitiliza moja kwa moja kwenda jikoni.



    Akarusha macho kumtazama. Kidogo akahofu mkewe asije akawa ameenda kujidhuru. Akakodoa mpaka pale Josephine alipotoka huko jikoni na kutembea kudaka korido. Akamwita tena, mara hii Josephine akaitika kwa kumtazama.



    Macho yake yalikuwa yamekauka machozi lakini yakiwa bado mekundu. Uso wake ulikuwa umesinyaa kwa huzuni na mdomo wake umevimba.



    “Una nini Josephine?” swali hilo likafungua tena mifereji ya machozi. Josephine akabubujikwa na machozi na mdomo wake ukatetemeka akiumauma meno. Hakuwa anaweza kuongea. Kuna kitu alikuwa anahisi kinamkaba kooni. Mdomo ulikuwa ni mzito na kichwa chake kilikuwa kinagonga.



    Hakuwahi kuwaza … hakuwahi kuwaza kabisa kama Darren anaweza kumsaliti kwa kuwa na mwanamke mwingine.



    Kila alipotaka kuongea akajikuta taya zinagongagonga. Mdomo unajawa na uchungu usio wa kawaida. Akaamua tu kuondoka zake. Mumewe akamsindikiza kwa macho yenye itilafu mpaka alipozama ndani ya chumba kabisa, akaufunga mlango.



    “Eh!” Darren akahema akijilaza kitini. “Kazi nnayo.”



    Akabaki hapohapo akitazama runinga na kurudi mawazoni, akitazama runinga na kurudi mawazoni mpaka mwishowe akabebwa na usingizi kabisa. Ulikuwa ni usingizi mwepesi lakini uliomfanya akapata kidogo afueni ya rundo la mawazo alokuwa anapitia.



    Lakini katika namna ya ajabu, ya ajabu kabisa, usingizi huo ukageuka kuwa mzito kupita kiasi! Darren akajikuta analala akikoroma kabisa, hata kumwaga udenda akiachama kinywa. Ni kama vile hakuwa amelala kwa juma zima, au amefanya kazi kubwa sana na hakupata muda wa kupumzika.



    Akiwa ndani ya usingizi huo akazamia ndotoni ambapo alijiona yu ndani ya nyumba ya bibi yake, kule kijijini. Alikuwa sebuleni akifanya usafi akiwa anangojea ugeni muda si mrefu.



    Kidogo akiwa anaendelea na kazi hiyo, mkewe akaja akiwa amembebelea mtoto. Mtoto alikuwa analia lakini punde akanyamaza. Josephine akaketi kwenye kiti na kumtazama Darren.



    “Ungesogea kando kidogo na mtoto kwani kuna vumbi!” Darren akamwonya mkewe kisha akaendelea na kazi yake akijua mkewe atafanyia kazi ushauri wake. Lakini baadae alipokuja kutazama, akatahamaki mkewe alikuwa bado amekaa kwenye kiti!



    “Josephine!” Darren akaita. Mkewe alikuwa bado anamtazama. “Si nimekwambia utoke hapo lakini? Huoni vumbi?”



    Josephine akaendelea kumtazama tu. Hakuonyesha dalili yoyote ya kusikia anachoambiwa. Kidogo, mbele ya macho ya Darren, Josephine akachomoa kisu toka nyuma ya mgongo wake. Kilikuwa ni kisu kipana na kirefu. Kisu kinachometa kwa upya. Na ndani ya sekunde moja tu, kufumba na kufumbua, Josephine akamdidimizia mtoto kisu chote kifuani!



    Darren akatoa macho haswa. “Mungu wang - Josephine! Nini unafanya?”



    Josephine akamweka mtoto kando na kisha akanyanyuka kumfuata Darren akiwa amebebelea kisu chake mkononi. Darren akapiga yowe kali. Akashuka toka alipokuwa amekwa na kuanza kupambana kujiweka mbali na Josephine kwasababu za usalama wake.



    Josephine akazidi kumjongea na kisu kinachochuruza damu. Uso wake ulikuwa umekengeuka kuwa wa ajabu. Macho yake yamekuwa ya kijani na mdomo wake unaapa kifo.



    Hakuwa Josephine uliyemzoea, mkarimu, mpole na mwenye kutenda yaliyo mema. Alikuwa ni Josephine kutoka kuzimu. Josephine mwenye umbo la binadamu lakini roho ya shetani!



    “Josephine! Hapana! Tafadhali usifanye hivyo!” Darren aliwaka kwa woga. “Tafadhali, Josephine. Mimi ni mume- ” hajamalizia, Josephine akamrukia na kunyanyua mkono wake wenye kisu.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hapo ndipo Darren akaamka toka kwenye lindi zito la usingizi! Akiwa anahema kama mbwa, akatazama kushoto na kulia kwake. Macho yamemtoka na mdomo ameachama!



    Kidogo tu, akasikia sauti kali ya mtoto ikilia. Haraka akanyanyuka na kukimbilia chumbani. Upesi akamwangalia mtoto, alikuwa yu kwenye kitanda chake analia haswa. Basi akamnyanyua na kujaribu kumbembeleza. Kitandani Josephine alikuwa amelala.



    “Josephine,” Darrena kaita na kuuliza, “Hausikii mtoto analia?”



    Kimya.



    Darren akaita tena na kuuliza. Bado kimya. Basi akadhani bado Josephine ameendeleza mgomo wake. Lakini ndiyo mpaka kwa mtoto? Akajiuliza. Akatoka chumbani humo na kwenda mpaka sebuleni akiwa anambembeleza mtoto wake, hatimaye mtoto akalala.



    Basi akaona ni vema akamlaze mtoto kitandani chumbani. Alipofanya hivyo, kabla hajatoka chumbani akamwita tena Josephine. Bado kimya. Saa hii akaamua kutoondoka mpaka pale atakapotimiza adhma yake, kuongea na mkewe.



    Akamgusagusa na kumshtua. Akamsogezasogeza na kumwita. Kidogo ndipo akabaini ya kuwa mkewe alikuwa amemeza vidonge vingi, kumbe pale hakuwa mzima. Povu lilikuwa linamtoka mdomoni na macho yake yamekwisha panda juu!



    Akachanganyikiwa haswa.



    Uopesi akambeba mkewe na kumkimbizia kwenye gari, na pasipo kufunga mlango akatia moto gari na kuendesha kwa haraka amwahishe hospitali. Lakini kufika mbele ndipo akabaini hata na mtoto alikuwa amemwacha ndani!



    “Mungu wangu!” akajikuta anatoka na maneno. Akarudi nyuma upesi na kujitengenezea vema kwenye barabara kisha akarudi nyumbani kwa kasi ya ajabu.



    Alipofika akakimbilia ndani na kumbemba mtoto, akamweka ndani ya gari na kutimka kama kimbunga!



