Search This Blog

MWANAMKE JINI - 3

 







    Simulizi : Mwanamke Jini

    Sehemu Ya Tatu (3)





    “Yaani nikafukue kaburi?’

    “Ndio”

    “Si nitaonekana na watu”

    “Huendi mchana, unakwenda usiku”

    “Mh!” nikaguna nilipofikiria kwenda usiku makaburini na kufukua kaburi.

    “kama hutaweza basi, tutakuwa tumeshindwa”

    “Nitakupa jibu hapo kesho kama nitaweza au la”

    “Kumbuka kwamba nitakuwa hapa Tanga kwa siku tatu. Nikitoka hapa ninakwenda Arusha”

    “Nimekuelewa, acha niende. Nitakuja tena kesho”

    Nikaagana na yule mganga na kutoka, Nilipanda pikipiki yangu nikaenda nyumani kwa kaka. Kaka mwenyewe sikumkuta, mke wake aliniambia kaka aliondoka tangu saa tisa na hakumwambia anakwenda wapi.

    Nikaona niende kwa mama. Nilipofika nilimueleza kwamba kaka alinipeleka kwa mganga aliyetoka Pemba na mganga akanieleza kwamba nimpelekee kucha za maiti.

    “Kucha za maiti utazipata wapi?” mama akaniuliza kwa mshangao.

    “Tena anataka maiti aliyekwishazikwa”

    “Sasa utampataje huyo maiti aliyezikwa ukate kucha zake?”

    “Sijui”

    “Mh! Hayo ni makubwa”

    “Maana yake niende nikafukue kaburi”

    “Kaburi gani utakalokwenda kulifukua?”

    “Kaburi lolote tu”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Mh! Si utaonekana ni mchawi!”

    “Labda niende usiku”

    SASA ENDELEA

    “Utaweza kufukua kaburi mpaka uipate maiti kisha uikate kucha?” Mama aliniuliza kwa mshangao.

    “Nitajaribu, nikishindwa nitaacha”

    “Mh!”

    “Sasa nitafanyaje mama?”

    “Najua kuwa huna la kufanya”

    “Basi ngoja nijaribu”

    Nilipoondoka kwa mama nikaanza zoezi la kuzungukia makaburi niliyokuwa nayafahamu. Pale jirani na nyumba niliyokuwa nikiishi paliwa na makaburi lakini yalikuwa karibu na makazi ya watu, ningeweza kuonekana.

    Nilikwenda katika eneo la Usagara ambako pia kulikuwa na makaburi. Nikaangalia angalia kisha niliondoka tena nikaenda Gofu. Kulikuwa na makaburi yaliyokuwa kando ya barabara. Mahali hapo ndipo paliponiridhisha.

    Laiti ningejua ni balaa gani ambalo ningekutana nalo usiku kwenye makaburi hayo, nisingekwenda na mpango huo ningeuacha kabisa!

    Baada ya kupata uamuzi kuwa niende katika makaburi yale wakati wa usiku, nilikwenda katika duka moja la vifaa vya ujenzi nikanunua shepe, viatu vya mvua na mipira ya kuvaa mikononi. Nikavifunga nyuma ya pikipiki yangu kisha nikarudi nyumbani kwangu.

    Nilikuwa nimepanga nitoke saa nane usiku ambapo hakutakuwa na watu mitaani na hivyo nisingeweza kuonekana na mtu.

    Wakati nimekaa sebuleni nikiwaza nikasikia mlango wa mbele ukigongwa.

    Nilisubiri, ulipogongwa tena ndipo nilipoinuka na kwenda kunako mlango huo.

    “Nani?” nikauliza.

    “Ni mimi Marijani”Sauti ya kaka yangu ikajibu kutoka nje.

    Nikafungua mlango.

    “Karibu kaka” nikamkaribisha ndani huku nikimpisha kwenye mlango.

    Kaka aliingia ndani, nikafunga mlango.

    “Umenishitua kidogo” nikamwambia.

    “Kwanini?”

    “Nilivyokuona umekuja kwangu huu usiku moyo wangu umeshituka”

    “Nimekuja na wazo”

    “Kaa kwenye sofa” nikamwambia kwa shauku ya kutaka kulisikia wazo alilokuwa amekuja nalo.

    “Sitakaa. Nimekuja mara moja tu. Nataka niwahi kurudi”

    “Pikipiki ipo nitakurudisha kaka”

    “Usijali Amour tunaweza kuzungumza tukiwa tumesimama, sisi bado ni vijana. Tusiogope kusimama”

    “Sawa kaka, nieleze hilo wazo ulilokuja nalo”

    “Kwanza nilipata salamu kutoka kwa mke wangu kwamba ulikuja nyumbani ulipotoka kwa yule mganga”

    “Ndio nilikuja lakini nikaambiwa na shemeji kuwa ulitoka”

    “Ni kweli nilitoka, niliporudi ndio nilipata hizo salamu. Nikaenda kumuuliza mama kama ulifika kwake akaniambia ulifika na akanieleza ulivyoelezwa na yule mganga”

    “Umeona kuwa mganga wako amenipa mtihani mkubwa”

    “Ni mtihani mkubwa. Mama ameniambia ametaka umpelekee kucha za maiti”

    “Tena maiti aliyezikwa, yaani niende nikafukue kaburi”

    “Sasa mimi nilikuwa na wazo”

    “Ndio”

    “Kwanini usiwatumie vijana?’

    “Kuwatumia kivipi?”

    “Yaani unamtafuta kijana wa maskani unampa pesa kisha unamtuma hiyo kazi na unamuahidi kuwa akikuletea hizo kucha za maiti utampa pesa nyingine”

    “Ni wazo zuri, sikuwahi kulifikiria wazo hilo”

    “Yaani badala ya wewe kupata kazi ya kufukua kaburi, kazi hiyo unampa yeye. Hawa vijana ukiwapa elfu ishirini tu ya kunywea gongo na bangi wanaweza kukupatia hizo kucha”

    “Ni kweli. Nitawatafuta huu usiku”

    “Tena makaburi yako pale karibu tu. Kuna vijana wanaovutavuta bangi pale”

    “Nashukuru kaka kwa wazo lako, umenisaidia sana”

    Baada ya kunipa wazo lake hilo nilimrudisha kaka nyumbani kwake kwa pikipiki yangu.

    Wakati narudi nyumbani nikawa nalitafakari lile wazo alilonipa kuona kama lilikuwa la busara.

    Kwa upande mmoja wa akili yangu niliona lilikuwa wazo la busara kwa sababu lingenigharimu pesa lakini lingenirahisishia kazi. Badala ya mimi kwenda kufukua kaburi, ningempa pesa mtu mwinginne akanifanyie kazi hiyo.

    Wahuni walikuwa wengi tu katika mtaa niliokuwa nikiishi, ningeweza kumtuma mmojawapo na akanifanyia kazi hiyo bila wasiwasi.

    Lakini kwa upande mwingine niliona halikuwa wazo zuri. Halikuwa wazo zuri kwa sababu huyo mtu nitakayemtuma hiyo kazi nitamuaminije. Atakaponiletea hizo kucha akaniambia kuwa ni za maiti, nitaaminije kuwa ni kucha za maiti kweli?

    Je kama atakwenda kukata kucha zake mwenyewe na kuniletea, nitajuaje?

    Muhuni ni muhuni tu, anaweza kuona kazi ya kufukua kaburi ni ngumu na pesa haiachiki hivyo akaenda kujikata kucha zake mwenyewe na kuniletea. Sitaweza kujua kama kucha hizo si za maiti au ni zake mwenyewe.

    Hivyo nikajiambia, si vizuri kufanya jambo la kubahatisha. Ni vizuri nifanye jambo la uhakika. Na nitakuwa na uhakika wa kucha hizo endapo nitakwenda mimi mwenyewe kufukua hilo kaburi na kukata kucha hizo.

    Nilipofika nyumbani niliingiza pikipiki yangu nikasubiri saa nane ifike. Wakati nimeketi sebuleni nikiendelea kusubiri muda, nikapitiwa na usingizi.

    Katika usingizi huo eti nikaota nimekwenda kufukua kaburi. Nikakuta mtoto mchanga aliyezikwa, hana hata kucha, Nikalifukia na kufukua kaburi jingine, hilo nalo nilikuta mtu aliyekuwa amekatwa mikono na miguu. Alikuwa amefariki kwenye ajali ya gari.

    Nikalifukia tena na kutafuta kaburi jingine ambalo nilianza kulifukua. Wakati nakaribia kulifikia sanduku mvua ikanyesha kwa kishindo. Kaburi likawa linajaa maji. Kazi ikanishinda! Kutahamaki kulikuwa kunaanza kupambazuka.

    Ikabidi niondoke nikiwa nimechukia. Hapo hapo nikazinduka.

    Nilitazama saa yangu na kuona ilikuwa saa saba ikielekea kuwa na nusu. Nikaona wakati huo pia ulikuwa muafaka kuondoka. Nikaenda kunawa uso kisha nikarudi sebuleni na kuvaa vile viatu vya mvua kwa ajili ya kujikinga na tope wakati wa kufukua kaburi.

    Ile mipira ya mikononi sikuivaa kabisa. Nikatoa pikipiki yangu. Lile shepe nilikuwa nimeshalifunga katika siti ya nyuma ya pikipiki.

    Kifaa cha kukatia kucha nilikuwa nimeshakitayarisha. Ulikuwa wembe mpya.

    Nikaondoka.

    Niliendesha piki piki yangu taratibu hadi nikafika Gofu. Usiku huo kulikuwa kimya. Hakukuwa na gari wala watu waliokuwa wakipita. Nilikuwa na hakika kwamba hakukuwa na mtu yeyote ambaye angeniona.

    Nilifika katika lile eneo la makaburi. Nikaiingiza pikipiki yangu ndani ya eneo hilo lililokuwa na mti pamoja na vichaka vidogo vidogo.

    Nikaiegesha pikipiki chini ya mti huku nikiangaza macho huku na huku. Mbalamwezi ililiangaza vizuri eneo hilo kiasi kwamba sikupata taabu kuyaona makaburi hayo.

    Nilianza kuvaa mipira ya mikononi kisha nikalifungua lile shepe. Nililishika mkononi nikaanza kutafuta kaburi la kuchimba.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Makaburi mengi yalikuwa yamewekewa zege, nikaenda mbele zaidi. Nikakuta kaburi moja ambalo halikuwa limewekewa zege na lilionesha lilikuwa jipya. Huenda kulikuwa na mtu aliyekuwa

    amezikwa siku iliyopita.

    Nikaanza kulichimba. Kwa vile mchnaga wake ulikuwa laini nililichimba haraka harka huku nikirundika mchanga upande mmoja juu ya kaburi hilo. Shimo lilipokuwa kubwa niliweza kuingia ndani nikaendelea kuchimba.

    Baada ya kama nusu saa tu nikawa nimelifikia sanduku lililokuwemo ndani. Nilipofanikiwa kuuondoa mchanga wote uliokuwa juu ya sanduku hilo nikaufungua mlango wa sanduku na kuuacha wazi. Ndani ya sanduku hilo niliona maiti ya mwanamke.

    Nikatia mkono mfukoni mwangu na kutoa ule wembe. Niliufungua kwenye karatasi yake nikaushika kisha nikaushika mkono wa ile maiti ya mwanamke. Hapo hapo nikaona mwanga wa tochi unanimulika kutoka juu ya kaburi kisha sauti nzito ikaniuliza.

    “Wewe nani na unafanya nini hapa?”

    Kwa kweli nilishituka sana. Wembe uliniponyoka. Miguu ikanitepeta. Nikainua uso wangu haraka na kutazama juu ya kaburi hilo.

    Nilijuta!



    Nilimuona mtu aliyekuwa akinimulika tochi akiwa juu ya kaburi lakini sikuweza kumuona vizuri kwa sababu ule mwanga wa tochi ulikuwa unapiga kwenye macho yangu.

    “Ulikuwa unafanya nini?’ Mtu huyo aliendelea kuniuliza kwa ukali.

    Sikumjibu. Yeye alikuwa amesimama upande mmoja wa kaburi. Na mimi nilikurupuka kuelekea upande mwingine wa kaburi nikapanda juu haraka.

    Wakati ninainuka ili nikimbie, alinirushia rungu. Nikainama na kulikwepa. Wakati nainama niliona kitu kikiruka kutoka mfuko wa shati langu na kuanguka chini. Sikujua kilikuwa kitu gani. Na sikuwa na muda wa kukitazama vizuri.

    Yule mtu nilimuona. Kwa jinsi alivyovaa niligundua alikuwa mlinzi. Nikahisi alikuwa mlinzi wa eneo lile.

    Nikatimua mbio kuelekea nilikoiacha pikipiki yangu. Wakati nakimbia nilijiuliza kama kulikuwa na mlinzi, alikuwa wapi wakati nafika na kufukua lile kaburi?

    Nilitazama nyuma na kumuona alikuwa ananikimbiza.

    “Simama wewe, utakufa!” aliniambia.

    Lakini sikugeuka wala sikusimama. Niliendelea kukimbia hadi nikaifikia pikipiki yangu, yeye bado akiwa mbali. Niliiwasha haraka haraka. Pikipiki ilikubali mara moja. Nikaipanda na kuondoka kwa kasi.

    “Wewe…bahati yako!” aliniambia baada ya kunikosa.

    Alikuwa amesimama akinielekeza rungu lake. Niligeuza uso mara moja tu nikamtazama.

    Alipoona namtazama aliniambia kwa hasira.

    “Usije tena hapa mchawi mkubwa. Ningekuua leo!”

    Niligeuza uso wangu nikatazama mbele ninakoelekea. Kimoyomoyo nilikuwa nikijiambia.

    “Ningekufa leo!”

    Nilikuwa nimekaa kwenye pikipiki huku nikijihisi wazi kuwa nilikuwa natetemeka. Sikuwa nimezoea mapambano hivyo tukio lile la kufumwa na kutimuliwa kwa sime lilitosha kunifanya nitetemeke.

    Nilikuwa nikijiambia laiti yule mtu angenishika angeniua kwa vile mwenzngu alikuwa na silaha, mimi niko mikono mitupu.

    Nilirudi nyumbani nikiwa nimeacha shepe langu ndani ya lile kaburi.

    Lakini halikuwa mali kuliko uhai wangu. Kucha za maiti zilitaka kunitoa roho yangu!

    Nilipofika nyumbani nillikuwa nahema kama vile nilikimbia njia nzima kurudi nyumbani. Niliingiza pikipiki yangu. Nikavua vile viatu nilivyovaa kuzuia tope pamoja na mipira ya mikononi kisha nikaingia bafuni kuoga.

    Nilipotoka bafuni niliona afadhali kidogo. Nikaenda kulala. Hata usingizi wenyewe sikuupata. Nilianndamwa na njozi za ajabu ajabu hadi kunakucha. Moja ya ndoto iliyonitisha ilikuwa ile maiti niliyoifukua imegeuka mzuka na kunifuata nyumbani ikiwa imetoka kucha ndefu vidoleni.

    Kucha hizo ndizo zilizokuwa zinatoboa mlango wa chumbani kwangu. Wakati nashituka mlango wa chumbani kwangu ulikuwa umeshafunguka.

    Laiti nisingewahi kuamka sijui ingekuwaje?

    Ilikuwa miujiza mitupu!

    Baada ya kuoga na kuvaa nilitoa pikipiki yangu. Hapo ndipo nilipogundua kuwa leseni yangu sikuwa nayo mfukoni. Usiku uliopita niliiweka kwenye mfuko wa shati langu na kwa muda ule sikuwa nayo.

    Nikahisi ndio iliyonianguka kule makaburini usiku wakati yule mlinzi akinikurupusha.

    Nikawa nimegwaya. Nilijiambia kama yule mlinzi ataiona ile leseni yangu ambayo ilikuwa na picha yangu anaweza kuipeleka polisi. Kwa vile tayari nilikuwa na rikodi mbaya polisi, kugunduliwa kwangu kungekuwa rahisi sana.

    Polisi watakapoiona picha yangu watanifuata kazini kwangu na kunikamata.

    Imeshakuwa balaa!

    Licha ya kupatwa na fadhaa kiasi hicho nilipanda pikipiki yangu. Kwanza nilikwenda Chuda kumueleza kaka yangu mkasa mzima.

    “Amour umefanya uzembe mwenyewe!” kaka akaniambia baada ya kunisikiliza.

    Uso wake ulionesha wazi kuwa hakufurahishwa na kitendo changu.

    “Nimefanya uzembe kivipi kaka?” nikamuuliza.

    “Jana nilikwambia nini?”

    “Hebu nikumbushe pengine nimesahau”

    “Si nilikwambia kwamba tuma mtu”

    “Kaka kutuma mtu kunaweza kuleta matatizo”

    “Matatizo gani?’

    “Sitakuwa na uhakika kama hizo kucha atakazoniletea ni za maiti kweli. Anaweza kwenda kujikata kucha zake mwenyewe akaniletea”

    “Ungetafuta mtu unayemuamini”

    “Wahuni hawaaminiki kaka. Wangechukua pesa zangu halafu wakaniletea kucha zao wenyewe”

    Kaka yangu akanywea.

    “Saasa umeshajitia kwenye balaa jingine!”

    “Kwa kweli ni balaa, sasa sijui itakuwaje!”

    “Kwani hivi sasa unakwenda wapi?”

    “Ninakwenda kazini”

    “Ukitoka kazini nenda ukamueleze yule mganga”

    “Nitakwenda”

    “Basi wewe nenda kazini kwako, punguza wasiwasi”

    Nikaondoka kwa kaka na kwenda kazini. Lakini njia nzima nilikuwa nawaza tu.

    Nilipofika niliingia kazini kama kawaida. Baadaye kidogo mhasibu alifika na kuingia ofisini kwake. Haukupita muda mrefu mhasibu alitufuata akatueleza kisa kilichonishitua.

    “Jana tulikwenda kuzika kule Gofu, shemeji yangu alikuwa amefariki. Hivi sasa napigiwa simu naelezwa kwamba kuna mtu alikwenda kulifukua lile kaburi usiku. Sijui alitaka kuichukua ile maiti?”

    “Labda ni wachawi, lakini hakuwahi kuichukua?” Mfanya kazi mmoja akamuuliza.

    “Hakuwahi, alikurupushwa na mlinzi. Lile eneo linalindwa kwa ajili yakuzuia watu kama hao”

    “Angemkamata ingekuwa vizuri kwa sababu angefahamika” Mfanyakazi mwingine alidakia.

    “Alikimbia na pikipiki. Mlinzi amesema huyo mtu alikuja na pikipiki”

    Niliposikia hivyo moyo wangu ulishituka. Kama namba za pikipiki yangu nazo zimeonekana nimekwisha!

    Sikujua kama ile maiti ilikuwa ni ya shemeji yake mhasibu wetu. Nikaona nimejiingiza katika matatizo mengine ambayo sikuyatarajia.

    “Hivi sasa nimeitwa polisi nikatoe maelezo, ile maiti imepelekwa hospitali kufanyiwa uchunguzi kujua kama ilibakwa. Kuna watu wanabaka maiti” Mhasibu aliendelea kutueleza.

    “Inawezekana. Ni vizuri kama amepelekwa hospitali kufanyiwa uchunguzi. Binaadamu hivi sasa hawaaminiki kabisa” nikajidai kusema ili nisionekane nimefadhaika.

    “Kumbe yule mlinzi alikwenda kuripoti polisi” Mwenzetu mwingine akauliza.

    “Alikwenda polisi asubuhi. Ndio maana ninaitwa polisi” Mhasibu akamjibu kisha akatuaga na kuondoka.

    Niliwaza kwamba kama mlinzi alikwenda kuripoti polisi, ile leseni yangu pia aliipeleka baada ya kuiokota pale ilipoanguka. Polisi watakuwa wameshaiona picha yangu. Bila shaka mhasibu wetu ameitwa ili kuoneshwa ile leseni ili athibitishe kama ndiye mimi.

    Sasa sijui nikimbie kuepusha aibu, au niwangoje polisi waje wanikamate hapa hapa?

    Kwa kweli nilikuwa nimechanganyikiwa.





    Kwa dakika kadhaa sikuweza kujua nifanye nini. Wafanyakazi wenzangu walikuwa wakilizungumzia lile tukio la kufukuliwa kaburi, mimi nilikuwa kimya. Moyo wangu ulikuwa ukihangaika. Lakini hakukuwa na yeyote aliyeweza kunigundua.

    Wasiwasi uliponizidi nilitoka nje ya duka letu. Kilichonitoa ni ule wasiwasi kwamba polisi wakitokea niweze kuwaona mapema. Nilikuwa nimeshapanga kuwakimbia.

    Ilikuwa bora kupotea kuliko kupatwa na fedheha kama ile mbele ya wafanyakazi wenzangu.

    Nilisimama nje ya duka letu kwa karibu nusu saa, nilipoona hakukuwa na polisi wowote waliokuwa wanakuja nikarudi ndani. Baadaye nikatoka tena. Nikaangalia pande zote za barabara kisha nikarudi.

    Wakati nimekaa nikiendelea na mawazo yangu nilishituka nilipomuona mhasibu akiingia. Nilijua kuwa alikuwa amefuatana na polisi waliokuja kunikamata.

    Lakini sikuona polisi. Alikuwa peke yake. Nikamkodolea macho ya tashiwishi. Nilikuwa na hisia kwamba alikuwa ameoneshwa leseni yangu na kunitambua.

    Mfanyakazi mwenzetu mmoja akamuuliza kilichotokea huko polisi alikokwenda.

    “Nimekwenda kutoa maelezo yangu” akasema na kuongeza.

    “Ule mwili bado uko hospitali kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi”

    “Huyo mtu aliyefukua hilo kaburi hakufahamika?’ nikauliza ili kuondoa dukuduku nililokuwa nalo.

    “Si rahisi kufahamika. Mtu mwenyewe alikimbia na pikipiki” Mhasibu akanijibu.

    Hapo wasiwasi ukanipungua kidogo.

    Baada ya mhasibu kuzungumza na sisi kwa dakika chache akaingia ofisini kwake.

    Haukupita muda mrefu, simu tuliyokuwa tunaitumia ikaita. Ilikuwa inapokelewa na mtu yeyote aliye karibu nayo. Akaipokea mfanyakazi mmoja akasikiliza kisha akaniita.

    “Amour ni simu yako”

    Moyo ukanipasuka.

    Ni nani tena?CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nikaenda na kukipokea chombo cha kuzungumzia. Nikakiweka sikioni na kusema.

    “Hello!”

    “Naongea na bwana Amour?” Sauti nzito tena inayokwaruza ikauliza kutoka simu ya upande wa pili.

    Moyoni mwangu nilikuwa nikijiuliza ni nani mwenye sauti hii? Akilini mwangu sikuweza kukumbuka mtu yeyote ninayemfahamu mwenye sauti inayolingana na ile.

    Nikashuku kwamba anaweza kuwa afisa wa polisi ananipigia kuniita kituo cha olisi.

    “Ndio. Wewe nani?”

    “Hebu njoo hapa Tropicana, utanijua tu”

    Tropicana ulikuwa mkahawa uliokuwa mtaa wa pili ambao wafanyakai wengi hupenda kunywa chai wakati wa saa nne na hata kula chakula cha mchana.

    “Ni vizuri unifahamishe wewe nani?”

    “Usiwe na wasiwasi. Ukifika hapa utaniona na utanijua”

    Nikaurudisha mkono wa simu kisha nikatoka. Niliwaaga wenzangu kuwa ninakwenda kunywa chai.

    Nilipotoka nje ya duka letu nilizunguka mtaa wa pili ambako kulikuwa na huo mkahawa wa Tropicana. Wakati natembea nilikuwa nikiwaza huyo mtu aliyeniita atakuwa nani kama si afisa wa polisi.

    Nilikuwa na hakika kwamba sikuwa nikifahamiana na mtu aliyekuwa na sauti kavu kama ile.

    Nilipofika kwenye mkahawa huo nikaingia. Nilisita kidogo kando ya mlango nikawatupia macho watu waliokuwamo ndani. Nikaona mtu mmoja aliyekuwa amekaa katika meza ya pembeni akinipungia mkono kuniita.

    Sikuweza kumfahamu mpaka nilipofika karibu yake.

    “Ah Mgosingwa!” nikasema mara tu sura yake iliponijia akilini mwangu.

    Alikuwa mlinzi wetu ambaye alifukuzwa kazi kwa tabia yake ya ulevi wa kupita kiasi. Tulikuwa tunamuita Mgosingwa, neno la kabila la kizigua linalotokana na neno mgosi, yaani mwanamme.

    Kwa vile yeye mwenyewe alikuwa mzigua, alikuwa akimuita kila mtu “mgosingwa” hasa pale anapotaka kumkopa mtu pesa ya kwenda kulewea. Na sisi tukampa jina hilo la mgosingwa. Nilizoea kumuita hivyo na jina lake halisi nilikuwa silijui.

    “Vipi Mgosingwa?” akaniambia huku akinipa mkono kunisalimia.

    “Salama tu Mgosingwa. Wewe ndio uliyenipigia simu kuniita?’

    “Ndiye mimi Mgosingwa. Karibu ukae”

    Nikakaa kwenye kiti.

    “Ulikuwa unasemaje Mgosingwa?” nikamuuliza nikiwa na shauku ya kutaka kujua alichoniitia.

    “Mgosingwa unatakiwa polisi!”

    Kusema kweli nilishituka aliponiambia hivyo. Moyo wangu ukawa unadunda pu!pu!pu!

    Nikajidai natabasamu.

    “Nimefanya kosa gani Mgosingwa?”

    Mgosingwa alitia mkono kwenye mfuko wa shati lake akatoa ganda kama la kitambulisho akaniwekea mezani.

    “hii si leseni yako Mgosingwa?’ akaniuliza.

    Nikalichukua lile ganda na kulifungua. Naam. Ilikuwa ni leseni yangu niliyokuwa nimeitupa kule makaburini. Pale pale uso wangu ulibadilika rangi kwa hofu iliyochanganyika na fadhaa. Nikamtazama mgosingwa huku nikijiuliza ameipata wapi leseni yangu.

    “Huku nikiendelea na tabasamu langu la kulazimisha nilimuuliza.

    “Mgosingwa umeipata wapi hii leseni yangu?’

    “Si nimekwambia unatakiwa polisi?”

    Jibu lake hilo lilizidi kunichanganya na kunifadhaisha. Midomo yangu niliyokuwa ninailazimisha kutabasamu huku nikiwa na fadhaa ilianza kutatizika na kutetemeka. Sasa haikuweza tena kutabasamu.

    “Mgosingwa unanichanganya. Sasa nani kakupa hii leseni na kakupa kwa madhumuni gani?” nikamuuliza huku nikiizuia modomo yangu isitetemeke wakati nikimuuliza hivyo.

    Mgosingwa aligundua kuwa nilikuwa nimetaharuki. Akacheka. Hata hivyo kwa vile uso wake ulikuwa umekunjana kutokana na kuendeleza kilevi, kicheko chake hakikuufanya uso wake upendeze, bali ulionekana kama anataka kulia.

    “Mgosingwa hukumbuki uliiacha wapi leseni yako?” akaniuliza.

    Nikatikisa kichwa.

    “Sikumbuki” Nilimjibu hivyo ili nijue ataniambia nini.

    “Mgosingwa jana usiku si ulikuja kule makaburi ukafukua lile kaburi nikakukurupusha”



    Aliponiambia hivyo nikanywea na kumtazama. Alipoona nipo kimya aliendelea kunieleza.

    “Wakati unakimbia mgosingwa uliiangusha hii leseni yako”

    “Kumbe wewe ndiye unayelinda pale?” nikamuuliza.

    “Nilipoacha kazi STC niliajiriwa na kanisa kulinda yale makaburi. Sasa jana usiku niliondoka kidogo kwenda kupata ulabu (kilevi), niliporudi nikakuta mtu amechimba kaburi na kuingia ndani. Hii leseni niliiokota asubuhi ndio nikagundua kuwa ulikuwa wewe”

    “Sasa Mgosingwa umeshakwenda kutoa ripoti polisi?”

    Polisi nimeshakwenda lakini nilipoona hii leseni yako sikuwapa. Niliwambia huyo mtu sikumuona vizuri”

    Hapo hapo nilitia mkono mfukoni nakutoa pochi yangu. Niliifungua na kuchomoa noti za shilingi elfu ishirini, nikampa.

    “Asante sana Mgosingwa, umenisaidia sana”

    SASA ENDELEA

    “Tunajuana Mgosingwa , hatuwezi kusalitiana” Mgosingwa aliniambia wakati akipokea zile pesa.

    “Unajua lile kaburi ni la shemeji yake mhasibu wetu. Mimi sikujua kabisa”

    “Kwani ulikuwa unataka nini Mgosingwa?”

    “Kuna kitu nilikuwa nataka”

    “Kitu gani?”

    Kwanza nilisita kumwambia nilikuwa nataka nini lakini nikaona ni vizuri nimwambie.

    “Nilikuwa nataka kucha za maiti”

    “Mgosingwa unataka kwenda kuroga au kuua mtu?”

    “Hapana. Ni kwa mambo yangu binafsi”

    “Mgosingwa ungeniambia, ningekupatia. Mimi Ndio nalinda yale makaburi”

    “Bado ninazihitaji Mgosingwa, nifanyie huo mpango”

    “Utanipa shilingi ngapi?”

    “Ukiniletea hizo kucha nitakuongezea kumi nyingine”

    “Fanya ishirini Mgosingwa, kumi ndogo sana”

    “Si kitu, nitakupa hizo ishirini”

    “Sasa Mgosingwa nitafutie shepe na kiwembe. Niletee pale saa nne usiku. Mimi nitafukua kaburi, asubuhi nitakuletea hizo kucha nyumbani kwako”

    “Hakuna tatizo. Nitakuletea hilo shepe. Kiwembe utanunua mwenyewe”

    “Sasa Mgosingwa fanya kitu kimoja, nipatie kianzio cha shilingi elfu kumi, hiyo kumi nyingine utanipa asubuhi”

    Nilitaka kucheka lakini nilisita kwa sababu tulikuwa katika suala nyeti sana kwa upande wangu.

    “Kwanini usisubiri hadi hiyo asubuhi nikupe zote?” nikamuuliza.

    “Ninahitaji hiyo pesa kwa sasa”

    “Mgosingwa si nimekupa elfu ishirini za bure?”

    “Mgosingwa si za bure, polisi ungetoa ngapi ili wakuachie”

    “Sawa. Sasa si hizo nimekupa”

    “Hazitoshi Mgosingwa”

    “Wewe unataka kwenda kulewa tu” nikamwambia huku nikitia mkono kwenye mfuko wa suruali yangu.

    Nilitoa pochi yangu nikaifungua na kumpa shilingi elfu kumi alizotaka.

    “Umeridhika?” nikamuuliza.

    “Hapa Mgosingwa umeniokoa sana”

    “Utapata chupa ngapi”

    “Acha mzaha Mgosingwa. Mimi siendi kulewa. Mke wangu amekwenda kwao kujifungua. Nilitaka kumtumia hzi pesa”

    “Sawa Mgosingwa mtumie, nilikutania tu”

    “Sasa Mgosingwa niletee shepe saa nne usiku pale pale”

    “Sawa, nitakuletea”

    Nikaagana na Mgosingwa na kuondoka.

    Nilipotoka kazini jioni nilikwenda kununua shepe jingine nikaenda nalo nyumbani. Nikawa nasubiri saa nne usiku ifike nimpelekee Mgosingwa.

    Kwa mara ya kwanza niligundua hata mlevi anaweza kuwa na manufaa yake. Sikutarajia kuwa Mgosingwa mlevu wa gongo na pombe ya mnazi angeweza kunisaidia. Licha ya msaada wa kucha za maiti alioniahidi, kile kitendo chake cha kuiokota leseni yangu na kuja kunipa mwenyewe bila kuipeleka polisi ulikuwa msaada mkubwa kwangu.

    Nilimshukuru sana nikijua kama si yeye ningeumbuka. Pengine muda ule ningekuwa niko mahabusi.

    Ilipofika saa nne usiku nililifunga lile shepe sehemu ya nyuma ya siti ya pikipiki yangu nikatoka.

    Nilikwenda katika lile eneo la makaburi analolinda Mgosingwa. Niliposimamisha tu pikipiki, Mgosingwa akajitokeza. Alitazama kila upande, alipoona kuko kimya akasogea kwenye pikipiki yangu na kunisaidia kulifungua lile shepe.

    Ile hewa yake ya mwilini tu ingetosha kumlewesha mtu. Alikuwa akinuka pombe aina ya gongo kama vile alikuwa mtambo wa kuitengenezea. Muda ule tayari alikuwa ameshalewa.

    Sikumlaumu. Kulinda makaburi wakati wa usiku ilikuwa kazi ya kutisha. Alihitaji kupata kitu cha kutuliza akili yake, vinginevyo anaweza kuota ndoto za maiti waliozikwa usiku kucha.

    Hatukuungumza chochote. Alipochukua lile shepe, alinionesha ishara kuwa tukutane asubuhi akatokomea makaburini.

    Nikapanda pikipiki yangu na kuondoka. Nilipofika nyumbani nilifikia kuoga na kulala.

    Kulikuwa kunaanza kupambazuka nilipoamshwa usingizini kwa kishindo cha mlango wa mbele uliokuwa unabishwa. Nikatazama saa yangu na kuona ilikuwa saa kumi na mbili kasorobo. Nikajiuliza ni nani abishae mlango? Sikupata jibu.

    Nikashuka kitandani na kuvaa suruali yangu kisha nikafungua mlango wa chumbani mwangu na kutoka ukumbini. Nilikwenda kwenye mlango wa mbele na kuuliza.

    “Nani abishaye?”

    “Ni mimi Mgosingwa!” nikaisikia sauti ya Mgosingwa ikisikika kwa nje.

    “Ahaa ni wewe!” nikasema huku nikifungua mlango.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nikamuona mgosingwa amesimama mbele ya mlango. Kando ya baraza ya nyumba niliyokuwa naishi kulikuwa na baskeli iliyoegeshwa. Katika kiti chake cha nyuma ilikuwa imefungwa shepe.

    “Kumekucha mgosingwa. Habari ya leo?” Mgosingwa akaniambia kwa uchangamfu.

    “Nzuri Mgosingwa, je umefanikiwa?”

    “Nisifanikiwe kwanini?” akaniuliza huku akitia mkono kwenye mfuko wa shati lake na kutoa kibiriti.

    Nilidhani alikuwa anataka kuwasha sigara lakini alipokifungua alikielekeza mbele ya macho yangu. Nikaona alikuwa ameweka kucha nyeupe.

    “Ndio hizo Mgosingwa?” nikamuuliza.

    “Si ulitaka kucha za maiti?”

    “Ndiyo”

    “Ndio hizo nimekuletea”

    “Ulifukua kaburi?”

    “Kulikuwa na kaburi moja la maiti iliyozikwa jana, nililifukua usiku nikaikata kucha ile maiti kisha nikalifukia kama nilivyolikuta. Kucha zenyewe ndio hizo”

    Nilizitazama vizuri zile kucha alizoziweka ndani ya kibiriti kisha nikakifunga.

    “Asante sana Mgosingwa” nikamwambia Mgosingwa kisha nikamtazama.

    “Mgosingwa fanya basi hayo makwarukwaru” Mgosingwa akaniambia huku akinitazama kwa jicho la tamaa.

    Makwarukwaru ni lugha ya mitaani. Mgosingwa alikuwa akimaanisha nimpe pesa.

    “Makwarukwaru yapi Mgosingwa?”

    “Si tuliongea jana, nikikuletea hizo kucha utanipa shilingi elfu ishirini”

    “Mgosingwa si nilikupa kumi?’

    “Ndio, ikabaki kumi”

    Nikatia mkono kwenye mfuko wa suruali yangu na kutoa noti za shilingi elfu kumi nikampa.

    “Asante Mgosingwa, wewe hata kama utataka mguu wa maiti niambie nitakupatia”

    “Sawa bwana”

    Mgosingwa akachukua baskeli yake na kuniaga. Na mimi nikarudi ndani.

    Nilipoingia ndani nilikwenda kuoga nikavaa na kutoka na pikipiki yangu. Nikaenda kwa yule mganga wa kipemba. Kwa vile ilikuwa bado mapema nilisubiri nje ya gesti hadi mlango wa gesti ulipofunguliwa, nikaingia.

    Nilibisha mlango wa chumba cha mganga. Baada ya muda kidogo mlango ulifunguliwa. Mganga aliponiona tu akanikumbuka.

    “Oh karibu, wewe si ndiye yule jamaa uliyekuja juzi?” akaniuliza.

    “Ndiye mimi”

    “Karibu ndani”

    Alinipisha kwenye mlango nikaingia mle chumbani.

    “Kaa kwenye kiti” akaniambia na kuongeza.

    “Bahati yako umenikuta, leo ndio siku yangu ya kuondoka. Naenda Arusha. Nilikutazamia jana sikukuona”

    “Jana sikufanikia kupata zile kucha”

    “Sasa leo umezipata?”

    “Nimezipata”

    “Ni kucha za maiti khaswa?”

    “Ni kucha za maiti. Kuna mtu alifukua kaburi jana usiku akamkata kucha maiti”

    Nilitia mkono kwenye mfuko wangu wa shati nilikoweka kile kibiriti alichonipa mgosingwa.

    “Kama umezipata hizo kucha nitaahirisha safari yangu ili nikufanyie kazi yako” Mganga alinaimbia.

    Nilikitoa kile kibiriti.

    “Ni hizi hapa” nikamwambia na kukifungua kile kibiriti na kumuonesha.

    “Ziko wapi. Mbona sioni kitu” Mganga akaniuliza.

    Nikashituka na kuangalia ndani ya kile kibiriti.

    Hamkuwa na kitu. Kibiriti kilikuwa kitupu kama mkono uliorambwa!

    Mbali ya kukichomoa kabisa kwenye ganda lake sikuona chochote.

    “Jamani zile kucha zimekwenda wapi?” nikajiuliza kwa mshangao.

    “Ulikuwa umezitia humu?” Mganga akaniuliza.

    “Ndio, nilizitia humu. Wakati naondoka nyumbani zilikuwamo!”

    “Sasa zimekwenda wapi?”

    “Sijui”

    “Au umezimwaga bila kujua?’

    “Sijazimwaga. Nilipoondoka nyumbani kucha zilikuwemo. Nikakitia hiki kibiriti mfukoni na sijakitoa mpaka muda huu”

    “Basi itakuwa ni miujiza”

    “Sasa miujiza hii inatokea wapi?”

    Mganga akawa anafungasha vitu vyake kwenye begi lake alilokuwa ameliweka kitandani. Niliona kama amenipuuza.

    “Sasa miujiza hii imetokea wapi?’ nikamuuliza tena.

    “Hilo jini limekutawala sana, itakuwa vigumu kuliepuka” Mganga akaniambia huku akiendelea kupanga nguo zake.

    “Limenitawala kivipi?’

    “Wauliza jibu, wewe huoni mambo yako yanakwenda ovyo unadhani ni kwa sababu ya nini?’

    Sikumpinga, mambo yangu yanaenda ovyo kweli.

    “Ndio sababu hizi kucha zimepotea?” nikamuuliza.

    Mganga hakunijibu. Badala yake aliniambia.

    “Kazi kama hizo sizitaki kabisa, zitaniletea nuksi bure”

    “Wewe ndiye mtaalamu nilitegemea kuwa utanisaidia”

    “Sitaweza kukusaidia, naomba uende zako. Nina safari ya arusha nisije nikachelewa gari” Mganga aliniambia akionesha wazi kukasirika.

    Sikuwa na jingine isipokuwa kuinuka kwenye kiti. Nikamuga na kuondoka zangu. Nilivyomuaga hata hakunijibu kitu. Sijui nilimkosea nini. Alikuwa amehamaki mara moja.

    Wakati natoka mle chumbani yale maneno yake kwamba hilo jini limenitawala sana na kwamba itakuwa vigumu kuliepuka, yalikuwa yakinirudia akilini mwangu.

    Kusema kweli niliondoka pale gesti nikiwa na fadhaa sana. Nilipanda pikipiki yangu. Sikutaka kwenda kwa kaka ingawa hapakuwa mbali na pale gesti, nikaenda kazini kwangu.

    Nilifanya kazi huku nikiwaza jinsi zile kucha zilivyopotea kwenye kibiriti. Kwa kuzingatia maneno ya yule mganga iliwezekana kwamba zile kucha zilipotezwa na Zainush.

    Lakini kubwa ambalo lilinitia fadhaa ni yale maneno ya yule mganga kwamba hilo jini limenitawala sana na itakuwa vigumu kuliepuka.

    Kama mganga wa majini amesema hivyo, je juhudi zangu za kumuondoa zainush zitafanikiwa kweli, nikajiuliza kwa fadhaa.

    Mganga mwenyewe amenifukuza, nikaendelea kuwaza, bila shaka na yeye alikuwa amepata hofu baada ya kuona jinsi zile kucha zilivyotoweka kwenye kibiriti.

    “Una nini leo Amour?” Wafanya kai wenzangu walikuwa wakiniuliza.

    “Nikoje?’



    “Leo unaonekana una mawazo sana” Mfanyakazi mmoja akaniambia.

    “Kawaida tu”

    “Tuambie kama kuna kitu kimekukwaza”

    “Kwa hapa kazini?”

    “Popote tu”

    “Hakuna kitu. Binaadamu kuwaza ni kawaida”

    “Mwenzetu leo umezidi sana”

    “Basi nitapunguza” nikasema kwa utani kisha nikacheka ili kukatisha yale mazungumzo yake.

    Nilipomwambia hivyo naye akacheka, akaniambia.

    “Sawa bwana”

    Maneno yakaishia hapo hapo. Sikujua kama wafanyakazi wenzangu walikuwa wananiona nilikuwa na mawazo. Baada ya hapo nikajitia kufanya kazi ili nionekane wa kawaida. Sikutaka mtu yeyote ajue lililokuwa moyoni mwangu.

    Jioni nilipotoka kazini nikaenda Chuda kwa kaka. Nilimueleza juhudi nilizozifanya jana yake hadi nikafanikiwa kupata zile kucha na hatimaye zikatoweka zikiwa ndani ya kibiriti wakati nikiwa kwa yule mganga.

    “Mganga alipata hasira akanifukuza. Aliniambia niondoke na kwamba yule jini ameshanitawala, itakuwa vigumu kumuondoa” nikamwambia.

    “Sasa kwanini alikufukuza?’

    “Sijui”

    “Na hizo kucha zilitoweka vipi?’

    “Sijui. Mgosingwa aliniletea asubuhi zikiwa ndani ya kibiriti. Sasa nafika kwa mganga nafungua kibiriti, kucha hazimo!”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Na wewe ulihakikisha ulipopewa hicho kibiriti kucha zilikuwemo?”

    “Ndio. Mgosingwa aliponipa hicho kibiriti alinifungulia akanionesha. Kucha zilikuwemo”

    “Mganga alikwambia hizo kucha zimnmekwenda wapi?’

    “Aliniambia huyo jini ndiye anayeniharibia mambo yangu”

    “Kwa hiyo huyo jini ndiye aliyezipoteza?’

    “Itakuwa ni yeye”

    Kaka alifikiri kisha akaniuliza.

    “Hizo kucha zilikuwa ndogo sana?”

    “Ndio zilikuwa ndogo”

    “Inawezekana zilichomoka moja moja kwenye kibiriti bila wewe kujua. Siamini kwamba huyo jini amezichukua yeye”

    “Unafikiria hivyo?’

    “Acha wasiwasi. Kwanza huyo jini kuna muda mrefu hajakutokea. Mimi nafikiri ameshakata tamaa”

    “Sawa kaka, nimekuelewa”

    Sikuwa na uhakika kwamba kaka alikuwa akiniambia ukweli kutoka ndani ya moyo wake au alikuwa akinituliza tu.

    Baada ya mazungumzo yetu mafupi nikamuaga na kuondoka.

    Baada ya wiki moja kaka yangu aliniita na kunishauri nioe.

    “Umeshakuwa mkubwa sasa, unatakiwa uwe na mke wako” aliniambia.

    “Ni kweli kaka. Haya mambo ya huyu jini aliyekuwa akiniandama ndio yaliyonizubaisha”

    “Mimi naamini akikuona una mke hatakufuata tena. Atakwenda kutafuta mtu mwingine. Kama atakubali, awe mke mwenza” Kaka akanichekesha.

    Tukacheka sote.

    “Nadhani hawezi kukubali kuwa mke mwenza” nikamwambia.

    “Ndio atakuacha sasa”

    “Ni kweli kaka, ni bora niwe na mke”

    “Sasa unaye msichana unayemfikiria kwamba anafaa kuwa mke wako ili tukakuposee”

    “Nitakujibu”

    “Lini?”

    “Nipe siku mbili tu”

    “Sawa”

    Lile wazo la kuoa alilonipa kaka nilikwenda kulitafakari nyumbani na kuona lilikuwa wazo la busara sana. Mbali ya kwamba nilishafikia umriwa kuwa na mke pia niliona nitakuwa na mwenzangu wa kunifariji kutokana na matatizo yaliyokuwa yananikabili.

    Pia nilizingatia kauli ya kaka kwamba nikioa, huenda yule jini akaacha kuniandama.

    Kulikuwa na msichana mmoja aliyekuwa akiishi mtaa wa pili na ule niliokuwa nikiishi mimi. Alikuwa akiitwa Salma.

    Salama nilikuwa nikimfahamu tangu alipokuwa anasoma shule ya sekondari ya Usagara. Alipomaliza kidato cha nne niliwahi kumtamkia kuwa ninampenda.

    Akaniuliza. “Unanipenda kweli au unanidanganya?’

    “Ninakupenda kweli” nikamjibu.

    “Sasa kama unanipenda kweli, waone wazazi wangu. Mimi nimeshakukubalia”

    Kwa vile muda ule sikuwa na mawazo ya kuoa, sikumpatiliza tena ila kila tulipoonana nilimtania kwa kumwambia, “Nitakuja kwa wazazi wako”

    Na yeye hucheka na kunijibu. “Njoo tu, njia nyeupe”

    Alikuwa mzuri mwenye heshima na alikuwa na sifa zote zinazostahili kuwa mke wangu.

    Yeye ndiye niliyemfikiria.

    Hata hivyo wakati ule wazazi wake walikuwa wameshahama katika mtaa waliokuwa wakiishi. Mwenyewe aliniambia walihamia Chumbageni.

    Kwa wakati ule Salama alikuwa akifanya kazi Shirika la Posta. Nikapanga nimfuate nizungumze naye ili nimueleze nia yangu ya kupeleka posa yangu kwa wazazi wake.

    Siku iliyofuata nikaenda kazini. Saa nne wakati wa kwenda kunywa chai nikaenda posta. Nikamkuta.

    Nilisubiri watu wawili aliokuwa akiwahudumia walipoondoka nikamsalimia.

    “Hujambo mrembo?”

    “Sijambo, sijui wewe”

    “Mimi ni mzima tu kama unavyoniona, hivi kule Chumbageni unaishi mtaa gani?” nikamuuliza.

    Salama akanielekeza mtaa anaoishi. Kwa vile na mimi nilikuwa mwenyeji wa mitaa ya Chumbageni niliifahamu mpaka nyumba waliyokuwa wanaishi.

    “Si ile inayotazamana na Cumbageni Guest House?” nikamuuliza.

    “Ndiyo hiyo hiyo”

    “Natarajia kutuma mshenga kwenu” nikamdokeza.

    Salama hakunijibu kitu. Nikaridhika. Kuwa kimya inachukuliwa na masheikh wa kiislamu kuwa ni ishara ya kukubali, kwa vile suala hilo tulishalizungumza.

    Nilipotoka kazini jioni nilikwenda kwa kaka nikamueleza kuhusu msichana huyo.

    “Umeshazungumza naye” akaniuliza.

    “Niliwahi kuzungumza naye siku nyingi lakini ilikuwa kama mzaha, leo ndio nilimfuta kazini kwake nikamwambia kuwa nitatuma mshenga kwao akanyamaza. Nimechukulia ishara kwamba amekubali”

    “Sasa tujaribu kupeleka ujumbe kwao?”

    “Ndio hivyo”



    “Kwa hiyo utaandika barua utaniletea hapa, halafu mimi nitatafuta mzee mmoja niende naye. Unasema anaishi wapi?’

    “Anaishi chumbageni lakini usiku tutakwenda kama tunapita njia ili nikuoneshe nyumba yao”

    “Sawa, utanifuata saa ngapi?’

    “Saa mbili usiku”

    “Nitakusubiri”

    Baada ya mazungumzo yetu na kaka nikarudi nyumbani. Saa mbili usiku nikamfuata tena na pikipiki yangu. Nilimpakia na kwenda kumuonesha ile nyumba aliyonielekeza Salama. Nilipata uhakika kwamba sikuikosea kwani tulimkuta baba yake ambaye namfahamu, ameketi barazani kwenye kiti cha uvivu akivuta mtemba wake.

    Tukapita na pikipiki yetu.

    Wakati tunarudi kaka alinaimabia.

    “Kama nyumba ni ile nimeshaiona”

    “Na yule mtu uliyemuona ameketi barazani kwenye kiti cha uvivu ni baba yake”

    “Kumbe baba yake ni yule mzee?”

    “Ndio yule”

    “Basi tutamuona hapo kesho”

    Nikamrudisha kaka nyumbani kwake, akanisisitizia tu nisisahau kuandika barua ya posa.

    Nilipofika nyumbani niliiandika barua hiyo usiku ule ule nikaitia ndani ya bahasha. Kwa kawaida barua za posa kama zile huwekwa kitu kidogo. Nikatia shilingi elfu hamsini.

    Asubuhi wakati naenda kazini nikaipeleka ile barua kwa kaka. Kaka aliifungua kwa vile sikuwa nimeifunga kabisa. Aliisoma kisha akaniambia.

    “Umeiandika vizuri”

    “Nimeweka na shilingi elfu hamsini, sijui zinatosha”

    “Zinatosha, hizi huwekwa kama ada tu”

    “Sawa, sasa mimi naenda kazini utatafuta mtu wa kwenda naye”

    “Barua yako itafika leo leo”

    Nikaenda zangu kazini.

    Saa nne nikaenda posta kwa Salama. Baada ya kusalimiana naye nilimwambia.

    “Ujumbe wangu utaupata leo”

    Salama akatabasamu.

    “Naungojea” akaniambia. Nilikuwa na hakika kwamba alijua ni mzaha wangu.

    Jioni nilipotoka kazini nilikwenda kwa kaka. Akaniambia.

    “Barua yako imefika”

    “Umeshaipeleka?” nikamuuliza kwa tashiwishi.

    “Tuliipeleka mchana. Mzee ameniambia nifuatie majibu kesho”

    “Hakukuwa na maswali yoyote aliyokuuliza?”

    “Kuuliza ni lazima. Aliniuliza ile posa ilikuwa ni ya nani wangu. Nikamjibu ni ya mdogo wangu. Akaniuliza anafanya kazi wapi nikamueleza. Akataka pia kujua unaishi wapi nikamueleza”

    “Yule mzee hatufahamiani isipokuwa nafahamiana na binti yake”

    “Aliuliza pia kama wewe ulishamueleza binti yake kuhusu nia yako”

    “Ukamjibu nini?”

    “Nilimwambia mlishazungumza na mlikubaliana. Akaniambia kwamba atazungumza naye na kwamba nifuatie majibu kesho”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kwa hiyo mtaenda tena hapo kesho?”

    “Tutakwenda”

    “Sawa kaka”

    Jioni yake niliporudi kazini nikapitia kwa kaka kupata majibu.

    Akaniambia. “Kazi imekamilika”

    “Kivipi?” nikamuuliza.

    “Posa yetu imekubaliwa. Mzee ameniambia wanataka mahari ya shilingi laki tano”

    “Mahari yake ni shilingi laki tano?” nikamuuliza kwa mkazo.

    “Inaelekea yule mzee msomi. Amesemi yeye hana mambo ya Kiswahili. Hakutaka kututajia gharama kubwa. Mimi naona laki tano si nyingi”

    “Sawa”

    “Mimi mchango wangu nitakusaidia shilingi laki moja”

    “Mimi mwenyewe nitatoa laki nne”

    “Lini zitapatikana hizo laki nne”

    “Hata kesho zinaweza kupatikana”

    “Utaniletea asubuhi?”

    “Nitakuletea jioni, wewe utazipeleka kesho kutwa”

    “Sasa tupange harusi, sipendi uchumba wenu uchukue muda mrefu sana”

    “Tukishalipa hizo pesa tutakaa na mama tupange harusi itakavyokuwa”

    “Sawa jitahidi upate jiko lako”

    “Nitajitahidi kaka”

    Nikaagana na kaka na kwenda nyumbani kwa mama. Nilimueleza ile habari. Akaniambia ameshaelezwa na mwanawe, yaani kaka yangu.

    “Ni jambo zuri” akasema.

    “Kesho kutwa tutakuja kufanya kikao cha harusi hapa kwako”

    “Kwani mambo tayari?’

    “kaka atapeleka mahari kesho kutwa”

    “Hizo shilingi laki tano?”

    “Ndio”

    “Umeshampa?”

    “Nimemwambia nitampa kesho”

    “Yeye atakusaidia shilingi ngapi?’

    “Ameniambia atanitolea shilingi laki moja, mimi mwenyewe nitatoa laki nne”

    “Kwa hiyo mnasubiri mmpeleke mahari ndio tufanye kikao”

    “Ndiyo”

    “Mimi nawaunga mkono. Nilitaka sana wewe uwe na mke. Hilo wazo nililitoa mimi”

    “Lilikuwa wazo zuri na natumaini nikiwa na mke matatizo yangu yatapungua’

    “Utakuwa vizuri mwanangu”

    “Sawa mama, basi mimi narudi nyumbani”

    Nikaagana na mama na kuondoka.



    Siku iliyofuata nilikwenda benki, nikatoa shilingi laki tano kutoka katika akaunti yangu. Jioni nilipotoka kazini nikampelekea kaka shilingi laki nne kama tulivyokubaliana.

    Nilipotoka kwa kaka nikaenda kwa mama. Nikamueleza kuwa nimeshampa kaka shilingi laki nne.

    Mama akafurahi.

    “Nawatakia heri na mafanikio” akaniambia na kuniuliza.

    “Zitapelekwa kesho?”

    “Kaka ameniambia atazipeleka kesho na kesho hiyo hiyo tutakuwa na kikao hapa kwako”

    “Saa ngapi?’

    “Nadhani itakuwa usiku”

    “Sawa wanangu, nawasubiri”

    Siku iliyofuata ilikuwa jumapili, sikwenda kazini. Nilibaki nyumbani kufanya usafi na kufua nguo zangu zilizochafuka.

    Saa saba ndipo nilipotoka. Nilikwenda kwenye mkahawa mmoja kula chakula. Nilipotoka hapo nikaenda kwa kaka. Aliniambia ndio kwanza amerudi kutoka chumbageni.

    “Mzee ameniambia baada ya kupata mahari anachosubiri ni kutajiwa siku ya harusi” kaka akaniambia.

    “Sasa tujiandae, tupeleke siku”

    “Kwani tutakutana saa ngapi kwa mama?’

    “Nimemwambia tutakutana usiku”

    “Usiku saa ngapi?’

    “Tukutane kuanzia saa moja”

    “Sawa”

    “Naona mambo yanakwenda vizuri”

    “Yanakwenda vizuri sana”

    Saa mbili usiku tulikutna nyumbani kwa mama. Mimi nilifika mapema zaidi kabla ya kaka. Ilibidi niwahi kwa sababu mimi ndiye niliyekuwa na shughuli, ilikuwa vyema mwenzangu anikute pale nyumbani na sio nimkute yeye.

    Kaka alipofika tukaanza mazungumzo. Mazungumzo yetu yalikuwa marefu na yaliishia saa nne usiku. Tulipanga kila

    kitu. Kwa vile mimi nilikuwa na akiba yangu ambayo nilipanga niitumie kwa ajili ya harusi yangu, tulikubaliana kwamba harusi ifanyike haraka, baada ya wiki mbili.

    “Hizi wiki mbili ndio za kufanya maandalizi, mnaonaje zinatosha au tuongeze siku?” kaka alituuliza wakati tunaendelea na kikao chetu.

    Nikamtazama mama, nikaona mama naye ananitazama mimi.

    “Mimi naona zinatosha, hakuna haja ya kuongeza siku zaidi” nikasema.

    “Mama unasemaje?” Kaka akamuuliza mama aliyekuwa kimya.

    “Mimi sina usemi, nawasikiliza nyinyi”

    “Na wewe unaafiki kwamba wiki mbili zinatosha kwa maandalizi?” Kaka akamuuliza.

    “Kama Amour mwenyewe amesema zinatosha na mimi nasema hivyo hivyo zinatosha”

    “Sawa. Naona tumeafikiana kwa hilo. Sasa tupange siku yenyewe ya kufunga ndoa” kaka akatuambia.

    “Tuweke siku ya ijumaa baada ya mshuko. Muda huo ni mzursana kufunga ndoa” nikasema.

    “Mimi pia naafikiana na muda huo. Kwa hiyo hatuhitaji kwenda kutazamia siku wala saa?’

    “Enzi zetu tulikuwa tunatazamia siku lakini siku hizi mambo yamebadilika” mama akasema.

    “Mama unajua kutazamia siku ni kuleta ushirikina. Siku zote zinafaa kuoa na saa zote mtu unaweza kuoa. Mtume ametuambia saa nzuri ni baada ya mshuko wa ijumaa” nikamwambia mama.

    “Swadakta Amour, umesema sawa. Umekuwa answar sunna” Kaka akanikubalia.

    “Si lazima niwe answaar sunna. Hivi ndivyo tulivyofundishwa na mtume wetu. Kufanya vinginevyo ni ushirikina”

    “Wanasema kwamba usipotazamia siku unaweza kuoa siku mbaya na maisha yako ya ndoa yakawa ya mikosi na vifo” kaka akayuambia.

    “Uongo mtupu. Ni imani tu za watu” nikasema.

    “Sawa. Tumeshakubaliana kwamba ndoa itafanyika baada ya mshuko wa ijumaa. Kutahitajika tende kidogo na kahawa au siyo”

    “Ndiyo”

    “Ndoa itafanyika wapi?”

    “Msikiti wa ijumaa”

    “Msikiti ule ni mkubwa, siku za ijumaa unakuwa na watu wengi, haluwa haitatosha. Tuchague msikiti mwingine” kaka akashauri.

    “Basi tutatafuta msikiti mwingine kule kule Chumbageni”

    “Hilo tumelimaza. Sasa tayarisha kadi mapema uzitoe kwa wafanyakazi na rafiki zako. Na mimi nitachukua kiasi. Baada ya wiki moja tukutane tena tuone tumepata kiasi gain”

    “Sawa kaka”

    Tulimaliza mazungumzo yetu. Nikampakia kaka kwenye pikipiki yake kumrudisha nyumbani kwake. Na mimi nikarudi nyumbani kwangu.

    Usiku wa siku ile ndoto zangu zote zilikuwa za harusi. Niliota ninamuoa Salma aliyekuwa akingara kama mwezi. Ingawa mwenyewe nilipanga kumuoa mchana, niliota ninamuoa usiku wa manane.

    Ndoa yenyewe ilifanyika kwenye kisiwa kisicho na watu. Tulikuwa mimi na yeye na muozeshaji wetu..

    Baada ya kuota ninaona na salama nikaota Salama amepata mtoto wa kiume, mzuri ajabu.

    Nilipoamka asubuhi na kiondoka nyumbani nilikwenda kazini kwangu. Siku ile ile nikashughulikia mpango wa kuchapisha kadi za harusi ambazo nilizipata siku ile ile.

    Wakati tunatoka kazini jioni nilimkabidhi kiasi kikubwa cha kadi msichana mmoja ambaye ni mfanya kazi mwenzangu ili anichangie kwa marafiki zake na kwa wafanyakazi wenzetu. Nikawataarifu baadhi ya wafanyakazi wenzangu kuhusu ndoa yangu.

    Nilipotoka kazini nilikwenda nyumbani kwa kaka. Naye nikampa kiasi cha kadi ili azigawe kwa marafiki zake.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mimi mwenyewe nilibaki na kiasi kidogo cha kadi hizo kwa ajili ya kuwagaia marafiki zangu.

    Nilishukuru kwa jinsi nilivyoungwa mkono. Kadi zote ziligaiwa kwa watu na kila aliyepewa kadi aliahidi kunichangia baada ya wiki moja.

    Kweli, baada ya wiki moja nilipata mchango wa kutosha sana ambao ulinipa matumaini kuwa ndoa yangu itafanikiwa. Ile wiki tuliyopanga nifunge ndoa, kaka alipeleka taarifa ukweni kuwa ndoa itafanyika siku ya ijumaa. Tulikuwa tumewapa siku saba tu za maandalizi lakini walikubaliana na sisi.

    Naam siku ikawadia. Niliwekwa ndani kama mwari, nikasingwa kwa msio na mafuta ya nazi. Walionisinga walikuwa ni binamu zangu. Ilikuwa raha asana.

    Ndoa ilifungwa katika msikiti mmoja uliokuwa maeneo ya Chumbageni.

    Nakumbuka hadi leo jinsi sheikh mmoja alivyonifungisha ile ndoa.

    Aliniita jina langu kisha akaniambia nimuitikie “Labaika”

    “Labaika” nikamuitikia.

    Akaniita tena.

    “Amour Amrani”

    “Labaika” nikamuitikia.

    “Ninakuozesha Salama binti Riyami kwa mahari mliyokubaliana, umekubali?”

    “Ndiyo” nikamuitikia huku midomo yangu ikitetemeka. Sikujua ilitetemeka kwa sababu gani.

    “Hapana. Hilo silo jibu linalotakiwa ujibu. Unatakiwa useme nimekubali kumuoa Salama binti Riyami kwa mahari tuliyokubaliana”

    “Sawa”

    “Amour binti Amraani” Sheikh akaniita tena.

    “Labaika”

    “Ninakuozesha Salama binti Riyami kwa mahari mliyokubaliana, umekubali?”

    Nikayakumbuka yale maneno aliyonifundisha.

    “Nimekubali kumuoa Salama binti Riyami kwa mahari tuliyokubaliana” nikajibu.

    Sheikh alirudia tena kuniambia hivyo mara tatu na mimi nilijibu mara tatu. Baada ya hapo ikasomwa hutuba ya ndoa iliyochukua karibu nusu saa.



    Baada ya ndoa kufungwa nilipewa mawaidha. Niliambiwa siku ile nimeoana na Salama kwa wema, kwa hiyo niishi naye kwa wema na kumpa huduma zote zinazopaswa kutolewa kwa mke.

    Sheikh aliendelea kuniambia kuwa kama itabidi kuachana, pia tuachane kwa wema kwani hivyo ndivyo ambavyo tumeusiwa na mtume wetu.

    Baada ya hapo halua na tende pamoja na visheti ziikagaiwa. Watu wakala na kufurahi.

    Baada ya shughuli kumalizika tukaenda nyumbani kwa mke. Nilikuwa nimekodi magari matano. Tulipofika tulikuta shamra shamra zikiendelea. Tuliingia chumbani kwa mke wangu aliyekuwa amepambwa vilivyo.

    Nikampa mkono. Hapo hapo sheikh akatuombea dua na kututakia afya njema na maisha mema ya ndoa. Tulipiga picha za kumbukumbu zikiwemo za mnato na za video.

    Ikafuatia pilau. Mimi na mke wangu tuliletewa sahani ya pamoja na jagi la juisi.

    Tulishindwa kula sana kwa sababu ya zile hekaheka. Si unajua siku ya ndoa mtu unapata fadhaa kidogo.

    Baada ya shughuli zote kumalizika, mtu aliyekuwa amesimamia ndoa upande wangu alitaka tuondoke. Wenyeji wetu wakapinga na kutaka tuendelee kuwepo kwa vile sherehe ilikuwa ikiendelea.

    “Hapana, sisi hatukufuata sherehe hapa. Tumekuja kuoa” Msimamizi wangu alisema.

    “Na ndoa ni sherehe, kama mtaondoka mapema hakutakuwa na sherehe tena” alijibiwa na msemaji wa upande wa mke wangu.

    “Tatizo ni nini? Kama tumeshaoa tunachukua mke wetu tunaondoka” Msimamizi wangu akachachamaa.

    “Msiondoke jamani, sherehe bado zinaendelea. Mkiondoka nyinyi mtatukatisha”

    Msimamizi wangu akanishika mkono na kuniinua.

    “Sisi tunaondoka. Nyinyi endeleeni na sherehe zenu. Na sisi huko tuna sherehe zetu”

    Tukatoka.

    “Jamani mnaondoka!” Wenyeji wetu wakalalamika.

    “Waswahili bwana, wanataka tuendelee kukaa hapa, tufanye nini? Kwani sisi hatuna kwetu?” Msimamizi wangu alisikika akisema peke yake.

    Tulitoka nje, gari zilikuwa zikitusubiri. Tukajipakia. Mimi nilipanda gari moja na mke wangu pamoja na wapambe wetu.

    Gari nyingine mbili zikapanda watu wengine.

    Tukaelekea Msambweni ilikokuwa nyumba yangu.

    Nyumbani kwangu pia kulikuwa na sherehe. Tulipokewa kwa vifijo na hoihoi. Tulipoingia chumbani. Wapambe wetu wakatuacha.

    Sherehe ziliendelea hadi saa sita usiku. Sisi tulikuwa chumbani tumelala.

    Nilikuwa nimeomba ruhusa ya siku tatu kazini kwangu. Kwa hiyo nilikaa siku tatu bila kwenda kazini. Katika siku hizo tatu sikuchezea mbali. Muda wote nilikuwa chumbani na mke wangu Salma. Mara chache nilitoka peke yangu na kukaa sebuleni.

    Baada ya siku hizo tatu kwisha nilikwenda kazini. Huko nilipata pongezi nyingi sana kwa kupata jiko (kuoa).

    Sasa nikawa nimefungua ukurasa mpya wa maisha yangu. Siku za mwanzo mwanzo nilipotoka kazini tu nilirudi nyumbani haraka. Siku za jumapili sikuondoka nyumbani.

    Ile tabia ya kula kwenye mikahawa ikaisha, nikawa nakula nyumbani tena chakula kizuri kilichopikwa na laazizi wangu. Naam. Maisha yalikuwa matamu sana!

    Ilikuwa imepita miezi mitatu. Usiku mmoja wakati tumelala na Salma, Salama alianza kuweweseka akiwa

    usingizini. Nilimuamsha na kumuuliza alikuwa na nini, akaniambia alikuwa anaota kuna msichana mmoja anamuamrisha aondoke pale nyumbani.

    “Ananiambia hapa si kwangu, ni kwake yeye” Salma aliniambia.

    Nikashituka na kumuuliza.

    “Huyo msichana yukoje?”

    “Umbo lake ni kama mimi ila yeye ni mweupe sana na ana sura kama muarabu”

    Mara moja nikamkumbuka Zena ambaye nilikuwa nimeshamsahau.

    “Anakwambia uondoke hapa nyumbani?”

    “Ndio. Tena amenishikia bakora, anataka kunichapa”

    Ili kumtoa hofu Salama nikajaribu kuzuga.

    “Unajua ulikuwa umelala kichali chali halafu ulishiba sana. Lazima uote ndoto zisizoeleweka”

    “Nilaleje sasa?” Salma akaniuliza kwa hofu.

    “Lala kiubavu ubavu, elekea huku kwangu” nikamwambia”

    Salma alipoelekea upande wangu akaniambia.

    “Nikumbatie naogopa”

    Nikamkumbatia. Salma hakuchelewa kupata usingizi. Akalala fofo. Mawazo yakabaki kwangu.

    Asubuhi tulipoamka nilimuuliza.

    “Uliota tena”

    “Hapana, sikuota” akaniambia.

    Nikashukuru aliponiambia hivyo. Nikajitayarisha kwenda kazini. Muda wangu wa kutoka ulipowadia nikatoka.

    Nilichapa kazi hadi saa kumi jioni nikarudi nyumbani. Nilikuta nyumba ilikuwa imefungwa. Funguo nilipewa na mpangaji mwenzangu wa upande wa pili.

    “Mke wako aliondoka, akaniachia hizi funguo. Amesema ukija nikupe”

    “Amekwambia amekwenda wapi?”

    “Hakuniambia”

    Nikazichukua zile funguo na kufungua mlango huku nikiwa na mawazo. Nilipoingia chumbani nilikuta karatasi ya barua iliyokuwa imeachwa kitandani. Nikaichukua na kuisoma.

    Mwandiko ulikuwa wa mke wangu Salma. Iliandikwa.

    “Nimelazimika kuondoka hapa nyumbani ili kuokoa maisha yangu. Ile ndoto ilinijia tena mchana. Nilimuota tena yule msichana. Aliniuliza kwanini sijaondoka. Akaanza kunitandika bakora. Ngozi yangu ya mgongo imeharibika kwa jinsi alivyonichapa. Hali yangu ni mbaya. Ninakwenda hospitali na nikitoka hospitali narudi kwetu. Naomba uniletee talaka yangu. Huyo msichana ninayemuota ameniambia kama nitaendelea kukaa ataniua”

    Salama alimaliza barua yake kwa kuweka jina lake.

    Kusema kweli maneno ya Salma aliyokuwa ameniandikia yalinishitua sana. Nilipomaliza kusoma barua ile niliona miguu ikininyong’onyea na kuishiwa na nguvu.



    Nikakaa kitandani na kuanza kutafakari. Tayari nilihisi presha yangu ikiwa juu na moyo ukienda mbio.

    Nilirudia kuisoma tena ile barua. Nikaona kama uso wa Salma umetokeza katikati ya ile karatasi ukitamka yale maneno aliyoandika.

    Nikaisikia waziwazi sauti yake ikimalizia kusoma barua hiyo kwa kuniambia.

    “Naomba uniletee talaka yangu. Huyo msichana ninayemuota ameniambia kama nitaendelea kukaa ataniua…”

    Nilihisi sasa mwili mzima ukipoteza nguvu. Tukio lile lilikuwa limenichoma mithili ya mkuki wa moto moyoni mwangu. Picha ya kuachana na Salama haikukubalika akilini mwangu. Si tu nilikuwa nampenda bali alikuwa ni kila kitu kwangu.

    Tukio lile liliniashiria kwamba sitaweza tena kuishi na mke yeyote.

    Zena amemtandika bakora Salma kama alivyowatandika wale vijana waliomuibia pochi.

    Nilijua kuwa kama Salma asingeondoka na yeye angeuawa. Kuondoka kwake ulikuwa uamuzi wa maana ingawa sikuupenda.

    Pia nilijua huo ulikuwa ndio mwisho wangu na Salma. Salama singeweza kurudi tena pale nyumbani na asingetaka tena kuishi na mimi.

    Yale mawazo niliyokuwa nayo kwamba nikioa mke zena atakuwa mbali na mimi hayakuwa sahihi. Sikuweza kutambua huyu jini alikuwa na nia gani na mimi.

    Kusema kweli nilisikia uchungu sana. Nikatikisa kichwa changu kusikitika. Nilishindwa kuvumilia machungu niliyokuwa nikiyasikia moyoni mwangu, nikaona machozi yakinitiririka.

    Wakati nimeinamisha kichwa changu, nilihisi kama Zena amesimama mbele yangu akinicheka. Nikashituka na kudhani alikuwa Zena kweli. Kumbe yalikuwa ni mawazo yangu tu.

    Nikajiuliza niende kwa kina salma nizungumze naye, lakini nikajiuliza tena ningekwenda kuzungumza naye nini wakati Salama ameshaamua kuondoka kusalimisha roho yake?

    Nikajiambia kuwa si ajabu ameshagundua kuwa nina jini mwanamke ambaye hataki niwe na mke. Kama itakuwa hivyo nikifika kwao Salama anaweza kukataa nisizungumze naye zaidi ya kudai talaka yake kama alivyoniandikia kwenye barua.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nilijihisi nilikuwa nimekabiliwa na uamuzi mgumu sana. Baada ya kuwaza kwa dakika kadhaa bila kupata ufumbuzi niliamua kutoka na kwenda kumueleza kaka kilichonitokea.

    Kaka akapatwa na mshangao hasa nilipomueleza kuwa Salama ametandikwa bakora na Zena na ameshaondoka nyumbani.

    “Sasa tufanye nini?” Kaka akaniuliza. Swali lake lilinikatisha tamaa. Nilichotarajia ni kupata ushauri kutoka kwake na sio mimi nimueleze yeye la kufanya.

    Ilionesha mpaka kufikia kuniuliza tufanye nini ni kwamba alikuwa amekwama.

    “Mimi sijui la kufanya. Nimekuja kwako ili nipate ushauri” nikamwambia.

    “Mmh!” kaka aliguna kwanza kabla ya kuniambia.

    “Sijui nikupe ushauri gani. Nikikwambia umbembeleze mke wako arudi ni kwamba atatandikwa tena na nikikwambia muache huko huko kwao, unyumba wenu utakuwa haupo tena!”

    “Yaani tangu sasa unyumba wetu hauko tena, anadai nimpe talaka yake!”

    “Ndio hapo sasa!”

    “Mimi siwezi kumpa talaka. Nataka nipambane na hili tatizo kwa nguvu zote”

    “Utapambana nalo kivipi?”

    Swali hilo likanifanya nihamaki. Niliona kama vile kaka hakuwa pamoja na mimi.

    “Kaka kwa mara ya kwanza naona una maswali ya kunikatisha tamaa” nikamwambia huku nikitikisa kichwa kusikitika.

    “Hapana Amour, usinifikirie hivyo. Mimi niko pamoja na wewe. Nimekuuliza ili unieleze jinsi tutakavyopambana na hilo tatizo”

    Nilikuwa nimeshahamaki. Nikaondoka kwenye kiti.

    “Sasa unakwenda wapi?” Kaka akaniuliza.

    “Niache kwanza” nilimwambia na kufungua mlango ili nitoke.

    Kaka akanyanyuka.

    “Hebu subiri Amour…!”

    Nikatoka haraka. Nilipanda pikipiki yangu nikaiwasha na kwenda kwa mama.

    Mama alivyouona uso wangu alijua kulikuwa na jambo lisilo la kawaida. Akaniuliza.

    “Kulikoni?”

    “Kuna matatizo yametokea” nikamwambia na kumueleza tatizo la kutandikwa bakora kwa mke wangu na kuondoka nyumbani.

    “Nimekwenda kwa kaka, kaka ameshindwa kunisaidia kimawazo. Sasa mimi naondoka nyumbani nitakwenda kokote ambako naona nitapata msaada. Kama itashindikana, basi bora nife huko huko!”

    Nilipomwambia hivyo mama nilitoka na kupanda pikipiki yangu. Mama alikuwa ametoka nje akinisemesha lakini sikujua alikuwa akiniambia nini na sikutaka kumsikiliza. Nikaondoka.

    Nilirudi nyumbani, nikapanga baadhi ya nguo zangu kwenye begi. Nilikuwa na akiba ya pesa nilizokuwa nimeziweka kwenye kabati. Nikazichukua.

    Kwa vile kichwa kilikuwa kimenichafuka, nilimuachia funguo mwenzangu wa upande wa pili nikaenda kulala gesti.

    Kitu ambacho kilinikera sana, niliota Zena amesimama kwenye jangwa akinicheka. Alikuwa akinicheka hadi anayumba kama mlevi.

    Asubuhi kulipokucha nilitoka nikaenda kituo cha mabasi. Nilipanda basi la kuelekea Dar. Nilifika Dar saa sita mchana nikaenda kutafuta gesti. Nilipopata gesti niliacha begi langu na kwenda kwenye mkahawa uliokuwa karibu kupata chakula kwani sikuwa nimekula chochote tangu subuhi.

    Baada ya kula chakula nilirudi pale gesti. Kulikuwa na mgeni mmoja wa kipemba aliyekuwa amepangisha chumba. Tulikutana ukumbini. Nikamsalimia na kumuuliza kama alikuwa anatoka Zanzibar.

    “Natoka Mwanza, ndio niko safarini kuelekea Zanzibar” akaniambia.

    “Unakwenda Unguja au Pemba?”

    “Mimi naenda Pemba”

    “Unatarajia kwenda lini?”

    “Kesho asubuhi Mungu akipenda”

    “Basi tutaondoka sote, nilikuwa na tatizo linalohusu huko Pemba na nitakueleza”

    “Ni tatizo gani?”

    “Hebu njoo huku chumbani kwangu nikueleze”

    Yule mtu alikubali kuingia chumbani kwangu. Nikamueleza yale matatizo yangu.



    “Sasa shida yangu ni kupata mganga ambaye ataliondoa hili tatizo” nikamwambia.

    Mpemba alinyamaza kimya akafikiri kisha akaniambia.

    “Yuko mama mmoja pale Pemba ni mganga anayetegemewa sana kwa matatizo ya majini. Kama yeye atashindwa ujue hutapata tena mganga ambaye atamuweza huyo jini wako”

    “Ningekuomba unipeleke kwa huyo mwanamke”

    “Nitakuelekeza na hutapotea”

    “Lakini wewe pia si unakwenda huko huko”

    “Ndio, mimi nakwenda Pemba lakini ninakokwenda ni kwingine na huyo mganga yuko kwingine. Yaani hata tukienda sote tutaachana bandarini”

    “Si kitu, wewe nielekeze tu, nitafika”

    Kwa vile mji wenyewe nilikuwa siujui, yule mtu alinichorea ramani ikianzia bandari ya Pemba hadi ulikokuwa mtaa huo. Akaniambia nyumba ya mganga huyo iko kwenye kona. Ni nyumba kubwa lakini ni ya kizamani sana na imepakwa chokaa nyeupe.

    “Alama yake ni kuwa mlango wa mbele wa nyumba hiyo umechorwa picha ya nyota na mwezi” akaniambia.

    “Nitapaelewa tu” nikamwambia.

    Asubuhi ya siku iliyofuata tukasafiri sote kwenye boti. Tulipofika Pemba akanielekeza tena. Nikaenda mwenyewe katika huo mtaa.

    Kwa vile nilikwenda kwa miguu ili nisipotee nilitembea sana

    Mara kwa mara nilikuw a nawauliza watu niliokutana nao njiani kama wanamfahamu mganga huyo. Baadhi ya watu hao walikuwa wanamfahamu na wakanielekeza zaidi mtaa aliokuwa anaishi.

    Baada ya mwendo mrefu nikafika katika mtaa huo, nikawa naitafuta ile nyumba. Baada ya kuhangaika sana nikaiona. Ilikuwa kwenye kona na ilipakwa chokaa nyeupe.

    Alama kubwa iliyonipa moyo ni picha ya nyota na mwezi niliyoikuta kwenye mlango.

    Kama alivyonieleza yule mtu niliyesafiri naye, nyumba hiyo ilikuwa ya kizamani sana na ilikuwa kwenye hatari ya kuanguka kwani ilikuwa ni nyumba iliyojengwa kwa mawe na udongo ingawa ilipauliwa kwa bati. Bati hilo lilikuwa limeota kutu na kuchakaa.

    Nikaenda kwenye mlango na kubisha. Nilibisha mara mbili bila kupata jibu. Nilipobisha mara ya tatu nikajibiwa.

    “Karibu” Ilikuwa sauti ya mwanamke. Nilishaambiwa kuwa mgaga mwenyewe ni mwanamke.

    Baada ya sekunde chache mlango ukafunguliwa. Ndani kulikuwa kiza. Hata mtu aliyenifungulia mlango sikuweza kumuona vizuri.

    “Karibu ndani” Sauti ya mwanamke ikaniambia.

    Nikaingia. Kulikuwa na ukumbi mpana uliokuwa umetandikwa jamvi.

    “Karibu ukae kwenye jamvi”

    Nikakaa. Yule mwanamke naye akakaa kando yangu.

    “Pole kwa safari, naona umetoka mbali” akaniambia huku akinitazama. Sasa pale ndipo nilipomuona vizuri. Kumbe alikuwa Zena!

    Nilishituka sana nilipogundua kuwa mwanamke mwenyewe alikuwa Zena.

    Nilishindwa kuelewa kwanini amekuwa Zena wakati niliambiwa kulikuwa na mwanamke ambaye ni mganga.

    “Habari za huko?” Zena aliniuliza alipoona nimepigwa na butwaa.

    Niligeza haraka uso wangu nisitazamane naye. Nikawa natazama chini.

    “Nzuri” nikamjibu. Sauti yangu ilikuwa nzito ya mtu aliyetahayari.

    “Mbona umekuja huku, una shida gani?” akaniuliza huku akinitazama kwa makini. Nilikuwa nimeinamisha uso wangu lakini nilikuwa namuona kwa pembeni mwa macho yangu.

    Nilishindwa kujibu Swali lake kwa sababu sikujua ningemjibu nini. Nimjibu kuwa nimekwenda Pemba kufuata mganga na badala yake nakutana na yeye? Hapana.

    “Nimekuja kutembea tu” nikamwambia

    baada ya kushindwa kumueleza ukweli.

    “Umekuja kutembea tu huku Pemba?” Zena akaniuliza kwa sauti iliyoonesha kuwa hakuyaamini maneno yangu.

    “Ndio” nikamjibu.

    “Sasa umeshatembea na kuuona mji?”

    “Ndio”

    “Umeuonaje?”

    “Ni mji mzuri”

    “Kumbe unatembea hadi huku Pemba?’

    “Ni leo tu”

    “Umepanga kurudi lini?”

    “Nitarudi leo”

    “Si ulale uondoke kesho?”

    Nikatikisa kichwa.

    “Nitaondoka leo leo”

    “Nisubiri basi tuondoke sote”

    Zena akainuka. Aliingia kwenye chumba kimojawapo ambacho mlango wake ulikuwa wazi. Nikamuona anavaa baibui. Akachukua mkoba wake na kutoka.

    “Twendezetu” akaniambia kama vile tulikuja safari moja.

    Nikainuka na kumfuata. Tulitoka kwenye ile nyumba tukashika njia ya kuelekea bandarini.

    Wakati wote nilikuwa nikijiuliza kwanini nilimkuta Zena pale nyumbani. Huyo mganga mwenyewe alikuwa wapi?

    Ile ilikuwa ni miujiza ya ajabu ambayo sikuwahi kuiona katika maisha yangu.

    Matarajio yangu ya kumpata mganga wa kuliondoa tatizo langu yalififia kabisa moyoni mwangu. Huyu jini alikuwa amenizingira kila pembe.

    Tulipofika bandarini Zena alikata tikiti mbili za boti inayokwenda kasi. Boti hiyo ilikuwa inakwenda Dar. Siku ile hakukuwa na chombo chohote kinachokwenda Tanga.

    Tulipojipakia kwenye boti nilikaa na Zena siti zilizokuwa zimepakana. Tulisubiri kwa muda wa saa nzima kabla ya safari kuanza.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kweli kupambana na jini aina ya Zena ni kazi! Sasa alikuwa akinirudisha Dar. Niliamini kuwa alikuwa akijua kilichonipeleka Pemba ingawa hakuniambia. Kitu ambacho nilishindwa kuelewa ni jinsi nilivyomkuta yeye pale nyumbani kama vile ni kwake.

    Wakati boti iko katikati ya safari nilimuona Zena amelala usingizi kabisa. Nikawa namtazama. Alikuwa na weupe uliochanganyika na wekundu. Uso wake ulikuwa na pozi la kiarabu ingawa alionekana kuchanganya damu ya Kiafrika. Sikujua kama majini nao wanakuwa machotara kama binaadamu.

    Kwa uzuri alikuwa mzuri sana, sikuwahi kuona msichana mwenye mvuto wa sura na umbile kama yeye. Tatizo lake ni kwamba alikuwa jini tena jini mbaya mwenye vituko vilivyoshindikana.

    Hadi pale nilikuwa nimesalimu amri. Nilishasema kuwa Zena sitamuweza tena na hakukuwa na mganga yeyote atakayemuweza.

    Ghafla tuliona boti ikikata moto. Ikawa inasuasua juu ya bahari. Muda si muda ikapigwa na wimbi kubwa. Sote tulitikiswa. Hapo ndipo watu walipoanza kwenda mbio na kuifanya boti ilale upande mmoja.

    Baadhi ya abiria wakaanza kujitosa baharini. Nikaona sasa hali ilikuwa mbaya. Nilijikuta nikimuamsha Zena bila kupenda. Zena akaamka.

    “Nini. Mbona kuna hekaheka?” akaniuliza.

    “Boti inazama” nikamwambia.

    “Boti inazama?” akaniuliza kwa fadhaa.

    Kabla sijamjibu, ule upande wa boti uliokuwa unazama ukazidi kulala.

    “Duh ni kweli, twende tukaruke, tutakufa humu!” akaniambia huku akiinuka kwenye siti.

    Tulikwenda kwenye mlango wa boti tukatoka. Watu walikuwa wakiendelea kuchupa baharini.

    “Chupa!” Zena akaniambia.

    Laiti angejua jinsi ambavyo sikuwa nikijua kuogelea asingeniambia chupa.

    Upande wa pili wa boti nao ikaanza kuzama.

    “Chupa, boti inazama!” akaniambia tena.

    Sikuthubutu. Nilibaki kuitazama bahari.

    “Amour unasubiri kufa humu ndani ya boti?” Zena akaniuliza kwa hasira.

    Nikatikisa kichwa.

    “Siwezi kuogelea, nikiruka ndio nimekwisha!”

    “Mwanaume mzima unasema huwezi kuogelea, mimi mwanamke nisemeje?” akaniuliza.

    Sikuwa na jibu. Nikaendelea kutikisa kichwa changu.

    Sikujua ilikuwaje. Zena alinishika mkanda wa suruali yangu kwa nyuma kisha akanirusha baharini. Hadi leo nashindwa kujua alinirushaje.

    Kabla ya kutumbukia baharini, nilijiambia ule ulikuwa ndio mwisho wangu.

    Nilitanguliza mikono na kichwa, Nikazama chini kabisa.



    kisha nikarudishwa tena juu. Wakati natokeza juu nilimuona Zena akijirusha baharini. Alichupa kama samaki. Akawahi kunishika kabla sijazama kwa mara ya pili.

    Nilivamia mwili wake ili nijiokoe kwani pumzi zilikuwa zimeniishia.

    “Usinivamie, tutazama sote. Tuliza akili yako” akaniambia huku akielea juu ya maji.

    Niliendelea kumg’ang’ania.

    “Usining’ang’anie, tutazama sote. Shika miguu yangu. Usishike mwili wangu!” Zena alinipigia kelele. Sasa nilikuwa kama hayawani nisiyejielewa.

    Zena alipoona bado simsikilizi alinipiga ngumi ya shavu, nikamuachia na kuzama chini. Wakati niko ndani ya maji nikipelekwa chini, Zena alipiga mbizi akaniwekea mgongo wake kwenye kifua changu kisha akaibuka na mimi juu ya maji.

    ”Tulia kwenye mgongo wangu, ukifurukuta nakuacha. Nishike mabega yangu” akaniambia.

    Nikafanya vile alivyotaka.

    Zena akaanza kuogelea huku nikiwa kwenye mgongo wake. Yule msichana alikuwa hodari sana.

    Aliweza kuogelea kwa mwendo mrefu akiwa na mimi bila kunidondosha na bila kuonesha kuchoka.

    Ile boti iliyokuwa inazama tuliiacha mbali kabisa.

    Zena aliendelea kuogelea tu kama vile alikuwa na mashine iliyokuwa inampa nguvu. Nikakumbuka maneno ya watu wanaosema kwamba majini huzaliwa baharini. Nikahisi kuwa hiyo ndio sababu akawa na uzoevu mkubwa wa kuogelea.

    Hatimaye ile boti sikuiona tena. Sasa nikawa najiuliza tunaelekea wapi. Sikupata jibu. Jua lilikuwa linakuchwa kwa haraka upande wa magharibi na tayari lilionekana likitoa mionzi ya kimanjano iliyoashiria kuwa wakati wa magharibi ulikuwa unakaribia.

    Mbele yangu nikaona kitu kimejitokeza. Baadaye niligundua kuwa tulikuwa tunatokea kwenye kisiwa. Kilikuwa bado kiko mbali na sisi. Kwanza nilianza kuona majani ya miti yaliounda shada kubwa la rangi ya kijani. Halafu nilianza kuona msitu mkubwa.

    Kadiri tulivyokuwa tunakikaribia kisiwa hicho ndivyo nilivyoweza kukiona vizuri. Naam kilikuwa ni kisiwa. Sasa ardhi yake ilionekana waziwazi. Kilikuwa kisiwa kidogo kilichokuwa na msitu mkubwa wa miti.

    Tulipofika maji madogo Zena aliniambia niondoke mgongoni kwake.

    Sikumsikia vizuri, nilikuwa nimeendelea kumshikilia. Ile harufu ya udi wa mawaridi niliyokuwa nikisikia mgongoni mwake ilikuwa imenilewesha.

    “Ondoka bwana, mwenzako nimechoka!” akaniambia kwa sauti ya ukali.

    Nikajaribu kuishusha miguu yangu taratibu, taratibu, nikaona ninakanyaga mchanga lakini maji yalikuwa yakinifika kwenye kifua. Nikaanza kutembea kwa miguu nikiwa bado nimemshikilia Zena. Ilibidi nipate kitu cha kushika, vinginevyo maji yangeweza kunikupua.

    Niliendelea kutembea hadi maji yaliponifikia kiunoni ndipo nilipomuacha Zena. Sasa tulikuwa tukitembea pamoja. Nguo zetu zilitota chapa. Maji ya chumvi yalikuwa yakitutiririka mwilini.

    Tulifika ufukweni mwa kisiwa hicho. Fukwe yake ilikuwa nzuri yenye mchanga mweupe.

    “Hapa ni wapi?” nikamuuliza Zena.

    Zena aliyeonesha wazi kuwa alikuwa amechoka hakunijibu chochote, aliendelea kwenda hadi tukaingia kwenye ule msitu.

    Zena alitafuta sehemu iliyokuwa juu akapanda na kujilaza chini.

    “Oh leo nimechoka sana. Sijaogelea mwendo mrefu kama leo” Zena akajisemea peke yake akiwa amejilaza kichali chali.

    Baibui alilokuwa amevaa lililoa maji na kuonya kama kioo. Nguo aliokuwa amevaa ndani nayo ilikuwa ikionya kwa sababu ya kutota maji. Ngozi nyeupe ya mwili wa Zena iliyokuwa na malaika marefu ilikuwa ikionekana wazi wazi.

    Mimi nilikuwa nimeketi nikihema huku nikiyatembeza macho yangu kila upande wa kile kisiwa. Sikujua tulikuwa katika kisiwa gani na kilikuwa wapi.

    Pia sikujua tungeondokaje katika kisiwa hicho ambacho hakikuonesha dalili yoyote ya kuishi watu. Nilikuwa nikijiambia kama kutakuwa na wanayama wakali wanaweza kutudhuru.

    “Unangoja hizo nguo zako zikaukie mwilini mwako?” Zena akaniuliza.

    “Sasa nizifanye nini?”

    “Si uzivue?”

    “Nizivue nikae uchi?”

    “Kwani huna chupi?”

    “Acha tu, zitakauka humu humu”

    “Mimi nguo zangu ni nyepezi, zitakauka mara moja”

    Niliyapuuza yale maneno ya Zena. Akili yangu ilikuwa kwingine. Nilikuwa nikijiuliza jinsi tutakavyoondoka kwenye kisiwa kile.

    “Tutaondokaje hapa?” nikamuuliza Zena.

    Kabla ya Zena kunijibu nikaona kitu kikitokeza kwenye miti mbele yetu. Nilishituka nilipogundua kuwa lilikuwa joka kubwa na refu. Lingeweza hata kutumeza mimi na Zena kwa wakati mmoja.

    “Zena! Zena!” nikamuita Zena.

    Zena akainua kichwa na kunitazama.

    “Nini?’ akaniuliza.

    “Angalia kule!” nikamwambia huku nikimuonesha lile joka kwa kidole.

    Zena akapeleka macho yake na kuliona.

    “Sijakwambia lakini sasa nakwambia, hiki kisiwa ni cha majini. Lile si joka kama unavyoliona ni jini limejigeuza joka. Wako wengi tu hapa”

    Maneno yake yalizidi kunitisha.

    “Sasa kwanini tumekuja hapa?” nikamuuliza kwa taharuki.

    “Unawaogopa? Si majini wakubwa kama sisi, ni visubiani vya ovyo ovyo tu. Ngoja nitamfukuza”

    Lile joka lilikuwa limetusogelea, likitaka kupandisha kichwa chake juu ya ile sehemu tuliyokuwa.

    Zena akaanza kulifokea kwa lugha ya kikwao. Mimi nilisogea nyuma ya Zena kwa hofu. Zena akanyanyuka na kulifuata kabisa huku akiendelea kulifokea.

    Lile joka lilibaki pale pale likinitazama mimi.

    Zena akavua kiatu chake akakishika na kulipiga kichwani. Joka hilo likatoweka hapo hapo.

    “Shika” alinipa kile kiatu. Akaniambia.

    “Ukiona joka linakufuata lipige na hiki kiatu changu, litatokomea”

    “Halitanimeza?” nikamuuliza huku nikipokea kile kiatu.

    “Hapana”

    “Kumbe hapa mahali ni pa hatari namna hii?”

    “Wewe ndio umetaka tufike hapa”

    “Nimetaka mimi?”

    “Ndio”

    “Nilikwambia kuwa tuje hapa?”

    “Kwani wewe siku zote unajua mimi nataka nini kwako?”

    Hapo nikagwaya.

    Zena akaendelea kuniuliza.

    “Ulifuata nini Pemba?”

    Sikuwa na la kumjibu.

    “Sasa niambie utanioa niwe mke wako au bado hutaki?”

    “Nikishakuoa tutakwenda kuishi wapi?’ nikamuuliza.

    “Kule kule unakoishi wewe”

    “Turudi kule kwanza ndio tupange mipango ya ndoa, si hapa”

    “Nataka tukirudi niwe tayari ni mke wako”

    “Kwani tutakwenda kuoana wapi?” nikamuuliza Zena.

    “Mtu huolewa kwao na mimi utakwenda kunioa kwetu”

    “Kwenu wapi?”

    “Kwetu hukujui?”

    “Sikujui”

    “Kwetu ni ujinini”

    “Yaani tutakwenda kuoana kwenu ujinini?”

    “Ndio”

    “Sasa ungeacha kwanza nirudi nyumbani nikajiandae. Hatuwezi kuoana ghafla”

    “Wewe umekuwa mkaidi mara nyingi. Siwezi kukupa nafasi hiyo. Madhumuni yangu ya kukuleta hapa ni kuwa twende tukaoane. Muda umeshafika”

    Nikanyamaza kimya.

    Zena alikuwa akiendelea kuniambia.

    “Ile boti niliizamisha mimi kusudi ili nikulete hapa. Ninajua tukiwa hapa hutakuwa na ujanja wowote”

    Ndipo nilipogundua kuwa Zena alikuwa amenizunguka! Kumbe ile boti aliizamisha yeye ili anipate mimi…

    Kufika Kwetu pale kisiwani nilidhani nilikuwa nimesalimika na kifo, kumbe nilikuwa ninasubiriwa na matatizo mengine.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kama alivyoniambia Zena, ni kweli pale kisiwani nisingekuwa na ujanja wowote zaidi ya kusalimu amri.

    Lakini akili yangu bado ilikuwa haikubaliani na mawazo ya Zena. Kumuoa jini lilikuwa jambo ambalo sikuwa tayari nalo.

    “Sikiliza Zena, naona sasa unatumia jazba ambayo si nzuri” nikamwambia Zena. Lakini hataka kabla sijamaliza sentensi yangu au alinikatiza.

    “Kumbe ulitaka nifanye nini?”

    Sasa sauti yake ilikuwa ya hamaki.

    “Nilitaka unisikilize ninachokwambia”

    “Kipi?”

    “Turudi Tanga ili nijiandae kwa jambo hilo, kwanini wewe unachukulia nguvu?”

    “Nachukulia nguvu kwa sababu nimeshaakuona kuwa huko tayari kunioa”

    “Niko tayari, nani kakwambia kama siko tayari. Ninachotaka mimi unipe muda tu wa kujiandaa”

    “Amour usinidanganye, huko tayari. Kama ungekuwa tayari usingekwenda kumuoa yule mwanamke wako niliyemfukuza pale nyumbani”

    “Yule nilimuoa kwa sababu ndugu zangu walimtaka yeye lakini sasa nitawaambia kuwa nataka kuoana na wewe”

    “Usiniambie habari ya ndugu zako, nyote nyinyi ni kitu kimoja”

    “Mbona hutaki kunisikiliza Zena!”

    “Sitakusikiliza. Wewe ni muongo ingawa sipendi kukuita hivyo. Wewe hunitaki mimi wakati mimi nimekusaidia sana. Kwanza niambie ulifuata nini Pemba?”

    “Si nimekwambia kwamba nilikwenda kutembea”

    “Usinidanganye. Usinifanye mimi sina akili. Wewe ulikwenda Pe,mba baada ya kuambiwa kuna mganga ambaye ataweza kupambana na mimi”

    Nikajikuta natikisa kichwa changu kwa fadhaa.

    “Si kweli” nikamwambia lakini uso wangu ulikuwa umetahayari.

    “Unaona aibu mwenyewe kutokana na hila zako, Unadhani kuna mganga ataniweza mimi?”

    Nikabaki kimya. La kusema nilikuwa sina.

    “Sasa usinipotezee muda wangu, nataka jibu lako. Tutakwenda ujinini kuoana au hatutakwenda?” Zena akaniuliza.

    Nilikuwa nimeinamisha kichwa changu nikiwaza. Sikuwa na jibu la kumpa, nikabaki kutikisa kichwa kuashiria kutokukubaliana naye.

    “Amour nakuuliza tena, tutakwenda ujinini tukaoane au hatutakwenda?”

    Niliendelea kutikisa kichwa.

    “Una maana huko tayari siyo?”

    Sikumjibu.

    “Sasa mimi nakwenda zangu, nakuacha hapa hapa. Hutaniona tena”

    Nikainua uso wangu haraka ili nimwambie asiniache pale lakini Zena alitoweka ghafla kama upepo. Kama alivyoniambia sitamuona tena na kweli sikumuona tena!

    Nikatazama huku na huku, Zena hakuweko. Nikabaki peke yangu kwenye kisiwa kile cha majoka!



    Kile kiatu chake alichokivua na kulipiga lile joka nikabaki nacho. Mwenyewe amekwenda na kiatu kimoja.

    Nilipata hofu kweli kweli.

    Jua lilikuwa limeshakuchwa na kiza kilikuwa kinaingia. Nikajiuliza “nitafanyaje Amour?”

    Zena alikuwa ameshaniacha peke yangu. Nikawa nahisabu dakika zangu za kufa au kuliwa na majoka.

    Nikaondoka mahali pale nilipokuwa nakwenda kupanda juu ya mti nikiwa na kile kiatu. Nilikaa kwenye tawi moja nikawa naitazama bahari. Hakukuwa na mtumbwi wala ngarawa iliyokuwa ikipita. Bahari ilikuwa nyeupe.

    Kusema kweli nilijuta kufunga safari ile ya kwenda Pemba kufuata mganga. Na kama niliamua kwenda ningekwenda na ndugu yangu na si peke yangu kama nilivyofanya.

    Nilianza kusikia baridi mwilini, sikujua itakapofika usiku ingekuwaje.

    Nilitamani Zena anionee huruma aje anichukue. Lakini mawazo yangu yalikuwa sawa na dua la kuku. Hakuna aliyelisikia.

    Wakati nimekaa kwenye tawi nikiendelea kuwaza nikasikia majani yakichakachika juu ya ule mti kama vile kulikuwa na kitu kinatambaa.

    Nikainua uso wangu juu kutazama kulikuwa na nini.

    Nikashituka. Niliona kichwa cha joka kikiwa karibu yangu kabisa. Kumbe katika ule mti niliokuwa nimeupanda kulikuwa na joka ambalo sikuliona.

    Kile kiatu cha Zena nilikuwa nacho mkononi, nikakipiga kile kichwa. Nikadhani lile joka lingeniangukia lakini pale pale lilitoweka. Sikuliona tena.

    Nikagundua kuwa licha ya Zena kunikimbia alikuwa ameniachia silaha ya maana sana.

    Nikaangaza angaza juu ya ule mti kuona kama kulikuwa na joka jingine. Sikuona joka.

    Hata hivyo sikuamini. Kila wakati nilikuwa natazama tena.

    Kiza kiliendelea kushamiri na baridi ilizidi kuwa kali lakini sikuwa na la kufanya. Nilibaki kutetemeka tu.

    Nilijiambia kama nitakufa pale kisiwani maiti yangu haitapatikana. Mama yangu na kaka yangu hawatajua nimepotelea wapi na hawatajua kuwa mwenzao ni marehemu.

    Eti wakati nawaza vile nikapitiwa na usingizi ghafla. Nikalala pale pale juu ya mti bila kujitambua.

    Nikaota nimelala chumbani kwangu, mara nikaona mwanamke ametokea kwenye dirisha langu lakini alikuwa kama kivuli. Sikuweza kumuona sura yake. Akaniambia.

    “Ni mpaka uirithi pete ya Sulaiman Dauud na hutairithi mpaka uishuhudie damu ya kaka yako ikimwagika”

    Hapo hapo nikazinduka. Ile ndoto haikuwa ngeni kwangu nakumbuka katika kipindi cha mwaka mmoja nilishaiota zaidi ya mara tatu. Lakini sikujua maana yake.

    Wakati nazinduka niliona mawingu yakianza kun’gaa. Kumbe kulikuwa kunanaanza kupambazuka. Nikatambua kuwa nililala usiku kucha pale juu ya mti ingawa niliona nililala kwa muda mfupi.

    Wakati naangaza macho baharini nikaona boti moja kubwa inakuja kwa kasi. Nikashukuru ingawa sikujua ilikuwa boti ya kina nani.

    Boti ile ilikuja hadi maji madogo ikatia nanga. Nikaona watu watano wanashuka na kutembea kuelekea ufukweni. Walikuwa wamesega suruali zao ili zisitote.

    Mmoja wa watu hao alikuwa amebeba tenga kubwa kichwani. Nikasikia sauti kama ya mlio wa mbuzi.

    Watu hao walipofika ufukweni walitembea hadi kwenye ule msitu. Yule aliyebeba tenga akalitua chini. Ule mlio wa mbuzi uliendelea kusikika.

    Nikaona mbuzi mweusi anatolewa kwenye tenga hilo. Sikuweza kuona vizuri kilichokuwa kinaendelea isipokuwa niliona kama walikuwa wanamchinja yule mbuzi na kumuacha pale chini.

    Nikapata hisia kwamba watu hao walikuwa wanafanya kafara lakini ghafla nikaona wanaingia katika ule msitu.

    Baada ya muda wa kama nusu saa hivi wakaanza kutoka mmoja mmoja lakini kila aliyetoka alikuwa amebeba pembe nne za ndovu.

    Walikwenda nazo kwenye ile boti wakazipakia kisha wakarudia zingine.

    Walirudia mara kumi, zilikuwa pembe nyingi sana. Ile mara ya kumi waliobeba pembe walikuwa watu wawili. Nikahisi walikuwa wamemaliza pembe zao na kwamba walikuwa wanakwenda zao.

    Nikadhania tu kuwa wale watu walikuwa wafanya magendo na walikuwa wakificha pembe zao katika kisiwa kile.

    Nikaona nisiipoteze ile nafasi ingawa sikujua watu wale walikuwa wanaelekea wapi.

    Nikashuka haraka kwenye ule mti na kuwakimbilia.

    “Jamani naomba mnichukue!” nikawa nawapigia kelele.

    Watu hao walipoona ninawafuata huku nikiwaomba msaada wakasimama na kunisubiri.

    Nilipowafikia, mtu mmoja mfupi aliyekuwa amevaa pama jeusi akaniuliza.

    “Wewe nani na umetokea wapi?”

    “Mimi ni mwananchi niliyekuwa natokea Pemba nikielekea Dar kwa boti inayokwenda kasi ambayo ilizama jana” nikamwambia.

    “Boti ilizama jana mbona wewe upo hadi leo”

    “Nilinusurika baada ya kuogelea….”

    Kabla sijamaliza kile nilichotaka kumueleza akanikatiza.

    “Ulifuata nini kwenye kisiwa hiki?”

    “Niliogelea hadi nikafika hapa”

    “Tangu jana ulikuwa unafanya nini hapa?”

    “Nilikuwa nimekaa tu nikisubiri msaada”

    “Wewe ni muongo sana!”

    “Hapana. Ninachokieleza ni ukweli mtupu”

    “Wewe ni mpelelezi siyo, umekuja kutupeleleza sisi?”

    “Hapana, hapana. Mimi siwajui, nimewaona tu hapa. Ninachoomba ni msaada wenu tu”

    “Haya twende tukaingie kwenye boti”

    “Asante bwana, nakushukuru sana kwa maana nilikuwa sijui ningefikaje Tanga”

    Nilifuatana na wale watu hadi kwenye boti yao nikajipakia. Yule mtu aliyekuwa akinihoji ambaye alionekana kama mwenye mali alikuwa akiamrisha kila kitu ndani ya ile boti.

    Safari ikaanza. Nikadhani kwamba nilikuwa nimenusurika. Sikujua tulikuwa tunaelekea wapi na jinsi nilivyowaona watu wenyewe ni wakali nilishindwa kuwauliza.

    Nilikuwa nimeshaamua popote watakaponifikisha patatosha. Kama watanirudisha Pemba au kama watakwenda Unguja au Dar itakuwa sawa.

    Boti iliendelea na safari kwa kasi. Kitu kilichonishitua ni kwamba baada ya kukiacha kile kisiwa, yule mtu aliyekuwa amevaa pama jeusi alikwenda kukaa peke yake akatoa bangi na kuanza kuvuta.

    Moshi wa bangi ulienea kwenye boti ukawa unaniumiza kichwa lakini yule mtu hakujali kabisa. Alikuwa akiendelea kuvuta tu.

    Baada ya kwenda mwendo wa karibu kilometa thelathini tukaona boti nyingine inatufuata. Wale watu walipoiona ile boti walishituka.

    Yule mtu aliyevaa pama akakitupa kipisi cha bangi baharini kisha akanitazama na kuniambia.

    “Polisi wenzako wanatufuata, mimi nilishajua kuwa wewe ni mpelelezi!”

    “Polisi gani?” nikamuuliza.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Utawaona sasa hivi”

    Mazungumzo ya polisi yakaanza ndani ya boti huku wale watu wakinishutumu mimi kuwa ni mpelelezi niliyekuwa nimetumwa katika kile kisiwa kuwachunguza.

    Kumbe ile boti iliyokuwa inatufuata ilikuwa boti ya polisi wanamaji iliyokuwa kwenye doria.

    Upande mmoja wa moyo wangu nilipata hofu lakini kwa upande mwingine nilipata matumaini. Nilipata hofu kutokana na zile shutuma nilizokuwa ninazipata kutoka kwa wale watu kuwa mimi ni mpelelezi. Na nilipata matumaini kujua kuwa kulikuwa na polisi wanatufuata.

    Sikuwa na hofu na polisi hao kwa sababu sikuhusika na wafanya magendo hao ambao hata sikujua walikuwa wanaelekea wapi.

    Kadiri ile boti ilivyokuwa inatukaribia wale watu walikuwa wakihaha huku wakitukana.

    Boti ya polisi ilipotufikia polisi wanne waliingia kwenye ile boti. Polisi mmoja alikuwa ameshika bunduki.

    “Mnakwenda wapi?” Polisi aliyeshika bunduki akatuuliza.

    Polisi hao hawakupata jibu. Jamaa wote walikuwa kimya.

    Katika kukagua kagua ndani ya ile boti, polisi hao wakaziona zile pembe za tembo.

    “Kuna meno ya tembo mengi sana wanayasafirisha!” Polisi mmoja akawapigia kelele polisi wengine waliokuwa kwenye boti ya pili.

    Yule mtu aliyevaa pama aliingia kwenye kijichumba kilichokuwa ndani ya boti hiyo. Muda ule ule alitoka akiwa ameshika kitu kama chupa kubwa iliyokuwa na utambi uliokuwa ikiwaka moto, akairusha ile chupa kuelekea kwenye boti ya polisi. Ile chupa ilipotua chini ililipuaka kama bomu.

    Kitendo kile kilinishitua. Mara moja ile boti ya polisi ililipuka moto. Wale polisi walioingia kwenye boti niliyokuwemo walikuwa wameduwaa. Hapo hapo wakavamiwa na wale watu, wakapigwa na kufungwa kamba. Yule polisi aliyekuwa na bunduki alinyanganywa bunduki yake.

    Jambo lililonishitua zaidi ni kuwa hata mimi nilikamatwa nikafungwa pamoja na polisi hao.

    “Tutakwenda kuwatosa huko mbele ya safari” aliyekuwa amevaa pama akatuambia.

    “Lakini mimi ninahusikaje, mimi niliwaomba msaada tu kwanini mnataka kwenda kunitosa?” nikawalalamikia.

    “Wewe ndio mpelelezi uliyekuwa ukitoa taarifa kwa wenzako. Pale nilipokuwa nakupakia nilishakupangia kwenda kukutosa” Mwenye pama akaniambia.

    “Balaa gani hili jamani linalonikuta. Jana nilikaribia kufa, leo tena balaa jingine linaningoja. Nimekosa nini jamani!” nikalalamika peke yangu.

    Wakati huo ile boti ya polisi tulishaiacha mbali ikiendelea kuwaka.

    Mpaka jua linafika utosini ikiashiria ilikuwa saa sita mchana, boti ya watu hao ambao sasa niliwahisi walikuwa majambazi ilikuwa ikiendelea kukata maji.

    Nilikuwa nimeshafuta mawazo kwamba tulikuwa tunaelekea katika miji iliyokuwa karibu kama Pemba au Unguja. Nilihisi kwamba tulikuwa tunaelekea mahali kwingine kusikojulikana.

    Hofu ya kuuawa ilikuwa imenitawala. Wakati wote moyo wangu ulikuwa ukienda mbio. Sikujua kwamba tungeuawa au tungetoswa baharini saa ngapi.

    Mara nikamuona yule mtu aliyekuwa amevaa pama akitoka kwenye kile chumba kilichokuwamo ndani ya boti, akawambia wenzake.

    “Eneo hili lina papa wengi, tuwatose hapa hapa”

    Kauli yake ile ilinishitua. Ilikuwa kama nyundo ya moto iliyopigwa kwenye moyo wangu.

    Mapama aliposema hivyo aliwaagiza watu watatu wamuinue polisi mmoja na kumtosa. Polisi huyo alilalamika kuomba asitoswe lakini hakukuwa na aliyekuwa akimsikiza. Jamaa hao walimbeba na kumtosa baharini akiwa amefungwa kamba miguu na mikono.

    Mara moja tukaona damu kwenye eneo lile la bahari. Kipande kimoja cha mwili wa polisi huyo kiliibuka juu na kwenda na maji. Bila shaka kipande kingine kilikuwa kimeshamezwa na papa.

    Hapo hapo tukamuona papa upanga akibuka kutoka chini ya bahari na kuking’ata kipande kingine cha ule mwili na kuzama nacho baharini.

    Tayari jamaa hao walikuwa wameshambeba polisi wa pili ambaye kama mwenzake alikuwa akilalamika bila kusikilizwa, naye akatoswa.

    Polisi wa tatu naye akatoswa. Nikabaki mimi na polisi mmoja. Nilikuwa nikiomba toba kimoyomoyo ili nipate msamaha huko ahera ninakokwenda.

    Machozi yalikuwa yametosa kifua changu na yalikuwa yakiendelea kunitoka hasa nilivyoona vipande vya miili ya wale polisi ilivyokuwa ikidakwa na papa.

    Wale jamaa wakatufuata tena.

    Sikujua ilikuwa zamu ya nani, mimi au yule polisi?

    Jibu nililipata baada ya nusu dakika. Watu hao wakamshika mwenzangu. Bila shaka mimi waliniweka mwisho. Polisi huyo alibebwa juu juu. Ingawa alikuwa akipiga kelele, hakukuwa na aliyemjali. Kiasi cha kufumba na kufumbua tu akawa ametoswa baharini. Kwa vile alikuwa mnene na mzito kuliko wenzake waliokuwa wametoswa, alisababisha kishindo kukubwa, maji ya bahari yakaruka na kuingia kwenye boti!

    Wakati wote nilikuwa na matumaini kuwa wangewatosa wale polisi kwa kuamini kuwa mimi sikuwa mwenzao na ndio maana waliniacha.

    Lakini matumaini yangu yaliyayuka mara tu nilipowaona wale watu wakinifuata mimi baada ya kumtosa yule polisi wa mwisho,

    Nilipoona wananishika nikawambia.

    “Jamani, jamani mimi nina kosa gani. Kuwaomba msaada ndio kosa, mnataka mniue”

    Hawakunijibu na hawakuonesha kama walihitaji kunijibu, Walinibeba kama walivyowabeba wenzangu. Vile ambavyo mwili wangu haukuwa mzito walinichota kama takataka. Wakanipeleka kwenye ukingo wa boti.

    Kufika hapo waliniinua juu wakahesabu moja...mbili…

    Kabla hawajafika tatu, kuliibuka kitu kilichotokea baharini. Kiliibuka kwa nguvu na kwa kishindo huku kikitoa mlio uliofanana na mlio wa fataki iliyorushwa.

    Yale maji yaliyorushwa juu na kitu hicho yalitutosa wote. Ghafla kitu hicho kikatuvamia. Mimi niliachiwa nikaangukia ndani ya boti. Wale watu pia walianguka na kulaliwa na kitu hicho kizito kilichotua ndani ya boti.

    Nilikuwa nimefungwa kamba mikono na miguu. Nilipoanguka sikuweza kusimama ila niliweza kujigeuza ili nikione kitu hicho kilichoibuka kutoka baharini na kuvamia ndani ya boti ile.

    Nilishindwa kuamini macho yangu! Lilikuwa dude kubwa kama joka lililokuwa na mikono yenye vidole vyenye kucha ndefu. Urefu wake ulikuwa kama guzo la umeme. Lilipokuwa ndani ya ile boti lilikuwa limejikunja. Mwili wake ulikuwa na magamba makubwa kama ya samaki.

    Kwa kutumia kucha zake lilimvamia mtu mmoja na kuruka naye juu kisha likajitosa baharini likiwa na mtu huyo.

    Sote tulikuwa tumetaharuki na hatukujua ni jambo gani lilitaka kutokea. Wakati wale watu wanajiinua pale chini, joka hilo likaibuka tena likiwa halina mtu. Likavamia mtu mwingine na kuruka naye kisha likajitosa baharini.

    Watu hao wakawa wanapigana vikumbo ndani ya boti kutafuta pa kujificha. Kutahamaki joka hilo likatokea tena, likamnyakua mtu mwingine na kuzama naye chini ya bahari. Watu wote wakamalizwa nikabaki mimi na Mapama

    Mapama alikuwa akihangaika akijua kwamba joka hilo litaibuka tena na kumchukua yeye.lakini dakika zikapita hatukuliona. Kwa sababu ya hofu na kujiona amebaki peke yake mtu huyo alikuja kunifungua zile kamba.

    “Njoo huku” akiniambia akitangulia kuingia katika kile kijichumba kilichokuwa ndani ya ile boti.

    Nikainuka na kumfuata. Mikono yangu ilikuwa imekufa ganzi kutoka na kufungwa kamba kwa muda mrefu. Nikawa ninainyooshanyoosha.

    Ndani ya chumba hicho kulikuwa na kioo cha kutazamia mbele. Pia kulikuwa na sukani na mitambo ya boti.

    “Samahani bwana, naona tumebaki sisi wawili tu. Sijui lile lilikuwa joka gani na limetokea wapi?” Mapama akaniambia kwa hofu.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog