Search This Blog

MWANAMKE JINI - 2

 







    Simulizi : Mwanamke Jini

    Sehemu Ya Pili (2)





    ILIPOISHIA

    Zena akacheka. Alipofanya hivyo haiba ya uso wake ilibadilika na kuwa ya kupendeza zaidi.

    “Uliniona katika umbo gani?” akaniuliza.

    “Mwili wako ulikuwa na manyoya marefu na miguu yako ilikuwa na kwato kama ya punda. Kwa kweli nilipatwa na uoga mkubwa”

    “Ndiyo maana siku ile uliponiona kule Mabanda ya Papa ukaongeza mwendo mpaka ikatokea ile ajali?”

    “Kumbe unajua. Ni kweli niliongeza mwendo baada ya kukuona wewe”

    Msichana akacheka tena.

    “Hukupaswa kunikimbia. Iile umbo uliloniona nalo nyumbani siku ile ndilo umbo langu kwa maana mimi si binaadamu bali ni jini”

    “Nilishafahamu kuwa wewe si binaadamu. Binaadamu hawezi kuwa na umbo kama lile”

    “Nimefurahi kama umenielewa, kwa hiyo usiniogope tena”

    “Kukuogopa ni lazima kwa sababu sijakuzoea”

    “Taratibu tu utanizoea. Mimi nimekuwa na wewe kwa miaka mingi bila wewe mwenyewe kujua”

    “Umekuwa na mimi kwa miaka mingi?”

    “Ndiyo. Naweza kusema tangu ukiwa kijana mdogo”

    “Ulikuwa uko wapi?”

    “Nilikuwa na wewe”

    “Sijawahi kukuona”

    SASA ENDELEA

    “Ni kweli. Sikutaka unione wala kujitambullisha kwako kwa sababu muda wa wewe kunitambua mimi ulikuwa haujafika”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nikaguna. Lakini niliguna moyoni mwangu.

    “Siku ile niliyokuazima kitabu ndio siku ambayo nilipanga kujitokeza rasmi kwako”

    Nikabaki kimya nikimsikiliza. Maneno yake yalikuwa yameshitua akili yangu.

    “Samahani kwa matatizo yote yaliyokutokea ambayo kwa namna moja au nyingine niliyasababisha mimi. Haikuwa kusudio langu kukusumbua bali nililazimika kufanya vile ili uweze kunitambua” Zena aliendelea kuniambia.

    “Umeniambia kwamba wewe ni jini, ni jini wa aina gani na unaishi wapi?” nikamuuliza ili niweze kumuelewa vizuri.

    “Mimi ni jini wa ukoo wa Ummi Subian, yaani nimechanganya kabila mbili, upande mmoja ni ruhani na upande mwingine ni subian. Yaani ninatumia bara na pwani lakini zaidi mila zangu ni za kipwani”

    Nilidhani alikuwa amemaliza. Akaendelea.

    “Umeniuliza ninaishi wapi. Kwetu ni Sham na kwa hapa Afrika Mashariki maskani zangu zipo katika eneo lote hili la pwani ya Afrika Mashariki kuanzia Somalia, Kenya na Tanzania.

    “Niliwahi kukwambia jina langu ninaitwa Zena. Baba yangu anaitwa Jabalkeys na mama yangu ni Ummi Mariam. Huko ujinini mimi natambulika kama Zainush binti Jabalkeys”

    Alipofika hapo Zena alinitazama akaniuliza.

    “Umenielewa vizuri?”

    “Nimekuelewa” nikamjibu.

    “Kuna kitu kimoja nataka nikwambie” akaniambia.

    “Niambie”

    “Nimekuchunuka na ninataka uwe mume wangu. Ninakuahidi kuwa nitakupa utajiri”

    Nikashituka.

    “Kama wewe ni jini, nitawezaje kuwa mume wako?” nikamuuliza.

    “Majini huoana na binaadamu. Kama huamini nenda kwa bibi yako aliyemzaa baba yako, muulize baada ya kuachika yeye mume wake alioa mke gani?”

    “Una maana gani, una maana kwamba babu yangu alioa jini?” nikamuuliza kwa mshangao.

    “Nataka uende ukamuulize yeye, akueleze”

    “Sawa. Nitakwenda kumuuliza”

    “Tutakutana lini tena?”

    “Niambie wewe”

    “Unadhani ni lini utakuwa na jibu?”

    “Labda keshokutwa”

    “Basi nitakutafuta”:

    “Sawa”

    Zena akafungua mkoba wake. Nilikuwa namtazama pembeni mwa macho yangu.

    Nikaona akitoa kitita cha noti nyekundu. Nilizikisia zilikuwa zaidi shilingi milioni moja. Akanipa bila kuzihesabu.

    “Chukua hizo zitakusaidia” akaniambia.

    “Asante sana” nikamwambia.

    Zena akafunga mkoba wake na kunitazama huku akitabasamu.

    “Una kitu chochote unataka kuniambia?” akaniuliza.

    “Hapana, sina kitu cha kukwambia”

    “Basi tuagane uende zako na mimi niende zangu”

    “Mimi nashukuru tu kukutana na wewe”

    Huku tabasamu likiendelea kutawala usoni kwake akaniambia.

    “Asante”

    Akanyanyuka.

    “Kwaheri” akaniaga na kuondoka.

    Nikiwa bado nimekaa nilimtazama wakati akienda zake. Alivuka viti kadhaa kabla ya kutokea kwenye njia iliyokuwa ndani ya bustani. Kulikuwa na vijana wawili waliokuwa wamekaa katika kiti kimoja nyuma yetu. Walikuwa na baskeli waliyokuwa wameiegesha mbele ya kiti walichokuwa wamekaa.

    Walipomuona yule msichana Zena anaondoka waliinuka wakapakiana kwenye baskeli na kumfuata.

    Wakati wanampita, yule kijana aliyekuwa amepakiwa nyuma aliuvuta mkoba wa Zena akauchomoa na kuuchukua. Zena alipogutuka vijana hao walimpita na baskeli na kukimbia.

    Zena akabaki amesimama akiwatazama vijana hao kwa hasira. Mkoba wake ulikuwa umekwenda!

    Nikanyanyuka kwenye kiti na kumfuata haraka. Wale vijana walikuwa wameshafika barabarani wakaelekea upande wa Chumbageni kwa mwendo wa kasi.

    “Wamepora mkoba wako?” nikamuuliza.

    “Basi waache tu, huwezi kuwafanya kitu” Zena alisema. Sauti yake ilikuwa tulivu lakini ilionesha ghadhabu.

    “Wale vijana walikuwa wamekaa muda mrefu nyuma yetu, kumbe walikuwa na lao wanalongojea”

    “Hakuna tatizo”

    Nilikuwa nafuatana naye kuelekea kwenye lango la kutokea kwenye bustani hiyo.

    “Dah!....”

    “Usijali, waache tu. Mimi nakwenda zangu”

    Ile teksi iliyomleta Zena ikatokea tena na kusimama mahali pale pale pa mwanzo.

    Zena akaifuata na kujipakia. Teksi ikaondoka. Niliisindikiza kwa macho hadi ilipokata kona.

    “Majini pia wanapanda teksi!” nikajisemea moyoni mwangu kisha nikaanza kutembea kwa miguu kurudi nyumbani.



    Kile kitendo cha wale vijana kilikuwa kimefadhaisha akili yangu.

    Sikurudi nyumbani moja kwa moja, nilikwenda nyumbani kwa kaka. Aliponiona tu akaniuliza.

    “Ulifika huko Uhuru Park?”

    “Nimefika na nimekutana naye”

    “Enhe amekueleza nini?”

    “Kwanza amenirudishia hiki kitabu changu nilichokuwa nimemuazima siku ile kisha akaniomba msamaha kwa usumbufu wowote ambao niliupata kutokana na yeye”

    “Enhe…?”

    “Baada ya hapo akanithibitishia

    mwenyewe kwamba yeye ni jinni. Akaniambia kwamba nisimuogope kwani hatakuwa na madhara na mimi. Lakini la msingi aliloniambia ni kuwa anataka niwe mume wake…”

    “Mume wake kivipi?”

    “Nafikiri anataka tuoane”

    “Eh…utamuweza kweli mke wa kijini? Kumbe ana makubwa!”

    “Nimemuuliza kwani majini wanaoana na binaadamu? Akaniambia niende nikamuulize bibi mzaa baba, eti baba yangu baada ya kumuacha yeye alioa mke gani?”

    “Alikuwa na maana gani?”

    “Ameniambia nikamuulize tu halafu nije nimpe jibu”

    “Kumbe anamjua pia bibi yetu?”

    “Ameniambia amekuwa na mimi tangu nikiwa mdogo lakini hakuwa amejitokeza, kwa hiyo familia yetu atakuwa anaijua”

    “Itakubidi hayo maneno ukamueleze mama”

    “Nitakwenda kumueleza”

    “Twende kwake sasa hivi”

    Tukatoka na kaka kwenda nyumbani kwa mama. Tulienda kwa miguu. Njiani tulikuwa tukiendelea kuzungumza.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ameniambia kama nitaoana naye atanipa utajiri”

    “Hilo si tatizo, tatizo ni kuwa na mke jini” Kaka akaniambia.

    Nikajua suala hilo lilikuwa limemshitua na yeye.

    Tulipofika nyumbani kwa mama, nikamueleza mazungumzo yote tuliyozungumza na Zena. Mama naye akashituka.

    “Hebu nenda ukamuulize bibi yako kuhusu huyo babu yako usikie atakueleza nini lakini nakushauri usikubali kuoana na huyo mwanamke hata kama atakupa utajiri” Mama akaniambia.

    “Mimi sijakubali, bado niko kwenye utafiti”

    “Wewe ni binaadamu huwezi kuishi na mwanamke ambaye ni jini” Mama aliendelea kunisisitizia.

    “Nitazingatia ushauri wako na nitakwenda kwa bibi hapo kesho” nikamwambia.

    Bibi mwenyewe alikuwa akiishi Mwambani, mwendo wa kama kilometa kumi kutoka Tanga mjini. Kitongoji hicho kipo upande wa Kaskazini mwa jiji la Tanga katika barabara inayoelekea wilaya ya Pangani.

    Siku ya pili yake nikaenda huko Mwambani kwa kutumia pikipiki yangu. Nilipofika nilimkuta bibi yuko barazani mwa nyumba yake akisuka ukili wake. Ingawa alikuwa kikongwe sana lakini bado alikuwa akijiweza kiasi kwamba alikuwa anaweza kusuka ukili wake.

    Nilikuwa nimemnunulia kilo tano za sukari, nikampa.

    Baada ya kuulizana hali nilimwambia licha ya kwenda kumsalimia pia nilikuwa na shida yangu.

    “Shida gani?” akaniuliza.

    “Nilikuwa nataka kujua eti baada ya wewe kuachana na marehemu mume wako yaani babu yangu, babu alioa mke mwingine?”

    “Ndio alioa”

    “Enhe niambie alimuoa nani?”

    “Inasemekana alioa mke wa kijini, alikuwa akiitwa Zena na huyo Zena ndiye aliyefanya babu yako aniache mimi. Lakini mimi sikuwahi kumuona”

    Nikashituka niliposikia maneno yale.

    “Alimpata wapi huyo mke wa kijini?” nikamuuliza.

    “Alimchunuka tu akamwambia aniache mimi amuoe yeye. Babu yako akakubali kuniacha kwa ajili ya kupata utajiri”

    “Na ni kweli alipata utajiri?”

    “Alipata utajiri mkubwa sana lakini siku chache kabla ya kufa kwake utajiri wote ulipotoea na huyo mke wake alitoweka pia”

    “Wakati huo alikuwa umeshamzaa baba?”

    “Baba yako alikuwa ameshazaliwa pamoja na kaka yake Abdul yaani baba yako mkubwa ambaye alifariki nchi za nje”

    “Sasa baada ya babu kuoa mke wa kijini, nani aliwalea kina baba?”

    “Aliniachia nao mimi, nikawalea hadi wakawa wakubwa”

    Nikanyamaza kimya nikijiuliza kama Zena anayemsema bibi ndiye yule anayetaka nioane naye.

    “Kwanini umeniuliza hivyo?” Bibi aliniuliza na kunizindua.

    “Nimekuuliza tu bibi, kuna mzee mmoja alikuwa akifahamiana na marehemu babu, alinieleza kuhusu kisa hicho ndio nikaona nije nikuulize” nikamdanganya bibi. Sikutaka kumueleza ukweli kwamba kuna mwanamke wa kijini alinituma nimuulize.

    “Ulikuwa huamini?”

    “Nilikuwa siamini lakini baada ya wewe kunithibitishia sasa ninaamini”

    “Wakati babu yako anakufa, watu walishangaa kuona mali yote aliyokuwa nayo imepotea. Na yule mke wake naye hakuonekana tena. Alitoweka wiki moja kabla ya kifo cha babu yako”

    “Na huyo babu na mke wake walikuwa wakiishi maisha ya aina gani?”

    “Waliishi maisha ya kawaida tu lakini mke wake alikuwa hajitokezi katika shughuli za watu”

    “Babu alipokuacha uliona uchungu sana bibi?”

    “Kwa kweli niliumia sana kwa sababu sikuwa nimemtenda kosa lolote na bado nilikuwa nampenda babu yako”

    “Pole sana bibi”

    “Oh! Wanipa pole leo wakati mambo yameshapita zamani!”

    “Lakini bibi uliona babu alifanya jambo la busara kuoa mwanamke wa kijini?”

    “Alilazimishwa na yule jini na aliahidiwa kupata utajiri. Kuna mganga mmoja aliniambia kama babu yako asingeniacha yule jini angeniua”

    “Eh kumbe ni viumbe hatari kiasi hicho!”

    “Ndivyo nilivyoambiwa, sijui kama ningeuliwa kweli”

    Pakapita ukimya wa sekunde kadhaa. Bibi alikuwa akiendelea kusuka ukili wake na mimi nilikuwa nikiumiza kichwa kwa kuwaza. Hatimaye nikauondoa ule ukimya.

    “Kwa mfano mimi nikipata mke wa kijini, unanishaurije nioane naye?” nikamuuliza.

    Bibi akacheka.

    “Bibi mbona unanicheka?”

    “Unanichekesha. Huyo mke wa kijini utampata wapi?”

    “Kwani babu alimpata wapi?”

    “Yule ni mpaka akuchunuke mwenyewe”

    “Sawa. Je akinichunuka na kuniambia anataka tuoane, nikubaliane naye?”

    “Hayo ni mawazo yako sasa, mimi nikushauri nini?”

    “Unaweza kunishauri kwamba nioane naye au la”

    “Hilo sio jambo la kushauriwa, ni uamuzi wako na huyo jini kama utampata. Kwani na wewe unataka kupata utajiri?”

    “Hakuna asiyetaka utajiri bibi”

    “Angalia sana, utajiri mwingine una matatizo. Ni bora uishi masikini hivyo hivyo”

    Baada ya kimya kingine kifupi nikamuaga bibi. Wakati nataka kuondoka nikampa shilingi elfu ishirini. Bibi akanishukuru.

    “Haya bibi nakwenda” nikamuaga bibi na kupanda pikipiki yangu.

    “Uende salama, nisalimie wenzako”

    “Nitakusalimia”



    Nikawasha pikipiki yangu na kuondoka. Wakati narudi mjini mawazo yalikuwa yamesonga katika kichwa changu kuhusu yale maneno aliyonieleza bibi.

    Sikuwa nikijua kama babu yangu alimuacha mke wake na kuoa mke wa kijini. Kwa vile babu mwenyewe alikufa zamani habari zake zilikuwa zimeshahaulika.

    Lakini nilijiuliza Zena alijuaje habari ile? Nikawa na shaka sana kwamba huyo Zena aliyetajwa na bibi ndiye Zena yule yule.

    Nikakumbuka kwamba aliniambia alikuwa na mimi kwa miaka mingi isipokuwa hakuwa amejitokeza kwangu hivyo nilikuwa sijui kama nina jini aliyenichunuka.

    Pamoja na kufahamu ukweli wote huo bado nilikuwa na mtihani mgumu mbele yangu, mtihani wa kukubali kuoana na Zena kama alivyoniambia au kumkataa.

    Mpaka muda ule naondoka kwa bibi sikuwa na uamuzi wowote. Nilitegemea kupata ushauri kwa kaka yangu na kwa mama yangu.

    Nilikwenda moja kwa moja nyumbani kwa kaka. Nikamwambia.

    “Ninatoka Mwambani kwa bibi”

    “Umezungumza naye?” akaniuliza kwa shauku.

    “Nimezungumza naye na anawasalimia”

    “Amekuelezaje kuhusu madai ya babu kuoa mke wa kijini?”

    “Amesema ni kweli, babu alioa mke wa kijini baada ya kumuacha yeye”

    Kaka akashituka.

    “Kumbe babu alioa mke wa kijini!”

    “Tena alikuwa anaitwa Zena, jina lile lile la huyu anayenifuata mimi”

    Kaka alikuwa amepigwa na butwaa.

    Nikamueleza kwa kirefu maelezo ya bibi ambayo yalimshangaza sana.

    “Isije kuwa jini huyo ndiye huyu huyu amejitokeza tena”

    “Hata mimi nimekuwa nikijiuliza swali hilo hilo”

    “Huyo bibi alikwambia aliwahi kumuona?’

    “Ameniambia hakuwahi kumuona”

    “Mimi nadhani jini mwenyewe ndiye huyo huyo, amejitokeza kwako”

    “Inawezekana lakini nitakuja kumuuliza tupate uhakika”

    “Sasa umeamua nini?”

    “Bado ninakabiliwa na maswali mengi. Ninahitaji ushauri wenu ili niweze kuamua”

    “Nenda nyumbani umueleze mama, usikilize atakwambia nini”

    “Kwa upande wako unanishauri nini?”

    “Hili ni suala la kujadiliana sote kwa pamoja lakini kwanza nenda kamueleze mama tusikie kauli yake”

    “Sawa. Nitakwenda kumueleza mama”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Baada ya kuzungumza kirefu na kaka nikaondoka nyumbani kwake na kwenda nyumbani kwa mama.

    Wakati nafika nyumbani, mama alikuwa amelala. Mjukuu wake alikwenda kumuamsha chumbani. Alipoamka akaja sebuleni.

    “Shikamoo” nikamwamkia.

    “Marahaba. Habari za huko?” Mama akaniuliza.

    “Huko ni kwema. Natoka Mwambani kwa bibi?”

    “Ndio ulikwenda kumuuliza kuhusu babu yako?”

    “Nimemuuliza ameniambia kwamba babu yetu alimuacha yeye akaoa mke wa kijini”

    “Unaniambia ukweli mwanangu?” Mama akaniuliza kwa mshituko.

    “Ameniambia bibi mwenyewe”

    “Kumbe babu yako alioa mke wa kijini?”

    “Alioa, na bibi anasema waliishi pamoja hadi babu alipofikiwa na umauti, yaani wiki moja kabla ya babu kufariki jini huyo alitoweka”

    “Kama ni hivyo inaelekea babu yenu alikuwa mtu hatari sana!”

    “Bibi ameniambia babu alipomuoa jini huyo alipata utajiri mkubwa, yaani yule jini alimpa utajiri lakini alipokufa utajiri wake ukapotea”

    “Hata kama alipata utajiri, si jambo la kukubaliana nalo kirahisi”

    “Sasa kitu ambacho kimenitisha ni kuwa huyo jini alikuwa anaitwa Zena kama jini huyu anayenifuata mimi!”

    “Isije kuwa ndiye jini huyo huyo. Kwanini alikuwambia uende ukamuulize bibi yako”

    “Inawezekana ndiye jini huyo huyo”

    “Sasa sikiliza mwanangu, huyo jini epukana naye mara moja!”

    “Kwanini mama?”

    “Atakuharibia maisha yako, kama ni kuoa oa binaadamu mwenzako si jini”

    “Kwa hiyo unanishauri hivyo?”

    “Inawezekana ni ushauri au ni amri yangu na naomba unisikilize”

    “Sawa, nitakusikiliza. Nilitaka tu nijue una maoni gani”

    “Atakapokufuata tena mwambie mimi siwezi kukuoa wewe, nitaoa binaadamu mwenzangu. Kwani majini madume hakuna mpaka akufuate wewe!”

    “Ndio nashangaa!”

    “Huyo mke wa kijini kweli utamuonesha kwa wa watu, uwambie mke wangu huyu!”

    “Hiwezekani”

    “Kwanza watu watakushangaa na hawatakuja kwako. Mimi pia sitakuja”

    Mama alikuwa amekasirika, sikutaka tena kumjibu kitu. Nikanyamaza kimya.

    “Upuuzi mtupu! Amekutia katika misuko suko chungu nzima halafu uje uishi naye kama mke wako, kwanza hao watoto mtakaozaa watakuwa ni watoto wa aina gani...epukama na huyo shetani asikuletee mikosi. Kama ndiye huyo aliyeolewa na babu yako atokomee huko huko alikokuwa. Mimi simtaki!” Mama aliendelea kuniambia kwa hasira.

    “Sawa mama nimekusikia”

    Nilipoondoka kwa mama nikarudi nyumbani kwangu. Kusema kweli nilikuwa na mawazo mengi sana. Maneno ya mama yalikuwa yameingia akilini mwangu na wakati huo huo nilikuwa nafikiria endapo nitamueleza yule jini kwamba siwezi kuoana naye atanifanya nini.

    Wakati naendelea kutafakari nikasikia mlango wangu wa mbele unabishwa. Nikanyanyuka na kwenda kuufungua.

    Nilimuona mzee mmoja aliyekuwa amevaa koti jeusi na kanzu ya darizi pamoja na baraghashia. Nikamuamkia.

    “Shikamoo mzee?”

    “Marahaba, waonaje hali yako?”

    “Nzuri, karibu”

    “Asante. Nadhani hunifahamu?” akaniuliza.

    “Ndiyo sikufahamu mzee wangu”

    “Ninaishi mtaa wa pili. Kuna mwanangu mmoja ndiye aliyenielekeza hapa kwako”

    “Una tatizo gani?” nikamuuliza kistaarabu.

    “Unakumbuka jana majira ya saa nne asubuhi mpaka tano ulikuwa wapi?”

    “Nilikuwa maeneo ya mjini”

    “Bila shaka ulikuwa umekaa katika Bustani ya Uhuru na msichana mmoja?”

    “Ndio nilikuwa nimekaa hapo”

    “Nimeambiwa kwamba wakati yule msichana uliyekuwa naye anaondoka, kuna vijana wawili waliokuwa na baiskeli walimpora yule msichana mkoba wake na kukimbia nao, ni kweli?’

    “Ni kweli’

    “Yule mzee alinyamaza kimya akitafakari kwa sekunde zisizopungua tano kisha akaniuliza.

    “Huyo msichana ni nani wako?”

    “Tunafahamiana tu, tulikuwa tumekaa tunazungumza”

    “Sasa nataka kukueleza kitu kimoja. Mmoja wa wale vijana waliompora huyo msichana ni mwanangu. Jana usiku aliporudi nyumbani hatukulala”

    “Kwanini?”

    “Yule kijana alipoingia chumbani mwake tulisikia anapiga kelele. Mimi nikaenda kumuuliza ana matatizo gani, akaniambia kwamba kila anapopitiwa na usingizi anamuona mwanamke anampiga bakora. Nikamuuliza ni mwanamke gani huyo, ndio akanieleza kwamba kuna mwanamke walimpora mkoba wake na ndiye huyo anayemuona anampiga bakora.

    “Hiyo hali iliendelea hadi asubuhi, kila akifumba macho tu anamuona, anamtandika. Bakora zimeota mgongoni mwake. Huyo mwanamke haonekani, anamuona yeye tu pale anapolala.

    “Hii asubuhi tukaenda kwa huyo mwenzake, kumbe na yeye hali ni hiyo hiyo. Amepigwa bakora usiku kucha. Bakora zimeota kwenye mgongo wake. Kwa kweli nimewagombesha sana wale vijana kwa kututia aibu sisi wazazi wao kwa kujihusisha na vitendo vya kihalifu wakiwa bado wadogo, kuibia watu, kupiga watu na kuvuta bangi. Imebidi niwaulize ni mwanamke gani huyo waliyempora mkoba wake ndipo mwanangu aliponielekeza kwako. Kumbe alikuwa anakufahamu.

    “Sasa mwanangu nimekuja, nakuomba unioneshe yule mwanamke nimlipe ule mkoba wake na nimuombe radhi ili wale vijana waondokewe na ile hali”

    Yale maneno aliyonieleza yule mzee yalinishangaza na kunishitua. Wakati yule mzee ananieleza mimi nilikuwa natokwa na jasho.

    “Kwani mpaka hii asubuhi wanaendelea kuchapwa bakora?’ nikamuuliza.

    “Labda wakae bila kusinzia au kulala. Wanapolala kidogo tu tayari wanapiga kelele wanasema wanachapwa. Ni mpaka hii asubuhi hawajalala tangu jana wako macho tu. Wameshadhoofika. Kama hii hali itaendelea watakufa”

    “Mzee wangu nikwambie ukweli, yule mwanamke tulikutana pale pale. Sijui anapoishi na sidhani kama nitamuona tena”



    Mzee akashituka na kujishika kichwa.

    “Mimi nilidhani unajuana na huyo mwanamke. Basi wale vijana hawatakuwa na maisha tena” Mzee akasema kisha akaniuliza.

    “Unasema kweli, hujuani naye kabisa?’

    “Sijuani naye mzee wangu, siwezi kukudanganya. Tulikutana pale pale, kila mmoja alikuja kivyake na aliondoka kivyake’

    Mzee aliduwaa kwa sekunde zisizopungua kumi, alipozinduka aliniuliza.

    “Hivi mwanangu utanisaidiaje na balaa hili?”

    “Mzee wangu sina namna yoyote ya kukusaidia”

    “Tuseme yule mwanamke alikwenda kwa mganga kuwaroga wale vijana?”

    “Kwa waswahili hilo jambo linawezekana lakini siwezi kujua”

    “Sasa nifanyeje?”

    Sikumjibu yule mzee. Alionesha wazi alikuwa amechanganykiwa. Alipoona nipo kimya, aligeuka bila kuniaga na kushuka kwenye baraza ya nyumba yangu. Nikamsikia akisema peke yake.

    “Kama hawatakoma, hawatakoma tena!”

    Alipofika chini ya baraza ndipo alipokumbuka kuniaga.

    “Haya kwaheri mwanangu” akaniambia.

    Nilimuangalia yule mzee hadi alipokata kona mtaa wa pili, lakini mawazo yangu yalikuwa kwa Zena. Kitendo kile cha kuwatandika wale vijana bakora kilionesha kuwa mwanamke yule wa kijini alikuwa wa hatari.

    Nilikumbuka wakati wale vijana wamempora mkoba wake alionekana mtulivu ingawa alionesha kuwa na hasira. Aliniambia “Waache tu” kumbe alikuwa na lake alilokuwa amelipanga.

    Japokuwa niliwahurumia hao vijana lakini sikujua ningempata wapi huyo Zena ili nimwambie awasamehe hao vijana. Na hata kama ningekutana naye na kumwambia hivyo sikudhani kama angenisikia.

    Nilirudi ndani na kuendelea kujiwazia. Nilihisi kwamba hata mimi maisha yangu yangeweza kuwa katika hatari kama nitakataa kumuoa Zena na kwa kweli hata hapo nitakapokutana naye nitashindwa kumueleza ukweli kwamba sikubaliani na matakwa yake ya kumuoa.

    Kwa vyovyote vile yule mwanamke anaweza kunidhuru!

    Nilipowaza hivyo nilitoka tena. Nikafunga mlango wangu na kuondoka na pikipiki yangu, nikaenda nyumbani kwa mama.

    Kitendo cha kurudi tena kwa mama kilimshitua, akaniuliza.

    “Kulikoni?”

    “Nimerudi tena” nikamwambia.

    “Ndio mana nimekuuliza kulikoni?”

    Nikamueleza mama kile kisa cha yule jini kuwatandika bakora wale vijana waliomuibia mkoba wake.

    “Baba wa mmoja wa wale vijana ameniambia hao vijana hivi sasa wako taabani wanamtafuta yule msichana wamuombe msamaha” nikamwambia.

    Mama naye alishituka.

    “Yaani wanapolala ndio wanamuona huyo msichana anawatandika bakora?”

    “Ndio mama, na inakuwa usiku kucha na mchana kutwa. Miili ya wale vijana imeota makora migongoni”

    “Huyo jini ni mbaya sana”

    “Sasa nimefikiri hata mimi anaweza kuja kuniletea madhara kama nitakataa kumuoa”

    “Ni kweli, sasa nikupeleke kwa mganga”

    “Wapi?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kule Mnyanjani, ni hodari sana kwa majini”

    “Ndio maana nimekuja ili tushauriane kwenda kwa huyo mganga, vinginevyo naweza kupata balaa”

    “Sasa nikupeleke lini?”

    “Leo, twende leo”

    “Saa ngapi?’

    “Maliza kazi zako nitakufuata saa tisa twende”

    “Sawa. Basi njoo hapo saa tisa twende”

    Tulipokubaliana na mama nikaondoka. Wakati nafika nyumbani kwangu nikakutana na yule mzee akiondoka.

    “Nimegonga mlango, nimeona kimya. Nilikuwa naenda zangu” akaniambia.

    “Nilitoka kidogo”

    “Nimekuja kukujulisha kuwa yule mwanangu ameshafariki dunia”

    Nikashituka.

    “Eh ameshafariki!”

    “Amefariki kama nusu saa hivi iliyopita akiwa kwa mganga. Tulikuwa tumempeleka kwa mganga baada ya mateso kumzidia”

    “Poleni sana jamani. Yule mwenzake naye anaendeleaje?’

    “Sijapata habari zake. Nimekuja kukwambia hivyo, kwaheri mwanangu”

    Mzee huyo akaondoka. Nilipata hofu sana. Sikuweza hata kuingia ndani. Niliona kama vile nitakutana na jini huyo, nikageuza pikipiki na kurudi kwa mama.

    Nilipofika nilimuhadithia lile tukio la kufa kwa mmoja wa wale vijana.

    “Nimekuja nikusubri hapa hapa, sikuingia hata nyumbani kwangu” nikamwambia.

    Chakula cha mchana nilikula pale pale kwa mama. Baada ya kula ndipo tulipoondoka. Nilimpakia mama kwenye pikipiki tukaelekea huko Mnyanjani.

    Wakati huo eneo hilo la Mnyanjani lilikuwa kama kitongoji cha mji huo. Likiwa karibu na ufukwe wa Bahari ya Hindi, lilikuwa moja ya maeneo ya kiasili ya mji wa Tanga yenye historia iliyosheheni utamaduni wa jiji hilo.

    Eneo hilo hivi sasa limebadilika na kuwa na nyumba za kisasa na kuwa sehemu ya jiji hilo.

    Ili ufike Mnyanjani unapita vitongoji kadhaa pamoja na viunga vya minazi. Ni mwendo wa karibu kilometa kumi.

    Mama alinionesha nyumba ya mganga huyo iliyokuwa imejengwa kwa miti na udongo na kuezekwa makuti ya minazi.

    Tukasimama na kubisha mlango.

    “Karibuni” tukasikia sauti ya kiume ikitukaribisha.

    Tukaingia ndani. Ukumbi ulikuwa giza. Kulikuwa na mwanga hafifu uliotokea kwenye mlango wa nje na wa uani.

    Mganga mwenyewe alikuwa amekaa kwenye jamvi lililokuwa limetandikwa pale ukumbini. Alikuwa akikatakata mizizi ya dawa.

    “Karibuni” akatuambia tena huku akitutazama.

    “Tumeshakaribia” mama akamwambia na kisha kumuuliza hali.

    Mimi nikamuamkia. “Shikamoo”

    “Marahaba. Karibuni mkake kwenye jamvi”

    Tukakaa kwenye jamvi.

    “Tumekuja tuna shida” Mama akaanza kumwambia mzee huyo aliyekuwa amevaa kikoi cha rangi nyeupe.

    “Shida gani?”



    Mama akamueleza mkasa mzima. Yule mganga naye alishangaa akasema.

    “Huyo atakuwa Ummi Subian au Kamari wa Subian”

    “Tunataka aondoke kwa mwanangu, asimfuate fuate tena”

    “Ngoja nimtazame nijue ni jini gani”

    Mganga akachukua kitabu akakifungua kisha akatazama saa yake.

    “Ni saa nane sasa” alisema peke yake kisha akatazama kwenye kitabu.

    “Aliyetawala muda huu ni Zuhra Kadhi Lhawaiju” Mganga aliendelea kujisemea kisha akatutazama.

    “Huyu mwanamke wa kijini ni ruhani aliyechanganya na usubian”

    “Yeye mwenyewe pia aliniambia hivyo hivyo” nikamkubalia mganga huyo.

    “Hawa majini ni ving’ang’anizi sana na ni wabishi, akitaka jambo lake ni mpaka alitimize”

    “Lakini ataweza kumuacha huyu mwanangu?” Mama akamuuliza kwa wasiwasi.

    “Ni kazi kubwa. Huyu jini ni wa kurithi, zamani aliwahi kuwa na babu yake huyu kijana”

    “Ni kweli, bibi yangu alinieleza leo” nikamwambia mganga huyo.

    “Alikuelezaje?”

    “Aliniambia kuwa babu yangu alikuwa na mke wa kijini, anaitwa Zena”

    Mganga akamtazama mama.

    “Unasikia. Sasa kumtoa jini wa aina hii inataka kazi kubwa, si kazi ndogo”

    “Sasa tufanyeje?” Mama akamuuliza.

    “Nitahitaji mbuzi watatu, wa rangi nyeupe, rangi nyeusi na rangi mchanganyiko” Mganga alituambia kisha akatuuliza.

    “Mtaweza kuwapata?”

    “Watapatikana” nikajibu mimi.

    “Mbali na hao mbuzi watatu, mnipatie maji ya bahari lita tatu, mchanga wa pwani unaofikia kilo moja na kipande cha mti kilichotoka katika eneo lililopiganwa vita”

    “Hicho kipande cha mti tutakipata wapi?” nikamuuliza.

    “Najua hiki kitawapa tabu, nitawapatia mimi”

    “Huo mchanga wa pwani na maji ya bahari pia ungetusaidia wewe, tunaona hapa ni karibu na bahari”

    “Gharama yake itakuwa shilingi elfu kumi na tano”

    “Sawa.Tutatoa”

    “Hao mbuzi watatu pia mnaweza kuwapata hapa hapa kama mtataka”

    “Watakuwa kiasi gani?”

    “Kila mbuzi mmoja ni shilingi elfu arobaini”

    “Kwa hiyo kwa mbuzi watatu itakuwa shilingi laki moja na ishirini elfu”

    “Ingiza na hizi elfu kumi na tano za vifaa”

    “Zitakuwa laki moja na hamsini na tano elfu”

    “Na kazi yangu shilingi laki moja”

    “Jumla laki mbili na hamsini na tano elfu”

    “Hizo pesa zikipatikana, njooni niwafanyie kazi yenu”

    “Pesa zipo lakini zipo nyumbani, labda utupe muda nikazichukue” nikamwambia mganga huyo.

    “Hizo pesa nikizipata leo, kwanza nitashughulikia kupata hivyo vitu, Kesho saa mbili asubuhi ndio nitakushughulikia wewe mwenyewe”

    “Sawa. Sasa acha turudi. Baadaye nitakuja na hizo pesa.

    Baada ya kukubaliana na mganga huyo tuliondoka. Nilimpakia mama kwenye pikipiki nikamrudisha nyumbani kwake kisha mimi nikaenda nyumbani kwangu kuchukua hizo pesa. Zilikuwa ni pesa zile zile alizonipa Zena.

    Nilitia mfukoni shilingi laki tatu nikaondoka tena na pikipiki kwenda Mnyanjani. Nilipofika nilimpa yule mganga shilingi laki mbili na hamsini na tano elfu.

    “Sasa nenda, uje kesho saa mbili asubuhi, utakuta kila kitu kipo tayari” Mganga akaniambia.

    “Sasa nilikuwa na ombi moja” nikamwambia.

    “Ndio”

    “Nina wasiwasi huyo jini anaweza kunifuata hii leo kutokana na hivi ambavyo nataka kumshughulikia, sasa itakuwaje?

    “Nitakupa hirizi, kuwa nayo mfukoni hadi hapo kesho”

    “Nikiwa na hiyo hirizi hatanifuata?’

    “Abadani. Hawezi kukufuata”

    “Basi nipatie hiyo hirizi’

    Hirizi yenyewe ilikuwa imeshatayarishwa tayari. Mganga akanipatia. Nikaichukua na kuitia mfukoni.

    Nikatoka na kupanda pikipiki yangu. Sasa kidogo moyo wangu ulikuwa na matumaini. Ile hofu niliyokuwa nayo ya kukutana na Zena ilikuwa imenitoka.

    Wakati nakaribia kulitoka eneo la Mnyanjani, niliona mtu amesiamama pembeni mwa barabara chini ya mti wa mwembe. Nilipoukaribia mwembe huo nilishituka nilipoona mtu mwenyewe alikuwa Zena. Alikuwa amesimama kama aliyekuwa akisubiri mtu.

    Nikaongeza mwendo ili kumkwepa na nikajifanya sikumuona. Wakati pikipiki imeshika kasi nikahisi kama kulikuwa na kitu nyuma yangu. Nikageuza uso wangu kutazama nyuma. Nilishituka tena. Alikuwa ni Zena aliyekuwa amekaa kwenye siti ya nyuma ya pikipiki yangu!

    Sikuweza kujua alipakiaje kwenye pikipiki yangu wakati alikuwa amesimama kwenye mti ambao nilikwishaupita, tena nikienda kwa kasi. Kutokana na mshituko nilioupata mikono yangu ilitetereka nikajikuta ninaanguka na pikipiki. Mimi na Zena tukawa chini!

    Nikainuka haraka. Lakini Zena alikuwa mwepesi zaidi. Nilimkuta tayari ameshasimama.



    “Inua pikipiki yako” akaniambia.

    Nikiwa nimetahayari nikaushika usukani wa pikipiki na kuiinua.

    “Isimamishe” akaniambia tena.

    Nikaiwekea standa.

    “Unatoka wapi?”

    “Mimi?’

    “Jamani kwani nazungumza na nani?”

    “Natoka kule…”

    “Wapi?”

    “Mnyanjani”

    “Kufanya nini?”

    Nikatunga uongo.

    “Kumsalimia mjomba wangu”

    Zena akanitazama kwa karibu nusu dakika bila kuniambia chochote. Bila shaka aligundua kuwa nilikuwa namdanganya. Wakati Zena akinitazama jasho jembamba lilikuwa linanitoka. Nilikuwa nikilihsi likitiririka kwenye uti wa mgongo wangu.

    Nilikuwa najiuliza yule mganga alinipa hirizi akaniambia nikiwa nayo mfukoni Zena hatanifuata, mbona niko naye hapa?

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Humo mfukoni umetia nini?” Sauti ya Zena ikanishitua.

    Alikuwa akiutazama mfuko wa suruali yangu ambao nilitia ile hirizi.

    “Wapi?” nikamuuliza tena nikijifanya sikumuelewa.

    “Nimekuuliza humo mfukoni mwako umetia nini?” Zena akaniuliza tena sasa kwa sauti ya ukali kidogo.

    “Sijatia kitu, ni pesa zangu tu” nikamjibu.

    “Hebu tia mkono wako mfukoni” akaniambia.

    Nikatia mkono kwenye mfuko mwingine.

    “Sio huo, tia kwenye mfuko huu”

    Zena alinionesha mfuko huo kwa kidole chake.

    Nikatia mkono kwenye mfuko huo.

    “Hebu toa hicho kitu ulichokigusa”

    Bila kupenda niliitoa ile hirizi.

    “Hebu nioneshe”

    Nikamuonesha, hata haikumshtua.

    Akaishika na kuiweka kwenye kiganja chake kisha akanitazama.

    “Nini hii?’ akaniuliza kwa dharau.

    Sikumjibu. Nilikuwa nimefadhaika sana.

    “Wewe unajidanganya sana, sikujua kama unaweza kuwa mpumbavu kiasi hicho. Shika hirizi yako” akaniambia.

    Nikaichukua ile hirizi.

    “Itupe kule!” akaniambia akinionesha kitu kilichokuwa kando yetu.

    Nikaitupa. Ningefanyaje? Sikuwa na la kufanya. Hirizi yenyewe haikumtisha hata kidogo. Bora kuitupa tu.

    “Nipakie twende zetu” akaniambia akiwa ameridhika kwa kile kitendo cha kuitupa ile hirizi.

    Sikutaka hata kumuuliza twende wapi, nikawasha pikipiki iliyokuwa imezimika kisha nikaipanda. Zena akakaa nyuma yangu. Nikatia gea na kuondoka.

    Nilikuwa naendesha pikipiki huku natetemeka mpaka Zena akaniuliza.

    “Unatetemeka nini?”

    “Sitetemeki” nikamjibu huku nikijua kuwa nilikuwa natetemeka.

    Akanyamaza kimya. Hakunisemesha kitu mpaka tulipoingia mjini.

    “Nishushe hapa” akaniambia mara tu tulipoipita hospitali ya Makorora.

    Nikashukuru kusikia kauli hiyo. Nilikuwa nikihisi kama nimepakia chatu nyuma yangu. Nikaisimamisha pikipiki haraka na kushusha mguu wangu.

    Zena akashuka.

    “Niache hapa hapa. Wewe nenda zako” akaniambia.

    Ingawa sauti yake ilikuwa tulivu lakini uso wake ulikuwa umekasirika. Nikamuona anavuka barabara na kuelekea upande wa hospitali ya Makorora.

    Nikatia gea na kuiondoa pikipiki yangu taratibu. Sikutazama nyuma tena. Nilipofika kwenye mzunguko wa barabara ya Pangani nilikata kulia nikaelekea nyumbani kwa mama. Sikutaka kwenda nyumbani kwangu ingawa palikuwa karibu na hapo.

    Nilipofika nyumbani kwa mama nikamueleza tukio zima lililokuwa limenitokea. Mama akashituka.

    “Sasa huyo shetani amekwenda wapi?” akaniuliza.

    “Sijui amekwenda wapi. Nimemuacha karibu na hospitali ya Makorora”

    “Ina maana alikufutilia kule kwa mganga”

    “Nafikiri. Amejua kuwa nimepewa hirizi na akaona iko mfukoni mwangu”

    “Sasa itakuwaje?”

    “Hata sijui. Hapa mwili wote unanitetemeka”

    “Sasa ungerudi umueleze yule mganga”

    “Unanishuri nirudi tena kwa yule mganga?”

    “Ndio. Umueleze habari yote. Yeye ndio atajua la kufanya”

    “Sasa twende sote. Yule jini asije akanifuata tena”

    “Ngoja twende”

    Dakika chache baadaye mimi na mama yangu tukawa kwenye pikipiki tukielekea Mnyanjani kwa yule mganga. Tulipofika pale mahali nilipoanguka na pikipiki nilimuonesha mama.

    “Mahali tulipoanguka ni hapa” nikamwambia.

    “Na huyo jini mwenyewe ulimuona amesimama wapi?”

    “Alikuwa amesimama kwenye mti ule pale”

    Nikamuonesha mti wa mwembe nilipomuona Zena amesimama.

    “Inaonekana alikuwa akikufuatilia wewe” Mama akaniambia.

    Tulipofika nyumbani kwa mganga tulikuta vilio vimetawala ndani ya nyumba huku nyumba yenyewe imeja watu hadi nje.

    “Kuna nini?” nikamuuliza mama kabla ya kushuka kwenye pikipiki.

    “Ngoja tuulize” Mama akaniambia.

    Tulishuka kwenye pikipiki. Mtu mmoja alipotuona tulikuwa wageni akatufuata.

    “Karibuni” akatuambia.

    “Tumeshakaribia” Mama akamjibu.

    “Habari za hapa?” nikamuuliza.

    “Hapa si kwema, tumepata msiba” yule mtu akatuambia.

    “Msiba wa nani?”

    “Msiba wa huyu bwana aliyekuwa anaishi katika nyumba hii”

    Nikatazamana na mama yangu kisha nikaendelea kumuuliza yule mtu.

    “Sisi tunachojua ni kuwa mwenye nyumba hii ni yule mganga wa kienyeji”

    “Niye huyo huyo aliyefariki”

    Nikatazamana tena na mama yangu, sasa kwa mshituko.

    “Dakika chache tu zilizopita si nilikuwa naye hapa?” nikauliza.

    “Kufariki kwake kulikuwa kwa miujiza sana. Niliambiwa alikuwa akizungumza na mteja wake mmoja aliyefika na pikipiki, nafikiri ulikuwa wewe”

    “Nadhani nilikuwa mimi kwani si muda mrefu sana nilipoondoka hapa”

    “Basi mara tu ulipoondoka, yule mganga aliingia chumbani mwake. Mke wake alikuwa jikoni akasikia sauti ya mume wake akipiga kelele kuwa anakabwa na mwanamke. Mpaka mke wake anaingia chumbani alimkuta ameshakufa”

    “Nikaguna na kumtazama mama.

    “Mama umelisikia hilo tukio?”

    “Nimelisikia” Mama akajibu kwa sauti iliyonywea kisha akaniambia.

    “Basi twende zetu”

    “Nilikuwa nimempa pesa kwa ajili ya kunifanyia kazi yangu ambayo tulipatana aifanye kesho lakini nitamsamehe” nikasema.

    “Ulimpa kiasi gani?’ yule mtu akaniuliza.

    “Kama laki mbili hivi. Lakini nitasamehe”

    “Kama umeamua kuzisamehe ni jambo zuri”

    “Poleni sana kwa msiba huo” nikamwambia na kupanda kwenye pikipiki yangu.

    “Haya kwaheri baba” Mama akumuaga yule mtu kabla ya kukaa nyuma yangu. Tukaondoka.



    “Mama umeona mambo hayo!” nikamwambia mama wakati ninaendesha pikipiki kurudi mjini.

    “Nimeona. Kwa kweli ni kifo cha kushangaza sana”

    “Mimi nadhani ni yule jini amekuja kumuua yule mganga”

    “Itakuwa ndiye yeye, kwa sababu alisema kuna mwanamke anamkaba. Sasa alikuwa mwanamke yupi kama sio yule jini?”

    “Sasa haya yamekuwa mapambano!”

    “Tutatafuta mganga mwingine”

    “Sasa usalama wangu utakuwa wapi? Nimeshashuhudia watu wawili waliouawa leo. Yule kijana aliyekuwa anatandikwa na huyu mganga. Bado kuna na yule kijana mwingine. Naona pia atakuwa ameshakufa”

    “Tukifika tutakwenda kulizungumza vizuri hili suala pamona na kaka yako”

    “Sasa nimeshaona huyu mwanamke ni wa hatari”

    Nilimpeleka mama nyumbani kwake kisha nikaenda Chuda kumchukua kaka.

    Nilimueleza kwa kifupi hayo matukio.

    “Mama ameniambia nije nikuchkue twende tukayazungumze haya mambo”

    Ule muhutasari wa habari niliomueleza kaka tayari ulikuwa.

    Nikampakia kwenye pikipiki yangu tukaondoka.

    Tulipofika nyumbani kwa mama tukalizungumza lile suala ambalo kaka lilimshitua sana.

    “Kumbe yule jini ni hatari sana. Tulivyomuona pale mahakamani siku ile alionekana ni msichana mpole sana” Kaka akasema kwa mshangao.

    “Lile umbile ulilomuona nalo ni la kujipachika, si umbile lake halisi. Katika umbile lake halisi anatisha” nikamwambia kaka.

    “Kwa kweli inabidi muepukane haraka, sasa tutafanyaje wakati mtaalamu muliyemtegemea ndio ameuawa kwanza?”

    “Itakuja kuwa yeye!” Mama akamalizia akimaanisha mimi.

    “Sasa tufanyeje jamani, jua linakuchwa hili!” nikawahimiza wenzangu.

    “Hapa la kufanya ni kumuona mganga mwingine haraka iwezekanavyo” Kaka akashauri.

    “Bila kupata mganga mwingine, mimi leo sitalala, nina hofu” nikawambia.

    “Usijali, tutkwenda kwa mganga wa Amboni. Yeye pia namfahamu. Ni hodari” Mama akasema.

    “Sasa twende sasa hivi kwa sababu jua linakuchwa”

    “Ingekuwa kaka yako anapafahamu angekupeleka lakini itabidi nikupeleke mimi”

    “Mpeleke tu halafu mtakuja kunijulisha” Kaka akamwambia mama.

    Dakika chache baadaye tulikuwa tumetoka nje, nilimpakia mama kwenye pikipiki. Kaka yangu naye akaondoka kurudi kwake kwa miguu.

    Amboni ni kitongoji cha mji wa Tanga kinachokuwa kwa haraka. Kipo katika barabara ya Horohoro inayokwenda Mombasa nchini Kenya. Kutoka Tanga hadi Amboni ulikuwa mwendo upatao kilometa nane hivi.

    Kitongoji hicho kimepata umaarufu kutokana na mapango yaliyoko katika eneo hilo, maarufu kama Mapango ya Amboni.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wakati tunafika Amboni jua lilikuwa limeshakuchwa. Matumaini yangu yalikuwa madogo sana kupata huduma katika muda ule. Hofu yangu kubwa ilikuwa ni kwa usiku. Kama Zena alikusudia kunifanyia jambo baya lolote, nilijua kuwa alikuwa akisubiri usiku nikiwa niko nyumbani peke yangu.

    Hapo Amboni palikuwa na eneo linaitwa Mafuriko. Eneo hilo liliwahi kupata mafuriko makubwa katika miaka ya nyumba na kusababisha kupewa jina hilo.

    Mganga tuliyemuendea alikuwa akiishi katika eneo hilo. Kwa vile mama aliwahi kufika kwa mganga huyo katika siku za nyuma hatukusumbuka kuuliza. Tulikwenda moja kwa moja kwenye nyumba yake.

    Tulikuta mzee aliyeketi barazani mwa nyumba hiyo akivuta Mtemba. Alikuwa amekaa kwenye kiti cha uvivu kando ya mlango wa nyumba yake.

    Kumbe alikuwa ndiye mganga mwenyewe tuliyemuendea.

    Tulisaliana naye. Mama akamwambia kuwa tulikuwa tumemfuata yeye.

    “Karibuni ndani” akatuambia.

    Nikapata matumaini kidogo.

    Mganga huyo alikuwa na chumba chake maalum cha uganga. Tulipoingia katika chumba hicho alitukaribisha kwenye majamvi, yeye mwenyewe aliketi kwenye kigoda kidogo kilichokuwa kwenye pembe moja ya ukuta.

    “Habari za huko mtokako?” akatuuliza.

    “Habari si nzuri. Tuna matatizo” Mama akamwambia.

    “Matatizo gani?”

    “Ni matatizo ambayo si ya kawaida. Huyu niliyenaye hapa ni mwanangu. Yeye ndiye anayehusika na hayo matatizo….”

    Mama akamueleza matatizo yaliyokuwa yametupeleka. Mganga akatuambia.

    “Subirini kidogo niwaite wenyewe muwaeleze”

    Akamuita mke wake. Mwanamke huyo alipokuja alimwambia amletee moto. Baada ya muda kidogo mwanamke huyo alileta makaa ya moto kwenye chetezo ambacho alikiweka mbele ya mganga huyo.

    “Niletee mavumba yangu na shuka yangu” Mganga akaendelea kumuagiza.

    Mwanamke huyo alikwenda pembeni mwa chumba hicho ambako kulikuwa na meza iliyokuwa na vitabu pamoja na vichupa na vikopo kopo. Alichukua kikopo kimoja, akatungua na shuka moja ya rangi nyeupe iliyokuwa imetundikwa kwenye ukuta.

    Alikwenda navyo kwa mganga akakiweka kile kikopo mbele yake kisha akamfinika ile shuka pale alipokuwa amekaa.

    “Na wewe ukae hapa hapa, usiondoke” Mganga akamwambia mwanamke huyo.

    Mwanamke huyo akakaa karibu yetu.

    Mganga alikisogeza kile chetezo cha moto karibu yake kisha akakifungua kile kikopo kilichokuwa na mavumba akachota kidogo na kuyatia kwenye ule moto kisha akajifinika shuka vizuri ili ule moshi uliokuwa unafuka uingie ndani ya ile shuka.

    Baada ya sekunde chache yule mganga akaanza kusema maneno niliyodhani kuwa yalikuwa ya lugha ya Kijerumani.

    Nilisikia maneno kama “Dachi…pontia…n

    a mengine ambayo sikuweza kuyakariri.

    Wakati huo uso wake alikuwa ameufunika ndani ya shuka. Ghafla akafunua shuka na kuutoa uso wake. Alikisogeza kile chetezo pembeni kisha akatutazama.

    “Dachi…jerumani nimekuja hapa” akasema lakini hatukuelewa maana ya maneno yale.

    Mke wa mganga akatueleza.

    “Anasema yeye ni jini wa Kijerumani anaitwa Dachi, amekuja kuwasikiliza”

    “Sawa, tumemuelewa” Mama akamjibu.

    “Asalaam aleykum” mganga akaendelea kwa kutupa salamu.

    “Wa alaykumu salaam” tukamuitikia.

    “Nini shida yenu?”

    “Mwanangu anasumbuliwa na jini mwanamke” Mama akamwambia.

    “Mwanao yuko wapi?”

    “Huyu kijana niliyenaye hapa”

    “Oh mwano amepata mchumba wa kijini, anaitwa Zainush”

    Mgnga huyo alipotuambia hivyo mimi na mama tukatazamana. Tulitazamana kwa mshangao kwa jinsi alivyoweza kujua lile jina la Zena ambalo hatukuwa tumelitaja.

    “Mwanangu hataki mchumba wa kijini, tunataka aondoke asimfuate tena mwanangu” Mama akamwambia.



    “Yule jini ni mkorofi, ameshaua watu watatu” Mganga huyo aliendelea kutuambia.

    Tukatazamana tena na mama. Mama hakulieleza suala hilo la watu waliouawa, yaani yule mganga wa Mnyanjani na wale vijana wawili walioiba mkoba wa Zena.

    Tukawa tunajiuliza amelijuaje tukio hilo la kuuawa kwa yule mganga na wale vijana.

    Kama ambaye aliyagundua mawazo yetu, mganga huyo akacheka.

    “Huyo jini anakufuata wewe kila wakati, ameshapata wasiwasi. Anajua unataka kumfukuza” akatuambia.

    Alinyamaza kimya kisha akaendelea.

    “Lakini mimi haniwezi, naweza kumpiga makofi mara moja”

    “Sasa utatusaidiaje?” nikamuuliza mganga huyo.

    “Mimi naweza kumuita halafu nitamfunga kamba, hataweza kukufuata tena”

    “Utamuita lini?” nikamuuliza tena.

    “Nitamuita kesho”

    “Sasa leo akija kunidhuru usiku?”

    “Nitamzuia” Mganga akaniambia kisha akaitenga shuka na kunyanyuka.

    “Nisubirini hapa hapa” akatuambia na kutoka.

    Tulisubiri kwa karibu nusu saa. Mke wake alituambia kuwa mganga huyo alikuwa amekwenda kuchuma dawa makaburini.

    Aliporudi alikuwa ameshika rundo la majani, akampa mke wake.

    “Yaroweke kwenye maji” alimwambia.

    Mke wake aliyekuwa ameketi na sisi aliinuka na kuyachukuaa yale majani.

    “Changanya na huu mvuje” Mganga aliendelea kumwambia mke wake huku akielekea kwenye meza iliyokuwa na chupa na makopokopo. Alichukua kopo mojawapo akachota kiasi cha mvuje uliokuwa umesagwa na kumpa mke wake.

    Baada ya hapo mganga alirudi kwenye kigoda chake.

    “Nimekutayarishia dawa ambayo utakwenda kuoga na nyingine utajifukiza” akaniambia.

    “Sawa. Kwa hiyo nitakwenda kuoga nyumbani?”

    “Hapana. Utaoga hapa hapa na utajifukiza hapa hapa”

    “Sawa”

    Baada ya kama dakika tano hivi mke wa mganga alirudi akiwa amebeba ndoo ya maji ambayo aliitia yale majan.

    “Tayari” akasema.

    “Sasa nenda kamuwekee chooni” Mgnaga akamwambia.

    Mwanamke huyo akaibeba tena ndoo hiyo na kutoka nayo.

    Mganga akanitazama.

    “Mfuate, utakwenda kuyaoga yale maji yote” akaniambia.

    Nikanyanyuka na kumfuata yule mwanamke. Tulitoka uani mwa ile nyumba. Mwanamke huyo aliingia kwenye choo akaiweka ile ndoo kisha akatoka.

    “Haya nenda sasa’ akaniambia.

    Nikaingia kwenye kile choo. Nilivua nguo nikazitundika kwenye mlango wa choo. Niliona kata iliyokuwa imetiwa kwenye ndoo nyingine niliyoikuta mle chooni, nikaichukua na kujimwagia yale maji. Yalikuwa yakinuka harufu mbaya sana isiyovumilika.

    Lakini kwa vile nilikuwa na shida nilivumilia hivyo hivyo. Nilipomaliza nilijifuta futa maji kwa mikono kisha nikavaa nguo zangu na kutoka na ile ndoo ambayo niliiacha pale uani.

    Nilienda kule chumbani kwa mganga huku maji yakiwa yametosa shati langu.

    “Umeshaoga?” Mganga akaniuliza.

    “Nimeoga” nikamjibu.

    “Umemaliza maji yote?”

    “Nimeyamaliza yote”

    “Sasa bado dawa ya kujifukiza” Mganga aliniambia kisha akawageukia mke wake na mama yangu.

    “Hebu mpisheni ajifukize dawa” akawambia.

    Mama yangu na yule mwanamke wakatoka.

    Mganga akanipa shuka.

    “Vaa shuka. Vua nguo zako kisha chutama ujifukize dawa”

    Nikajifunga ile shuka kiunoni kisha nikavua suruali yangu pamoja na shati. Mganga alinisogezea kile chetezo cha moto. Akakitia aina fulani ya dawa ya unga. Chetezo kikawa kinatoa moshi.

    Nilikuwa nimeshachutama. Ile shuka ndio nilijifunika kukinga ule moshi uingie mwilini mwangu. Harufu yake ilifanana na yale maji niliyooga.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wakati ule moshi ukinipata mwilini. niliisikia sauti ya mganga akisema maneno kwa lugha ambayo sikuweza kuijua huku akilitaja jina la Zainush.

    Moshi ulipokwisha, mganga aliniambia nininuke na nivae nguo zangu. Nikainuka na kuvaa nguo.

    “Sasa kazi yako imekwisha kwa leo, rudi nyumbani ila kesho asubuhi uje tena” Mganga akaniambia.

    “Hii kazi yaa leo ni shilingi ngapi?” nikamuuliza mganga huyo.

    “Kwa leo utanipa shilingi elfu ishirini”

    “Nikatoa shilingi elfu ishirini na kumpa mganga huyo.

    “Sasa mnaweza kwenda zenu”

    “Yule jini hataweza kunifuata tena leo?” nikamuuliza.

    Mganga akatikisa kichwa.

    “Hawezi kukufuata. Hiyo harufu unayonuka hataweza hata kukusogelea”

    “Nashukuru sana’

    “Ila kumbuka kitu kimoja. Ukifika nyumbani usioge tena. Lala hivyo hivyo”

    “Sawa”

    Baada ya kumalizana na mganga huyo nilitoka ukumbini. Mama yangu alikuwa amekaa na mke wa mganga, nikamwambia.

    “Twenzetu”

    “Umeshamaliziwa?” Mama akaniuliza.

    “Tayari”

    Mama akamuga mwenzake kisha akaingia kwenye kile chumba alichokuwemo mganga akaagana naye kisha akatoka.

    Tulitoka nje tukapanda pikipiki na kuondoka.

    “Dawa inanuka kweli!” nikamwambia mama.

    “Dawa za kufukuza mashetani ndivyo zilivyo, vumilia tu”

    Nilipomfikisha mama nyumbani kwake, nikaenda Msambweni nilikokuwa nikiishi.

    Licha ya kuwa na hofu sikuona tatizo lolote usiku ule. Nikalala hadi asubuhi.

    Wakati naamka, shuka za kitanda na ile niliyojifinika zilikuwa zikinuka ile harufu ya dawa za mganga. Niliziondoa kitandani nikatandika zingine kisha nikaenda kuoga. Licha ya kujisugua kwa sabauni zaidi ya mara moja, ile harufu bado nilikuwa nikiisikia mwilini mwangu.

    Nilikwenda mkahawani nikanywa chai kisha nikapanda pikipiki yangu na kuelekea Chuda kwa kaka yangu.

    Nilipofika nilimueleza nilivyoshughulikiwa na yule mganga na alivyonieleza kuwa niende tena siku ile.

    “Jana usiku yule mwanamke hakukufuata?” akaniuliza.

    “Sikumuona lakini nadhani kama nisingekwenda kwa yule mganga wa Amboni, angenifuata. Naamini zile dawa ndizo zilizomzuia”

    “Sasa leo utaakwenda na mama au utakwenda peke yako?”

    “Nitakwenda kumsikiliza mama, kama atasema twende tutakwenda”

    “Hata kama atakwambia uende peke yako wewe nenda tu, ukirudi utakuja kunieleza”

    “Sawa kaka”



    Nyumbani kwa mama nilimkuta mama akinisubiri. Nilipomuuliza kuhusu safari ya Amboni akaniambia tutakwenda sote. Mama yangu alikuwa na huruma sana. Nikampakia kwenye pikipiki tukaenda Amboni.

    Tulipofika tulimkuta mganga akiwa kwenye chumba chake cha uganga akishughulika. Tulisalimiana naye akatuambia tumsubiri nje. Baada ya muda kidogo alitoka nje. Uso wake ulikuwa umefadhaika sana. Akatuambia.

    “Jana niliwambia mje lakini usiku nilipolala yule jini wako alinifuata na kuniletea vitisho vikali sana. Aliniambia kuwa kama nitaendelea kukushughulikia kitanikuta kile kilichomkuta mganga wa Mnyanjani. Kwa kweli nilipata hofu sana”

    “Lakini jana si ulituambia kuwa huyo jini unaweza hata kumpiga makofi?”

    “Baba! Ni kweli nilisema lakini sikujua kama jini mwenyewe ni yule aliyenifuata. Yule jini ni mkali. Alipokuja, majini yangu yalinywea”

    Maneno ya mganga huyo yalinifanya nimtazame mama. Mama naye akanitazama kwa mshangao.

    Kama ambaye aligundua kuwa maneno yake yalikuwa yamemdhalilisha mwenyewe mganga huyo aliendelea kutuambia.

    “Sidhani kama utaweza kuepukana na jini yule. Ameniambia kuwa hakuna atakayeweza kuwatenganisha, atakuwa na wewe mpaka kufa”

    “Yaani ameshajihakikishia ushindi?” Mama akamuuliza kwa mshangao.

    “Yeye mwenzetu ni jini, sisi ni binaadamu. Anatuona lakini sisi hatumuoni mpaka anapotaka mwenyewe” Mganga akasema.

    “Sasa unatushauri nini?”

    “Lakini huyu jini hana matatizo kama mnavyomdhania, tena ni jini tajiri na kisha ni mganga, kwanini hutaki kuwa naye?” Mganga akaniuliza.

    “Siwezi kuwa na mke jini wakati mimi mwenyewe ni binaadamu. Nitaishi naye vipi?” Nikamuuliza mganga.

    “Sasa utafanyaje wakati ameshakuchunuka?”

    “Nitajitahidi kuhangaika kwa waganga wengine”

    “Ukibahatika kwenda Pemba naamini unaweza kupata waganga ambao wataweza kukusaidia. Wapemba ni hodari sana kwa majini”

    “Kama hakuna budi nitafika hata huko Pemba”

    “Kama utaweza kwenda naamini utafanikiwa”

    Tuliondoka kwa yule mganga tukiwa tumenywea. Mategemeo yangu yote yalififia ghafla. Suala lile sasa lilianza kunipa changamoto kali.

    “Maneno ya yule mganga yamenitisha sana” Nilimwambia mama wakati namuendesha.

    “Hakuna lisilo na mwisho, jini si Mungu, usitishike mwanangu. Endelea kumuamini Mungu. Jini ni kiumbe kama wewe naye ameumbwa na Mungu. Mungu ndiye wa kumuogopa”

    Maneno ya mama yalinipa matumaini kidogo. Nilipomfikisha nyumbani kwake aliendelea kuniambia.

    “Makosa yetu ndiyo yanayotuponza. Imani za watu zimekuwa ndogo sana katika dini. Watu wanapenda dunia zaidi. Sasa vile vitu ambavyo vilipaswa kuwa chini yetu vinakuwa juu yetu. Mwanaadamu ndiye aliyetakiwa kutawala dunia hii lakini baada ya watu kupunguza kumcha Mungu, sasa majini yanataka kututawala sisi”

    “Leo mama umeniambia maneno ya akili na ya kufikirisha sana” nikamwambia mama.

    “Rudi nyumbani na muamini Mungu wako, jini hatakufuata”

    “Asante mama”

    Nikaondoka na pikipiki yangu kurudi nyumbani nikiwa na imani tele. Nilijiambia kama mimi ndiye niliyepaswa kuwa mtawala wa dunia hii sitakubali jini anitawale wala kunitia hofu.

    Ni kweli imani ina nguvu, nilikaa wiki nzima bila kuona kitisho chochote. Nikaona kama vile tatizo langu lilikuwa limekwisha.

    Wiki iliyofuata nikiwa kazini kwangu, tuliendelea kufanya biashara hadi saa kumi jioni, yaani siku ile kulitokea biashara ya ajabu. Tulipata wateja wengi kutoka vijijini kwa vile ulikuwa msimu wa kuuza mazao.

    Nikajikuta nilikuwa na pesa nyingi kwenye dawati langu. Muda huo sikuweza kuzifikisha pesa hizo benki kwa sababu benki zilikuwa zimeshafungwa.

    Nilizihesabu pesa hizo, zilikuwa shilingi milioni kumi. Hizo zilikuwa za mauzo ya jioni tu, za mauzo ya asubuhi na mchana zilishapelekwa benki.

    Nikaamua kuziacha pesa hizo kwenye dawati langu kwa vile nilifunga kitasa kwa funguo. Tukafunga duka na kuondoka.

    Asubuhi ya siku ya pili yake nilikwenda kazini kama kawaida. Nilipofika kitu cha kwanza nilitaka nizitoe zile pesa ili zipelekwe benki. Nilipofungua dawati sikuona kitu.

    Nikashituka na kutumbua macho yangu. Sikutosheka kutazama kwa macho, nilitia mkono wangu na kupapasa. Hakukuwa na kitu. Dawati lilikuwa tupu kama mkono uliorambwa!

    “Pesa za watu zimewenda wapi jamani?” nikajiuliza kwa fadhaa.

    Meza yangu ilikuwa na madawati matatu. Pesa niliziweka katika dawati la juu. Baada ya kuzikosa pesa katika dawati hilo nilianza kuzitafuta katika madawati ya chini yake japouwa nilikuwa na hakika kuwa pesa hizo niliziweka katika dawati la juu.

    Nilikuwa kama niliyerukwa na akili. Licha ya kupekua kwenye madawati yote matatu, pesa sikuziona. Akili yangu ilikuwa haiamini kama pesa hizo hazikuwemo kwa sababu niliziweka mwenyewe na dawati nililifunga kwa funguo.

    Nikarudi tena kwenye dawati la juu kutazama tena. Nikaja kwenye dawati la pili na la tatu. Lakini hakukuwa na pesa.

    Ule mchezo wangu wa kufungua madawati kuanzia la juu hadi la chini na kisha kurudia tena, uliwashitua wafanyakazi wenzangu wakaanza kuniuliza ninachotafuta.

    “Amour mbona umeshughulika sana, unatafuta nini?” Mfanyakazi mmoja akaniuliza.

    “Natafuta pesa. Jana tulipoondoka niliacha shilingi milioni kumi katika dawati hili la juu, sasa sizioni!” nikamwambia.

    “Zimekwenda wapi?”

    “Sijui!”

    “Kwani ulipoondoka hukulifunga?”

    “Nililifunga na funguo niliondoka nazo, sasa nashangaa pesa sizioni!”

    “Haiwezekani! Hebu tazama vizuri”

    “Nimetafuta sana, pesa hazimo. Sijui nani amezichukua!”

    “Na haiwezeani zichuuliwe na mtu wa sababu funguo uliondoka nazo mwenyewe”

    Nikanyamaza kimya huku macho yangu yakitanga tanga kwenye meza.

    Wafanyakazi wengine waliposikia mazungumzo yetu wakasogea karibu.

    “Umepoteza nini, pesa?” mfanyakazi mmoja akaniuliza.

    “Ndio pesa”

    “Uliziweka wapi?”

    “Nilizizifungia kwenye dawati hili hapa jana jioni tulipotoka kazini, sasa nashangaa pesa sizioni”



    “Ulifunga kwa funguo?” Mhasibu aliniuliza.

    “Nilifunga kwa funguo na funguo niliondoka nazo”

    “Sasa nani atazichukua kama dawati ulilifunga?”

    Katika maswali yote niliyokuwa nikiulizwa, swali hilo ndilo lililonikera kwa sababu sikuwa na jibu nalo na lilinifanya nionekane mzushi na mpumbavu.

    “Hilo ndilo jambo la ajabu” nilijikuta ninatoa jibu hilo.

    Baada ya muda mfupi nikawa nimezungukwa na wafanyakazi wenzangu waliokuwa wakilishangaa tukio hilo.

    “Hebu jaribu kukumbuka kama uliziweka sehemu nyingine” Mhasibu akaniambia.

    “Sikuweka sehemu nyingine, niliziweka kwenye dawati hili hapa” nilimuonesha lile dawati la kwanza.

    “Sasa zitakuwa zimekwenda wapi?”

    “Sijui bosi”

    “Na ni kwanini hizo pesa hazikupelewa benki tangu jana ?”

    “Ni pesa za mauzo ya jioni, benki zilikuwa zimeshafungwa bosi”

    “Mara ngapi umeshalaza pesa kwenye droo lako?”

    “Mara nyingi tu lakini leo ndio nimekomolewa”

    “Sasa umekomolewa na nani? Mhasibu akaniuliza.

    “Siwezi kujua”

    “Bado sikuelewi Amour, pesa uliziweka mwenyewe na hakuna aliyejua isipokuwa wewe mwenyewe. Sasa utasema umekomolewa, umekomolewa na nani?”

    Nikabaki kimya. Sikuwa na jibu

    Msibu akanitazama.

    “Umehakikisha kuwa hizo pesa hazipo?” akaniuliza.

    “Sizioni” nikamjibu kwa sauti iliyonywea

    “Sasa njoo ofisini kwangu”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Moyo wangu ukashituka lakini nilijikaza kiume. Nikamfuata mhasibu ofisini kwake. Kwa pembeni mwa macho yangu niiwaona wafanyakazi wenzangu wakinitazama. Kuna niliowaona wakinihurumia na kuna waliokuwa wakiona nilikuwa nimefanya ulaghai wa kuiba pesa za shirika.

    Nilipoingia ofisini mwa mhasibu, mhasibu aliniambia.

    “Kaa hapa” alinionesha kiti.

    Yeye mwenyewe alizunguka nyuma ya meza yake, naye akaketi.

    “Nataka nikwambie kitu” akaniambia. Sauti yake na uso wake haukuonesha urafiki hata chembe.

    “Ndiyo” nikamuitikia nikiwa sijui anataka kuniambia nini.

    “Umekuwa mfanya kazi muaminifu kwa muda mrefu sana lakini hii haitufanyi tusikuchukulie hatua kutokana na wizi huu wa pesa za shirika. Ninachokuomba ni kuwa nakupa siku mbili tu utupatie zile pesa” Alipofika hapo alinikazia macho kisha akaniuliza.

    “Sijui umenielewa?”

    “Nimekuelewa” Sikuwa na jibu jingine zaidi ya hilo.

    “Sasa nenda katuletee zile pesa”

    “Si kwamba hizo pesa ninazo, pesa zimeibiwa”

    “Sasa nenda katutafutie pesa za watu uzilete”

    “Nitakwenda kuzitafuta wapi bosi?”

    Nilijua kwamba niliuliza swali la kipumbavu lakini lilitokana na hoja ya kipumbavu.

    “Popote utakapojua utazipata, sisi shida yetu ni pesa tu”

    Nikageuza uso wangu pembeni kutafakari.

    “Nimekupa siku mbili uje na hizo pesa, vinginevyo itabidi suala hilo nilifikishe polisi”

    Nilihisi kijasho chembamba kikinitiririka kwenye mfereji wa uti wa mgongo wangu.

    “Tumeelewana?” Bosi akaniuliza alipoona nipo kimya.

    “Sawa bosi” nikamjibu kisha nikainuka kwenye kiti.

    Nilikwenda kwenye mlango. Wakati naufungua mlango huo nikaisikia sauti ya mhasibu akiniambia.

    “Kumbuka kwamba nimekupa siku mbili”

    Nikageuza uso na kumtazama.

    “Nimekuelewa” nikamjibu kisha nikafungua mlango na kutoka.

    Wakati natoka, macho ya wafanyakazi wenzangu yaligeuka kwangu. Sikuwapatiliza wala kuwajali. Nilihisi walikuwa miongoni mwa walionikomoa. Mimi nimeshapewa onyo la kusulubiwa, wao wanafurahia milioni kumi za bure.

    Nilitoka nje ya duka letu bila kuzungumza na mfanyakazi yeyote. Nilikuwa nimefadhaika kweli. Nilipanda pikipiki yangu nikaiwasha na kuondoka.

    Sikujua nilikuwa naenda wapi, nikaona niende kwa mama nikamueleza kuwa nimefikwa na mitihani. Wakati naendesha nilikuwa najiuliza nitazipata wapi shilingi milioni kumi ili nirudishe pesa za watu.

    Pale nilipomkubalia bosi, aliponiambia niende nikazitafute pesa hizo nilimkubalia tu ili niweze kuondoka kwani nilijua kuwa sitazipata.

    Nilipofika kwa mama yangu nilimueleza mkasa ulionitokea, mama alitaharuki sana.

    “Imekuwaje tena mwanangu?” akaniuliza.

    “Kwa kweli sielewi kitu mama. Huyo mtu aliyenichezea mchezo huu amenikomoa kweli”

    “hilo dawati ulikuta limevunjwa?”

    “Halikuvunjwa. Watu wana mbinu nyingi za wizi. Inawezekana kuna ufunguo mwingine uliotumika”

    “Kwanini usiwaeleze hivyo wakubwa wako wa kazi?”

    “Nani atanisikiliza. Unapotoa malalamiko unatakiwa utoe na ushahidi, ushahidi uko wapi kwamba kuna mfanyakazi mwenzagu amefungua dawati langu kwa ufunguo mwingine na kuiba hizo pesa!”

    “Sasa wewe utazipata wapi milioni kumi?”

    “Hiki ni kifungo mama!”

    “Umekwenda kumueleza kaka yako?”

    “Sijakwenda bado”

    “Hebu nenda kamueleze usikie atakupa ushauri gani?”

    “Sawa. Acha niende nikamsikilize”

    Nilipofika nyumbani kwa kaka Chuda, ilikuwa ikikaribia kuwa saa sita mchana.

    “Leo hukwenda kazini?” kaka akaniuliza.

    “Nimekwenda lakini kumetokea matatizo”

    “Matatizo gani?”

    “Kuna pesa zimeibiwa kwenye dawati langu”

    “Lini?”

    “Leo hii”

    “Kiasi gani?”

    “Shilingi milioni kumi”

    Kaka akashituka. Enzi hizo pesa hizo zilikuwa nyingi sana.

    “Zimeibiwaje?”

    Nikamueleza kaka jinsi wizi huo ulivyotokea.

    “Inawezekana huyo jamaa alikuwa na ufunguo mwingine ambao aliutumia kufungua dawati lako akaiba hizo pesa”

    “Ndio hivyo lakini sasa dhima imeniangukia mimi”

    “Kwa hiyo umeambiwa nini”

    Nitoke nikatafute pesa za shirika nizirudishe, nimepewa siku mbii tu”



    “Kama hukuzipata itakuwaje?”Kaka akaniuliza.

    “Suala hilo litapelekwa polisi”

    “Ukisikia balaa ndio hilo, wadhani utazipata wapi milioni kumi?”

    “Hiki ni kifungo kinaningoja”

    Kaka akatikisa kichwa kusikitika.

    “Nakuhurumia sana mdogo wangu sijui nitakusaidiaje?”

    “Msaada ni kupata hizo pesa na pesa hazipo”

    “Umekwenda kumueleza mama?”

    “Nimekwenda, nimemueleza”

    “Amesemaje?”

    “Hakuwa na usemi, amesikitika tu”

    Wakati ninasema hivyo nilimuona kaka amezama katika fikira. Nikajua lile tatizo lilikuwa limeugusa moyo wake.

    “Sasa itabidi tusubiri tuone uamuzi wa wakuu wako” Kaka akaniambia baada ya kimya kifupi.

    “Uamuzi! Kuna uamuzi gani tena kaka zaidi ya kufunguliwa kesi ya wizi. Kwani si nimeshaambiwa kama pesa hazitapatikana baada ya siku mbili, hili suala linafikishwa polisi!” Nikamwambia kaka.

    Kaka alikuwa amejishika kichwa akisikitika.

    “Kilichobaki sasa ni kuomba Mungu hizo pesa zipatikane”

    Wakati kaka akisema hivyo mimi nilikuwa kimya.

    “Mungu amtie imani huyo aliyeziiba azirudishe kabla ya hizo siku mbili” Kaka aliendelea kuniombea.

    Hakuna mwizi au jambazi anayerudisha kile alichokiiba lakini kwa vile kaka yangu alikuwa akiniombea ilibidi nimsikilize.

    Siku ile nilishinda bila furaha na kusema kweli nilishindwa hata kula chakula. Nilikwenda nyumbani kulala tu.

    Siku ya pili yake nilikwenda kazini. Mhasibu aliponiona akaniita ofisini kwake. Nilipokwenda aliniuliza kama nimefanikiwa kupata zile pesa.

    “Sijazipata bosi” nikamwambia.

    Uso wa mhasibu ukaonesha kuhamaki.

    “Unajua kuwa zile ni pesa za shirika?” akaniuliza kwa ukali kidogo.

    “Ninajua bosi”

    “Na unajua kuwa nilikupa siku mbili urudishe zile pesa?”

    “Ninajua”

    “Kama unajua hivyo sawa. Kesho uje na hizo pesa vinginevyo sitakuelewa”

    Sikuwa na jingine la kumjibu zaidi ya kumuitikia. Nilishajua kuwa nisipokuja na pesa hizo atanifikisha polisi. Na mimi nilikuwa nimeshajitolea kwenda jela.

    Siku ile nilishinda kazini hadi muda wa kutoka kazini nikatoka na wenzangu. Tulipokuwa nje baadhi ya wafanyakazi wenzangu waliniuliza kuhusu upotevu wa zile pesa. Kila mtu alionekana kushangaa jinsi pesa hizo zilivyoibiwa.

    “Nimepewa siku mbili nizirudishe hizo pesa vinginevyo suala litafikishwa polisi kwa hatua zaidi” nikawambia.

    Kila mtu aling’aka na kunihurumia.

    “Sasa ni nani aliyefanya mchezo huo. Hapa kazini kweli hakuna mchezo wa kuibiana pesa” Mfanyakazi mmoja akaniambia.

    “Hata mimi nashindwa kuelewa”

    Baadhi ya wafanyakazi wenzangu walikuwa wamenizunguka wakinisikiliza na kunihoji. Baadaye tulichangukana tukarudi majumbani.

    Lakini mimi sikurudi nyumbani. Nilikwenda nyumbani kwa mama. Ukiwa na mama, hata ukiwa mtu mzima utamdekea tu. Pale kwa mama ndipo nilipopaona mahali muafaka wa kupeleka kilio changu ingawa hakuwa na uwezo wowote lakini alikuwa ni mama.

    Nikamueleza mama yaliyojiri huko kazini kwangu. Nikamwambia kwamba kesho ndio natakiwa kupeleka hizo pesa vinginevyo ninafikishwa polisi.

    “Itabidi hapo kesho uende kazini na kaka yako ili litakalotokea aweze kulijua” Mama akaniambia.

    Jioni ile ile nilikwenda kwa kaka nikamueleza na tukakubaliana kwamba nimpitie asuhuhi anisindikize kazini.

    Siku ile nilipanga vizuri vitu vya nyumbani nikijua kwamba kesho yake ninakwenda jela. Usiku wake sikupata usingizi kwa mawazo.

    Nakumbuka nilipata usingizi majira ya saa kumi alfajiri nikaota ndoto ya kutisha. Niliota nimesimamishwa kizimbani nikihukumiwa kwa kosa la wazi wa fedha za shirika.

    Hakimu aliniambia. “Ushahidi uliotolewa hapa mahakamani umeonesha na kuthibitisha bila shaka yoyote kwamba umeiba shilingi milioni kumi fedha za shirika ukiwa mfanyakazi wa shirika hilo. Hivyo mahakama hii imekutia hatiani”

    Hakimu akainua uso wake na kunitazama kisha akaniuliza.

    “Una lolote la kuiambia mahakama hii kwanini isikupe adhabu kali?”

    “Mheshimiwa hakimu ninaiomba mahakama yako tukufu isinipe adhabu kali kwa kuzingatia kuwa fedha zenyewe sikuziiba mimi na kwa kweli sijui zimeibiwa na nani” nikasema.

    Hakimu akaandika maelezo yangu kisha akainua tena uso wake na kuniambia.

    “Maelezo yako hayawezi kuizuia mahakama hii isikupe adhabu kali. Ninakuhukumu kifungo cha miaka thelathini jela ili iwe fundisho kwa wengine”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hapo hapo nikaacha mdomo wazi kwa mshangao kama ambaye sikuamini kuwa nilihukumiwa kifungo hicho. Uso wangu ukiwa umenywea nilimtazama mama yangu na kaka yangu waliokuwa wamekaa katika safu za mbele.

    Nikamuona mama yangu anaangua kilio akinililia…

    Sauti yake ya kizee ndio iliyoniamsha usingizi. Wakati nazinduka moyo ulikuwa ukinienda mbio na mwili wote ulikuwa umenitota jasho. Nilijiinua kitandani nikaketi.

    Nikajiuliza, je ndoto ile ndio inanitabiria hatima yangu, kwamba nitahukumiwa kifungo cha miaka thelathini kama jambazi?

    Kama ni hivyo, niliendelea kujiambia, nitafia jela. Sitamuona tena mama yangu, sitamuona tena kaka yangu.

    Wazo la kufungwa miaka thelathini lilinifanya nitaharuki. Nikajiambia “…sijui nikimbie nisiende tena kazini…”

    Lakini nikajiuliza nitakimbilia wapi katika Tanzania hii ambapo mkono wa serikali hautakuwepo?

    Kukimbia ni kama kujidanganya na kuonesha kuwa zile pesa niliiba mimi wakati sivyo, nikajiambia, la msingi ni kwenda kazini, litakalotokea na litokee. Kama ni kufungwa au kuachiwa, ingawa tegemeo la kuachiwa sikuwa nalo.

    Mpaka inafika saa moja kamili asubuhi nilikuwa nimeshafika nyumbani kwa kaka. Nilitangulia kwenda kwa mama nikaagana naye. Mama aliniombea Mungu kile ‘kikombe’ kiniepuke.

    Nilisubiri kaka ajitayarishe hadi saa moja na nusu ndipo tulipoondoka.

    Tulifika kazini saa mbili kama na robo hivi nikaingia ndani na kaka. Tulikwenda katika ofisi ya mhasibu. Mhasibu aliponiona tu akaniuliza.

    “Umekuja na pesa?”

    Nikatikisa kichwa taratibu.

    “Sikufanikiwa bosi”

    “Mimi ni kaka yake” Kaka yangu akajitambulisha na kumuuliza mhasibu.

    “Mheshimiwa kwani hiwezekani kumkata katika mshahara wake wa kila mwezi hadi hizo pesa zikaisha?”

    Mhasibu akakasirika.

    “Nyinyi mnaleta utani na kazi. Huu ni wizi, huyu hakukopa pesa hapa hadi tumkate kila mwezi. Shilingi milioni kumi tutamkata kwa miaka mingapi wakati pesa za shirika zinahitajika? Nimeshamwambia kama hakuja na pesa leo atakwenda kujieleza polisi” Mhasibu alifoka na kuinuka kwenye kiti, akaniambia.

    “Twende!”

    Tukatoka mle ofisini na akawaambia wafanyakazi wengine kuwa tunakwenda kituo cha polisi. Tulikuwa tuna magari mawili ya shirika yenye madereva wake. Tukapanda kwenye gari mojawapo. Kaka yangu tulimuacha pale pale.

    Wakati napelekwa polisi na nikijua kuwa ninakwenda kufungwa nilimlaani sana yule aliyeiba zile pesa. Nilipata uchungu nilipowaza kwamba mimi ninakwenda kufungwa, yeye yuko ofisini akiwa ameficha shilingi milioni kumi nyumbani kwake.

    Tulikwenda kituo cha polisi cha Chumbageni. Tulipoingia katika kituo hicho mhasibu akatoa maelezo yote kuhusiana na wizi huo.



    Baada ya kumaliza kutoa maelezo yake na mimi nikatakiwa nijieleze.

    Nikaeleze hali iliyotokea ambapo fedha hizo zilichukuliwa ndani ya ndroo yangu wakati ndroo hiyo niliifunga kwa funguo.

    Baada ya maelezo yangu nikaanza kukabiliwa na maswali ya polisi.

    “Baada ya kufungia hizo pesa kwenye droo yako, asubuhi ulipokwenda kazini kwako ulikuta droo imevunjwa?”

    “Ndroo haikuvunjwa”

    “Untaka utuambie huyo aliyeziiba pesa hizo alizichukuaje bila kuvunja droo?”

    “Pengine alikuwa na ufunguo mwingine”

    “Funguo za droo yako ziko ngapi?”

    “Ni mbili na zote ninazo mimi”

    “Unaona sasa unajiingiza mwenyewe, huo ufunguo wa tatu alioutumia huyo mtu umetokea wapi wakati funguo ni mbili na unazo mwenyewe?”

    “Unaweza kuwa ufunguo wa kuchongesha. Kuna mafundi wa kuchonga funguo”

    “Tunajua kuwa wapo lakini hata wao ni mpaka uwapelekee ufunguo wa sampuli ndio wanaweza kukuchongea”

    “Wezi wana mbinu nyingi. Kama mtu alishapanga kufanya uwizi anaweza kuvizia hizi funguo ninapoziacha juu ya meza yangu wakati sipo, akaukandamiza ufunguo mmoja kwenye sabuni ili kupata meno yake halafu sabuni ile anaipeleka kwa fundi. Fundi anaweza kuchonga ufunguo kama ule”

    “Unaweza kuzungumza mengi lakini hayana ushahidi. Hebu twendeni tukaione hiyo droo yako”

    Huo ndio ukawa mwisho wa maswali.

    Tulitoka na polisi. Mimi nilipakiwa kwenye gari la polisi, mhasibu akaondoka na gari la shirika.

    Wakati tunaondoka ndio kaka yangu alikuwa anafika pale kituoni. Akatuona tunaondoka. Siku ile nilimsumbua sana kaka kwa sababu alikuwa akitembea kwa miguu.

    Tulipofika kazini kwetu tuliingia ndani, mhasibu akawapeleka polisi kwenye meza yangu.

    “Pesa ziliibiwa kwenye meza hii” Mhasibu aliwambia polisi.

    “Hebu toa hizo funguo tuzione” Polisi mmoja akaniambia.

    Nikazitoa funguo zangu kutoka mfukoni na kuwaonesha

    Polisi walizitazama kisha polisi mmoja akaniambia nifungue ile droo. Nikaifungua.

    Sote tuliokuwa tunashuhudia, mimi mhasibu na wale polisi pamoja na baadhi ya wafanyakazi, tuling'aka baada ya kuziona zile pesa zilizokuwa zimetoweka zikiwa ndani ya droo.

    “Na hizo ni pesa zipi?” Polisi mmoja akaniuliza kwa mshangao.

    “Sijui, ndio naziona sasa. Zilikuwa hazimo” nikamjibu.

    “Hapo mwanzzo mlihakikisha kwa makini kuwa hizo pesa hazikuwemo?”

    “Mimi nilihakikisha na mhasibu pia alihakikisha”

    “Hebu zitoe”

    “Nikazitoa na kuziweka juu ya meza

    “Ni kiasi gani?” Mhasibu akaniuliza

    Nikazihesabu na kuona zilikuwa shilingi milioni kumi.

    “Sasa nani amezitia hizo pesa?” Mhasibu akauliza kwa mshangao.

    Hakukuwa na jibu

    “Asubuhi uliangalia kwenye hii droo?” akaniuliza tena

    “Sikuangalia”

    Mhasibu alipowauliza wafanya kazi wenzangu kuhusu zile pesa hakukuwa na yeyote aliyeeleza kuwa alijua chochote kuhusu pesa hizo.

    “Mimi naamini kuwa hizi pesa zimerudishwa kwa sababu mimi mwenyewe niliangalia kwenye hii droo juzi, sikukuta kitu” Mhasibu akatuambia.

    “Hapa pana mchezo umepita, mimi nimechezewa na wenzangu” nikasema kwa hasira. Sasa nilikuwa na nguvu baada ya zile pesa kuonekana.

    “Sasa ni nani aliyefanya mchezo huu? Tunataka tumjue” Mhasibu akauliza.

    “Huu ni wizi ulikuwa umefanyika. Huyo aliyeiba alipoona suala hili limefika polisi ndio aliamua kuzirudisha pesa hizi” Polisi mmoja akasema.

    “Tunashukuru kwa vile amezirudisha lakini tunaomba mchezo huu usirudiwe tena” Mhasibu akaonya

    “Basi sisi tunakwenda zetu” polisi wakatuambia.

    “Mimi naona mwende kwa sababu tatizo lilikuwa ni kwenye hizi pesa ambazo zimeshaonekana” Mhasibu akawambia polisi

    Polisi hao wakatuaga na kuondoka.

    Mhasibu akachukua zile pesa na kuniambia nimfuate ofisini kwake.

    Tulipokuwa ofisini aliniambia.

    “Usirudie tena kuacha pesa kwenye droo, sasa hivi sina imani tena na wafanyakazi wa shirika hili”

    “Kutokana na msukosuko huu ulionipata, sitarajii kulaza pesa tena kwenye droo yangu”

    “Shukuru kwamba hizi pesa zimepatikana, vinginevyo ungelala ndani leo”

    “Ni kweli. Hilo nilikwishalijua”

    “Kuwa makini sana na wenzako”

    “Nitakuwa makini”

    Mhasibu akawa anahesabu zile pesa. Alipohakikisha kuwa zilikuwa shilingi milioni kumi taslim nilimuomba anipe mapumziko ya siku moja ili niende nikatulize presha yangu nyumbani.

    Mhasibu akaniruhusu, nikaondoka. Wakati natoka mlangoni nikakutana na kaka akitokea kituo cha polisi. Alikuwa amechoka kwa mwendo.

    “Imekuwaje?” akaniuliza huku akinitazama kwa uso wa sintofaham.

    “Twenzetu” nikamwambia

    Akanifuata. Tukashuka baraza.

    “Tunakwenda wapi?” akaniuliza akionesha kuwa na wasiwasi

    “Nyumbani”

    Nikaona uso wake unachanua tabasamu.

    “Kwani imekuwaje?”

    “Zile pesa zimeonekana”

    Kaka akashituka.

    “Zimeonekana wapi?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kwenye droo”

    “Droo ya nani?”

    “Droo yangu”

    “Zimeonekana kivipi?”

    “Ni tukio la ajabu sana” nikamwambia kisha nikamueleza jinsi tulivyozikuta pesa hizo kwenye droo yangu.

    “Una maana huyo aliyeiba ameamua kuzirudisha?”

    “Itakuwa ndio hivyo”

    “Kwa hiyo zile pesa alikuwa amezificha sehemu nyingine, alipoona unapelekwa polisi akaamua kuzirudisha”

    “Bila shaka. Lakini sasa nimepata fundisho sitaacha pesa tena kwenye droo yangu kwa maana wanataka kunitoa kafara”

    “Ni tukio ambalo sikulitarajia”

    “Naona dua za mama zinafanya kazi. Mama aliniombea sana”

    “Wakati tunavuka barabara tukapishana na msichana mmoja ambaye naye alikuwa anavuka kutoka upande ule tuliokuwa tunakwenda sisi. Alinitupia jicho mara moja ili kujua kama nimemuona.

    Nukta ile ile nikamtambua.

    Alikuwa Zena!



    Niliendelea kuvuka barabara huku uso wangu nimeugeuza nyuma nikimtazama yule msichana.

    Baada ya yeye kunitupia macho mara moja tu, aliugeuza mbele uso wake akaendelea na safari yake. Mimi ndiye niliyekuwa nikiendelea kumtazama.

    Kaka yangu alikuwa akinisemesha bila kujua kwamba akili yangu ilikuwa imeshughulishwa na kitu kingine.

    Tulipomaliza kuvuka barabara nilimuona Zena akikata kona kwenye jengo lililokuwa na ofisi yetu na kupotea

    Hapo ndipo nilipomshitua kaka.

    “Nimemuona zena!” nikamwambia.

    “Zena….Zena yupi?” akaniuliza.

    “Yule msichana wa kijini”

    Kaka akageuka kwa hamaki.

    “Yuko wapi?”

    “Wakati sisi tunavuka barabara na yeye alikuwa anavuka kutoka huku kwenda kule upande wa pili. Tulipishana katikati ya barabara. Nimemuona na yeye ameniona lakini hakunisemesha kitu”

    Kaka alikuwa akigeuza uso huku na huku kumtafuta.

    “Yuko wapi sasa?”

    “Ameshakata kona kwenye hili jengo, hebu njoo tumuangalie”

    Tukasogea kwenye ile barabara aliyoelekea Zena na kumchungulia.

    Hatukumuona tena.

    “Ameshapotea”

    “Ungenishitua pale pale ulipomuona” Kaka akaniambia

    “Sijui anatoka wapi na anakwenda wapi?”

    “Labda ana safari zake mwenyewe”

    “Unajua tangu nilipokwenda kwa mganga wa Amboni sjakutana naye hadi hii leo!”

    “Lakini yule mganga si alisema asingeweza kumuondoa”

    “Alituambia hivyo lakini mama alinipa moyo. Niliamini Mungu”

    Baada ya kutomuona yule msichana tukawa tunatembea kurudi nyumbani.

    “Sasa ni kwanini unarudi nyumbani?” Kaka akaniuliza.

    “Nimeomba mapumziko ya siku moja, unajua ule msukosuko ulikuwa mkubwa”

    “Ni kweli inabidi upumzike”

    Tulitangulia kwenda kwa mama. Aliponiona nikiwa na uso wa tabasamu alishangaa.

    “Imekuwaje wanangu?” akatuuliza.

    “Kesi imekwisha mama, dua zako zimesaidia” nikamwambia huku nikiendelea kutabasamu

    “Imekwisha kivipi?”

    “Zile pesa zimeonekana” Kaka ndiye aliyejibu.

    “Zimeonekana!” mama akauliza kwa mshangao.

    “Kuna mchezo walinichezea pale kazini” nikamwambia mama.

    “Hebu nielezeni vizuri Nataka kujua hizo pesa zimeonekana wapi?”

    Nikamueleza tukio lilivyotokea.

    “Wenzako unaofanya kazi nao si wazuri” mama akaniambia na kuongeza.

    “Jihadhari nao”

    “Nimemwambia hivyo hivyo, kesho na kesho kutwa wanaweza kukufanyia tena” Kaka akasema.

    “Nimepata fundisho. Sitaacha tena pesa kwenye droo, hata iweje”

    “Usiache mwanangu, utajitafutia matatizo ya bure”

    Tuliongea mengi na kaka yangu pamoja na mama yangu. Baadaye mimi na kaka tukaondoka kwa mama. Nilimpeleka kaka Chuda kisha nikarudi nyumbani kwangu.

    Nilipofika nilipanda kitandani nikajilaza. Wakati nawaza hili na hili usingizi ukanipitia nikalala. Wakati niko usingizini nikaota ilikuwa ni siku ile niliyoweka pesa kwenye droo yangu. Usiku wake Zena akafika kwenye mlango wa duka letu.

    Alisimama mbele ya mlango wa duka hilo, milango ukafunguka yenyewe. Akaingia ndani.

    Alikwenda hadi ilipokuwa meza yangu akavuta ndroo ambayo ilifunguka. Akachukua zile pesa nilizokuwa nimeziweka akazitia kwenye pochi yake. Wakati akifanya hivyo nilimsikia akisema. “Akijifanya anajua vile na mimi najua hivi, atakoma!”

    Alipozitia zile pesa kwenye mkoba wake akatoka. Alipotoka ile milango ya duka ikajifunga yenyewe.

    Wakati ule nahangaika kutafuta zile pesa Zena alikuwa yuko mle ofisini lakini alikuwa haonekani. Mpaka siku ile ambayo nilipelekwa polisi alikuwa amekwenda tena usiku kwenye duka letu akazirudisha zile pesa alizokuwa amezichukua kwenye droo yangu kisha akafunga ndroo na kutoka.

    Vile nilivyokuwa napelekwa polisi Zena alikuwa ameketi kando yangu kwenye gari lakini tulikuwa hatumuoni. Wakati ule nahojiwa na polisi na yeye alikuwa akisikiliza.

    Niliporupi ofisini na polisi Zena alikuwa yuko sambamba na mimi hadi zile pesa zipoonekana.

    Sasa wakati ule navuka barabara nikiwa na kaka alijipitisha kusudi ili nimuone kisha akapotea.

    Nikazinduka usingizini. Wakati nazinduka niliisikia sauti ya Zena ikiniambia.

    “Hilo ni onyo!”

    Nikadhani kwamba zena alikuwa mule chumbani. Nilipofumbua macho nikainuka na kuketi, nikaanza kutazama huku na huku kwa hofu kwamba ningemuona Zena mle chumbani. Lakini sikumuona.

    Nikashuka kitandani na kutoka sebuleni ambako nilikaa kwenye kochi na kuifikiria ile ndoto.

    Hapo ndipo nilipoanza kufahamu kuwa zile pesa zilikuwa zimechukuliwa na Zena ili kunikomoa. Nikajiambia kama asingezirudisha ndio ningekiona cha moto.

    “Huyu msichana ataendelea kuniamndama hadi lini?” nikajiuliza.

    Nilihisi kwamba kama sitachukua hatua thabiti za kuhakikisha kwamba ninaepukana naye, mwisho wake anaweza kunitia katika matatizo makubwa.

    Baada ya kufikiri sana nilitoa pikipiki yangu nikaenda kumueleza mama kuhusu ile ndoto. Mama naye alistaajabu.

    “Kumbe bado anakufuatilia!” akaniambia

    “Huyu jini atakuja kunitia kwenye matatizo makubwa hapo baadaye” nikamwambia mama.

    “Sasa fanya mpango wa kwenda huko Pemba”

    “Inabidi nipate mwenyeji au mtu wa kufuatana naye ndio nitaweza kufika”



    “Ulizia kwa marafiki zako unaweza kupata mtu anayekwenda. Hapa Tanga watu wa Pemba wako wengi” Mama akaniambia.

    “Nitaanza kuuliza uliza kwa watu. Nikipata mwenyeji au mtu anayekwenda huko itabidi niende”

    Baadaya kuzungumza na mama nilikwenda kwa kaka, naye nikamueleza kuhusu ile ndoto.

    “Mimi naamini majini wana matatizo sana na huyo jini hawezi kukuachia kirahisi lakini kwa vile humuhitaji nitakusaidia kukuulizia waganga kwa wenyeji wa Pemba” Kaka akaniambia.

    “Na mimi mwenyewe pia nitakuwa naulizia ulizia kwa jamaa”

    Ikapita wiki moja. Siku moja ya jumapili kaka yangu akaja nyumbani. Hakuwa na kawaida ya kufika kwangu, hivyo nilipomuona nilishituka.

    Akaniambia kulikuwa na mganga aliyetoka Pemba amefikia katika gesti moja pale Chuda. Katika matangazo yake ameeleza pia kuwa anafukuza majini wabaya.

    “Nataka twende umueleze matatizo yako anaweza kukusaidia” Kaka akaniambia.

    Nilipopata habari zile nilimwambia kaka anisubiri. Baada ya dakika chache tukawa njiani tukielekea Chuda. Nilikuwa nimempakia nyuma ya pikipiki yangu.

    Tulipofika Chuda alinipeleka katika gesti alikofikia huyo mganga aliyeniambia. Ilikuwa mtaa wa pili na ule aliokuwa akiishi yeye.

    Wale watu niliowakuta hapo nje wakisubiri zamu ya kuingia kwa mganga huyo walinipa matumaini kwamba huyo mganga alikuwa mganga kweli.

    Alikuwa ameweka tangazo lake mbele ya gesti lililoandikwa matatizo aliyokuwa akiyashughulikia likiwemo tatizo la majini.

    “Ninafukuza majini mabaya katika mwili au nyumba. Pia ninatuliza wale majini wa kichwa wanoleta maradhi na matatizo mengine” Ilisema sehemu ya tangazo hilo.

    Mwisho wa tangazo lake aliandika.

    “Njoo ujaribu kwani wengi wamefanikiwa. Nitakuwa Tanga kwa siku tatu”

    Kutokana na wale watu niliowakuta kuwa wengi nilitaka kumwambia kaka turudi baadaye, watu watakuwa wamepungua lakini nilivyoona pameandikwa kuwa mganga atakuwa Tanga kwa siku tatu nikaamua nisubri hapo hapo.

    Siku tatu ni chache sana. Kama ningemkosa siku ile na pengine siku inayofuata, uwezekano wa kumpata tena ungekuwa mdogo sana. Nilijiambia.

    Watu tuliowakuta walifikia arobaini. Nilimwambia kaka kama hatakuwa na muda wa kusubiri hapo aende zake.

    “Niache niendelee kusubiri hata kama itafika jioni” nilimwambia.

    “Sawa, basi wewe subiri ikifika zamu yako utaingia na utamueleza tatizo lako. Ukitoka hapa utakuja nyumbani kuniambia”

    Tulipokubaliana na kaka aliondoka akaniacha pale. Mpaka inafika saa nane mchana walikuwa wamebaki watu kumi nikiwemo mimi. Nikaendelea kusubiri hadi saa kumi jioni ndio ikafika zamu yangu.

    Nikaingia.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Chumba cha mganga kilikuwa cha kwanza cha mkono wa kushoto. Niliingia katika chumba hicho nikamkuta mganga aliyekuwa amekaa chini kwenye mswala. Kando yake alikuwa amechoma udi wa kijiti uliokuwa unafuka moshi.

    Mbele yake kulikuwa na vitabu kadhaa vya kiarabu pamoja na chupa za dawa za kiasili.

    Alikuwa amevaa kofia ya darize aliyoiweka katika muundo wa jahazi. Pia alikuwa amevaa shati jeupe na shuka nyeupe. Hakuwa amevaa suruali.

    “Karibu” akaniambia alipoona nimesita baada ya kuingia humo chumbani.

    “Asante” nikamjibu.

    “Kaa kwenye kiti”

    Kulikuwa na kiti kilichokuwa kando ya ukuta kushotoni kwake. Nikaenda kuketi.

    “Niambie shida yako” akaniambia.

    Nikamueleza matatizo yangu mwanzo hadi mwisho.

    “Umepata bahati sana. Kule kwetu ukiwa na jini kama huyo tayari unajihesabu kuwa ni tajiri” Mganga akaniambia baada ya kunisikiliza.

    “Huko kwenu kuna watu waliooa majini”

    “Enhe! Wapo”

    “Mimi simuhitaji huyu jini”

    “kama wewe umuhitaji ndipo anapokutia kwenye matatizo”

    “Ndio nimekuja kwako unisaidie”

    “Unataka nikusaidieje?”

    “Umuondoe”

    “Una uhakika kuwa umuhitaji kabisa, usije ukajuta baadaye”

    “Hapana, siwezi kujuta”

    “Kwangu mimi si kazi kubwa kama utanipatia vitu ninavyotaka”

    “Unataka vitu gani?”

    “Ninahitaji kucha zako na kucha za maiti aliyezikwa. Unaweza kuzipata kucha za maiti?”

    “Mh! Itakuwa ngumu!”

    “Bila kupata kucha za maiti kazi itakuwa ngumu. Nenda kanitafutie kucha za maiti. Ukizipata niletee nitamuondoa huyo jini siku hiyo hiyo. Mimi nikalipo (nitakuwepo) hadi kesho kutwa. Ukiniletea kesho itakuwa bora”

    “Bila hizo kucha haitawekana?” nikamuuliza”

    Mganga akatikisa kichwa.

    “Itakuwa vigumu”

    Nikawaza kidogo kisha nikamwambia.

    “Basi acha niende nikafikirie nitakavyoweza kuzipata hizo kucha halafu nitakuja hapo kesho”

    “Sikiliza. Kucha zenyewe ni lazima ziwe za maiti aliyezikwa si za maiti ambaye hajazikwa”

    “Sasa maiti ambaye amezikwa nitampata wapi?”

    “Kaburini”

    “Yaani nikafukue kaburi?’

    “Ndio”

    “Si nitaonekana na watu”

    “Huendi mchana, unakwenda usiku”

    “Mh!” nikaguna nilipofikiria kwenda usiku makaburini na kufukua kaburi.

    “kama hutaweza basi, tutakuwa tumeshindwa”

    “Nitakupa jibu hapo kesho kama nitaweza au la”

    “Kumbuka kwamba nitakuwa hapa Tanga kwa siku tatu. Nikitoka hapa ninakwenda Arusha”

    “Nimekuelewa, acha niende. Nitakuja tena kesho”

    Nikaagana na yule mganga na kutoka, Nilipanda pikipiki yangu nikaenda nyumani kwa kaka. Kaka mwenyewe sikumkuta, mke wake aliniambia kaka aliondoka tangu saa tisa na hakumwambia anakwenda wapi.

    Nikaona niende kwa mama. Nilipofika nilimueleza kwamba kaka alinipeleka kwa mganga aliyetoka Pemba na mganga akanieleza kwamba nimpelekee kucha za maiti.

    “Kucha za maiti utazipata wapi?” mama akaniuliza kwa mshangao.

    “Tena anataka maiti aliyekwishazikwa”

    “Sasa utampataje huyo maiti aliyezikwa ukate kucha zake?”

    “Sijui”

    “Mh! Hayo ni makubwa”

    “Maana yake niende nikafukue kaburi”

    “Kaburi gani utakalokwenda kulifukua?”

    “Kaburi lolote tu”

    “Mh! Si utaonekana ni mchawi!”

    “Labda niende usiku”



    MAKUBWA! MAMBO SASA NI YA KUFUKUA ,MAKABURI! MMH! KAZI IPO JAMANI!

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog