Search This Blog

NILIPANGA NYUMBA MOJA NA MAJINI - 5

 





    Simulizi : Nilipanga Nyumba Moja Na Majini

    Sehemu Ya Tano (5)





    “Umeona nini mzee wangu?”

    “Nimeona msichana ananizomea.”

    “Kweli?”

    “Ee. Ndiyo hayo mambo unayosema?”

    “Ndiyo hayo mzee.”

    “Twende,” alisema, nikaanza kutangulia mbele, mzee akanifuatia kwa nyuma. Hatukuwa tukiongea chochote, najua sababu. Kila mmoja alikuwa anaiwaza hatari ya mbele.

    Tuliingia ndani, tukafika sebuleni, lakini sikuiona simu kwenye kochi.

    “Ona sasa mzee, simu niliitupia hapa, lakini haipo.”

    “Au unayo mfukoni kijana?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hapana, nina uhakika,” nilisema huku nikijipapasa mifukoni, hakukuwa na simu.

    “Nitajie namba nijaribu kuibipu,” yule mzee aliniambia huku akitoa simu yake mfukoni. Nilimtajia namba zote, akawa anaziandika, kisha akapiga huku simu akiwa ameiweka kwenye sikio lake la kulia. Nilishtuka sana  kusikia simu yangu inaita kutokea kwenye chumba cha wale wapangaji wenzangu.

    “Si hiyo?” yule mzee aliniambia akiniangalia kwa mshangao.

    Mzee alikata kisha akapiga tena, ikaita tena kutokea kulekule, nilizidi kuogopa, nikamwambia tutoke lakini uzee kweli dawa, aliniambia hakuna haja ya kutoka dawa ni kupambana tu.

    Alinisogelea na kuniambia kwa sauti ya chini:

    “Niwagongee mlango?”

    “Si watakasirika?”

    “Sasa kama unaogopa watakasirika, unadhani simu yako utaipataje?”

    “Haya wagongee. Lakini subiri, kwa nini tusiende kwanza chumbani tukajua nani alikuwa anachungulia nje?”

    “Kijana unaonekana muogamuoga sana, we mwanaume bwana, jifunze kukabiliana na hali kama hii, sawa?”

    “Sawa mzee.”

    “Haya twende huko chumbani kwako unakotaka tukaone huyo msichana.”

    Tulifungua mlango wa chumbani, hakukuwa na mtu, ila shuka nililoliacha kitandani asubuhi silo, lilitandikwa jingine pia la kwangu.

    “Khaa!” nilishangaa.

    “Nini?”

    “Hili shuka.”

    “Limefanyaje?”

    “Silo nililolitandika asubuhi.”

    “Lakini la kwako?”

    “Ndiyo langu.”

    Niliangalia mazingira mengine ya mle ndani na kubaini kwamba, kuna vitu vingi sana vilikuwa ndivyo sivyo.

    “Si umeona hayupo?” yule mzee aliniuliza, nikamjibu ndiyo, akasema twende tukachukue simu yetu kwenye kile chumba ambacho ilikuwa inaita.

    Moyo wangu ulikuwa mzito sana, nilihisi kizunguzungu, nilitamani kukaa chini na kumwomba yule mzee asichukue uamuzi wa kuifuata ile simu, lakini ningeipataje simu yangu wakati ina namba kibao?

    “Kijana, ngoja nikuoneshe dawa moja ya hao viumbe wasiotaka kuonekana,” alisema yule mzee, nikamuuliza ni ipi hiyo.

    “Tulia wewe,” alisema huku akiingiza mkono mfukoni na kutoa kimfuko kidogo, akakifungua akatoa kitu. Nilipomuuliza ni nini akajibu:

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ni bangi.”

    “Sawa kabisa, hiyo ndiyo dawa, ngoja nikupe kiberiti.”

    Katika mambo yaliyonishangaza ni hilo, tulitafuta kiberiti chumbani hadi sebuleni lakini hakikuonekana, mbaya zaidi mimi nilikuwa na kawaida ya kununua viberiti bunda zima, lakini pia sikuona popote.

    “Kweli una kiberiti ndani?” yule mzee aliniuliza.

    “Kiberiti kipo na uzuri ni kwamba, nina bunda zima, pia silioni.”

    Nilimwona yule mzee akisimama wima na kunyoosha mikono juu kama mtu anayeomba dua kwa Mungu.

    “Kijana nimejua sasa, ngoja kidogo,” alisema huku akitoka na mimi nikimfuata kwa nyuma.

    Wakati tunapita kwenye korido jirani na vyumba vile vya wenzangu, nikaisikia simu yangu ikiita.

    “Mzee mzee, hiyo bwana,” nilisema, mzee akasimama na mimi nikasimama nyuma yake, tukasikia sauti ya mwanaume ikipokea simu yangu:

    “Haloo…Juma…Juma gani wewe? Nakuuliza Juma gani maana mimi ndiyo mwenye simu hii, huyo unayemsema simjui na wala hajawahi kumiliki simu hii,” sauti ya kiume ilisema, ukapita ukimya kidogo kisha sauti hiyohiyo ikasema:

    “Kama unabisha siyo simu yangu ongea na mke wangu huyu hapa.”

    Mara nikasikia:

    “Haloo…ni kwa nini mnapenda sana kumfuatafuata mume wangu, mara mzungumzie bangi, mara mtusemee kwa watu.”

    Nilitamani sana kumwambia asiniache katika safari yake maana kwangu kwa muda ule palishaharibika, ningeuawa na watu wasioonekana.

    “Wewe nisubiri kijana,” mzee aliniambia akiendelea kwenda nje sikukubali.

    “Mzee humu ndani mimi sikai, nimeshajua sasa.”

    “Umejua nini?”

    “Huyo Juma anayetajwa hapo nafanya naye kazi na ilikuwa aje na bangi kwa ajili ya hawahawa watu wa humu ndani.”

    Mzee aliniangalia, akaniuliza:

    “Wewe kijana unaye Mungu?”

    “Ninaye.”

    “Huwa unakwenda kusali?”

    “Sana.”

    “Lini umekwenda mara ya mwisho?”

    “Ungeniambia tatizo ni kusali au?”

    “Si hilo tu, ila una matatizo mengi. Hivi hapa tumesimama, nyuma yako nimemuona yule msichana amekuinamia akikung’ong’a kama mara tatu kwa harakaharaka.”

    Nilitimua mbio kuelekea kusikojulikana, nikaenda kufunga breki kwenye mtaa mmoja ambao ukienda kushoto kwangu unakwenda kutokea kwenye barabara ya kwenda Kigogo Mbuyuni.

    Baadhi ya watu walioniona nilivyo walitambua nina tatizo zito kichwani, mzee mmoja aliniuliza kama nakimbizwa nimefumaniwa.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Sijafumaniwa mzee, lakini kwa tatizo langu afadhali ningefumaniwa.”

    Huyu mzee alikuwa amebeba kibegi kidogo mgongoni, alivaa suti nyeusi huku akionekana ni mzee mwenye heshima kubwa katika jamii inayomzunguka.

    “Tatizo nini, hebu nisimulie kidogo tu,” alisema huku akinivutia pembeni. Nilimsimulia kila kitu, alichokuwa akinishangaza sasa, kila hatua ya maelezo yangu alikuwa akiachia tabasamu hata pale nilipoamini kwamba ninachokisema kwa wakati huo asingetabasamu na uso wake ungeonesha kushtuka.

    Nilipomaliza nikanyamaza na kumwangalia kwa woga, nilitaka kuamini ni yule mwanaume aliyepokea simu yangu kule nyumbani amenibadilikia ili nisiweze kumtambua.

    Moyoni nilisema kuwa, kama kweli ni yeye atakapojidhihirisha  tu kwangu nitoke mbio na kwenda kuingia kwenye nyumba ya mtu yeyote mbele yangu.

    “Tatizo ni hilo dogo tu?” aliniuliza.

    “Ni hilo tu mzee wangu. Ukiweza kunisaidia nitashukuru sana.”

    “Nyumba yenyewe iko wapi?”

    “Kule nyuma nyuma.”

    Nilimwona akiingiza mkono mfukoni na kuchomoa simu nyeusi ndogo, wengi wanaziita za tochi kisha akabonyezabonyeza na kuiweka sikioni. Moyoni nilisema yaleyale.

    “Si ajabu anawasiliana na yule mwanamke wa kule nyumbani.”

     Nikamsikia akiuliza:

    “Isdory, bado mpo hapo?”

    Nadhani huyo jamaa alisema yupoyupo maana nilimsikia huyo mzee akisema: “Unaweza kuja na akina Tino hapa kwenye kibanda tulichotuma pesa asubuhi ya leo? Haya njooni.”

    Niligeuzageuza kichwa na kukiona kibanda cha kutuma pesa kwa kupitia mitandao mbalimbali ya simu. Nikajua amewaita watu waje pale.

    Baada ya dakika kama tatu, wakafika watu kama saba, wanne wanawake, watatu wanaume akiwemo Isdory na Tino.

    “Huyu bwana anaitwa,” alianza kusema yule mzee akiniangalia nikajua anataka nijitambulishe jina mimi mwenyewe, nikafanya hivyo. Nilipomaliza, ndipo yule mzee akawaambia wenzake kisa chote cha kwangu, mwanzo hadi mwisho kama nilivyomsimulia awali.

    “Ndugu, sisi wote walokole, kazi hiyo tunaimudu kwa vile mara nyingi huwa tunatumia jina la Bwana na Mwokozi wetu kufukuza uchafu kama huo, sasa itabidi utupeleke kwenye hiyo nyumba,” alisema yule mzee.

    Nilianza kutembea mimi na wao wakawa wananifuata kwa nyuma. Wale wanawake niliwasikia wakizungumzia mwanamke mmoja aliyeangushwa chini na mapepo akawa anataka kupigana na wale waliokuwa wakimwombea. Moyoni nikasema:

    “Leo huko sijui.”

    Tulifika nje ya nyumba, kitendo cha kwanza ambacho si cha kawaida, nilimwona yule kijana muuza maji akitoka ndani. Alivaa kama siku alivyokuja nikamwingiza ndani.”

    Nilishtuka sana, yeye hakushtuka, ila aliponiona akaniambia:

    “Bro nashukuru sana wamenilipa pesa zangu.”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Sijui ni nini kilinipata nilijikuta nikisema sawa, sikuongeza neno jingine lolote lile.

    “Ni humu waheshimiwa,” niliwakaribisha wale watu nikiwa nimeshapishana na yule kijana.

    Waliingia wote ndani, wakasimama katikati ya korido kisha wakawa wananiangalia, yule akaniuliza:

    “Hivyo vyumba ni vipi?”

    Sikumjibu kwa sauti, nilinyoosha mkono kuelekea kwenye vyumba vyote viwili. Vilioneshwa kufungwa kwa ndani lakini hakukuwa na sauti ya muziki wala maongezi yao.

    “Baba katika jina la Yesu,” yule mzee alianza ghafla.

    “Amiiiin,” walijibu wote aliofuatana nao, tena walijibu kwa sauti ya juu kisha wakatulia kimya.

    Akaanza kusali akitaja maneno ya kutisha, nilimsikia akisema, choma moto roho mtakatifu, mara Malaika Michael shuka na panga likatalo kuwili.

    Kifupi yule mzee alisema maneno ya ki-Mungu kwa jinsi nilivyoelewa mimi. Ikafika mahali akasema:

    “Paaza sauti yako.”

    Ndipo wengine nao wakapokea kwa kila mmoja kuomba kivyake. Wengine walisikika wakisema wanaangusha na kuvunja ngome za ibilisi, wengine wanachoma moto makazi ya shetani, wengine wanamwagia damu ya Yesu pale ndani. Nilianza kuhisi amani iliyoje, niliamini ukombozi umefika tayari kwani sauti tu niliisikia ikipenya hadi kwenye mbavu zangu.

    Waliomba sana, kuna wakati mimi nilihisi kuchoka lakini wao waliendelea tu hadi moyoni nikasema kweli ni watu wa Mungu.

    Ghafla nilianza kuona moshi mweusi ukitoka chini ya milango yote ya wale ndugu, mlango wa sebuleni kama sikikosei na mlango wa chumbani. Moshi ulikuwa mzito kiasi kwamba, kuna wakati nilihisi kupaliwa na kukohoa kwa nguvu lakini wao hawakuonesha dalili ya kusumbuliwa na moshi huo.

    Mara, milango yote miwili ikaanza kufunguka yenyewe polepole huku maombi yakiendelea kwa kasi na nguvu ya ajabu. Milango hiyo ilifunguka hadi ikafika mahali ndani kukaonekana.

    Cha ajabu sasa, vyumba vilikuwa vyeupe, ndani yake hakukuwa na kitu chochote, hata karatasi. Ilikuwa kama chumba kilichopigwa deki au kufagiliwa kwa ajili ya maandalizi ya kuingia mkaaji mpya.

    “Ha! Oneni jamani,” nilijikuta nikisema hivyo. Nilibaini kwamba, wale watu hawakuona wakati milango inafunguka kwa vile walipokuwa wakiomba walifumba macho na walikuwa wakijipigapiga kwenye viganja kwa kutumia ngumi.

    Yule mzee alipoona vile akasema:



    “Katika jina la Yesu.”

    “Amiiin.”

    “Sasa tushushe uwepo wa Bwana mahali hapa, kwamba akapafanye pawe mahali salama, penye amani na utulivu wa hali ya juu, kila mmoja sasa amwombe Bwana hivyo.”

    Wakaanza kuomba tena, safari hii si kwa kukemea kama mwanzoni, ilikuwa sauti yenye upole na utii, mara nikasikia mlango mkubwa ukigongwa kwa nguvu.

    “Ngo ngo ngo ngoo.”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ingia,” nilisema lakini huku nikienda mlangoni, nikaufungua! Mbele yangu alisimama yule dalali.

    “Karibu bwana.”

    “Ee bwana nini umefanya sasa?” ndilo swali lake hata kabla ya salamu.

    “Kwa nini?”

    “We hujui umefanya nini? Si wako watu humo ndani, wamekuja kufanya nini hapa? Hujui kama kuna watu umewaumiza? Wewe ungefanyiwa hivyo ungekubali kweli?”  

    “Kaka unajua ukija kwangu njoo kwa heshima zako zote na hoja zenye msingi, usije kama mwendawazimu mpya, wewe unachokisema mimi sijakisema kwako? Ulichukua hatua gani wakati naumia mimi?”

    “Lini umeniambia?”

    “Wewe sijawahi kukupigia simu kukwambia? Tena ukasema kama vipi nihame lakini sitarudishiwa kodi ya nyumba na mimi nikakujibu niko tayari kwa hilo…”

    “Sasa wewe ulikuwa ukiteswa kwa lipi, weka ushahidi hapa kwamba ulikuwa ukiteseka sana.”

    “Sina haja, mimi ndiyo najua.”

    Wakati tukijibizana hivyo, wale waombaji walikuja juu kwa kuomba. Walipaza sauti sana wakisema moto uteketeze kila hila na jambo lolote ambalo linakwenda kinyume na mimi ndani ya nyumba ile.

    Ghafla, nilimwona yule dalali akianza kuyumba kama mlenvi, alikwenda kulia, kushoto, akasimama, akawa kama ananijia mimi, nikamkwepa, akaenda kushoto na kuanguka puu!

    Kwangu ilikuwa ni furaha kwani nilipata picha kwamba, yule dalali alikuwa anahusika moja kwa moja na matukio yote ya ajabu mle ndani. Niliwaita wale watu wanaofanya maombi na kuwataka washuhudie ambapo walipomwangalia dalali waliongeza mkazo wa maombi yao.

    Mwisho, dalali aliamka akiwa kama hana ufahamu, alikalishwa chini na kuhojiwa ambapo alisema mambo ya ajabu sana. Alisema mwanaume aliyekuwa akiishi ndani ya vyumba vile ni yeye na mkewe, akasema mkewe ni jini kwa asilimia mia moja ila yeye si jini bali mkewe alimfanya awe na uwezo wa kutoonekana wala kujulikana na mtu.

    Alipoulizwa kama alikuwa anapata faida yoyote kwa kitendo cha kugeuka kuwa jini alijibu hakuna ila alikuwa anasikia raha.

    “Mfano, huyu bwana tangu ameishi humu hajawahi kutuona kwa macho lakini sisi tulikuwa tunamuona siku zote, tulikuwa tunaingia chumbani mwake na kumfanyia mambo yetu yeye hajui.”

    Jambo lingine ambalo lilinishangaza sana ni pale dalali huyo aliposema yeye alikuwa na uwezo wa kujua anachokusudia kukifanya mtu hata akiwa Dodoma na akakizuia mapema. Ila, anashindwa kujua endapo mtu huyo atakuwa anakusudia kufanya jambo kwa kuliwaza moyoni mwake bila kulisema kwa mtu.

    Nilimuuliza mfano, akajibu mfano ni mimi na mfanyakazi mwenzangu tulipokuwa tumepanga kutumia bangi kuwaangamizi yeye na mkewe, walijua kwa sababu tulijadili kwa sauti ndiyo maana wao walijua. Akaongeza hata nilipoingia ndani na yule mzee aliyeshindwa akatimua, walijua tumepanga ndiyo maana wakawahi kwa kuchukua simu na kufanya mahoka mengine.

    Yule mzee mkubwa wa wale waombaji akamuuliza:

    “Ina maana mkeo jini kwa sasa yuko wapi?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Yule bwana akajibu atakuwa amerudi ujinini kwa sababu wakati wanaanza kuomba mkewe ndiye aliyekuwa wa kwanza kuhisi anaungua moto na kuanza kulia kwa sauti mpaka ndugu zake wakajitokeza kumtwaa kwenda naye ujinini.

    Yule mzee mkubwa wao akauliza swali jingine ambalo na mimi nilitaka kuuliza. Alimuuliza hivi:

    “Sasa watu wanasema majini wana uwezo mkubwa, wanaweza kupata fedha na mali yoyote ile, sasa kama wewe ulikuwa mume wa jini kweli ni kwa nini aliamua uwe dalali?”

    Dalali akajibu: “Mimi sikuwa dalali, bali nilijifanya dalali ili nipate mtu wa kumpangisha ndani kwa sababu mimi na mke wangu tulipenda kuwachezea watu wanaoishi ndani.

    “Mimi nina eneo Ilala la kuuza magari, pia nina duka kubwa sana Mnazi Mmoja, sina shida ya maisha wala ya fedha.”

    Kwa maneno yake hayo nilikubaliana na yeye kwani ni kweli hali yake haikuwa ya kuchoka. Hata siku ya kwanza nilipokutana naye nilishangaa dalali gani ana mwonekano wa kibosibosi ingawa hakuwa na gari. Hapo na mimi nikapata nguvu ya kumuuliza swali:

    “Sasa bwana dalali wa bandia, uliwezaje kusababisha mimi nipate namba yako ya simu kwa rafiki yangu anaitwa Mohamed Kombe na akasema wewe ni dalali unaitwa Yusuf Mwamba?”

    “Sikia bwana Humuli. Nimeshasema sisi tuna uwezo wa kujua kile kinachojadiliwa mahali na kukifanyia kazi. Dalali anayeitwa Yusuf Mwamba yupo, huyo rafiki yako tulimchezesha ulimi wakati wa kutaja namba, akazitaja zangu badala ya za Yusuf.”

    Nilichoka kabisa, yule mzee mkuu akasema tumwingize ndani maana watu waliokuwa wakipita walianza kukodolea macho pale nje.

    Kule ndani, dalali aliendelea kuzungumza mambo mengi sana lakini kuna wakati alijipinda na kujishika mgongo akidai anahisi maumivu makali ya moto. Alisema sehemu hiyo ipo kama kuna mtu amebandika jiko la mkaa.

    “Mungu amekuponya sana labda kama hutajutia matendo yako ya nyuma,” alisema yule mzee aliyenisaidia.

    “Mimi sitaki tena, kwanza najuta kwa nini niligeuka adui na kufanya vile kwa watu wengine. Naomba mniombee sana kwa huyo Mungu wetu.”

    Yule mzee alimwelekeza kanisa lake ambalo halikuwa mbali na pale nyumbani, yule dalali akasema atakwenda kesho yake mapema.

    Mimi pia nilialikwa, nikakubali kwenda kesho yake. Walipoondoka, nilibaki na dalali. Wasiwasi ulinishika lakini nikawa nasikilizia. Kila baada ya dakika tano dalali aliingia chumbani kwangu na kuniomba nimsamehe kwa yote yaliyopita.

    Usiku nililala usingizi mzuri hadi kunakucha kiasi kwamba sikuamini kama ni kweli ile nyumba ilikuwa vile. Kesho yake nilikwenda kazini, jioni nilikwenda kwenye lile kanisa ambapo nilimkuta dalali ameshafika.

    Tulianza kuwa waumini wa kanisa hilo. Baada ya wiki mbili, dalali alimleta mke wake  na mtoto mmoja ndani, kumbe alioa na familia yake ilikuwa Dodoma. Baada ya mwezi mmoja na mimi nilihamia Buguruni ambapo nilioa lakini bado nasali kulekule Magomeni na yule dalali.

    Namshukuru sana Mungu kwa kunipigania. Ile mikono ilikuwa si salama bila neema ya Mungu. Nadhani shetani alipanga nife lakini ameshindwa katika jina la Yesu. Amina.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



                                                        MWISHO.

0 comments:

Post a Comment

Blog