Search This Blog

MWANAMKE JINI - 4

 







    Simulizi : Mwanamke Jini

    Sehemu Ya Nne (4)





    ILIPOISHIA

    Nilishindwa kuamini macho yangu! Lilikuwa dude kubwa kama joka lililokuwa na mikono yenye vidole vyenye kucha ndefu. Urefu wake ulikuwa kama guzo la umeme. Lilipokuwa ndani ya ile boti lilikuwa limejikunja. Mwili wake ulikuwa na magamba makubwa kama ya samaki.

    Kwa kutumia kucha zake lilimvamia mtu mmoja na kuruka naye juu kisha likajitosa baharini likiwa na mtu huyo.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Sote tulikuwa tumetaharuki na hatukujua ni jambo gani lilitaka kutokea. Wakati wale watu wanajiinua pale chini, joka hilo likaibuka tena likiwa halina mtu. Likavamia mtu mwingine na kuruka naye kisha likajitosa baharini.

    Watu hao wakawa wanapigana vikumbo ndani ya boti kutafuta pa kujificha. Kutahamaki joka hilo likatokea tena, likamnyakua mtu mwingine na kuzama naye chini ya bahari. Watu wote wakamalizwa nikabaki mimi na Mapama

    Mapama alikuwa akihangaika akijua kwamba joka hilo litaibuka tena na kumchukua yeye.lakini dakika zikapita hatukuliona. Kwa sababu ya hofu na kujiona amebaki peke yake mtu huyo alikuja kunifungua zile kamba.

    “Njoo huku” akiniambia akitangulia kuingia katika kile kijichumba kilichokuwa ndani ya ile boti.

    Nikainuka na kumfuata. Mikono yangu ilikuwa imekufa ganzi kutoka na kufungwa kamba kwa muda mrefu. Nikawa ninainyooshanyoosha.

    Ndani ya chumba hicho kulikuwa na kioo cha kutazamia mbele. Pia kulikuwa na sukani na mitambo ya boti.

    “Samahani bwana, naona tumebaki sisi wawili tu. Sijui lile lilikuwa joka gani na limetokea wapi?” Mapama akaniambia kwa hofu.

    SASA ENDELEA

    “Nadhani limekuja kuwaua kutokana na ule unyama wenu wa kututosa baharini bila hatia”

    “Sio mimi, ni wale jamaa. Mimi sikuweza kuwazuia”

    Nikaona yule mtu alikuwa akijitetea kwa kusema uongo wakati yeye ndiye aliyeamrisha tutoswe.

    Sikutaka kumsuta kwa sababu hata mimi nilikuwa nimepata hofu na sikuwa nikijua hatima yangu.

    “Lakini sidhani kama litakuja tena” nikamwambia kumpa moyo. Hata hivyo nilijisemea tu bila kuwa na uhakika.

    Mapama alikuwa akiendesha lile boti huku akiwa matu matu. Kila mara alikuwa akitupa macho pande zote za boti. Nilijua alikuwa akihofia lile joka ambalo hata mimi liliniweka katika hali ya wasiwasi.

    “Tuombe Mungu. Tukinusurika tutatajirika” Mapama akaniambia.

    “Kwani tunaelekea wapi?” nikamuuliza.

    “Tunakwenda Somalia”

    “Kumbe mlikuwa mnakwenda Somalia?”

    “Mnunuzi wa hizi pembe yuko Somalia, ndio tulikuwa tunampelekea”

    “Ni mali ya nani?”

    “Mwenyewe yuko Dar. Mimi ndiye msimamizi wake na mmiliki wa hii boti. Mara kwa mara ananituma kupeleka pembe zake Somalia”

    “Huwa mnazihifadhi kwenye kile kisiwa?”

    “Pale ndio tunazificha tunapozikusanya kutoka kwa majangili”

    “Mnapokwenda pale mnachinja mbuzi kwa ajili ya nini?’

    “Kile kisiwa kinakaa majini. Hivyo tunapofika tunawapa kafara ili wasitudhuru. Na wewe ulifuata nini pale?”

    “Pale nilifika jana kwa kogelea. Mimi nilikuwa ninatoka Pemba kwenda Dar. Boti yetu ilizama.”

    “Ndiyo nilisikia. Kwa hiyo ulilala pale pale?’

    “Ndiyo nililala juu ya mti. Sasa nilipowaona leo asubuhi nikawafuata kuwaomba msaada lakini inaelekea hamkunielewa”

    “Unajua hii kazi ni ya siri na ya hatari, wale wenzangu walipokuona walidhani wewe ni mpelelezi ulikwenda pale kufanya uchunguzi”

    Jamaa yule alikuwa akiwasingizia wenzake kila kitu wakati yeye ndiye aliyekuwa akinituhumu.

    “Sasa ukifika Somalia unarudi lini huku Tanzania”

    “Tukifika tu tunapakua huu mzigo na kuupakia kwenye boti nyingine halafu tunarudi”

    “Hiyo boti tutaikuta wapi?”

    “Tukiingia Somalia tu tunaikuta inatusubiri”

    “Halafu hizi pembe zinapelekwa wapi?’

    “Zinasafirishwa kwa meli na kupelekwa nchi za kiarabu. Waarabu wanatengezea mipini ya majambia”

    Sikuwa nikijua kuwa pembe za ndovu hutengezwa mipini ya majambia. Hata hivyo niliyaacha yale mazungumzo ya pembe. Dukuduku langu lilikuwa ni kurudi nyumbani.

    “Tutafika leo huko Somalia?” nikamuuliza.

    “Hapa tuko katika bahari ya Mombasa nchini Kenya. Mpaka ikifika saa kumi na moja alfajiri tutaingia Somalia”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Eh! Kumbe safari bado ni ndefu?”

    “lakini tumeshafika nusu ya safari yetu”

    “Kama ni kurudi itakuwa kesho”

    “Kesho si mbali. Sasa hivi jua litakuchwa, usiku utaingia”

    Mapama aliposema hivyo alitoa kicheko cha kujilazimisha akaondoka kwenye sukani baada ya kuitegesha muelekeo aliokuwa anautaka. Akafungua kabati lililokuwa humo ndani na kutoa sufuri iliyokuwa imefunikwa.

    Aliiweka kwenye kimeza kisha akafunua ule mfiniko. Ndani ya sufuria hiyo mlikuwa na pilau na vipande vya nyama. Sijui ilikuwa nyama ya nini.

    Akapakua ile pilau kwenye sahani na kuniambia.

    “Tule”

    Kusema kweli nilikuwa na njaa lakini zile nyama ziliniogopesha kwa sababu zilikuwa nyingi na sikujua zilikuwa nyama za mnyama gani kwani zilikuwa na mafuta mengi.

    “Hizi ni nyama za nini?” nikamuuliza.

    “Nyama ya nyati, ni tamu sana. Hebu onja”

    Aliokota kipande cha nyama bila kuosha mkono akanipa.

    Alinishangza sana. Mikono yake ilikuwa imeshika kila kitu. Imeshika magwanda ya polisi waliowatosa baharini. Imeshika mapembe ya ndovu. Imeshika sukani ya boti. Imeshika bangi…loh! Hawa watu wachafu kweli!

    Alipoona nimesita nikimtazama akagutuka na kuinuka.

    “Ngoja nioshe mkono” akaniambia.

    Aliosha mkono kwa kutumia maji yaliyokuwa yamewekwa kwenye dumu.

    “Na wewe njoo uoshe mikono yako” akaniambia.

    Wakati wote nilikuwa nikisema na moyo wangu kuhusu kile chakula. Nilikuwa nikijiuliza nile kile chakula au nisile. Ukweli ni kwamba nilikuwa na njaa na njaa haina ustaarabu. Ikikushika unaweza kula hata kisocholika. Japokuwa kwanza nilisita sita lakini hatimaye niliinuka kwenda kuosha mikono.

    Baada ya kuosha mikono tukarudi pale tulipokuwa.

    “Kula” Mapama akaniambia.

    Tukaanza kula. Pilau ilikuwa ikinuka moshi wa kuni. Nikahisi kwamba waliipika wao wenyewe kwa kutumia kuni walizoziokota fukweni mwa bahari..

    Kwa sababu ya njaa niliyokuwa nayo nilikula sana mpaka nikahisi kwammba ningevimbiwa. Pilau ilikuwa nyingi hatukuimaliza.

    Nilimuacha Mapama akiendelea kula.

    “Ukiwa katika hali ya baridi unatakiwa ule sana” Mapama aliniambia.

    Tonge zake zilikuwa kubwa na nilihisi alikuwa akimeza bila kutafuna.

    Alipotosheka na yeye aliiacha. Akairudisha sinia kwenye kabati.

    Baada ya kuosha mikono Mapama alinipa maji ya kunywa nikayanywa. Na yeye akanywa.

    “Sasa baridi hatutaisikia. Tunaweza kuendelea na safari” Mapama akaniambia.

    Tukakaa na kuendelea kuzungumza. Mara moja moja alikuwa akitazama mitambo. Nilikuwa nimejifunza kwamba boti haikuwa ikiendeshwa kama gari.

    Haihitaji kushikiliwa sukani wakati wa kuendesha. Unaweza kuweka muelekeo wako na ukaiacha iende yenyewe.

    Ndivyo Mapama alivyokuwa akifanya. Hatimaye Mapama alianza kusinzia. Alikuwa akisinzia huku akishituka.

    “Nikuache uangalie, mimi najinyoosha kidogo” akaniambia.

    Nikajua kuwa pilau aliyokuwa ameila kwa wingi ilikuwa imemlewesha.

    “Wewe lala, baadaye nitakuamsha” nikamwambia.

    Mapama akajitupa chini. Baada ya muda kidogo nilimsikia akikoroma.

    Huku boti ilikuwa ikiendelea na safari. Masaa yalipita. Saa yangu ilikuwa imesimama kutokana na kuingia maji ya chumvi, sikuweza kujua ilikuwa saa ngapi.



    Mawazo yangu yalikuwa ni kurudi kwetu salama. Nilijiambia Zena alikuwa amenifikishia mkasa wa kutatanisha sana ambao sikutegemea kama ungenitokea.

    Niliamini kuwa siku zangu za kufa bado zilikuwa mbali, vinginevyo ningelikwishakufa.

    Kama nisingekufa kwenye ile ajali ya meli, ningekufa wakati Zena ananikokota baharini. Na kama nisingekufa baharini, ningekufa kwenye kile kisiwa chenye majoka na baridi.

    Lakini bado, japo nilinusurika kote, wale washenzi wenye ile boti wangeniua kama walivyowaua wale polisi waliowatosa. Na kama hawakuniua ningeuliwa na lile joka lililowaua watu wote na kumbakisha Mapama na mimi. Mpaka muda ule nilishindwa kujua joka lile lilitoka wapi na pia nilishindwa kujua jinsi nilivyonusurika

    .

    Kusema kweli niliona kunusurika kwangu kulikuwa kwa ajabu sana.

    Wakati nikiwa kwenye mchanganyiko huo wa mawazo huku macho yangu yakitazama mbele tunakoelekea, niliona kitu kama kimulimuli kikielekea upande wetu. Nikashituka na kuangaza macho vizuri.

    “Nini kile?” nikawa najiuliza kimoyo moyo.

    Baadaye kidogo niligundua kuwa ilikuwa boti iliyokuwa na kimuli muli na ilikuwa na maandishi yaliyosomeka POLISI KENYA.

    “Mama yangu we!”

    Kwa haraka nikamuamsha Mapama.

    “Hebu amka uone!”

    “Nini?” Mapama aliniuliza akiwa bado amefumba macho.

    “Polisi. Kuna boti ya polisi inatuufuata. Amka!” nikamwambia.

    “Polisi?”

    “Tunafuatwa na boti ya polisi!”

    Mapama akainuka.

    “Iko wapi?” akaniuliza.

    “Inakuja, imewasha kimulimuli. Simama uione”

    Mapama akainuka na kuitazama ile boti kwenye kioo. Nilidhani angeanza kubabaika kama nilivyokuwa nikibabaika mimi. Badala yake nilimuona akiizima boti na kujipekua mifukoni. Alitoa burungutu la pesa za Kenya akalishika mkononi.

    “Usiogope” akaniambia na kuongeza.

    “Watakwenda zao sasa hivi”

    Ile boti ya polisi ikatufikia. Ikawa ubavu kwa ubavu na boti yetu. Mapama akalirusha lile burungutu la noti kwenye ile noti. Polisi mmoja akalidaka. Hapo hapo nilimsikia akisema.

    “Safari njema”

    Mapama akaiwasha boti. Tukaendelea na safari. Ile boti nayo ikaelekea upande mwingine.

    “Wale wanataka pesa tu” Mapama akaniambia na kuongeza.

    “Kila tunapokuja huku tajiri wetu anatupa pesa maalum kwa ajili ya kuwapa polisi wa Kenya wanaofanya doria baharini. Wao wenyewe wanajua, wakiiona hii boti wanafuata pesa tu. Hawakagui kitu”

    “Mimi nilikuwa na wasiwasi sana. Nilijua tutaishia polisi”

    “Hapana. Hizi ni kazi zetu za kila siku, lazima tujuane na polisi. Huwezi kuvuka kwenda Somalia bila kukupamba nao”

    “Kile kimulimuli kilinitisha kweli”

    “Ile ni mikwara tu ya kutaka pesa. Hebu iangalie kama utakiona tena kimulimuli”

    Nikatazama upande ule ilikoelekea ile boti. Sikuona kimulimuli wala sikuiona boti yenyewe.

    “Boti yenyewe haionekani tena”

    “Ni kwa sababu wamekizima kimulimuli”

    “Huko Somali itakuwaje sijui?”

    “Hakuna tatizo. Huyo tunaempelekea huu mzigo ni mtu mzito sana. Serikali pia inamjua”

    Baada ya hapo tukabaki kimya.

    Hatimaye aflfajiri ilianza kuchomoza. Sikuona dalili yoyote ya kufika Somalia. Usingizi ukaanza kuniuma.

    “Uliniambia tutaingia Somalia wakati wa alfajiri” nikamwambia Mapama.

    “Bado kidogo, usiwe na wasiwasi”

    “Nasikia usingizi” nikamwambia.

    “Lala kidogo”

    Nikajilaza pale chini. Usingizi ukanichukua hapo hapo.

    Mpaka nakuja kuzinduka lilikuwa jua la utosi. Mapama ndiye aliyeniamsha. Boti ilikuwa imesimama na kulikuwa na boti nyingine kubwa iliyokuwa imesimama kando ya ile boti tuliyokuwamo. Ilikuwa boti kubwa na nzuri.

    “Tumeshafika?” nikamuuliza Mapama.

    Sikujua kabisa kuwa Mapama angenigeuka na kunisaliti kwa magaidi..

    Bila shaka, zile boti ndio zilikuwa zimekutana. Ile boti ya pili ilikuwa ndiyo ile ambayo Mapama aliniambia tutakutana nayo tutakapoingia Somallia ili ifaulishe ule mzigo wa pembe za ndovu.

    Wakati ule namuuliza Mapama kama tumeshafika, niliona mtu mmoja akitoka katika boti ile ya pili na kuingia katika boti ya Mapama. Alikuwa kijana. Ingawa alikuwa mwembamba alionekana kunawiri na alivaa mavazi yalliyompendeza japo shati alilovaa lilionekana kubwa kutokana na wembamba wake.

    Alikuwa Msomali mweusi mwenye nywele za singa. Mkono mmoja alikuwa ameshika kichanga cha mirungi aliyokuwa akitafuna na mkono mwingine alishika sigara iliyokuwa ikifuka moshi.

    Katika kiganja cha mkono wake wa kushoto alivaa pete kubwa iliyokuwa inang’ara.

    Niliukadiria umri wake kutozidi miaka thelathini na mitano. Alikuwa amenizidi kiumri kidogo.

    Kijana huyo alisalimiana na Mapama aliyekutana naye nje ya kile kijichumba nilichokuwemo. Nilimshangaa Mapama kwa jinsi alivyokuwa ametaharuki kiasi kwamba alipuuza hata kunijibu nilipomuuliza kama tumeshafika. Alikuwa amebadilika kabisa. Niliona kama hakuwa mwenzangu tena.

    Aliposalimiana na yule msomali alimuonesha ule mzigo wa Pembe. Msomali huyo aliutazama kisha akamuuliza.

    “Wenzako wako wapi?”

    “Nilikuja nao lakini tulipata matatizo makubwa”

    “Matatizo gain?”

    “Nitakueleza. Wambie jamaa wafaulishe huu mzigo”

    Msomali huyo alitumia lugha ya kisomali kuwambia wasomali wenzake waliokuwa katika ile boti ya pili waingie katika boti ya Mapama na kufaulisha ule mzigo. Wasomali hao walioonekana kama wapagazi wakaingia na kuanza kazi.

    Mapama na yule msomali niliyemdhania kuwa ndiye tajiri wa ule mzigo wakaingia katika ile boti nyingine. Sikujua walikwenda kuzungumza nini. Baada ya muda Mapama alirudi peke yake na kuniambia.

    “Yule jamaa anataka kukuona?”

    “Jamaa gani?” nikamuuliza.

    “Yule msomali niliyekuwa nazungumza naye”

    “Kwani mimi nahusikaje?”

    “Sasa utakwenda au utaleta ubishi?” Mapama akaniuliza kwa ukali.

    Kabla sijamjibu, Msomali mwenyewe akatokeza kwenye ile boti na kuninyooshea mkono kama ishara ya kuniita, nikaenda. Niliingia katika ile boti akanishika mkono na kuniingiza katika chumba kilichokuwa katika boti yake.

    Chumba hicho kilikuwa kikubwa kuliko cha boti ya Mapama na kilikuwa kizuri kilichozungukwa na kuta za vioo. Ndani kilikuwa na sehemu ya kulala na makochi ya kukalia.

    “Karibu, kaa hapo” Msomali akaniambia akinionesha moja ya makochi yaliyokuwa katika kile chumba.

    Nikakaa.

    “Asalaam alaykum” Msomali akaniambia huku akiketi upande wa pili wa chumba hicho.

    “Waalaika Salaam” nikamjibu kwa sauti iliyonywea huku nikimtazama usoni kwake.

    “Nimeelezwa na Nahodha kuhusu wewe na mkasa uliowatokea mlipokuwa mnakuja. Ameniambia kulitokea joka kama nondo na kuwaangamiza wenzake, ni kweli?”

    “Ni kweli”

    “Kwani walitaka kukufanya nini?”

    “Walitaka kuniua”

    “Wapumbavu wale, mtu unaomba msaada wanataka kukuua. Sasa hilo joka lilitoka wapi?”

    Nikabetua mabega yangu.

    “Sijui”

    “Bila shaka hilo ndilo lililokuokoa usiuawe, ungekuwa umeshatoswa na kuliwa na papa”

    Hapo sikumjibu kitu.

    “Wewe unaitwa Umar?” Msomali akaniuliza.

    “Hapana”

    “Unaitwa Amiri?”

    “Hapana”

    “Basi utakuwa unaitwa Amour”

    Nikamkubalia.

    “Ndio naitwa Amour, umejuaje?”

    Msomali huyo akacheka. Badala ya kunijibu akaniambia.

    “Nataka twende Somali mara moja”

    Nikashituka na kumuuliza.

    “Kwani hapa tuko wapi?’

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hapa ni Somalia, nina maana nataka twende Mugadishu”

    “Kufanya nini?”

    “Nitakuwa na kazi na wewe”

    “Mimi nataka kurudi. Nilishamwambia Nahodha akishafaulisha mzigo wake turudi”

    “Sasa amri ni yangu mimi si ya Nahodha. Mimi nataka twende Mugadishu”

    “Mimi sitakwenda huko”

    Msomali huyo hakunisikiliza akainuka na kutoka katika kile chumba. Na mimi nikainuka na kumfuata.

    Alipoona nimetoka alihamaki akaniuliza.

    “Unataka kuleta ubishi?”

    “Hapana”

    “Nani amekuamrisha utoke?”

    “Nilikwambia sitakwenda Mugadishu, nahitaji kurudi”

    Msomali huyo hakusema kitu tena, alitia mkono ndani ya shati lake akatoa bastola na kunielekezea.

    “Sasa chagua moja, nikutoe roho au baki kwenye hii boti!” akaniambia kwa hasira.

    Nikanywea hapo hapo.

    “Nenda kakae”

    Ikabidi nirudi kwenye kile chumba. Nilijua kama nitaendelea kubishana naye anaweza kuniramba risasi. Wasomali hawa hawana huruma, kuna wengine hawana utu kabisa.

    Nikakaa kinyonge kwenye kohi huku macho yangu yakimtazama yule Msomali kwa macho ya kulaani. Nikamuona mapama akiingia kwenye ile boti.

    Akasimama na yule Msomali na kuzungumza naye kwa kirefu. Sikuweza kusikia walichokuwa wanazungumza. Mara moja moja Mapama alikuwa akinitazama. Nilikuwa nikimuonesha ishara ya kumuita ili nimuulize mbona ananigeuka.

    Lakini Mapama licha ya kuona kuwa nilikuwa ninaashiria kumuita hakunijali hata chembe.

    Pembe za ndovu zilikuwa zikiendelea kingizwa kwenye boti hiyo. Kazi ilipokwisha, Msomali aliingia katika kile chumba akafungua dawati mojawapo na kutoa mfuko ambao alitoka nao.

    Ule mfuko ulikuwa na pesa. Sikujua zilikuwa pesa za wapi isipokuwa niliona Msomali akitoa vitita vya noti na kumhesabia Mapama. Mapama naye alizitia pesa hizo kwenye mfuko wa ngozi aliokuwa ameushika kisha nikaona wanaagana kwa furaha.

    Hapo ndipo nilipotoa sauti nikamuita.

    “Nahodha!”

    Nilimuita zaidi ya mara tatu lakini hakunipatiliza akatoka kwenye ile boti na kuingia kwenye boti yake. Yule Msomali akaingia kwenye kile chumba. Bastola yake ilikuwa bado mkononi ingawa aliishika kwenye mtutu.

    Boti ya Mapama ikawashwa moto. Nikajua kuwa Mapama alikuwa ameshaniuza kwa wasomali hao. Kwa lugha nyingine ilikuwa sawa na kusema kuwa Nilikuwa nimetekwa nyara na kupelekwa mahali bila hiyari yangu.

    Boti ya Mapama ikaondoka, ilikata kona ndefu na kugeuka ilikotoka. Nikaachwa mikononi mwa wasomali.

    Nilikuwa nimetaharuki na akili yangu iliniruka. Boti ya wasomali ikawashwa, nayo ikaondoka kuelekea Somalia.

    Sikujua Mapama alikuwa amezungumza nini na yule msomali na pia sikujua walikuwa wananipeleka Somalia kwa ajili gani.

    Pia nilikuwa nimeshangazwa na jinsi msomali huyo alivyolitambua jina langu ambalo sikuwahi kumtajia hata Mapama.

    Kijana huyo wa kiosamali alikuja kukaa kando yangu na kuendelea kutafuna mirungi yake. Bastola yake aliipachika kiunoni. Bila shaka alifanya hivyo mbele yangu ili kunionya nisimletee ukaidi.

    Lakini ukiacha muda ule aliponichomolea bastola hiyo ambapo alionesha kukasirika, uso wake ulikuwa wa kirafiki wakati wote.

    “Mimi naitwa Abdi” akaniambia wakati akiendelea kutafuna mirungi kisha akaniuliza.

    “Unakula mirungi?”

    Nikatikisa kichwa. Mdomo ulikuwa mzito kumjibu.

    “Najua wewe ni mzaliwa wa Tanga lakini sijui unaishi sehemu gani?” akaniuliza.

    Swali lake hilo nalo lilinishangaza. Alijuaje kuwa mimi ni mzaliwa wa Tanga?

    “Ninaishi sehemu inayoitwa Msambweni” nikamjibu.

    “Wazazi wakao wako wapi?”

    “Baba yangu alikwishakufa, mama yangu ndio yupo”

    Msomali huyo alinikubalia kwa kichwa.

    “Unafanya shughuli gani?”

    “Nimeajiriwa katika shirika moja linaloitwa CTC”

    “Najisikia ni mwenye furaha sana kukutana na mtu kama wewe”

    “Umelitambuaje jina langu pamoja na mahali nilipozaliwa?” nikamuuliza.

    Badala ya kunijibu aliangua kicheko.

    “Nilikuwa nakisia tu kumbe nilipatia”

    “Haiwezekani ukisie halafu iwe sawa”

    “Amour sina jibu jingine la kukupa kwa sasa”

    “Uliwahi kufika Tanga?”

    Abdi akatikisa kichwa.

    “Sijawahi”

    “Kwanini unalazimisha twende Somalia?”

    “Ni kwa sababu za kiudugu na kiurafiki tu. Utakuwa huko kwa muda tu halafu utarudi kwenu na kama utapenda kuendelea kuishi huko huko nitakupatia nyumba, kazi na gari”

    “Kwa vyovyote vile itabidi nirudi, mama yangu na ndugu zangu hawajui niko wapi”

    “Basi utarudi”

    Boti iliendelea kusonga mbele. Baada ya mwendo wa kilometa tano hivi tukakutana na meli iliyokuwa imetia nanga. Boti ilikwenda kusimama ubavuni mwa meli.

    Abdi aliniacha akatoka kwenye kile chumba. Kuna ngazi iliyoshushwa kutoka kwenye meli. Abdi alipanda ngazi hiyo akaingia ndani ya meli. Baada ya muda kidogo alishuka akiwa na maafisa wawili wa meli hiyo ambao niliwatambua kutokana na mavazi yao.

    Waliyakagua yale meno ya tembo kisha nikaona krini ya meli inashushwa kutoka kwenye meli. Yale meno ya tembo yalikuwa yamepangwa kwenye turubai. Turubai hilo lilikuwa na vipete vinne vilivyowekwa kwenye pembe nne za turubai hilo. Kamba ikapitishwa kwenye vipete hivyo kisha ikapachikwa kwenye mkono wa krini.

    Turubai likavutwa juu pamoja na pembe zake. Zilivutwa juu kuupita usawa wa meli kisha zikaingizwa ndani ya meli.

    Abdi pamoja na wale maafisa wawili wa meli walirudi melini. Walipoteza muda wa karibu saa nzima kabla ya Abdi kurudi akiwa peke yake.

    Aliingia kwenye kile chumba akiwa na mfuko uliotuna ambao aliuweka kwapani. Akafungua dawati mojawapo na kuuweka.

    “Hizi ni pesa” akaniambia bila kumuuliza.

    Sikumjibu kitu. Akarudi kuketi pale alipokuwa.

    “Zile pembe zinakwenda Oman kwa waarabu” akaniambia lakini mimi bado nilikuwa kimya. Kitendo kile cha kunipaleka Mogadishu kwa lazima kilikuwa kimenifadhaisha sana.

    Sikuwa nimeamini zile sababu zake kwamba alinipeleka kwa sababu za kiudugu na kiurafiki. Sikuwa na udugu naye wala urafiki naye na hatukuwa tukijuana zaidi ya kukutana siku ile.

    Nilihisi kuna kitu ambacho alizungumza na Mapama ndio wakapanga niende Mogadishu. Sasa sikujua kama walikuwa wanakwenda kuniua au kunifanya nini.

    Wakati niko katika lindi la mawazo nilianza kuona mataa kwa mbali. Ilikuwa ni bandari ya Mogadishu. Tulifika katika gati moja boti ikasimama.

    Abdi akasimama alifungua dawati akauchukua ule mfuko wake wa pesa akaniambia.

    “Tushuke”

    Tulishukia kwenye gati. Tulikuta gari ndogo ya kifahari ya rangi nyekundu ikitusubiri.

    Abdi alifungua mlango wa nyuma wa gari hilo akaniambia nijipakie. Nikajipakia.

    Yeye alifungua mlango wa mbele kando ya dereva akajipakia. Gari ikaondoka.



    “Tunakwenda wapi?” Mtu aliyekuwa akiendesha alimuuliza Abdi tulipoingia kwenye mitaa.

    “Nipeleke hotelini kwangu nikamuweke mgeni wangu halafu utaniachia gari”

    Hapo ndipo nilipoliona na kulijua jiji la Mugadishu. Ilikuwa ni kabla ya serikali ya Somalia ya Rais Siad Barre kupinduliwa na kuanza kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyoendelea hadi leo hii na kuzua vikundi vya kigaidi.

    Jiji lilikuwa zuri na la kisasa. Nililifananisha sana na jiji la Nairobi ambalo niliwahi kufika.

    Baada ya kupita katika barabara kadhaa, gari hilo lilisimama mbele ya hoteli moja iliyokuwa na ghorofa tano.

    “Zima gari unipe funguo” Abdi alimwambia dereva wa gari hilo ambaye alilizima gari na kuchomoa funguo akampa Abdi.

    “Utatumia ile gari nyingine” Abdi alisema huku akifungua mlango wa gari na kushuka.

    “Amour shuka twende nikakupatie chumba”

    Abdi aliniambia huku akivuta hatua kuelekea kwenye mlango wa hoteli hiyo.

    Nikafungua mlango wa gari hilo na kushuka, nikamfuata Abdi Msomali.

    “Hii ni hoteli yangu” akaniambia na kuongeza.

    “Inaitwa Handeni Hotel”

    Alipotaja jina ‘handeni’ nilishituka kidogo kwa sababu Handeni ni moja ya walaya za mkoa wetu wa Tanga.

    “Inaitwa Handeni au sikukusikia vizuri?” nikamuuliza.

    “Inaitwa Handeni, pia ndio jina la eneo hili tuliopo”

    “Handeni ni moja ya wilaya za mkoa ninaotoka mimi”

    “Ninajua. Niliwahi kusikia kuwa Wasomali wanaoishi katika eneo hili wana asili ya kizigua. Ninajua kwamba Wazigua wako Handeni au nimekosa?”

    “Ni kweli. Hata mimi ni mzigua”

    “Basi hapa utakutana na ndugu zako”

    “Lakini ndugu zangu hao ni Wasomali?”

    “Ndio ni Wasomali kama mimi lakini babu zao walitokea Handeni miaka mingi iliyopita”

    “Nimekuelewa”

    SASA ENDELEA

    “Kama usingefika hapa ungeijuaje historia?”

    “Kwa kweli nisingeijua”

    Tulikuwa tumeshaingia ndani ya jingo hilo la hoteli. Tulikwenda mapokezi ambapo niligundua msomali huyo alikuwa akiheshimiwa sana na wafanyakazi wa hapo.

    “Nipatieni chumba kimoja” alimwambia mmoja wa wahudumu wa mapokezi huku akiegemea kaunta hiyo.

    Mhudumu huyo ambaye alikuwa msichana wa kisomali aliyekuwa amevaa sare ya koti jeusi na sketi alichukua kitabu cha wageni na kukifungua.

    “Niandike jina gain bosi?” akamuuliza Abdi kwa nidhamu huku akishika kalamu.

    “Niandike mimi mwenyewe” akamwambia.

    “Nitumie jina gani?”

    “Una maana hujui ninaitwa nani?”

    “Samahani bosi, ninalijua jina lako”

    Msichana aliandika kwenye kitabu hicho kisha akainua uso wake na kumtazama Abdi.

    “Niandike chumba cha daraja gani?”

    Abdi akanitazama. Bila shaka alikuwa akinipima kama ninastahili chumba cha daraja gani.

    “Mpatie chumba cha daraja la kwanza”

    Mhudumu aliandika kisha akanitazama mimi.

    “Ungependa ukae ghorofa ya ngapi?”

    “Ghorofa ya kwanza au ya pili”

    “Nitakupatia ghorofa ya kwanza”

    Msichana alijaza kwenye kitabu kisha akamtazama Abdi.

    “Mgeni atakaa kwa siku ngapi”

    Abdi akanitazama tena kisha akamjibu.

    “Hapo paache tu…”

    Msichana akageuka na kuchukua funguo.

    “Nimekupatia chumba namba 85 ghorofa ya pili” akaniambia.

    Sikumjibu kitu kwa sababu hicho chumba sikukitaka mimi.

    “Mpeleke” Abdi akamwambia.

    “Twende nikakuoneshe chumba chako” Msichana akaniambia.

    Alitoka nyuma ya kaunta akaelekea kwenye ngazi.

    “Mfuate akakuoneshe chumba utakachokaa” Abdi akaniambia.

    Nilimfuata yule msichna. Wakati anapanda ngazi nilikuwa nyuma yake. Niliuona mwili wake. Ulikuwa wa kuvutia. Alikuwa na umbo lililofinyangwa kisomali hasa..

    Nilifuatana naye hadi ghorofa ya kwanza. Akanionesha chumba namba 84. Akakifungua na kuingia ndani pamoja na mimi.

    Baada ya kukiona chumba hicho msichana alitoka na kuniacha. Kwa vile sikuwa nimepata maelezo yoyote kutoka kwa Abdi na mimi nikatoka. Nilifunga mlango nikashuka ngazi.

    Nilimkuta Abdi akinisubiri mapokezi.

    “Umekiona chumba?” akaniuliza.

    “Nimekiona”

    Akamgeukia mhudumu wa mapokezi.

    “Mtakuwa mnamuhudumia kwa kila kitu muda wote atakaokuwa hapa. Mtampatia chai ya asubuhi, chakula cha mchana na cha jioni, vinywaji na kila kitu atakachohitaji ikiwa ni pamoja na kufua nguo zake na kuzipiga pasi. Bili itakuwa juu yangu” akamwambia.

    “Sawa bosi, tumekuelewa”

    Abdi akanitazama.

    “Twenzetu” akaniambia.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Sikujua aliniambia twenzetu wapi lakini kwa vile nilishakuwa kama mateka wake sikumuuliza kitu nikamfuata.

    Tulitoka nje ya hoteli tukajipakia kwenye gari lake na kuondoka.

    Tukiwa ndani ya gari nilitarajia angeweza kuniambia tunakwenda wapi lakini hakuniambia kitu. Nilimuona alikuwa katika lindi la mawazo. Sikujua alichokuwa akiwaza.

    Baadaya kukata mitaa miwili mitatu alilisimamisha gari mbele ya jingo moja

    la ghorofa lililokuwa na maduka makubwa. Akaniambia tushuke.

    Tukashuka na kuingia katika duka mojawapo. Wakati tunaingia aliniambia.

    “Hili pia ni duka langu”

    “Ahaa…kumbe pia una maduka?” nikamuuliza.

    Licha ya kwamba nilikuwa na fadhaa kwa kutojua hatima yangu, nilijaribu kujichangamsha na kuzungumza naye kwa vile alionesha kama ananijali.

    “Sina maduka, nina duka moja tu” akaniambia.

    Tulipoingia ndani ya duka hilo nililiona lilikuwa duka kubwa la nguo za wanaume. Kulikuwa na suti, mashati, fulana, suruali na aina kadha wa kadha ya nguo za kiume.

    “Angalia nguo unazopenda, upate nguo za kubadili” akaniambia.

    Ilikuwa kweli nilihitaji kubadili nguo. Licha ya kuwa sikuwa na nguo za kubadili, zile nilizovaa zilikuwa zimechafuka na zilikuwa zinanitia aibu.

    Nikachagua nguo. Nilichukua shati moja

    na suruali moja pamoja na viatu na soksi.

    “Ongeza” Abdi akaniambia.

    Nikaongeza shati moja.

    Abdi akanichagulia mashati mengine matatu.

    “Ongeza suruali tatu” akaniambia.

    Nikachagua suruali zingine tatu, nikawa na suruali nne.

    Abdi akaniita upande uliokuwa na suti.

    Nilipokwenda alinaiambia.

    “Mimi napenda sana kuvaa suti na wewe chagua suti moja ya kuvaa”

    Nikatabasamu. Ilikuwa ni mara ya kwanza kukunjua uso wangu tangu ile boti tuliyokuwa tukisafiria kutoka Pemba ilipozama.

    Abdi alipoona natabasamu akacheka.

    “Chagua suti moja au nikuchagulie mimi?” akaniuliza.

    Kabla sijamjibu alishachomoa suti moja ya rangi ya kijivu.

    “Chukua hii” akaniambia.



    Nikaichukua ile suti.

    “Nenda kajaribu hizo nguo kwenye kile chumba pale” akaniambia huku akinionesha mlango wa chumba hicho.

    Nikaingia kwenye hicho chumba. Unapoingia katika chumba hicho unajiona mwenyewe kwani kilikuwa na vioo vitupu. Nilizijaribu nguo zote na kuona zilikuwa sawa.

    Nilipotoka katika chumba hicho nilimwambia Abdi.

    “Bado viatu na soksi”

    “Kachague jozi mbili za viatu na soksi” akaniambia.

    Nikaenda kuchukua jozi mbili za viatu na jozi mbili za soksi.

    Abdi alinifuata na kuninong’oneza.

    “Chukua na chupi kumi”

    Aliponiambia hivyo sote tukacheka.

    Baada ya kufanya manunuzi hayo ambayo Abdi aliyalipia kwa dola za Kimarekani tuliondoka kwa gari. Tulirudi kule hoteli ambako Abdi aliniacha.

    “Nitakupitia baadaye” aliniambia wakati nikishuka kwenye gari. Alinyamaza kidogo kisha akaongeza.

    “Najua utahitaji kujiweka vizuri kidogo na pia kupata chakula kizuri”

    “Ndio. Nahitaji vyote hivyo”

    “Kwa upande wa chakula nimeshaagiza utakula unachopenda”

    “Sawa”

    “Mimi naondoka kidogo, nitakupitia baadaye”

    Abdi akatia gea gari lake na kuondoka.

    Niliingia hotelini nikiwa na begi langu lililokuwa na nguo. Mhudumu mmoja alioniona aliniekea lile begi akapanda ngazi na kwenda kunisubiri kwenye mlango wa chumba changu.

    Nilipofika nilifungua mlango nikamwambia.

    “Karibu ndani”

    Alikuwa msichana mweupe wa kisomali mwenye mwili wa kutamanisha.

    Msichana alitabasamu akaliingiza lile begi chumbani kwangu kisha akaniaga

    na kutoka.

    Sikujua kama wasomali walikuwa wanazungumza Kiswahili. Pale hotelini niligundua baadhi ya wasomali walikuwa wanajua kuzungumza Kiswahili tena Kiswahili cha kipwani kilichonyooka.

    Nilipobaki mle chumbani nilivua nguo nikaenda kuoga. Niliotoka bafuni nilivaa ile suti mpya aliyoninunulia Abdi. Nikajitazama kwenye kioo na kuona nilipendeza. Angalau ilinisahaulisha madhila niliyokuwa nayo moyoni.

    Baada ya kuvaa nilishuka chini nikaingia katika eneo la mkahawa. Yule mhudumu aliyeniokea begi alinifuata.

    Akanisemea kwa kisomali.

    “Sijui hiyo lugha labda mnifundishe” nikamwambia.

    “Unajua Kiswahili peke yake?” akaniuliza.

    “Na kizigua”

    “Unatoka Handeni Tanzania?”

    “Umejuaje”

    “Kule ndio kuna wazigua”

    “Nasikia na nyinyi pia mna asili ya huko”

    “Babu zetu wametoka huko lakini mimi unaniona mweupe mama yangu ni mbarawa”

    “Mmejifundisha Kiswahili?”

    “Mimi nilizaliwa Garisa nchini Kenya, kule watu wanazungumza Kiswahili. Wenzangu wengine wametoka Mombasa”



    “Nashukuru kwa mazungumzo, ninahitaji chakula”

    “Upatiwe menyu?”

    “Kwani wewe si ndiye unayehusika”

    “Mimi pia nahusika lakini kuna mhudumu maalum wa hapa. Ngoja nimuite”

    Shamsa akamuita msichana mmoja na kumwambia.

    “Mgeni wa bosi. Bosi ameagiza apatiwe kila atakachohitaji. Bili itakuwa juu yake”

    “Sawa” Msichana alimkubalia kisha akaniuliza.

    “Nikupatie menyu?”

    “Ndio nipatie”

    Menyu alikuwa anayo mkononi, akaniwekea juu ya meza.

    Nikaishika na kutazama orodha ya vyakula. Nikachagua wali kwa samaki na juisi.

    Wasichana wote wawili waliondoka na kuniacha.

    Baada ya muda kidogo nililetewa chakula nilichoagiza. Wakati nakula nilianza kujiwazia mustakbali wangu kule Somalia. Nilijiuliza Abdi alikuwa na madhumuni gani kunichukua mimi Somalia, kuniweka hoteli na kunihudumia kama rafiki yake wakati tulikuwa hatujuani.

    Pia nilijiuliza ningekaa Somalia hadi lini. Ingawa niliingia kienyeji lakini wakati ule Somalia ilikuwa na serikali. Nilitakiwa kuwa na paspoti. Nilijiambia kama ningekamatwa nitakuwa na kosa la kuingia nchi ya watu bila paspoti.

    Nilishindwa kumuuliza Abdi kuwa ningekaa hapo Somali kwa siku ngapi, hasa nikikumbuka muda ule alionitolea bastola kwa kumhoji niende Somalia kufanya nini.

    Niliogopa kuwa ningeweza kumkasirisha na hivyo akanipiga risasi na kwenda kuutupa mwili wangu jalalani. Mtu mwenyewe licha ya kuwa mchangafu, mkarimu na anayependa kutabasamu, alionekana kuwa katili na asiyejali kitu.

    Mtu wa aina yake kuua ni kazi ndogo tu!

    Nilipomaliza kula niliondoka nikarudi ghorofani. Niliingia chumbani nikaenda kusimama kando ya dirisha na kutazama mandhari ya nje.

    Niliendelea kusimama hapo nikiangalia magari na watu waliokuwa wakipita barabarani huku akili yangu ikitafuta jibu la kwanini niko pale Somalia lakini sikupata jibu.

    Nilipitisha kama nusu saa nikiwa hapo, nikaingia chumbani na kuvua koti kisha nikajilaza kitandani.

    Nilikuwa nina uchovu na nilikuwa na usingizi. Kwa vile moyo wangu kidogo ulikuwa umetulia nikaona naweza kulala.

    Na nililala. Nilipokuja kuzinduka niliona giza. Ilikuwa ni usiku. Kwa vile sikuwa na saa sikuweza kujua ilikuwa ni usiku wa saa ngapi.

    Nikainuka kitandani na kuwasha taa. Pale mchagoni mwa kitanda palikuwa na simu. Nikainua mkono wa simu na kuzungumza na opereta.

    “Abdi ameshafika?” nikamuuliza.

    “Wewe nani?”

    “Mimi ni mgeni wake, niko ghorofa ya kwanza”

    “Alifika, akakupigia simu lakini haikupokelewa akajua umelala”

    “Sasa yuko wapi?”

    “Ameshaondoka, ametuambia tukuambie kuwa mtakutana asubuhi”

    “Ni saa ngapi sasa?”

    “Saa mbili inakwenda kwenye na nusu”

    “Nitashuka sasa hivi kuja kupata chakula”

    “Sawa, chakula kipo”

    Nikauweka mkono wa simu mahali pake na kuvua nguo. Nilikwenda kuoga tena.

    Nilipomaliza nilirudia kuvaa suti yangu kisha nikashuka chini. Niliingia katika ukumbi wa mkahawa wa hoteli hiyo.

    Mhudumu aliponiona tu akanifuata na kunipa menyu.

    “Nahtaji chai tu” nikamwambia.

    “Chai na nini?”

    “kama kuna sambusa nipatie tatu”

    Mhudumu aliondoka. Baada ya muda kidogo alirudi akiwa na chano kilichokuwa na kisahani kilichokuwa na sambusa tatu, birika ndogo ya maziwa, kipakiti cha majani ya chai, jagi la sukari na kikombe kitupu kikiwa na kisahani chake.

    Aliniwekea juu ya meza. Nikachukua birika na kumimina maziwa kwenye kikombe nikatia kijiko kimoja na nusu cha sukari na kukoroga.

    Baada ya sukari kukolea, nilitumbukiza kile kipakiti cha majani ya chai ambacho kiliyafanya maziwa kuwa na rangi ya chai.

    Nilitumia nusu saa nzima kunywa chai huku nikijiwazia. Mpaka muda ule sikuwa nimeitambua dhamira ya Abdi.

    Nikajiambia baada ya siku tatu nitamwambia kuwa nahitaji kuondoka kurudi kwetu kwani sikuwa na sababu yoyote ya kuendelea kukaa Somalia huku ndugu zangu na mama yangu wakiwa hawajui niliko.

    Baada ya kumaliza kunywa chai nilikwenda kujipumzisha kwenye eneo la wazi la hoteli ambapo palikuwa na upepo mwanana kutoka Bahari ya Hindi.

    Pale nilipoteza dakika kadhaa kabla ya kuamua kurudi chumbani kwangu.

    Mawazo ya Zena yalinijia usiku ule. Nikajiambia msichana wa kijini aliamua kunisaliti kwenye kile kisiwa baada ya kukataa kuoana naye.

    Kitendo cha kutoonana tena na Zena kilinipa picha kwamba Zena aliamua kuachana na mimi.

    Nikajiambia kama kweli alikuwa ameamua hivyo lilikuwa jambo la kushukuru sana kwani msichana yule alikuwa ananisababishia matatizo makubwa.

    Baada ya kuwaza sana nilipitiwa na usingizi. Sikujua nililala kwa muda gani lakini nilihisi kama nilishituka katikati ya usiku au nilikuwa katika ndoto. Nikaona kama mlango wa chumba nilichokuwa nimelala unafunguliwa taratibu.

    Kitendo hicho kilitokea nikiwa na kumbukumbu kamili kichwani mwangu kwamba mlango wa chumba hicho niliufunga kwa ndani na kuhakikisha kuwa ulikuwa umefungika.

    Mlango ulipokuwa wazi nilimuona mtu akiingia. Alikuwa mzee mwembamba na mrefu. Wembamba wake ulichanganyika na kukonda. Alikuwa na nywele ndefu, nyeupe tupu.

    Alikuwa amejifunga shuka nyeupe kiunoni na mabegani alijitanda shuka nyingine nyeupe kuziba kifua na tumbo lake. Hata hivyo upande mmoja wa kifua chake ulikuwa ukionekana. Mbavu zake zilikuwa zimetokeza na kuhisabika.

    Akaingia mle chumbani kwa kunyata. Wakati akiingia nilikuwa nikijiuliza nilikuwa ninaota au nilichokuwa nakiona kilikuwa ni kweli.

    Muda huo niligundua kuwa sikuwa sawa. Nilikuwa kama niliyepatwa na jinamizi. Mwili wangu haukuwa na uwezo wa kufanya chochote hata kupiga kelele.

    Kadhalika akili yangu ilikuwa imepoteza uwezo wake na nilikuwa kama taahira au zezeta. Sikuweza kujua ni kwanini nilijihisi kuwa vile.

    Yule mzee wa kisomali alikuja hadi karibu na kitanda nilichokuwa nimelala.

    Nilimuona vizuri. Alikuwa na pua ndefu na macho makali na madogo. Akasimama na kuniita.

    “Amour!”

    Nikanyamaza kimya. Nikamuona anasema maneno fulani kwa lugha ya kisomali kisha akanyoosha mkono wake na kupapasa kitanda nilichokuwa nimelalaa akashika mkono wangu na kuubana.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Aliubana kwa nguvu nikaona kama nilishikwa kwa koleo.

    “Inuka” akaniambia.

    Kwa sababu nilikuwa kama taahira nisiyejielewa nikainuka kweli.

    “Shuka kwenye kitanda” akaendelea kuniambia.

    Nikashuka kwenye kitanda. Nilikuwa nimevaa chupi tu. Akaichukua ile shuka aliyoitanda mabegani mwake akanifunga nayo kiunoni kisha akanishika tena mkono na kuniambia.

    “Twende”

    Nikatoka naye mle chumbani.

    Tulishuka ngazi, akatumia mlango wa nyuma wa hoteli kunitoa. Nilikuta gari limewekwa sambamba na mlango. Nikafunguliwa mlango wa nyuma wa gari, nikajipakia bilakuambiwa.

    Mzee naye aliingia katika siti ya nyuma. Kulikuwa na mtu aliyekuwa kwenye siti ya dereva ambaye sikuweza kumuona vizuri. Sikujua alikuwa nani.

    Kama ningemchunguza ningeweza kumjua lakini akili yangu haikuona umuhimu wa kutaka kumjua wala kujua nilikuwa napelekwa wapi.

    Gari likapigwa moto na kuondoka. Safari ikaanza. Mji ulikuwa kimya na hakukuwa na watu wowote walioonekana barabarani zaidi ya walinzi wa maduka waliokuwa wakisinzia.

    Baada ya mwendo wa karibu kilometa tano nilihisi kuwa tulikuwa tumeuacha mji kwani sikuona tena majumba ya ghorofa isipokuwa nyumba ndogo ndogo.

    Tulikuwa tumeingia katika maeneo ya ambayo kwa lugha ya kwetu tungeyaita ‘uswahilini’

    Mwanga wa gari tulilokuwemo ulimulika mapaka yaliyokuwa yakirandaranda kutafuta vyakula vilivyotupwa kwenye mapipa ya takataka. Ingawa ilikuwa usiku maji taka yalikuwa yakitiririka kutoka kwenye majumba ya watu na kuunda vidimbwi vya maji taka kandokando ya barabara.

    Wakati wote nilikuwa nashindana na akili yangu. Nilikuwa naona kichwa kizito kama niliyelemewa na usingizi, wakati huo huo sikutaka usingizi unichukue.

    Kila muda nilikuwa najigutuka na kukaza macho yangu ili nisilale. Lakini mwisho wake nilizidiwa nguvu, usingizi wa moja kwa moja ukanichukua ghafla.

    Hata sikuweza kujua tena lile gari lilielekea wapi.

    Lakini nilipokuja kuzinduka nilijiona mimi na yule mzee tumekaa kando ya shimo lililokuwa mbele yetu. Shimo hilo lilichimbwa usawa wa kaburi kando ya mti mkubwa. Mahali tulipokuwa palikuwa ni porini.

    Kulikuwa na taa ya chemli iliyokuwa inawaka pembeni mwa kaburi hilo na kufanya sehemu ile tuliyokuwa iwe na mwanga kwani eneo lote lilikuwa na kiza totoro.

    Yule mzee wa kisomali aliingia kwenye lile kaburi akasimama na kuniambia.

    “Ingia”

    Na mimi nikaingia.

    “Kaa hapo chini”

    Akanionesha mahali pa kukaa, nikakaa. Nikaona analishika sikio langu la upande wa kulia na kusema maneno kwa lugha ya kisomali kama mtu aliyekuwa anasoma dua kisha akaniinamia na kukigandamiza kichwa chake kwenye komo langu.

    Alinishika na kunigandamiza kwa nguvu sana mpaka nikasikia maumivu ya kichwa. Nilitaka kupiga kelele nilipomuona amerushwa na kuanguka chini. Alikuwa kama aliyerushwa na umeme.

    Akainuka taratibu na kutoka kwenye lile kaburi. Kilichofuatia baada ya hapo sikukifahamu, nilishitukia tu nikiamka kitandani pale hoteli nilipokodiwa chumba na Abdi.

    Nikahisi kwamba labda nilikuwa katika ndoto. Moyo ulikuwa ukinienda mbio. Nikainuka na kwenda kuutazama

    mlango wa mle chumbani. Niliukuta umefungwa kwa ndani. Kitu ambacho kiliashiria kuwa hakukuwa na mtu aliyeingia humo chumbani.

    Lakini ni ndoto gani ile? Nikajiuliza. Kila kitu nilikiona waziwazi kama vile kinatokea kweli.

    Kama ilikuwa ndoto ilikuwa ya ajabu sana, nikajiambia.

    Wakati ule nilipoamka kulikuwa kumekucha. Nikaingia maliwatoni. Nilipotoka nikavaa nguo. Nilivaa suti ile ile niliyonunuliwa na Abdi.

    Nikashuka chini na kuingia mkahawani. Nilipatiwa kifungua kinywa. Wakati nakunywa chai nikamuona Abdi akiingia.

    “Amour salaam alaykum” akanisalimia kwa bashasha huku akinipa mkono.

    “Alayka salaam. Habari ya tangu jana?”

    “Nzuri bwana, umeamkaje?”

    “Nashukuru, nimeamka salama. Sijui wewe”

    Na yeye akaagiza kifungua kinywa.

    “Kuna sehemu nataka twende” akaniambia.

    “Wapi?”

    “Mogadishu ni kubwa sana. Kuna sehemu nyingi nataka kukuonesha”

    “Sawa”

    Tulipomaliza kunywa chai tukatoka.

    “Jana nilikufuata usiku nikakuta umelala” Abdi aliniambia wakati tunatoka.

    “Nililala mapema kwa sababu ya uchovu”

    “Niliwambia wale wasichana wasikuamshe. Nilijua ulikuwa na uchovu mwingi”

    Tulitoka nje ya hoteli tukajipakia kwenye gari. Lilikuwa ni gari la aina nyingine sio lile la jana yake.

    Baada ya kujipakia tukaondoka.

    “Nataka uuone mji wetu vizuri” Abdi alikuwa akinizungumzisha huku gari likiwa katika mwendo wa taratibu au wa kinyonga . Nilikuwa sijui tunakwenda wapi.

    “Mji wenu ni mzuri sana. Una majumba makubwa na umejengeka sana” nikamwambia.

    “Bado. Kuna maeneo mengi hujayaona”

    “Inavyoonekana mmepiga hatua kubwa ya maendeleo”

    “Sana”

    Baada ya mwendo wa karibu nusu saa tuliingia katika maeneo ya mashamba. Nilikuwa nikijiuliza alikuwa akinipeleka shambani kwake au alitaka kunionesha kitu gani?

    Tulitokea katika mtaa mmoja uliokuwa umezagaa uchafu. Tulipishana na mbuzi, kondoo na kuku wa kienyeji. Abdi alikuwa akikata kona ovyo kukwepa mashimo na vidimbwi vya maji machafu.

    “Tuache gari hapa” Abdi akaniambia huku akifunga breki pembeni mwa njia. Bila shaka alishindwa kuendesha kutokana na barabara yenyewe kujaa mazagazaga.

    Tulishuka tukatembea kwa miguu. Tulizipita nyumba mbili za ghorofa. Zilikuwa nyumba zilizoonekana zimeshapitwa na muda wake wa kuishi watu kwani zilichakaa sana. Huenda zilijengwa miaka mia moja iliyopita. Enzi za utawala wa kikoloni.

    Tuliingia mtaa mwingine uliokuwa na tifutifu jingi. Tukapita msikiti. Tulikwenda mbele kidogo, Abdi akasimama mbele ya mlango wa nyumba moja iliyokuwa imepakwa rangi nyeupe.

    Mlango wake ulikuwa umechorwa picha ya nyota na mwezi.

    Abdi alibisha mlango huo. Baada ya muda kidogo mlango ukafunguliwa.

    Mzee mmoja akachungulia nje. Alimtazama Abdi kisha akanitazama mimi.

    “Karibuni” akatuambia na kurudi ndani.

    Abdi akaingia na kuniambia.

    “”Karibu”

    Na mimi nikaingia. Tulitokea katika ukumbi mpana kama darasa. Harufu tuliyokutana nayo humo ndani ni ya udi na marashi.

    Katikati ya ule ukumbi palitandikwa jamvi. Katika lile jamvi niliona sinia iliyotiwa vitu mbalimbali kama vile ndizi mbivu, vipande vya miwa, mkate wa mchele, tende na vitu vingine ikiwemo chupa kubwa lenye asali.

    Katika kila pembe ya lile jamvi kuliwekwa nazi moja. Jumla zilikuwa nazi nne.

    Yule mzee wa kisomali alikuwa amesimama nyuma ya mlango.

    Alimwambia Abdi maneno kwa lugha ya kisomali. Abdi akaniambia mimi.

    “Twende tukakae pale”

    Alinionesha lile jamvi.

    Tukaenda kukaa. Yule mzee wa kisomali alitoka uani. Baadaye akarudi tena akiwa ameshika kitabu kikubwa cha kiarabu na yeye akakaa kwenye lile jamvi.

    Sasa niliweza kumuangalia vizuri. Nikajiuliza mbona amefanana na yule msomali niliyemuota akinichukua kule chumbani? Alikuwa mrefu vile vile na pua yake pia ilikuwa ndefu.

    Nikashangaa sana.



    Mzee huyo wa kisomali akamtazama Abdi kisha akamuuliza maneno na kwa kisomali.

    Abdi akanitazama kisha akamwambia.

    “Amour”

    Nikahisi labda alimuuliza jina langu.

    Mzee wa kisomali akanitazama kisha akafungua kitabu chake. Karasa zilikuwa zimegandana akakigusisha kidole chake kwenye ulimi kukitia mate kisha akaufungua ule ukurasa.

    Akaanza kusoma maneno ya kiarabu. Sikuwezaa kujua alikuwa anasoma nini lakini nilisikia akitaja jina la Zena Binti Jabal Keysi. Wakati mwingine akitaja jina langu.

    Mara kwa mara nilikuwa nikimtazama Abdi kuona kama mwenzangu alikuwa anaelewa chochote. Abdi alikuwa amenyamaza kimya. Alikuwa ametulia kama aliyekuwa anaaguliwa.

    Ghafla tukaona nazi iliyokuwa katika pembe moja ya lile jamvi inapasuka yenyewe. Mzee alikuwa akiendelea kusoma tu. Naizi ya pili ikapasuka. Ilipopasuka nazi ya tatu ukuta wa uliokuwa mbele yetu ulifanya ufa akatokea mtu.

    Alikuwa mwanamke aliyevaa vizuri. Gauni alilovaa lilikuwa limedariziwa vimemeta vya dhahabu. Alikuwa amevaa mkufu wa dhahabu na bangili za dhahabu. Masikioni alikuwa amevaa vipuli vya dhahabu.

    Kichwani kwake nywele zake zilibanwa kwa taji la dhahabu lililomfanya aonekane kama malikia wa visiwa vya Sheba.

    Alipotokea sote tulishituka tukamtazama. Ilinichukua sekunde mbili au tatu kutambua kuwa alikuwa Zena!

    Zena alikuwa amependeza kuliko siku zote nilizowahi kumuona. Alikuwa aking’ara kama mwezi mpevu! Sikuweza kujua ni kitu gani kilichomleta pale na kwanini alitokea katika hali tofauti na anavyotokea siku zote.

    Siku zote nilizokutana naye alinitokea katika hali ya kawaida, si hali kama ile ya kuibuka kutoka kwenye ufa wa ukuta. Ilikuwa hali ambayo si tu ilinitisha mimi, ilimtisha hata Abdi aliyekuwa ameketi karibu yangu. Nilimuona akimtazama kwa shauku iliyochanganyika na hofu.

    Mzee wa Kisomali alimtazama kisha alimwambia maneno kwa lugha ya kiarabu.

    Zena hakusema chochote. Akiwa miguu pekupeku alikuja taratibu hadi ilipokuwa ile sinia iliyokuwa na vitu akaipindua kwa miguu. Sinia ilipinduka, na vitu vyote vilimwagika chini.

    Alipomaliza kuipindua ile sinia alimfuata yule mzee wa kisomali akampiga kibao cha shavu. Mzee alianguka chini. Hakuinuka tena. Sasa akamfuata Abdi. Abdi alipoona anafuatwa aliinuka haraka akatoka mbio. Na mimi nikainuka na kutoka mbio kumfuata Abdi.

    Tulitoka kwenye mlango. Abdi kama ambaye alibadili mawazo alirudi kwenye mlango huo na kuchungulia. Na mimi nikarudi kuchungulia.

    Zena hatukumuona tena. Tulimuona yule mzee akijiinua na kukaa. Abdi akarudi. Mimi sikurudi.

    Nilibaki kwenye mlango nikichungulia.

    Nikawasikia Abdi na yule mzee wakizungumza kwa lugha ya kisomali. Mzee alikuwa akifoka na akimuashiria Abdi aondoke.

    Abdi akatoka na kuniambia.

    “Twenzetu”

    Wakati tunatembea kurudi tulikoliacha gari Abdi hakunieleza chochote na mimi sikumuuliza chochote.

    Nilibaki kujiuliza mwenyewe ni kitu gani kilichokuwa kimetendeka pale hadi Zena akatokea na kumwaga vile vitu na kisha kumpiga kibao yule mzee? Sikupata jibu.

    Nilihisi kuwa jibu alikuwa analo Abdi lakini hakuonesha dalili yoyote ya kutaka kunieleza chochote. Na mimi nikashindwa kumuuliza.

    Niliona uso wake ulikuwa umefadhaika na alikosa raha. Hakuwa hata akinitazama.

    Tulirudi kwenye gari lake tukajipakia na

    kuondoka.

    Wakati Abdi akiendesha gari kurudi mjini aliniambia.

    “Nina hoteli mbili. Ile unayokaa wewe na nyingine mpya. Nataka uwe mneneja wa ile hoteli yangu mpya”

    “Nitawezaje kuwa meneja wa hoteli yako wakati nataka kuondoka?” nikamuuliza.

    “Huwezi kuondoka bila paspoti. Subiri nikutengezee paspoti”

    “Utanitengezea lini?” nikamuuliza.

    “Usiwe na haraka Amour. Ninakuhakikishi

    a kuwa nitakutengezea isipokuwa katika kipindi hiki cha kusubiri paspoti yako iwe tayari nataka uwe meneja wa hoteli yangu. Nitakupa nyumba na gari na kama utahitaji mke wa kisomali nitakutafutia msichana mrembo”

    Abdi alianza kunitia tamaa ya maisha na kunipa ushawishi wa kubaki Somalia.

    Hata hivyo moyo wangu ulikuwa mzito kukubaliana naye. Nilikuwa simuelewi japokuwa mipango aliyonieleza ilikuwa ya maana kwa upande wangu.

    “Unataka kurudi Tanga, kuna nini? Kama utakaa hapa kwa muda mfupi tu Amour unaweza kupata maendeleo makubwa na ukarudi kwenu ukiwa tajiri” Abdi aliendelea kunishawishi.

    Muda wote nilikuwa nimebaki kimya nikiyatafakari maneno yake. Alipoona nipo kimya na yeye akanyamaza. Sikuweza kujua ni kwanini aliileta ile mada ya hoteli wakati kulikuwa na tukio jingine la kuibuka kwa Zena ambalo ndilo alilopaswa kunieleza.

    Kwanza kile kisomo alichokuwa anasoma yule mzee hadi nazi zikapasuka na Zena akatokea, nilijiuliza, kilikuwa kiosomo cha nini. Hapo pia sikupata jibu.

    Dakika chache baadaye Abdi alilisimamisha gari mbele ya nyumba moja iliyokuwa katika mtaa mtulivu.

    Aliniambia tushuke, tukashuka.

    “Nifuate” akaniambia.

    Tuliingia katika geti la ile nyumba tukakuta mafundi wakipaka rangi kwenye kuta. Alizungumza nao kwa kiomali kisha tukaingia ndani ya ile nyumba.

    Ilikuwa nyumba nzuri na ya kupendeza. Abdi alitazama sehemu zilizokuwa zimeshapigwa rangi, akaniambia.

    “Hii ni nyumba yangu. Ninaifanyia ukarabati kwa ajili yako. Wewe utakuja kuishi hapa”

    “Wewe mwenyewe unaishi wapi?”

    “Nitakupeleka ukapaone nyumbani kwangu”

    “Ni lini hii nyumba itakuwa tayari?”

    “Leo watamaliza kupiga rangi. Labda keshokutwa unaweza kuhamia. Kesho nitakuwekea fanicha mpya”

    Alifungua milango ya vyumba na kunionesha ndani.

    “Patakufaa sana hapa” akaniambia.

    Sikumjibu kitu. Nilikuwa bado ninajadiliana na moyo wangu kuhusu suala la kubaki pale Somalia.

    “Amour unafikiria nini. Unataka kuiacha bahati kama hii?” Abdi aliniambia kisha akacheka peke yake.

    “Twenzetu” akaniambia.

    Tukatoka tena. Tulijipakia kwenye gari tukaondoka.

    Breki ya kwanza ilikuwa mbele ya hoteli moja iliyokuwa katika mtaa mwingine. Ilikuwa hoteli ndogo ya ghorofa moja, Ilikuwa imeandikwa kwa herufi kubwa. AL ASAD.

    “Hii ndio hoteli ambayo nitakuachia wewe, itakuwa kama mali yako kwani tutakuwa tunagawana faida kila mwezi na kila mwaka kama utapenda kuendelea kubaki Somalia” Abdi aliniambia tukiwa bado tupo kwenye gari.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alipoona nilikuwa nikiiangalia angalia ile hoteli, aliniambia.

    “Tushuke uione vizuri”

    Tukashuka.

    Tuliingia ndani ya ile hoteli. Kwa kweli ilikuwa imechangamka.

    “Sasa nani anaiendesha kwa hivi sasa?” nikamuuliza.

    “Yuko mtu lakini nitamuondoa”

    “Sasa ni kwanini umuondoe?”

    “Lengo langu ni kukunufaisha wewe rafiki yangu au nimefanya kosa?’

    “Hapana. Ni vizuri”

    Abdi alinitembeza hoteli nzima kisha tukaingia katika ofisi ya meneja.

    Meneja mwenyewe alikuwa mtu mzima. Kichwa chake kilishaanza kutoka mvi.



    Walizungumza kwa kisomali huku meneja huyo akinikodolea macho.



    Walizungumza kwa karibu robo saa kisha tukatoka.



    “Yule ndiye meneja aliyeko sasa” Abdi aliniambia wakati tunatoka nje ya hoteli hiyo.



    “Utamuhamishia mahali pengine au unammuondoa kabisa?’ nikamuuliza.



    “Nitamfikiria”



    “Umeshamwambia?”



    “Nilitaka kwanza nikubaliane na wewe”



    “Mimi nimeshakubali”



    “Una uzoevu wa kuendesha hoteli?”



    “Kwa kweli sina uzoefu huo”



    “Utajifundisha hapa hapa. Ninaamini hutaweza kushindwa”



    “Nitajaribu”



    “Kazi yako itakuwa kuongoza na kukagua. Kuna kijana ambaye amesomea uendeshaji wa hoteli yuko pale atakusaidia”



    “Nafikiri nitaweza. Usiwe na wasiwasi”



    Baada ya hapo hatukuzungumza tena. Mwenzngu alikuwa amenyamaza, sikujua alikuwa akiwaza nini. Mimi nilikuwa na mawazo ya kubaki Somalia kuendesha shughuli ya hoteli.



    Kikubwa kilichonipa tamaa ni kuwa kazi ya umeneja wa hoteli ni ya heshima na aliniambia kuwa angenipa ile nyumba pamoja na gari. Isitoshe tungegawana mapato ya hoteli..



    Nilijiambia kama ningeweza kuchuma pesa pale Somalia na kurudi kwetu nikiwa na utajiri kama alivyoniahidi Abdi, sikuona haja ya kung’ang’ania kurudi Tanga ambako sikuwa na hakika kama nisingefukuzwa kazi kutokana na kutoonekana kazini kwa kipindi kirefu bila taarifa yoyote.



    Abdi akanipeleka nyumbani kwake. Ilikuwa nyumba nzuri ya ghorofa moja iliyokuwa ndani ya geti. Mlinzi wake alitufungulia geti. Gari la abdi likaingia.



    Kulikuwa na banda la magari lakini Abdi alilisimamisha gari hilo mbele ya mlango wa nyumba yake ya kifahari.



    Tukashuka. Abdi alikwenda kufungua mlango akaniambia.



    “Karibu kaka”



    Tukaingia ndani. Alikuwa na sebule ya kupendeza iliyokuwa imepambwa vizuri kwa fanicha za thamani. Wakati tunaingia kulikuwa na msichana mmoja aliyekuwa akifanya usafi kwa kutumia kufaa maalum cha kuondoa vumbi.



    “Karibu ukae” Abdi aliniambia huku naye akikaa. Akaongeza.



    “Jisikie uko nyumbani. Hapa ndio kwetu bwana”



    Nikawa natupa macho huku na huko kuiangalia sebule.



    “Asante. Nimefurahi kupafahamu nyumbani kwako”



    “Utakunywa kahawa?” Abdi akaniuliza.



    “Hapana”



    “Tangu uje Somalia sijakuonesha nyumbani kwangu. Hii nyumba ni yangu na mimi ninaishi hapa” Abdi aliendelea kuniambia kisha akaongeza.



    “Unaweza kuona nyumba iko kimya kwa sababu watoto hawapo”



    “Wako wapi?”



    “Shemmeji yako amekwenda kwao Kismayuu. Mama yake ni mgonjwa. Atarudi pindi mama yake akipata nafuu”



    Yule msichana aliyekuwa akifanya usafi alikuwa ameshaondoka.



    “Nilipomuona huyu msichana nilidhani ndiye shemeji?”



    “Hapana. Yule ni mfanyakazi wangu. Kwa sasa ninaishi na wafanyakazi wangu tu”



    Hatukukaa sana hapo. Abdi akainuka na kuniambia.



    “Sasa acha nikurudishe kule hoteli. Nataka niende shambani kwangu. Niliambiwa baadhi ya ng’ombe wangu ni wagonjwa”



    Tukatoka na kujipakia tena kwenye gari, tukaondoka.



    Abdi alinirudisha hotelini akaniacha na kuondoka. Niliingia chumbani nikaketi. Mawazo ya Zena yakaanza kunijia. Sikutaka kuendelea kumuwaza mwanamke huyo wa kijini lakini mawazo yake yalinijia kwa nguvu na sikuweza kuyazuia.



    Kikubwa kilichosababisha nimuwaze ni kule kujitokeza nyumbani kwa yule mzee wa kisomali na kumpiga kibao yule mzee. Mpaka muda ule tukio lile lilikuwa kama kitendawili nilichoshindwa kukitegua.



    Lakini jambo moja ambalo halikuwa na shaka akilini mwangu ni kwamba Abdi na yule mzee wa kisomali walikuwa wanajua ni kwanini Zena alitokea pale.



    Kama walikuwa hawajui ni lazima Abdi angeonesha mshangao wake na angenieleza kitu. Lakini hakutaka kunieleza chochote kama vile ilikuwa ni siri.



    Kadhalika sikuweza kujua yule mzee alikuwa ni nani, ana uhusiano gani na Abdi na kwanini nilimuota usiku akiniingiza ndani ya kaburi?



    Pia nilijiuliza kile walichokuwa wanasoma pale ni kitu gani na kwanini kuliwekwa vitu mbalimbali kama vya uganga? Kwa kweli licha ya kujiuliza mara kadhaa sikupata jibu la kuridhisha.



    Kwa vile sikuweza kuelewa kitu niliona nisiumize kichwa kwa kujiuliza maswali ambayo hayakuwa na majibu. Nikayaacha mawazo yale.



    Siku ile sikumuona tena Abdi hadi siku ya pili yake ambapo alikuja hoteli asubuhi kunijulia hali.



    “Nyumba yako itawekewa fanicha mpya leo. Kesho utaanza kuishi kule na kesho kutwa utakwenda kuanza kazi kule hotelini. Yule meneja ataondoka leo” Abdi akaniambia.



    “Sawa”



    “Amour unajua kuendesha?”



    “Kuendesha nini?”



    “Nina maana kuendesha gari”



    “Ninajua lakini sikuja na leseni yangu”



    “Si tatizo. Tutakwenda studio utapiga picha kadhaa za  paspoti, baadhi yake tutazitumia kukutengezea leseni ya hapa Somalia”



    “Nitaipata lini hiyo leseni?’



    “Kesho tu utaweza kuipata”



    “Bila mimi mwenyewe kwenda kujaribiwa?”



    “Hiyo kazi niachie mimi. Hata paspoti utapata bila kwenda wewe mwenyewe”



    “Lakini hiyo paspoti itakuwa ya nchi gani?”



    “Wewe ulitaka ya nchi gani?”



    “Ya Tanzania”



    “Utaipata bila shaka yoyote. Hapa kuna mabingwa wa kugushi. Nipe wiki moja tu. Utawekewa na mihuri ya tarehe uliyoingilia hapa Somalia”



    Aliponiambia hivyo nilitabasamu.



    “Inaonekana wewe hushindwi na kitu hapa Somalia” nikamwambia.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Serikali yenyewe nimeiweka mikononi mwangu. Kuna maafisa wa polisi ambao wanakuja kuchukua mishahara kwangu kila mwezi kwa ajili ya kulinda miradi yangu. Wewe umeona mwenyewe juzi meno ya tembo tulivyoyaingiza na kuyapakia kwenye meli. Usifikiri kuwa polisi hawajui, wanajua. Baadhi ya mawaziri pia ni marafiki zangu. Likitokea tatizo niwapigia simu”



    “Ninakuamini. Mambo yako ni makubwa!”



    Nilipomsifu Abdi alicheka akanipa mkono. Alionekana kuwa ni mpenda sifa.



    Tuliondoka hapo Hoteli tukaenda studio kupiga picha za papo kwa papo. Alichukua picha zangu kadhaa za usawa wa paspoti.



    Wakati ananirudisha hotelini, nilimwambia kuwa nilikuwa ninahitaji saa.



    “Saa tu, twende dukani tukanunue” akaniambia.



    Abdi akageuza gari. Tulikwenda katika duka moja la kuuza saa akaniambia nichague saa niliyokuwa nahitaji. Nikachagua saa moja. Abdi akailipia.

    “Unahitaji nini tena?” akaniuliza.

    “Nilikuwa nahitaji saa tu”

    “Basi twenzetu”

    Tukaondoka. Alisimama tena kwenye duka moja akashuka na kuniambia nimsubiri. Baada ya muda kidogo alirudi akiwa ameshika gomba lililokuwa limefungwa vichnga vya mirungi.

    Akaliweka kwenye siti kisha akawasha gari tukaondoka. Alinirudisha hoteli akaniacha hapo na kuondoka.

    Sikumuona tena hadi siku ya pili yake. Alikuja hotelini saa nne akaniambia nichukue vitu vyangu.

    “Kule nyumba iko tayari”

    “Sawa. Ngoja nitie nguo zangu kwenye begi, sina vitu vingi hapa”

    Nilitia vitu vyangu kwenye begi nikalishika begin a kumwambia Abdi.

    “Twenzetu”

    Tukatoka. Tukiwa nje ya hoteli tulijipakia kwenye gari tukaondoka.

    Tulikwenda katika ile nyumba ambayo Abdi alikuwa ameitayarisha kwa ajili yangu.

    Tulipoingia ndani nilikuta ilikuwa imebadilika. Kulikuwa kumewekwa fanicha mpya. Nilikagua sebule, vyumba, hadi jiko. Kote kulikuwa kunaridhisha sana.

    Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu ndio nilianza kuishi katika nyumba yenye hadhi kama ile. Kama ingekuwa Tanga ningeonekana mtu wa kuheshimika sana. Lakini historia inaonsha mara nyingi mtu hupata utukufu mbali na kwao. Ndiyo ilivyokuwa kwangu mimi.

    “Umeangalia kila kitu, labda kuna kitu kilichopungua” Abdi akaniuliza baada kuipitia nyumba nzima.

    “Naona kila kitu kipo”

    “Mimi nafikiri bado kitu kimoja tu?” Abdi akaniambia.

    “Kitu gani?” nikamuuliza.

    “Nyumba inahitaji kupambwa”

    “Ipambwe kivipi?”

    Abdi akacheka kidogo.

    “Hivi hujaelewa kama nyumba hupambwa kwa kuwa na mke mzuri”

    “Na mimi nikacheka.

    “Ni kweli, sasa huyo mke yuko wapi?”

    “Ndiyo nataka tukae chini tulizungumzie suala hilo”

    “Sawa”

    “Sema mwenyewe unataka mke wa kibarawa, wa kigunya au wa kisomali?”

    “Wote uliowataja wanafaa”

    “Nikutafutie mke wa kisomali aliyechanganya na ubarawa, mweupe kama karatasi”

    Abdi aliponiambia hivyo tukacheka.

    “Abdi bwana! Mweupe kama karatasi?”

    “Huyo akiwa chumbani uhitaji kuwasha taa, nuru yake inatosha kabisa kuangaza chumba!”

    “Atapatikana kweli?”

    “Mbele ya fedha hakuna kisichopatikana”

    “Sawa. Mimi namsubiri”

    “Nipe muda kidogo nikuchagulie mke anayefaa. Najua kuwa wewe unahitaji mke mweupe”

    “Umenijuaje”

    Abdi akacheka kisha hakunijibu chochote, akagonga mkono wangu na kuelekea kwenye mlango. Alikuwa kama aliyetaka kutoka kisha akageuka na kunitazama.

    “Suala lako ninalishughulikia, usijali. Nilikuahidi kukupatia gari, ungependa gari hii ninayotumia au nikupatie gari jingine”

    “Wewe ndio utajua”

    “Basi ngoja nikupatie leseni hapo kesho, nitakupa gari zuri”

    “Sawa”

    Nilipomjibu hivyo Abdi aligeka akafungua mlango na kutoka bila kuniambia chochote. Nilimchungulia kwenye dirisha nikaona akipanda gari lake na kuondoka.

    Alikuwa kama aliyekwishamaliza kazi.

    Niliingia katika chumba changu nikafungua kabati na kulikagua ndani. Lilikuwa tupu na safi. Nikaanza kupanga nguo zangu chache..

    Nilipomaliza nilitoka nikaenda kukaa sebuleni kujipumzisha Siku ile nilishinda pale nyumbani. Saa saba mchana Abdi alikuja akanipa shilingi laki moja za kisomali kwa ajili ya matumizi yangu.

    Akaniambia kwamba leseni yangu inashugulikiwa. Alinichukua kule hotelini kwake tukala chakula pamoja kisha akanirudisha nyumbani.

    Saa mbili usiku alikuja tena tukaenda kula.

    Siku ile nililala peke yangu katika ile nyumba. Asubuhi kulipokucha Abdi alinifuata kwa ajili ya kunipeleka kule hoteli kuanza kazi.

    Tulipofika alinitambulisha kwa wafanyakazi kama meneja mpya. kuanzia siku ile. Abdi pamoja na mtu ambaye aliwekwa awe msaidizi wangu walinitembeza katika hoteli nzima kabla ya kunikabdidhi ofisi pamoja na nyaraka zote zinanazihusu shughuli za hoteli.

    Kutoka siku ile nikaanza kazi ya umeneja katika hoteli ya AL ASAD. Siku iliyofuata Abdi alinipatia leseni ya kuendesha na akanikabidhi moja ya magari yake.



    Baada ya kuendesha kazi kwa mwezi mmoja Abdi akaniambia kuwa alikuwa ameshanitafutia mchumba.

    “Ni nani?” nikamuuliza.

    “Shamsa. Naona Shamsa anakufaa, au unasemaje?”

    Shamsa alikuwa ni yule msichana wa kisomali aliyekuwa akifanya kazi katika ile hoteli ya Abdi niliyofikizia.

    “Shamsa anafaa sana” nikamwambia.

    “Yule baba yake ni msomali lakini mama yake ni mbarawa”

    “Umeshazungumza naye?”

    “Nimeshazungumza naye”

    “Amekubali?”

    “Kwanini akatae amri ya bosi wake. Kiufupi ni kuwa amekubali. Hivi leo ndio nataka kuwakutanisha mzungumze wenyewe”

    “Utatukutanisha wapi?”

    “Popote utakapotaka wewe”

    “Anaweza kuja nyumbani ninakoishi?”

    “Kwa mila za wasomali hawezi kuja nyumbani kwako ila wewe mfuate kazini kwake, gari si unayo?”

    “Ndiyo gari ninato”

    “Sasa wewe mfuate kazini, utakaa naye mtazungumza”

    “Sasa nimwambieje?”

    Nilipouliza swali hilo Abdi akacheka.

    “Usicheke Abdi. Mimi sijui mila zenu huku!”

    “Muulize umepata ujumbe wangu kutoka kwa Bwana Abdi. Sasa akikupa jibu ndio, mtaendeleza mazungumzo yenu”

    “Sawa. Nitakwenda baadaye kidogo”

    “Na mimi nitamjulisha kuwa utakwenda kuongea naye”

    “Sawa”

    Nilisubiri hadi nilipopunguza kazi zangu nikatoka kwa gari niliyokuwa nimepewa na abdi. Muda huo ilikuwa ikaribia kuwa saa tano.

    Nilipofika nilitafuta meza nikakaa. Shamsa alishaniona akanifuata na kuketi na mimi.

    “Asalaam alaykum” akanisalimia huku akinitolea tabasamu la aibu..

    “Wa alayka salaam. Hujambo Shamsa?”

    “Sijambo, sijui wewe”

    “Mimi nashukuru sana”

    Nikayakumbuka maneno ya Abdi.

    “Je umepata ujumbe wangu?” nikamuuliza.

    “Nimeupata”

    Alponiambia hivyo nilitabasamu.

    “Ndiyo nimefuata jibu”

    Shamsa akanitazama kwa makini mpaka nikaona aibu. Labda alikuwa akinihakiki kama ni mume ninayeweza kumfaa.

    “Mbona tulishakubaliana” akaniambia baada ya kimya cha sekunde chache..

    “Mimi sielewi. Mlikubaliana nini?”

    “Kwani wewe si ulikuwa unataka mchumba?”

    “Ndiyo”

    “Nimekubali kuwa mchumba wako”

    Aliponiambia hivyo niliushika mkono wake aliokuwa ameuweka juu ya meza. Niliushika kirafiki tu kisha nikamtazama. Nilimuona alikuwa amevutiwa na kitendo changu.

    “Shamsa una umri gani?” nikamuuliza.

    “Miaka ishirini na mitano. Na wewe una umri gani?”

    “Miaka ishirini na tisa. Ikifika mwakani mwezi wa nne nitatimiza miaka thelathini”

    “Ni mwenyeji wa wapi?”

    “Abdi amekwambia mimi ni mwenyeji wa wapi?”

    “Sikumuuliza hivyo”

    “Unaonaje kama utamuuliza yeye?”

    “Kwanini nimuulize yeye wakati mwenyewe upo?”

    Nikanyamaza kidogo kabla ya kumwammbia.

    “Mimi natokea Tanzania”

    “Wewe ni mzigua”

    “Ndiyo mimi ni mzigua”

    “Hata babu yangu mzaa mama alitokea huko huko zigua”

    “Kwa hiyo wewe ni mzigua?”

    Shamsa akacheka kidogo.

    “Hapana. Babu yangu mzaa mama ndiyo alikuwa mzigua lakini mimi mwenyewe ni msomali, upande mwingine ni mbarawa”

    “Mmezaliwa wangapi katika familia yenu?”

    “Tulizaliwa wawili tu, mimi na dada yangu ambaye alishafariki zamani. Kwa hiyo nimebaki mimi peke yangu”

    “Wazazi wako wapo?”

    “Pia walishafariki. Kwa sasa hivi mtu pekee ambaye niko karibu naye ni Abdi”

    “Oh Pole sana”

    “Asante. Abdi ameniambia kama nitafunga ndoa na wewe, yeye ndiye atakayenisimamia kwa sababu sina ndugu”

    “Nimekuelewa. Pole sana”

    “Asante. Abdi ameniambia wewe ni ndugu yake, ni kweli?”

    “Ni kweli”

    Hapo nilisema uongo kumuunga mkono mwenyeji wangu. Abdi hakuwa ndugu yangu. Kwa vile alishamwambia

    msichana huyo kuwa mimi ni ndugu yake, nikaona nikubali. Pengine Abdi alimwambia hivyo ili msichana huyo aweze kunikubali kirahisi.

    “Kwa hiyo umeamua kuja kuishi hapa Somalia?” Shamsa akaniuliza.

    “Ni ushauri wa Abdi, amenitaka nibaki huku”

    “Ameniambia amekupa ile hoteli yake ya Al Asad?”

    “Amenipa kwa maana ya kuiongoza”

    “Lakini wewe si ndiye meneja wake?”

    “Ndiyo”

    “Sasa turudi katika mazungumzo yetu, unatarajia utanioa lini?”

    “Hilo ni suala ambalo nitalipanga na Abdi. Kwa upande wangu ningependa tuoane haraka iwezekanavyo”

    “Sawa”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Usiku wa siku ile Abdi alikuja nyumbani kwangu akaniuliza.

    “Mmezungumzaje na Shamsa?”

    “Tumekubaliana”

    “Umemuonaje yule binti, si anakufaa?”

    “Anafaa”

    “Sasa ungependa umuoe lini?”

    “Mimi nakusikiliza wewe”

    “Wazazi wake walishafariki na hana ndugu. Nimemwambia kuwa ndoa yake nitaisimamia mimi”

    “Sasa panga siku”

    “Nisingependa ichukue muda mrefu, unaonaje kama tutasubiri kwa wiki mbili hivi?”

    “Si mbaya”

    “Si najua kuna matayarisho ingawa nisingependa iwe ndoa ya sherehe kubwa”

    “Sawa”

    Siku iliyofuata Abdi alimzuia Shamsa kuja kazini kwa ajili ya maandalizi ya ndoa yetu. Abdi ndiye aliyeshughulikia kila kitu. Kutoka siku ile nilikutana na Shamsa mara mbili tu.

    Baada ya hapo sikukutana naye tena hadi siku ya ndoa yetu. Ndoa ilifanyika usiku. Niliozeshwa mke msikitini saa mbili usiku. Baada ya ndoa, mimi, Abdi na wasindikizaji wetu tulikwenda nyumbani kwa shamsa. Nikampa mke wangu mkono.

    Usiku huo huo nikamchukua mke wangu nyumbani kwangu. Hakukuwa na sherehe kubwa. Abdi aliniambia sherehe kubwa itazusha umbeya.

    Baada ya kuoana na Shamsa ndipo nilipoanza kusahau kwetu. Msichana alinionesha mapenzi ya kisomali ambayo nilikuwa siyajui. Aliniheshimu, alionesha upendo wa dhati na alijivunia kuolewa na mimi.

    Siku zikapita. Biashara ya hoteli ilikuwa inakwenda vizuri. Abdi aliniruhusu kuchukua kiasi chochote cha pesa ninachotaka kila mwezi ila niweke katika hesabu.

    Aliniambia kuwa kila mwaka tutakuwa tunagawana mapato.

    Kwa vile nilishadhamiria kuendelea kuishi Somalia nilikubaliana naye.

    Sikuona kitu cha kunirudisha nyumbani. Nilikuwa na nyumba nzuri ya kuishi. Nilikuwa na gari zuri la kutembelea

    nilikuwa na kazi nzuri iliyokuwa ikinipatia kipato cha kutosha, isitoshe nilikuwa na mke mzuri wa kunituliza. Sikuona sababu yoyote ya kutaka kurudi Tanzania.

    Siku moja baada ya chakula cha usiku, Shamsa aliniambia.

    “Unajua huyu ndugu yako Abdi ana siri kubwa sana”

    “Siri ya nini?”

    “Unajua alitaka kukuozesha wewe mke lakini yeye hana mke?”

    “Hivi hana mke, siku zote ananiambia mke wake yuko kwao. Kumbe ananidanganya”

    “Hana mke”

    “Aliachana naye au hajaoa”

    “Ni afadhali angeachana naye”

    “Kumbe…!”

    “Kulikuwa na tetesi kuwa alimuua!”

    “Ha! Unaniambia ukweli? Kwanini amuue mke wake? Alimkosea nini?”

    “Ni afadhali angemkosea lakini hakumkosea kitu chochote”

    “Alimuua bure bure tu?”

    “Alimuua kutokana na imani zake za kishirikina”

    Nikanyamaza kimya na kumtazama Shamsa ili aendelee kunieleza.

    “Huyu ni mtu tajiri lakini anataka utajiri zaidi…”

    “Una maana kwamba alimuua mke wake ili apate utajiri kwa njia za kishirikina?”

    “Ina fanana na hivyo lakini yeye aliambiwa na mganga wake kuwa katika familia yao kuna jini la utajiri. Mganga alimwambia hivyo baada ya kuona ile pete anayovaa, alimwambia ile ni pete ya jini ambaye ukiwa naye unakuwa tajiri wa kupindukia”

    Hapo ndipo nilipoanza kuzinduka.

    Shamsa akaendelea kunieleza kuwa alivyoelezwa na Abdi mwenyewe kuwa asili yake ni mzigua. Baba yake alitoka Tanga, Tanzania. Alikuwa mvuvi wa samaki. Siku moja boti aliyokuwa anavulia samaki na wenzake ilipata hitilafu wakiwa baharini.

    Walikokotwa na maji hadi katika pwani ya Somalia. Wenzake wane walifariki dunia lakini yeye alipona. Baada ya kuokolewa na wavuvi wa Somalia alihifadhiwa kwenye nyumba ya mvuvi mmojawapo na akalowea huko huko Somalia.

    Shughuli zake zikawa ni zile zile za uvuvi. Akaoa mke wa kisomali akamzaa Abdi na mdogo wake ambaye anaitwa Yusufu.

    Abdi hakupata elimu yoyote lakini ni mjanja, ana akili ya kuzaliwa. Tangu akiwa mtoto alionekana kuwa na kipaji.

    Alipokuwa mkubwa alijiingiza katika biashra za magendo ya pembe za ndovu zilizompa utajiri mpaka akaweza kununua hoteli anazomiliki pamoja na kuanzisha miradi mengine.

    Baba yake Abdi alikufa wakati Abdi akiwa mkubwa. Huyo baba yake ndiye aliyekuwa na ile pete aliyokuwa anavaa Abdi. Abdi aliichukua siku baba yake alipokufa akaivaa yeye bila kujua maana yake.

    Kwa vile Abdi ni mpenda ushirikina alikuwa mganga wake mzee mmoja mrefu ambaye alimwambia kuwa ile pete ni ya jini mwanamke ambaye alikuwa mke wa babu yake aliyekufa zamani huko Tanga.

    Abdi akaambiwa kwamba kama atampata jini huyo na atamuoa na yeye atakuwa tajiri. Hapo ndipo Abdi alipopata kichaa. Akaanza kufanya makafara ya kumvuta huyo jini lakini ilishindikana.

    Akaambiwa na mganga, kwa vile yeye ameshaoa mke, huyo jini hawezi kumpata kwani jini huyo haendi kwa mtu mwenye mke wake. Asubiri kama mke wake atakufa ndio huyo jini anaweza kumpata.

    Abdi akaona hakuwa na sababu ya kumtaliki mke wake akamtilia sumu kwenye chakula ili afe. Baada ya kumuua mke wake akarudi tena kwa yule mganga. Akafanyiwa makafara lakini huyo jini hakutokea.

    Safari hii akaambiwa kwamba huyo jini tayari ana mtu mwingine na mtu huyo ni ndugu yake aliyeko Tanga, yaani mwana wa baba yake mdogo.

    Akaambiwa ndugu yake huyo anaitwa Umari au Amiri au Amour na nyota yake ni Nge.



    Shamsa aliendelea kunieleza kuwa mganga alimwambia Abdi kuwa dalili ya kumtambua huyo ndugu yake ni kuwa anapokabiliwa na hatari jini wake anajigeuza joka kubwa na kuwashambulia watu wanaotaka kumdhuru huyo ndugu yake.

    Siku moja wakati Abdi yuko kwenye boti yake akifuatilia pembe zake za ndovu kutoka Tanzania, alielezwa na nahodha wa boti iliyotoka Tanzania kuhusu mkasa uliowafika ambapo baada ya kumkamata mtu waliyemdhania kuwa ni mpelelezi likatokea joka ambalo liliwaua wenzake.

    Abdi aliposikia mkasa huo akayakumbuka yale maneno ya mganga wake kwamba huyo ndugu yake mwenye huyo jini, jini wake hujigeuza joka.

    Shamsa alinieleza wazi kuwa mimi ni ndugu yake Abdi na jini anayemtaka Abdi ni Zena.

    Siku ile nilipokutana na Abdi kwenye ile boti, Abdi aliniambia.

    “Wewe unaitwa Umar au Amiri au Amour”

    Nikamwambia ninaitwa Amour.

    Akajua ndio mimi mwenye huyo jini aliyekuwa anamtaka. Maelezo ya Shamsa yalinifanya nigundue sababu ya Abdi kunichukua kwa nguvu huko Somalia.

    Mganga wake pia nilishamfahamu, alikuwa ni yule mzee mrefu wa kisomali.

    Kumbe ndiyo maana yule mzee alinifuata usiku akanichukua pale hoteli kimiujiza na kunipeleka katika shimo. Kumbe alikuwa ananifanyia uganga wa kumpata Zena!

    Halafu siku ile Abdi alinipeleka kwa yule mganga ambaye alifanya makafara yake mpaka Zena akatokea na kumpiga kofi, mimi na Abdi tukakimbia. Kumbe zile zilikuwa jitihada za kumpata Zena!

    Shamsa alinieleza kuwa mganga alishindwa kumchomeka Zena kwa Abdi na hivyo walibuni mpango mwingine.

    Mpango huo ulikuwa ni wa kuniua mimi kikatili. Abdi aliambiwa anikamate na kunining’iniza kichwa chini kisha atoboe utosi wangu kwa msumari. Damu itakapotoka aikinge kwenye kikombe cheupe kisha ajipake yeye kwenye utosi wake ili aweze kumpata Zena.

    “Shamsa umeijuaje habari yote hii?” nikamuuliza Shamsa baada ya kunieleza mkasa huo.

    “Hii ni habari ya siri, usimwambie Abdi na wala usiniulize nimeijuaje isipokuwa mtahadhari Abdi. Abdi ni ndugu yako lakini ni mshenzi. Au utakataa kwamba huna baba yako mdogo aliyepotea baharini miaka ya nyuma.?”

    “Yupo. Niliambiwa kuwa alipotea baharini lakini mimi nilikuwa mdogo au sijazaliwa”

    “Basi ndiyo hivyo”

    “Siku zote nilikuwa ninajiuliza kwanini Abdi amenileta hapa Somalia kwa nguvu, kwanini ananiita ndugu yake na kwanini alilitambua jina langu mara tu baada ya kuniona. Kumbe kuna vitu vilivyojificha nyuma ya pazia

    “Pia nilikuwa nikijiuliza kwanini alinipeleka kwa yule mganga na kwanini Zena alitokea na kumpiga kibao…”

    “Amekubali apate gharama za kukuweka wewe hapa Somalia, lengo lake ni hilo”

    “Nashukuru kwa kunifahamisha. Sasa unanishauri nifanye nini?”

    “Endelea kumuangalia tu, jifanye kama hujui lolote”

    “Si anataka kuniua?”

    “Huo mpango wao bado, siku watakayotaka kufanya hivyo nitakwambia”

    “Mh! Kwa kweli umenitia hofu!”

    “Una maana kwamba huniamini mimi mke wako?” Shamsa akaniuliza.

    “Ninakuamini” nikamjibu.

    “Kama unaniamini endelea kuniskiliza mimi na fuata vile ambavyo nitakwambia”

    “Sawa. Lakini ninataka kujua wewe umejuaje habari zote hizo?”

    “Mimi niko karibu sana na Abdi”

    “Na kuhusu upande wa baba yangu mdogo aliyekuja huku Somalia umejuaje habari zake?”

    “Hakuna kisichofahamika Amour. Au ulikuwa hutaki miye mke wako nijue habari zako?”

    “Hapana. Ukijua habari zangu ni vizuri kwa sababu mimi ni mume wako”

    “Sasa tulia. Endelea na kazi yako kama kawaida, zungumza na kaka yako Abdi bila uoga, siku ya watakayopanga kufanya ushenzi wao nitakwambia siku moja kabla na nitakupa mbinu ya kufanya”

    “Nakushukuru sana mke wangu kwa kunizindua. Umejibu maswali yangu mengi niliyokuwa nikijiuliza bila kupata majibu. Ninaamini kuwa wewe ni mke wangu wa kweli”

    “Na mimi nakushukuru sana mume wangu kwa kunisikiza na kuniamini. Wewe utakuwa mume wangu wa kudumu”

    “Asante sana”

    Shamsa alitabasamu kisha akanipiga busu kwenye shavu langu.

    “Hebu niambie ilikuwaje siku ile kwenye ile boti wakati wale jamaa walipotaka kukutosa?” akaniuliza.

    Nikamueleza Shamsa ilivyokuwa.

    “Lilipotokea hilo joka na kuwazamisha hao waliotaka kukutosa, wewe ulifikiri nini?” akaniuliza.

    “Leo ndio nimepata jibu kutoka kwako. Hilo swali nilikuwa nikijiuliza sana. Nilikuwa sijui ni kwanini lile joka linetokea na lilitoka wapi. Kumbe ni jini linalonifuata mimi”

    “Kumbe wewe siku zote tunaishi lakini kulikuwa na kitu unanificha!”

    “Kitu gani?”

    “Kwamba una jini wa kike mwenye utajiri”

    “Kwa kweli niliogopa kukutia hofu. Huyu jini mimi simtaki na amekuwa akinifanyia vituko vingi sana mpaka nimekimbia huko kwetu…”



    Sikutaka kumueleza mengi kwamba jini huyo hataki nioe mke wa binaadamu, anataka nimuoe yeye.

    Nilidhani Shamsa angeniuliza ni vituko gani alivyokuwa akinifanyia huyo jini lakini hakuniuliza.

    “Sasa mwenzako anamtaka huyo jini kwa udi na uvumba” akaniambia.

    “Kwa kweli kama alifikia kumuua mke wake kwa sababu ya jini ambaye hamjui, ni mtu hatari na mshirikina sana”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ile mirungi anayokula inaharibu akili yake lakini mwenyewe hajui. Inamfanya awaze utajiri wakati wote. Na kila apatavyo hatosheki”

    “Mtu namna ile mwisho wake ni kufa tu. Wahenga wanasema tamaa mbele mauti nyuma binaadamu katikati”

    Shamsa akacheka.

    “Amour umenichekesha!” akaniambia huku akiendelea kucheka.

    “Kweli kabisa. Mtu namna ile mwisho wake ni kufa tu”

    “Akifa wewe na Yusufu mtarithi mali zake”

    “Ni mpaka aandike hivyo”

    “Hata asipoandika ni lazima mtamrithi”

    “Yusufu hatakubali”

    “Labda kwa hapo. Lakini kama atamwambia kuwa wewe ni ndugu yao, unaweza kupata sehemu ya mali yake”

    “Siwazii sana huko, mimi nawazia maisha yangu yatakavyokwenda. Naona sitakaa sana hapa Somalia”

    “Hutakaa sana utakwenda wapi?”

    “Nitarudi kwetu”

    “Na mimi utaniacha na nani wakati nimeshakuwa mke wako?”

    “Nitakuomba twende tukaishi Tanzania, si utakubali?”

    Shamsa akabetua mabega yake.

    “Nitakubali, nitafanyaje sasa wakati umeshanioa!”

    Jibu lake lilinifurahisha nikamvuta kwangu na kumkumbatia. Shamsa alijilegeza nikamtuliza kifuani kwangu. Nilikuwa nikiusikia moyo wake ulivyokuwa ukipiga taratibu, pu! pu! pu!

    Kwa vile aliendelea kutulia kifuani kwangu na mimi niliendelea kumkumbatia.

    ***********

    Asubuhi ya siku iliyofuata nilikwenda kazini kwangu huku nikijua kuhusu mambo kadhaa ambayo nilikuwa siyajui.

    Moja ya mambo hayo ni kuhusu Abdi kunileta pale Somalia kinguvu na kunipa shughuli ya kufanya.

    Sasa nilijua lengo la Abdi lilikuwa ni kumtaka jini aliyekuwa akinisumbua ili apate utajiri.

    Kama ni hilo tu nisingeshituka wala nisingejali. Abdi amekwenda mbali zaidi kutaka kuniua. Jambo hilo halikuwa la

    kupuuza. lakini nilimtegemea sana Shamsa aliyenidokolea siri hiyo.

    Kutokana na mpango wake huo niliamini kwamba Abdi alikuwa mpumbavu sana. Ushirikina wake ulikuwa ni wa hatari na si wa kupuuzwa na mtu yeyote mwenye akili timamu.

    Nilipofika kazini kwangu niliendelea kufanya kazi huku nikiwa nimetingwa na mawazo ya mchanganyiko. Mara kwa mara Shamsa alikuwa akinipigia simu kuniuliza jinsi nilivyokuwa ninaendelea na kazi.

    “Naendelea vizuri” nilimjibu.

    “Abdi hajafika hapo?”

    “Hajafika bado”

    “Tafadhali usimuulize chochote”

    “Sitamuuliza kitu”

    “Na wewe pia kuwa na amani. Usiwaze sana”

    “Nisiwaze nini?”

    “Yale niliyokueleza jana usiku”

    “Yale hayapo tena kichwani mwangu, naendelea na kazi yangu”

    “Sawa”

    Nilipomaliza tu kuzungumza na Shamsa nilimuona Abdi akiingia ofisini kwangu. Uso wake ulikuwa umetaharuki.

    Kabla hata ya kunipa salamu aliniambia.

    “Watu wengine sijui wana tabia gani?”

    Jinsi nilivyouona uso wake umetaharuki na yale maneno aliyosema, vilinishitua nikamuuliza.

    “Kuna nani?”

    “Si huyu mpuuzi!”

    “Nani?”

    “Yusufu ameondoka nyumbani kwake tangu jana. Hajamuaga mke wake anakwenda wapi. Mke wake sasa ananisumbua mimi!”

    “Una maana kwamba tangu jana hajafika nyumbani kwake?”

    “Hajafika na hajulikani yuko wapi”“Kwani walikuwa na ugomvi?”

    “Hawakuwa na ugomvi wowote. Yule mdogo wangu tu hana akili. Ndio maana sielewani naye”

    “Sasa atakuwa amekwenda wapi?”

    “Nitajuaje?”

    “Mh…!”

    Pakapita kimya kifupi Abdi akionesha kuchukizwa akaniambia.

    “Nimekufuata twende kituo cha polisi kumuulizia”

    “Unadhani atakuwa amekamatwa?” nikamuuliza.

    “Si lazima awe amekamatwa, anaweza kuwa amepata ajali na ripoti yake kufikishwa polisi”

    “Haya twende”

    Tukatoka mimi na Abdi. Tulijipakia katika gari lake na kuelekea kituo cha polisi.

    Vile tulivyokuwa tumekaa pamoja ndani ya gari niliyakumbuka maneno ya Shamsa kuhusiana na Abdi, nikaona kama niliyekuwa nimekaa na nyoka mwenye sumu kali.

    Tukaendelea na safari.

    Nilikuwa nikimfahamu vizuri Yusufu mdogo wake Abdi ingawa hakuwa karibu sana na mimi. Muda mwingi alikuwa akishughulika na mambo yake mwenyewe.

    Niligundua pia kuwa Abdi hakuwa akisikizana sana na mdogo wake jambo ambalo lilifanya mara kwa mara wakwaruzane.

    Lakini ndugu ni ndugu. Licha ya kuwepo kwa hali hiyo, Abdi alipopata habari kuwa mdogo wake alikuwa hafahamiki alipo ameanza kupata wasiwasi na kumuhangaikia.

    Tulifika kituo cha polisi ambapo Abdi alikuwa akifahamika vizuri. Aliwaeleza polisi tatizo lake.

    Polisi hao wakamfahamisha kuwa hawakuwa na taarifa yoyote ya mdogo wake.

    “Amepotea tangu lini?” Polisi mmoja akamuuliza.

    “Si kwamba amepotea bali hajulikani yuko wapi”

    “Tangu lini?”

    “Tangu jana alipoondoka nyumbani kwake hajarudi hadi sasa na hajulikani yuko wapi”

    “Ana mke na watoto”

    “Ndio ana mke na watoto”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hakuwahi kumwambia mke wake anakwenda wapi?”

    “Huyo mke wake ndiye aliyenifahamisha mimi kuwa Yufusu hajarudi nyumbani tangu jana”



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog