Search This Blog

UFALME WA NUGUTU - 4

 







    Simulizi : Ufalme Wa Nugutu

    Sehemu Ya Nne (4)





    "Watu husema mapenzi uunganisha pande mbili zisizofahamiana, mapenzi uleta furaha na amani, lakini mboni sioni amani wala furaha yeyote ile. Mapenzi ni mtego wa maumivu, yeyote aingiaye humo, lazima atoke na majeraha, dah! Nimekuaje mjinga hivi, nimekubalije kuwa dhaifu na kuingia kwenye mtego huo, ila hilo halitatokea tena" Mdidi alijiuliza na kujijibu mwenyewe, huku mama yake akimtazama kwa kumhurumia mno.

    “Mama Nkalo anaolewa wala sitamani kuendelea kukaa hapa"

    "Mwanangu itabidi uvumilie ili kulipa fadhila kwa chifu Mzovu ambaye wametusaidia sana," alisema Mdidi.

    "Mama nitalipaje fadhila hizo?"

    "Hakikisha ndoa ya Nkalo inafungwa bila kizuizi chochote"

    "Aah! Mama!"

    "Usiulize zaidi fanya kama nilivyokuamuru".

    Mdidi akakubali kile mama alichokisema ikabidi aende kwa chifu Mzovu kusaidia maandalizi ya mwisho kabla ya harusi. Chifu alifurahi sana alipomuona Mdidi,

    "Karibu kijana"

    "Uishi miaka mingi eeh mtawala wa Kigomile" Mdidi akainama na kutoa salamu zake.

    "Kijana wangu tunapanga muda ambao ndoa ya binti yangu itafungwa"

    "Mwanaume atakaye muoa Nkalo anatoka milki gani?"

    "Yeye ni chifu wa Tangeni, aliyerithi mamlaka ya baba yake Chifu Magambi"

    "Naweza kumuona huyo mtoto wa chifu Magambi"

    "Bila shaka unaweza, atakuja hapa ndani ya muda mfupi ujao"

    Kabla hajaongea zaidi tayari Magambi akiwa na baba yake na walinzi wengine wakawa wanakuja alipo Chifu Mzovu na Mdidi. Mdidi akamwangalia Magambi kwa umakini, akatuliza fikra zake kumtazama juu mpaka chini akafanya vile zaidi ya mara 3,

    "Huyu si mwanaume sahihi kwa Nkalo na wala si mtoto wa Chifu Magambi kama wanavyozani," Mdidi aliongea kwa sauti ya chini lakini Chifu Mzovu na wengine waliweza kuyasikia maneno yale bila shida.

    "Mdidi unasemaje!"

    "Lazima nimuone Nkalo kabla ya jua halijachomoza"

    Mdidi alikuwa kama yupo usingizini kwani aliongea kile alichokifikiri wala hakuweza kusikia wala kujua kuwa yupo sehemu gani

    "Wee Mdidi...!” CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Chifu Mzovu akaongeza sauti kumuita lakini Mdidi macho yakawa kwa wale wanaokuja

    "Hawa si watu wakawaida kama tunavyowaona, hili ni jeshi la giza!"

    Baadhi ya wazee walivyoona Mdidi amsikii chifu wakamsogelea na kumtishika apo Mdidi akawa kama aliyetoka usingizini

    "Una nini wewe?" wazee wakamuhoji baada ya kumsogeza pembeni ili kupisha maongezi yaendelee kati ya chifu Mzovu na Magambi.

    "Ndoa hii ni kiunganisho cha undugu kati ya watu wa Tangeni na wa Kigomile, hivyo tutaufanya umoja huu"

    Chifu Magambi akaongea nao wote wakaliunga mkono swala lile, ikawa ni furaha kubwa kwenye jumba lile la chifu Mzovu.

    "Ninamaanisha na ninachokiongea nimeona kitu cha tofauti kwa wageni hao, si watu wakawaida kwa hakika!"

    Wazee wale ambao ni washauri wa Chifu Mzovu wakacheka sana, kusikia kauli ya mdidi.

    "Kijana hivi unatuona sisi watoto wadogo tusiokuwa na uelewa wa mambo! Nani asiyejua kuwa wewe unampenda Nkalo na tunahisi upo hapa kwa ajili ya kuvuruga ndoa ya binti Chifu, sasa kabla hatujamwambia lolote Chifu Mzovu na akachukua maamuzi mabaya juu yako ni vyema ukaondoka mahali hapa" akasema mzee mmoja kwa ukali na msisitizo

    "Laah! Mzee wangu mimi nipo hapa kuhakikisha hakuna baya linalomkuta Nkalo, na uamuzi mnaoufanya hakika mnadidimiza uhai wake, naomba niongee na chifu"

    Chifu akaja Mdidi akaeleza kila kitu alichokiona na hata juu ya uvamizi wa jeshi la giza.

    "Mtukufu mtawala wa kigomile!! Kijana huyu anampenda binti yako na hayo yote anayoyaeleza ni uongo mtupu, anajaribu kuharibu furaha ya bintiyo na wananchi wote wa Kigomile" Mshauri wa kulia wa chifu akasema.

    "Kamuekeni kwenye chumba cha giza hadi harusi ya binti yangu itakapopita" Chifu akatoa agizo hilo.

    "Hapana chifu hii si haki mimi sina hatia."

    Nkalo akapata habari juu ya Mdidi kuwekwa chumba cha giza, ikabidi aende kwa haraka kumtazama,

    "Nani aliowaambia mmuweke chumba cha kiza? mtoeni sasa hivi tafadhali," alisema Nkalo.







    "Wewe! Usitake kunivuruga saa hii, nenda kajiandae na ndoa yako kesho"

    "Baba sijakataa kuolewa ila nataka Mdidi ashuhudie jinsi ninavyoolewa"

    "Mwanangu wewe hujui lolote Mdidi yupo hapa kuharibu ndoa hii isifungike"

    "Baba toka lini ukawa huna imani na bintiyo ni kweli nampenda Mdidi tena sana ila kwa alichokifanya lazima naye aonje maumivu kwa kushuhudia harusi yangu".

    Chifu akamuangalia bintiye kisha akaagiza askari wake wakamtoe Mdidi, wakamchukua hadi alipo chifu.

    "Akhsante sana chifu! Uishi miaka mingi!"

    Mdidi alishukuru mno alipofikishwa mbele ya Chifu na Nkalo, akainamisha kichwa kutoa heshima kwa chifu kisha akainamisha kichwa tena kwa Nkalo kutoa heshima zake.

    "Mdidi mimi ndiye niliyemshawishi baba hadi akutoe ila haina maana nitayabadilisha mawazo yangu, Magambi ni kijana mzuri, anayejali na mwenye upendo mwingi, naamini sitojuta kuwa nae"

    "Samahani sana chifu kwa usumbufu niliousababisha katika kipindi hiki, naona haya sana hata kukutazama hasa kwa wema uliotutendea mimi na mama yangu, nakili kuwa sina cha kulipia wema wako, ila mimi na mama yangu usiku huu tutaondoka katika milki yako," alisema Mdidi.

    Nkalo akashtuka mno kwa kauli ya Mdidi ata Chifu mwenyewe hakutegemea kama anaweza kufikia uamuzi ule.

    "Nkalo kila la kheri katika maisha yako, chifu pia yawezekana bado unahisi nina nia mbaya ila si uhamuzi sahihi kumuoza bintiyo kwa familia ya Chifu Magambi".

    Mdidi akainamisha kichwa na kutoa heshima tena kisha akaondoka. Nkalo alihisi kama amechomwa msumari wa moto kwenye kidonda kibichi akashindwa zuia machozi yake na chifu akiligundua ilo toka kwa bintiye

    "Baba mzuie asiende tafadhari!"

    "Nkalo...! Tunza heshima yangu na yule hawezi kumwaga chozi lako na akaishi, hawezi toka kigomile mzima”.



    *************************



    "Mama tunaondoka hapa usiku huu, ni vyema ukajiandaa na tafadhari mama usiniulize swali lolote sababu sina majibu ya hayo maswali"

    “Mdidi mwanangu, Kuna nini?"

    "Mama!"

    Kabla hajaendelea kuongea mlango ukagongwa kufungua kulikua na maaskari wa kutosha, mmoja kati yao akasogea mbele na kusema,

    "Agizo kutoka kwa chifu Mzovu kuwa hamna yeyote kati yenu atakayeruhusiwa kwenda popote hadi ndoa ya binti yake ipite"

    "Hatuna akiba ya chakula chochote humu ndani tutawezaje kuishi?"

    "Mtapata kila mtakachoitaji tafadhari naomba muwe na utii juu ya hili!"

    Baada ya kusema hayo askari wakafunga mlango, Mama Mdidi akabaki na maswali lukuki kwa mtoto wake,

    "Naomba uniambie kila kitu bila kificho".

    “Mama mapenzi huja yenyewe, hamna anayeweza kuyalazimisha kwa namna moja au nyingine, sasa kwanini nyoyo zilizoungana zihisi kupoteza tumaini juu ya penzi lile. Mama nimekuwa kama kipande cha karatasi nisiyeweza kujikinga hata kwa upepo wa mdomo, nimegeuka muhalifu pia adui tishio mbele ya macho yao"

    "Mhmh wee mwana unachokiongea unakielewa au unalopoka?"

    "Mama ndoa hii haiwezi kufungika sababu tayari jeshi la giza lipo hapa na bwana harusi ni mmoja kati ya maaskari wa jeshi hilo, nilijaribu kumuelezea chifu hata Nkalo mwenyewe juu ya hilo lakini hamna aliyenisikia na wote wakaniona nina nia mbaya kwao, mama siwezi kukaa nakuona mauaji ya kikatilii" CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Aah! Mwanangu muda gani umebaki hadi hayo kutimia?"

    "Saa 3 baada ya jua kuchomoza hayo yatatimia na hili kuwaumbua waovu harusi inatakiwa isogee tatu mara tatu yaani saa tisa baada ya jua kuchomoza"

    "Mhmh Mdidi fanya jambo mwanangu muokoe Nkalo na Chifu pamoja na watu wote wa Kigomile"

    "Mama sina namna ya kufanya humu ila nitajitahidi"

    Wakati maongezi hayo yakiendelea Balanoga alikuwa amejibanza sehemu na kusikiliza kila kilichoongelewa

    "Hutoweza kufanya lolote juu ya hili na hayo yote lazima yatimie"

    Akacheka kinafsi na kuchukua chai kupeleka alipo mama Mdidi na mwanae, kila mmoja akanywa na maongezi yakaendelea, haikupita muda mama Mdidi akahisi usingizi mzito na kwenda kulala. Balanoga akabaki na Mdidi pekee,

    "Vipi nikuongeze chai"

    "Nitashukuru Balanoga"

    "Usijali nipo kwa ajili yako".

    Akainuka na kwenda jikoni akamimina chai kisha akachukua kitu chenye ncha kali akatoboa kidole chake akanyunyiza damu kwenye chai kisha akaongea maneno yasiyoeleweka na kwenda kumkabizi chai ile Mdidi. Mdidi akaipokea na kuiweka mezani,

    "Aanh! Kuna kitu nimekisahau jikoni nakuja sasa hivi" Balanoga akasema na kuondoka, aliporudi akakuta Mdidi ameshamaliza ile chai.

    "Mhmh mara hii umemaliza?"

    "Ndiyo Balanoga na sijui kwanini chai ya sasa hivi nimeiona tamu kuliko ile ya kwanza"

    Balanoga aliposikia vile akacheka na kumkariibia Mdidi kisha akamshika kiganja

    "Balanoga kaa mbali na mimi tafadhali!"

    "Kwanini Mdidi?"

    "Siwezi kukifanya hiki mwili wangu unachohisi kukifanya nawe sasa"

    Balanoga akatabasamu zaidi sababu alishajua udhaifu wa Mdidi ivyo kwa njia ile alikuwa na uhakika wa kumzima Mdidi siku nzima hadi mambo yote yatakapokamilika. Balanoga akamsogelea zaidi Mdidi kisha akamwambia,

    “huna shida ya kumshikia manati ndege aliye tunduni, fanya lolote litakalo kutuliza na kukupa faraja ya moyo!"

    Mdidi hakuweza sema jambo lolote tayari Balanoga akawa amemkaribia akimkubatia na kumbusu kama ilivyokawaida kwa Mdidi safari hii alijikuta akipoteza nguvu kwa haraka mno, pia kichwa kikamuuna kuliko ilivyo kwa siku zilizopita. Balanoga alivyoona hayo akacheka kwa sauti kubwa mno iliyosikika hadi nje ya nyumba ambapo maaskari wamekaa kuhakikisha hamna anayetoka wala kuingia ndani ya nyumba hiyo,

    "Mhm jamani nimesikia kama mtu amecheka!!"

    “Aah! Usingizi huo jamaa angu mbona mimi sijasikia chochote"

    "Hata mimi sikusikia"

    Akadakia mwingine basi wote wakajikuta wanaangua cheko kwa pamoja wakimkebehi mwenzao kuwa huenda alikuwa akiota huku akiwa macho.

    Jua likachomoza, kila mtu alionesha kuifurahia siku ile, shamrashamra za hapa na pale zikapamba moto, saa mbili baadae Nkalo na Magambi wakawa tayari wameshafika katika sehemu iliyoandaliwa maalumu kwa ajili ya kuibariki ndoa ile. Chifu akawatuliza watu wake na kuwaambia

    "dakika kumi zijazo tutaanza maombi maalumu kwa ajili ya binti yangu na mumewe Magambi, hivyo baada ya maombi hayo nitakabidhi mamlaka yote kwa Magambi na kuanzia apo Tangeni na Kigomile itakuwa kitu kimoja na kuongozwa na mtu mmoja".

    Watu wote wakapiga makofi, nderemo na vifijo, Chifu Mzovu akakaa na watu wote wakaa kusubiri kengele kugongwa na maombi kuanza, hamna aliyeonekana na wasiwasi wowote ule kila mtu alijawa na furaha isiyo na kipimo, lakini kwa Nkalo akajikuta machozi yakimdondoka hamna aliyejua nini hasa kina mliza, baba yake akamsogelea na kumnong'oneza.

    "Unatakiwa kuwa na furaha sasa, muda si mrefu utakuwa mtawala wa Kigomile na Tangeni nasi sote tutatii amri yako".

    "Baba kweli umemzuia Mdidi asifike hapa?!"

    "Wewe mtoto acha balaa lako sasa hivi utaenda kukaa karibu na mumeo kwa ajili ya ndoa pia maombi maalumu ya kuwakabidhi utawala".

    Kengele ikagongwa na wote wakasimama, Nkalo akapiga hatua fupi fupi kuelekea alipo Magambi kadri alivyopiga hatua ndivyo hali ya hewa ikazidi kubadilika ilikua asubuhi yenye jua la kung'aa lakini wingu zito likatandana na kufanya kuwe na giza.

    "Chifu! wingu ni ishara mbaya kwa wanandoa hawa kama hutojali tusubili hadi jua litakapochukua nafasi yake," aliosema yule aliyepewa dhamana ya kufungisha ndoa hiyo.

    "Mimi sioni haja ya kusubili hadi jua litakapo shika nafasi yake huu ni muda muafaka kwa ndoa hii" chifu Magambi akasema.





    "Endelea na maombi” chifu Mzovu akaamuru harusi iendelee.

    "Lakini chifu kwa uzoefu wangu hapa hamna baraka ila ni laana".

    "Endelea tuu hatuwezi ahirisha".

    Kiongozi wa ibada ya ndoa akawa hana namna zaidi ya kufanya kama chifu Mzovu alivyoamuru, Giza likazidi kuwa nene upeo wa macho ya kila mmoja ukawa hafifu hatimaye kimbunga kikali kikatokea eneo hilo na kuanza kuharibu kila kitu,

    "Kiongozi simamisha maombi hatuwezi kuendelea tukiwa katika hali hii" Chifu Mzovu akamwambia mnajimu naye akaacha maombi.

    "Kuna nguvu ya ziada hapa inapingana na sisi embu angalieni ni nani huyo mpinzani wetu" Mzee mmoja akamnong'oneza Magambi.

    "Fanyeni kila muwezalo simamisheni kimbunga hiki na yaondoeni haya mawingu kazi lazima ikamilike kabla yaa saa 9 alasiri"

    "Sawa tutajitahidi".

    Kikundi cha wazee waliokuja na chifu Magambi wakajitenga pembeni na kuanza kufanya maombi yao huku wakichoma udi na ubani, Mpambano kati ya nguvu za pande mbili zisizoonekana ulikuwa mkali sana.

    Wananchi wa kigomile wakabaki wameduwaa wasijue nini kinaendelea maana dakika 2 jua dakika 2 giza

    "Hamna mwenye uwezo wa kufanya haya isipokuwa Mdidi lakini Mdidi hajiwezi yupo ndani amelala sasa ni nani mwingine awezaye fanya haya"

    Balanoga alikuwa mmoja katika kikosi cha giza kilichoagizwa toka Nugutu na kazi yake alishaikamilisha vilivyo, lakini anakutwa na mshangao baada ya kukuta kuna nguvu kubwa inayowazuia wao wasifanye walitakalo.

    "Jamani hapa tutaumbuka muda unazidi kwenda achieni jeshi letu lifanye kazi yake"

    "Sawa hakikisha hamna kitu kitakacho baki hai"

    Wale wazee wakachukua pembe ya ndovu na kuipuliza papo hapo ardhi ya Kigomile ikatetema na baadhi ya watu wakageuka na kuwa midudu ya ajabu tena yenye kutisha, Kigomile nzima ikajawa na tahayaruki, hasa pale walipoona wale walokuja kuoa nao wamekuwa midudu ya kutisha vile,

    "Mungu wangu nini hii!!, Mdidi alikuwa sahihi bora tungemsikiliza" Chifu Mzovu akaongea na kumchukua Bintiye na kuanza kukimbia bila kujua wapi wanaelekea.

    Sauti za vilio vya uchungu na maumivu vilivuma katika kigomile damu zilitapakaa kila kona lile jeshi la giza likauwa kila kitu bila huruma yeyote. Watu wote wakakusanywa kama mateka na tayari kwa kuuwawa.

    "Je kuna yeyote aliyesalia popote!" Mkuu wa jeshi la giza akauliza

    "Ndiyo wapo"

    Balanoga msichana mwenye urembo na sura ya kuvutia kwa kumtazama lakini aliye na ukatili mkubwa nafsini mwake. CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Jeshi kawaleteni hao wakiwa wazima"

    Jeshi likaanza safari kuelekea kule ambapo Balanoga ameelekeza. Safari ya kwenda walipoelekezwa ikaanza huku kile kikosi cha maombi ya kuleta jua kikiendelea kushindana na nguvu ile inayozuia jua kuwaka. Ngurumo ya radi ikapiga ardhi ikatetema taratibu nyufa zikaanza kuonekana katika ardhi ya kigomile, Kadri jeshi lilivyozidi kulisogelea eneo waliloelekezwa na Balanoga ndivyo nyufa zilivyozidi kuwa kubwa.

    "Si-ma-me-ni....." ilikuwa ni sauti kali iliyojaa mitetemo ikiwazuia maaskari wa jeshi lile la giza kuendelea mbele lakini haikufaa kitu kwani walishazungukwa na nyufa nyingi.

    "Tumieni nguvu zenu za ziada kujiokoa tumezidiwa"

    Mkuu wa msafara ule aliwaambia maaskari wake lakini radi likawa kali sana, mvua kubwa ikanyesha na kuifanya ardhi ya Kigomile kuwa tepe ivyo kuifanya ianze kutitia, ndani ya muda mfupi jeshi lote la giza liloshuhudiwa likimezwa na ardhi.

    Tukio lile liwaogopesha sana Chifu Magambi na kamati yake, Balanoga akaelewa kuwa ni Mdidi pekee awezaye kufanya hayo. Kimbunga kikali kikatokea na kuanza kuangusha miti iliyozunguka eneo lote la Kigomile ajabu miti ile ilikuwa kama inarushwa na kuwalenga maadui, Mpambano ukawa mkali japo haikuwa rahisi kwa watu wa Kigomile kujua ni nani hasa mtetezi wao.

    "Waelekezeni watu wote kwenye pango la Ng'enge"

     Ilikuwa kauli ya chifu Mzovu kwa maaskari wake ambao ni wazi hawakuwa na la kusaidia katika vita ile, Nkalo akisaidiana na maaskari wakafanikiwa kuwatoa mateka wote na kuwapeleka pangoni kwa usalama zaidi.

    "Eeh! Mungu ni nini hiki kinatukuta watu wako?"

    Yalikuwa maswali ya kina mama waliowakumbatia watoto zao huku wakijawa na hofu juu ya hatima yao.

    "Nguvu niliyonayo hamna wa kuishinda, aliyeuwa kwa upanga atauwawa kwa upanga na ninyi mnaofanya uovu kwa giza mtaukumiwa kwa giza", Ilikuwa sauti ya mzee mmoja aliyeshika fimbo na jambia ambalo linafanana na lile alilokabidhiwa Mdidi.

    "Mhm huyu ni nani? Na kwa nini atoe msaada kwa watu wa kigomile" Balanoga alijiuliza.

    "Inawezekana Mdidi akawa bado ndani ya nyumba au ni yeye mdidi amejibadili?"

    Maswali yake yalikosa majibu akaamua atoke na kwenda kwenye nyumba alipomuacha mdidi na mama yake. Akafungua mlango kwa haraka alipotupa jicho kitandani hakuamini alichokiona.

    Mdidi alikua bado amelala huku akiwa hana alitambualo juu ya kinachoendelea,

    "Mhm! Kumbe naweza endelea kumpumbaza Mdidi asijue uovu wangu" Balanoga akaongea huku akitabasamu.

    "Yule mzee ni nani!?" alijiuliza bila kupata jibu.

    *****************

    Kigomile ilikombolewa na kuwa salama salmini, Kazi ya kuijenga upya ikaanza huku Balanoga akiendelea kuishi miongoni mwa jamii ile na hamna aliyemgundua kutokana na uwezo wake wa kujibadili maumbo mbali mbali ya binadamu, Mdidi na mama yake wakawa wanashangaa juu ya yale yaliyotokea pasi na wao kuelewa. Chifu Mzovu akatoa agizo Mdidi aitwe mara moja, taarifa ikamfikia Mdidi nae taratibu akajongea katika jumba la chifu Mzovu,

    "Wewe ni nani hasa, hata kuona mambo yajayo kabla?" Mdidi akashindwa ajibu vipi swali la chifu,

    "Kama tungali kusikiliza mapema, maafa haya yasingaliikumba Kigomile, una kitu cha ziada na cha tofauti"

    "Chifu mimi sina nikielewacho na sina majibu ya swali lako" Mdidi alihofia kufichua ukweli kuhusu yeye alipenda kuonekana wakawaida.

    "sawa waweza kwenda"

    Mdidi akainamisha kichwa na kuondoka kwa chifu, wakati anatoka akakutana uso kwa uso na Nkalo, wakatazamana kwa muda bila kusemeshana lolote, kila mmoja akawa hajui ni vipi atamuanza kumuongelesha mwenzie, Nkalo alijua ni wazi kuwa Mdidi ameoa, alipokumbuka hilo akampita bila kunena jambo na kuendelea na safari yake, Mdidi aliumia mno ila akawa hana namna ya kufanya.

    Mama mdidi akamkabidhi mwanae ramani yenye kuelekeza hazina ya Nugutu ilipo, akaamini huko kutamsaidia yeye kufahamu vitu vingi vilivyojificha.

    "Mwanangu wakati wa kuangusha ufalme wa Msongo umewadia lakini kabla ya hayo lazima uende kwenye hazina ya Nugutu huko utapata nguvu kamili ya kukabiliana na utawala mbovu na wakikatili wa Msongo"

    "Sawa mama nitafanya kama ulivyonambia"

    “Kama nguvu zilizopo kwenye hazina atazipata mtu tofauti na wewe basi jua Nugutu na Falme zote za jirani zitakuwa matatani, usiku wa leo kabla ya jua halijachomoza unatakiwa uwe nje ya kigomile"

    "Sawa mama!".

    Mdidi akamuangalia Balanoga ambaye muda wote alikuwa kimya akiwasikiliza mama na mwana wakiongea,

    "Naomba umtunze mama yangu"

    "Shaka ondoa" Balanoga akajibu.

    Mdidi kuondoka bila kumuaga kipenzi chake Nkalo ilikuwa ngumu, ikabidi jioni iyo aende kwa chifu Mzovu ili kuonana na Nkalo.

    "Mdidi sina la kuongea na wewe!"

    "Mhm! Nkalo vile unavyofikiria wewe ni tofauti na uhalisia wa mambo"

    "Mimi sio mpumbavu Mdidi, kusikia nisisikie, lakini hata picha nisielewe"

    "Unamaana gani!?"

    "Mdidi nifanyie hisani, ulijaribu kuniokoa sawa nashukuru, tafadhari nenda maana kadiri unavyoniongelesha ndivyo nnavyozidi kuhisi hasira, nakuchukia sana".

    "Kwani Nkalo kosa langu lipi?"

    "Sina muda wa kupoteza kwako nina shughuli nyingi na itakuwa vyema kama hauto nitafuta tena," alisema Nkalo kisha akaondoka.

    "Nkalo! Nkalo....." Mdidi akaita na Nkalo akageuka kumtazama.

    "Baada ya hapa nakuahidi kuwa hutoniona tena," alisema Mdidi lakini  Nkalo akasonya na kuondoka.





    Giza likaingia na Mdidi akawa tayari kuelekea katika milima ya Madora ambapo huko ndipo ilipo hazina ya Nugutu, Safari ikaanza huku akiwa amebeba jambia, kitabu na ramani aliyopewa na mama yake.



    *********************



    "Tumepata habari kuwa kuna mtu tayari yupo njiani kuelekea kwenye hazina na yeye pekee ndiye mwenye ramani ya huko. Hazina ipo katika milima ya Madora mzuieni kabla hajafika huko"

    ilikua kauli ya mfalme Msongo kwa jeshi lake, wote wakatii na kuanza safari ya kuelekea huko Videte, Mdidi alitembea sana na jua likawa karibu kuchomoza akatafuta mahari akapumzika huku akiisoma ile ramani vizuri ili asipotee, ghafla akahisi ardhi ikitetema akatega sikio ardhini kusikiliza ni nini akagundua kuwa kuna jeshi kubwa lenye farasi likiwa katika mwendo wa kasi linakuja eneo alipo yeye, akatafuta mahala pazuri na akajificha.



    Baada ya muda mfupi jeshi la Nugutu likapita kuelekea njia ambaye yeye alipanga kuitumia na kama ramani inavyoonesha ili aweze kufika katika milima ya Videte. Akatoa ramani yake tena na kutazama uelekeo wa jeshi lile, kengele ya hatari ikagonga kichwani mwake akahisi kuna mtu aliyetoa taarifa juu ya safari yake ya hazina, akamfikiria mama yake lakini ni wazi mama yake hawezi kufanya vile, akamfikiria Balanoga kidogo akapata wasiwasi, hasa kutokana na vitu visivyo vya kawaida ambavyo Balanoga alikua anavifanya lakini akikumbuka upendo wa dhati ulioneshwa na Balanoga toka ile siku anatoroka katika mikono mwa maaskari wa Nugutu akajipa moyo kuwa awezi fanya jambo lolote. Baada ya kufikiri kwa kina, akainuka na kuendelea na safari, akabadili njia na kupita poli kwa poli kuepuka jeshi lile la Nugutu.

    CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alitembea kwa muda mrefu sana hatimaye akatokea kwenye kijiji ambacho hakufahamu kinaitwaje alipotazama ramani yake akafurahi kwani baada ya kijiji hiko ndipo milima ya Madora inafata lakini kila akijaribu kuangalia hakuona dalili yeyote ya milima karibu na hapo, akairudia tena ramani lakini ilimuonesha vile vile kuwa karibu na kijiji hiko ndipo ilipo milima ya Madora, kwa kuwa hakuwa na mahala pa kufikia akatafuta sehemu iliyotulia na kukaa peke yake.

    Masaa, siku ikapita bila kuelewa wapi pa kuelekea kwa bahati kuna wawindaji wakawa wanakimbiza ng'ombe pori ambaye alikua akielekea sehemu alipo Mdidi, ikabidi Mdidi ainuke na kuokota kipande cha mti ambacho alikirusha na kumpiga yule mnyama mguuni na kuanguka papo hapo, wawindaji walifurahi kupata kitoweo kile.

    "Asante sana kijana ni muda mrefu tumewinda bila mafanikio bila shaka wake zetu na watoto zetu watafurahi leo" Mdidi akatabasamu tuu bila kuongea jambo,

    "Wewe ni mgeni hapa"

    "Ndiyo"

    "Aah! bila shaka hauna mwenyeji ila usijali kuanzia sasa sisi ni kama nduguzo twende nyumbani."



    *******************



    Walipofika kijijini kwao walipokewa kwa furaha na kila muwindaji kurejea katika kaya yake. Mdidi alipewa hifadhi katika familia ya muindaji aliyekuwa maarufu sana kwa jina la Ngoo. Baada ya utambulisho mfupi akaoneshwa sehemu ya kupumzika, Mdidi akabeba kifurushi chake na kuingia ndani, akatoa ramani yake na kuitazama kwa makini zaidi, akagundua kuwa milima ya Madora inapatikana katika kijiji hiko, ikabidi atoke nje na kuangaza huku na huko lakini asione dalili yeyote ya uwepo wa milima karibu na hapo. Akazunguka nyuma ya nyumba na kumkuta mwenyeji wake akichonga mishale,

    “Naona unawajibika!”

    “Hivyo hivyo ndugu yangu hizi ndio zana zenyewe bila hivi tutakufa na njaa”,

    “Ngoja nikusaidie”

    “Mhm! Utaziweza kazi hizi wewe?” Ngoo akauliza.

    “Aah! Mimi nimezaliwa porini maisha yangu yote ni kuwinda na kilimo” Mdidi akajibu na wote wakajikuta wanacheka kwa pamoja.

    “sasa ndugu yangu leo usiku, hapa kijijini kuna ngoma inaitwa Chagulaga’

    “Mhmh! Chagulaga ndo ngoma gani? Sijawahi isikia Mimi!”

    “Hahaha! Mdidi hiyo ngoma inahusu wasichana na waliofikia umri wa kuolewa, hivyo mmoja mmoja ucheza na wanaume uchagua Yule atakayewavutia na taratibu za ndoa zinatangazwa”

    “Khaa! Kwa hiyo huku hamna ile mvulana kumfata msichana na kumuelezea hisia zake?”

    “Hiyo huku hamna, utajionea mwenyewe usiku wa leo”.

    Sekunde, dakika, saa zikapita hatimaye kiza kikaingia na wanakijiji wote wakakusanyika tayari kwa kushuhudia ngoma ya chagulaga, wavulana siku hiyo walipendeza sana na wasichana urembo wao ukaongezeka maradufu. Viongozi wa kijiji hiko wakaa sehemu ya mbele kabisa huku wasichana wakikaa kushoto na wavulana wakikaa kulia, Mdidi na mwenyeji wake wakakaa sehemu ambayo waliweza kuona kila kilichoendelea kwa uzuri zaidi, baada ya muda mfupi, mtu mmoja toka katika sehemu ile waliyokaa viongozi wa kijiji iko akasimama na kusema,

    “Ndugu zangu wanakijiji leo tuna jumla ya wasichana 13 waliofikia umri wa kuolewa na vijana wetu wakiume wapo 7, hivyo juhudi zao katika kucheza ndizo zitawafanya waweze kuteka nyoyo za hao wavulana”.

    Baada ya kusema hayo ngoma ikapigwa na kila msichana kutoka mbele na kuonesha ufundi wake katika kucheza ngoma iyo. Wavulana wakajikuta wanashindwa kuchagua maana kila mmoja alikuwa na kionjo chake katika kucheza.

    Baada ya wote kucheza wasichana wakaitwa mbele na kutakiwa kucheza kwa pamoja kisha wavulana watainuka na kuchagua. Ngoma ikapigwa na wakaanza kucheza safari hii sura za wasichana zilionekana vizuri hama kwa hakika wote wana uzuri usio na kifani, Moyo wa mdidi ukashtuka baada ya kuona kunamsichana ambaye anafanana kwa kila kitu na Nkalo, Ngoo akamtazama Mdidi na kugundua kitu kisicho cha kawaida kwa Mdidi.

    Akafatilia macho ya Mdidi na moja kwa moja yakatua kwa msichana ambaye kiukweli katika uzuri na umbo yeye ni zaidi ya neno uzuri, Ngoo akacheka na kumgusa Mdidi begani

    “Nkalo..!” Mdidi akasema,

    “Mhm! Nkalo ndio nani?”

    “Ni Yule msichana pale”

    “Mhm! Nahisi umechoka sasa twende ukapumzike” Ngoo akamwambia Mdidi.

    Mdidi akakubaliana na Ngoo sababu si rahisi kwa watu kufanana kiasi kile, akahisi yawezekana akili yake imechoka.



    *****************



    Asubuhi na mapema wawindaji wakakusanyika tayari kuingia msituni kuwinda, Mdidi akawa mmoja wao, japo wazo lake lilikuwa kupeleleza zaidi sehemu ambayo milima ya Madora inapatikana, hivyo aliamini kuandamana na wawindaji kungeweza kumsaidia yeye kupata taarifa za muhimu.

    Safari ya msituni ikaanza huku soga na utani wa hapa na pale ukiendelea, wakatembea sana hatimaye wakafika sehemu ya njia panda, wakasimama kwa mda na kuiangalia ardhi, mmoja wa wawindaji akatega sikio lake ardhini kisha akaangalia sana upande wa mashariki, akawaambia wenzie

    “Inaonekana upande huu wa mashariki unawanyama wengi na wakubwa hivyo tukienda huko tutanufaika”.

    “Hapana tusiende huko twende upande huu wa kaskazini” wawindaji wote wakatazama na kumwangalia Mdidi.

    “Sikiza ndugu, wewe ni mgeni na hujui mazingira ya huku, ukweli kwamba hamna binadamu anayeweza kwenda upande huu wa kaskazini na kurudi akiwa hai”

    “Mnamaanisha nini?” Mdidi akaulizaa.

    “Mhm! Kuna siri kubwa upande wa kaskazini na kwa umri wako huwezi kuhimili”.





    Mdidi akajawa na shauku kuu, akahisi uwenda ikawa iyo ndiyo njia ya kumfikisha videte.

    “Jamani eenh! Muda unazidi kwenda na hatujaambulia kitu, tutafute kitoweo kwanza hayo tutaongea wakati mwingine, ila tusiende kaskazini wala mashariki, twende magharibi”.

    Wawindaji wakakubaliana na safari ikaanza mara moja, lakini kabla hawajafika mbali wakasikia sauti ya bundi, wote wakasimama na kuangalia pande zote kwa makini zaidi, Bundi akalia tena.

    “Jamani! Leo inaonekana si siku njema kwetu turejee nyumbani tujaribu tena kesho” Ngoo akaongea.

    “Hapana hatuwezi kurudi mikono mitupu lazima tutafute walau digidigi turudi nao”.

    Wakati wakiongea hayo wakaanza sikia kishindo kikubwa kikija walipo, kwa haraka ikabidi waingie kichakana na kujificha. Kishindo kikaongezeka na wote hawakuamini kile walichoshuhudia mbele yao, hofu kuu ikawatanda hawakujua wafanye nini,

    “Wameenda wapi? Mboni tuliwaona hapa!”.

    “Acheni uzembe pekua kila kichaka hakikisha hawatoroki!”

    Zilikuwa kauli za wanajeshi la Mfalme msongo waliopewa agizo la kuzuia mtu yeyote asiingie katika milima ya Madora, japo hawakuona ilipo milima ila wakaimarisha ulinzi kuzingira njia zote zilizo karibu. CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mdidi akiwa na wawindaji wengine wakajawa na hofu Zaidi, hawakuelewa uhalifu gani hasa walioufanya hata kusakwa vile, kadri muda ulivyozidi kusonga ndivyo baadhi ya wanajeshi wakazidi kukaribia kichaka walichojificha.

    “Mungu wangu! Tumekwisha hapa hamna namna yeyote ya kujiokoa!” akasema Ngoo.

    Mdidi akawahurumia wawindaji wale ambao karibu wote walikua tegemeo kubwa kwa familia zao na kijiji kwa ujumla.

    “Nafikilia kufanya jambo, nyie tulieni hapa hapa”

    “Wewe Mdidi tulia ni hatari kwa maisha yako”

    “Hapana hatuwezi kukaa hapa eti tusubiri kukamatwa na kuuwawa lazima tutafute namna kabla ya wao hawajatufikia”.



    Mdidi akatambaa kama nyoka kwenye zile nyasi alipofika umbali kidogo akaporomosha mawe ambayo yakawa yanaenda kwa kasi bondeni, kisha akajificha sehemu, wale wanajeshi walivyosikia vishindo vile wakafikiri ni watu wote wakaanza kukimbia kuelekea kule waliposikia vishindo. Mdidi akawazunguka na kurejea walipo wenzake kisha akawaambia wakimbie, bila kupoteza muda wakaanza kutimua mbio, walikimbia umbali mrefu na kwa haraka mno, kila mmoja akahisi kuchoka ikabidi wajipumzishe, kando ya mto Nongeni.

    “Hivi kwanini hawa wanajeshi wapo huku?”

    “Mhmh mimi sifahamu kwa kweli maana haijawahi tokea”.

    “Jamani hivi itakuaje kama lile jeshi litafika kijijini?”

    Ngoo akauliza na wote wakajikuta uchovu ukiwaisha kila mmoja akaiwaa familia yake ivyo kwa haraka zaidi wakarejea nyumbani.



    Wakati wanakaribia kufika kijijini kabisa wakasikia sauti ya msichana ikipiga yowe la kuomba msaada. Wote wakadhani kuwa jeshi limefika kijijini ikabidi wafatilie sauti inapotokea kufika, wakakuta msichana amevingwa vingwa na chatu. Kila mmoja akapigwa na butwaa wala wasijue waanzie wapi kumsaidia Yule msichana, Mdidi akaiona hatari iliyopo kwa msichana Yule.

    “Jikaze kidogo asikuangushe chini nakuja sasa hivi”

    “Hapana siwezi tena, nguvu zimeniishia” Msichana alitoa sauti yake ambayo ni wazi alionesha kuelemewa na lile joka.



    Mdidi akachukua upanga kisha akasogea hadi alipo msichana akamvizia chatu na kumjeruhi mkiani, Yule chatu ndo kama alichokozwa akaanza kufoka kwa hasira, Mdidi akasogea na Yule chatu akajifungua toka kwa Yule msichana na kumrukia Mdidi. Ngoo na wenzie wakaja wakamtoa msichana na kumpa huduma ya kwanza kwa haraka, Mdidi akaanza kubilingishana na lile joka hatimaye akafanikiwa kulizibiti na kulikata kichwa. Kila mmoja akamuona kama mkombozi, sifa kede kede zikamwagikia.

    “Mhmh wee jamaa uko vizuri, kwa mambo uliotuonesha leo kuanzia kule na lile jeshi hadi hapa na hili joka daah hatarii” akasema mwindaji mmoja.

    Wote wakafika kijijini na Mdidi akafikia kuoga kutokana na kasheshe alopitia, kisha akaa chini ya mti na mwenyeji wake, baada ya muda mfupi akaja mama wa makamo hadi alipo Mdidi kisha akaanza kulia huku akitoa shukrani za dhati.

    “Ahsante kwa kuyaokoa maisha ya binti yangu, sina cha kukulipa ila mungu mwenyewe atakulipa pale ulipopungukiwa”.

    “Hapana mama usijali, sisi ni binadamu lazima kusaidiana uwe na amani tuu moyoni mwako”

    “Namuonea fahari mwanamke aliyekuzaa wewe, Batuli ni mtu pekee niliyebaki naye, kwa kuyaokoa maisha yake nahisi furaha mno”

    “Usijali mama nitakuja kumjulia hali yake baadae’.

    Jioni ikafika Mdidi na Ngoo tayari wakawa wamefika kwenye kaya ya mama Batuli,

    “Karibuni jamani!”



    Mama Akawakaribisha nao wakakaa baada ya muda mfupi Batuli akatoka Mdidi alipomuona akashikwa na mshangao mkubwa, Batuli ni msichana aliyemuona usiku uliopita akiwa amefanana karibu kila kitu na Nkalo, akamtazama kwa sekunde kadhaa hadi Ngoo akashtukia mchezo akamfinya na kumnong’oneza

    “Vipi jamaa mbona macho kodo kwa binti wa watu”

    “Mhmh hamna kitu asee!”.

    “Mdidi asante sana kwa kuyaokoa maisha yangu”

    Sauti ile ilipenya moja kwa moja kwa mtima wa Mdidi, bado akazidi kushangaa yawezekanaje watu kufanana mbali na sura, umbo hadi sauti pia. Mdidi akabaki kimya wala asijue kile alichoongeleshwa, Moyo ukaenda mbio, Ngoo akamstua tena jamaa ake naye akajikuta akisema

    “Nkalo..!” Mdidi akajikuta akitamka hilo jina.

    Mama Batuli aliposikia lile jina naye akashtuka na kuuliza,

    “Mdidi! Unamfahamu Nkalo?”

    “Ndiyo mama namfahamu, macho yangu yalipotua kwa Batuli nikafikiri ni Nkalo” Mama akaanza kulia.

    “Asante Mungu kumbe binti yangu bado anaishi’

    “Binti yako!” Mdidi akauliza kwa mshangao mkubwa.

    “Miaka 20 iliyopita nilijifungua watoto mapacha ambao ni Nkalo na Batuli, lakini katika kipindi kile nilikataliwa  na kuamriwa kuuwawa mimi na watoto zangu, sababu wengi waliamini kuzaa watoto mapacha ni mkosi, hivyo kabla sijauwawa nikamwacha binti yangu mkubwa kwa baba yake name nikatoroka na huyu”.CHANZO : http://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Basi mama usilie, yawezekana mungu anakusudi lake mimi kukutana nanyi”

    “Niambie unamfahamu vipi Nkalo?”

    Mdidi ikabidi aelezee kila kitu kilichotokea kati yake na Nkalo, pia hata kuhusu ile ndoa na mambo yalivyobadirika, Mama alihuzunika sana,

    “Lakini bado wampenda binti yangu?” mama akauliza.

    “Ndiyo, nampenda tena sana tuu”

    “Usijali atakuwa wako”

    Mdidi akahisi kama yupo nyumbani sababu tayari alishafamiana na watu wengine, akamuomba Ngoo amuache kwa usiku huo akae pamoja na ile familia, Ngoo akakubali na kurejea kayani mwake na kumwacha Mdidi akiwa na Batuli pamoja na mama yake.



    *****************



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog