Simulizi : Sherehe Kuzimu
Sehemu Ya Tano (5)
Nelson alipotoka gerezani jambo la kwanza alimtafuta mke wake ili aweze kufahamu habari za nyumbani kwake. Alifurahi sana alipojulishwa kwamba mwane Benedict yupo nyumbani anaendelea vizuri. Kiukweli alifurahi sana na kumshukuru Mungu. Baada ya hapo siku iliyofuata asubuhi na mapema alifunga safari kutokea stendi ya mabasi ubungo, kuelekea mkoani Mbeya kuonana na Isaka. Alisafiri salama na kufika stendi ya mabasi ya mbeya usiku. Kwa vile walikuwa wakiwasiliana kwa njia ya simu, Isaka alifika mapema ili kuweza kumlaki. Nelson aliposhuka garini alikutana na Isaka kisha wakakumbatiana kwa furaha sana. Baada ya salamu walikwenda moja kwa moja hadi nyumbani kwa Isaka.
Walipofika nyumbani, Nelson alikuta wageni wengi, ambao alitambulishwa kuwa wanatokea Uingereza kwenye taasisi moja binafsi lijulikanalo kwa jina la ‘Spiritual health.’ Katika maelezo aliyopewa Nelson ni kwamba taasisi hiyo inajishughulisha na kutoa misaada ya ujenzi wa makanisa katika nchi zinazoendelea. Pia wanatoa misaada ya kuwasomesha watoto ikiwa ni sambamba na kuwajenga kiroho katika shule zao za seminari zilizopo ulaya.
Watoto wawili wa Isaka ambao ni John na Peter wapo nje ya nchi wanasomeshwa na taasisi hiyo.
Walizungumza mengi sana usiku huo. Nelson alipata wasaa wa kutoa ushuhuda wake ambao uliwagusa kwa kiasi kikubwa wageni wale. Mkurugenzi wa taasisi hiyo Mr Lee alidondokwa na machozi tangu Nelson alipoanza kusimulia ushuhuda wake hadi mwisho. Tamati ya simulizi ya Nelson ilipelekea watu wote waliokuwa wakimsikiliza kupanguza machozi yaliyokuwa yakiwatoka mfululizo. Kwa kuwa muda ulikuwa umesonga sana, walikwenda kulala.
Ugeni mkubwa uliokuwa umekusanyika nyumbani kwa Isaka, ni kwasababu kesho yake ilikuwa ni siku ya uzinduzi wa kanisa ambalo limejengwa na ile taasisi. Kanisa hilo litakuwa chini ya mchungaji Isaka. Palipokucha mchungaji Harris Phillips, ambaye alikuwa mgeni rasmi kutoka Uingereza aliongoza shughuli nzima ya uzinduzi wa kanisa.CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com
Ilikuwa ni siku ya furaha sana. Waumini wa kanisa la Isaka walijawa na furaha kubwa kwavile walipata mahala pema pa kufanyia ibada. Mwanzoni walikuwa wakiabudu katika jengo ambalo halikuwa hata na paa. Lakini sasa wamepata jengo jipya na la kisasa kabisa. Baada ya uzinduzi walikula na kunywa vilivyokuwa vimeandaliwa palepale kanisani.
Siku moja baadaye Mr Lee na wenzake walifunga safari ya kurudi nchini Uingereza kuendelea na majukumu mengine. Mkurugenzi huyo alimwahidi Nelson kuwa atamtafuta siku chache za mbeleni kusudi waweze kufahamiana zaidi. Ilikuwa ni furaha kubwa kwake kuweza kukutana na kufahamiana na raia wale wa nchini Uingereza.
Nelson alimshukuru Mungu kwa kumkutanisha na rafiki mwema maishani mwake, Isaka. Alifurahi zaidi na zaidi kushiriki katika uzinduzi wa jengo hilo la kanisa. Baada ya hapo na yeye alisafiri kuelekea nyumbani kwake mkoani Mwanza. Aliwasili salama nyumbani kwake na kupokelewa na mke wake na mwanae Benedict. Alifurahi sana alipomtazama mwanae na kumwona ni mzima na mwenye furaha.
Aliamini kupona kwake ni kwasababu ya uweza wa Mungu pekee na sio madaktari wala wauguzi. Alipiga magoti chini kisha akamshukuru Mungu wa mbinguni kwa kumponya mwanae, ambaye hali yake ilikuwa ni mbaya sana.
Vivian alishangaa kumuona mume wake anapiga maombi yasiyokuwa na mfano pale nyumbani. Licha ya kushangaa lakini pia alishikwa na hasira baada ya kusikia mume wake akitamka jina ambalo lilikuwa linamfanya apoteze nguvu na kuhisi kuungua.
Alipoona moto unazidi kumuwakia aliamua kuondoka mahali pale wakati Nelson alipokuwa anazidi kuchapa maombi kwa kwenda mbele. Robo saa ilipopita Nelson alifumbua macho yake baada ya kumaliza sala, na kukuta mke wake hayupo.
Nelson hakujali sana mke wake kutoweka wakati walipokuwa wakisali. Alijipa moyo labda pengine kwasababu utaratibu ulikuwa mpya na pia hakuwa amemweleza chochote kuhusu mabadiliko makubwa maishani mwake.
Usiku muda wa chakula Nelson aliamua kutumia nafasi ile kuzungumza na mke wake pamoja na mwanae.
“Jamani, nimechukua uamuzi wa kumpokea Mungu ndani ya maisha yangu kwa maana neno lake kupitia zaburi 25: 2 inasema hivi; ‘Ee Mungu wangu, nimekutumaini wewe nisiabike, Adui zangu wasifurahi kwa kunishinda.’ Maana yake ni kwamba adui wetu hapa duniani ni shetani ambaye katu hatuwezi kumshinda bila kuwa na Mungu ndani yetu.” Sauti ya Nelson ilisikika.
Mkewe na mwanae walikuwa kimya wakimtazama kwa makini bila kuzungumza chochote. Nelson aliendelea kuzungumza nao kwa upendo ingawa Vivian hakufurahishwa kabisa na mazungumzo ya mume wake. Uso wake ulionyesha hasira za waziwazi.
Kwasababu Mungu alikuwa hajamfunulia Nelson roho wa ibilisi aliyekuwa ndani ya nafsi ya mke wake, ndiyo maana hakuweza kuelewa sababu ya mke wake kununa pindi asikiapo habari za Mungu.
Tangu siku ile alipompokea Yesu maishani mwake alipokuwa ndani ya gereza, kuzimu walilijua hilo. Kitendo kile kililaaniwa vikali na ulimwengu wa kuzimu kwasababu ilikuwa ni njia ya kumkosa katika ulimwengu wao. Kwa kuwa walikuwa na malengo marefu naye, walijaribu kumuuwa mapema kabla hajakomaa kiimani lakini ilishindikana.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com
Nelson alikwenda kutembelea makaburi ya binamu zake, Frank na Christopha. Japokuwa lilikuwa ni pengo kubwa kwake lakini moyoni alijihisi kutopungukiwa na kitu kwavile alikuwa amempata mfariji wa kweli maishani.
Ile kampuni aliyokuwa anafanya kazi, waliamua kumsimamisha kazi kwa kuwa, muda mwingi anautumia katika mambo yake badala ya kufanya kazi. Kampuni ilipata hasara kubwa kutokana na kutokuwepo kwake kazini kwa muda mrefu. Kwavile alikuwa ameshapewa barua ya onyo kwa zaidi ya mara tatu, ulifuata uamuzi wa kumsimamisha kazi.
Ingawa ni kawaida habari za kufukuzwa kazi huwa zinakuwa ni mbaya kwa watu wengi, lakini kwa Nelson hali ilikuwa tofauti sana, kwasababu alipopewa barua ya kusimamishwa kazi alionekana kuwa na furaha na mwenye kumshukuru Mungu kila wakati. Baadhi ya marafiki zake walimuona kama vile hana akili nzuri tena, kwavile habari ya kufukuzwa kazi haikumsumbua akili hata kidogo. Mbaya zaidi ni kwamba, barua ya Nelson kufukuzwa kazi ilimtaka pia kukabidhi vitu vyote vya ofisi ikiwa ni pamoja na nyumba aliyokuwa anaishi. Alipewa wiki moja awe ameshakabidhi nyumba kwa mkurugenzi mkuu wa kampuni hiyo kwavile kuna mfanyakazi mwingine alipaswa kuhamia kwenye nyumba hiyo haraka iwezekanavyo.
Wakati hayo yote yanatokea Nelson alikuwa na shilingi elfu 20 kwenye akaunti yake. Fedha hizo zilikuwa ni kidogo sana, kwavile hazikuwa na uwezo wa kumuhamisha wala kumpatia nyumba nyingine kwa haraka. Ni wazi kabisa kwamba familia hiyo ilikuwa ikipitia katika wakati mgumu, lakini Nelson alizidi kulia na Mungu wake ili afungulie milango mingine ya baraka.
Lile duka la nguo lililokuwa linaendeshwa na Vivian kwa njia ya kichawi, liliwaka moto siku moja baada ya Nelson kupokea barua ya kufukuzwa kazi. Nelson aliendelea kumshukuru Mungu akiamini kwamba yeye ndiye mwenye kuruhusu hayo yote yatokee.
Kwa upande wa Vivian hali ilikuwa tofauti sana, baada ya duka la nguo kuteketea. Alihisi kuchanganyikiwa kwasababu ule mpango wa kuwapeleka watu kuzimu, usingefanikiwa tena kwa kiasi kikubwa. Jambo lile lilikuwa linakwenda kupunguza uhusiano mzuri aliokuwa nao na kule kuzimu. Malikia mkuu wa kuzimu alimpenda sana kwasababu yeye ndiye aliyekuwa anaongoza kwa kuwapeleka watu huko. Kwahiyo kutokuwepo tena kwa duka lile kungepunguza sana idadi ya watu wanaopelekwa katika ulimwengu huo wa ibilisi shetani.
Wiki moja ilikatika, Nelson akiwa bado hajapata pa kwenda ili aweze kukabidhi nyumba ya kampuni. Kilichofuata baada ya kuonekana kukahidi amri hiyo ya kuondoka ni kwamba, uongozi wa kampuni hiyo walitoa vitu vyake vyote, nje ya geti kwa nguvu. Bila kupoteza muda, siku hiyohiyo akaingia mfanyakazi mwingine katika nyumba hiyo, ambaye ndiye aliyekaimu nafasi yake kazini.
Baada ya Nelson kutolewa vitu vyake nje ya geti, uso wake ulitawaliwa na huzuni kubwa. Wapita njia pamoja na majirani walikusanyika kwa wingi katika eneo lile huku kila moja akizungumza lake, alilojisikia.
“Acha wafukuzwe, huwa wanaringa sana.” Nelson alisikitika sana baada ya kusikia maneno hayo yakitamkwa na mama mmoja jirani yake.
Kimya kimya Nelson alitamka maneno haya “Kama kweli wewe Mungu ndiye umeamua niabike, basi mapenzi yako yatimizwe, lakini kama ni hila la shetani, jitokeze Mwamba wangu unitetee.”
Kwa kadiri giza lilivyokuwa likipambana na nuru, umati wa watu waliokuwa wakimshangaa Nelson na familia yake, ulizidi kupungua. Giza lilipoishinda nuru, Nelson alibaki na familia yake pale nje wakipigwa na baridi huku mbu nao, wakiwashambulia sawasawa. Nelson alitumia hekima kumwendea jirani yake mmoja ambaye, walikuwa wanaivana sana, kisha akamuombea hifadhi mke wake na mwanae hadi siku inayofuata. Yeye alirudi kukesha kulinda vitu vyake ambavyo vilikuwa pembezoni mwa barabara.
Ng’ai ng’ai hadi pana kucha hakufumba macho yake, alikesha akiimba na kusali ndani ya gari lake ambalo nalo lilikuwa nje ya geti. Usiku kucha alihisi kuna nguvu fulani inamwambia aviuze vile vitu vyote alivyokuwa navyo, kisha fedha atakazozipata awasaidie wasiojiweza. Alipata mkanganyiko kidogo kutokana na nguvu ile iliyokuwa inamsukuma kufanya hivyo. Alijiuliza inawezekana vipi afanye hivyo ili hali hana pa kwenda? Alizidi kusali na kumuomba Mungu amwonyeshe mlango wa jaribu lile lakini alizidi kusikia sauti ya nguvu ile iliyokuwa inamsukuma kuuza vitu na kisha kusaidia masikini. Kwavile nguvu ile alikuwa anaisikia katikati ya maombi, moja kwa moja alijua ni nguvu ya roho mtakatifu iliyokuwa inamwongoza kufanya hivyo.
Kweli bila kupoteza muda palipokucha, ulifanyika mnada mkubwa wa kuuza vitu vyote palepale pembezoni mwa barabara. Kufikia saa tano asubuhi vitu vyote vilikuwa vimeshanunuliwa. Sio gari, sio kikombe cha kunywea chai, vyote vilipata wateja ambao walilipa fedha taslimu.
Benedict na mama yake walihisi huenda baba huyo amerukwa na akili, kutokana na mambo aliyokuwa anayafanya.
“Eti mama, kweli ni sahihi baba kuuza hivi vitu vyote na kisha fedha zikasaidie masikini? Kwani sisi tuna tofauti gani na masikini wakati tumefukuzwa kwenye nyumba tuliyokuwa tunaishi?” Benedict alimtwanga mama yake maswali yaliyokuwa yanamtatiza.
“Sidhani kama akili ya baba yako iko sawasawa.”CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com
“Kwani kakueleza baada ya mnada tunakwenda kuishi wapi?” Benedict alizidi kuuliza maswali.
“Ukitaka kujua kuwa amechanganyikiwa ni kwamba, hata yeye hatambui pa kwenda baada ya haya yote.”
“Ama kweli leo ni leo asemaye kesho ni mwongo.” Benedict na mama yake walikuwa njia panda.
Mnada ulipoisha Nelson alifanikiwa kupata jumla ya shilingi milioni 20. Bila kuchomoa hata senti tano, alizipeleka zote hadi kwenye kituo cha watoto yatima kilichokuwa jirani na pale kwake. Baada ya kuzikabidhi fedha zile alibakiwa na nguo alizovaa pamoja na simu yake ya mkononi. Hakuwa na kitu kingine chochote.
Mke wake ndiye alibakiwa na begi moja kubwa, ambalo ndani yake kulikuwa na nguo na vitu vyake vidogo vidogo pamoja na kibuyu cha kichawi.
Watoto yatima waliokuwa wakilelewa na kituo kile cha ‘Baraka village’ walifurahia msaada mkubwa walioupata siku ile kutoka kwa familia ya Nelson.
Lisaa limoja baada ya Nelson kumaliza kutoa msaada katika kituo cha watoto yatima, alipokea barua pepe kwenye simu yake kutoka kwa Mr Lee, mkurugenzi wa wa taasisi ya ‘Spitual health’ ya nchini Uingereza.
“Hellow! I would like to inform you that, our institution have decided to work with you immediately, to cover the chance of our engeneer who is suffering from stroke. We are willing to pay, all the cost of transfer to London, as well as to buy you, a new house. Also we are ready to assist your son in education up to university. We are waiting for your answer within 24 hours. Thank you. From Chief executive officer, Mr Lee.” (Habari yako, ninapenda kukujulisha kuwa, taasisi yetu imependekeza kufanya kazi na wewe kwa haraka sana kuziba pengo la mhandisi wetu mkuu ambae ameshikwa na kiharusi. Tupo tayari kugharamia gharama zote za kuihamishia familia yako huku London, sambamba na kuwanunulia nyumba mpya. Pia tupo tayari kumsomesha mwanao bure hadi chuo kikuu. Tunasubiri jibu lako ndani ya masaa 24. Ahsante. Imetoka kwa mkurugenzi mkuu. Mr Lee.)
Nelson hakuamini macho yake, alirudia kusoma ujumbe ule mara mbili mbili. Moyo wake ulilipuka kwa furaha isiyokuwa na kifani. Muda huohuo alijibu ule ujumbe kwamba yupo tayari kufanya kazi na taasisi ile. Alimsimulia mke wake ule muujiza ambao Mungu alimtendea, lakini simulizi hilo kwa Vivian ilipita sikio moja na kutokea lingine kwavile hakutaka kabisa kusikia habari za Mungu.
Baada ya muda mfupi Nelson alitumiwa barua pepe nyingine kutoka kwa Mr Lee iliyokuwa inamshukuru kwa kukubali kufanya kazi nao. Siku hiyo hiyo Nelson aliingiziwa fedha taslimu milioni 40 kwenye akaunti yake ya benki kwaajili ya maandalizi ya safari ya kuhamia Uingereza. Huo ni muujiza mkubwa ambao ulimtokea Nelson maishani mwake.
Nelson alichukua hifadhi ya muda mfupi katika hoteli ya M- tower jijini mwanza. Siku iliyofuata utaratibu wa kutafuta passport za kusafiria ulianza mara moja.
Kuzimu hali ilizidi kuwa mbaya, kila mara maombi ya Nelson ilikuwa ikiharibu vikao vyao. Walikosa kabisa muda mzuri wa kufanya vikao vyao, kwasababu ule muda waliokuwa wakiutumia, saa sita kamili hadi saa tisa usiku ndio muda ambao Nelson alikuwa akichapa maombi ya nguvu. Ulikuwa ni wakati mgumu sana kule kuzimu, kwasababu hakuna chochote kilichokuwa kikifanyika kikafanikiwa. Hakuna kafara za damu zilizokuwa zikitolewa tena kwasababu majini na maajenti hawakuwa na nguvu ya kwenda duniani kuchukuwa watu.
Nelson aliendelea kupambana nao katika ulimwengu wa roho. Siku ya nne wakati Vivian yupo hotelini kibuyu kilihitaji damu kama kawaida. Hakuna kipindi ambacho kilikuwa kigumu kwake kama hiki, kutokana na kwamba kila aliyejaribu kumtoa kafara ilishindikana. Alizidi kuwa matatizoni kwasababu kibuyu kile kinaposhindwa kupata damu kwa muda muwafaka basi kitapambana na nafsi yake.
Mama yake Vivian alionekana kupaniki vilevile kwasababu kulikuwa na kila dalili ya damu yake na ya mwanae kumwagika. Kwa jinsi ilivyo ni kwamba, endapo Vivian atashindwa kabisa kumtoa mtu kafara katika msimu ule, basi mama yake ndiye atatumika katika kafara hiyo na mwisho wa siku yeye ndiyo atakuwa wa mwisho.
Ilifanyika kila namna kusudi damu ya kibuyu iweze kupatikana lakini kila njia ilionekana kubuma. Vivian na mama yake walikonda kwa mawazo. Vivian alikuwa akikutana na mama yake katika mikutano yao kwa njia za kichawi, kwavile mama alikuwa Arusha na Vivian alikuwa mwanza.
Siku chache baadaye mama yake Vivian alionekana kurukwa na akili, kwasababu alianza kuongea peke yake kwa kutoa siri za watu ambao aliwai kuwauwa. Majirani walisikitika sana, baada ya kusikia kwamba, mama huyo ndiye aliyeuwa watoto wake pamoja na mume wake. Haikuishia hapo walishikwa na butwaa zaidi baada ya kufahamu kuwa mama huyo ndiye aliyeuwa wajukuu zake pamoja watu wengine pale kijijini.
Baada ya kumaliza kutoa siri zake, jamii nzima ilifahamu maovu yaliyofanywa na mama huyo. Siku chache baadae alipoteza maisha kutokana na kufanyika kafara ya kibuyu cha mwanae. Mazishi yalifanyika huko nyumbani kwake Sakina, Arusha.
Ilibidi Nelson aahirishe safari ili aweze kumzika kwanza mama mkwe. Kwahivyo walifunga safari kutoka Mwanza kwenda Arusha kwenye msiba.
Vivian alikosa raha na alipoteza kabisa matumaini ya kuishi kwavile alijua kuwa, yeye ndiye atakayefuata kufa.
Zilipopita siku tatu baada ya Marwa kuzikwa, Adela aligundua kuwa amefanya kosa kubwa sana maishani mwake. Roho ilimuuma sana kwasababu usichana wake ulitolewa na mvulana ambaye hakuwa chaguo lake. Muda mwingi alikuwa ni wa kulia na kujilaumu sana kwa kufanya kitendo cha kumsaliti mwanaume wa ndoto zake. Hakujua nguvu iliyomsukuma hadi akajikuta anatumia shuka moja na marehemu, Marwa.
Alilia na kuteseka sana binti wa watu lakini ukweli ni kwamba kupenda kwake kulisababishwa na nguvu za giza. Ingawa hakujua kuwa Benedict ni mzima au ameshakufa lakini alijipa moyo ipo siku atakutana naye. Nafsi yake haikumtuma kabisa kuamini kwamba mvulana huyo ni marehemu. Alijipa matumaini kila kukichwa kwamba ipo siku ataonana na mwanaume huyo hatimaye watafunga pingu za maisha.
Suala la kujinga na shule kwa mwaka huo ilishindikana kwavile walitumia muda mwingi katika matibabu. Kwahiyo alijipanga mwakani ndiyo aendelee na masomo yake. Aliapa mwili wake kutoguswa na mwanaume mwingine tofauti na yule ambaye amechaguliwa na moyo wake. Kila alipolala kila alipoamka akili yake ilikuwa ikimuwaza mpenzi wake wa moyo. Ombi lake kuu kwa Mungu ni kukutana na laazizi wake.
Siku moja alipokuwa katika mawazo mazito ya kumuwaza mpenzi wake, alikumbuka kuwa, kumuomba Mungu pasipo kuwa na bidii ya kutafuta kile unachohitaji ni kazi bure. Aligundua kwamba, Mungu humbariki zaidi yule mwenye bidii ya utafutaji kuliko yule anayepiga magoti kila kukicha pasipo kujishughulisha. Kumbukumbu zilimjia siku moja walipokuwa wakisafiri kuelekea katika mashindano ya somo la mathematics shule ya jirani.
Siku hiyo, ndiyo siku ambayo aliweza kufahamu nyumbani kwa kina Benedict, japokuwa alionyeshwa wakati walipokuwa safarini. Nafsi ilimsukuma kufunga safari ya kuelekea Mwanza kwenda kumsaka mpenzi wake. Mapenzi yana nguvu sana jamani, kwani siku hiyohiyo baada ya kupata wazo hilo, alianza safari kutokea kijijini kwao kuelekea Mwanza. CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com
Jua lilikuwa limeshatua tayari, wakati alipokuwa anaanza safari. Alipanga siku hiyo atakapowasili, afanye kila liwezekanalo aonane na mwanaume huyo, kusudi siku inayofuata asubuhi na mapema arudi shinyanga kwavile ilikuwa ni siku ya ubatizo wa mtoto wa dada yake.
Kwa bahati mbaya gari alilopanda liliharibika zaidi ya mara tatu wakati alipokuwa safarini. Lakini kwa kuwa Mungu ni mwema alifika salama, ingawa ilikuwa usiku sana. Kuharibika kwa gari mara nyingi pamoja na kuchelewa kuanza safari ndiyo ilipelekea kuwasili jijini mwanza majira ya saa tano usiku.
Tayari ilikuwa ni usiku sana. Kwahiyo ilimuwia vigumu kupata usafiri wa daladala ya kuweza kumfikisha mtaa aliokuwa anaishi huyo mpenzi wake. Ilimlazimu kuchukua usafiri wa bodaboda ambayo ndio usafiri pekee uliokuwepo kwa wakati ule. Alijaribu kuvuta kumbukumbu vizuri ya mazingira yale kusudi asiweze kupotea usiku ule. Zilipokatika dakika kumi na tano alimwambia dereva asimame. Tayari alikuwa ameshawasili katika mtaa husika.
Alifanikiwa kuiona nyumba yenyewe japokuwa macho yake yalikataa kuamini kilichokuwa kinaonekana. Watu wengi walionekana kuzingira nyumba ile ambayo ilikuwa inamalizikia kuteketea kwa moto. Alihisi kuchanganyikiwa kutokana na tukio lile la kutisha lililokuwa linatokea kwa wakati ule. Moyo wake ulikataa kukubaliana na kile ambacho macho yake yalikuwa yanashuhudia. Alijisogeza zaidi na zaidi ili aweze kushuhudia vizuri. Jeshi la zima moto pamoja na majirani walikuwa wanaendeleza juhudi za kupambana kuuzima moto ule.
Hata hivyo hakuna kilichokuwa kinaonekana kusalia ndani ya nyumba ile, kwani moto ulikuwa umeshachoma kila kitu. Moyo ulikuwa ikimwenda mbio sana. Shauku yake kubwa ilikuwa ni kutaka kujua kuwa, wenye nyumba wamesalimika ama wamefia ndani ya nyumba. Alimsogelea mmoja wa majirani ambaye alionekana kuwa na masikitiko makubwa sana. Dhumuni lake kubwa ni kutaka kufahamu kama moto ule umegharimu uhai wa mtu yeyote.
Adela aliihisi uchungu ambao hakuwahi kuhisi tangu alipotoka tumboni kwa mama yake. Alisikitika na kulia sana, aliposikia kwamba wenye nyumba wote wamefia ndani ya nyumba. Juhudi za kuwaokoa zilifanyika lakini ilishindikana kutokana na ukubwa wa moto. Ilikuwa ni kipindi kigumu sana kwake. Alijua kuwa mpenzi wake atakuwa ameteketea ndani ya moto ule. Hakuona sababu ya kuendelea kuishi bila kuwa na Benedict maishani.
Alichukua uwamuzi wa kukimbilia ndani ya nyumba ili na yeye aweze kuteketea na mpenzi wake. Malengo yake hayakufanikiwa kwasababu alikamatwa na askari wa zima moto. Adela alizidi kulia kwa uchungu hadi mashuhuda wa tukio lile wakamuonea huruma. Baada ya kulia kwa muda mrefu alipoteza fahamu hadi saa mbili asubuhi alipojikuta yupo hospitali.
Mshumaa uliokuwa unaangaza nuru maishani mwake tayari ulikuwa umeshazimika. Aliyachukia maisha kiujumla. Alihisi moyo wake umepata jeraha ambalo hakujua litapona mwaka gani. Hakuona sababu ya kuendelea kukaa jijini Mwanza, ili hali kilichokuwa kimempeleka kilikuwa kimefikia tamati japo kwa maumivu makubwa.
Aliondoka hospitalini pale na kuelekea katika kituo cha mabasi, kusudi aweze kurudi kijijini kwao. Alipanda daladala ya kumtoa pale hospitali kumfikisha kituo cha mabasi. Daladala ilipowasili mjini aliteremka na kuanza kutembea kuelekea kwenye vibanda vya kukatia tiketi. Wakati alipokuwa akitembea alishangaa ghafla amevamiwa na chizi na kuanza kupewa kipigo kisichokuwa na mfano.
“Wee achaaa achaaa.” Watu walijaribu kumkemea mwendawazimu yule lakini hakuonekana kujali kelele zao. Dhamira ya chizi yule ilikuwa ni kumbaka, kwahiyo alizungushana naye huku na kule ili aweze kumuangusha chini. Alikuwa akipiga kelele kuomba msaada huku akijaribu kujinasua mikononi mwake. Nguo zake zilichanika kiasi kwamba, alikuwa akidhalilika kwa jinsi ambavyo walikuwa wakizidi kuparangana kufa kuona. Hata hivyo mwanaume ni mwanaume tu, alizidiwa nguvu na kuangushwa chini, puuuu!
Wakati kichaa yule alipokuwa anapambana naye pale chini ili aweze kumbaka, wanaume wenye nguvu waliokuwa pale stendi walifanikiwa kumkamata chizi yule hatimaye Adela akasalimika. Wanawake walivua kanga zao viunoni na kisha kumsitiri Adela ambaye alikuwa amechaniwa nguo zake na kichaa yule. Alilia sana kutokana na kitendo kile cha udhalilishaji alichofanyiwa. Macho yake yalijawa na aibu kutokana na kwamba alidhalilika kwa kiasi kikubwa. Achilia mbali hayo yote lakini pia mwili wake ulijaa majeraha ya kung’atwa na kukatwa na wembe uliokuwa mkononi mwa chizi.
Kwa hasira wananchi walimvamia chizi yule na kuanza kumuangushia mkong’oto mkali, lakini baada ya muda polisi waliweza kuingilia kati kumuokoa. Adela alihisi kuchanganyikiwa kwasababu maisha yake yalikuwa hatarini kutokana na kwamba, alikatwa katwa na wembe ambao hakujua ulikuwa unatumikaje awali. Zaidi ya hilo, chizi yule alikuwa na kidonda kibichi katika mdomo wake wa chini. Hivyo basi kama chizi yule ameathirika na virusi vya UKIMWI basi moja kwa moja atakua amemuambukiza na yeye kwa njia ya yale majeraha ya kung’atwa.
Adela alijawa na wasiwasi mwingi sana. Machozi yahayakukauka katika macho yake. Kilichofanyika ni kwamba maaskari walimchukua kichaa yule pamoja na Adela na kuongozana nao hadi hospitali. Lengo ni kwenda kumpima yule kichaa ili kufahamu kama ana maambukizi ya VVU. Majibu ya vipimo vya daktari vilithibitisha kuwa yule kichaa ni muathirika wa virusi vya UKIMWI. Kwahiyo moja kwa moja Adela atakuwa ameambukizwa virusi hivyo.
Adela aliposikia hivyo alidondoka chini na kupoteza fahamu kwa muda wa masaa manne.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com
Presha ilipanda ghafla baada ya kusikia kwamba yule chizi ni muathirika wa virusi vya UKIMWI. Alilia sana na kumlaumu Mungu kwanini ameruhusu yale yote yatokee katika maisha yake. Alitafakari jinsi ambavyo familia yake inajitahidi kumsomesha kwa shida ili mwisho wa siku aje kuwa msaada kwao katika maisha ya mbeleni, lakini tayari maisha yake yalikuwa yameshadondokewa na doa lisilobanduka hata kwa jiki. Alivuta picha jinsi ambavyo mama yake atamlilia siku ambayo atakuwa amelazwa ndani ya jeneza, kwasababu ya gonjwa ambalo limemdondokea kama zali. Fikra zake zilienda mbali zaidi kwa kuwaza ni mkosi gani unamuandama katika maisha yake kwavile amekuwa akibadili matatizo kama nguo. Yaani leo ana nyekundu, kesho nyeusi, kesho kutwa kijani.
Mawazo mazito yaliuchosha ubongo wake, mara baada ya kupata fahamu. Alijihisi mchovu na asiye na nguvu asilani. Alishindwa kuzuia hisia za uchungu zilizokuwa zinapelekea machozi na makamasi kumtoka bila breki.
Baada ya muda mfupi, mlango ulifunguliwa nesi akachungulia mule wodini na kisha akaufunga mlango tena, na kuondoka bila kuzungumza naye chochote. Zilipopita dakika tatu nesi yule alirudi huku akiwa ameongozana na daktari mmoja.
“Nyamaza kulia binti, usiwe na wasiwasi wala presha kwasababu tatizo lako linatatulika.” Daktari alisikika.
Adela alizidi kulia kwa masikitiko makubwa kwasababu alijua maneno yale ni ya kumtia moyo. Aliona safari ya matumaini imewadia bila kupenda.
“Nisikilize kwa makini, nakupatia huduma ya dharura ijulikanayo kwa jina la ‘POST- EXPOSURE PROPHYLAXIS’ (PEP) ambayo husaidia kuzuia maambukizi ya virusi vya UKIMWI ndani ya masaa 72 baada ya maambukizi ya virusi hivyo. Huduma hii huenda sambamba na chanjo iitwayo ANTIRETROVIRAL MEDICINES (ART) yenye nguvu ya kukukinga na maambukizi ya VVU.”
“Eehuuuu!” Adela alishusha pumzi huku akitabasamu kwa mbali, baada ya maneno ya daktari kurejesha matumaini yaliyokuwa yamepotea.
“Kwahiyo dokta sitapata maambukizi?”
“Haswaaaa, bila shaka, maadamu tunakupatia kinga hii ndani ya masaa 72, ninauhakika utaendelea kuwa mzima usiye na maambukizi. Baada ya miezi mitatu nenda kapime afya yako kwa uhakika zaidi.”
“Sawa, lakini kwani huduma hii ni ngeni?” alihoji ili aweze kufahamu zaidi kwavile hakuwahi kuisikia hata siku moja. Jibu la swali hilo, halikutoka kwa daktari tena, bali Nesi alimjibu kwa kumpa simulizi fupi iliyowahi kumtokea maishani mwake.
“….Hapana, huduma hii ipo kwa miaka mingi sana, na iliwahi kunisaidia miaka mitano iliyopita wakati nilipokuwa nikimuhudumia mgonjwa mmoja wa malaria. Katika harakati za kumsaidia kwa vile alikuwa katika hali mbaya, nilijikuta nimejichoma na sindano ambayo tayari nilikuwa nimeshaitumia kwake. Nilichokifanya nilimtoa damu kisha nikapeleka maabara kucheki. Kwa bahati mbaya nikakuta yule mgonjwa ni muathirika wa virusi vya UKIMWI, nilihisi kuchanganyikiwa kwasababu ilikuwa imebaki miezi minne nifunge harusi na mchumba wangu kutoka ng’ambo. Baada ya hapo nilipewa huduma hii ya PEP hadi leo mimi ni mzima sina maambukizi ya ugonjwa huo.”
Adela alifurahi sana baada ya kusikia ushuhuda ule kutoka kwa muuguzi. Alihisi mwili wake umepata nguvu. Alimshukuru sana Mungu kwasababu hakutegemea kwamba amenusurika kupata maambukizi. Alipomaliza kuhudumiwa alikwenda hadi stendi ili aweze kurudi nyumbani kwao. Tayari ilikuwa ni jioni wakati alipopata gari linaloelekea shinyanga.
Hakuwa na hamu ya kuwahi sherehe ya ubatizo wa mtoto wa dada yake tena. Mambo yaliyokuwa yamemtokea mkoani mwanza yalimchosha mwili na roho. Alijutia uwamuzi wake wa kwenda kumtafuta mpenzi wake, kwavile amerudi na majeraha ndani ya moyo, halikadhalika katika mwili wake pia. Safarini alikuwa ni mtu wa kulia kwavile fikra zake zilikataa kung’ooka kwa Benedict.
Alitamani kupata nafasi nyingine na mwanaume huyo kwakuwa ndiye alikuwa furaha yake. Aliwaza maisha yake yatakuwaje bila mtu huyo ambaye anampenda kuliko kitu chochote humu ulimwenguni. Licha ya kwamba mwili wake ulikuwa umejaa majeraha yenye kumpa maumivu makali lakini hakujali hilo. Hakuona kabisa thamani ya mwili wake ili hali mwenye dhamana ya kuutumia alikuwa ameshatoweka katika uso wa dunia.
Usiku wa saa nne kasoro aliwasili kijijini kwao, Ibinzamata akiwa amechoka kupita kiasi. Mama alihuzunika sana kutokana na majeraha aliyoyaona mwilini mwa binti yake. Adela alieleza ukweli kwamba alivamiwa na chizi asubuhi ya siku hiyo wakati alipokuwa stendi ya mabasi Mwanza. Kuhusu habari za Benedict, hakuthubutu kuzizungumza mbele ya mama yake kwasababu alishakatazwa kujihusisha na mapenzi angali bado anasoma.CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com
Kwahiyo aliendelea kuugulia maumivu ya msiba wa mpenzi wake ndani kwa ndani. Alikonda na kubaki kama moja kwasababu ya mawazo. Alishindwa kula na kunywa ipasavyo kwasababu ya kumuwaza mtu wa ndoto zake. Alitamani angalau apate japo dakika mbili na mpenzi wake huyo, ili aweze kumweleza jinsi ambavyo anampenda.
Baada ya miezi mitatu alikwenda hospitali kupima afya yake ili aweze kujua kama ile kinga ilifanya kazi ama la! Baada ya vipimo iligundulika ni mzima asiye na maambukizi ya virusi vya UKIMWI. Alimshukuru sana Mungu kwa kumnusuru na gonjwa hilo la hatari. Kufikia muda ule afya yake, ilikuwa imehimarika vya kutosha. Tatizo lake lilibaki kuwa moja tu, ambalo ni la kuonana na mpenzi wake. Hakuchoka kumuomba Mungu siku moja aweze kuonana na Benedict hata kama sio duniani, iwe hata peponi.-
Mazishi ya mama mkwe yalipomalizika, Nelson alirejea Mwanza akiwa ameongozana na familia yake. Aliwasiliana na Mr Lee na kumjulisha msiba mzito aliokuwa ameupata. Aliongezewa wiki zingine mbili kwaajili ya maandalizi ya safari. Alifurahi sana kwasababu mke wake alionekana kuchoka sana kutokana na kufiwa na mama yake. Akilini aliwaza hadi zile wiki mbili ziishe mke wake atakuwa amepata nguvu na pia wataweza kupata muda wa kuudhuria mkutano mkubwa wa injili ambao ulikuwa unaanza siku chache za mbeleni. Mkutano huo ulikuwa umeandaliwa na mtumishi wa Mungu Isaka akishikiana na ile taasisi ya nchini Uingereza kwa muda wa siku saba jijini humo.
Siku ilipofika, huduma ya maombezi na uponyaji ilianza rasmi. Umati mkubwa wa watu walikusanyika kwa wingi katika kiwanja cha CCM KIRUMBA. Watu wengi walipata uponyaji kwa njia ya maombi. Ulikuwa ni mkutano mkubwa na wa kiistoria kufanyika mkoani humo. Mara tu baada ya mkutano huo kuanza Vivian alianza kujifanya anaumwa ili asiweze kuudhuria. Japokuwa alielezwa, uponyaji ataupata atakapokwenda katika mkutano huo wa injili, lakini aligoma kabisa. Kwa wakati huo Nelson hakuwa amegundua kuwa ule ni ujanja wa shetani aliyekuwa ndani yake. Hata hivyo alizidi kumwomba Mungu ili aweze kumuwezesha mke wake kuhudhuria mkutano ule wa kipekee kabisa.
Siku ya mwisho kabisa ya mkutano, Vivian alijihisi kuna nguvu inamsukuma kwenda katika mkutano ule pasina kutambua ni nguvu gani. Mume wake na mwanae walikuwa tayari wameshatangulia mkutanoni. Baada ya kupingana kwa muda mrefu na nguvu ile iliyokuwa inamsukuma hatimaye alijikuta njiani, akitembea kwa mwendo mkali kuelekea kule kwenye mkutano. Kwa vile hapakuwa mbali sana muda mfupi baadae alifika eneo la tukio. Ghafla mapepo yaliyokuwa ndani yake yalianza kufurukuta kwa vile lile eneo halikuwa la kawaida. Wahudumu walijaribu kumshika lakini hakushikika kwa vile alikuwa na nguvu zisizo za kawaida. Alianza kukimbia kuelekea madhabauni ambapo kulikuwa na watumishi mbalimbali wa Mungu.
Watu wote waliacha kusikiliza mahubiri na kumtazama Vivian ambaye alionekana kuwa na mapepo hatari. Alikuwa akilia kama paka, wakati mwingine alijongea mithili ya nyoka mwenye sumu kali. Watumishi wa Mungu, walianza kufanya maombezi ya kukemea mapepo yaliyokuwa ndani yake. Yalifanyika maombi mazito ya kuvunja maagano ya Viviana na kuzimu. Ilikuwa ni shughuli kwelikweli kwavile alikuwa na maagano mengi katika ulimwengu wa giza. Wachungaji waliomba maombi ya kuvunja maagano yale. Watu wote waliokuwa uwanjani pale walishiriki katika mapigano makali ya kiroho, kumpigania Vivian ambaye alikuwa mateka wa siku nyingi katika ulimwengu wa kuzimu.
Kwa kuwa hakuna nguvu inayoweza kusimama juu ya nguvu ya Mungu, maagano yote ya kuzimu yalivunjwa na hatimaye VIVIAN akawa huru.
Alipewa nafasi ya kutoa ushuhuda pamoja na kumshukuru Mungu. Alipokea kipaza sauti na kuanza kuzungumza huku akilia. Kwa masikitiko makubwa alisimulia kila kitu ambacho aliwahi kukifanya yeye na mama yake wakishirikiana na ulimwengu wa kuzimu. Ilikuwa ni hadithi iliyokuwa inaonekana kama vile ya kusadikika lakini ilikuwa na ukweli wa asilimia mia moja.
Alipomaliza kutoa ushuhuda wake alishangaa kumuona mume wake pamoja na mwanae wakimfuata pale madhabauni na kumkumbatia huku wakilia sana. Waumini walishangilia kwa vigelegele baada ya kuona tukio lile. Isaka alishangaa sana kumuona rafiki yake pale mbele akikumbatiana na mwanamke yule. Alimpa kipaza sauti na yeye aweze kuzungumza na ndipo alingundua kuwa yule ni mke wake.
Nelson na mwanae walilia sana baada ya kugundua kuwa vifo pamoja na matatizo yote waliyokuwa wakipitia katika familia yao, yalisababishwa na Vivian ambaye, hawakuwai kumdhania hata siku moja kwamba anaweza kufanya mambo makubwa namna ile. Pamoja na hayo lakini waliishia kumshukuru Mungu kwa kumkombo katika mapito ya kuzimu.
Mtumishi wa Mungu alimuongoza Vivian katika sala ya toba na hatimae akampokea Yesu kuwa bwana na mokozi wa maisha yake. Baada ya hapo aliagiza kile kibuyu cha kichawi kikaletwe ili kije kuchomwa. Vivian alikwenda hadi hotelini na kukichukua na kisha kukifikisha kwa mchungaji. Kilipokelewa na mchungaji kisha kikachomwa palepale uwanjani huku watu wakishangilia kwa ishara ya ushindi. Baada ya maombezi Nelson na familia yake walirudi katika hoteli waliyokuwa wanaishi kwa muda.
********CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com
Ndani ya wiki hiyo hiyo kulifanyika mkutano mwingine wa injili kijijini kwa kina Adela. Mtumishi wa Mungu, Abeli kutoka nchini Kenya aliongoza huduma ya maombezi na uponyaji. Adela na ndugu zake walihudhuria mkutano huo ambao ulifanyika jirani kabisa na nyumbani kwao. Roho mtakatifu alimuonyesha mtumishi wake kwamba, ukoo wa akina Adela ulikuwa katika mateso makubwa ya mizimu. Yalifanyika maombi ya kuvunja na kuharibu kabisa nguvu ya mizimu hiyo, iliyokuwa inawafuatilia miaka na miaka, hatimae wakawa huru.
********
Siku chache baadae Nelson na familia yake waliwasili London International airport kwa ndege aina ya Boeing 222-400ER-Condor. Walipokelewa na Mr Lee na kisha wakafikishwa katika nyumba iliyokuwa imeandaliwa kwaajili yao. Siku iliyofuata Nelson alisaini mkataba wa kufanya kazi na taasisi ile kwa muda wa miaka 10 kama mhandisi mkuu. Walianza maisha mapya huko nje ya nchi huku wakiendelea kumtumikia Mungu kwa furaha.
Miaka kumi baadae Nelson na mke wake walikuwa na mafanikio makubwa ya kimwili na kiroho.
**********
Ulipoanza mwaka mpya wa masomo, Benedict alianza kusomeshwa bure kama ambavyo baba yake aliahidiwa mwanzoni. Elimu yake ya kidato cha tano na sita, alisoma katika shule iitwayo Heven star high school iliyopo jijini London. Shule hiyo ilikuwa chini ya taasisi ‘spiritual health.’ Baada ya miaka miwili, alipata ufaulu wa juu sana na kufanikiwa kujiunga na chuo kikuu cha Harvard kilichopo nchini marekani, kusomea Bachelor of science in mathematics (yaani shahada ya sayansi katika hisabati). Alifurahi sana kuwa mmoja wa wanafunzi wa chuo kile kwasababu, ilikuwa ni ndoto yake tangu alipokuwa sekondari. Marafiki zake wote ambao aliwahi kusoma nao, walikuwa wanafahamu jinsi ambavyo alikuwa anakipenda chuo hicho.
Aliendelea kupenda somo la hesabu, kwasababu ilikuwa ikimkumbusha kipindi cha nyuma, alipokuwa na mpenzi wake. Aliapa kulipenda somo hilo hadi mwisho wa maisha yake kama ishara ya kumuenzi Adela. Hakuwa na matumaini ya kuonana nae tena kwasababu hakujua kuwa ni mzima ama ni mfu. Walipotezana katika kipindi kigumu mno. Umbali wa kijeografia ndiyo uliopoteza kabisa ndoto zake za kuonana na binti huyo kama endapo angekuwa ni mzima. Hakuwa na matumaini ya kurejea Tanzania ili hali wazazi wake hawana mpango huo.
*******
Adela alipohitimu kidato cha sita alifanikiwa kuongoza kitaifa katika mitihani ya taifa. Jina lake lilitikisa kwenye vyombo vya habari vya hapa nchini, kwa vile alifanya vizuri sana, katika masomo yake yote. Kwa bahati nzuri alipata ufadhili wa kwenda kusoma katika chuo kikuu cha Harvard cha nchini Marekani. Alifurahi na kufarijika sana kwasababu katika kumbukumbu zake anakumbuka kwamba kipindi alipokuwa sekondari alikuwa akimsikia Benedict akisema kuwa, anatamani siku moja kusoma katika chuo hicho maarufu duniani.
Siku moja Adela alikwenda kufanya manunuzi ya vyakula katika supermarket iitwayo Morton Williams iliyopo jirani kabisa na chuoni. Baada ya manunuzi hayo wakati anatoka nje, ghafla mlangoni alikutana na Benedict anaingia ndani. Wote kwa pamoja walishikwa na bumbuwazi kwavile hakuna aliyekuwa akiamini kwamba amemwona mpenzi wake. Adela alidondosha mifuko iliyokuwa mikononi mwake na kisha akakumbatiana na Benedict huku wote wakilia kwa furaha.
“Are you the one?” (Hivi ni wewe jamani?) Adela alizungumza huku uso wake akiwa ameuangalizia mgongoni mwa mpenzi wake wakati alipokuwa amemkumbatia kwa nguvu zote.
“Naam!, ndiyo mimi Benedict wala hujakosea mpenzi.” Kijana alizungumza kwa furaha huku mikono yake ikifanya kazi ya kufuta machozi yaliyokuwa yanaendelea kumdondoka mwenzie.
“Nilijua ulifia katika ajali ya moto iliyoteketeza nyumba yenu.”
“Hapana, familia yetu iliondoka katika nyumba ile baada ya kufukuzwa na uongozi wa kampuni ambayo baba alikuwa akifanya kazi. Kwahiyo waliopoteza maisha katika ajali ile ya moto walikuwa ni watu wengine ambao walihamia pale.” Benedict alisikika.
Siku ile ilikuwa ni ya furaha, kuliko siku zote ambazo waliwahi kufurahi maishani mwao. Walianza kusimuliana yaliyojiri tangu ile siku waliyopotezana, hadi sababu zilizopelekea kufika chuoni pale. Walipohitimu chuo kikuu, Benedit alimpeleka Adela nyumbani kwao Uingereza kwenda kumtambulisha kwa wazazi wake. Walipokelewa vizuri sana na kutakiwa kila heri katika maandalizi ya harusi, ambayo walipanga kufanyia jijini London.
Wote walikuwa na bahati sana kwakuwa walipata kazi yenye kipato kizuri, siku chache baada ya kuhitimu elimu yao. Mwaka mmoja baadae walioana kwa harusi kubwa ambayo ilihudhuriwa na ndugu na marafiki wa pande zote mbili. Adela hakupenda kuwa mbali na mama yake kwahiyo, alifanya mpango mama yake na kaka yake wakaamia nchini humo miezi michache baadae.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com
Mwisho
#Mwisho
#Funzo: Usichoke kumtumainia MUNGU katika maisha yako kwavile huijui kesho yako.
AHSANTE SANA.
0 comments:
Post a Comment