    Laiti askari angemwona namna alivyokuwa anaendesha, asingeshani hata kama mwanaume huyo amembembelea mtoto na mwanamke ndani. Akili yote ya Darren ilikuwa imeruka! Alikuwa anamuwaza mkewe tu. Lakini pia akidhani huenda akawa amempoteza, au atampoteza akiwa njiani.



    Kheri akafika hospitalini salama. Akamtua mke wake na kumwahisha kupatiwa huduma. Yeye na mwanaye wakakaa kitini kungoja taarifa ya daktari.



    Darren akiwa amekaa hapo akawa anaomba kila aina ya sala mkewe anusurike.



    Kama baada ya dakika tatu, Isabel akampigia simu.



    Akaitazama simu hiyo na kusonya, hakutaka kupokea, lakini ikaita pasipo kukoma, hatimaye, kwa kuepusha usumbufu, akapokea na kuiweka sikioni.



    “Hey Darren,” Sauti ya Isabel ikasalimu na kisha kuuliza, “Kuna shida?”



    Swali hili likamshtua kidogo Darren. Alijiuliza kama Isabel amemwona ama? Mbona ni mara ya pili hii akimuuliza swali hilohilo?



    “Isabel,” Darren akaita na kuuliza, “Una maanisha nini kuniuliza hivyo?”



    “Najua una matatizo, Darren,” Isabel akasema kwa kujiamini.



    “Umejuaje kama nina matatizo?”



    “Uso wako tu unaonyesha. Niambie ukweli Darren, hauna shida?”



    Darren akawa kimya kidogo.



    “Ni sawa, Darren. Kama utakuwa una shida basi unajua pa kunipata.” kisha Isabel akakata simu na kumwacha Darren akiwa kwenye lindi la mawazo. Ni kweli Isabel anayajua anayoyapitia ama anahisi tu? Je ni sahihi kwake kumshirikisha mwanamke huyo ama akaze kifua tu?



    Alijiuliza pasipo na kikomo. Daktari akaja na kumshtua amwitaji ofisini. Alipoenda huko Daktari akamweleza maendeleo ya mkewe kuwa ameathirika sana na madawa aliyoyatumia. Kurudi kwenye hali yake itawachukua muda kidogo.



    “Laiti ungemuwahisha, kazi ingekuwa nyepesi zaidi,” Daktari alisema vivyo na kisha kumpatia moyo bwana Darren, “Usijali, atapona tu. Japo yatupasa tuchukue muda kwa mwili wake kurejea kwenye hali ya kawaida.”



    Basi Darren baada ya habari hizo, akajiendea kwenye benchi kuketi zaidi. Hapo akawa na mwanaye aliyekuwa anambembeleza. Mwanaye aliyekuwa anamwonea huruma kwa mama yake kuwa hoi kwa ugonjwa.



    Alikaa hapo kwa masaa mawili kabla hajaona ni vema kumjuza Roby ili aje kumjulia hali. Punde kidogo, Roby akaja na angalau Darren akapata muda wa kutoa yaliyo kifuani mwake. Angalau akajihisi mwepesi kwa kunena yanayomsibu.



    Kuongea napo ni tiba.



    Roby akampa pole sana na kumfariji. Akakaa naye kwa muda mrefu kabla hajamuaga aende kupumzika nyumbani.



    “Utaniambia kitakachotokea, Darren. Lakini nakushauri kwanza uende nyumbani ukapumzike na kumpatia mahitaji huyo mtoto,” alishauri Roby kabla hajajiendea zake. Darren akamsindikiza kwa macho akitamani kumwambia mwanaume huyo asimwambie Melissa chochote kile.



    Alijua fika angemwambia hivyo Melissa basi mwanamke huyo angefika hapo ndani ya masaa machache. Hakutaka kabisa kuwa karibu na mwanamke huyo. Lakini angemwelezaje hivyo Roby?



    Roby akaenda zake. Darren akajikusanya na kwenda nyumbani kumlisha mtoto na kuweka mambo mengine sawa. Alipohakikisha kila kitu kipo kwenye utaratibu, akaenda kuoga aondoe uchovu.



    Alipotoka bafuni na kutazama simu yake akakuta ‘missed calls’ toka namba ya Roby. Baada ya kujiuliza kidogo akapiga na kupachika simu yake sikioni. Baada ya kuita kidogo, ikapokelewa. Ajabu likuwa ni sauti ya kike. Sauti ambayo si ngeni masikioni mwa Darren.



    “Hujambo?”



    “Sijambo. Nani?”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Umeshanitambua, Darren. Najua namba yangu umeifunga.”



    “Unataka nini Melissa?”



    “Nimesikia una matatizo. Vipi upo sawa?”



    “Ndio, nipo sawa. Kuna lingine?”



    “Pole sana, Darren. Najua matatizo unayoyapitia hivi sasa. Usi--”



    “Melissa! Naomba niskize vema, sawa? Sitaki kuwasiliana na wewe. Naomba uachane na mimi. Tafadhali. Na kama ukiendelea kunisumbua basi nitamwambia Roby juu yako.”



    Melissa akaangua kicheko.



    “Huoni utakuwa umenirahisishia kazi, Darren?” akauliza. “Kama ukimwambia Roby kuhusu mimi na wewe, nami nitamkubalia kila kitu na kumwongezea taarifa zaidi. Mosi, urafiki na ubia wenu utakuwa hatihati, pili, utakuwa umenisafishia njia ya mimi kurudi kwa--”



    Darren akakata simu. “Shenzi!” akatupia simu kochini na kudaka kichwa chake kwa mawazo.



    Melissa akasonya akitazama simu yake, kisha akamtazama Roby aliyekuwa amelala kitandani fofofo. Akanyanyuka na kujiondokea zake akimwacha mwanaume huyo hajielewi A wala Z.



    Akashuka mpaka chini na huko akapanda gari la Roby na kutimka akienda tusipopajua.



    Baada ya muda kidogo, Darren akamwona akiwa anasinzia. Alikuwa tayari ameshakula na ni usiku sasa. Aliwaza kumlaza mtoto huyo alafu aende mwenyewe hospitali, lakini akasita. Atamwachaje mtoto hapo? Akafikiri afanye nini.



    Baada ya muda kidogo akaona ni kheri tu kama ataenda na mtoto huyo hospitali. Asingekuwa na amani kama mtoto huyo angelibaki mwenyewe nyumbani. Hakuwa na budi. Akajifungia mwanaye kifuani kwa kibebeo maalum kisha akabeba chupa ya maziwa endapo kama mtoto atahitaji hapo baadae.



    Akajiweka kwenye gari na safari ya kwenda hospitali ikaanza. Alifikiri sana alipokuwa njiani. Maisha yalikuwa yamebadilika pasipo mkewe, inabidi atafute namna, hawezi akawa anaongozana na mtoto muda wote. Vipi akihitaji kwenda kazini?



    Akiwa kwenye foleni la mataa, akakubali na nafsi yake kuwa kwa kipindi hiki ambacho mkewe anaumwa, inabidi amtafute ‘babysitter’ atakayemtazama mtoto na kumpa mahitaji yake. Na pale mkewe atakaporejea kwenye hali yake basi mhudumu huyo atajiendea zake.



    Ila akapata tena wazo jingine, vipi kama akiwa anampeleka mtoto huyo mahali pa kutunzia watoto, ‘daycare’, huko awe anampitia akitoka kwenye mihangaiko yake?



    Kidogo wazo hili likawa gumu. Aliona ni kama kumtupa mtoto wake kwa kufanya hivyo. Hapana, siwezi, akawaza. Hakuwa na imani sana na hiyo njia hivyo akachagua ile ya kwanza, amtafute dada atakayekuwa anamsaidia.



    Akaendesha gari mpaka hospitali. Alipofika huko akazima gari lake na kukwea kwenda juu. Aliposonga kuendea pale ambapo mkewe alikuwa amepumzishiwa, akastaajabu kumwona Melissa!



    Mwanamke huyo alikuwa amesimama akitazamatazama huku na huko, mkononi mwake ana simu kubwa nyeusi anayoipigapiga kiganjani. Alikuwa ni kama mtu aliyepotea.



    Darren akamfuata kwa hasira na kusimama mbele yake akimuuliza, “Umekuja kufanya nini hapa Melissa?”



    “Kukuona,” Melissa akajibu kwa tabasamu. “Kwani kuna ubaya?”



    “Melissa, nikuambie mara ngapi wewe?”



    “Kwani Darren mimi nimekuambia mara ngapi? Ushawahi kunielewa?”



    “Hivi hauogopi hata Roby akijua upo hapa.”



    Melissa akaguna kwa cheko. “Roby?” akauliza na kisha akatabasamu. “Hawezi jua. Amejilalia hajiwezi!”



    “Melissa, nikuombeje uachane na maisha yangu? Nikuombeje, ebu niambie. Melissa achana na maisha yangu. Naku--” Mara nesi akapita na kuzama ndani ya chumba alicholazwa Josephine. Kidogo tena, mlinzi aliyekuwa amevalia sare zake akajongea eneo hilo na kuuliza, “Kuna tatizo hapa?”



    Darren akamtazama Melissa, Melissa akamjibu mlinzi, “Hamna tatizo, bwana. Waweza tu kuendelea na majukumu yako mengine.”



    Lakini kabla mlinzi hajaondoka hapo, mara nesi akatoka chumba cha mgonjwa akiwa anatembea kwa kasi sana. Darren akapatwa na hofu. Kidogo tu, nesi akarejea na daktari wakazama mule chumbani.



    Kama baada ya robo saa, daktari akatoka na kumwambia Darren kuwa mke wake amefariki.



    Darren alihisi daktari anamtania. Aliuliza mara nne kama alichoambiwa ni kweli na daktari asibadilishe maneno akarejelea kauli yake ile ile na kisha kumpa pole Darren kwa kumpoteza mtu wake wa karibu.



    Darren akalia kama mtoto mdogo. Msalaba huu ulikuwa ni mkubwa sana kwake. Hakujiona kama anaweza kuubeba. Bado alikuwa anamhitaji mke wake haswa kipindi hiki ambacho mtoto ni mdogo.



    Ataishije? Alijiuliza akiwa anamwaga machozi kwenye benchi. Melissa alijaribu kumtuliza lakini asifanikiwe. Bwana huyo aliendelea kulia kwa uchungu kwa kumpoteza mpendwa wake. Mwishowe hata machozi na sauti ikawa imemkauka.



    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    **



    Baada ya watu wote kuondoka na kumwacha makaburini, Darren aliijipangusa mdomo wake na kutazama kaburi la mkewe. Bado halikuwa limesimikwa jina wala maelezo yoyote yale. Macho yake yalikuwa makavu na meupe, hakulia siku hiyo.



    Alichuchumaa na kusema mwenyewe akiamini anateta na mkewe, “Nakupenda sana, mke wangu. Umeondoka tukiwa hatujamaliza tofauti zetu. Roho inaniuma sana kwa hilo lakini sina cha kufanya. Nisamehe sana mpenzi.”



    Aliposema maneno hayo akanyamaza kwanza. Macho yakaanza kujawa na machozi. Akajipangusa na kuendelea kusema, mara hii sauti yake ikiwa inatetemeka. “Sijui nitaishi vipi pasipo wewe. Sijajua …” akajipangusa chozi. Alikuwa anahisi kifua chake kinawaka moto. Moyo umekuwa mzito sana. Alikuwa anajihisi hovyo, hovyo ambayo haiwezi kuelezeka.



    “Umekuwa mwanamke wangu wa kujivunia kwa muda wote huo. Siwezi kueleza ni kwa namna gani ulijaza upendo na furaha ndani ya nyumba yangu. Hakika hakuna wa kuziba pengo lako. Maisha yangu hayatakuwa sawa tena pasipo na wewe.”



    Kisha akanyanyuka na kuendea gari, akajipakia kwenye viti vya nyuma na kufunga mlango, gari likaondoka. Dereva alikuwa Roby, pembeni yake akiwa amekaa Melissa.



    Japo watu walikuwa wawili kwenye gari, Darren hakuongea chochote. Alikuwa kwenye ulimwengu wake wa pekee kabisa. Akiwa amelaza kichwa chake kwenye kiti, alikuwa anatazama nje. Uso wake ulikuwa umepooza na kupwaya. Alikuwa mbali sana kimawazo.



    Gari lilisimama mbele ya nyumba yake, Roby akamgeukia na kumuuliza kama yuko sawa, lakini hakuwa anasikia kitu. Ilimbidi Roby arejelee swali lake mara tatu ndipo Darren akamtazama na kumjibu. “Niko sawa, nashukuru.”



    Na kabla halijaongezewa neno lingine, akafungua mlango na kutoka ndani ya gari. “Kwaheri!” akapunga mkono wake mara moja kwa Roby kisha akajigeuza na kuelekea ndani kwake.



    Basi baada ya hapo maisha ya Darren yakabadilika kabisa. Hakuwa mtu wa kuzungumza bali kukaa kimya na kujitenga. Mara nyingi alikuwa ni mtu wa mawazo sana na hata kulia. Ndani ya juma moja tu akapungua uzito kwa kiasi kikubwa sana. Alikuwa ni kana kwamba mtu anayeliwa na kansa hatua ya nne.



    Hakuwa na raha. Ilikuwa ni nadra kwake kutabasamu ama kucheka. Roby akajitahidi sana kukaa naye na kumhasa lakini haikusaidia. Naye Isabel akajaribu sana kujiweka karibu na Darren, lakini bado jitihada zake zikagonga mwamba. Darren hakuwa anataka kukaa karibu na mtu. Alikuwa anataka kukaa mwenyewe tu.



    Akirudi nyumbani humuuliza dada wa kazi juu ya maendeleo ya mtoto kisha anamwona mwanaye kwa muda mfupi na kwenda kujilaza. Siku nyingine akawa anarudi nyumbani akiwa na chupa za vinywaji vikali. Anakunywa pasipo kujionea huruma na kisha analala kama mfu.

    Siku nyingine hata kazini akawa haendi. Anakunywa tu siku nzima. Afya yake ikaendelea kuzorota.



    Ikiwa ni mwezi mmoja umepita tangu Josephine afariki, Darren akajiona sasa anahitaji msaada. Alionana na mwanasaikolojia na kumweleza shida yake kwa ajili ya ‘counselling’. bwana huyo mwanasaikolojia, bwana Hamlet, akajitahidi kadiri ya uwezo wake kumsaidia Darren kwa kumpatia ushauri, lakini Darren akaenda mbele zaidi kwa kumwambia na yale mengine yakutisha. Mambo anayoona usiku na viumbe wa ajabu.



    Hapo bwana Hamlet akasita kumshauri. Mwanzo alihisi Darren atakuwa amekanganyikiwa kutokana na kumpoteza mtu wake wa karibu lakini baadae akaja kuelewa baada ya Darren kumwambia alishawahi kuyaona mambo hayo hata kabla ya mkewe kufariki.



    “Tafadhali, unaweza kunisaidia?” Darren alilia. Bwana Hamlet akamtazama kwanza mwanaume huyo kwa mafikirio kisha akamsihi apate muda wa kupumzika zaidi, pia kama itakuwa inawezekana basi akatafute mahali pengine pa kuishi mbali na hapo alipo. Pengine yaweza kumsaidia.



    Darren akashukuru kwa ushauri na kwenda zake. Alipojiweka kwenye gari akafikiria kwanza maneno aliyoambiwa na bwana Hamlet.



    Akiwa fikirani humo, mara upepo wa wastani ukapuliza kiasi na kupeperusha gazeti fulani lililokuwa chini mpaka kwenye kioo cha gari lake. Gazeti hilo lilikuwa la kale kidogo. Upande ambao ulijipachika kiooni ulikuwa na picha ndogo tatu na maelezo kadha wa kadha.



    Katika maelezo hayo, mojawapo ilisomeka; *“MWANAMKE ANAYESUMBULIWA NA VIUMBE WA AJABU, APOTEA.”*



    Habari hiyo ilikamata fahamu za Darren. Kidogo upepo ukalisomba gazeti hilo na kulitupia kando na kuliburuza zaidi na zaidi. Darren akatoka kwenye gari na kulikimbilia. Akalinyaka na kurudi ndani ya gari. Akatulia na kusoma taratibu habari ile ambayo ilimkamata hisia.



    Alipomaliza kusoma akaliweka gazeti hilo kando na kutazama akiwa amejawa na mawazo. Kidogo akawasha gari na kuendea anwani ya nyumba ambayo ameona taarifaze kwenye gazeti.



    Alitembea barabarani kwa masaa matano. Ilimlazimu aweke mafuta ili akamilishe safari yake. Alipofika, ilikuwa ni nyumba ya mbao yenye ukubwa wa wastani, akagonga na punde akafunguliwa na binti mwenye makamo ya miaka ishirini, akaeleza shida yake anataka kuonana na wazazi.



    Binti akamkaribisha ndani na kidogo akaja mwanamke mnene kidogo mwenye nywele fupi nyeusi. Mwanamke huyo alikuwa ana macho makali na mkononi mwake alikuwa amebebelea kitambaa alichokuwa anatumia kukaushia vyombo. Yule binti aliyemkarimu mgeni akaenda zake chumbani.



    “Habari, naitwa Darren.”



    “Karibu, naweza kukusaidia,” aliuliza yule mwanamke akiwa anatazama kwa mashaka. Hakuwa na imani machoni. Darren akaeleza shida yake akionyesha lile gazeti. Alikuwa anataka kusikia habari zaidi za yule mwanamke aliyepotea. Kwa namna moja ama nyingine alikuwa anaona habari hiyo na ile ya maisha yake zinawiana.



    Baada ya kusema hivyo yule mwanamke mwenyeji akatazama chini na kisha akarudi alipotokea, jikoni, kisha baada ta muda kidogo akarudi akiwa hana kile kitambaa bali ana kisu. Kidogo Darren akahofia. Mwanamke yule akaketi kiti kitazamanacho na Darren alafu akaweka kisu chake mezani.



    Kisu kilikuwa kina mpini wa bluu, na kama ungekitazama vema ungeona maandishi yasomekayo ‘stainless steel’ kwenye shina la makali yake. Kilikuwa ni kisu kirefu chenye ncha kali. Darren alishindwa kujizuia kutokutazama kisu hicho.



    “Upo tayari na utasadiki?” akauliza mwanamke yule akiwa anamtazama Darren machoni.



    “Ndio, nipo tayari,” Darren akajibu. Basi mwanamke yule akanyanyua kisu kile na kukichomeka kwanguvu mezani. Kisu kikachimba meza na kusimama dede. Darren akazidi kuhofu.



    Basi mwanamke yule akaanza kusimulia kwa sauti yake inayofanana na kasuku. Akiwa ameongea sentensi mbili tu, upepo ukapuliza dirishani na kupeperusha pazia kama bendera. Darren akatazama huko upesi akiwa mjawa wa mashaka.





    Mwanamke yule akiwa anamtazama Darren machoni akasema ya kwamba yeye hana majibu ambayo Darren alikuwa anayauliza, ila tu amefurahishwa sana na uwepo wa Darren hapo. Lakini inawezekanaje hilo na ingali Darren hajuani na mwanamke huyo?



    Darren alipouliza, akatahamaki mwanamke yule anabadili rangi ya macho yake na kuwa nyeusi kama bendera. Alafu mwanamke huyo akachomoa kisu chake toka mezani na kumrukia Darren akitaka kumchoma.



    Ilikuwa ni swala la kufumba na kufumbua tu, nyumba ile ikawa ghofu kabisa. Paa lake lilijawa na tando za buibui na madirisha yakiwa yamepotea yasionekane. Kulikuwa giza, mwanga hafifu rangi nyekundu ikiwa inatambaza kwa mbali.



    Ilikuwa ni ajabu namna gani ambavyo mambo yalbadilika kwa upesi namna ile! Nyumba iliyokuwa ni nzuri ikageuka na kuwa nyumba ya mizimu, nyumba ya majini! Harufu ya damu ilitawala na mifupa huku na kule.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kwa Darren yalikuwa ni kama mazingaombwe ama maigizo! Hakuwa anaelewa kinachoendelea hapa. Kila kitu kwake kilikuwa ni kama amerukwa na akili. Kitu pekee alichokuwa ana kijua na kupambana nacho ni kuokoa nafsi yake dhidi ya umauti uliokuwa unataka kumkumba.



    Hakujua alikuwa amezama. Tena amezama kwenye lindi zito la kifo. Ameshikwa kwenye tego kali la kummaliza.



    Akapambana kumzuia mwanamke yule asimkite na kisu, na alipofanikiwa kufanya hivyo baada ya kumtwanga mwanamke huyo kichwa cha puani, akakimbilia mlango afungue na kwenda, lakini alipofika mlango haukufunguka abadani! Haikujalisha ni nguvu kiasi gani alitumia, mlango ukamtazama kodo pasipo mafanikio.



    Yule mwanamke akacheka sana. Akanyanyuka toka chini huku akijitoboatoboa na ncha ya kisu kana kwamba godoro. Ilikuwa ni ajabu kwamba ahisi maumivu? Akavuja damu na kujichafua haswa lakini hakuwa anajali hata kidogo.



    Alimtazama Darren kwa macho ya matamanio, alafu akalamba kisu chake kana kwamba mtoto na mche wa ‘ice-cream’, alafu kufumba na kufumbua akamkimbilia mwanaume huyo akammalize. Mwendo wake ulikuwa wa kasi sana, lakini kabla hajafika aendapo, kumbe Darren alikuwa ameshakamata stuli kwa mikono yake miwili, akamkandika kwanguvu mno! Puuh!!! Mwanamke huyo akasombwa na kubwagwa ukutani, kisha kukawa kimya!



    Darren, akiwa anahema kwa hofu, akamtazama mwanamke yule kwa jicho la tahadhari. Bado mikononi akiwa ameshikilia ile stuli yake endapo lolote litajiri. Ikapita dakika ya kwanza kukiwa kimya. Dakika ya pi… akasikia mlango unafunguliwa! Akatupa macho yake kupambana na kiza kilichopo apate kuona.



    Hakuona kitu!



    Moyo wake ulikuwa unamwenda mbio sana. Kwasababu kulikuwa na ukimya wa kufanya masikio yawe kiziwi, Darren alikuwa anaweza kusikia mapigo yake ya moyo kwa uzuri kabisa. Angeliweza kuyahesabu pasipo matatizo kabisa.



    Kidogo, akapata wazo la kutumia stuli ile kubomolea mlango. Akabondea hapo mara kadha wa kadha. Akaponda na kubonda lakini mlango haukufunguka. Ulikuwa ni migumu kama ile ya kasri ya mfalme. Ulikuwa ni mgumu kana kwamba malighafi yake ni chuma na metali! Badala ya mlango kukongoroka, ni stuli ndiyo ikaanza kuwa dhoofu na kuanza kumomonyoka!



    Mwishowe Darren akabakiwa na vipande tu vya stuli mkononi mwake ingali mlango ukiwa madhubuti.



    Akainama kwa kuchoka. Akahema sana akivuja jasho. … lakini nyuma yake kule kulipotoka sauti ya mlango kulikuwa na nini? Kama ungetazama vema, kwa kuyafinya macho na kusisitiza maono yako basi ungeliona kuna kiumbe kilikuwa kinatembea gizani kumjongea.



    Miguu ya kiumbe huyu ilikuwa inakanyaga sakafu taratibu. Kwasababu ya kiza, hakikuwa kinaonekana vema.



    Kilisonga kwa hatua ya karibu lakini harakaharaka.



    Darren alihisi kitu, upesi akageuka na kuangaza koridoni, kizani. Hakuwa anaweza kuona kitu. Japo alikodoa bado hakuwa na uwezo wa kuona jambo. Alipomtazaa yule mwanamke aliyemsomba kwa kumkita awali, akamwona bado amelala palepale. Sasa ni nini hicho anahisi? Akajiuliza.



    Kufumba na kufumbua, Darren akastaajabu kuona kitu juu ya paa. Hajakaa vema wala kujitengenezea, kiumbe hicho kikamvamia na kumwangusha chini kikimkaba na kumng’ata shingoni!



    Mdomo wake ulikuwa wa baridi sana. Meno yake yaliyochongoka yalikita kwenye mishipa ya shingo ya Darren na kisha koo lake likawa linamnyonya damu!



    Kwa ubaridi wa kinywa hicho, Darren akahisi mwili wake umezamishwa kwenye dimbwi la barafu. Alihisi baridi toka kwenye nyayo yake mpaka utosini. Lakini baridi hili likiwa linakera! Baridi linalotisha.



    Pumzi ya kiumbe hicho ilisabahi shingo yake na kuzidi kumtia hofu na kimuhemuhe.



    Kheri Darren bado alikuwa na vipande vile vya stuli mkononi. Kama mtu aliyepandwa na kichaa, akatumia vipande hivyo kwanguvu na pasipo mafikirio kumshabulia kile kiumbe kilichomshikilia.



    Akamtoboatoboa kiasi kwamba hata yeye akajiumiza. Kile kiumbe kikapiga kelele na kuangukia chini. Kabla Darren hajamtazama mvamizi wake huyo akagundua kuwa shingoni alikuwa anachuruzwa na kimiminika cha moto. Alipojipapasa akagundua ni damu! Alikuwa anchuruzwa na damu nyingi na akihisi maumivu makali.



    Alimtazama kiumbe kile alichoadhibu na kubaini alikuwa ni yule mtoto aliyemkaribisha na kumfungulia. Alikuwa amejilaza akiwa ametulia na kuvuja damu. Alipotazama kule ambapo alikuwa amelala yule mwanamke aliyemwadhibu mwanzoni, ajabu hakuona kitu!



    Akiwa ameweka kiganja chake shingoni kuzuiza damu zinazotiririka, akajongea na kuangaza pale alipokuwa amemwona mwanamke yule mwanzoni. Lah! Hakuwapo. Hapo akapata hofu sana. Kutokuwapo kwa mtu huyo kulikuwa ni ishara mbaya kwa usalama wake.



    Akatazama kushoto na kulia, juu na chini asione kitu! Moyo wake bado ulikuwa unadunda kwa kasi, na damu bado zamchuruza kufurika vidole vyake. Ni wazi alikuwa ana muda mfupi wa kuwa hai kama jeraha hilo lisingepata huduma ya upesi.



    Aliendelea kuangaza na kuangaza. Kidogo akahisi upande wake wa kulikuwa na kiumbe. Alirusha macho yake upesi akikodoa. Mkono wake wa kuume alikuwa amebebelea kipande cha stuli na ule wa kushoto ukiwa umehifadhi jeraha.



    Baada ya muda kidogo, akaona kuna kitu chenye rangi nyeupe ya kufifia mule kizani. Alipojaribu kukaza macho yake atazame, akashindwa. Alikuwa ameanza kuishiwa na nguvu na macho yake yakijawa na ukungu.



    Aliona kiza kimeongezeka maradufu … Mkono uliobebelea silaha nao ukaanza kupwaya.



    Kidogo akaona kitu kile chenye rangi nyeupe kikisogea zaidi karibu yake. Alikuwa ni mtu lakini alishindwa akumtambua kutokana na macho yake kudhoofu. Na hata alipotaka kumshambulia mtu huyo kwa kutumia silaha yake, hakuweza. Hakuwa na nguvu hiyo tena. Jeraha lilishamzidi nguvu.



    Akazabwa kofi shavu lake la kulia na kudondoka chini. Hata hakuhisi maumivu tena. Kitu pekee ambacho kilikuwa hai kwenye mwili wake ni macho yake yaliyokuwa yamekodoa na kuoa ukungu. Aliona tu kiza, kiza na yeye.



    Na jambo la mwisho ambalo alilielewa ni kushikwa shati lake na kuburuzwa. Kidogo tu akapoteza fahamu kabisa.



    Yalikuwa yamekwisha.



    Hakuelewa kinachoendelea hata kidogo. Alikuja kupata ufahamu wake akiwa kwenye gari, viti vya nyuma. Alikuwa amechoka mno, kichwa kinamuuma. Mwili wake anauhisi dhaifu viungio vyote vikiwa vinapwita.



    Alijaribu kunyanyuka, akashika kiuno kwa kulalama. Alijikaza akanyanyuka vivyo hivyo na kisha akatupa macho yake kwenye kioo cha mbele cha gari. Ajabu alipotazama hapo akaona kipande kile cha gazeti chenye taarifa juu ya mwanamke yule aliyekumbwa na mikasa kama yake. Kipande kilekile cha gazeti ambacho kilimwelekeza kwenda kule kwa watu wa ajabu.



    Akashtuka baada ya kukumbuka mkasa alopitia. Hakika haukufaa kusimulia. Kidogo gazeti lile likapeperushwa na upepo na punde akaonekana mtu akiwa amekaa kwenye kiti cha pembeni ya dereva. Mtu huyo ametulia tuli akitazama mbele.



    Darren akashtuka kumwona mtu huyo maana hakumwona hapo awali. Hakujua wapi ametokea. Akaita kwa woga na kuuliza ni nani? Kidogo mtu huyo akageuka na kumwangazia Darren. Kumbe alikuwa ni Melissa.



    “Melissa!” Darren akafoka. “Kumbe ni wewe?”



    Alipandwa na hasira sana. Alijikuta ananyanyuka toka kwenye kiti chake na kumvamia Melissa. Akamkaba na kumtwanga ngumi mfululizo kwa hasira akiwa anafoka, “Niache na maisha yangu! Niache wewe mpuuzi! Niache! Niache!”



    Melissa akajikinga na mashambulizi makali ya Darren, lakini alipoona yanamzidia, akamtupia mwanaume huyo nyuma ya gari! Alimnyanyua kana kwamba usufi. Na Darren, kama mfuko wa saruji, akadondokea vitini na kulalamikia maumivu ya kiuno chake.



    “Niskize Darren!” Melissa akapaza sauti yake kali. Vioo vikachipua nyufa. “Kwanini hautaki kunielewa?” akauliza akiwa anamtazama mwanaume huyo kwa macho mekundu. “Kwanini unakuwa na moyo mzito na kichwa kigumu?”



    Akaongea sana lakini Darren asijali. Alikuwa anagugumia maumivu ya kiuno huku akiwa anamtazama Melissa kwa jicho la mbali. Melissa alipomaliza kujichosha kwa kuongea, Darren akamwambia kwa sauti ya chini akiwa anachuruza chozi jicho lake la kushoto, “Toka kwenye gari langu. Ondoka mbele yangu Melissa.”



    Melissa akamtazama Darren kwa sekunde nne pasipo kusema jambo. Macho yake yalidondosha machozi. Alifungua mlango wa gari na kujiondokea, Darren akashusha pumzi ndefu. Alikuwa anazidi kumwaga machozi aking’ata meno. Mwishowe alishindwa kabisa kujizuia, akalia kilio kikuu.



    Akalia sana akiwa anajiona yupo kwenye lindi kubwa la matatizo. Akalia haswa akihitaji kusafisha kifua na kichwa chake. Mwishowe alipojiona kuwa yu sawa, akasonga kwenye kiti cha dereva na kuwasha gari lake aondoke.



    Akiwa njiani akawaza sana namna gani aenende. Aliwaza sana nini afanye kujiondokea na matatizo, hata akawaza kujiua, lakini akifanya vivyo nani atakaye mwangalia mtoto wake? Mkewe alishafariki.



    Aliendesha akiwa anamwaga tu machozi. Alipofika nyumbani akajilaza kitandani kwake pasipo kumtazama mwanaye. Alikuwa anawaza sana. Ilipofika majira ya usiku, Isabel alimpigia na kumwomba waonane.





    **

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Usiku wa saa tatu ….



    Kulikuwa kumetulia kabisa, ungeweza kusikia mdomo wa Isabel ukitafuna. Mwanamke huyo aliyekuwa amevalia suti rangi ya zambarau alikuwa ameshikilia sambusa mkononi mwake na glasi ya sharubati ikiwa mezani.



    Mbele yake alikuwa ameketi Darren akiwa na glasi ya mvinyo mwekundu pekee. Hakutaka kula maana hakuwa na hamu wala kujisikia kufanya hivyo, uso wake ulikuwa umepoa, mara nyingi akitazama watu wanaoingia na kutoka eneo hilo walilopo. Hakuwa sawa.



    Kidogo Isabel akamshtua na kumuuliza, “Utakuwa kwenye hali hiyo mpaka lini, Darren?”



    Darren akaminya lips zake asiseme kitu. Alitazama glasi yake ya kinywaji kwa mawazo.



    “Inabidi uniruhusu nikusaidie Darren. Tafadhali.”



    Bado Darren hakusema jambo. Isabel akanywa sharubati yake na kisha akajifuta mdomo kwa ‘tissue’.



    “Darren ukiendelea hivi utashindwa kufanya kazi zako. Maisha yako yatapotea. Serious, inabidi ubadilike. Niambie nini tatizo.”



    Darren akanywa kwanza mafundo mawili alafu akashusha pumzi ndefu kabla hajasema, “Unajua hapa karibuni nimepitia mambo makubwa sana. Nadhani badi sijapata muda wa kutulia. Bado akili yangu haijakaa sawa.”



    “Najua, Darren,” akasema Isabel. “Najua umepitia milima na mabonde hapa karibuni. Lakini inabidi uache vitu viende, sawa? Hauwezi kuishi hivi milele? Hauoni namna unavypungua kwa mawazo? Inatosha Darren. Mfikirie mwanao. Vipi kama ukipatwa na tatizo, atakuwa kwenye hali gani?”



    Darren akakosa majibu. Alifikicha macho yake akashika tama.



    “Sikia, Darren. Ningependa niwe karibu zaidi na wewe. Naomba uniruhusu,” Isabel akapendekeza.



    “Ukaribu kiasi gani, Isabel?” Darren akauliza. “Kwani hapa hatuko karibu?”



    “Tuko karibu lakini nataka kuwa karibu zaidi. Naomba uniruhusu Darren. Nataka kuwa karibu na wewe zaidi.”



    Wakatazamana kwa kama sekunde tano. Kulikuwa na kitu machoni mwa Isabel.



    “Unaweza ukaja kuishi kwangu,” Isabel akapendekeza. “Naishi mwenyewe pamoja na wafanyakazi. Nadhani nitakuwa na wigo mpana wa kukusaidia. Mtoto wako pia hatapata shida. Unasemaje Darren?”



    Darren akabinua mdomo wake. Akanyanyua glasi ya kinywaji na kupiga mafundo mawili tena kisha akamtazama Isabel machoni.



    “Hapana, Isabel. Haiwezi kuwa haraka kiasi hicho.”



    “Nini tatizo?” Isabel akauliza kwa kujiamini. Macho yake makali yalikuwa yanamtazama Darren barabara.



    “Si kwamba kuna shida,” Darren akajibu. “Ila tu sijajiandaa kufanya hivyo. Hauoni kama ni hatari?” Isabel akatikisa kichwa.



    “Kwa upande wangu, sioni kama kuna shida. Sijajua kwako.”



    “Nipe muda nifikirie zaidi juu ya hilo. Siwezi harakisha.”



    “Sawa. Muda gani unakutosha kufanya vivyo?”



    “Nitakutaarifu, usijali.”



    Lakini jibu hilo halikumridhisha Isabel. Alipokunywa fundo moja kumalizia kinywaji chake akauliza, “Kwanini usinipe muda halisia, Darren. Huoni unaweza kuningojesha milele kwa kauli hiyo?”



    Basi Darren kwa kulazimika, akasema mpaka juma lijalo atakuwa tayari ameshampatia jibu. Angalau Isabel akafurahi. Wakamalizia maongezi yao kwa kuongea biashara juu ya ile nyumba ya bibi yake Darren kule ‘countryside’, wakaafikiana mpaka bei, ambapo ilikuwa pesa kubwa sana.



    Kwa mawazo ya Darren aliona ni kheri akamuuzia Isabel nyumba hiyo kwani haikuwa na faida tena kwake, lakini zaidi apate kiasi cha pesa kitakachomwezesha kuwa na makazi mapya, makazi ambayo yatakuwa salama kwake na familia yake. Aliwaza pengine akihama, anaweza akapata pumziko la kichwa chake.



    “Kwahiyo utaingiza lini hiyo pesa?” Akauliza.



    “Kesho mchana,” Isabel akamjibu. Kidogo Darren akashangazwa, kilikuwa ni kiasi kikubwa cha pesa kupatikana haraka namna hiyo!



    “Kuna shida, Darren?”



    “Hapana. Hamna tatizo kabisa.”



    “Sawa. Kesho tazama akaunti yako kuanzia majira ya saa sita mchana.”



    Wakakubaliana hilo na basi kama alivyomleta, Isabel akamrejesha Darren nyumbani kwake, lakini kabla hajashuka, akamshika mwanaume huyo mkono wake wa kushoto na kumtazama kidogo.



    “Kama kutakuwa na tatizo nijulishe Darren.”



    Darren akatikisa kichwa chake kuafiki alafu akashuka toka kwenye gari na kwenda ndani. Kulikuwa ni kimya. Alishangaa kukuta hali hiyo. Akamwita dada wa kazi mara tatu pasipo majibu. Akapata shaka kidogo. Akanyanyuka na kwenda vyumbani, akakagua kila chumba lakini hakumwona dada wa kazi wala mtoto wake. Hapa shaka lake likakua zaidi.



    Akajaribu kupiga simu ya dada wa kazi, ikaita, ila alipotulia na kuskiza vema akagundua simu hiyo inaitia ndani. Alipoenda chumbani kwa dada huyo akabaini simu ilikuwa imefunikwa na shuka. Sasa ameenda wapi na mtoto?



    Tumbo likaanza kumsokota.



    Alitoka ndani kwake akaenda kuuliza majirani kama wamemwona msichana huyo na mtoto wake lakini hakupata kitu. Alihisi kuchanganyikiwa. Alirejea ndani akaketi akiwaza na kuwazua. Muda ukaenda mpaka majira ya saa tatu usiku.



    Sasa akaona ni vema atoe taarifa polisi kwa uchunguzi zaidi. Akatoa kila taarifa aliyoifahamu na polisi wakaanza kazi yao. Lakini kwenye majira ya saa nne usiku, dada wa kazi akarejea akiwa na mtoto.



    Dada huyo mkononi alikuwa amebebelea vitu vya mtoto na kwa kutumia kibebeo maaulum alikuwa amembelea mtoto kifuani mwake. Darren akafurahi sana kumwona mwanae. Akamkumbatia kwanguvu na kumuuliza dada wa kazi wapi alikwenda kwa muda wote huo.



    “Nilienda kumchukulia mtoto mahitaji yake,” dada akajitetea. “Lakini nilikutana na msongamano mkubwa wa magari sababu ya ajali. Samahani sana.”



    Baada ya maelezo hayo, dada huyo akaenda chumbani kwake akimwacha Darren na mwanaye pale sebuleni. Darren akatoa taarifa polisi juu ya kumpata mwanaye.



    “... Nashukuru sana, nitakuwa mwangalifu zaidi siku nyingine.”



    Alipokata simu ndipo akagundua kuna kitu kwa mwanaye.





    Nyuma ya mgongo wa mwanaye, chini kidogo ya bega la kushoto, aligundua kuna chapa fulani ndogo. Chapa hiyo ilikuwa nyeusi yenye ishara kama ya msalaba lakini ikiwa na mikono miwili.



    Hakujua maana ya chapa hiyo lakini alijikuta akiwa na wasiwasi nayo. Alijaribu kuifuta kwa kutumia kidole chake, haikufutika. Akajaribu kumfuta na kitambaa bado napo haikufutika, ilikuwa ni alama ya kudumu!



    Upesi akamuuliza dada wa kazi apate kujua nini kimemtokea mtoto. Lakini dada, akiwa ameparamiwa na uso wa hofu, akajitetea sana. Hakuwa anafahamu lolote. Hakuwa anajua hata kama mtoto ana chapa hiyo? Amemwogesha jana yake na hata siku hiyo asubuhi lakini hakuona alama kama hiyo.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Darren akatingwa na maswali lakini pia na hofu. Hakuhisi kama mwanaye yuko salama. Kila mara alitazama alama hiyo na kujiuliza maswali mengi kichwani. Mwishowe aliona ni kheri akafanya jitihada zaidi kung’amua chapa hiyo na hapo ndipo akazama kwenye mtandao na kusaka alama ile baada ya kuiweka kwenye mashine yake.



    Baada ya muda kidogo akapata kuona taarifa chache juu ya chapa hiyo ikiwa inahusishwa na habari za zamani sana kuhusu huko Uajemi tena ni ishara aghalabu ya majini!



    Alipotafuta sana akabaini kuwa mwanawe hakuwa mtu wa kwanza kuwa nayo, takribani watu watatu walikuwa nayo, ila mwisho wao wote ilikuwa ni kifo! Alipohangaika zaidi kutafuta mengineyo, akapata kukutana na mwanamke mmoja ambaye mwanaye alikuwa na chapa hiyo. Alituma hilo swala mtandaoni kuomba ushauri.



    Basi hilo likawa kama neema kwa Darren. Alitafuta zaidi taarifa za mwanamke huyo akafanikiwa kupata anwani yake, akapanga kesho yake akamtafute amwambie zaidi kuhusu hiyo chapa.



    Alihofia sana juu ya mwanaye. Na kwa hofu hiyo akataka alalae nae ndani ya chumba chake.



    Ulipofika usiku wa manane, Darren akiwa amelowea kwenye usingizi mzito, na pia nyumba ikiwa imetulia tuli sawa sawa na mtaa mzima, taratibu mlango wa chumba alalacho dada wa kazi, ulifunguliwa na kisha ukatuama pasipo lolote kutokea.



    Kulikuwa kimya.



    Zilipopita kama sekunde tano, ndipo mkono uliobebelea kisu ukatoka kwenye mlango huo. Bada ya punde, ukafuatia na mguu na kisha mtu mzima kabisa. Alikuwa ni yule dada wa kazi.



    Aliyatoa macho yake akikodoa. Alitazama kushoto na kisha kulia, alafu akauendea ule mlango wa chumba cha Darren. Alipoufikia, hakugonga, lah! Akapindua kitasa taratibu na mlango huo ukafunguka. Alipousogeza vya kutosha, akatulia hapo akisimama.



    Zikapita kama sekunde nne. Basi taratibu akazamisha mguu wake ndani ya chumba, na taratibu sana, akaweka nyayo zake sakafuni akisonga. Alimwendea mtoto na kumpakua toka kwenye kitanda chake. Lakini mikono yake ilikuwa ya baridi sana. Alipomshika mtoto tu, akaanza kulia.



    Akakodoa kumtazama Darren. Darren alikuwa amelala bado fofofo. Lakini sauti ya mtoto iliyokuwa inaendelea kupaza na kupaza ilimshtua sasa akaamka na kuangaza.



    alipotazama kwenye kitanda cha mtoto, hakukuwa na kitu. Kitanda kilikuwa tupu kikianza kujenga ubaridi! Akachanganyikiwa sana. Alitazama kushoto na kulia kwake asione kitu, mlango ulikuwa umefungwa, ila sauti ya mtoto bado akiisikia!



    Sauti hiyo ilikuwa ikiishilia!



    Haraka akatoka kitandani na kudaka korido. Akatazama na kupekua kwa macho yake, kidogo, masikio yake yakamwambia kuwa sauti ya mtoto inatokea kwenye chumba cha dada yake wa kazi!



    Akauendea mlango huo na kubisha kwa kuutwanga ngumi. Akaukandika na kuukandika lakini haukufunguliwa. Mtoto bado aliendelea kulia!



    Akiwa amepandwa na akili za ukichaa, Darren akaubamiza teke kali mlango huo na kuuvunjia mbali. Alipotazama, akamwona dada wa kazi akiwa amemkabia mtoto kitandani kwa kutumia mkono wa kushoto na ule wa kulia ukiwa umeshikilia kisu akitaka kumchoma.



    “Tafadhali, usimuue mwanangu!” Darren akapaza sauti akimtazama dada wa kazi kwa imani. Dada akatabasamu na kusema, “Lazima afe, Darren. Hata kama nisipomuua mimi!”



    “Kwanini?” Darren akalia. “Kwanini afe? Sina kitu kingine mbali na huyo mtoto. Nambie unataka nini nitakupatia!”



    Dada akatabasamu almanusura kucheka. Alimtazama mtoto kisha akayarudisha macho yake kwa Darren na kusema, “Sitaki chochote Darren. Kama ningekuwa nataka chochote kile basi ningekitafuta na kukichukua mwenyewe. Kwa sasa ninachotaka ni roho ya huyu kiumbe tu, si kingine!”



    “Lakini amekukosea nini?” Darren akauliza. Macho yake yalikuwa mekundu yakikaribia kudondosha chozi.



    “Hajafanya kitu,” Dada akajibu akitikisa kichwa. “ila si mali yako tena. Huyu ni mali ya majini, na ni wa kufa tu!”



    Dada aliposema hayo akamkandika mtoto kisu cha kifuani, chote kikazama na kutosha kumfanya mtoto mfu. Darren akalia sana. Akakurupuka toka kitandani mwake na kumtazama mwanaye pembeni. Nalikuwa ni ndoto. Mtoto alikuwa yu kwenye kitanda chake ila akilia sana.



    Upesi akamnyanyua na kujitahidi kumbembeleza … sh!-sh!-sh!-sh!-sh!-sh! … lakini alipotazama dirishani akabaini kuwa li wazi. Akalisongea na kutazama nje kama kuna lolote lile, hakuona jambo. Mtaa ulikuwa umetulia sana. Ni upepo wa baridi ndio ulikuwa ukipuliza tena kwa mbali.



    Akalifunga dirisha hilo, bado mtoto akilia, alipomaliza akasikia hodi mlangoni mwake. Kidogo mapigo yake yakaruka. Akiwa amemshikilia mtoto wake vema, akapaza sauti kuuliza,



    “Nani?”



    “Dada wa kazi!” sauti ikamjibu toka mlangoni. Kidogo akajawa na mashaka.



    “Unataka nini?”



    “Nimemsikia mtoto analia. Vipi kuna shida?”



    “Hapana. Hamna shida.”



    “Naweza kukusaidia kumbembeleza?”



    Darren akasita kwanza.



    “Hapana, ahsante. Nitambembeleza mwenyewe.”





    ITAENDELEA

Blog