Search This Blog

NILIVYOTESEKA KWENYE MIANZI YA KICHAWI - 4

 





    Simulizi : Nilivyoteseka Kwenye Mianzi Ya Kichawi

    Sehemu Ya Nne (4)



    Baadaye nikawaambia nimemchinja rafiki yangu Chambilecho na sasa namrejeshea uhai wake. Nilifanya vitu vyangu na mara akawa mzima.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/-

    Nilimuambia arukeruke ili kuthibitishia umma ule kwamba yu mzima, akafanya hivyo na kuzidi kushangaza watu.

    Niliomba yaletwe maji kwenye mitungi, nikafanya mazingaombwe na maji yale yakawa divai tamu, niliwaambia watu wainywe, wakainywa na kuzidi kushangaa huku wengine wakisema hakika huyu ni nabii.

    Kama vile hiyo haitoshi, nilimchukua ndege na kumuweka kwenye kopo na wote wakashuhudia nikilipondaponda lile kopo lakini nilipofunua kikapu kilichozibwa juu ili ndege asiruke alikutwa mle akiwa hai. Watu walipigwa na butwaaa na kusema mimi ni nabii kweli na kwamba nikitupwa kwenye shimo la kifo, nchi itatikisika.

    Mfalme alisimama akautazama umati uliokuwa ukinishangaa huku wengine wakisema sikuwa mtu wa kawaida.

    “Sikilizeni,” yule mfalme akaanza kuhutubia.

    “Katika maisha yangu sijaona mambo ya ajabu kama haya.”



    Tuliamriwa  kusimama na kuanza safari na kuelekea kwenye shimo ambalo limeandaliwa kwa shughuli hiyo.

    Yule msichana aliyekuwa mjamzito alikuwa akilia kwa sauti huku akipunga mikono ishara ya kutuaga.

     Kilio chake kilifanya hata sisi wanaume tuanze kulia, mimi huwa mgumu sana kulia lakini yowe za yule dada zilinifanya nitokwe na machozi.



    Dereva Limbende na utingo wake ambao nao walisalimika kutupwa kwenye shimo la kifo, niliwaona wakibubujikwa na machozi kutulilia.

    Vijana wenzangu tuliokuwa tumepangwa kwenye mstari wote walishindwa kusema chochote kwa kujua kwamba sasa tunakwenda kufa.

    Wasichana tuliohukumiwa nao ambao walikuwa watano wote walikuwa wakilia. Mmoja aliishiwa nguvu kabisa za kutembea tukaamriwa tumbeba.

    Kazi hiyo niliifanya mimi nikisaidiwa na kijana Kwiimukaga.

    Hata hivyo, kazi ya kumbeba msichana ambaye alizimia wakati tunakwenda kutupwa shimoni ilikuwa ngumu ilibidi kupokezana kwa sababu msichana huyo alikuwa pandikizi la mtu.

    Lakini pia kazi hiyo ilikuwa ngumu kwa kuwa tuliishiwa nguvu hasa kwa kuwa usiku uliopita hatukuweza kula chakula kutokana na hofu ya kifo ambacho sasa tunakwenda kukabiliana nacho.

    Wakati wa msafara huo, kulikuwa na kikundi cha wapiga ngoma waliokuwa wamezifunga viunoni mwao.

    Mwendo kutoka pale kwenye kiwanja cha mikutano hadi kwenye shimo ilichukua saa nzima ni mbali kutoka makazi ya watu na ni kwenye msitu mnene.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Tulipofika pale ajabu ya kwanza tuliyoiona ni kwamba shimo lile ni pango kubwa ambalo sijajua lilitokana na nini lakini lilikuwa na mfuniko mkubwa wa jiwe.

    Kwa wale wasoma maandishi ya vitabu vya dini, niwakumbushe kuwa jiwe lile linafanana na lile ambalo lilitumika kufunikia kaburi la Yesu.

    Tofauti na zama hizo ambapo jiwe hilo kubwa lilivingirishwa na askari, lile la pale lilitolewa na winji maalum ya kunyanyulia vitu vizito.

    Ajabu ya pili ni kwamba kulikuwa na kiti maalum cha chuma ambacho kilikuwa na minyororo ambacho kilikuwa pale, kando kidogo na ile winji.

    Nilijiuliza, kiti kile cha chuma, tunauawa kwanza kwa umeme baada ya kukikalia kisha tunatupwa shimoni?

    Hilo lilikuwa swali langu kichwani na sikuwa na uwezo wa kupata jibu wakati ule.

    Ajabu ya tatu ni kwamba karibu na kile kiti kulikuwa na askari wanne ‘walioshiba’ ambao nilikuwa sijajua walikuwa pale kwa kazi gani.

    Baadaye aliitwa kijana wa kwanza aanze kutekeleza adhabu yetu, alichukuliwa na askari walioshiba na kukalishwa kwenye kile kitu cha chuma.

     Baadaye alinyanyuliwa huku akimwaga machozi na kuwekwa kwenye mlango wa lile pango.

    Alishushwa taratibu kwa ile winji. Ilielekea kuwa shimo lile ni refu sana kwa sababu minyororo iliyokuwa imeshikilia kiti ilikuwa mirefu na iliisha yote.

    Baadaye nilishuhudia ile minyororo minne ikirudi ardhini na kipande kimoja kimoja cha kile kiti cha chuma kilichoshuka chini na kijana wetu.

    Zoezi hilo liliendelea mpaka wote wakaisha nami nikawa mtu wa mwisho kushushwa chini ya shimo.

    “Wewe Issa Namakoto tumekufanya kuwa wa mwisho kushushwa kwenye hili shimo la kifo ili utoe neno lako la mwisho kwetu,” alisema Kamanda Ben Mtwanga aliyeoongoza zoezi hilo la kututumbukiza shimoni.

    Nilifikiria haraka japokuwa akili ilikuwa siyo yangu lakini niliamua kuwatisha tu.

    “Mimi naitwa Namakoto au ukienda kijijini kwetu huwa naitwa Maharage ya Zambia. Nawaahidi kwamba sisi hatutakufa na tutakuja kutokea tena katika nchi hii. Mtashangaa lakini hiyo ndiyo ahadi yangu.”

    Baada ya kusema hayo niliona watu waliokuwa pale wakishangazwa na kile nilichokisema.

    “Anasemaje? Watakuja tena? Wangapi wametumbukizwa kwenye shimo hilo na hawajawahi kurudi duniani?” nilisikia mtu mmoja akiuliza.

    Hapohapo nikajua kuwa kumbe lile shimo limewahi kutumika kufunika watu wengine tofauti na tulivyokuwa tukidhani kwamba tungefukiwa kwenye shimo kwa mchanga.

    Mimi tofauti na wenzangu ambao walikuwa wakiishiwa nguvu na kubebwa kuketishwa kwenye kile kiti cha chuma, nilikwenda na kukaa mwenyewe.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kwa kawaida kila anayetupwa ndani ya chimo hili hupewa chakula cha siku saba na maji ili atumie muda huo kumuomba Mola wake kabla ya kifo, hivyo, baada ya wewe kutiwa shimoni kuna chakula na maji tutawaletea, muwe tayari kuvipokea,” alisema Kamanda Mtwanga.

    Sikuwa na la kusema zaidi ya kumuitikia “Sawa.” Winji iliwashwa na nikaanza kuteremshwa shimoni na kwa kuwa nilikuwa mtu wa mwisho, ngoma ambazo zilitulia wakati wa zoezi zima, zikaanza kupigwa tena.

    Nilifika chini ya shimo na kukuta wenzangu wakiwa wamejikunyata huku wengi wakilia na baadhi yao wakiwa wamezimia.

    Kwa kuwa jiwe lilikuwa halijafunikwa, tuliweza kuonana vizuri kwa sababu mwanga ulikuwa ukiingia.

     Niliweza kuona kando ya pale tulipokuwa tumeketi kuna mifupa ya watu, hiyo iliashiria kuwa watu waliotupwa ndani ya shimo hilo walifariki dunia na kwamba siyo utani.

    Baada ya dakika kadhaa niliona kile kiti kikishuka, kilikuwa na maboksi kumi ya maji. Nilishusha, yakaletwa tena mara saba baadaye ililetwa mikate mingi, sikuwa na sababu ya kujua ilikuwa mingapi kwa sababu nilijua walaji watakosekana.

    Wasichana ambao walikuwa wakilia tukiwa mle shimoni waliruka ghafla:“ Nini?” nilihoji.

    “Kuna panya,” alijibu msichana mmoja.

    Akili yangu ilifanya kazi haraka na kujiuliza, ‘huyu panya anaishije kwenye shimo hilo refu? Je, inawezekana hutoka nje kupitia lile tundu lililotumika kutushushia sisi humu?”

    Jibu sikupata kwa sababu panya mwenyewe hakuwepo aliingia shimoni lakini hata kama angekuwepo nisingeweza kumuuliza kwa kuwa ni panya.

    Nilisimama na kwenda kuangalia lile tundu aliloingia panya, akili zikanituma kwamba utafiti wangu uanzie pale.



    Nilisimama kwenye lile tundu kwa dakika tano hivi, wenzangu wakawa wananiangalia wasijue nilikuwa nawaza nini.

    “Mbona kaka Namakoto unaangalia tundu la panya kisha huseni lolote?” alinihoji Kwiimuka.

    “Nadhani wote au baadhi yenu mmemuona panya hapa.”

    “Ndiyoo,” waliitikia baadhi ya vijana niliotupwa nao kwenye shimo lile la kifo.

    “Nani ana wazo kuhusu panya huyu?”

    Kimyaa. Ukimya wao ulinifanya nigundue kuwa hakuna mtu mwenye mawazo, walimuona kama walivyokuwa wanamuona tukiwa nje ya pango lile.

    “Hamuoni kuwa panya huyu anaweza kutuokoa?”

    “Kivipi?” aliuliza tena Kwiimuka.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Huyu panya kwa mawazo yangu naamini anatoka nje ya shimo hili na inawezekana huwa anakwenda kujitafutia chakula nje ya pango hili.”

    Baada ya kusema hayo kuna baadhi ya wenzangu walikasirika, bila shaka waliona wazo langu ni la kipuuzi na nawapotezea muda.

    Lakini nilijiuliza kupoteza muda ili wafanye nini kwa sababu sikuona hata mmoja ambaye alikuwa na wazo lolote la kuweza kujiokoa.

    “Sasa kaka Namakoto unafikiri panya huyu kachimba shimo hadi bustani ya Nangose?”

    Kabla sijajibu mwingine akadakia:

    “Sasa hata kama huyu panya kachimba shimo kutoka bustani ya Nangose, sisi tunaweza kupita katika tundu lake?”

    Huyu wa swali la pili nilimuona kama alitaka kuelekea kule nilipokuwa nawaza, lakini akashindwa kufikiri zaidi.

    “Niwaambieni jambo?” nilianza kuongea nao, nikanyamaza kidogo ili kumeza mate.

    “Huyu panya inawezekana ni Mungu ameamua kutuonesha ili kutuokoa, mnasemaje?”

    “Atatuokoaje?” aliuliza msichana mmoja.

    “Sikiliza. Ni lazima tutumie mifupa ya watu waliotangulia waliotupwa humu ili kujinasua. Wazo langu ni kwamba tuchimbue kufuata njia hii ya panya. Tuchimbe taratibu na kwa bidii naamini tutatoka nje ya pango hili. Kuna mwenye swali?”

    Wote nikawaona wanakunjuka sura zao na kuonesha nyuso za matumaini.

    “Ni wazo zuri na hiyo kazi tuianze sasa hivi,” alichombeza kijana mmoja aliyekwenda moja kwa moja kuchukua mfupa wa maiti na kuja pale kwenye shimo la panya.

    Kazi ya kuchimbua haikuwa ngumu sana kwa sababu udongo ulikuwa tifutifu na hali hiyo ilitushangaza.

    “Hapa inavyoelekea shimo hili lilikuwa likitumika zamani kwa kazi fulani na hii ilikuwa njia ya watu kufika shimoni,” nilisema.

    “Lakini sasa kwa nini walifukia?” mwingine alihoji.

    “Huwezi kujua labda walikuwa na sababu maalum, labda za kivita enzi hizo. Inawezekana walikuwa wakijificha watu hapa wakiona maadui enzi hizo za ujima,” akadakia kijana mwingine.

    “Msifurahie jamani, huwezi kujua, panya anaweza kupita katikati ya miamba iliyoungana, hivyo, tutafurahi kama tutatoboa juu ya ardhi,” nilisema na baada ya kutamka hivyo nyuso za watu niliona zimekunjamana.

    “Sisemi hivyo ili kuwakatisha tamaa, la hasha. Nataka tuzidi kumuomba Mungu ili tusikutane na mwamba ambao utatuzuia kuendelea na kuchimba njia,” niliona niwape moyo.

    Kazi ilikuwa ngumu kwa sababu ilikuwa ni kufa na kupona. Kwamba tukifanikiwa kutoboa ardhi itakuwa ndiyo kupona kwetu na tusipofanikiwa itakuwa ndiyo kifo chetu.

    Kubwa kuliko yote ni kwamba nilitaka tufanye kazi kwa bidii kabla ya chakula tulichopewa hakijaisha.

    Siyo chakula tu, bali hata maji tulipewa kidogo ili tufe haraka na kwa kazi nzito tuliyokuwa tukifanya huku tukivuja jasho, ilikuwa ni hatari sana kama tungeishiwa maji.

    Ni kwamba kuishiwa maji maana yake tungeshindwa kazi ya kuchimba mtaro wa kutuwezesha kutoka ndani ya lile shimo la kifo.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Tatizo lingine ambalo tulikumbana nalo ndani ya shimo lile ni vitendea kazi. Ile mifupa ambayo tulikuwa tukiitumia kuchimbulia ardhi ilikuwa ikilika.

    Hilo lilinitia hofu sana na nilipoichunguza baadhi ya mifupa niligundua kuwa ni ya watu wa zamani sana hivyo haikuwa na uwezo wa kuhimili ardhi ambayo licha ya baadhi ya sehemu kuwa tifutifu, kuna sehemu zilikuwa ngumu.

    Changamoto nyingine ni baadhi ya vijana kuchubuka viganja, yaani kuota mafindofindo kutokana na kutozoea kazi ngumu kama ile tuliyokuwa tukiifanya kwa vifaa duni, mifupa ya watu.

    Lakini changamoto nyingine ni vifaa vya kusombea mchanga kwani tulikuwa tumeshachimba umbali wa hatua ishirini za mtu mzima.

    Hatukuwa na makarai au ndoo badala yake tukawa tunatumia mafuvu ya watu ambayo kwa kweli yalitusaidia.

    Wakati naanza kuwahimiza kutumia mavufu hayo baadhi ya wasichana walikwa waoga.

    “Mnaogopa nini? Haya mafuvu hayadhuru, tumieni kusombea mchanga,” niliwaambia.

    “Lakini mimi naogopa sana,” alisema msichana mmoja. Ni wazi kwamba wasichana karibu wote tuliokuwa nao ndani ya shimo lile la kifo ilikuwa mara yao ya kwanza kuona mifupa ya watu waliokufa.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog