Search This Blog

WAKALA WA SHETANI - 4

 





    Simulizi : Wakala Wa Shetani

    Sehemu Ya Nne (4)



    Ng’wana Bupilipili aliposhtuka, alijikuta amelala kwenye kitanda kilichoashiria kuwa pale ni hospitali. Alijiuliza amefikaje mahali pale, akajikuta akichanganyikiwa. Alipotaka kuamka, mwili wake haukuwa na nguvu na kumfanya arudi kulala kitandani.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Akiwa bado amejilaza na maswali lukuki yakiendelea kupita kichwani kwake, ghafla mlango ulifunguliwa, Ng’wana Bupilipili alifumba macho kwa haraka na kutulia tuli kitandani kusikilizia aliyeingia ni nani.



    “Itakuwa amepata nafuu,” ilikuwa ni sauti ya kiume.

    “Ni kweli, ilionesha alitumia nguvu nyingi sana pia mwili umepungukiwa maji.”

    “Atakuwa anatoka wapi?”

    “Hilo swali tumsubiri aamke mwenyewe.”

    “Kwa hiyo tumuache alale?”

    “Hapana mshitue aamke ili apewe uji wa maziwa na baadaye chakula aweze kupata nguvu, zaidi ya hayo hana tatizo kubwa.”

    Baada ya muda, Ng’wana Bupilipili alisikia akitingishwa taratibu huku akiitwa.

    “Mama mdogo... mama mdogo.”

    “Mmh,” Ng’wana Bupilipili aliitikia kama yupo usingizini.

    “Dokta anaamka.”

    “Muamshe kabisa kisha fanya nilivyokueleza, mimi nipo ofisini taarifa zingine utaniletea.”

    “Sawa dokta.”

    Yote Ng’wana Bupilipili aliyasikia na kuamini sehemu aliyokuwepo ni salama kwake. Alipoitwa mara ya pili aliitikia huku akifumbua macho, akakutana na muuguzi mbele yake.

    “Pole,” muuguzi alisema kwa sauti ya upole.

    “Asante.”

    “Unajisikiaje?”

    “Mwili hauna nguvu.”

    “Basi amka upate uji kisha ule chakula utajisikia vizuri.”



    Ngw’ana Bupilipili aliamka kitandani kwa msaada wa muuguzi na kukaa kitako, muuguzi alitembea naye akiwa amempa msaada wa kumshika mkono hadi chumba cha chakula. Alimketisha kwenye kiti na kumletea uji wa maziwa ambao aliunywa wote.



    Baada ya kunywa uji, alijikuta akitokwa na jasho jingi, muuguzi aliyejitambulisha kuwa anaitwa Sabina alimuonesha bafuni ambako alienda kujimwagia maji na kupata nguvu. Alirudi naye chumba cha chakula na kumpatia chakula ambacho nacho alikila chote kuonesha alikuwa na njaa kali.



    Baada ya kula alirudishwa wodini ili apumzike kabla ya kuonana na mganga mkuu. Baada ya nusu saa, alifuatwa na muuguzi kupelekwa kwa mganga mkuu. Ng’wana Bupilipili aliongozana na yule muuguzi akijua lazima kuna maswali ya kuulizwa juu ya kuwepo pale na mahali alikotokea.



    Aliingizwa katika ofisi ambayo haikutofautiana na ya Father Joe, pia mganga mkuu alikuwa Mzungu. Alipowaona wanaingia, aliacha kazi zake na kuwakaribisha.

    “Ooh, karibuni.”

    “Asante,” alijibu Ng’wana Bupilipili.

    “Pole na matatizo.”

    “Asante.”

    “Unaitwa nani?”

    “Malimi,” Ng’wana Bupilipili alidanganya.

    “Unatokea wapi?”

    “Kijiji cha Sanza.”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kijiji cha Sanza mpaka huku umefikaje?”

    “Kulitokea vita ya familia ambayo ilifanya wanakijiji tutawanyike na kukimbia kusikojulikana kuokoa maisha yetu.”

    “Umetumia muda gani kufika barabara kuu?”

    “Siku tatu.”

    “Mmh, pole sana.”

    “Asante.”

    “Una mpango gani?”

    “Kwa kweli mpaka sasa sijajua niende wapi hata hapa nimefika sijui ni wapi?”

    “Hapa ni Sangema, je, upo tayari kurudi kijijini kwako?”

    “Bora nife lakini sipo tayari kurudi huko.”

    “Una familia?”

    “Yote imeteketea vitani.”

    “Pole sana.”

    “Asante.”

    “Basi mama, sijui unaitwa nani?”

    “Baba si nimekueleza naitwa Malimi.”

    “Ooh samahani, sasa mama Malimi utaishi hapa kwa vile kituo hiki kinatunza watu wenye shida.”

    “Nashukuru baba yangu, asanteni kwa moyo wenu wa kujitolea Mungu awazidishie.”

    “Amen.”

    “Sabina kamuoneshe chumba apumzike mambo mengine atapangiwa kesho.”

    Sabina alimchukua Ng’wana Bupilipili na kwenda kumuonesha chumba cha kupumzika.



    MIAKA SABA BAADAYE

    Kusekwa aliendelea kukua vizuri akiwa katika kambi aliyoachwa huku akiendelea na masomo ya awali ya chekechea wakati akiandaliwa kwenda shule ya msingi. Kabla hajaanza shule ya msingi, alitokea Mzungu mmoja aliyekuwa akimiliki machimbo ya dhahabu.



    Mzungu huyo aliyejulikana kwa jina la John Brown ‘Mr Brown’ alikuwa na mgodi mkubwa uliokuwa na wachimbaji wengi sana. Kutokana na uwezo wake wa kifedha aliweza kuwasaidia wanakijiji waliokuwa jirani na machimbo yale. Alijenga zahanati na



    miradi ya maji na umeme ambayo ilikuwa msaada tosha kwa wanakijiji ambao walifaidika na machimbo yake.

    Mr Brown ndani ya eneo lake la machimbo alijenga shule kwa ajili ya watoto kuanzia miaka miwili na kuendelea. Sifa zake zilizagaa kila kona ya nchi na kuifanya serikali impunguzie kodi pamoja na kumpa misamaha katika vitu alivyokuwa akiingiza nchini.Kingine ambacho kiliungwa mkono na wengi ilikuwa ni kuwachukua walemavu wa ngozi (albino) ambao walianza kusoma pale na baadaye kuwapeleka nje ya nchi kwa masomo zaidi.





    Kusekwa naye alichukuliwa na Mr Brown na kuanza masomo yake ya darasa la kwanza.

    Baada ya miezi miwili, Kusekwa alipata nafasi ya kusafiri kwenda Ulaya kimasomo. Aliandaliwa sherehe kama wenzake waliotangulia na safari yake ilikuwa siku ya pili alfajiri.



    Kama kawaida, Kusekwa alikwenda kulala kusubiri asubuhi asafiri. Siku hiyo alilala sehemu tofauti na anapolala siku zote. Majira ya saa nane za usiku, alishtushwa na watu walioingia chumbani kwake wakiwa wameziba nyuso zao, kabla hajajua nini kinaendelea alivamiwa na kuzibwa mdomo kisha alibebwa juujuu na kupelekwa asikokujua.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kusekwa alibakia na mawazo wale ni akina nani na mbona wamembeba vile au ndiyo mtindo wa wote wanaosafiri kwenda Ulaya? Alijifikiria kama wangekuwa ni majambazi au watu wabaya wamepitia wapi mpaka kuingia kule chumbani kwenye kambi yenye ulinzi mkali?



    Alijikuta akiwa njia panda huku wale watu wakimpeleka kimyakimya bila kuongea chochote. Baada ya muda, aliingizwa kwenye chumba kimoja ambacho kilikuwa na kiti na kukalishwa pale. Baada ya kukalishwa, mtu mmoja aliwasha swichi, mikono na miguu ya Kusekwa ilishikiliwa na vyuma.



    Kusekwa alizidi kushangaa watu wale kumfanya vile walikuwa na shida gani tena walionesha siyo wema kwake. Baada ya kubanwa na vyuma, mashine iliwashwa ili kumkata viungo. Lakini ilikuwa ajabu mashine iligoma kuwaka, kitu kilichowachanganya wale watu na kujaribu mara ya pili lakini iligoma.



    “Sasa itakuwaje?” Mmoja aliuliza jasho likimtoka baada ya mtambo kugoma.

    “Tatizo hili lilitokea hata mwezi uliopita tulipotaka kumkata viungo yule albino lakini baadaye ilikubali na kufanya kazi yake.”



    Kauli ile ilimshtua sana Kusekwa na kuona kumbe safari ya Ulaya ni kifo, alianza kulia kwa sauti kuomba msaada lakini aliambulia makofi yaliyomfanya anyamaze kusubiri hatima yake. Alimuomba Mungu kwa kila lugha aliyoifahamu. Aliiomba mizimu ya baba na mama yote imtangulie kumponya katika kinywa kile cha mauti.



    Walikubaliana kumfungua ili kurekebisha ule mtambo ambao uligoma kukata viungo vya albino. Walimfungua Kusekwa ambaye alikuwa amepoteza fahamu kwa woga wa kupoteza maisha. Walimlaza chini na kuanza kuufanyia matengenezo mtambo ili uweze kufanya kazi yake vizuri.



    Walijitahidi kufanya kazi kwa haraka ili waifanye kazi kwa wakati na kurudisha salamu kwa Mr Brown. Wakiwa katika hali ya kutengeneza mtambo, walimuacha Kusekwa amelala chini kwenye sakafu akiwa kifua wazi. Kutokana na ubaridi wa kwenye sakafu uliosababishwa na kiyoyozi, Kusekwa alizinduka.



    Alipofumbua macho taratibu, aliwaona wabaya wake wakihangaika kutengeneza mtambo wa kukatia viungo vya albino. Alitembeza macho taratibu na kuangalia mandhari ya mle ndani na kugundua kuna mitambo mingine miwili na milango minne, kati ya hiyo mitatu ilikuwa wazi.



    Ndani ya kile chumba kilichokuwa na mtambo mmoja wa kukatia viungo na mitambo mingine ambayo hakuifahamu, pia kulikuwa na majokufu yaliyoonekana yana kazi ya kuhifadhi viungo vya albino.



    Watu wale walikuwa wamemsahau na akili zao zote zilikuwa katika mashine. Akiwa bado amejilaza chini bila kujitikisa kwa kuogopa kumuona na kuhamishia mawazo yao kwake, Kusekwa alipata wazo la kutoroka kwa kunyata huku akimuomba Mungu aweze kutoka salama.



    Kabla hajachukua uamuzi huo ambao kwake ilikuwa ni kama kucheza mchezo wa pata potea. Umeme ulikata ghafla na wote waliokuwa katika kile chumba walishtuka, alimsikia mmoja akisema.



    “Huu mkosi gani? Mashine ilibakia kidogo kieleweke, kukatika kwa umeme kumeturudisha nyuma kabisa.”



    “Unajua kazi hii tunaidharau lakini inaweza kututoa jasho,” mwingine aliongeza.

    “Wasiwasi wenu tu, umeme unawaka na kazi inaendelea, tatizo tumeshalijua hatutachukua muda mrefu kulitatua,” wa tatu naye alisema.



    Kusekwa aliwashangaa wale watu ambao hawakuwa na chembe ya huruma kwa kutengeneza mtambo ule haraka ili wamgawanye viungo vyake bila huruma. Akiwa bado amejilaza chini, aliwashangaa watu wale pamoja na umeme kukatika hawakumgusia yeye zaidi ya mtambo uwahi kupona na kumtenganisha viungo vyake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Aliamini muda ule wakati wauaji wasio na huruma wakisubiri umeme uwake naye angejaribu bahati yake ya kutoroka. Alinyanyuka taratibu pale chini alipolazwa na kuanza kutembea kwa mwendo wa kunyata. Aliutafuta mlango, akafanikiwa kuupata na kutoka kwa kunyata bila kujua anaelekea wapi.



    Aliendelea kutembea kuelekea nje katika giza nene huku akimuomba Mungu amuepushe na kikombe kile. Baada ya kutembea kwa muda huku akipapasa na kuomba Mungu umeme usiwake upesi, alijikuta akijigonga kwenye kitu, alipopapasa aligundua ni gari.



    Alipopapasa vizuri aligundua ile ni Toyota Pick Up, akiwa anajiuliza pale ni wapi, mara umeme uliwaka. Kusekwa alijiona yupo kwenye maegesho ya magari ambayo yalikuwa na magari mengi, kabla hajaamua afanye nini aliwasikia watu wakielekea kwenye ile gari wakizungumza.



    “Inabidi tuwahi kuondoka muda huu mzigo umefika tangu saa saba.”

    “Itakuwa vizuri, Mr Brown alikuwa hana raha kabisa.”



    Sauti zile zilimfanya Kusekwa aingie chini ya gari ile na kujificha, akiendelea kumuomba Mungu. Kuwaka kwa umeme kulifanya eneo lote ling’ae kama mchana na kumfanya aamini lazima atakamatwa kutokana na kuwaona askari wakipishana kuhakikisha ulinzi wa mule mgodini.



    Ndani ya chumba cha kukatia viungo vya albino, baada ya umeme kurudi wauaji wale walishtuka kukuta Kusekwa hayupo sehemu waliyokuwa wamemlaza Kusweka.



    “Wazee yule mtoto amekwenda wapi?” mmoja alishtuka na kuuliza huku macho yakiwa yamemtoka pima.

    “Si alikuwa amelala hapa?” mmoja alionesha kwa kidole alipokuwa amelala Kusekwa.

    “Utani huu, au ametoroka?”

    “Inawezekana lakini hata akitoroka atafika wapi? Lazima tutamkamata tu.”

    “Tatizo si kukamatwa bali kuokoa muda, mtambo bado kidogo ufae, tukimaliza tuanze kumtafuta, kibaya hatujui katokea mlango upi.”

    “Mmh! Kazi ipo jamani, kila mtu atoke na mlango wake ili kumtafuta.”



    Baada ya kupeana majukumu, waliingia kwenye kazi ya kumtafuta Kusekwa ambaye alikuwa bado yupo chini ya gari akisikiliza mazungumzo ya dereva na mwenzake.



    Kila mmoja alikimbia huku akiulizia walinzi kama wamemuona mtoto albino akipita maeneo hayo. Kila aliyeulizwa alisema hajamuona, kila mmoja akapagawa na kujiuliza atakuwa wapi. Wazo la kuwatoroka hawakuwa nalo zaidi ya kufikiria kuchelewa kutekeleza kazi yao kwa muda muafaka.



    Waliamini kabisa mtoto huyo lazima angepatikana asubuhi kama hatajitokeza au kumuona sehemu alipojificha. Kusekwa aliiona miguu ya mbaya wake aliyekuwa amesimama karibu yake kabisa akiwauliza wahusika wa lile gari.



    “Wazee hamjamuona mtoto albino?”



    “Hatujamuona mtu yeyote, tena bahati nzuri tumefika hapa umeme ukiwa umeshawaka lakini eneo hili hatujaona kiumbe chochote, kwani vipi?”



    “Kile kitoto kimetoroka, tulikuwa ndiyo tunatengeneza mtambo kwa ajili ya ishu ya bosi.”

    “Sasa?”



    “Baada ya umeme kuwaka hatukumuona japo tunajua lazima atapatikana.”

    “Sasa fanyeni hivi, toeni taarifa kisha endeleeni na kazi ya kuutengeneza mtambo, mnafikiri atafika wapi? Lazima atapatikana tu. Mkianza kumtafuta hamjui mtachukua muda gani na mkimpata ndiyo muanze kazi ya kutengeneza mtambo.

    “Hamuoni mtachukua muda mrefu? Lakini mtambo ukitengemaa na akipatikana mtafanya kazi kwa urahisi,” dereva wa gari alishauri.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hapo umesema neno, ngoja nitoe taarifa kisha turudi kutengeneza mtambo.”

    Maneno yote hayo, Kusekwa aliyasikia na kuendelea kumuomba Mungu japokuwa aliamini kupona ni sawa na ngamia kupita katika tundu la sindano. Aliomba Mungu wasiliondoe gari haraka kwani lazima angeonekana.



    Wale watu baada ya kusema hivyo, waliondoka na kumuacha chini ya lile gari. Baada ya kuondoka Kusekwa alimsikia dereva akisema:

    “Acha tuwahi, muda umekwenda.”

    Kusekwa alihofia kukanyagwa, alitoka chini ya gari kwa tahadhari kubwa, alipoliangalia lile gari aligundua kuwa nyuma lilikuwa na turubai. Wazo la haraka lilikuwa kuingia nyuma ya gari na kujifunika lile turubai huku akimuomba Mungu atoke salama kwenye mgodi wa kifo.



    Mara gari lilianza kuondoka, mapigo ya moyo yalikuwa yakimwenda kwa kasi, kama mtu angekuwa karibu yake angesikia jinsi moyo unavyodunda. Gari lilipofika getini, askari alilisimamisha.

    “Jamani simameni tukague gari.”



    Kauli ile ilimfanya Kusekwa atokwe na haja ndogo kwa wasiwasi, alimuomba Mungu kwa kujua lazima ataonekana. Gari lilisimama na mlinzi alizunguka nyuma ya gari na kuanza kufunua turubai. Alishangazwa na sehemu moja iliyokuwa na mwinuko.



    Bila kusema neno, alisogea hadi kwenye mwinuko na kufunua. Alipofunua turubai alishtuka kumuona mtoto albino akiwa nyuma ya gari, akiwa amejifunika turubai lile. Alipigwa na bumbuwazi na kujiuliza yule mtoto mbona yumo kwenye lile gari tena kajificha,



    alishangaa kumuona mtoto akimuomba msamaha kwa kukutanisha mikono yake bila kusema neno huku machozi yakimtoka.

    Alikumbuka taarifa ambazo alizipata juujuu kuhusu mauaji ya walemavu wa ngozi kwa imani za kishirikina katika mgodi wa Mr Brown. Aliamini kabisa mtoto huyo alikuwa akitoroka. Alishindwa aseme nini, alibaki kumtazama kwa huruma.

    Dereva baada ya kuona muda unakatika kwa ukaguzi wa dakika mbili, aliuliza:



    “Mzee Kondo mbona unauweka usiku? Umekuta nini naona umeganda?”



    “Hakuna kitu, mnaweza kwenda,” alisema huku akirudisha turubai na kumuacha yule mtoto albino kwenye gari.



    Alimruhusu dereva ambaye aliondoa gari na kutoka nje ya mgodi bila kujua nyuma ya gari kuna mtu. Kusekwa alimshukuru Mungu



    gari kutoka salama mgodini. Gari lilikwenda kwa mwendo mrefu bila Kusekwa kuelewa alikuwa akielekea wapi, akaendelea kujificha kwenye turubai kutokana na upepo mkali. Sehemu moja gari lilisimama, akawasikia wale jamaa wakizungumza.



    “Bwana eeh, tuchimbe dawa hapa.”

    “Siyo mbaya.”



    Kusekwa alitulia wakati watu wale wakiteremka kwenda kujisaidia haja ndogo. Wakati wanaingia kwenye gari ili waondoke,



    Kusekwa aliteremka haraka na kuliacha gari liende. Sehemu aliyoshuka ilikuwa ngeni kwake. Kulikuwa na vichaka ambavyo hakuwa na uhakika wa usalama wake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    baada ya kutoka ndani ya kinywa cha mauti aliamini alikuwa salama, wakati akitafakari afanye nini mara kwa mbali aliona gari likija na kuwasha taa. Kwa woga alikimbia na kujificha nyuma ya kichaka ili wenye gari wasimuone. Gari lilipita bila wale watu kumuona na kumfanya abaki anajiuliza nini cha kufanya.

    Baridi ya alfajiri ilikuwa kali lakini kwa Kusekwa haikuwa shida kwa vile furaha ya kubakia hai ilikuwa zaidi ya baridi ile. Kutokana na kiza cha alfajiri ile aliamua kujilaza pembeni ya kichaka ambacho hakujua usalama wake upo kiasi gani.

    Pamoja na kutetemeka, alimuomba Mungu kupambazuke ili ajue yupo wapi na afanye nini. Pamoja na kuwaogopa wanadamu lakini aliamini wapo wenye roho nzuri kama Father Joe ambaye alionesha upendo wa hali ya juu. Aliwachukia binadamu kama Mr Brown ambao hujionesha wana roho nzuri usoni lakini moyoni wana roho mbaya zaidi ya nyoka.

    Na pia aliamini kabisa Father Joe hajui chochote toka kwa rafiki yake mkubwa, Mr Brown kuwa anawachukua watoto wenye ulemavu wa ngozi na kwenda kuwakata viungo huku akidanganya kawapeleka Ulaya na kumbe Ulaya yenyewe ni kuzimu.

    Kutokana na akili yake kufanya kazi na kujua haki ya mwanadamu inapatikana wapi, alipanga kama atapona katika kile kifo basi atakwenda kwenye vyombo vya sheria. Alikumbuka siku moja aliyoelezwa na Father Joe kuwa kila kitu kinaongozwa na sheria na chombo kinacholinda raia ni jeshi la polisi.

    Alimuomba Mungu aweze kufika polisi kufichua uovu ule wa Mr Brown, kila alipojaribu kufumba macho, jinamizi la kutaka kukatwa viungo lilimjia na kumfanya akae macho mpaka kunapambazuka.

    Kutokana na baridi kuwa kali, ilibidi Kusekwa ajiingize katikati ya kichaka ili kupunguza ukali wa baridi lile. Kwa bahati mbaya, sehemu aliyoingia kulikuwa na nyoka amelala ambaye alimkanyaga. Naye nyoka katika kujitetea alimgonga mguuni.

    Kusekwa alishtuka na kupiga kelele za maumivu, wakati huo nyoka alikuwa akikimbia eneo lile kwa kutoa mlio wa kutambaa. Kusekwa alitoka kichakani mbio huku akishikilia mguu na kusogea barabarani.

    Baada ya kwenda mwendo mfupi kuondoka eneo la tukio akiogopa kushambuliwa tena na nyoka, alianza kusikia kizunguzungu ambacho kiliongezwa na mwanga mkali wa gari uliompiga usoni na kumfanya aanguke chini, hakujua kilichoendelea.

    MIAKA SABA BAADAYE

    Ng'wana Bupilipili alikuwa katika Kijiji cha Sangema kwenye kituo cha kuwatunza watu wenye maisha magumu, baada ya kupata hifadhi. Kituoni hapo hapakuwa tofauti na kituo alichokimbia. Shughuli zilikuwa zilezile za kazi za mikono. Kutokana na uzoefu alioupata, alijikuta akipewa kipaumbele na mkuu wa kituo, Mr Harrison kuwa kiongozi na mwalimu msaidizi.

    Kutokana na kupewa uongozi alijikuta akipata posho ndogondogo tofauti na kituo cha awali ambacho malipo yake yalikuwa kula na kulala. Alijikuta akifurahia maisha kule, kila siku dua zake zote alizielekeza kwa mwanaye Kusekwa ili Mungu amtangulie na kumkinga na roho mbaya za watu na kumpa maisha marefu.

    Aliendelea kuwa mwalimu mwanafunzi pale kituoni, akawa anajifunza asichokijua na kuwafundisha wenzake anachokijua. Kwa kadiri siku zilivyozidi kusonga mbele ndivyo alivyokuwa akiongeza ujuzi wa kazi yake. Siku moja akiwa darasani, juu ya meza ya mwalimu wao kulikuwa na gazeti.

    Ng'wana Bupilipili alilichukua lile gazeti na kuanza kulisoma, ndani yake alikutana na picha yake iliyokuwa robo ukurasa, ikiwa na maandishi makubwa; ANATAFUTWA. Chini ya picha kulikuwa na maneno yaliyosomeka: Mtuhumiwa hapo juu anayetambulika kwa jina la Rozalia Bupilipili au maarufu kwa jina la Ng'wana Bupilipili anatafutwa na jeshi la polisi kwa mauaji ya wanakijiji cha Nyasha pamoja na askari wawili. Ni mwanamke hatari sana mwenye mafunzo ya kigaidi. Yeyote atakayemuona atoe taarifa kituo chochote cha polisi. Zawadi nono itatolewa.

    Ng'wana Bupilipili alishtuka kuona picha yake kwenye gazeti huku akituhumiwa kufanya mauaji ya kutisha ya wanakijiji wa Nyasha pamoja na askari wawili. Aliamini usalama wake upo mashakani, kwani kwa yeyote atakayebahatika kuiona ndani ya kituo kile lazima atamuogopa na kisha kuripoti polisi na kusababisha akamatwe.

    Kwa jinsi ilivyoonesha, gazeti lile lilikuwa la siku ile, hata mkuu wa kituo kile, Mr Harrison alikuwa bado hajaliperuzi. Alipata wazo la kulichana lakini wasiwasi wake ulikuwa mtu yeyote atakayebahatika kuliona gazeti hilo lazima angemtambua. Kwa ajili ya kuhofia maisha yake, alipata wazo la kutoroka eneo lile ili kujiokoa.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alitoka darasani taratibu na kuelekea chumbani kwake, akachukua vitu muhimu tu na kuondoka eneo la kituo bila mtu yeyote kujua. Alijitanda khanga na kuuficha uso wake kwa sehemu kubwa kisha alikwenda hadi kituo cha basi ambako alipanda gari kuelekea asikokujua, akawa anatafuta sehemu za kijijini zaidi ambazo magazeti hayafiki.

    Mr Harrison baada ya kumaliza shughuli zake ndogondogo, alirudi darasani kuulizia wamefikia wapi. Lakini alishangaa kutomkuta mwalimu, ilibidi amuulize kwa wenzake

    "Mwalimu wenu yupo wapi?"

    "Mmh! Alikuwa anasoma gazeti hapo kisha alitoka nje, huenda amekwenda msalani."

    Mr Harison alichukua gazeti lake na kuanza kulisoma taratibu, alipofika kwenye ukurasa uliokuwa na picha ya Ng'wana Bupilipili alishtuka. Aliiangalia ile picha kwa muda kisha akasoma maelezo yake ambayo yalimshtua sana, habari hiyo ilionesha kuwa mwanamke huyo ni hatari sana.

    Ili kutaka ukweli, alitoka na lile gazeti hadi kwa wenzake ambao aliwaonesha ile picha, kila mmoja alimtambua Ng'wana Bupilipili. Kwa vile walijua amekwenda msalani, walimsubiri ili wambane na kumuuliza kuhusu uhusiano na ile picha lakini ajabu muda ulizidi kukatika bila kuonekana.

    Ilibidi ufanyike msako wa siri kutaka kubaini yupo wapi, lakini hakukuwa na taarifa zozote. Mr Harrison alikumbuka kauli za wanawake waliokuwa kwenye mafunzo kwamba baada ya kusoma lile gazeti alitoka darasani. Aliamini kabisa ni mwenyewe na ameamua kukimbia.





    Waliongeza msako kila kona lakini waliambulia patupu. Ng'wana Bupilipili alikuwa ameshapotea eneo lile. Taarifa zile alizirudisha kwa wenzake ambao walipigwa butwaa wasiamini tuhuma zile kuwa zake kutokana na tabia yake ya upole tena yenye huruma na mapenzi kwa watu wote.

    Hakuwa mbaguzi, alikuwa akijitoa yeye kwa wenzake ili kutatua matatizo yao, hata kutoa sehemu ya posho yake kuwasaidia wenzake. Japokuwa picha ilifanana kwa asilimia mia, bado shoga zake walisema siyo yeye. Lakini kizungumkuti kikabakia kama siyo, yeye yupo wapi?

    Lilibakia fumbo zito vichwani mwao, wasijue Malimi kipenzi chao amekwenda wapi.

    ***

    Kusekwa aliposhtuka alijikuta amelala kwenye kitanda cha kamba, alipozungusha macho alijikuta yupo kwenye chumba cha nyumba ya udongo. Alijiuliza pale ni wapi na amefikaje. Alisikia sauti za watu wakizungumza nje ya chumba.

    "Dogo lazima atakuwa ameamka."

    "Ngoja nikamcheki."

    Kusekwa aliangalia mlangoni na kumuona mtu mmoja akiingia, walipokutanisha macho alisema kwa sauti:

    "Ameamka."

    "Poa, njoo naye apate uji na viazi inaonekana hajala tangu jana," sauti kutoka nje ilisema.

    "Hakuna tatizo, dogo amka," jamaa alisema na kumfanya Kusekwa anyanyuke kitandani.

    Alitoka nje ya chumba na kukuta sebuleni kuna watu wengine wawili.

    "Hujambo dogo?" walimsalimia.

    "Sijambo, shikamooni."

    "Marahaba."

    Walimpatia uji na viazi vya kuchemsha, baada ya kula, walimuuliza sehemu waliyomuokota amefikaje na alikuwa anatoka wapi. Kusekwa aliwaeleza yote yaliyomkuta baada ya kuamini wale ni watu wema kutokana na walivyomuokoa na kumtunza kama mdogo wao.

    Jamaa alishtuka na kumpa pole huku wakimhakikishia kuishi naye maisha mazuri pale na kumtafutia shule yenye usalama. Aliwashukuru kwa kumuokoa na kuwa tayari kumlea. Siku ilipita wakimlea kama mtoto wao kwa kumuonesha upendo wa hali ya juu.

    Usiku ulipofika walikwenda kulala na Kusekwa alipewa chumba chake, majira ya usiku wa manane Kusekwa alishtuka usingizi baada ya kuvamiwa na kuzibwa mdomo. Ghafla alisikia maumivu makali mkono wake wa kushoto. Alitaka kupiga kelele lakini mdomo ulikuwa umezibwa.

    Alihisi maumivu makali na kupoteza damu nyingi, aliteseka bila msaada wowote huku akijiuliza wenyeji wake wapo wapi mpaka watu wale wabaya wameingia na kumkata mkono. Baada ya kutoka damu nyingi alipoteza fahamu.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Aliposhtuka alijikuta yupo hospitali lakini hakuwa na mkono mmoja, aliangua kilio kitu kilichofanya wauguzi wafike na kumbembeleza. Baada ya kutulia alielezea yote tangu kuchukuliwa na Mr Brown na kukosa kukatwa viungo na siku aliyovamiwa na watu wabaya na kumkata mkono wake wa kushoto.

    Kwa vile ilikuwa hospitali ya dini walimpa malezi mazuri ya kumfajiri, aliendelea kuuguza jeraha la mkono. Baada ya siku mbili zilipatikana taarifa kuna watu wamekamatwa na mkono wa albino. Kwa vile Kusekwa alikuwa amekatwa mkono siku chache. Alichukuliwa kwenda kuwatambua watu wale japokuwa aliamini kwa usiku alivyovamiwa asingeweza kuwajua.

    Lakini alipofika polisi ilikuwa tofauti na alivyofikiria, watu waliomuokota na kumuahidi kumtunza ndiyo waliokamatwa na mkono wake. Roho ilimuuma na kuona hakuna kiumbe wa kuaminiwa diniani, kama waliomuokota ndiyo waliomtenda.

    Alirudishwa hospitali na watu wale walifunguliwa mashitaka ya kukutwa na mkono wa mtu. Kusekwa naye aliendelea vizuri na jeraha lake ambalo kila siku lilionesha maendeleo vizuri. Baada ya kupata nafuu alihamishwa kutoka wodini na kupelekwa kwenye kituo kidogo cha kulelea watoto yatima ambao huchukuliwa na wafadhili mbalimbali.

    Alikaa pale kwa mwezi mmoja akitunzwa na kupata mafunzo ya awali ambayo alianza kuyapata kwenye mgodi wa Mr Brown. Siku zote alijenga chuki kwa watu, kiumbe aliyemwamini alikuwa mwanamke peke yake. Lakini wanaume wote aliwaogopa kwa kuwaona wana sura za furaha lakini mioyo yao ilikuwa na nia mbaya kwao.

    Alizidi kuwachukia baada ya kuwasikia mganga mkuu na msaidizi wake wakizungumza juu ya wao maalbino kutolewa kafara kwa ajili ya utajiri wa watu. Hakuamini kama kweli Mungu aliwaumba wawe dawa ya utajiri bali viumbe wenye haki ya kuishi kama wengine.

    Alijiuliza haki yake itapatikana wapi kwa vile wale wanaoonekana wema mbele ya watu ndiyo haohao walio mstari wa mbele kusaka roho zao kwa udi na uvumba.

    Baada ya mwezi kupita huku afya yake ya jeraha ikizidi kuimarika, alipewa taarifa ambazo kwa wengine waliamini ni njema lakini kwake haikuwa hivyo. Walielezwa mfadhili atakuja kuwachukua watoto wawili, mmoja akiwa yeye Kusekwa.

    Kilichomshangaza ni kuchaguliwa yeye na mwenzake ambaye alikuwa albino aliyekuwa na umri mdogo kuliko yeye. Alikumbuka jinsi alivyochukuliwa kwenye kambi ya Father Joe na Mr Brown kuwa anakwenda kumtunza kumbe kumtoa roho.

    Alitaka kukataa kwenda popote lakini bado hakutakiwa kuonesha kiburi kwa vile kuna watu wenye roho nzuri kama Father Joe. Hakuwa na uwezo wa kukataa kwenda kwa huyo mfadhili. Alikubali kwa shingo upande huku uhai wake akimkabidhi Mwenyezi Mungu.

    Siku ya kuja kuchukuliwa ilipofika alikutwa akiwa amejipumzisha kwa vile haikuwa siku ya masomo. Aliliona gari likija, halikuwa geni machoni mwake, baada ya wageni kushuka, jicho lake lilitua kwa hasimu wake mkubwa Mr Brown. Akiteremka kwenye gari akiwa na wapambe wake walewale aliokuja nao kumchukua kwa Father Joe.

    Aliamini kabisa Mr Brown hakujua anayemfuata ni Kusekwa, angejua ni yeye asingekuja zaidi ya kuwatuma wapambe wake. Alimuona akitembea kuelekea ofisini kwa mkuu wa kituo kile cha Misheni chenye hospitali kubwa. Moyo ulimlipuka na kujua alichokuwa akikiwaza kilikuwa kimetimia. Mr Brown alikuwa amemfuata kwa kivuli cha wema wa kuwasaidi huku wengi wakijua ni viumbe kama yeye wanapewa upendeleo wa kwenda nje ya nchi kusoma.

    Kumbe ilikuwa safari ya kuzimu yenye maumivu makali ya kukatwa viungo bila ganzi, akiwa bado anatafakari, dada mlezi wa kituo kile alimfuata.

    "Kusekwa jiandae basi wageni wameshafika, tena una bahati nasikia watu wa aina yenu ndiyo hupata nafasi ya kwenda nje kusoma."



    Kusekwa hakujibu zaidi ya kutokwa machozi, Sister Anna alimshangaa Kusekwa alikuwa tofauti na Albino mwenzake aliyekuwa na furaha.

    "Kusekwa mbona unalia hukufurahia safari hii?"

    "Hii dada si safari ya Ulaya bali ya kifo."

    "Kusekwa una maana gani?"

    "Dada ni hadithi ndefu ya maisha yangu, nimeweza kuruka mkojo nikakanyaga kinyesi."

    "Kusekwa una siri gani ya muda mrefu uliyoiweka moyoni mwako?"

    "Wee acha, maisha yangu yamezungukwa na shetani wa mauti."

    "Ni kweli, sasa hivi mmekuwa akitafutwa sana na watu wabaya kwa ajili ya kuwatoa kafara. Ndio maana tumekuwa makini kuwalinda kwa nguvu zote ndani ya kituo chetu, muda wote mmepewa kipaumbele hata wafadhili wanapokuja ninyi ndio mnaotakiwa kuondoka.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Huoni wenzako wana miaka miwili hawakupata nafasi hiyo, lakini wewe na mwenzako mmepewa upendeleo. Huyu mfadhili aliyekuja ni mtu tunayemuamini amekuwa akiwachukua watoto wengi hasa wenye hali kama yako na baada ya muda hutuletea taarifa kuwa amewapeleka nje kusoma."

    "Dada mpaka sasa mmeshampa watoto wenye hali kama yangu wangapi?" Kusekwa aliuliza.

    "Ni wengi hata thelathini wanafika."

    "Mungu wangu!" Kusekwa alishika kichwa.

    "Kwani vipi mbona unanitisha Kusekwa?" Sister Anna alishtuka.

    "Mna dhambi ya kutoa roho ya watu wote hao na kesho kwa Mungu mna la kujibu."

    "Kusekwa kwanini unasema hivyo?"

    "Wote uliompa Mr Brown sasa hivi ni nyama ya udongo wakiwa na viungo nusu."

    "Mungu wangu, unasema kweli! na umemjuaje Mr Brown?"

    "Ndio ushangae kumjua Mr Brown, ni kiumbe mbaya kuliko nyoka aliyelaaniwa na Mungu, cheko lake nyuma ameficha madhambi ya damu za watu wasio na hatia. Kama hapa ameua watu zaidi ya thelathini unafikiri vituo vingine wameuawa watu wangapi?"

    "Kusekwa unayosema ni kweli?" Sister Anna alizidi kumshangaa.

    "Chanzo cha mimi kukatwa mkono kilikuwa yeye, nilikuwa nimepona kwenye kinywa cha mauti na kuangukia kwenye mikono ya viumbe wenye uchu. Nashukuru nimekatwa mkono lakini kwa Mr Brown ningebakia kiwiliwili kisicho na mikono na miguu."

    "Wewee!!"

    "Dada yangu shangaa ya Musa uyaone ya Firauni."

    "Kusekwa, ilikuwaje?"

    Kusekwa alimueleza toka alipokuwa katika kituo cha kulelea watoto wenye matatizo, na chanzo cha yeye kuwa pale. Kutokana na historia aliyopewa mama yake alitoroka baada ya kulipa kisasi cha kuua wanakijiji waliomuua baba yake pamoja na kuchukua mali zao kinguvu yakiwemo mashamba na mifugo.

    Sister Anna alibakia mdomo wazi huku muda ukiwa umekwenda.

    "Lazima nikiri kuwa Mungu mkubwa ndiye aliyeniokoa na mauti yale, nilikuwa nimeshafungwa kwenye mashine tayari kukatwa viungo bila ganzi. Tena kibaya wanaofanya hivyo ni miongoni mwa ndugu zetu tunaoishi nao sehemu moja kutokana na tamaa ya pesa wanakosa utu ndani ya mioyo yao na kututoa uhai wetu ambao hatukupewa kimakosa na Mungu."

    Maneno mazito yaliyochanganyikana na kilio yalimfanya sister Anna kutokwa ma machozi bila kujijua, akiwa hajapata cha kumwambia Kusekwa, walishtuliwa na mkuu wa kituo aliyewafuata baada ya kuona wanachelewa.

    "Anna unafanya nini, mtoto mmoja tayari huyo unafanya naye nini muda wote niliokutuma?" mkuu wa kituo aliuliza kwa ukali.

    "Samahani mkuu, anakwenda kuoga sasa hivi," alimjibu bila kugeuka.

    "Kwa vile hajachafuka kambadilishe nguo tu umlete haraka."

    "Sawa."

    "Haya fanyeni haraka," baada ya kusema vile aligeuka na kuondoka akimuacha Sister Anna akitazamana na Kusekwa. Kama mkuu wa kituo angemuangalia vizuri Anna usoni angegundua kitu, lakini haraka yake ilimfanya afikishe ujumbe kuliko kuwaangalia wahusika.

    Sister Anna alikuwa akitokwa na machozi kwa maneno mazito ya Kusekwa juu ya vijana maalbino wengi waliopoteza maisha yao bila hatia kwa kisingizio cha kupelekwa nje ya nchi kusoma. Alimtazama Kusekwa na kukosa cha kumwambia kwani aliamini kabisa hatakubali kuondoka na Mr Brown baada ya kunusurika kwenye kinywa cha mauti.

    "Sasa Kusekwa tufanye nini?" Sister Anna alimuuliza Kusemwa.

    "Dada Anna mimi huko siendi labda mauti yangu, siwezi kurudi ndani ya kinywa cha mauti."

    "Sawa, sasa tutafanyeje na muda unakwenda?"

    "Mimi natoroka siendi huko."

    "Hata mimi sikushauri uyafuate mauti tena uliyakimbia kwa muujiza wa Mungu , lakini nitamueleza nini mkuu anielewe?"

    "Mweleze ukweli wala usimfiche, acha niondoke eneo hili kabla hajaja tena."

    Kusekwa alikwenda chumbani kwake na kuvaa nguo nzito na viatu na kuondoka eneo la kambi aliyokuwa karibu msitu wa miti ya asili, iliyopandwa kwa ajili ya kulinda mazingira na kutengeneza vyanzo vya maji.

    Kusekwa akiwa amevaa nguo zake za baridi aliingia porini na kuanza kukimbia katikati ya msitu akiwa na mkono wake mmoja lakini alikuwa ameshauzoea.

    ***

    Baada ya Kusekwa kukimbia na kuondoka eneo la kambi ile, Sister Anna alijikuta akitafuta cha kumwambia mkuu wake. Alikwenda taratibu hadi ofisini ambapo mtoto mwingine albino alikuwa tayari ameandaliwa kwa ajili ya kuondoka na Mr Brown.

    Mkuu wake alishangaa kumuona Anna peke yake bila Kusekwa.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Vipi mbona unakuja peke yako?"

    "M..mm...," Sister Anna alikosa jibu.

    "Vipi! Mbona sikuelewi yupo wapi muda unakwenda si unajua wanakaa mbali?"

    Anna alishindwa kujibu na kubakia akitoa macho kama kameza mfupa, kitu kilichomfanya mkuu wake anyanyuke kwa kuwaomba samahani wageni.

    "Jamani samahanini, nakuja?"

    "Bila samahani," walijibu kwa pamoja.

    Alimfuata Anna na kutoka naye nje baada ya kugundua alikuwa na kitu kilichokuwa kikimtatiza kwani haikuwa kawaida yake kuwa vile. Baada ya kutoka naye nje alimuuliza kwa sauti ya upole.

    "Vipi mbona hivyo, Kusekwa yupo wapi?"

    "Kuna tatizo father!"



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog