Search This Blog

UNA NINI LAKINI MELISSA - 5

 

    Simulizi : Una Nini Lakini Melissa

    Sehemu Ya Tano (5)





    Baada ya hapo sauti ya dada haikusikika tena bali mtoto akiwa analia tu. Darren akaendelea kumbembeleza mwanaye akimsihi anyamaze kwani usiku umekuwa mkubwa na yeye amechoka sana. Kwa kama lisaa limoja, mtoto akaendelea kulia tu, akipunguza sauti na kurudi tena upya.



    Darren akachoka sana kumbembeleza, mikono ikawa inamuuma, macho yanamsaliti kwa kuwa mazito, kichwa nacho kinachoshwa na sauti kali ya mtoto.



    Mlango ukagongwa tena.



    “Nani?” akauliza kwa sauti ya uchovu.



    “Dada wa kazi!” sauti ikamjibu toka mlangoni.



    “Unataka nini?”



    “Mtoto ana shida gani?”



    “Amekurupuka tu toka usingizini, usijali. Unaweza kulala.”



    “Naweza kukusaidia?”



    “Hapana! Usijali, nitambembeleza mwenyewe mpaka alale.”



    Basi baada ya hapo sauti ya dada wa kazi haikusikika tena, Darren akaendelea kumbembeleza mtoto. Kwa kama nusu saa akawa anafanya zoezi hilohilo tu. Kila alipojaribu kumweka mtoto kitandani ambembelezee hapo, ikawa tabu zaidi, mtoto aliongeza kilio.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hakujua sasa cha kufanya. Kila mtindo alitumia lakini haikusaidia. Ilifikia kipindi akawa anapitiwa na usingizi ingali amesimama. Alimweka mtoto kitandani kwa kulazimisha akaendelea kumbembeleza hapohapo, kidogo akapitiwa na usingizi.



    Kama baada ya dakika mbili akakurupushwa na hodi ya tatu mlangoni mwake. Akauliza, “Nani?”



    “Dada wa kazi!”



    “Unataka nini?”



    “Mtoto anasumbuliwa na nini?” dada akauliza.



    “Si nilishakwambia!” Darren akafoka kidogo.



    “Naomba nimbembeleze,” sauti ya dada ikaomba.



    “Nimesema nambembeleza mwenyewe. Hukunielewa?”



    Kukawa kimya kidogo.



    Punde sauti ya dada ikasema tokea mlangoni, “Utanipa nimbembeleze ama nije nimchukue mwenyewe?” mara hii sauti ilikuwa na amri ndani yake.

    .



    Darren akajawa na hofu. Akamnyakua upesi mtoto wake na kumfichama kwenye mikono yake akiwa anatazama mlango kwa hofu. Punde mlango ukaanza kubamizwa kwa nguvu na kwanguvu! Darren akajaribu kuteka simu yake atoe taarifa polisi lakini hakuiona. Kwa muda alikuwa kama mtu aliyechanganyikiwa. Hakujua cha kufanya.



    Mlango ukaendelea kubamizwa na kubamizwa. Mwishowe ukaanza kudhoofu na kubomoka. Vipande vyake viliruka huku na huko. Ilikuwa ni ajabu mbomoaji alikuwa anatumia nyenzo gani kufanyia zoezi lake hilo.



    Darren alichofanya ni kutwaa kipande kidogo cha mbao ya mlango na kubebelea kama silaha. Ni ajabu kama mtu ameweza kubomoa mlango atamzuiaje kwa kipande cha mbao, lakini alikuwa na imani.



    Mkono wake uliobebelea kipande hicho cha mbao ulikuwa unatetemeka. Macho yamemtoka na paji lake la uso linatiririsha jasho.



    “Ni nani wewe?” Darren akauliza kwa sauti yenye kusita. Hakujibiwa. Kilichokuwa kinafanyika ni mlango kubamizwa tu! Tena kubamizwa kwanguvu mno.



    Kidogo, kwasababu ya hofu na kukurupushwa usingizini, mtoto naye akaanza kulia. Alikuwa analia kwanguvu haswa kiasi cha kumchanganya Darren. Ingawa Darren alimsihi anyamaze, haikusaidia kitu.



    Mwisho wa siku mlango wote ukawa upo chini na mlangoni akiwa amesimama mwaname anayechuruza damu mikononi. Mwanamke huyo si mwingine bali dada wa kazi. Mikono yake ilikuwa imejeruhiwa vibaya mno kwa kubamiza mlango hata kuvunjika. Macho yake yalikuwa makubwa yanayong’aa, uso wake umepauka kuwa mweupe.



    Alimtazama Darren kisha akainamisha shingo yake kwenda kushoto na kulia, kisha kulia na kushoto. Akamnyooshea kidole Darren pasipo kusema jambo. Alafu kama mtu aliyegandishwa na barafu, akaanza kupiga hatua kumwendea Darren.



    Darren akamtisha na kipande chake cha mbao, “Kaa mbali!” akafoka. “Kaa mbali na mimi!” lakini mwanamke yule hakuwa anasikia wala kujali, akaendelea kusonga kumfuata Darren, na alipomkaribia akanyoosha mikono yake yote miwili na kisha akasimama.



    Kukawa kimya kidogo. Darren akamtazama mwanamke huyo kwa hofu na maulizo. Naye mwanamke huyo akawa anamtazama Darren kwa macho ya kumpembua. Kidogo akashusha macho yake kwa mtoto na kumtazama kwa sekunde kadhaa, alafu akasema kwa sauti ya kukoroma, sauti ya chini, “namtaka huyo mtoto.” alafu akahema kwanguvu na kusema kwa sauti ya hewa, “Nipatie, nami nitaenda nisirudi nyuma!”



    “Wewe ni nani?” Darren akauliza akiwa anamshikilia vema mwanaye. Alikuwa amejiminyia kwenye kona akitamani kutoboa ukuta atokee nje.



    Yule kiumbe akamtazama Darren alafu akapindishia shingo yake kushoto. Aliporejesha shingo yake kulia, akasema, “Mimi Melissa.”



    “Melissa!” Darren akastaajabu. Hakujua alipata wapi nguvu ila alijikuta akisimama huku akitusi na kulaani. “nimekwambia kaa mbali na mimi Melissa!” punde akazabwa kofi lililomtupia ukutani yeye na mwanaye. Kwa muda kidogo akashindwa kuelewa kinachoendelea. Kwa mbali alisikia sauti ya mwanae ikilia sana lakini hakuwa anaweza kufanya kitu.



    Kama baada ya dakika tano, akiwa ameanza kupata nguvu, akasikia sauti yaita,



    “Hey! Helloooow!” kidogo mwanga ukatua kwenye macho yake yalofumba, akayafinya na kuyafumbua akiwa anajikinga na mkono wake wa kuume.



    “Upo sawa?” alisikia sauti inauliza. Kidogo akabaini sauti hiyo inatokea dirishani. Walikuwa ni majirani, wanaume wawili. Mmoja alikuwa amebebelea bunduki kubwa na mwingine amebebelea gongo kubwa na kurunzi. Walikuwa wamesikia zile kelele na walikuja kutazama jirani yao amepatwa na nini.



    Kabla Darren hajajibu kitu, alitazama kwanza kando yake kumtafuta mwanaye. Akamwona akiwa amelala kama hatua tatu tokea alipo. Alikuwa kwenye ukimya wa mbao. Na dada wa kazi alikuwa amelala kwa pembeni yake naye akiwa kimya.



    Upesi akamfuata mwanaye na kumtazama. Hakuwa na dalili ya uhai. Alimwita na kumwita lakini ikiwa bure, mtoto hakuitika kwa kucheka wala kulia. Darren akapatwa na hofu kubwa sana ya kumpoteza mwanaye. Alimtikisatikisa aone kama ataamka lakini napo haikusaidia. Mtoto alikuwa amenyamaza. Alikuwa amenyazama milele.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Darren akapiga magoti na kugugumia kwa kilio. Alipata hasira sana. Alinyanyuka kama mbogo akamwendea dada wake wa kazi na kumvuta kwanguvu akimuuliza amemfanya nini mtoto wake, lakini dada naye alikuwa kimya. Hakuweza kuongea wala kujitetea kwa njia yoyote ile.



    Darren asijali, akaanza kumuadhibu dada huyo kwa kumkandika mateke. “Shetani! Shetani! Shetani mkubwa wewe! Nitakuua!”



    Kama si majirani kuvunja mlango na kuja kumshika, sijui hatma ilikuwa ni nini. Waligundua dada wa kazi alikuwa yu mzima, ila kama mtu aliyekuwa kwenye ‘coma’, hali mfu ya kupoteza fahamu, ila mtoto alikuwa amekwishafariki.



    Basi dada wa kazi akawahishwa hospitali kwa matibabu zaidi. Mtoto naye akapelekwa huko kuhifadhiwa kwa ajili ya mazishi, na Darren pia, kwakuwa alihisiwa anaweza akawa si mzima, naye akapelekwa hospitali.





    **



    Baada ya juma moja …



    Darren alikuwa ameketi kwenye kingo ya bahari. Alikuwa amevalia bukta na miguu yake ikiwa tupu pasi na viatu.



    Upepo ukimpuliza taratibu, alikuwa anatazama bahari kwa umakini. Kuna kitu alikuwa anawaza kichwani ingawa macho yake yalikuwa yanatazama mawimbi ya bahari. Mkono wake wa kuume ulikuwa umebebelea mchanga, ila akiwa ameuminya kana kwamba anataka kuukosesha hewa.



    Macho yake mekundu yalitazama mbali na karibu ya bahari. Yalitazama kushoto na kisha kulia ya bahari alafu akashusha pumzi ndefu. Akanyanyuka na kuanza kurandaranda.



    Alitembea akiwa anawaza na kuwazua kichwani mwake. Kila alipofunga macho alimwona mwanae, alimwona mkewe. Ilikuwa ni ajabu na ghafla kwake. Kuna muda hakuwa anaamini kama Josephine hakuwapo naye, wala mtoto wao. Ilikuwa inamuwia ugumu sana kuamini kuwa yu mwenyewe hatimaye.



    Alihisi maisha yake yanaparanganyika kama kioo kilichobondwa na jabali. Alikuwa anahisi hana umuhimu wowote maishani hivi sasa. Alikuwa anajihisi mfu anayetembea.



    Alikunja ngumi yake akiendelea kutembea. Aling’ata meno yake na kutazama bahari tena, alafu punde akasema, “Melissa!” kwa sauti ya kufifia. Akarudia tena, “Melissa. Melissa. Melissa!” alafu akaapa, “Nitakumaliza kwa mkono wangu mwenyewe. Nitakumaliza Melissa!” alipomaliza kusema maneno hayo macho yake yakawa yanamwaga machozi. Alishindwa kujizuia kuumia. Moyo wake ulikuwa unavuja damu.



    Jua likiwa linaanza kuwa kali kumaliza asubuhi, Darren akajirejesha kwenye gari lake na kutimka kuelekea upande wa magharibi. Alitembea kwenye gari kwa takribani masaa matatu kabla ya kuja kukomea kwenye nyumba kubwa namba 4089 kibaoni. Nyumba ya mwanamke yule aliyemwona mtandaoni kwa swala la mtoto wake kuwa na chapa mwilini.



    Kabla hajashuka na kuzama humo, akalipekua kwanza jengo hilo kwa macho yake mepesi, kisha akashuka na kuliendea. Alipogonga kidogo akafunguliwa na mlinzi, akajitambulisha na mlinzi akamruhusu kuingia ndani maana alikuwa na miadi na mwenye nyumba.





    “Nilipata shida sana. Nilitafuta kila namna lakini haikusaidia. Na nakumbuka vema ikiwa ni usiku wa manane, nikampoteza mwanangu wa pekee!”



    Darren akataka kujua zaidi kumhusu mwanamke huyo. Mbali na mtoto je yeye alishawahi kukumbwa na kadhia yoyote ile? Basi mwanamke yule akaeleza kuwa kwa kitambo kifupi baada ya mama na baba yake kufariki, ndipo alipoanza kuona mambo fulani ya ajabu ndani ya mji wao. Mwanzoni alikuwa anadhani anawehuka na labda ana laana na ule mji, hivyo akafanya kuhama aende mbali.



    Alipoenda huko, akatuama na kuanzisha familia ambayo iliishi kwa amani mpaka pale mambo yalipokuja kuibukia katika namna ambayo hakuwa anaweza kuelewa vema.



    “Ninachokumbuka ni kwamba, baada ya tetemeko kubwa la ardhi lilitokea miaka mitano nyuma, maisha yangu yakaanza kubadilika kwa wepesi sana. Sikuwa tena mtu wa amani bali kuona vituko na viroja. Mtu wa kuona mambo ya ajabu yasiyokuwa na mithili. Ajabu ni kwamba, baada ya mtoto wangu kufariki, mambo hayo yalipotea mpaka sasa.”



    “Na vipi kuhusu mume wako?” Darren akadadisi. Charlie akatabasamu kwanza ila macho yake yakiwa kinyume. Alitazama chini kwa sekunde chache kabla hajabinua kinywa chake na kusema, “Alikuwa mwanaume niliyekuwa namhitaji. Mwenye kujali na kujua kupenda. Nilijihisi nimekamilika nilipokuwa naye. Alinifanya nisahau kifo cha wazazi wangu kwa muda kwani alikalia sehemu tupu ambayo iliachwa wazi.”



    Akadondosha chozi. Akalifuta kwa kidole chake onyeshi kabla hajaendelea kuongea, “nilimpoteza kwenye ajali!” akapandisha mabega yake akisema, “sijui nini kilitokea lakini aliacga daraja na kutumbukia baharini. Waokozi walipokuja kumtazama, hakuwa hai tena.”



    “Gari lake lilipata hitilafu?” Darren akauliza.



    “Sidhani,” Charlie akajibu. “Gari lake lilikuwa sawa kabisa isipokuwa tu sehemu ambayo iligonga daraja. Sijajua kumhusu yeye. Sijajua alikuwa kwenye hali gani. Ila kwa mujibu wa shuhuda wa tukio, mume wangu alibamiza kioo chake cha pembeni kwanguvu kabla gari halijapoteza mwelekeo na kudumbukia.”



    Kwa namna moja Darren akaona simulizi ya huyo mwanamke inawiana na ya kwake. Kwa kutaka kuhakikisha zaidi, akamuuliza Charlie, “Kuna mtu yeyote ambaye ulikuwa naye kwenye mahusiano kabla ya mumeo? Namaanisha mpenzi wako wa kwanza?”



    Charlie akafikiri kidogo kabla hajasema, “Niliwahi kuwa naye. Ila ni kipindi cha zamani za utotoni. Sichukulii mahusiano yale kama yalikuwa serious.”



    “Je haujawahi kumwona mwanaume huyo uliyewahi kuwa naye kwenye mahusiano? Yaani baada ya kuoana na mumeo? Au kipindi chochote kwa namna yoyote?”



    “Hapana,” Charlie akakataa. “Sijawahi kuonana naye tangu kipindi hicho.”



    Hapa kidogo Darren akajiona ni wa tofauti na Charlie. Mbona yeye anasumbuliwa na Melissa? Basi akaamua naye kumshirikisha Charlie kuhusu habari zake. Alipomaliza kumweleza kila kitu, Charlie akamuuliza Darren, “Unapajua anapokaa huyo Melissa?”



    “Ndio, napajua,” Charlie akajibu.



    “Naweza nikaonana naye?” Charlie akauliza akiwa ametoa macho kidogo.



    “Unahitaji kuonana naye?”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ndio, kama itawezekana.”



    Darren akanyamaza kidogo kisha akasema, “Si mtu mzuri kama unavyoweza kudhani.”



    “Najua,” Charlie akamkatiza. “Sitegemei awe mtu mzuri, ila ningependa kuonana naye.”



    “Kwanini? Huoni utakuwa umejiweka kwenye hatari?”



    “Hatari ipi, Darren? Nimepoteza mume na mtoto wangu, kuna hatari nyingine zaidi ya hiyo?”



    Kimya kidogo. Charlie akaendelea kuzungumza, “Nadhani kuna maswali yangu atakuwa na majibu nayo.”



    “Yapi hayo?”



    Hapa Charlie akamweleza Darren kuwa anahisi mama yake alikuwa ni mtu mwenye agano tokea nyuma. Mara kwa mara mama yake alikuwa anamwambia kuwa maisha yake hayatakuwa ya furaha kwakuwa yeye ni kizazi cha shetani. Damu yake inachembechembe za majini. Alipotaka kujua zaidi, mama yake hakumweleza kwa kumwambia muda bado mpaka pale utakapowadia na basi atajua.



    “Una picha ya mama yako?” Darren akauliza. Charlie akafungua simu yake na kumwonyesha Darren picha ya mama yake, “huyu hapa wa kwanza upande wa kulia.” darren alipotazama vema, akagundua sura ya mama huyo haikuwa ngeni. Ilikuwa ni sura anayoijua. Aliionea wapi? Akajiuliza akirusha macho huku na kule.



    “Vipi, Darren?” Charlie akamuuliza.



    “Nahisi namjua huyu mtu,” Darren akajibu akiendelea kufikiri na punde akakumbuka. Sura hiyo aliionea kwenye ile picha ambayo aliipata kwenye jengo la bibi yake! Akamweleza Charlie habari hiyo.



    “Kweli?” Charlie akastaajabu.



    “Ndio, ni kweli!” Darren akaapa. Basi Charlie akafikiria kwa udogo na kusema, “Darren, nadhani sasa utakuwa unaona kuna haja gani ya kuonana na Melissa. Yeye anaweza kutueleza mambo haya kwa undani.”



    Darren akashika kichwa, “Lakini Melissa si mtu mzuri hata kidogo. Ameyfanya maisha yangu yawe magumu kupita kiasi. Sikutaka kabisa kuhusiana naye.”



    Charlie akauweka mkono wake begani mwa Darren, “sikia, Darren. Hatuna machaguzi hapa. Na kati ya wewe na mimi, hakuna mwenye maelezo ya kumtosha mwenzake isipokuwa huyo Melissa. Hima twende tukamwone!”



    Darren akafikiri kidogo kabla hajanyanyuka na kumpakia Charlie kwenye gari yake, safari ikaanza. Walitembea kwa muda wa kama nusu saa pasipo kuzungumza. Charlie ndiye alikuja kuuvunja ukimya kwa kumuuliza Darren, “Ulimpenda Melissa?”



    Darren akanyamaza kwanza kama mtu anayepangilia jibu kichwani kisha akasema kwa ufupi, “Ndio.”



    “Na yeye alikupenda?” Charlie akauliza akimtazama Darren anayatazama mbele.



    “Sidhani,” Darren akajibu.



    “Haudhani?”



    “Ndio. Kama angekuwa ananipenda basi angeniweka bayana kila kitu,”



    “Kila kitu kama kipi Darren? Kuwa yeye ni jini aliyeishi na bibi zetu tuokea huko nyuma? … ungemwelewa? Ungeendelea kuwa naye?”



    “Charlie, sijui haya mambo yaendavyo. Ila nisingeweza kuishi na Melissa zaidi. Unawezaje kufanya hivyo punde unapohisi kuwa uliyenaye si binadamu?”



    Charlie akanyamaza asinene tena. Wakaumaliza huo mjadala. Kwenye majira ya saa tano za usiku wakawa wamewasili kwenye makazi ya Robson. Hapo waliposhuka, Charlie akauliza, “Hapa ndipo kwake?”



    “Hapana, bali kwa mpenzi wake! Nadhani atakuwapo hapa,” Darren akaji bu wakisonga.



    “Na vipi kama hatokuwapo?” Charlie akauliza.



    “Basi mpenzi wake atakuwa anajua alipo,” Darren akamalizia kauli na kubisha hodi mara tatu. Punde akafunguliwa na Robson ambaye alishangaa kumwona Darren hapo wakati huo.



    “Vipi, Darren?”



    “Naweza kuonana na Melissa?” Darren akaenda moja kwa moja kwenye lengo lililomleta.



    “Vipi, kuna tatizo?” Robson akauliza.



    “Ndio, lipo,” Darren akajibu na kisha akarudia tena kauli yake, “Naweza kuonana na Melissa?”



    Robson akawafungulia mlango wakaingia ndani. Ila walipoketi, simu ya Darren ikaingiwa na ujumbe. Alipoutazama kuusoma, ulikuwa unatokea kwa Melissa.



    “Sipo hapo. Nikuteni fukweni,” ujumbe ulisoma.



    Upesi Darren na Charlie wakaelekea huko ufukweni ambapo Melissa alikuwapo, na kweli wakamkuta akiwa ameketi mchangani akitazama maji ya bahari. Mbali na hivyo kulikuwa kimya sana isipokuwa upepo.



    Darren akamwita Melissa akiwa anamtazama, naye Melissa akamtazama na kumkaribisha, “Nadhani hapa ni eneo zuri la kufanyia maongezi.” Darren na Charlie wakaketi wakimweka Melissa katikati yao.



    “Ulimwambia Robson kama nipo huku?” Melissa akauliza.



    “Hapana, hajui hilo,” Darren akajibu kisha akamuuliza Melissa kama anamjua mwanamke yule aliyekuja naye, yaani Charlie. Pasi na kumtazama, Melissa akasema anamfahamu hata kabla hajaja hapo.



    Aliposema hayo akamtazama Darren. Macho yake yalikuwa tayari yameelekea kuwa mekundu. Akamshika mkono na kumuuliza kwa upole, “Darren, utasadiki nitakayokuambia?”



    Darren alipojibu swali hilo, Melissa akamuuliza na Charlie swali hilohilo. Alipolijbiwa ndipo akaanza kunena. Darren na Charlie wakawa wametega masikio yao vema kabisa. Japokuwa upepo ulikuwa unapuliza, bado sauti ya Melissa ilisikika vema.



    “Pengine mimi naweza nikawa mtu mbaya sana kwenye vichwa vyenu. Hamtaki kuniona na sifai kuwa hai wala kuwa mbele yenu hapa nilipo. Ila …” alipokomea hapo akamtazama Darren, “Kama si upendo wangu kwako, Darren. Basi usingalikuwa hai mpaka sasa. Haujui ni makovu mangapi umenisababishia kwa maneno yako lakini sikuwahi kuacha kukupenda.”



    Aliweka kituo na kutazama bahari kwa sekunde kama sita akiwa kimya. Kuna kitu alikuwa anawaza kichwani mwake. Na basi alipojiona yu tayari ndipo akaendelea kunena ya kuwa hapo zamani kabisa ya miaka takribani mia tatu iliyopita, walikuwa kwenye familia kubwa ya bwana Roddeth. Bwana huyo alikuwa ni mtu mwenye nguvu kubwa na mwenye kuhofiwa sana.



    Alikuwa na nguvu za ajabu. Watu wangekusanyika kwake awasaidie matatizo mbalimbali lakini kwa sharti la kutoa sadaka. Alikuwa si mtu wa kawaida bali jini, lakini alistahimili kuishi miongoni mwa binadamu. Na kwa uzao wake basi akapata watoto watano wa kike ambao kwa mujibu wa maelezo ya Melissa, mmoja wa hao watoto alikuwa ni yeye, na wengine ni pamoja na bibi yake Darren na Charlie na wengineo wawili.



    Walikuwa ni watu wapendanao mpaka pale siku moja baba yao alipokufa na kugawa mali zao pasi na usawa. Walichukiana na kila mmoja akaelekea upande wake. Lakini kwasababu Melissa alikuwa ni kipenzi kikubwa wa baba yao basi ingali baba yupo kwenye kitanda chake cha kifo alimkabidhi mwanaye huyo kito cha moja ya mkufu wake akimwambia, “Utaishi milele, mimi safari yangu naona ikomee hapa.”http://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    Alificha kito hicho kwa namna zote ili ndugu zake wasije kukiona na kumpokonya. Na kwake haikuwa ngumu sana kwani walikuwa tayari wameshatengana na kila mmoja akaenda njia yake binafsi.



    Basi miaka ikapita kila mmoja akiwa na chuki na mwenzake na uadui pia. Kila mmoja akapata kuishi kwa namna ajuavyo huko mbali. Wengine wakafikia kuanzisha maisha kwa kuwa na mahusiano na binadamu.



    “Halikuwa jambo jema. Baba yetu wakati yu hai alikuwa akitusisitiza juu ya hilo. Endapo tutakapokuwa kwenye mahusiano na binadamu basi si kwamba tutawafanya watoto waingie kwenye damu yetu isiyo ya kawaida, bali damu hiyo itawawinda na kuwaangusha,” alisema Melissa.



    Lakini kwasababu za mapenzi, wenzao wawili walizaa na binadamu. Na kama ilivyokuwa neno la baba yao, watoto hao wakawa wanasumbuliwa kwa kutokewa na mambo ya ajabu wasiyoweza kuyaeleza. Mengine hata yakitishia uhai wao.



    Kutokana na hayo ndipo binadamu hao wakawa wanatafuta tiba ya kujikinga dhidi ya maajabu waliyokumbana nayo. Na kila tiba walipoipata wakaifungia kwenye vitabu walivyovihifadhi maeneo ya mbali kabisa na makazi yao. Maeneo salama ambayo hayafikiwi na binadamu.



    Vitabu hivyo vilikuwa ni vifungo vya kufunga yale yote yaliyokuwa yanawasumbua, na wakafanikiwa kufanya vivyo kwa muda.



    “Shida ni kwamba, vitabu hivyo vinakuwa si vifungo tu bali hubeba roho za wale vinavyowalinda. Hivyo pale vinapopata madhara, basi na wale waliokuwa wanavimiliki hufa kwa aina hiyohiyo ya kifo,” maneno hayo ya Melissa ndiyo yakamkumbusha Darren kifo cha mama yake kilivyorandana na moto wa msitu. Akamuuliza naye Charlie akasema kuwa mama yake alikufa kwa kuzama maji ingali alikuwa chumbani mwake! Ikiwa ni muda mfupi baada ya tetemeko la ardhi kutokea.



    “Baada ya hapo basi ndipo matatizo yenu yakaanza upya,” Melissa akaendelea soga, “Kwakuwa vifungo vilikuwa vimeenda basi ndiyo maana mambo ya ajabu yakaanza kuwatokea upya kwenye familia zenu, na itakuwa vivyo mpaka pale damu mliyobeba itakapotulizwa.”



    Darren akamuuliza Melissa, “Mbona maisha yangu yalikuwa yametulia kabla ya kuja kukutana na wewe? Mbona kila mara ninapoonana na wewe huwa nakutana na jambo baya?”



    Melissa akamtazama Darren akiwa anadondosha chozi, “Darren kamwe hautokuja kuelewa ni mangapi nilikuwa nayapitia kwasababu yako. Maisha yako kutuama kabla ya kuja kukutana na mimi haikuwa inamaanisha kuwa utakuwa sawa, lah! Na hilo halikuwa kwako peke yako bali pia kwa Charlie.



    Mambo yalianza kubadilika si kwasababu ulikutana na mimi bali kwasababu ulikuwa umepata mtoto. Kama vilevile ilivyokuwa kwa Charlie. Mlikuwa mmefufua upya agano lenu, Darren,” Melissa alisema kwa sauti ya chini alafu akatazama chini kabla hajaendelea kunena, “Kila ulipokuwa unakutana na baya lolote, nami nilikuwapo pembeni, na ndiyo maana ulikuwa unatoka ama kushinda hai. Isingalikuwa hivyo, ungeshakufa muda mrefu Darren.”



    “Na vipi kuhusu ile siku nilipoenda kwenye ile nyumba iliyotangazwa kwenye gazeti? Ilikuwa ni kweli ama ndoto kukuona pembeni ya gari yangu?” Darren akauliza. Melissa, bado akiwa anamtazama mwanaume huyo, akamjibu, “Yote yalikuwa ni uhalisia, Darren. Na ni mimi ndiye nilikurudisha pale kwenye gari lako upesi baada ya kuzidiwa na wale wadhalimu. Lakini uliponiona pembeni yako haukunipa muda nikajitetea, bali ukanijaza shutma na kunifukuza!”



    “Kwanini hukuniambia yote hayo, Melissa?” Darren akauliza.

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kwasababu haukunipa muda huo Darren. Maisha yako yote umekuwa ukinichukulia kama adui yako. Mtu ninayekusababishia mabaya na nuksi,” Melissa akieleza hayo machozi yakamtiririka zaidi. Na Charlie akagundua kuwa mwanamke huyo alikuwa akimomonyoka miguu yake kuwa udongo.



    Akamshtua Darren atazame. Darren akapayuka kuuliza, “Melissa, nini kinatokea?” akiwa amemshika mkono mwanamke huyo. Melissa akatazama miguu yake inayomomonyoka na kisha akamtazama Darren na kusema, “Hii ndiyo gharama yangu kwa kusema haya. Yanipasa niende Darren. Maisha yangu yamekwisha hapa duniani.”



    “Hapana Melissa, si una kito cha kuishi milele?” Darren akauliza.



    “Sina kitu chochote Darren,” Melissa akasema akilaza kichwa chake kifuani mwa Darren, “Yote nimeyatoa kwa ndugu zangu kama sadaka ya kukubakiza wewe hai.” kisha akamtazama Darren na kumwambia, “lakini haikusaidia na wamenigeuka. Wanataka maisha yako, wanataka maisha yenu. Wanataka kila ambacho bibi yako alikuwa anamiliki. Siwezi kuwazuia tena, Darren. Sina nguvu hiyo.”



    Melissa alipomaliza kauli hiyo, mwili wake ukawa umeshapukutika mpaka kufikia tumboni. Mwili uwake ulikuwa kichuguu cha mchanga. Akamwaga Darren, “Kwaheri, mpenzi”



    “Melissa!” Darren akaita akimshika Melissa vema. “Usiondoke, Melissa! Tutawezaje kupambana wenyewe? Tafadhali usituache!” Lakini tayari sasa mwili wa Melissa ulikuwa umepukutika zaidi mpaka kifuani. Maneno pekee ambayo aliyasema kabla hajamalizika kabisa ni haya,



    “Kuna kitu kwenye jeneza la bibi yako,” alipotaka kunena zaidi, kichwa chake kikamomonyoka na hatimaye akawa mchanga kabisa. Darren na Charlie wasiamini macho yao wakautazama mchanga ule wa bahari.



    “Amejitoa sadaka kwa ajili yetu,” akasema Charlie akimtazama Darren kisha akauliza, “sasa tunafanyaje?” Darren alipohakikisha kuwa kweli Melissa ameenda, akamwambia Charlie waende kule kwa bibi yake. Lakini muda ulikuwa umeenda sana.



    “Vipi tukadamka asubuhi?” Charlie akapendekeza.



    “Hapana,” Darren akatikisa kichwa. “Huoni ni hatari zaidi tukiendelea kungoja?” kweli Charlie akaafiki, lakini sasa wangefanyaje na muda ulikuwa umewatupa mkono?



    Wakiwa wanafikiri namna ya kufanya, simu ya Darren ikaita, alikuwa ni Isabel. Alipokea na kumjulia hali mwanamke huyo.



    “Upo wapi, Darren?” Isabel akauliza. Darren akamtazama Charlie na kujibu, “Nipo mbali.”



    “Wapi? Tafadhali waweza kuniambia?” Isabel akasisitiza, lakini kabla Darren hajajibu akamtazama kwanza Charlie, mwanamke huyo akamtikisia kichwa. Darren akakata simu.



    “Darren, usimwamini mtu yeyote kwa sasa hivi,” Charlie akamwambia akiwa amemkazia macho.



    “Kwanini? Huyu nafahamiana na--”



    “Hapana!”



    Punde simu ikaita tena, Darren akamtazama Charlie. Ajabu mwanamke huyo akampoka simu hiyo na kisha akaikata na kuizima. “Tuondoke, Darren!”



    Basi upesi wakalifuata gari lao na kujikwea. Charlie akamwambia Darren waelekee kwake alafu ndiyo waende huko waendako, Darren akatii. Walipofika kwa Charlie wakapakia silaha kadhaa ndani ya gari, Charlie akabeba na pesa, wakaanza safari ya kwenda kwenye nyumba ya marehemu bibi yake Darren.



    Wakatembea kwa muda mrefu sana mpaka pale ambapo usiku sasa ukawa mkubwa. Wakiwa kwenye majira ya saa tano usiku, wamebakiza kama kilomita ishirini kuwasili wanapoelekea, Charlie akahisi kuna gari linawafuatilia. Alimshtua Darren na kumtaka aongeze mwendokasi.



    Darren alipojaribu kutazama kwa kutumia vioo akaliona gari hilo wanalolishukia. Halikuwa ngeni machoni mwake. Alipoenda mbele zaidi na kulitazama vema, akagundua kitu,



    “Isabel!” alijikuta akinena mwenyewe.



    “Unamaanisha yule mwanamke?” Charlie akauliza. “Yule aliyekuwa anakupigia simu?”



    “Ndio!” Darren akajibu. “Ndiye yeye!”



    Charlie akatazama nyuma kuliangazia gari hilo. Lilikuwa linakuja kwa kasi. Alihofia sana.



    “Darren, sasa tunafanya nini?”



    “Sijui!” Darren akatikisa kichwa akiwa ametoa macho kukodolea kioo cha juu ya kichwa chake. Alikanyaga pedeli ya mafuta zaidi, gari likakimbia. Punde lile gari linalowafuata likatokomea wasijue limeenda wapi!



    “Unaliona?” Darren akamuuliza Charlie.



    “Hapana, silioni!” Charlie akajibu akiwa anaendelea kukagua. Kwa muda kidogo akaendelea kutazama asilione tena gari lile linalowafukuza, basi wakaendelea na safari yao mpaka waelekeapo. Walipofika wakajitua toka kwenye gari na kabla hawajaenda mbali sana, wakatupa macho yao kukagua.



    Ilikuwa ni nyumba iliyomezwa na kiza. Kulikuwa kimya sana. Kwa namna moja ama nyingine kulikuwa kunatisha.



    Wakiwa wanaendelea kutazama, Charlie akagundua kitu. Akamwita Darren na kumuuliza, “Nini kile? Ni gari ama macho yangu?” Darren alipotazama akaona gari kwa mbali upande wao wa kulia. Gari hilo lilikuwa limeegeshwa kwa ukimya. Lilikuwa ni lile gari waliloliacha barabarani. Gari ambalo Darren hudhania ni la Isabel.



    “Umeliona likiingia muda huu?” Darren akauliza.



    “Hapana,” Charlie akajibu na kuongezea, “Nimeliona likiwa tayari limeegeshwa.” kisha akauliza, “atakuwa amefika kabla yetu?”



    Darren hakuwa na majibu, upesi akamwamuru Charlie wachukue kila kinachohitajika kwenye gari na waelekee eneo la kaburi upesi. Walipofanya hivyo, mara gari lile likawasha taa zote kwa pamoja, pap! likawamulika na kuwaumiza macho!



    Upesi wakakimbia kule kaburini na kuanza kuchimba kwa maelezo ya Darren. Wakiwa wanaendelea kuchimba, Charlie akamwona mtu kwa mbali akija kwenye mwelekeo wao. Hakuweza kumwona vema maana alikuwa yu mbali, kitu pekee alichoweza kubaini ni kuwa mtu huyo ni mwanamke kutokana na umbo lake na mwendo pia.



    Mikono yake iliyokuwa tupu ilikuwa ikienda mbele na kurudi nyuma sababu ya mwendo.



    “Chimba, Charlie! Chimba!” Darren akabweka. Wakafukua kana kwamba sungura udongoni na mtu yule alipokaribia, Darren akamsihi Charlie aendelee na zoezi ilhali yeye akamkabili mtu huyo anayekuja.



    “Darren, una uhakika?” Charlie akauliza kwa mashaka.



    “Usijali, endelea,” Darren akasema akitoka shimoni na kupiga hatua kadhaa kusonga mbele. Alipomfikia mtu yule ndipo akabaini kweli alikuwa ni Isabel.



    “Isabel,” Darren akaita na kuuliza, “Ni nini unataka hapa?”



    Isabel akatabasamu na kuuliza, “Darren mbona haupokei simu yangu?” kabla Darren hajajibu, akauliza tena, “Kwani kuna tatizo lolote baina yetu?”

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Darren akamtazama kwanza Isabel kwa namna ya kumtilia mashaka. Alikuwa anahisi kuna kitu hakipo sawa.



    “Isabel, unataka nini hapa?”



    Isabel akatazama nyumba kubwa iliyokuwa kando yao, “Ni nyumba kubwa. Nimeipenda sana Darren. Vipi ile ofa yangu, waweza kuniuzia?”



    “Siuzi tena!” Darren akajibu.



    “Kwanini? Auhitaji pesa tena?”



    “Sihitaji pesa zako, Isabel.”



    Isabel akamtazama Darren na kumsogelea karibu zaidi.



    “Tangu lini umeanza kukataa pesa zangu, Darren?”



    “Kuanzia leo. Sihitaji tena. Na pia sihitaji kukuona pia!”



    Isabel akakunja shingo yake kutazama kule shimoni. “Naona umepata mwanamke mpya.”



    “Hayakuhusu, Isabel. Hicho ndicho kimekuleta?”



    “Hapana, Darren,” Isabel akajibu akiweka mkono wake begani mwa Darren. “Kilichonileta hapa ni kuchukua kilicho changu tu.”



    “Kipi chako hapa?” Darren akauliza.



    “Vyote unavyoviona hapa,” Isabel akajibu na kuongezea, “Vyote ni urithi wangu. Na kwakuwa haukutaka niuchukue kwa amani, basi nitatumia nguvu!”



    “Ebu tumia nione!” Darren akasema akimkazia Isabel macho.



    “Una uhakika?” Isabel akauliza akipandisha nyusi yake moja. Punde Darren akaanza kuhisi maumivu makali ya kichwa.



    “Darren nisingependa nitumie nguvu dhidi yako. Nitakumaliza. Kwahiyo kwa kunusuru maisha yako, songa kando nifanye kilichonileta.”



    Japo Darren alikuwa anasikia maumivu makali bado hakuwa radhi kumruhusu Isabel atende kile alichokuwa amekusudia. Basi akamvamia akimtupia maneno makali lakini alichoambulia hakikuwa kinasimulika vema. Alitupiwa mbali tena kwa mkono mmoja tu. Akaangukia tumbo na kulalama kwa maumivu makali!



    Isabel akapiga hatua nzito kumfuata Charlie. Alipomfikia akanyoosha mkono wake kumnyaka mwanamke huyo, ila upesi Charlie akatumia kifaa alichokuwa anachimbia kumwadhibia Isabel! Alimchana na kumvujisha damu!



    Isabel akautazama mkono wake unaovuja damu kisha akakunja ndita akimtazama Charlie. “Umekwisha!” akafoka na kujitupia ndani ya shimo. Charlie alipotaka kumwadhibu tena Isabel, nyenzo yake ikadakwa na mkono wa Isabel wenye nguvu.



    “Kamwe usijaribu!”



    Isabel akampokonya Charlie dhana hiyo na kisha akataka kumbamiza nayo kichwa. Kheri kabla hajatimiza adhma yake hiyo, nyenzo ikadakwa na mtu nyuma. Isabel alipogeuka kutazama, alikuwa ni Darren. Na kabla hajafanya jambo, mwanaume huyo akamwadhibu kwa kumzamishia ncha za reki usoni mwake! Kilikuwa ni kitendo cha kinyama ambacho Darren amewahi kufanya tangu azaliwe.



    Hata wakati Isabel anaanguka chini, Darreb alikuwa ameachana asiamini kama amelitenda hilo. Basi upesi, wakishirikiana, wakamtoa Isabel ndani ya shimo na Darren akamburuza kwa hatua kadhaa mbali na shimo kisha wakaendelea kuchimba kaburi.



    Walipofanya hivyo kwa takribani dakika sita, mara Isabel akanyanyuka akiwa na reki lake usoni. Si Darren wala Charlie aliyemwona. Mwanamke huyo akachomoa reki usoni na kulitupia kando. Alikuwa anachuruza damu lakini hakuwa anajali. Upande wake wa kushoto ulikuwa umefunikwa na damu inayotiririka kama bomba.



    Alipotupia reki kando ndipo Darren na Charlie wakasikia na kuhisi. Darren alipotazama na kubaini hilo akahofia sana. Hata Charlie vilevile. Ni mtu wa aina gani angenyanyuka baada ya kadhia ile? Lakini kwa ujasiri Darren akatoka ndani ya shimo baada ya kumwambia Charlie aendelee kufukua.



    “Darren!” Charlie akaita kwa hofu. Aliogopa. Aliona Darren angeenda kufa. Lakini Darren asijali akajiendea kifua mbele. Alipomfikia Isabel akasema, “Nitakuua!” naye Isabel akamwambia, “Karibu tena!” kisha akamnyaka shingo yake kwa nguvu na kumnyanyua juu juu!



    “Ndiyo kwanza tupo kwenye moja, Darren. Unadhani binadamu kama wewe anaweza kuniua?” Darren akarusharusha miguu akijitahisi kujinasua toka kwenye mikono ya Isabel. Hakika asingeweza kwani mikono ya mwanamke huyo ilikuwa imeshiba nguvu haswa. Ilikuwa inaminya uhai toka kwenye mwili wa Darren.



    Darren akapapatika sana pasipo mafanikio. Akarusha na mateke ambayo mengine yalikwenda hewa na mengine kumkita Isabel lakini haikusaidia, mwanamke huyo alikuwa mithili ya gogo kavu!



    Basi Darren aliyekuwa anaelekea kufa alipoona amefanya kila jambo pasipo mafanikio na sasa anaelekea kufa, akamtazama Isabela akilenga kumtusi ama kumlaani. Ni kheri katika hilo akabaini jeraha alilokuwa nalo Isabel mkononi, lile jeraha ambalo Charlie alimsababishia. Basi kama simba aliye na njaa, Darren akadaka kwa mikono yote jeraha hilo na kuliparua sana. Isabel akashindwa kuvumilia na hatimaye akamwachia Darren aliyejidondokea chini akikohoa.



    Darren alikuwa anahisi kifua kinambana, shingo nayo imeziba. Alikuwa anahema kwa tabu. Koo lake bado halikuachia. Alikohoa mara kadhaa akiwa anahangaika kumeza mate.



    Hakukaa sana akamwona Isabel akimfuata kwa hasira. Alipotaka kuamka akimbie, Isabel akamwendea kwa kasi sana na kumdaka. Darren akajitahidi kurusha ngumi na kutumia nguvu zake za kibinadamu lakini akashindwa kabisa! Isabel alikuwa ana nguvu mno!



    Mwanamke huyo pasipo kujiuliza mara mbilimbili, akadidimizia kucha za mkono wake wa kushoto kwenye tumbo la Darren, na hakufanya vivyo mara moja bali mara tatu! Darren akalalamika sana kwa maumivu. Isabel akamtupia mbali akiwa amemalizana naye.



    Darren, akiwa amelala kama mtu anayengoja kifo akiwa ameshika tumbo lake linalovuja, akamtazama Isabel. Akamwona mwanamke huyo akiwa anaenda kumfuata Charlie kule shimoni. Basi akapaza sauti kuu kumwita Isabel. Halikuwa zoezi rahisi, alikuwa anahisi maumivu makali sana lakini alifanikisha adhma yake hiyo.



    Isabel alipogeuka kumtazama, Darren akapaza sauti kumtusi na kumkebehi mwanamke huyo. Kitendo hicho kikamkasirisha sana Isabel, akaamua kuachana na Charlie akammalize mwanaume huyo kabisa. Basi akamjongea kwa madaha akiwa anamwambia ni kwa namna gani atakapofurahi akiona roho yake inaenda.



    “Kama bibi na mama yako, nawe utaenda hukohuko!” akasema Isabel. “Mwana usiwe na haya ukatembea na bibi yako. Hujui Melissa ni sawa na bibi yako, ati Darren?”



    “Na mbona na wewe ulikuwa unanitaka?” Darren akaguguma kuuliza. Saa hii kinywa chake kilikuwa kinachuruza damu pia. Isabel akacheka akiwa anazidi kujongea, “Mimi? Darren mpenzi nilikuwa nataka tu kukumaliza na si kingine. Unadhani mimi ni kama yule mpofu Melissa? Mjinga kama yule?”



    “Ni wewe ndiye mjinga, si Melissa!” Darren akafoka.



    “Pole sana, Daren,” Isabel akasema akiwa anamalizia hatua yake moja kumfikia Darren. “Mpumbavu wako ameenda, nani atakulinda sasa?” akauliza na kucheka. “Kwa akili yake amejitoa uhai kwa ajili yako. Wewe binadamu. Kwa sababu tu ya kukwambia yote yale ambayo hupaswi kuyajua. Shenzi kabisa!”



    Alipomaliza kusema hayo akamnyakua Darren na kisha anyanyue mkono wake ili apate kumkita tena tumboni kama alivyofanya hapo awali. Lakini mara hii kabla hajafanya vivyo, akastaajabu kuona mpini wa reki ukitokezea tumboni mwake! Hamaki alikuwa ni Charlie nyuma yake!

    http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Basi akamwacha Darren na kisha akapiga magoti akiwa anatazama chuma kile kilichomtoboa tokea mgongoni mpaka tumboni na kisha akadondoka puh! Na kutulia tuli,



    Charlie akamjulia hali Darren.



    “Niko sawa,” Darren akamjibu na kisha akamuuliza, “Umefanikiwa?”



    “Bado kidogo!” Charlie akajibu. Akatazama tumboni mwa Darren, kulikuwa kunamwaga damu sana. Akashikwa na imani, “Darren, nikuwahishe hospitali!” alisema akitaka kunyanyuka akaendee gari lakini Darren akamdaka mkono na kumwambia, “Hapana, Charlie. Nenda kamalizie kwanza ile kazi!”



    “Darren, nitaendeleaje na upo kwenye hali hii?” Charlie akauliza.



    “Hapana! Hapana! Nenda kwanza, tafadhali nenda!” Darren alisisitiza na basi kwa shingo upande, Charlie akaenda zake. Akazama shimoni na kufukua zaidi na zaidi, ndani ya dakika tano akawa amefikia jeneza, akafunua na humo ndani akakuta maiti ya bibi yake Darren ikiwa mifupa.



    Alipotazama vema akabaini kulikuwa na kito rangi ya asamawati, basi akakibeba na kupaza sauti, “Darren, nimekipataaaa!”



    Haraka akatoka ndani ya shimo na kumkimbilia Darren. Lakini alipofika akabaini Darren hakuwa anasogea wala kuashiria kama mzima. Alipotazama vema akabaini pia mwili wa Isabel ulikuwa umesogea kidogo toka pale alipouacha, na kama haitoshi, reki halikuwa tumboni, bali kwenye kichwa likiwa limemtoboa!



    Hapo Charlie akabaini ya kuwa Darren na Isabel walipambana kwa mara nyingine. Akapata hofu zaidi juu ya uhai wa Darren. Akamwita sana na kumtikisa, kwa mbali Darren akafungua macho yake kumtazama. Alikuwa ana mjeraha kooni na kifuani. Karibia mwili wake wote ulijawa damu.



    “Umepata?” Darren akauliza kwa kunong’ona.



    “Ndio, nimepata!” Charlie akajibu kwa kitete. Macho yake yalikuwa mekundu yakitaka kumwaga machozi. “Twende nyumbani, sasa!” akasema akijaribu kumnyanyua Darren.



    “Hapana, Charlie,” Charlie akasema na kuongezea, “Hapa ndiyo nyumbani kwangu, sina pengine. We nenda mimi utaniacha hapa.”



    “Nitakuachaje Darren? Tumekuja wote hapa! Nyanyuka tafadhali twende!”



    Charlie alipoona ni ngumu kumnyanyua Darren basi akaenda zake asogeze gari karibu. Alipojipaki kwenye gari, akaendesha upesi sana kumrudia Darren. Alipoliweka gari tenge akashuka na kumwendea Darren, ila kwa muda huo hakuwa Darren tena bali mwili tu.



    Akapambana kumweka kwenye gari, lakini kabla hajawasha gari Isabel akanyanyuka na reki lake kichwani! Mwanamke huyo akakaa mbele ya gari akimtazama Charlie kwa macho ya kukodoa.



    Charlie akastajabu sana. Akahangaika kuwasha gari, kabla hajafanikiwa, Isabel akawa tayari amezama ndani na kumkaba shingo kwanguvu! Charlie akaweweseka sana kujiokoa.



    Ajabu wakiwa kwenye zoezi hilo, wakasikia mtu akigonga kwenye kioo cha dirisha. Isabel alipotazama, akabaini ni Melissa! Akastaajabu akiwa ameachama mdomo!



    “Ina -- inawezekanaje?”



    “Unadhani nilikuwa mjinga, sio?” Melissa akauliza.



    Kufumba na kufumbua akafungua mlango wa gari na kumnyaka Isabel. Kwa mikono yake akamnyofoa mwanamke huyo koo na kisha akamtupia mbali kana kwamba kitenesi!



    “Melissa!” Charlie akaita kwa kustaajabu. Akamkumbatia Melissa kwanguvu na kisha akamwambia kumhusu Darren. Walipomtazama wakabaini mwanaume huyo alikuwa amekwisha kufa.



    Basi Melissa akachukua kile kito ambacho Charlie alikipata kwenye jeneza la bibi yake Darren kisha akakitazama na kusema, “Nilikuwa nayajua yaliyo mbele yangu hata kuhifadhi sehemu ya maisha yangu kwenye jeneza lile.” aliposema hayo, akamtazama Charlie na kumwambia, “Utakapokutana na Darren mwambie nampenda sana. Hatimaye amekuwa huru. Hatimaye mmekuwa huru.”



    Aliposema hayo akaingiza kile kito kinywani mwa Darren na kisha kumfumba mdomo. Charlie akamuuliza, “vipi kuhusu yule Isabel, hatarejea tena?”



    Melissa akamjibu hatorejea tena kwa roho zake zimekwisha. Ndani yake alikuwa na roho kadhaa na kadiri walivyokuwa wanamuua ndivyo walivyozimaliza mpaka kubakia moja aliyoimaliza yeye muda si mrefu.



    “Umejuaje?” Charlie akamuuliza.



    “Kwasababu isingekuwa rahisi kummaliza kama nilivyofanya,” Melissa akamjibu na kisha akamuaga. Moja kwa moja akaenda kwenye shimo la kaburi na kudmbukia humo. Punde, Darren akaamka. Alikuwa mzima wa afya kabisa asiye na jeraha.



    Charlie alipomweleza kila lililotokea, upesi akakimbilia kwenye kaburi kumtazama Melissa. Akamkuta mwanamke huyo akiwa ana uhai amekwishakufa. Akamwita na kumwita pasipo mafanikio, Melissa alikuwa ameenda.



    Melissa hakuwapo tena.



    Basi wakamfukia kwenye kaburi hilo na kwenda zao.





    MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog