Search This Blog

MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN - 3

 






Simulizi : Mkufu Wa Malkia Wa Gosheni

Sehemu Ya Tatu (3)







"Hata hapa mlipoingia humu ndani, mmeshakuwa wetu. Na hakuna yeyote atakayekuja kuwaulizia humu."

.

.

.

Baada ya maneno hayo, Malkia alifunga macho yake akaanza kunena kwa lugha isiyofahamika. Mdomo wake ulimamata maneno harakaharaka. Zura na Fluffy walitazamana wakistaajabu. Kuhani mkuu naye alipigwa na butwaa.





Wakati Malkia akiendelea kunena, mara ndani ya chumba cha kuhifadhia mali kukaanza kutikisika. Vitu vilianza kuparanganyika humo, mkufu ukijinyanyua toka chini ulipokuwa umefunikwa na vitu vingine vya thamani.

.

.

.

Kuhani mkuu aligundua hilo jambo. Sauti ya kutikisika iliyotoka kwenye stoo ilimfikia vema masikioni mwake. Haraka akajua itakuwa na mahusiano na kile akifanyacho Malkia.

.

.

.

"Anafanya nini huyo?" Kuhani mkuu alifoka akitoa macho. Bado Malkia aliendelea kuteta na kunena. Kuhani mkuu akachomoa kisu toka nyongani, akakirusha haraka kumfuata Malkia. .

.

.

Katika kasi ya ajabu, Fluffy akakipangua kisu hicho, kisha akasimama mbele ya Malkia.

.

.

.

Kuhani mkuu alitazama walinzi wake wawili, akawapa ishara ya kichwa. Mara wale walinzi, walioshiba misuli wakiwa wameshikilia mapanga, wakaanza mapambano makali na Fluffy.

.

.

.

Zura hakuwa na ujuzi na mapigano. Alichokuwa anakifanya ni kujikinga na mikono yake akipiga yowe. Alijifichama nyuma ya Fluffy, akimuweka Malkia nyuma yake.

.

.

.

Fluffy hakuweza kuwamudu wanaume wale walinzi wawili. Walimzidi wakamtupia mbali. Zura naye alikwapuliwa akarushiwa kando, Malkia akadidimiziwa panga kifuani na kudondoka chini.

.

.

.

Zura alipiga ukunga wa kilio. Huko nje wanaume wakasikia na kujikusanya nje ya makao. Fluffy alimtazama Malkia kama mtu asiyeamini. Machozi yalijaa upesi machoni.

.

.

.

Kuhani mkuu alisimama akitabasamu.

.

.

.

"Kwisha kazi. Unadhani unaweza kuleta utawala wako ndani ya tawala yangu?"





Kitu ambacho wote hawakijua ni kwamba, mkufu ulikuwa tayari mkononi mwa Malkia. Taratibu mwili wake ulianza kujirejesha na kujipa fahamu. Panga lilichomoka na kudondokea kando, Malkia akaamka.

.

.

.

Vita haikuwa imeisha, bali yaanza. Kuhani mkuu alitoa jicho.

.

.

.

***

***

Hakuamini kilichotokea. Mtu aliyekitwa na panga kifuani, aamke tena! Hofu ilianza kupalilia moyo wake. Alitazama walinzi akawaamrisha akimnyooshea kidole Malkia, "Malizeni huyo!"

.

.

.

Malkia alivaa mkufuwe shingoni, punde akaanza kubadilika. Macho yake yalibadili rangi na nguo zake zilikuwa mpya zilizomkaa vema, tena za vita. Viatu vipya vya mapambano vilifunika miguu yake. Viatu hivi vilikuwa vinang'aa na ni vya ngozi ngumu kana kwamba vimefumwa na ngozi ya mamba.

.

.

.

Wanaume wawili, miongoni mwa walinzi wa Kuhani mkuu, walimfuata Malkia kwa kasi. Walitumikisha mapanga yao kwa ustadi, ila hawakufua dafu. Malkia alipangua kila ncha iliyomkaribu. Mikono yake ilikuwa mepesi mno kama upepo.

.

.

.

Mwanaume mmoja alituma panga akitaka kumtoboa tumbo, Malkia akatengua panga hilo na kumzawadia teke la mzungusho. Upesi, mwingine akatuma panga lake kufuata shingo ya Malkia, Malkia akainama kwa haraka kisha akapiga teke mkono wa mwanaume huyo ulioshikilia panga, panga likadondoka chini.

.

.

.

Kabla mwanaume huyo hajafanya lolote, akajikuta chini kwa teke zito lililosigina taya yake. Alidondoka mithili ya kifusi. Tetemeko la adhi lilipita!

.

.

.

Wakati akiugulia maumivu, mwenzake alinyanyuka akamsogelea Malkia. Alitupa panga, likakwepwa, alitupa tena, Malkia akahepa. Alijaribu tena kwa mara ya tatu, Malkia akakata panga la mwanaume huyo kwa kutumia upanga wake. Kipande kikadondoka chini.





Mwanaume alishangazwa sana na hilo tukio. Akiwa kwenye bumbuwazi, alistaajabu kumuona Malkia yu hewani anazunguka kana kwamba tairi. Kufumba na kufumbua, alikitwa na miguu miwili kifuani, akacheua damu. Alidondokea chini asionyeshe dalili ya kusimama karibuni.

.

.

.

Malkia sasa akawa amesimama mwenyewe, adui walikuwa chini wakigugumia. Alimtazama Kuhani mkuu kwa uso makini, Kuhani akasaga meno. Hii kwake ilikuwa dharau. Aliwatazama walinzi wake wawili waliobakia, akawaamuru wakamshambulie Malkia na kummaliza.

.

.

.

Wanaume hao, waliokuwa wamejazia misuli, mara moja wakamfuata Malkia. Mmoja alikuwa amebebelea panga, mwingine akiwa ameshika rungu jeusi kubwa. Nyuso zao zilikuwa zinatisha kwa makovu. Macho yao yalikuwa yamebeba ukatili.

.

.

.

Wanaume hao walimzunguka Malkia wakimuweka kati. Mara ghafla kwa pamoja wakaanza kushambulia. Wote walirusha panga kwa mkupuo. Malkia alipangua panga hizo kwa kubinua na kunyanyua upesi mkono wake wenye silaha, kisha akajitoa katikati na kuwaweka maadui mbele yake.

.

.

.

Sasa alikuwa anawaona wote. Kichwani kwake alikuwa anapigia mahesabu juu ya namna ya kufanya, na kwa haraka akapata majibu. Haikuzidi hata sekunde tatu.

.

.

.

Haraka alikimbia kuwafuata maadui akinyooshea panga lake mbele. Adui wa kwanza alituma panga, Malkia akaruka juu na kulipangua kwa teke la kulia. Akiwa huko huko juu, akapangua na panga la adui mwingine kisha akajibedua akijilaza hewani, mmoja akamzaba mateke mawili, mwingine akimkata kifua.







Tukio hilo lilichukua nafasi ndani ya sekunde tatu tu! Wanaume wakawa wapo chini hoi. Malkia alifuta panga lake damu kwa kutumia mwili wa mwanaume aliyemkata, huku akimtazama Kuhani mkuu.

.

.

.

"Naomba niende nisikusababishie makubwa zaidi," alisema Malkia kwa kujiamini. .

.

.

Kuhani mkuu alisimama, akabinua mdomowe akisonga mbele kumfuata Malkia.

.

.

.

"Huwezi ukatoka hapa hai. Haitakuja kutokea," alisema Kuhani mkuu kisha akapiga makofi mawili kwa nguvu, mara milango ya jengo ikafunguliwa. Waliingia wanaume wale wakwapuzi wote. Kila mmoja alikuwa amebebelea silaha mkononi.

.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

.

.

Wakiwa katika hali ya utulivu, walisimama na kumtazama mkuu wao aliyekuwa anaelekea kwenye mpambano. Punde, kana kwamba wamapewa taarifa, wakaanza kupiga silaha zao kutengeneza mdundo wa muziki.

.

.

.

Ti! Ti! Ti! ... ti-ti-ti ... ti-ti-ti! Ti! Ti! Ti! ... ti-ti-ti! ... ti-ti-ti!

.

.

.

Ukimya uliokuwepo ulifanya mlio huo uwe mkubwa zaidi. Mlio huo ulipendeza mbele ya masikio ya Kuhani mkuu. Alikuwa anatikisa kichwa kuendana nao.

.

.

.

Alisukumia kando koti lake refu kisha akakunja ngumi na kutanua miguu yake kutafuta balansi. Akamuita Malkiakwa ishara. Wakaanza kupambana.

.

.

.

Kuhani huyu mkuu hakuwa na silaha. Alikuwa anatumia mikono yake mitupu.

.

.

.

Malkia akarusha panga, likapita. Upesi akarusha na mateke matatu ya mkupuo, Kuhani mkuu akayakwepa na kutabasamu. Akauliza:

"Hicho ndicho ulichonacho?"





Malkia akajituma tena. Akarusha mikono yake kwa upesi zaidi. Kuhani mkuu akakwepa lakini teke la Malkia lililokuja kwa kasi likamziba uso na kumwangusha chini. .

.

.

Akaamka upesi na kujikung'uta vumbi. Akakunja uso wake na mara kwa pupa akatupa mashambulizi. Aliruka juu kama sufi. Alipangua panga za fujo zilizotumwa na Malkia. Akiwa angani, akashika upinde wa koti lake akafyagia hewa.

.

.

.

Sijui ni kitu gani kilitoka kotini, ila punde Malkia akaanza kupiga chafya hatari. Hakupata muda wa kuzingatia tena mapambano. Akaanza kulewa. Akawa anapepesuka akiona maruwe ruwe.

.

.

.

Kuhani mkuu akacheka sana. Akavimba akiwaonyeshea umwamba watu wake kuwa yeye ni mkuu. Akazungukazunguka akinyoosha mikono yake minene juu. Akataka kummaliza Malkia, ila Fluffy akaingilia kati.

.

.

.

Alirusha panga lake likapunyua pua ya kuhani aliyewahi kulikwepa. Kuhani akamtazama Fluffy akinguruma kama simba. Akatembea haraka kumfuata mwanamke huyo ambaye uwezo wake haukuweza kupambana na wa Kuhani.

.

.

.

Akamkamata nywele mwanamke huyo kwanguvu. .

.

.

"Unataka kufa wewe si ndiyo?"

.

.

.

Fluffy akalalama kwa maumivu. Akafukurukuta asijiokoe. Zura alimrukia Kuhani mkuu mgongoni, mwanaume huyo akamtupia mbali, akazirai.

.

.

.

"Huyo mwenzako hawezi kuamka tena," akajivuna Kuhani mkuu. "Amelewa na unga wangu wa madawa ya siri. Hakuna aliyewahi kuwa sawa baada ya kuunusa unga huo."

.

.

.

Kuhani mkuu aliona ameshinda vita. Silaha yake ya unga ilikuwa imemfanyia kazi mujarabu kabisa na sasa alibakiza tone tu kulinywa.





Akanyanyua mkono wake amkite Fluffy kifuani. Kabla hajafanikiwa tendo hilo, akastaajabu kuona Fluffy anatabasamu.

.

.

.

"Sand ... arus!" Fluffy alisema akitazama nyuma ya Kuhani mkuu.

.

.

.

Kuhani akatazama nyumaye. La haula akamuona Malkia amesimama. Akastaajabu. Alimtupia Fluffy kando akamfuata Malkia akikunja sura.

.

.

.

"Nitakumaliza kwa mikono yangu mwenyewe malaya wewe!"

.

.

.

Alikunja ngumi akatawanya miguu yake tayari kwa ajili ya vita. .

.

.

Malkia akaja kwa haraka, Kuhani mkuu akarusha teke danganyifu, bahati haikuwa kwake Malkia akagundua tego hilo, hakuhangaika na mguu uliotangulizwa mbele, akahusika na ule uliodhamiriwa.

.

.

.

Alikwepa teke halisi, kisha akadaka mguu ule uliorusha teke la uongo. Akauvuta kwanguvu kumwangusha Kuhani, lakini mwanaume huyo akatafuta balansi na mguu wake mmoja. Alisimama nao huo huo mwingine ukiwa mikononi mwa Malkia aliyeliwacha panga lake chini.

.

.

.

Kosa akalifanya mwanaume huyo. Akarusha teke na mguu wake aliosimamia, Malkia akaudaka nao pia kisha kwa haraka akasigina sehemu za siri za Kuhani mkuu kwa nguvu kuu.

.

.

.

Kuhani akadondoka chini. Akalia kwa maumivu makali. Akabana miguu yake akiisindika na mikono. Hakuwa ameumizwa, alikuwa amepasuliwa kabisa. Nguo yake ilijaa damu maeneo nyeti.

.

.

.

Malkia akajongea kumfuata Kuhani na kumtazama. Kuhani alikuwa amebana meno yake akiyasaga kwa maumivu. Ila kama haitoshi, akanyanyua pindo la koti lake na kufyagia hewa.





Malkia akawahi kukimbiza uso wake kwa kuugeuza. Akafunika pua na mdomowe. Alipogeuka akammaliza Kuhani kwa kumkita magoti baada ya kujifunga na kujifungua juu hewani.

.

.

.

Kuhani mkuu akaenda. Kifua chake kilikuwa kimetulia tuli mdomo wake ukiachama. Mara muziki ukasimama. Wanaume wote hawakuwa wameamini kama Kuhani mkuu ameenda.

.

.

.

Kulikuwa kimya tuliii. Malkia akawatazama wanaume wale waliokuwa wamebebelea silaha. Uso wake ulikuwa unawaka. Bado alikuwa ana nguvu na mwenye haja ya mapambano.

.

.

.

Mara wanaume wote wakaweka silaha chini. Wakamsogelea Malkia na kuangukia magoti wakisema:

"Tupe nafasi tukutumikie. Turuhusu tuwe vijakazi wako, ewe malkia!"

.

.

.

Hakuna aliyekuwa anajua kama waliyekuwa wanamuomba ni Malkia. Ila walikuwa wanataka kumfanya Malkia wao. .

.

.

Katika hali ya hali ya kushangaza, Malkia akadondoka chini na kupoteza fahamu

.

.

.

.

.

.

*****

.

.

.

Majira ya jioni.

.

.

.

Mkononi mwake alikuwa amebebelea glasi ya mvinyo mwepesi aliokuwa anaupeleka taratibu kinywani. Wakati akifanya hivyo, macho yake yalikuwa yanatazama utajiri wa asili kwa kulisindikiza jua kuhitimisha safari yake ya siku.

.

.

.

Alikuwa mwenyewe hapo nje. Mwili wake aliulaza juu ya kamkeka kalikotandazwa kwenye kiti kirefu cha mbao. Miguu yake aliikunja nne, wa juu akiutikisa tikisa. Kuna jambo alikuwa analifikiria.

.

.

.

Huyu hakuwa mwingine bali mwanamke mbichi kabisa, mke wa mwisho wa Sultan.

.

.

.

Tangu alipopoteza dawa aliyopewa na bibi yake, hakuwa na furaha kabisa. Kila siku amekuwa akikaa hapa jioni kulisindikiza jua. Amekuwa mpweke maana Sultan hana muda naye tena kama hapo awali.







Zama zimebadilika.

.

.

.

Alimaliza mvinyo wake, akapaza sauti kumuita kijakazi. Kijakazi akaja upesi.

.

.

.

"Niongezee," akasema akinyoosha mkono wake uliobebelea glasi.

"Sultana, inatosha, umekunywa nyingi sana," akasema Kijakazi.

"Unanipangia kama nani?" Akauliza mwanamke. Alimtazama Kijakazi kwa macho mekundu yawakayo ghadhabu. Kijakazi akaogopa. Akajaza kikombe mvinyo na kisha akajiondokea upesi. Mke wa Sultan akaendelea kujihudumia.

.

.

.

Haukudumu muda mrefu, mara Mwanamke huyu akasikia sauti ya tarumbeta nje ya jengo lake. Akamwaga mvinyo wake upesi na kumuita kijakazi.

.

.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

.

"Toa hii glasi haraka!" Akaamuru. .

.

.

Alibashiri ugeni huo ni wa Sultan. Mwanaume huyo hapendi kumkuta akishindia kilevi hivyo basi akajitahidi kujiweka sawa asibakize kiashiria. .

.

.

Akasogea upande wa getini, tayari vijakazi wake walikuwa wameshafika, akasimama hapo kungoja ugeni. Akatabasamu tabasamu tashtiti akijitahidi kusimama sawia.

.

.

.

Mara farasi watano wakaingia. Miongoni mwa farasi hao, mmoja alikuwa amembebelea mke wa kwanza wa Sultan. Mwanamke mtu mzima mwenye pambe za urembo. Hakukuwa na ugeni mwingine zaidi ya huo.

.

.

.

Mwenyeji akazizima. Tabasamu likajifinyanga akijiuliza maswali kadhaa:

"Amekuja kufanya nini hapa? ... mbona amekuja muda huu?" Hakuwa na majibu.

.

.

.

Akaigiza tabasamu na kumkaribisha mgeni ndani. Akamhudumia kinywaji wakaketi chini.

.

.

.

"Mbona giza lote hili na njia?" Akauliza mwenyeji. Japokuwa nyuso zao zilikuwa zina tabasamu, mioyo yao ilikuwa meusi.







"Kuna jambo nimeshindwa lala nalo. Nikaamua kuja hapa kulitua," akajibu mgeni. Jibu hilo likamfanya mwenyeji kuguguma na moyo. Hakupata amani. Alihisi kuna jambo haliko sawa.

.

.

.

"Jambo gani hilo?" Akauliza. Alijaribu kufichama hisia zake za ndani asimpe mashaka mgeni.

.

.

.

"Usijali, nitakuambia," akasema mgeni. "Hatuna haja ya kuharakisha kwani leo usiku mzima nitakuwepo hapa."

.

.

.

Mwenyeji akazidi kupata shaka. Hakutegemea ugeni ule, lakini zaidi hakutegemea kama utadumu kwa usiku mzima. Hapa akashindwa kuficha hisia.

.

.

.

"Vipi kuna tatizo?" Akauliza mwenyeji. Mgeni akapachika tabasamu usoni haraka.

"Hapana, hamna tatizo."

.

.

.

Wakaendelea kuongea mambo mengine haswa juu ya tawala yao. Wakiwa wamepoteza kama lisaa hivi, mgeni akarudisha hofu haraka kwa mwenyeji kwa kuuliza:

"Unadhani kuna lolote haliko sawa baina yetu?"

.

.

.

Mwenyeji akanyamaza kwanza kwa sekunde tano. Akatikisa kichwa na kujibu;

"Hapana, sidhani."

"Una uhakika?" .

.

.

Swali hili la msisitizo likawasha alamu kwenye kichwa cha mwenyeji. Sasa akaamini kwa wazi kwamba kuna jambo halipo sawa. Alitazama macho ya mgeni wake, akaona kitu ndaniye: kujiamini.

.

.

.

Alichokuwa anaongea mgeni alikuwa na uhakika nacho. Mwenyeji akajikuta anatetemeka mkono. Kinywaji chake ndani ya glasi kilicheza.

.

."Ndio nina uhakika," akajibu mwenyeji. Macho yake yalikuwa yanamtazama mgeni wake kipembeni. "Sawa," mgeni akasema akipandisha mabega. Akanywa mafundo mawili ya kinywaji chake kabla hajaweka glasi chini na kuhema.

"Bila shaka utakuwa umeona kuna jambo linamtatiza Sultan," akasema mgeni. Uso wake haukuwa na ghafira, bali utulivu.

.

.

"Siku za karibuni amekuwa si mzima kabisa, hata kupungua amepungua. Amekwambia ni nini kinamtatiza?" "Hapana," mwenyeji akatikisa kichwa. "Hajanambia. Kwani kuna kitu gani?"

"Ila mabadiliko umeyaona?"

"Hapana."

"Unajua huu si muda wa kusumbuana kama paka na panya," mgeni alisema akisisitizia. "Sultan hukaa na wewe, na hapa karibuni amekaa na wewe kwa muda mrefu. Haingii akilini kusema hujaona tofauti yoyote kwake."

.

.

.

Kukawa kimya kidogo. Ni kana kwamba mwenyeji alikuwa anafikiri. Akanywa mafundo mawili ya kinywaji chake kisha akasafisha koo.

.

.

.

"Ni kweli," akasema. "Nilimuuliza kwanini yuko chini kihisia, akanambia kuna kitu amekipoteza, anakitafuta."

"Alikuambia ni nini?"

"Hakuniambia. Ila ni wazi hicho kitu ni cha thamani kubwa sana kiasi cha kumkosesha furaha."

"Ni kweli. Na hicho kitu ni mkufu, mkufu wa tawala ya mbali sana, wenye nguvu na mamlaka. Amefanya jitihada kuutafuta lakini hazijafanikiwa kuzaa matunda." .

.

.

Kukawa kimya. Mwenyeji akanywa kwanza kabla ya kuendelea.

.

.

.

"Kwa sasa ni kama amekata tamaa. Na chochote kitakachokuja mbele yake kumsaidia, ataking'ang'ania ... umewahi jaribu kumsaidia?"





Hapa ndiyo palikuwa kitovu cha maongezi. Mwenyeji alijaribu sana kuwa makini na haya maongezi, na hili swali likampa muelekeo wa wapi wanaelekea. Alijikuta akili yake inarudia juhudi alizofanya kumsaidia Sultan lakini mwisho sa siku hazikuzaa matunda.

.

.

.

Akatikisa kichwa.

.

.

.

"Hapana, sijawahi."

"Unasema ukweli?"

"Ndio."

"Basi haumpendi mumeo. Mwanamke yeyote hawezi muona mumewe akiwa tatizoni asijishughulishe kumsaidia."

.

.

.

Kukawa kimya tena. Mwenyeji akaomba radhi anaelekea chooni. Akatoka na kuelekea huko eneoni akimwacha mgeni peke yake.

.

.

.

Katika hali ya kustaajabisha, mgeni akatoa kichupa kidogo cha glasi toka kwenye upinde wake wa nguo. Kichupa hiki ndaniye kulikuwa na kimiminika chekundu kama mvinyo.

.

.

.

Akakifungua upesi na kumiminia kimiminika hicho ndani ya glasi ya mwenyeji wake alafu akakirudisha na kukificha. Akakoroga glasi hiyo ya mvinyo na kuirejesha ilipokuwa.

.

.

.

Baada ya muda mfupi mwenyeji akarejea. Akaketi na kuendeleza maongezi. Mara hii hawakuongelea tena mambo ya Sultan, ila tu mambo mengine yaundayo maisha yao.

.

.

.

Mwenyeji pasipo kujua, akanywa mvinyo wake kumalizia. Macho ya mgeni yakang'aa koo lake likisindikizia mafundo ya mwenyeji. Akafurahi maana dhamira yake ilikuwa imetimia.

.

.

.

"Nikuongeze?" Akauliza mwenyeji baada ya kuona glasi ya mgeni i tupu.

"Hapana, nashukuru," mgeni akajibu.





Baada ya muda mfupi, mwenyeji akaanza kupoteza uwezo wa kuona. Akapoteza pia na nguvu mwilini. Akajaribu kunyanyuka, akashindwa. Akajaribu tena, mara hii akadondoka chini. Akapoteza fahamu.

.

.

.

Mwenyeji akatabasamu. Akatazama usalama wa eneo la karibu, ukamridhisha. Akamfuata mwenyeji wake na kisha akamnyofoa nywele kiasi alizozihifadhi ndani ya mkono wake.

.

.

.

Akambeba mwenyeji na kumpeleka chumbani kwake alipomlaza. Akatoka huko chumbani akaenda chumba cha wageni kupumzika. Akajilaza chali akitazama nywele zile alizozichoropoa kwenye kichwa cha mwenyeji.

.

.

.

Akajikuta anatabasamu.

.

.

.

"Sasa tuone kiburi utatoa wapi?" Akajisemea. Akalala zake kwa amani.

.

.

.

Asubuhi ya majira ya saa kumi na mbili, mwenyeji, ama mke mdogo wa Sultan, akaamka. Alikuwa amechoka na kichwa kilikuwa kinamuuma mno. Alijaribu kukumbuka kilichotokea usiku, akafeli. Hakukumbuka zaidi ya kunywa.

.

.

.

Akatoka kitandani na kwenda bafuni kuoga angalau arefreshi mwili. Akiwa anajivesha nguoze, mara kijakazi akagonga mlango.

.

.

.

"Karibu!"

.

.

.

Kijakazi akaingia akiwa amebebelea chakula cha asubuhi; mikate, mayai na finyango mbili za nyama kavu pamoja pia na kinywaji cha moto. Chakula alikuwa amekifunika na kifungio kama chujio. Akakiweka pembezoni mwa kitanda. Hapo palikuwa na meza ndogo maridadi.

.

.

.

"Karibu Sultana," akasema kijakazi. Alikuwa mwanamke mnene aliyevalia sare. Nywele zake alikuwa kazibana vema kiustadi.





"Ahsante," akasema mke mdogo wa Sultan. Akasogelea chakula chake. "Umemhudumia na mgeni wangu?" Akauliza akijiandaa kula.

"Hapana," akajibu kijakazi. "Mgeni wako amekwishakwenda."

.

.

.

Jambo hili likamshangaza mke mdogo wa Sultan. Aliacha kula akauliza:

"Ameshaondoka? - ameondoka saa ngapi?"

"Asubuhi ya usiku," akajibu kijakazi. Uso wake alikuwa ameuelekezea chini.

"Amekuaga - amekuambia anaenda wapi?"

"Hapana, Sultana. Hakuniambia chochote zaidi ya kusema anaenda, lakini amewaachia walinzi maelezo zaidi. Nikakuitie?"

"Fanya hivyo," Malkia akaagiza. Kijakazi akatoka upesi na punde akarejea na mwanaume mrefu mweusi akaaye getini. Akamsalimu Sultana, na kusema ameitikia wito.

.

.

.

"Kwanini umemruhusu mtu atoke nyumbani kwangu usiku?" Akauliza mke mdogo wa Sultan. Macho yake yalikuwa yanawaka ukali. Uso wa mlinzi ulisadifu hofu.

"Haikuwa usiku, Sultana. Bali asubuhi ya mapema zaidi ... "

"Kwanini umemruhusu?"

"Sikuweza kumzuia, Sultana. Ni mtu mwenye madaraka na amri."

"Amekuachia maelezo yoyote?"

"Ndio. Alisema nikuambie ameenda nyumbani kwake. Anataka awahi kufika na ndio maana akatoka mapema. Ameomba radhi kwa kutokukuaga, ameahidi atarejea."

"Kuna kitu chochote alikuwa amebebelea?"

"Hapana, Sultana. Sikuona chochote kipya zaidi ya alivyoingia navyo."

.

.

.

Mke mdogo wa Sultan akaonyeshea ishara ya mkono, mlinzi akaondoka. Akabakiwa na kijakazi wake peke yake ndani ya chumba. Hakula sasa, mawazo yalikuwa yamemtinda kichwa na kumfumba mdomo.

.





Amekuja usiku na kudamkia safari alfajiri! Akawaza. Nimeongea naye kwa muda mchache kabla sijapoteza fahamu na kujikuta kitandani ... akachambua. Kuna kitu alikifuata. Kuna kitu alikitaka. Amekipata? Ndio, kama asingelipata asingeliondoka.

.

.

.

Mke huyu mdogo wa Sultan akajikuta anapoteza amani. Aliona kuna haja ya kufanya jambo haraka iwezekanavyo, basi akajiandaa kwa ajili ya safari ya kwenda kwa bibi yake kuomba msaada.

.

.

. ***

.

.

.

Majira ya mchana.

.

.

.

Jua likiwa linawaka, Rhoda alikuwa kazini kwake kwenye mgahawa ulioendelea kushamiri na kukua zaidi. Alikuwa amekaa kwenye chumba kidogo kilichojitenga kwenye ghorofa moja pekee iliyo mgahawani.

.

.

.

Chumba hicho kilikuwa mahususi kwa ajili ya mahesabu. Aliyekuwa anaruhusiwa kukitumia ni Rhoda peke yake. Humo ndani alikuwa akihifadhi makaratasi yake ya kimahesabu na hata pia dinari.

.

.

.

Akiwa anapitia mahesabuye, macho yake yakizama karatasini, akasikia hodi mlangoni. Akatazama mlangoni pasipo kuuliza, na mara akasikia sauti yasema:

"Una mgeni, mam."

"Nani?" Rhoda akauliza akikunja sura.

"Mfalme!" Sauti ikajibu. Haraka Rhoda akasimama. Akajitazama na kujitengenezea. Akatoka ndani ya chumba na muda si mwingi akarejea na Phares ndani ya chumba.

"Karibu sana," akasema akimtengea kiti Phares.

"Ahsante sana, nimekaribia." Phares akaketi akitazamatazama mazingira ya ndani ya chumba.

"Mbona umekuja kwa kun'shtukiza hivi? Hata sijapata nafasi ya kujiandaa!"

"Kujiandaa na nini?"





"Kumlaki mfalme!"

"Huna haja ya kujiandaa. Mimi sio mfalme wa kuja na maelfu ya watu. Napenda maisha yangu ya kawaida."

"Wewe si raia wa kawaida tena, Phares. Inabidi ujue hilo. Unapokuwa kiongozi mkubwa, maadui nao pia hunyanyuka. Watu hukutazama na kukutilia maanani. Ni lazima usalama wako uwe kipaumbele."

"Nimekuja na walinzi sita. Wadogo hao?"

.

.

.

Rhoda akaangua kicheko.

.

.

.

"Ni wadogo, Phares. Hawatoshi kabisa kwa mfalme."

.

.

.

Phares akatabasam na kunyanyua nyusi.

.

.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

.

"Tuachane na hayo, Rhoda," akasema. "Mie nimekuja hapa kuitikia wito wako. Siku ile ya kuapishwa ulisema kuna jambo tunatakiwa kulijadili na kulimaliza." "Ndio," Rhoda akadakia. Akafungafunga mahesabu yake na kuyaweka kando apate mwanya wa kuteta zaidi.

"Si jambo geni, Phares. Nawe pia unalijua hili. Ni jambo ambalo wewe na mimi tunalihitaji, lakini pia Goshen kwa ujumla," akachombeza Rhoda kabla hajaenda kwenye mada kuu. Phares akajikuta anatabasamu tabasamu la kujua kifuatacho.

.

.

"Ni mkufu, sio?" Akauliza.

"Ndio wenyewe," Rhoda akajibu na kuongezea, "Kama unataka kujua chimbuko lako, kama unataka kuilinda Goshen kwa kuwa mwenye nguvu zaidi, tunauhitaji mkufu."

"Na kwako je?" Phares akauliza. "Utanufaika na nini na mkufu huo?"

.

.

.

Swali hilo likamkaba Rhoda shingo. Akashusha pumzi yake kwanza kabla hajatabasamu.

.

.

.

"Phares," akaita. "Mkufu ule ni wa kike, unadhani utakaa kwenye shingo na kulala kwenye kifua cha mwanamke gani?"





Phares akashindwa kujizuia kutabasamu. .

.

.

Rhoda alikuwa mjanja na akili yake ilikuwa nyepesi kwenye kufanya maamuzi ya tija. Alikuwa anahitaji mkufu lakini haja hii haikutakiwa kuwa wazi, ni hatari.

.

.

.

"Sawa," Phares akasema. "Sasa tunafanyaje kuupata huo mkufu?" "Ni lazima twende Tanashe," akasema Rhoda kwa upesi. "Huko ndiko mkufu ulipo. Hatujapata taarifa nyingine zaidi ya makazi hayo."

"Tanashe?" Phares akauliza kana kwamba hajasikia.

.

.

"Ndio, Tanashe," Rhoda akasema akitikisa kichwa. "Au una njia mbadala?"

"Hapana, sina." Phares akatikisa kichwa. "Ila habari za huko Tanashe zinatisha. Nimesikia ni tawala ya wachawi, tena nguli. Wale wote walioasi na kukamatwa na ulozi, walitupiwa huko. Tutafanikiwa kweli kuupata mkufu?"

"Penye nia, hapakosi njia," Rhoda akasema. "Endapo kama hatutaupata mkufu huo, Goshen waweza utumia. Hiyo humaanisha kwamba nasi tutakuwa hatarini. Kumbuka mipaka yetu imepakana na tawala mbili hasimu, Tanashe na Devonship. Hakutakuwa na wa kuturehemu."

.

.

.

Phares akakaa kimya kwa muda. Akili yake ilikuwa nzito. Tayari alijiona ndani ya Tanashe akipambana na walozi, ila akizidiwa. Alikosa namna ya kupambana na maadui. Alijiona anashindwa kabisa kwa ukosefu wa mbinu ya vita. .

.

.

"Ila," Rhoda alisema kwanguvu, Phares akashtuka. "Kuna namna ya kufanya."

"Namna ipi hiyo?"

"Namna ya kutukinga dhidi ya walozi hao ndani ya Tanashe. Nadhani nina wazo la kusaidia."

"Ndio."





"Kuna mwanamke mmoja anaishi Haiba, almaarufu kwa jina la Venin. Yeye aweza kutusaidia kwa namna kubwa sana."

"Venin?"

"Ndio."

"Ni mtaalamu wa vita?"

"Tena sana. Ila vita ya ulimwengu wa pili."

"Ukimaanisha?"

"Vita ya kilozi. Ni mtaalamu wa mambo ya giza. Nguvu na uwezo wake havina mfano. Anaweza kututengenezea kinga tukapambana na walozi hao kama binadamu wenzetu."

"Kabisa?"

"Ndio. Lakini ..."

"Nini hiko?"

"Ada yake huwa kubwa sana. Na ni kwasababu hatakagi kuharibu kazi yake kwa kufanya mambo yenye uhakika."

"Sawa, unapendekeza nini sasa?"

"Tufunge safari kwenda kumuona. Najua umebanwa na majukumu ya kiuongozi ukizingatia umeingia madarakani hivi karibuni. Hivyo basi, ningependekeza niende mwenyewe kusimamia hilo jambo."

"Unaweza? - vipi kuhusu biashara yako?"

"Biashara yangu si kubwa kama himaya ya Goshen. Hatuwezi kutoenda wote tukaagiza wengine."

"Sawa," Phares akatikisa kichwa. "Tutafanya kama ulivyosema. Ila lini sasa?"

"Kesho!"

"Kesho?"

"Ndio, mfalme. Hatuna muda wa kwenda na maji."

"Sawa. Basi acha nikakuandalie utaratibu mzuri."

"Bila shaka sitakusumbua sana."

"Shaka ondoa."

.

.

.

****

.

.

.

Majira ya jioni.

.

.

.

Baada ya masaa kadhaa, Malkia akaamka na kurudi kwenye fahamu zake. Alikuwa amezingirwa na Fluffy na Zura ambaye juu ya mapaja ya huyo mwanamke alikuwa ameweka kichwa.

.

.

.

Mazingira yalikuwa tulivu sana. Walikuwa ndani ya chumba kimoja kidogo chenye mwanga hafifu.





Malkia alikohoa mara tatu kisha akajinyanyua kuketi. Akatazama watu waliomzunguka kabla hajashika kichwa chake na kuukunja uso.

.

.

.

"Pole sana, Malkia," akasema Zura. "Unajisikiaje?"

"Kichwa kinaniuma," Malkia akajibu, kisha akauliza; "hapa tupo wapi?"

"Tupo kwenye himaya ya wanyang'anyi," Fluffy akajibu.

"Wako wapi?" Malkia aliuliza.

"Wako nje," Fluffy akajibu upesi. Malkia akataka kunyanyuka.

"Tulia Malkia, hauna nguvu kwa sasa," Zura akawahi kumtuliza. "Unahitaji kupumzika zaidi. Na pia ule na kunywa vema."

.

.

.

Zura akamtazama Fluffy na kumtikisia kichwa. Fluffy akanyanyuka na kwenda nje, punde akarejea na mwanaume mmoja ambaye alisimama akimtazama Malkia kana kwamba kuna kitu anangojea.

.

.

.

"Huyu anaweza kukuelezea kidogo juu ya hali uliyomo," akasema Fluffy kisha akaketi akimwacha mwanaume asimame peke yake.

.

.

.

Mwanaume yule akasalimu kwa kuinamisha kichwa chake kisha akafungua mdomo.

.

.

.

"Hali unayojisikia sasa, na utakayoendelea kujisikia kwa muda, ni madhara ya vumba la Kuhani mkuu. Vumba hili hupatikana kwenye koti lake pindo la kushoto. Ni hatari sana. Endapo ukivuta vumba hili, hupoteza nguvu ya macho, mwili na kichwa huuma sana. Yeyote anayevuta vumba hili, akidondoka chini hawezi amka tena. .

.

.

Ni silaha kubwa sana anayoitumia Kuhani mkuu endapo akizidiwa. Silaha hii humuhakikishia ushindi katika vita yoyote ile. Aliitoa huko ng'ambo. .

.

.

Lakini tulistaajabu sana ulipovuta vumba hili na bado ukaamka. Hatukuwahi kuona hili. Achilia mbali kumshinda na kumuua Kuhani mkuu. Si jambo la kawaida kabisa. Na ndio maana tukaona tuwe wajakazi wako. Tupo tayari kukutumikia. Amri yako itakuwa maisha yetu."







"Hapana," akajibu Malkia. "Sihitaji kuongozana ma yeyote kwa sasa."

"Malkia," akaita mwanaume. Haikujulikana alijuaje kama aongeaye naye ni Malkia, aidha aliambiwa na Zura ama Fluffy. "Haujui tu ni namna gani umetusaidia kwa kummaliza Kuhani mkuu," mwanaume akaendelea kunena. "Tulikuwa tunashurutishwa kuiba kila mmoja akipigiwa mahesabu ya mapato yake ili apewe mgao wa chakula. Tulikuwa watumwa, hata pale tulipokimbia tulitafutwa na kuuawa.

.

.

.

Kumuua kuhani mkuu, si tu kwamba umetufanya tuwe huru, lakini pia umetufanya tuwe yatima tukimkosa kiongozi. Tunaomba ujaze nafasi hiyo kwa kuwa kiongozi wetu.

Tunaomba utufikirie."

"Sawa," Malkia akaitikia na kisha akasema: "Unaweza ukaenda."

.

.

.

Mwanaume akatoka ndani.

.

.

.

"Malkia," Fluffy akaita punde tu baada ya mwanaume kurudishia mlango. "Tafadhali naomba uwakubalie."

"Unawaamini vipi?" Malkia akauliza. "Na nitawalisha kipi?"

"Laiti kama wangelikuwa si kuwaamini, wamgetuvamia na kutumaliza pindi ulipokuwa hujitambui," akasema Fluffy. "Na kuhusu watakula nini, kumbuka hawa ni watu wazima, ni nguvu kazi kubwa ya kutenda jambo, tena kubwa. Fikiri mara mbili."

.

.

.

Malkia akabinua mdomo. Akamtazama Zura kwa macho ya maulizo. Zura akapandisha mabega yake juu.

.

.

.

"Endapo ukiwakubalia, utakomesha uhalifu kabisa upande huu wa dunia. Wanataka na wamedhamiria kuwamaliza makuhani wote."

"Makuhani?" Malkia akastaajabu.

"Ndio, makuhani," Fluffy akajibu na kuongezea: "Makuhani wapo wanne kwa idadi. Kila mmoja ana upande wake, tawala yake na watu wake. Watu hawa wanakuwa na alama ya kuwajulisha wao wanamilikiwa na nani.





Zaidi, Makuhani hawa japokuwa wapo himaya tofauti, wanashirikiana na kusaidiana. Endapo mtumishi wao mmoja akitoroka, basi yeyote atakayemuona atamkamata na kumrejesha.

.

.

.

Hivi alivyomalizwa mwenzao, basi nao watahaha kukutafuta popote ulipo, kwa gharama yoyote, wakumalize. Hawatalala mpaka wamwage damu yako."

.

.

.

"Hawataweza," akasema Malkia akitikisa kichwa. "Kabla hawajanitafuta wao, nitawatafuta mimi."

.

.

.Ndani ya majira ya usiku, wanaume wakaandaa karama kubwa kwa ajili ya kumkarimu Malkia. Walipika vyakula na pia wakapiga muziki. Waliyafuma mazingira yapendeze kwa ajili ya shughuli. Walijigawa na kupeana majukumu huyu akipika, na yule akihudumu.

.

.

.

Kwenye meza kuu aliketi Malkia, Zura pamoja na Fluffy. Meza yao ikajazwa na vyombo vya dhahabu vilivyobebelea mvinyo na vyakula pomoni. Vyakula kama nyama za kukaanga na vichezesha taya vingine vya mafuta, ndivyo vilijaza sinia. .

.

.

Wanaume watano wenye ujuzi walipiga vinubi na gitaa kwa ustadi. Wanaume kama kumi na tano wakawa wahudumu wa kuwaletea wenzao vinywaji na kuwajazia vyakula. Palipendeza, ungeweza kudhania sio pale penye mabati na vifaa vikuukuu.

.

.

.

Mwanaume mmoja, yule aliyetengwa kuwa msema chochote wa shughuli, akasimama na kutaka kuwe kimya. Watu wote wakanyamaza na kumuazima masikio na macho. Mwanaume huyu alikuwa na sauti kubwa iliyosikika na wote. Si bure alichaguliwa kuwa muongeaji.

.

.

.

"Karibuni sana karamuni," alipaza kisha akatabasamu. "Leo ni siku maalum na kubwa sana katika maisha yetu. Leo tunaenda kupata kiongozi mpya. Leo tunaanza mapinduzi ya makuhani!"

"Mapinduzi ya makuhani!" Wanaume wakapaza sauti wakipandisha vikombe vyao vya mvinyo juu.

"Leo cheni zinavunjwa, makoo yanaonja kileo. Leo matumbo yanajazwa nyama, mikono inanyooshwa. Ni lini?"

"Ni leo! Leo! Leo!" Wanaume wakaitikia wakinyanyua vikombe juu.





"Watoto waliopotea wanampata mama yao leo. Nisiwachoshe sana, leo tunamkabidhi koti la kuhani kiongozi wetu mkuu. Malkia Sandarus. Malkia aliye hai. Malkia anayeuongoza mkufu. Malkia wa Goshen amekuwa Malkia wa himaya ya wanyang'anyi!"

"Hapana!" Akasimama Malkia. Muongea chochote akaketi upesi.

"Nyie si wanyang'anyi tena," alisema Malkia akitikisa kichwa. Alikuwa amevaa gauni refu lilokaba mabega. Nywele zake zilikuwa zimekunjwa na kuviringitwa vema. Ndani yake cheni ya dhahabu ilikuwa imekatiza na kidani chake kikakomea kwenye paji la uso.

.

.

.

Kwenye shingo yake nyembamba ulizunguka mkufu wake, ukituamisha kidani kifuani.

.

.

.

"Hii siyo himaya ya wanyang'aji tena. Hii ni himaya ya Samaridi: ua ang'avu linalokaa pembezoni ya mto mpana usiokaukiwa na maji kamwe. Ua hili likachumwa na kupandwa bustanini. Huko nako likachipua na kuzaa kedekede!"

"Samaridi la bustanini!" Msema chochote akapaza sauti, wenzake wakaitikia: "Samaridi la bustanini!" Wakinyoosha juu mikono yao yenye vikombe vya mvinyo.

"Ndio, Samaridi la bustanini," akasema Malkia. "Hata zile harufu za pembeni zilizokuwa zinasumbua nyumba, sasa zitatokomezwa na Samaridi. Nyuki watasogea na kutengenza asali. Maisha yatakuwa yalivyokuwa, sivyo kama yalivyokuwa!"

.

.

.

Malkia akaketi, wanaume wakasimama. Walishangilia kwa juhudi. Walinyoosha mikono yao juu wakiimba jina la Malkia.

.

.

.

"Haya kaeni chini sasa," akaagiza Msema chochote akisimama. "Tumpe nafasi Malkia afanye uteuzi wake kisha mambo mengine yaendelee."





Malkia alikaribishwa, akasimama. Aliteua wanaume wanne ambao wangemsaidia katika uongozi. Kiukweli watu hao hawakuwa wapya, walikuwa ni viongozi tangu hapo awali, zaidi tu Malkia alikuwa ametia kauli kwenye uteuzi wao.

.

.

.

Baada ya hapo, Msema chochote, akiwa amebebelea koti kubwa jeusi, anamsogelea Malkia na kisha anapaza:

"Ewe Malkia wangu, hili ndilo koti la Kuhani mkuu. Sasa ni lako, umemkaimu rasmi."

.

.

.

Malkia alilipokea koti hilo akaliweka kando.

.

.

.

"Hiyo ni ishara kwa makuhani wengine wote, kuwa mwenzao umemmaliza. Hawaweza wakakuamini endapo hawatoona hilo. Hata wafuasi wake hawawezi kusadiki."

.

.

.

Malkia akatikisa kichwa kuafiki. Alinyanyua koti hilo juu pasipo kusema jambo, wanaume wakapiga kelele za ushindi.

.

.

.

"Unaweza ukaendelea sasa," akasema Msema chochote kisha akarudi zake kuketi.

.

.

.

Malkia alitabasamu pasipo kusema jambo mpaka pale wanaume waliponyamaza.

.

.

.

"Nashukuru sana kwa ukarimu, na kwa kuniunga mkono." Akatabasamu tena.

.

.

.

Unaweza ukadhani mwanamke huyu ni malaika pindi anapotabasamu. Uso wake ulikuwa unachanua na kuuchukua moyo wako kuukimbiza mbio. Lips zake nene ziliacha meno yake mazuri meupe yaangaze. Mashavu yake yalijaza uso. Macho yake mazuri yenye tembe za huruma na mvuto yalilengwa na machozi.

.

.

.

Ukimtazama mwanamke huyu unaweza hata ukala ugali mkavu na usinung'une. Anasisimua kwa uzuri. Lakini zaidi moyo wake mkarimu, msikivu, unaojali na kutunuku.





Kama kuna wanawake waliopewa upendeleo mpaka ukajiuliza ulimkosea nini Mungu asikuumbe hivyo, basi ni huyu: Sandarus. Ambaye waweza kuambiwa utafute kasoro yake ukaikosa.

.

.

.

"Moyo wangu unaniambia nimepata familia mpya nami nimekoshwa kwakweli," akasema Malkia. "Ila furaha hii haitakiwi iishie hapa bali isambae ikawe mali ya wote. Tunajua wenzetu wanateseka na kuhangaika. Wanahenyeka na kutumikishwa. Wangependa nao wapate mapumziko na faraja kama tuliyo nayo sisi, hatuna budi kuwasaidia.

.

.

.

Dunia inaangamia, si kwasababu ya watu wabaya bali kwasababu ya watu wazuri wasiochukua hatua.

.

.

.

Hatutaki kuwa miongoni mwa watu hao wazuri, tutapambana. Tutapambana kwa hali na mali kuwakomboa wengine na kuendelea kukuza jeshi letu zaidi na zaidi. Hatimaye tukawe na himaya kubwa ya maziwa na asali."

.

.

.

Malkia aliweka kituo akamtazama Fluffy, Fluffy akanyanyuka upesi.

.

.

.

"Huyu mnayemuona hapa, anaitwa Fluffy binti wa Gidion. Atakuwa jenerali wetu wa mapambano," alisema Malkia kisha Fluffy akaketi.

.

.

.

Malkia akamtazama Zura kwa tabasamu, Zura naye akasimama.

.

.

.

"Na huyo mnayemuona sasa huitwa Zura binti wa Ashok. Mshauri, kisima cha hekima na godoro la matumaini. Asingalikuwa yeye, nisingalikuwa hapa, nikiwa hai. Kwangu ni mama, mlezi na mkufunzi."

.

.

.

Zura akainamisha kichwa kisha akaketi.

.

.

.

"Nisiongee sana, kwa tahadhima naomba nimkaribishe jenerali wetu apate kutuanishia namna vile tutaenenda katika kuwakomboa wenzetu na kuwamaliza makuhani wote juu ya uso wa dunia."





Malkia akaketi, Fluffy akasimama. Gauni lake refu rangi ya kijani halimkufanyia unafki, alipendeza. Mikono yake iliveshwa bangili kubwa za thamani. Nywele zake ndefu alizibana na kuzilazia kifuani. Ungeweza dhani ni mlimbwende shindanoni, kumbe ni jenereali. .

.

.

Alisafisha koo lake akavuta pumzi ndefu, na mara akaanza kutema cheche. .

.

.

Mipango yote aliyoiweka bayana, haikuwa mipya kwani alikuwa tayari amekwishajadiliana na kuichambua na Malkia. Aliiwasilisha vema, alikamata masikio ya wasikilizaji wake kwa utamu wa sauti na mipango, kiasi kwamba alipoweka kituo kila mtu akashindwa kumnyima makofi.

.

.

.

Sasa ikawa imebakia utekelezaji tu. Amiri jeshi mkuu, Malkia Sandarus, akasimama na kulitolea ufafanuzi kwa mujibu wa mamlaka yake.

.

.

.

"Tutaanza utekelezaji kesho!" Alisema. Wanaume wakalipuka kwa shangwe!

.

.

.

.

. ***

.

.

.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

.



Usiku ulienda, jua likachomoza. Nalo halikusimama, likaenda na wakatiwe. .

.

.

Ilikuwa sasa ni majira ya mchana, ya mithili ya saa sita za majira yetu, msafara za farasi watano ukionekana kwa mbali ukishikilia barabara ya kufuata jengo kubwa la Karim: mganga maarufu kwenye himaya ya waarabu.

.

.

.

Msafara huo ukiwa huko huko mbali unaonekana, na mara taarifa zinafika kwa Karim kuulizwa kama anategemea ugeni. Mwanaume huyo alikuwa uani akifanya ulozi wake wa hali ya hewa. .

.

.

Kichwa chake alikuwa amekivesha kofia kubwa nyeupe mithili ya puto, ila lenye ncha. Alikuwa kifua wazi akivalia suruali nyeupe ambayo ilikaba kiuno na enka pekee huku kwengine kukiwa tepetepe. Miguuni alikuwa peku.





"Ugeni?" Aliuliza.

"Ndio, ugeni!" Akajibu kibaraka. Mwanaume mfupi mwekundu.

.

.

.

Karim akatikisa kichwa, kibaraka akaondoka. Alipangusa paji lake la uso kisha akasema maneno ya ajabu, mara akaanza kuona taswira kiganjani mwake. Taswira ya farasi watano migongoni wakibebelea wana adam.

.

.

.

Alitazama vema akamuona mke mkubwa wa Sultan. Akajikuta anatikisa kichwa.

.

.

.

"Dada," alijisemea mwenyewe, akatoka uani na kwenda kumlaki mgeni. Kujisitiri kifua, akajivesha koti refu la kanzu. Nalo rangi yake ilikuwa nyeupe. Ila bado alikuwa peku.

"Karibu sana," akasema Karim akipanua kwapa za mikono yake. Sultana akashuka wakasabahiana.

"Nimeshakaribia," alisema Sultana kwa bashasha la furaha.

"Sikutegemea ujio wako."

"Kwanini? Ulidhani nitachukua muda gani kupata nywele za yule mzandiki?"

.

.

.

Karim akacheka pasipo kutia neno. Walizama ndani wakaituliza miili yao kwenye kochi zenye minofu.

.

.

.

"Pole na safari, umetoka usiku sana."

"Hakika."

"Bila shaka Sultan hayupo, asingalikuruhusu."

"Kweli, hayupo. Amepata tripu ya kueleka Uajemi. Atakuwa huko kwa majuma."

"Vipi, mbona haehae hivyo? Unataka sema umepata nywele zake za utosi?"

"Ndio nimezipata. Bila shaka haukuwa unanitegemea kuniona upesi hivi."

"Kabisa."

"Nilipotoka hapa nilienda moja kwa moja kwenye makazi yake. Huko nikamtilia ile dawa ndani ya mvinyo. Hakuamka mpaka nikamaliza kazi yangu. Mapema nikaondoka."







"Ni lazima atajua kuna jambo ulilifuata, na pengine anaweza kuchukua hatua."

"Ipi? Sidhani kama anayo nyingine zaidi ya kukimbilia kwa bibi yake."

.

.

.

Wakaangua cheko.

.

.

.

"Endapo kama tusingeipoteza dawa ile kimazingara, hivi sasa yangekuwa mengine," alisema Sultana.

"Ni kweli," akadakia Karim. "Pengine usingekuwa na mume saa hii." .

.

.

Sultana akatabasamu. "Haiwezi kabisa kutokea." .

.

.

Alitoa nywele alizokuja nazo akiendelea kunena.

.

.

.

"Nilikuwa mke wa Sultan kabla Sultan hajawa Sultan. Kipindi hiko alikuwa ni mtoto wa Sultan. Mimo ndiye mwanamke wa kwanza kuniona na kunipenda, akaniweka ndani. Hao wengine ni nzi nje ya nyavu, hawawezi kunisumbua."

.

.

.

Akamkabidhi Karim nywele.

.

.

.

"Hizo hapo."

.

.

.

Karim akatabasam.

.

. "Sasa wataka nimfanye nini? Hapa twaweza kumfanya hata bundi."

"La hasha! Sitaki awe mnyama, roho itan'suta."

"Sasa nini wataka Sultana?"

"Kengeusha akili yake. Bakuli aite jibini. Hadubini aite miwani."

.

.

.

Karim akazalisha tabasamu usoni. "Hilo tu?"

"Hilo tu!"

"Basi umefika, sasa vita itakuwa ya mabua. Pumzika kwa muda huu, jioni itakapowasili tutamaliza kazi mara moja kwa zote."

"Sawa, ila kaka nina jambo."

"Lipi hilo?"

"Ni masiku sasa, hujapata nipa mrejesho wa mkufu - hujapata lolote kupitia macho ya ndege wako?"

.

.

.

Uso wa Karim ukanywea. Alitua pumzi ndefu kabla hajatikisa kichwa chake mara tatu.

.

.

.

"Sijapata kitu," akajibu. "Ni muda mfupi tu nimeshuhudia vibaraka wangu wakigeuka na kuwa wanyama. Kinga nilizowapa hazikuwasaidia. Sasa hivi wanarandaranda huko misituni."





"Sasa umepangaje?" Sultana akakohoa swali.

"Hakuna lingine zaidi ya kwenda mwenyewe," Karim akajibu akisimama.

"Nadhani nikuache upumzike, nami nikaweke mambo sawa kwa ajili ya zoezi la baadae," alisema mwanaume huyo, Sultana akamuunga mkono.

.

.

.

Ulipowadia wakati wa jioni, wote wakiwa wamejivesha kanzu nyeusi wakasimama huko uani. Walikuwa wamejichora michoro isiyo na mantiki nyepesi. Walikuwa peku. Vichwani walivalia viremba vyekundu kwa sare.

.

.

.

Mbele yao kulikuwa kuna chungu kikubwa ambacho makalio yake yalikuwa juu ya moto mkali. Kwenye kuta kulikuwa kumepachikwa vioo vikubwa hivyo kutengeneza mazingira ambayo yangekufanya uone eneo hilo ni kubwa kama kiwanja cha mpira.

.

.

.

"Nitakaposema maneno haya, nawe utanifuatiza," alisema Karim akimtazama Sultana.

"Sawa," Sultana akajibu. Uso wake ulikuwa na hofu.

"Usiogope, dada. Halitachukua dakika kumi kuisha. Umesikia?"

"Ndio."

"Kuna maneno nitayatamka, na mara utamuona mlengwa wako kwenye vioo vyote. Atakuwa anakutazama, na wewe utamtazama machoni na kunuwia unachokitaka. Umeelewa?"

"Ndio."

.

.

.

Karim akanyamaza. Palikuwa kimya kwa kama dakika mbili hivi. Mara Karim akaanza kuteta maneno kadhaa ya ajabu. Chungu kikaanza kufuka na kufuka kana kwamba kinapikiwa na magma.

.

.

.

Ila zoezi hilo lisidumu, mara kijakazi wa Karim akaja upesi na kuwashtua.

.

.

.

"Mkuu!" Kijakazi alipaza sauti.





"Nini?" Karim akawaka. Macho yake yalikuwa mekundu kwa ghafira.

"Tuna ugeni, mkuu! Sultan anakuja!"

.

.

.

Taarifa hiyo ikawa kama bomu la nyuklia. Sultana alichanganyikiwa. Alikung'uta mikono yake kama inawaka moto.

.

.

.

"Mamamama! Nakufa! Sultan akinikuta huku atanimaliza!"

"Tulia," Karim akaagiza. "Tulia ... tulia hivyo hivyo! Sasa sikia, nitakupoteza kwa muda. Upo tayari?"

"Utanipoteza?"

"Ndio!"

"Kivipi?"

"Sultana, nitakufanya uwe upepo kwa muda mchache. Sultan akiondoka, nitakurejesha."

.

.

.

Hilo swala bado likawa gumu kwa Sultana.

.





"Dada, hatuna muda, Sultan atatukuta hapa!" Alisema Karim akitoa macho kumtazama Sultana. Joto lilikuwa kubwa. Akili ya Sultana ilivurugika, alishindwa kufanya maamuzi akabaki tu ameduwaa.

.

.

.

Karim alinena maneno kadhaa kisha akapangusa viganja vyake kwanguvu, na kumpakaa Sultana usoni, kufumba na kufumbua Sultana akapotea! Alijitahidi kubadili mazingira yasilete walakini, akafanikiwa kwa kiasi kidogo sana kwani vitu vilikuwa vingi. Maandalizi yalichukua muda hivyo huwezi yatengua ndani ya sekunde chache tu.

.

.

.

Alijikuta anakutwa na Sultan akiwa anahangaika. Aliigiza kama mtu asiyejua ujio huo, akashangazwa na kumuona kiongozi mkubwa mbele ya macho yake.

.

.

.

Alitabasamu akikutanisha viganja.

.

.

.

"Sultan!" Aliita. Aliinamisha kichwa chake kisha akaendeleza soga. "Mbona ghafla kiongozi wangu, utokako kwema?"

.

.

.

Sultan alitazama mazingira kwa muda wa dakika tatu pasipo kusema jambo. Aligeuka akawatazama walinzi wake wawili na kuwatikisia kichwa, walinzi wakaanza fanya upekuzi wakienenda na kutazama huku na huko.

.

.

.

"Sultan, kuna shida gani kiongozi wangu?" Aliuliza Karim. Bado Sultan hakutaka kuongea, bali kutazama mazingira.

"Naomba unishirikishe, pengine naweza nikasaidia," alishauri Karim. Sultan akamtazama mwanaume huyo kwa macho ya ghafira.

.

.

"Ulishindwa kwenye mkufu, utaweza nisaidia na nini kingine?" Aliuliza. Karim akapata haya.

"Sijashindwa, Sultan. Ni kitendo cha muda tu."





"Karim, unadhani tunaishi duniani milele?"

"Hapana, kiongozi. Jambo hili limekuwa zito sana. Si jepesi hata kidogo. Kila kona ya ulimwengu huu inataka mkufu huo. Hakika ngoma hii si lelemama."

.

.

.

Ghafla walisikia sauti ya mwanaume inalia kwanguvu. Walishtuka wakakimbilia huko sauti ilipotokea. Walimkuta mlinzi akiwa amelala chini amefichama uso wake. Pembeni kulikuwa kuna chungu, kile Karim alikuwa anatumia kupikia madawa.

.

.

.

"Nini hiki?" Aliuliza Sultan.

"Ndio maana nikakuomba unishirikishe, Sultan, tuepushe mambo haya," Karim alisema na kuongezea: "Hii ni dawa niliyokuwa naitengeneza, ni kali na ya moto sana"

"Embu nione," Sultan akaagiza. Karim alifungua chungu, Sultan akatazama yaliyomo ndani akiwa amesimama mbali kupisha mvuke wa moto wenye harufu kali.

"Hizo ni nini, si nywele?" Sultan aliuliza akinyooshea kidole.

"Ndio, ni nywele, Sultan," akajibu Karim.

"Nywele za nani? Mbona ni ndefu, ni za mwanamke?"

"Ndio, Sultan. Nimezitoa huko kaskazini ya mbali, kwa mwanamke mmoja wa hadhi ya chini."

.

.

.

Karim alifunga chungu wakaongozana na Sultan kuelekea ndani.

.

.

.

"Karim, nimekuja kwako kwa madhumuni makubwa mawili, na sikuona kama nina haja ya kukutaarifu juu ya ujio wangu, ulipangwa uwe hivi hivi."

"Unanipa hofu, Sultan. Ingekuwa vema ukaniweka wazi," Karim alipendekeza. Walifika sebuleni wakaketi.

"Dhumuni langu la kwanza ni mke wangu, najua yupo hapa, japokuwa sifahamu haswa mahali gani. Nashindwa kuelewa mambo kadhaa kumhusu huyu mwanamke, na ningependa unipatie majibu ya mantiki."





Moyo wa Karim ukatikisika. Alimtazama na kumsikiza vema Sultan, alikuwa anaongea akiwa na uhakika kana kwamba aliambiwa na mtu anayemuamini kuwa Sultana yu pale. Alijikuta anaanza kuandaa na kupangilia majibu kichwani.

.

.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

.

"Nimesema hivyo kwasababu kwanza, wewe ni ndugu yake. Pili, wewe ni mganga, hivyo basi kwa hili nina uhakika waweza fua dafu. Sijamkuta mwanamke huyu nyumbani, na nimepewa taarifa hakuwepo pia kwa siku kadhaa. Kasri lilikuwa pweke akipuyanga. Nataka kujua kwanini."

.

.

.

Karim alishusha pumzi ndefu. Kwa kutazama mboni ya macho yake ungalifahamu namna gani alivyozama fikirani. Alichagua na kubagua maneno ya kujibu.

.

.

.

"Sultan, nimeshangazwa sana na habari zako," alisema Karim. "Sina taarifa yoyote kuhusu dada yangu, na wewe ndiwe umekuwa wa kwanza kunambia. Sijui alipo, lakini naweza kukusaidia kumtafuta."

"Alishawahi kuja hapa?" Sultan aliuliza. Karim alisita kujibu upesi swali hilo, ila kutokana na jibu lake la mwanzoni alikuwa tayari ameshajifunga. Hakuwa na budi kujibu:

"Hajawahi kuja."

"Tangu lini?"

"Ni muda mrefu sasa."

.

.

.

Sultan akatabasamu. Tabasamu hili halikuwa la kheri, hata Karim alilijua hilo.

.

.

.

"Vipi hao farasi na watumishi wangu niliowakuta kwenye ukumbi wa jengo lako? Ni wa nani?"

.

.

.

Hili swali likammaliza Karim. Sasa hakuwa na ujanja. Alijiona mjinga kwa kutojua hilo jambo na kulichukulia hatua mapema. Alijikuta anakosa jibu la maana, ila hakutakiwa pia kunyamaza. Akajitutumua kujibu:

"Watumishi na farasi hao niliwaagiza toka kasrini kwako. Nilituma ujumbe kwa Sultana kwamba nahitaji ulinzi zaidi, bila shaka akaamua kumsaidia kakaye."





"Ulituma ujumbe huo lini?"

"Siku kenda sasa zapita."

.

.

.

Sultan akasimama akiita:

"Karim!" .

.

.

Uso wake alikuwa ameukunja. Macho yake yakiwaka hasira.

.

.

.

"Unaiudhi sana kwa majibu yako. Hakika umenifanya nijihisi mtoto na mjinga mbele zako. Nimepoteza imani na wewe, na hata ile iliyobakia, ndogo mithili ya mbegu ya haradali, nayo umeisaga kwa ulimi wako.

Hautakiwi kuwa huru, wala hai."

.

.

.

Sultan alipiga makofi matatu, mara wanaume watano wakaingia ndani. Aliwaamuru wamkamate Karim haraka na kisha wakague nyumba nzima kumtafuta Sultana. Walinzi wakatii.

.

.

.

Walitafuta kila kona, hawakupata kitu. Walimfunga Karim mikono na miguu, wakamtia kwenye keji ngumu ya mbao waliyokuja nayo, wakaondoka naye.

Sultan hakupata wasaa wa kumalizia dhamira yake ya pili iliyomleta eneo hilo. Alipungukiwa subira.

.

.

.

.

.

***

.

.

.

.

Aliwasili mbele ya nyumba ya bibi yake ikiwa ni jioni nzito. Mwanamke huyu, Sultana mdogo, alikuwa ameongozana na wanaume wawili waliobebelea jambia ndefu na nguo za mapambano. Wanaume hao walikuwa warefu na wenye miili ya wana usalama. Nyuso zao zilikuwa ngumu,macho yao yalikuwa mepesi kurandaranda huku na kule.

.

.

.

Sultana alishuka upesi farasini, mlinzi mmoja akawakusanya farasi na kuwafungia, mwingine akaongozana na Sultana kuufuata mlango wa makazi, hapo Sultana akagonga si chini ya mara tatu pasi na mafanikio.

.

.

.

Aliita lakini bado ilikuwa bure. Alizunguka nyuma ya nyumba akaangaza, hakuona mtu. Alikasirika akavimbisha mdomo. Aliona muda unaenda kama vile risasi. Alienenda kwa majirani kuuliza, mmoja akamwambia bibiye ametoka tangu asubuhi, hakuaga anaenda wapi.





Sultana aliishiwa nguvu. Alirudi kwenye makazi ya bibi yake akaketi kibarazani akiweka tama. Alikuwa amechoka kweli, ila dhamira yake ya moyoni ilikuwa kubwa. Alisubiria kama lisaa limoja, akapitiwa na usingizi.

.

.

.

Hakujua alilala kwa muda gani, alikuja kushtuliwa na mlinzi aliyekuwa amesimama kandokando yake akimtaka aamke maana mwenyeji wake amekuja. Sultana akaamka upesi, akamkimbilia bibi yake na kumkumbatia. Bibi alikuwa amebebelea furushi kubwa alilolining'iniza kwenye mti uliolala begani.

.

.

.

Waliingia ndani, na pasipo kupoteza muda Sultana akamwambia Bibi kilichomleta.

.

.

.

"Kwahiyo hivyo tu?" Aliuliza Bibi.

"Ndio hivyo, bibi," akajibu Sultana, akiongezea: "Sijaelewa lengo lake lilikuwa ni nini, japokuwa najua si zuri. Haiwezekani aje usiku ghafla, nipoteze fahamu, nizinduke asubuhi, tayari ameshaondoka! Inaingia akilini kweli?"

.

.

.

Ungeweza kuona hofu juu ya uso wa Sultana.

.

.

.

"Usijali, mjukuu wangu. Ni jambo dogo sana hilo. Ilimradi umeshafika hapa, tena salama, basi kila jambo litaenda vema," alisema Bibi akimtazama mjukuu wake kwa macho ya matumaini. Alinyanyuka akaenda zake chumbani na kifurushi chake alichokuja nacho, baada ya muda kidogo akarejea akiwa amebebelea kachupa kadogo kanene chenye mfuniko mwekundu.

.

.

.

Ndani ya kachupa hako kulikuwa kuna vitu vidogo vidogo vya bluu vinavyowaka waka kama taa. Vitu hivi vilikuwa vinapaa vikienda huku na huku. Vilikuwa vingi kiasi. Mbali na vitu hivyo, chupa ilikuwa giza usimuone mtu wa upande wa pili.

.





"Vua nguo, ulale chini," Bibi aliagiza, Sultana akatii. "Fumba macho, hema kwa kina: vuta hewa ndefu ndani, toa hewa ndefu nje," Bibi alitoa maagizo mengine, Sultan akatii.

.

.

.

Akiwa ameshikilia kichupa kwa mkono wake wa kushoto, Bibi akaweka kiganja cha mkono wake wa kuume kwenye paji la uso la Sultana. Akafumba macho na kunena maneno kadhaa, alafu akaanza kuuzungusha mkono wake wa kushoto kila pande. Akanena tena maneno kadhaa yasiyoeleweka.

.

.

.

Bado akiwa amefumba macho, akaweka kichupa kile tumboni kwa Sultana, akasikilizia jambo hapo kwa sekunde tatu. Baada ya hapo aliweka kichupa kwenye paji la uso la Sultana, akasikilizia napo kwa sekunde tatu. Mara kichupa kikaanza kutikisika.

.

.

.

Bibi alifungua macho yake akatazama kichupa. Vile vitu vya bluu vilikuwa vinazunguka kwa kasi, na mara vikatengeneza taswira ya nywele, nywele alizokatwa Sultana.

.

.

.

"Alichukua hiki toka kwako," alisema Bibi akimuonyeshea Sultana kichupa. Sultana alifungua macho akatazama.

"Nywele!" Alistaajabu.

"Ndio, nywele," Bibi akajibu alafu akainamisha kichwa cha Sultana na kukipekua. Baada ya sekunde kadhaa, alisema:

"Amechukua nywele za utosi!" .

.

.

Macho ya bibi yalionyesha hofu. Nywele za utosi ni malighafi kubwa mno kwa walozi. Ni tofauti na nywele zingine, za upande mwingine. Nywele hizi zina mamlaka, na zina uwezo mkubwa wa kumfinyanga mwenye nazo kadiri mlozi anavyotaka. Utosi ni chanzo, lakini pia ni ufunuo.

.

.

.

"Sasa Bibi atakuwa amenifanyia nini?"

"Usijali mjukuu wangu, poa mama. Poa." .





Bibi alirudi chumbani, punde akatoka akiwa amevalia kitambaa cha rangi ya dhambarau kichwani na chupa ndefu yenye unga mweupe. Kitambaa hicho kilikuwa kimeandikwa lugha ngeni tusiyoitambua.

.

.

.

Bibi aliketi chini akifungasha miguu yake kana kwamba yu ndani ya dojo. Aifungua chupa akaweka unga kiganjani na kuanza kuurushia kwa Sultana aliyekuwa bado amelala chini. Baada ya hapo alifunga macho yake na kusafirisha mwili wake kilozi.

.

.

.

Akiwa fikirani humo, alipata kuona kila jambo alilolifanya Sultana mkubwa, na mpaka mwisho wake. Alirejea fahamuni akamwamsha Sultana, mjukuu wake, akiwa anatabasamu.

.

.

.

"Vipi Bibi?"

"Kila jambo lipo shwari," alijibu Bibi akionyeshea dole gumba. Alimwelezea mjukuu wake alichokiona huko ulimwengu mwingine. Sultana akachomoza tabasamu.

"Kwahiyo amekuwa upepo?" Aliuliza Sultana.

"Ndio, amegeuka upepo kumkimbia Sultan. Na Karim mgangawe amekamatwa, hamna wa kumrudisha kwenye umbo lake!"

.

.

.

Sultan alifurahi. Aliamka upesi akajivesha nguo.

.

.

.

"Vipi tena?" Bibi akauliza.

"Inabidi niwahi nyumbani, Sultan anaweza akaja," Sultana alijibu.

"Usiku huu?"

"Hapana, anaweza akaja asubuhi. Endapo nikitoka huku asubuhi, dhahiri ntachelewa. Unajua huku na makazi yangu kuna umbali mkubwa mno. Ila tokea kasri ya Sultan ni karibu usitoe jasho kabisa kufika."

"Vipi lakini usalama wako mjukuu wangu? Huoni hatari usiku mzito kuwapo njiani?"

"Ndio maana nimekuja na walinzi bibi!"





Sultana aliaga akatoka ndani, akakwea farasi na kutimka pamoja na walinzi wake.

.

.

.

***

.

.

.

."Kundi la kwanza litapita huku!" Alisema Fluffy akielekeza uelekeo wa kushoto. "La pili litapita huku." Akaelekezea kulia. "La tatu tutatumia njia hii." Akaelekeza kaskazini. "Tumeelewana?" Akaliza.

"Ndio!" Wanaume wakajibu kwa sauti kuu.

.

.

.

Mwanamke huyo alikuwa amevalia nguo za mapambano, ngumu na zenye uzibe mgumu kifuani. Miguu yake ilikuwa imefunikwa na viatu virefu mpaka magotini. Mkono wake wa kuume ulikuwa umeshikilia panga refu jembamba, na wa kushoto ulikuwa umebebelea ngao kubwa ya duara.

.

.

.

Alibana nywele zake vema. Mikono yake kwenye viwiko ilikuwa imefunikwa na kava gumu la ngozi. Alijiandaa kwa mapambano.

.

.

.

Alioongozana na wanaume mia tatu kwa idadi ya macho ya haraka. Wanaume hao nao walikuwa wamebebelea silaha mbalimbali, kama vile jambia, visu, shoka, miti yenye misumari na kadhalika. .

.

.

Malkia hakuwapo, alibakia nyuma pamoja na Zura wakiwa na idadi ya wanaume waliobakia.

.

.

.

Fluffy akiongozana na wanaume kadhaa, wakati wengine wakielekea pande zingine, walizama ndani ya himaya ya Kuhani wa pili mwanamke akiongoza msafara. Walitembea kwa takribani robo saa, wakaanza kuona makazi ya watu. Makazi haya yalikuwa dhoofu, useme yanaanguka upepo ukipuliza. Ndani ya makazi hayo kulikuwa kuna wanaume waliojilalia humo.





Tarumbeta kubwa lilipigwa na mwanaume aliyekuwa nyuma ya Fluffy. Tarumbeta lililia kwa sauti kuu na ikavuma ndani ya himaya nzima. Kila mtu mwenye uwezo wa kusikia akasikia, na kutazama itokeapo sauti hiyo. Kuhani alipanda chumba cha juu akaangaza, kwa mbali akaona kikosi cha watu wachache wakiongozwa na mwanamke.

.

.

.

Alijiuliza maswali kadhaa. Alishuka chini upesi akasimama mlangoni pa jengo lake kuu. Hapo alikuwa na wanaume takribani ishirini wakimlinda.

.

.

.

Kutokana na Fluffy kuongozana na wanaume ambao hawakuwa wageni ndani ya himaya ile, hakupata bughdha, bali alisindikizwa mpaka mbele ya nyumba kuu ya Kuhani mkuu, hapo akasimama.

.

.

.

"Wewe ni nani?" Kuhani mkuu aliuliza.

"Mimi ni Fluffy, kamanda mkuu wa himaya ya Sawaridi."

"Kamanda mkuu?" Kuhani mkuu aliuliza kisha akaangua kicheko. Wafuasi wake nao wakafuatia kwa cheko la haja.

"Kamanda mkuu? Sawaridi ndiyo nini? Na nyie ..." Kuhani mkuu aliwanyooshea kidole wanaume walioongozana na Fluffy.

.

.

.

"Huyu kikaragosi hapa ni nani?"

.

.

.

Kufumba na kufumbua, mkono wa Kuhani mkuu ulidondoka chini. Haikujulikana nini kilitokea, ila panga la Fluffy lilikuwa linachuruza damu.

.



Kuhani alitazama mkono wake uliokatiwa chini. Alichanganyikiwa kabla ya kuanza kulia kwa maumivu makali. Alipiga magoti akiuguza mkono wake uliokuwa unamimina damu pomoni.

.

.

.

Pasipo kuchelewa, wafuasi wa Kuhani wakawavamia Fluffy na jeshi lake, mapambano makali yakazuka. Waliwaweka walengwa wao katikati wakiwashambulia kwa silaha. Fluffy na jeshi nao wasiwe nyuma, wakajibu mapigo. Mwanamke aliwasulubu barabara! Alikuwa stadi kwenye kujilinda na kutumia jambia lake kukatakata maadui.

.

.

.

Pambano likadumu kwa dakika ndogo kabla Fluffy na kundi lake halijaibuka na ushindi. Ila vita haikuwa imekoma, kikundi walichopambana nacho kilikuwa kidogo tu, wanaume wengine wakaanza kujisogeza wakiwa wamejitosheleza kisilaha.

.

.

.

"Hatujaja kuwamaliza, bali kuwaokoa!" Akapaza Fluffy. .

.

.

"Ni muda wa nyie kuwa huru toka kwa Makuhani. Wenzenu wameweza, nanyi mnaweza pia. Mtaendelea kutumikishwa hivyo mpaka lini?"

.

.

.

Wanaume wa kuhani wakaendelea kuongezeka kwa wingi toka kila pande ya dunia. Nyuso zao zilikuwa zinatisha, walionyesha mioyo yao migumu kusadiki yaliyosemwa.

.

.

.

"Tusiuane wenyewe kwa wenyewe!" Akasema mwanaume mmoja aliyekuwa pamoja na Fluffy. Mwanaume huyu alikuwa ni miongoni mwa walioteuliwa kuwa viongozi. Alisonga mbele ya Fluffy akiwatazama wanaume wa Kuhani.

.

.

.

"Tusaidiane. Hii ndiyo nafasi yetu ya kutoka utumwani. Endapo tukiungana, makuhani wanakuwa si lolote si chochote,” akaendelea kusema mwanaume huyo kwa imani. “Tukipoteza nafasi hii tutakuja jutia na maisha yetu yote. Tutakuwa watumwa maisha yetu yote!”





“Muongo!” akapaza mwanaume wa Kuhani. Alisonga mbele kutazamana na mwenzake anayewashawishi. Akaendelea kuongea: “Usitufanye sisi wajinga, tuna akili timamu. Unataka kutuambia nyie …” akawa anawatazama Fluffy na wenzake. “Yani kwa mlivyo hivyo ndio wa kutuambia sisi kwamba mmefanya mapinduzi? Tena mkiongozwa na mwanamke!”

.

.

.

Kabla swali halijajibiwa, mara wanaume wote wa Kuhani wakapiga magoti wakiinamisha vichwa chini. Fluffy, pamoja na wenzake, wakatazama nyuma yao. La haula! Wakaona Kuhani amenyanyuka, na mkono wake uliokatwa ukiwa mwilini.

.

.

.

Ilikuwa ajabu na kweli. Haikujulikana ni kivipi Kuhani aliuunga mkono wake, na kwa muda gani. Hakuonyesha kabisa kama ametoka kupata majeraha, ama maumivu. .

.

.

Alikuwa amebadilika pia kimuonekano. Mwanzoni hakuwa na koti refu jeusi, ila sasa tunaliona. Mkononi alibebelea panga refu rangi ya fedha. Uso wake ulikuwa umejikunja kwa hasira ila akitabasamu kwa jazo la kejeli.

.

.

.

Fluffy alihofia kwa kiasiche. Halikuwa jambo la kawaida lile kulishuhudia, ukizingatia yeye ndiye aliyetenda tendo la kukata. Lakini kwakuwa yeye ni jemedari, hakutaka kukatisha tamaa wafuasiwe, akakamata panga lake ajitutumue.

.

.

.

Hakulirusha panga hilo hata mara moja, akasikia sauti kali ya kuamrisha toka kwa Kuhani. “Maliza wote!”

.

.

.

Haraka mwanaume yule upande wa Fluffy aliyebebelea tarumbeta, akalipuliza kwa nguvu na kwa ustadi. Sauti ya tarumbeta ikateka anga na kusafiri. Ikawafikia vikosi vingine ambavyo vilikuwa mbali.





Kufumba na kufumbua, vita ilishika moto. Fluffy na wanajeshi wake haki walizidiwa kutokana na idadi kubwa ya maadui. Wakati wakipambana Kuhani mkuu alikuwa amesimama kando akitazama.

.

.

.

Fluffy alipambana na kuwamaliza wanaume kadhaa, ila naye wafuasi wake wakauawa kadhaa. Hakuweza kuwalinda wote. Bahati nzuri, haukupita muda mrefu, wakatokea wenzao na kuwaongezea nguvu.

.

.

.

Kilikuwa ni kikosi kimoja, kile kilichoelekea kushoto pindi walipogawana mielekeo. Kuja kwa kikosi hiki kukawapa wenzao hamasa na nguvu zaidi ya kupambana japokuwa bado walikuwa wachache ukilinganisha na maadui wao.

.

.

.

Vita ilidumu kwa muda wa kama robo saa, mara kikosi cha tatu kikasikika kikija kwa shangwe. Walikuwa wamenyanyua silaha zao juu juu wakikimbia kwa kasi. .

.

.

Waliwaongezea nguvu wenzao, kwa kiasi fulani vita ikaonekana ya usawa. Lakini tendo hili la watu kuongezeka kwa watu, kukampa taarifa Kuhani mkuu, taarifa ambayo haikuwa nzuri fikirani.

.

.

.

Aliamini sasa mwanamke yule, Fluffy, alikuwa kweli ni kiongozi wa wanaume wale ambao anawajua yeye kama wafuasi wa Kuhani mwenzake. Na bado akaamini kuna uwezekano wa wao kuongezeka.

.

.

.

Alitazama mbali kwa sekunde kadhaa, lakini kichwani akijiuliza ni kwa namna gani mwanamke anayemuona, ambaye ni Fluffy, ameweza kufanya mapinduzi kwenye himaya ya mwenzake.





Alijikuta anapata mashaka, kama si hofu. Alimtazama vema Fluffy anavyopambana, ni kweli ana ujuzi, ila hakuona kama ulitosha kumfanya yeye anyooshe mikono juu na kuachia tawala yake.

.

.

.

Sasa ana nini cha ziada? Aliendelea kudadavua kabla ya kujiingiza mkenge. Macho na akili yake yakamuonyesha kwamba mwanamke huyo alikuwa na uwezo wa kuwapanga wanajeshi wake dhidi ya adui.

.

.

.

Kwa amri ya mwanamke huyo, wafuasi wake walikuwa wanajilinda na kushambulia kwa pamoja. Kutokana na nidhamu hiyo, walifanikiwa kuwapunguza maadui zao kwa wingi mkubwa mno. .

.

.

Kuhani akaona endapo akiacha pambano liendelee, hatabaki na mtu. Ni bora ajitose kati kupambana na Fluffy kwani alishaona mwanamke huyo yupo ndani ya uwezo wake jadidi. Akimmaliza, ndio utakuwa mwisho wa yote.

.

.

.

“Heeey!” akapaza sauti na mara watu wote wakamtazama. Akamnyooshea mkono Fluffy na kumuita akibinua mdomo wake.

.

.

.

Vita ikasimama kwa muda. Wanaume wakajitenga, wa Kuhani mkuu wakienenda upande wa kulia na wale walioongozana na Fluffy wakisimama upande wa kushoto.

.

.

.

Fluffy akasogea kwa ujasiri. Alimtazama Kuhani mkuu, akaona uso wake umejazwa na kebehi, dharau na majivuno.

.

.

.

“Upo tayari kufa?” Kuhani akauliza. Alikuwa anamtazama Fluffy kana kwamba mtoto swala mbele ya kucha ndefu za chui wakali.

.

.

.

Mwanaume aliyebebelea tarumbeta akapuliza mara nne kabla ya mpambano kuanza. Kuhani mkuu hakujali tarumbeta hilo, ila Fluffy alijua linamaanisha nini.





“Utakufa wewe kabla yangu,” alisema Fluffy. Alikuwa anajiamini. Hakutetereka akimtazama Kuhani machoni.

.

.

.

Kwa wepesi, Kuhani mkuu akatupa mkono wake wenye panga. Alikuwa na nguvu, hata pale Fluffy alipokuwa anapangua panga hizo, alionekana kupata shida ila alijitahidi kustahimili.

.

.

.

Alishambulia kwa mfululizo pasipo kumpa Fluffy nafasi ya kuvuta pumzi. Fluffy hakuwa na fursa ya kushambulia kwani alikuwa anajilinda muda wote dhidi ya ncha ya panga kubwa la Kuhani. .

.

.

Kadiri mwanamke huyo alivyokuwa anazidi kupambana, nguvu nayo ikawa inamuisha. Mbali na kwamba Kuhani alikuwa na nguvu, alikuwa na kasi pia ambayo ilikuwa inampelekesha puta Fluffy.

.

.

.

Ilimuwia vigumu kuendana na kasi hiyo, taratibu akaanza kujiweka wazi na Kuhani mkuu akamchanja takribani mara tatu kisha akammalizia mwanamke huyo kwa kumsindika teke na mguu wake wa kushoto, akarukia mbali.

.

.

.

Kuhani akaangua kicheko.

.

.

.

“Huyu ndiye wa kunipokonya himaya kweli?” akauliza akiwatazama watazamaji. Wafuasi wake wakapiga yowe za ushindi. Wafuasi wa Fluffy wakiwa wanamtazama jemedari wao anayejibaraguza chini kwa maumivu.

.

.

.

“Hakuna, na sijaona wa kunishinda. Kuna yeyote ajitokeze?” Kuhani akatazama upande wa wafuasi wa Fluffy. Kulikuwa kimya.

“Kuna yeyote anayetaka kuja kumtetea huyu malaya?” Akauliza tena. Punde akatoka mwanaume mmoja na kusimama mbele. Alikuwa ni yule mwanaume mshehereshaji – msema chochote tafrijani.





Wenzake walistaajabu. Hawakutegemea mtu yeyote kuthubutu kufanya hilo jambo. Ilikuwa ni kujitoa sadaka ukiwa na akili timamu.

.

.

.

Walitazamana kwa nyuso za maulizo. Walimtazama mwenzao kwa macho ya huruma. Ni kana kwamba walikuwa wanataka kumbadilisha mawazo, lakini haikuwa inawezekana.

.

.

.

Kuhani akacheka.

.

.

.

“Ndiyo wewe?” aliuliza kana kwamba haoni. Akacheka tena, wafuasi wake nao wakacheka.

.

.

.

Ila kabla pambano halijaanza, Fluffy akanyanyuka na kumtazama Kuhani mkuu. Alipaza sauti yake akisema:

.

.

“Anza na mimi kwanza!” .

.

.

Alikuwa amesimama nyuma ya Kuhani mkuu. Kwenye shavu lake la kulia alikuwa na chapa nyekundu kutokana na teke alilozabwa. .

.

.

Bado alionekana mwenye nguvu. Macho yake yalikuwa mekundu. Mkononi alikuwa ameshikilia panga peke yake, ngao akiwa ameiacha chini.

.

.

.

Kuhani mkuu akashangazwa. Hakutegemea kama Fluffy ataweza kunyanyuka tena kwa teke alilompa. Alimtazama mwanamke huyo kwa umakini akimsogelea. Kweli alikuwa ni mwanamke mwenye nguvu.

.

.

.

Wafuasi wa Fluffy wakalipuka kwa furaha. Walimtia moyo jemedari wao kupambana na kushinda. Walipaza sauti wakiita jina lake.

.

.

.

Fluffy hakungoja Kuhani mkuu aanze mashambulizi, akamvamia. Alijitahidi kupambana wakati Kuhani akipangua juhudi zake kwa wepesi, akitumia mkono mmoja. .

.

.

Kwa takribani dakika moja na nusu, Fluffy alitawala mchezo. Hakuweza kuendelea zaidi ya hapo kwani Kuhani alianza naye kurusha mashambulizi ya nguvu. Alimzidia Fluffy ambaye alianza kujongea akirudi nyuma.





Kama pambano lingeendelea kwa kama dakika moja tu mbele, haki Fluffy alikuwa anamalizwa. Mwanaume mshehereshaji aliligundua hilo, aliona Fluffy anahitaji msaada haraka.

.

.

.

Alikimbia akamrukia Kuhani mgongoni kisha akamkaba shingo kwa kutumia gongo lake kubwa. Kuhani akafurukuta kumbandua mwanaume huyo mgongoni. Fluffy akatumia nafasi hiyo kumshambulia Kuhani upesi kwa kumjeruhi kifuani na tumboni.

.

.

.

Kwa nguvu Kuhani akamtoa mwanaume mgongoni na kumrushia mbali. Kwa hasira akamfuata kwanza mwanaume huyo apate kumfunda adabu, ila kabla hajafika Fluffy akamkimbilia upesi.

.

.

.

Haraka Kuhani akageuka akabiliane na mwanamke huyo. Alikuwa makini na mikono ya Fluffy, ila pasipo kutarajia, Fluffy hakurusha panga, bali akachota mchanga na mguu wake, akamwagia Kuhani usoni.

.

.

.

Kuhani akapiga kelele, upesi alianza kufikicha macho yake kwa mkono mmoja huku uliobebelea panga ukihangaika kwenda huku na huko hovyo kumlinda dhidi ya Fluffy ambaye alikuwa hamuoni.

.

.

.

Hiyo ikawa fursa adhimu sana kwa Fluffy. Akaruka juu na kuchanua miguu yake kama maua, akamzaba teke maridadi Kuhani mkuu akitumia nguvu na uzito wa mwili wake wote. Kuhani akaanguka kama gunia la mkaa.

.

.

.

Kukawa kimya tuli. Hakuna aliyesema jambo zaidi ya wote kumtazama Kuhani. Fluffy alikuwa anahema kwanguvu. Akilini mwake alikuwa anachambua na kupanga jambo la kufanya.





Ni wazi hakutakiwa kungoja Kuhani mkuu asimame kwani itamuwia vigumu kumwangusha tena. Hii ndiyo ilikuwa fursa yake kuhitimisha mchezo. Kuhani mkuu alikuwa chini akigugumia kwa maumivu huku ameshikilia kichwa.

.

.

.

Panga la mwanaume huyo lilikuwa kando, isijulikane litanyanyuliwa muda gani. .

.

.

Fluffy akajongea kumfuata Kuhani. Akamtazama kwa hasira akinyanyua panga. Ajabu, ghafla, Kuhani akazunguka kwa mgongo wake akizungusha miguu yake mizito iliyomkita Fluffy na kumdondosha chini.

.

.

.

Kufumba na kufumbua, Kuhani mkuu ananyanyuka kwa kuchumpa na mikono yake. Alimgeukia mwanaume mshehereshaji, upesi akaruka juu akifungua koti lake refu kufyagia hewa. .

.

.

Mara mwanaume mshehereshaji akaanza kulia akifunika macho, mara kichwa! Alilia kwa sauti kuu. .

.

.

Kuhani, ambaye uso wake ulikuwa umejaa kwa hasira, akageuka na kumtazama Fluffy, bado alikuwa chini. Akanyanyua panga lake akimfuata mwanamke huyo kwa hatua pana.

.

.

“Nakumaliza malaya wewe!” akafoka.

.

.

“Si haraka kiasi hicho!” mara sauti ya kike ikajibu nyuma yake. Haraka Kuhani akatazama nani huyo aliyepaza sauti juu yake.

.

.

.

Uso kwa uso akakutana na Malkia. Alikuwa juu ya farasi wake mweupe. Nywele zake alizibana vema mgongo wake akiufunika na shuka la kahawia iliyokoza. Alikuwa tayari amejiandaa kwa pambano, kwa mujibu wa mavazi wake.

.





Farasi wake alikuwa anaendelea kutembea mpaka pale alipofika karibu kabisa na Kuhani. Malkia akashuka kwa kishindo. Macho yake mazuri yalikuwa yanamtazama Kuhani mkuu kwenye kiini.

.

.

.

Wafuasi wake walilipuka kwa shangwe. Walipiga nduru ndefu. Fluffy alijikuta anatabasamu kabla hajanyanyuka na kusimama sawa. Alikuwa anavuja damu kwenye kona ya kushoto ya mdomo.

.

.

.

“Huyu ni nani?” Kuhani akauliza akinyooshea kidole kwa Malkia.

.

.

“Huyo ni Malkia! - Malkia! - Malkia!” wanaume wakapaza sauti kuu.

.

.

“Mimi ni Malkia,” Malkia mwenye akajibu akijiwekea kidole kifuani.





Msafara wa farasi nane ulikuwa unakatiza katikati ya msitu wa wastani wenye umbijani wa kuvutia kana kwamba bustani. .

.

.

Hali ya hewa ilikuwa ni ya kaubaridi lakini jua likiwa limesimama. Kulikuwa tulivu haswa haswa, sauti za kwato za farasi ndizo zikisikika.

.

.

.

Farasi wawili walikuwa wamefungwa na kamba ngumu wakikokota kitoroli kidogo cha matairi. Dereva wa farasi hao alikuwa ameketi kwenye kakiti kadogo kalichojishkiza kwenye katoroli.

.

.

.

Mikono yake ilikuwa imeshikilia kamba alizokuwa anatumia kuwaongozea farasi. Alikuwa amejivika suti ya kale, mdomoni akiwa anavuta sigara kubwa rangi ya kahawia.

.

.

.

Mbali na farasi hao wawili, farasi wengine sita walikuwa wamewabebelea wanajeshi migongoni. Wanajeshi hawa walikuwa wamebebelea mikuki mirefu yenye nyoya za rangi nyekundu.

.

.

.

Walikuwa wamejipanga kimstari nyuma ya kitoroli kuhakikisha ulinzi.

.

.

.

"Bonas!" Sauti ya kike iliita tokea ndani ya kitoroli. Ilikuwa ni ya mwanamke Rhoda pasi na shaka lolote.

.

.

.

"Naam, mam!" Akaitikia dereva farasi akitenga sikio.

.

.

"Na hapa ni wapi?"

"Hapa ni msituni, mam. Tumebakiza kama maili thelathini sasa kufika."

"Kote huku ni kwa Venin?"

"Ndio, kote huku ni mali yake. Ana eneo kubwa mno. Wale wote wanaomkaidi, kumletea jeuri na kumshupazia shingo huwaua na kuwatupia huku msituni wawe chakula cha kunguru."





Kukawa kimya kidogo. Rhoda akafungua vizuri dirisha na kuangaza nje.

.

.

.

Baada ya muda mfupi, kwa mbali akaona mwili wa binadamu ukining'inia. Akashtuka na kuziba mdomo wake. Mwili huo ulikuwa tayari mweusi kwa kuoza.

.

.

.

Akamuita dereva farasi na kumuuliza:

.

.

"Anawaua kwa kuwanyonga?"

"Hapana, Venin hawezi nyonga mtu. Yeye hukumaliza mwenyewe kwa ulozi wake."

"Mbona nimeona mwili wa mtu unaning'inia?"

"Huyo hakuuawa na Venin, bali alijiua mwenyewe. Wafanyakazi wengi hujiua kwa kushindwa kuendana na mkuu wao.

.

.

.

Na hawana namna yoyote ya kumtoroka zaidi ya kujipokonya uhai."

.

.

.

Habari hizi zikamtetemesha Rhoda. Akameza fundo la mate kabla hajaendelea kutazama nje kana kwamba mtoto aliyejificha katikati ya mchezo wa komborela.

.

.

.

"Bonas, una uhakika tutatoka salama huko?"

"Bila shaka, mam. Tutatoka salama ... ila yatupasa tuwe wavumilivu na watiifu sana. Venin ana hasira za karibu. .

.

.

Muda mwingine hupenda kujaribia nguvuze kwa wengine. Ila baniani mbaya, kiatu chake dawa."

.

.

.

Mpaka wanamaliza msitu, Rhoda akawa ameshuhudia maiti za watu wasiopungua ishirini. Zingine zikiwa zinadonolewa na kunguru, zingine zikiwa zimeoza.

.

.

.

Mabaki mengine yalikuwa mifupa tu. Fuvu za vichwa vya binadamu, mbavu na mifupa mingine ya mwili.

.

.

.

Mambo haya yakachemsha hofu ya Rhoda. Isingalikuwa hitaji lake la mkufu lilikuwa kubwa, angeligeuza arudi nyumbani.





Baada ya masaa mawili wakawa wamefika mahali walipokuwa wanaona kasri kubwa ya Venin. Kasri hii ilikuwa inavutia kuitazama. Ilikuwa na rangi mbali mbali kama upinde wa mvua.

.

.

.

"Itabidi tuingilie geti la mashariki," akasema Bonas. "Kwanini?" Rhoda akataka kujua.

"Kwasababu ndilo geti la wageni. Tukipita huko kwengine tunaweza tukahisiwa vibaya. Mashariki ni kulia, kushoto ni kwa wenyeji tu."

"Bonas, ni mara ngapi umekuja huku kwa Venin? Unaonekana u mwenyeji sana!"

.

.

.

Bonas akatabasamu.

.

. "Mam, nimekuwa dereva wa wafalme kwa miongo kadhaa. Nimewapeleka wanapopataka, na hata wasipopajua. .

.

.

Nina uzoefu wa kutosha kwenye hii kazi."

"Ina maana kuna mfalme ulishawahi kumleta huku kwa Venin?"

.

.

.

Bonas akatabasamu. Hakujibu hilo swali, badala yake akabadili mada.

"Jiandae, mam. Tunakaribia kuingia kwenye kasri ya Venin."

.

.

.

Wakafika getini walipokuwa wamesimama walinzi wawili wa ajabu. Ngozi zao zilikuwa kama magome ya miti. Macho yao yalikuwa makubwa kama vibuyu.

.

.

.

Miili yao ilikuwa mipana na mizito. Kama viumbe hivi vikifumba macho, basi ungeweza kudhani ni miti ya miarobaini.

.

.

.

"Sandrit!" Bonas akasema akipandisha kiganja chake juu.

"Sandrit Vena bah!" Wakajibu wanaume hao wawili upesi.

"Gomi a tukir dumo Goshen. Fumik twenjher puska lakalabhante!"

.

.

Akasema Bonas kwa lugha waliyokuwa wanaelewana na walinzi hao.





"Bugku?" Akauliza mlinzi mmoja akinyoosha mkono wake wa kuume. "Mam," Bonas akaita. "Naomba unipatie ithibati."

.

.

.

Mkono wa Rhoda ukatoka nje ya kitoroli ukiwa umebebelea mto mdogo mwekundu wenye chapa ya Goshen iliyoshonelewa kwa nyuzi za dhahabu.

.

.

.

Mto huo ulikuwa unameremeta. Kwenye kila kona yake kulikuwa kuna manyoya yaliyobanwa kimafundo na pete za fedha.

.

.

.

Bonas akaupokea kwa mikono miwili kisha akauonyeshea kwa walinzi.

.

.

.

"Gee vah!"

.

.

Walinzi wakatikisa kichwa na kisha wakafungua geti. Rhoda na wafuasiwe wakaingia ndani.

.

.

.

Palikuwa pakubwa mno usidhanie kama ni eneo la jengo. Lakini palikuwa panatisha kwa namna palivyokuwa kimya kana kwamba eneo la makaburi.

.

.

.

Waliongozwa na mwenyeji wao mpaka eneo fulani hivi, chumba kidogo chenye viti vyekundu vya lakshari. Walinzi wakasimama wakati Rhoda akiketi pamoja na Bonas.

.

.

.

"Ngojeni hapa, atakuja hivi punde," akasema mwenyeji. Alikuwa mwanamke mweusi mwenye macho mekundu kama damu.

.

.

.

Akaondoka kuelekea upande wa kushoto.

.

.

.

"Bonas," Rhoda akaita.

"Naam!"

"Huyo Venin naye anaongea ile lugha uliyoiongea na wale watu kule getini?"

"Ndio," akajibu Bonas na kuongezea. "Ila anajua pia na lugha zingine hivyo usijali."

.

.

.

Kabla hawajatia tena neno jingine Venin akawa amefika na kusimama mbele yao. Hakuna aliyehisi ujio wake zaidi tu ya kumuona tayari ameshafika.





Alikuwa ni mwanaume mrefu mwembamba mweupe kama karatasi. Ndevu nyingi nyeupe. Macho yake yalikuwa mekundu mno. Alivalia kanzu nyeupe iliyoishia magotini ikapokelewa na suruali nyeupe iliyokomea kwenye enka.

.

.

.

Kisha viatu vinavyong'aa kama dhahabu.

.

.

.

Haki mtu huyu alikuwa anatisha kumtazama. Kama ungelikutana naye barabarani nyakati za usiku, basi ungeliweza kupoteza pumzi yako kwa hofu.

.

.

.

Alinyoosha mkono wake wa kuume, vidoleni alikuwa na pete kadhaa, akisema:

.

.

"Karibuni na poleni kwa safari."

"Ahsante sana," Rhoda akasema akisimama yeye na Bonas.

.

.

.

Wakapeana mikono na kutambulishana kabla hawajaenda ndani ya jengo, wakaketi sebuleni.

.

.

.

Sebule ilikuwa kubwa na pana. Ukutani kulikuwa kumepachikwa fuvu za kichwa na mifupa ya kwenye nyonga.

.

.

.

Chini kulikuwa kuna zulia jekundu lisiloonekana wapi komo lake. Samani za thamani ila kukiwa giza kwasababu ya kutokuwapo kwa madirisha.

.

.

.

Mishumaa iliyokuwa imepachikwa konani ndiyo ilikuwa inatoa mwanga, japokuwa bado ulikuwa ni hafifu.

.

.

.

"Ni nini kimekutoa huko Goshen mpaka hapa, binti?" Venin akauliza akisaidiwa na vidole vyake vyembamba vyenye kucha ndefu.

.

.

"Nimekuja unisaidie, Venin. Maana nguvu zako hazina mithili wala mipaka. .

.

.

Mie na jeshi langu tunataka kuingia ndani ya Tanashe. Kuna jambo marigoli nalitafuta. Ila najua fika tawala hiyo ni ya walozi wenye nguvu na mamlaka. Naomba unipatie ulinzi wako."





Venin akatabasamu pasipo kuonyesha meno.

.

.

.

"Tanashe?" Akauliza.

"Ndio, Tanashe," Rhoda akajibu upesi.

.

.

.

Venin akasugua kiganja chake kikavu kwa vidole. Akatazama chini akitengua jambo kichwani.

.

.

.

"Rhoda," akaita. "Ombi lako linawezekana. Ila gharama yake upo tayari kuilipa?"

.

.

.

Kabla Rhoda hajajibu, akamtazama kwanza Bonas. Kisha akaurudisha uso wake kwa Venin.

.

.

.

"Naomba uniambie gharama hiyo, nijitathmini."

"Mosi, tutahitaji siku tatu kukamilisha hilo zoezi. Pili, tutahitaji damu toka kwenye himaya yenu. Tatu na mwisho, ntashughulikia mwenyewe. Upo tayari?"

.

.

.

Shida ilikuwa hapo kwenye damu. Ataitoa wapi? .

.

Rhoda akamtazama Bonas. Bonas akamtazama mwanamke huyo wakiwa na nyuso za bumbuwazi. .

.

Rhoda alikuwa amejiandaa kwa kubebelea dinari lukuki za malipo. Ajabu Venin hakutaka dinari yoyote, anataka damu. Tena damu ya mtu toka Goshen.

.

.

.

"Ninaweza nikawapa muda wa kutafakari, wala msipate shaka," alisema Venin akisimama. .

.

.

Rhoda bado hakuwa na neno la kusema. Alimshuhudia Venin akipanda ngazi kuelekea juu. Akarudisha uso wake chini na kumtazama Bonas.

.

.

.

"Sasa tunafanyaje Bonas?"

"Inabidi tutafute damu."

"Najua! Tunaipatia wapi?"

"Sijui, mam. Hilo sina majibu nalo."

.

.

.

Rhoda akang'ata kidole chake. Mwanamke akachekecha kichwa chake kiundani.





Ilimbidi sasa ajivike roho ya chui, atoe maamuzi magumu. Maamuzi ya 'kiume'.

.

.

.

"Bonas, inabidi tummalize mlinzi mmoja."

"Unasema?" Bonas akastaajabu.

"Inabidi tumuue mlinzi mmoja tupate damu," Rhoda akaelezea. "Hamna namna nyingine zaidi ya hiyo!"

.

.

.

Kisha akasimama na kumpa maagizo Bonas.

.

.

.

"Niitie hapa walinzi wote kasoro mmoja tu."

.

.

.

Bonas akatenda agizo. Walinzi wakaja mbele ya Rhoda na kusimama kwa ukakamavu.

.

.

.

"Kammalizeni mwenzenu mliyemuacha nje. Mara moja!

.

.

. ---

.

.

.

Wakati huo chumbani mwa Venin.

.

.

Venin alikuwa amesimama mbele ya kioo kikubwa alichokuwa anakitazama kwa undani. Alikuwa tayari ameshabadili nguo akivalia nguo nyeusi ti. .

.

.

Nywele zake alikuwa ameziacha huru zikitambalia mabega. Macho yake mekundu alikuwa ameyatumbua, akihema kwanguvu.

.

.

.

Chumba kilikuwa giza, hakikuwa na dirisha hata moja. Ni mshumaa mmoja tu ndiyo ulikuwa umesimama kuangaza, tena ukiwa umesimama kwa mbali.

.

.

.

Kutokana na giza hilo, taswira ya Venin kwenye kioo ikawa ni ya kuogopesha zaidi. Hata kama mtoto aligoma kunywa uji, angeona hicho kioo angekomba bakuli zima.

.

.

.

Venin alipanua mdomo wake akahema kwanguvu kisha akaufumba. Akatulia kwa sekunde kama tatu kisha akasema maneno fulani yasiyoeleweka. .

.

.

Mara kioo kikaanza kutikisika. Mara kikakoma. Venin akarudia tena kusema maneno mengine yasiyoeleweka. Kioo kikaanza tena kutikisika. Haikudumu sana, kikakoma.





Mara hii Venin akapaza sauti kwanguvu kuyarudia maneno yake yasiyoeleweka. Mara kioo kikaanza tena kutetemeka. Mara hii hakikukoma mpaka pale kilipopiga nyufa.

.

.

.

Na mara akaonekana mtu kiooni. Alikuwa mweupe kama Venin. Alikuwa na nywele ndefu kama Venin. Alikuwa anatisha kama Venin.

.

. "Kaka!" Venin akaita. "Hatimaye utakuwa huru muda si mrefu!"

.

.

.

Venin akaangua kicheko kikali. Kisha akaendelea kusema:

"Kuna mtu atakuja huko Tanashe. Pasipo kufahamu atakutoa kifungoni. Nawe unywe damu zao kupata nguvu na kujirudufu upya."

.



Aliposema hayo, taswira ile ndani ya kioo ikatabasamu. Meno yalikuwa ya kahawia na yaliyochongoka. Badala ya tabasamu kumtengeneza uso, ikamharibu na kumfanya atishe zaidi. "Venin?" Taswira ikaita, na kuongezea: "Vita baina yangu nawe itakoma punde tu mpango huo utakapofanikiwa!"

"Pasi na shaka, kaka, mpango huu utatimia. Niamini mimi na kuwa na subra," akasema Venin kwa kujiamini.



Akaweka kiganja chake cha kushoto kwenye kioo akiitazama taswira machoni. Taswira nayo ikaweka kiganja chake vikagusana.

Mara taswira ile ikayoyoma kama vile sukari inavyozama kwenye uji. Kufumba na kufumbua haikuwepo.



Venin akabakia mwenyewe akiwa bado amepachika kiganja chake kiooni. Uso wake u na bumbuwazi, lakini pia huzuni.



Alikaa hapo kwa kama dakika tatu baada ya taswira kupotea, ndipo naye akatoka na kuendelea na shughuli zingine.

.

.

.

Akabadili nguo na kushuka chini alipomkuta Rhoda na Bonas wakiwa wamesimama wanateta jambo. Macho ya Venin yakamwona vizuri Rhoda na kushuhudia uzuri wake.

.

.

.

"Vipi, tayari?" Aliuliza.

"Ndio, Venin," Rhoda akajibu upesi. Swala hili likamshtua kidogo Venin.

"Mmetoa wapi haraka hivi?"

"Tumeona tuteke damu ya mlinzi wetu mmoja. Hatuwezi kurudi Goshen kwa huu muda na kurejea tena hapa," alijibu Rhoda. Venin akatabasamu. Haki alipendezwa na hilo jibu.

.

.

.

"Ama kweli wewe ni mwanamke jasiri," akasema akizidi kujongea.





"Nashukuru. Tunaweza sasa tukaendelea na mengine?"

"Bila tatizo lolote," akajibu Venin. "Lakini hamna haja ya kuwa na haraka, Rhoda."

.

.http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

.

Mwanaume huyo alizimaliza ngazi akasimama pembezoni mwa mwanamke huyo kiubavu, akimtazama kwa umakini. .

.

.

Akanyanyua kidole chake kionyeshi na kuteka unywele wa Rhoda kwa kucha. Akawa anauchezea kwa kuuviringita.

.

.



ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog