Search This Blog

WAKALA WA SHETANI - 5

 





    Simulizi : Wakala Wa Shetani

    Sehemu Ya Tano (5)



    "Tatizo! Kusekwa kafanya nini?" Father alishtuka.

    "Father kuna makosa makubwa tutakuwa tumefanya bila kujua."

    "Makosa gani?"

    "Kama ni kweli tutakuwa tumepata dhambi kubwa kwa kutoa roho za albino wasio na hatia."

    "Una maana gani kusema hivyo?"

    Anna alimueleza yote aliyoelezwa na Kusekwa na uamuzi aliochukua wa kukimbia.

    "Anna unasema kweli!?" Father alishtuka sana kusikia vile.

    "Ni kweli, Kusekwa amejuaje kama yule Mzungu anaitwa Mr Brown?"

    "Hapo si ndiyo nashangaa kusikia hivyo!"

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Inaonekana kumbe maalbino wote tuliokuwa tukimpa na kusema anawapeleka nje kusoma kumbe alikuwa akiwakata viungo kwa imani za kishirikina kwa ajili ya mgodi wake."

    "Lakini watakuwa wanamsingizia, mbona hafanani na tuhuma hizo?"

    "Kusekwa aliyosema mwanzo si alitueleza kuwa alitoroka katika mgodi, Mr Brown hana mgodi?"

    "Anao."

    "Na jina siyo lake?"

    "Ni lake."

    "Basi Father umiza kichwa, la sivyo tutaendelea kuwatoa kafara watoto maalbino huku tukijua kinachoendelea, tutakuwa wauaji."

    "Mmh! Hii mpya, sasa tutafanya nini maana jamaa anajua anaondoka na albino wawili?"

    "Hakuna cha kujiuliza, mueleze tumesitisha kuwatoa watoto maalbino."

    "Atanielewa kweli, mtu nilishamkubalia na mtoto tumeshamuandaa na amemuona?"

    "Mimi nafikiri suala la uhai wa mtu si la kufumbiwa macho, kama wewe huwezi niachie mimi nitamueleza. Huoni tuna dhambi ya watoto wote ambao tuliambiwa wamekwenda Ulaya kusoma kumbe ni Ulaya ya kuzimu?"

    "Mmh! Ipo kazi."

    "Father kama huwezi niachie niwaeleze, roho inaniuma sana kuona watoto wote tuliompa Mr Brown amewaua kikatili kwa kuwakata viungo," Sister Anna alisema kwa uchungu.

    "Okay, nimekuelewa niache nikawaeleze kwamba Filipo haondoki."

    Baada ya mazungumzo ya siri waliongozana hadi kwa wageni, mkuu wa kituo baada ya kukohoa akasema:

    "Samahani kwa kuwaweka kwa muda mrefu."

    "Bila samahani," walijibu wote.

    "Kutokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wetu, hatutakupa watoto kwa vile nilipitiwa kuwaeleza kuwa watoto kabla ya kuondoka walitakiwa kuonana na wazazi wao."

    "Mkuu mbona unaharibu mambo, si unajua kampuni yangu inahusika kuwapeleka nje watoto wenye ulemavu wa ngozi?" Mr Brown alilalamika.

    "Ni kweli, lakini hata watoto wasio na ulemavu wa ngozi nao wanahitaji kwenda nje," Father alisema.

    "Ni kweli, lakini wenye ulemavu wa ngozi ndiyo waliopewa kipaumbele kutokana na kusakwa na watu na kuwakata viungo. Hivyo tumewapa kipaumbele wao ili kuwaweka sehemu salama," Mr Brown alitetea hoja yake.

    "Sina hakika kama walemavu wanaoonewa huruma ni wa ngozi tu, mbona wapo wengi?" Sister Anna alihoji.

    "Huo ni mpango uliopangwa mwakani kuwachukua watoto mchanganyiko."

    "Sawa lakini kama nilivyokueleza hawawezi kuondoka bila kuonana na wazazi wao," Father alikataa kuwatoa watoto.

    "Wanakuja lini?"

    "Hawakusema ila walituma ujumbe lazima waonane na watoto wao."

    "Lakini nina siku moja tu, kama vijana hawa ningeondoka nao leo wangeungana na wengine wanane kuondoka keshokutwa, tena wana bahati ya mtende," Mr Brown alizidi kuwatia tamaa.

    "Ni kweli, lakini hatuwezi kukiuka kauli ya wazazi wao kwa vile sisi ni walezi lakini wenye haki ni wazazi wao."

    "Sasa mkuu, mimi nitakuachia hapa kiasi cha pesa wakija wape ili wasikusumbue."

    "Kama pesa hata mimi ningewapa, lakini naheshimu kauli zao kwa vile wao ni wazazi sisi ni walezi tu, hatuna mamlaka ya kwenda kinyume na makubaliano tuliyokubaliana. Mbona waliotangulia tulikupa bila kipingamizi tena wengi kuliko hawa wawili?"

    "Kwa hiyo nisubiri mpaka lini?"

    "Wakija leo nitakujulisha uje kesho, wakija kesho vilevile nitakujulisha, usife moyo."

    "Okay, hatuna jinsi."

    Mr Brown aliondoka akiwa amenyongea baada ya kuwakosa wale maalbino wawili, waliingia kwenye gari lao na kuondoka kurudi mgodini. Baada ya kuondoka walibakia mkuu wa kituo na Sister Anna wakijadiliana.

    "Father umeona?" Sister Anna aliuliza.

    "Nimeona."

    "Anataka kutoa pesa ili awanunue watoto, huoni kama ana maslahi nao?"

    "Ni kweli."

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Sasa hizi taarifa zifike kwenye vyombo vya dola ili wachunguzwe na wakigundulika wachukuliwe hatua kali."

    "Kuna muhimu wa kufanya hivyo, bado siamini kama kweli watoto wote aliowachukua amewaua kwa kuwakata viungo. Kama ni kweli tuna dhambi kubwa ya damu za watoto wale ambao tulijua wapo Ulaya kumbe kuzimu," Father alisema kwa masikitiko.

    "Mkuu hili lisilale, ikiwezekana tukaliripoti leoleo."

    "Hapana Anna tusifanye papara, nitampigia mkuu wa makosa ya jinai, ni rafiki yangu mkubwa. Atakuja hapa na tutamueleza, yote nina imani atayafanyia kazi."



    "Kama ni hivyo itakuwa heri."

    "Sasa Kusekwa atakuwa wapi?"

    "Sijui, nina imani akiwaona wameondoka atarudi."

    Kusekwa baada ya kutoka eneo la kambi, aliingia porini. Kutokana na hofu ya maisha yake, alikimbia kwa muda wa saa tatu bila kupumzika. Baada ya kukimbia kwa muda mrefu alijikuta akichoka na kuamua kujipumzisha kwenye mti uliokuwa na hewa safi.

    Bila kujielewa, usingizi mzito ulimpitia, alishtushwa na sauti za watu waliokuwa wakizungumza. Alipofumbua macho hakuamini kumuona Mr Brown akiwa na vijana wake mbele yake.

    "Bosi huyu si Kusekwa?"

    "Ni yeye, mbona hana mkono mmoja?"

    "Tumuulize."

    Kusekwa baada ya kukurupuka alipokuwa amelala, alitaka kukimbia lakini walimuwahi na kumkamata.

    "Vipi wewe mbona upo hapa?" Mr Brown alimuuliza.

    Kusekwa hakuwajibu, aliangua kilio cha hofu akiamini bado mauti yalikuwa yakimuandama, pamoja na kuyakimbia kila kukicha tangu alipozaliwa. Mr Brown alijifanya msamaria mwema kwa kumbembeleza.

    "Kusekwa usilie, nipo hapa kwa ajili ya kukusaidia, umefikaje huku na muda wote ulikuwa unaishi wapi?"

    Kusekwa hakujibu kitu, aliendelea kulia akiwa amekaa chini, pembeni ya ile barabara kulikuwa na bonde kubwa. Kusekwa wazo lake kubwa lilikuwa kujitupia bondeni, aliona heri afe kwa kujitupa bondeni kuliko kukatwa viungo na Mr Brown.

    Mr Brown aliagiza achukuliwe na kuingizwa kwenye gari, msaidizi wake alimbeba juujuu ili kumuingiza ndani ya gari. Kusekwa, kwa kutumia mkono wake mmoja alimshika jamaa jichoni nusura amtoe jicho, maumivu aliyoyapata yalimfanya amtupe chini.

    Alipofika chini alitimua mbio kuelekea kwenye lile bonde, hawakukubali, walianza kumfukuza ili wamshike. Alikimbia kwa nguvu zake zote ili kujiokoa katika mikono ya wauaji. Mr Brown baada ya kuona Kusekwa amewazidi mbio alisema kwa sauti ya juu:

    "Kama anawasumbua mpigeni risasi ya mguu."

    Kusekwa kusikia hivyo, alijua mauti yapo usoni kwake, bila kuangalia anaangukia wapi alijitupa bondeni. Kilichoendelea hakujua baada ya kujipiga sehemu na kupoteza fahamu.

    Mr Brown hakukubali, aliutaka mwili wa Kusekwa akiwa hai au umekufa, shida yake ilikuwa viungo vilivyobakia. Vijana wake waliingia bondeni kumtafuta. Kutokana na bonde kuwa refu kwenda chini na kutokuwa na njia ya karibu, walisogea mbele kutafuta njia ya karibu kisha kurudi eneo alilojitupia Kusekwa.

    Msako ulichukua zaidi ya saa mbili bila kuuona mwili wa Kusekwa. Kutokana na kina cha bonde kuwa na miti, waliamini huenda amekwama kwenye mti. Waliamua kupiga risasi ovyo kwenye miti, kwa bahati mbaya walikuwa na risasi chache hivyo walishindwa kuendelea kupiga.

    Kingine kilichowachanganya ni giza lililoanza kuingia, waliamua kuondoka huku wakijipanga kwenda kuwaita vijana walinde eneo lile mpaka aonekane. Walielekea katika gari lao ili waondoke huku Mr Brown akimlaumu kijana wake kuonesha uzembe wa hali ya juu kwa kushindwa kuvumilia maumivu ya makucha ya jicho aliyopigwa na Kusekwa.

    "John leo umeniangusha sana."

    "Bosi ningechelewa kidogo angenitoa jicho, aliingiza kucha kwenye mboni ya jicho."

    "Basi ungempigiza chini ili asikimbie kuliko kumuacha vile na kutufanya tuonekane wazembe kila siku kwa mtu mmoja. Mnaona alitoroka na mikono miwili lakini leo tumekutana naye akiwa na mkono mmoja? Tukimpoteza leo tutakutana na mzoga wake ukiwa umemalizwa viungo vyote, siyo sisi tu tunaotafuta viungo vyao, si mnajua kuna migodi mingapi?"

    "Bora iwe hivyo lakini kama ataokotwa na msamaria mwema lazima atatoa siri yetu, mnafikiri kutakuwa na usalama tena kwetu? Lazima serikali itataka kufanya uchunguzi juu ya maalbino wote tuliowachukua kwa kisingizio cha kuwapeleka Ulaya."

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Usemacho ni kweli, lazima tufanye msako wa kufa mtu ili tuhakikishe tunamtia mikononi huyu mtoto la sivyo tutaumbuka," Mr Brown alizungumza akiwa amekunja uso kwa hasira.

    "Ni kweli mkuu, kwa nini usipige simu mgodini ili kuleta jeshi litakalolinda eneo hili kuhakikisha huyu mtoto hatoki na kuangukia mikononi mwetu?"

    "Ni kweli lakini sehemu hii haina mawasiliano kabisa, mbona ingekuwa hivyo ingekuwa rahisi kwetu?"

    "Sasa tutafanyeje na usiku ndiyo unaingia?"

    "La muhimu tuwahi kambini tuchukue baadhi ya watu waje hapa. Nimepata wazo jingine, bora niwaache ninyi hapa ili mlinde eneo hili mimi nitaondoka kwenda kuleta vijana wa kulinda, ambao watawapokeeni au mnasemaje?"

    "Mkuu wazo zuri sana, hata mimi nilikuwa na wazo kama hilo."

    "Okay, mimi niwaache ili niwahi mgodini."

    Kabla hajaingia kwenye gari ili aondoke, lilitanda wingu zito lililoashiria kuteremka mvua kubwa. Mara mvua kubwa ilianza kunyesha, wote walikimbilia kwenye gari na kupandisha vioo juu. Mvua iliendelea kunyesha na kulifanya gari lao kuanza kuserereka kutokana na kulisimamisha pembeni ya bonde lile lenye udongo wa mfinyanzi.

    Dereva alipoona vile, aliliwasha harakaharaka na kuweka ;four wheel drive' kuliondoa lakini alikuwa kama ndiyo analiongeza kulitelezesha kwenda bondeni. Ilikuwa ajabu ya mwaka, kila walivyojitahidi kufungua milango ili waruke nje, iligoma kufunguka huku gari likizidi kuelekea bondeni.

    Wakati huo, mvua kubwa ilikuwa ikiendelea na kusababisha maporomoko ya maji yaliyotengeneza mto kutoka juu ya mlima. Gari lilizidi kuserereka kusogea kwenye ukingo wa bonde hilo na kumfanya Mr Brown na watu wake waanze kuhaha. Gari lilikosa kizuizi na kuporomoka hadi bondeni, likaangukia kwenye maji yaliyokuwa yamejaa na kwenda kwa kasi.Ilikuwa ajabu ya mwaka, kila walivyojitahidi kufungua milango ili waruke nje, iligoma kufunguka huku gari likizidi kuelekea bondeni.



    Wakati huo mvua kubwa ilikuwa ikiendelea kunyesha na kusababisha maporomoko ya maji yaliyotengeneza mto kutokea juu ya mlima. Gari lilizidi kuserereka na kusogea kwenye ukingo wa bonde lile na kumfanya Mr. Brown na watu wake kutahayari. Gari lilikosa kizuizi na kuporomoka hadi bondeni na kuangukia kwenye maji yaliyokuwa yamejaa mtoni na kwenda kwa kasi.

    Gari lilianza kuzama kwenye mafuriko ya maji yaliyotokea juu ya mwinuko, ilikuwa ajabu mvua kama ile ilikuwa haijanyesha kwa kipindi kirefu.

    Haikuwa na tofauti na ile iliyonyesha wakati Kusekwa alipozaliwa.

    Kila walivyojitahidi kujitoa kwenye gari walishindwa, maji yaliwafunika na kujikuta walikosa hewa, wote watano waliokuwa kwenye gari walikuwa wakifa pamoja na mkuu wao Mr. Brown.

    Mvua iliyokuwa ikiendelea kunyesha ilimzindua Kusekwa aliyekuwa amekwama kwenye tawi la mti. Alipotaka kujigeuza alijikuta akiporomoka kutoka juu ya mti na kuangukia kwenye maji yaliyokuwa yakitembea kwa kasi.

    Alipotua, maji yalianza kumsafirisha, alijikuta akipigania roho yake kwa kurusha mkono wake mmoja. Mungu alimsaidia aliweza kukwama kwenye rundo la majani lililokuwa limejikusanya baada ya kutolewa mbali na mvua.

    Kutokana na hofu ya kupoteza maisha kumtawala, alijikuta akipoteza tena fahamu. Alilala kwenye majani mpaka alfajiri aliposhtuliwa tena na sauti za wanakijiji waliomuona.

    Walimchukua na kumpeleka kwa mjumbe wa nyumba kumi ili apate hifadhi kabla ya kuhojiwa ili kujua amepatwa na masahibu gani. Kusekwa hakuamini kujiona akiwa bado yupo hai kwa yote yaliyomtokea baada ya kukutana na Mr. Brown. Kila dakika aliona miujiza ya Mungu iliyomtoa kwenye kinywa cha mauti.

    Baada ya kupatiwa huduma ya kwanza kwa kupewa kifungua kinywa na kupata muda wa kupumzika walimuuliza kwa utaratibu kujua amepatwa na nini.

    Kabla hajatoa maelezo yake zililetwa habari kuwa kuna gari limeangukia bondeni. Waliokwenda kulitazama walirudisha taarifa kuwa ndani ya gari wamekuta kuna maiti tano, ya Mzungu mmoja na Waswahili wanne.

    Wanakijiji waliungana tena kwenda kuzichukua zile maiti na kuzileta kijijini, Kusekwa pamoja na ugeni wake naye alikwenda kuziona maiti hizo. Mawazo yake yalimtuma huenda ni Mr. Brown japokuwa kwa akili ya kawaida alijua haiwezekani.

    Alipofika naye alijipenyeza kwenye kundi la watu, kingine, kilichomshtua ilikuwa kuwaona watoto maalbino zaidi ya kumi wakicheza bila hofu yoyote. Alipojipenyeza alifanikiwa kuziona sura za wabaya wake. Alipoiona maiti ya Mr. Brown aliangua kilio kilichowashtua watu wote waliokuwepo pale.

    Mjumbe alimchukua Kusekwa na kumpeleka nyumbani huku akimbembeleza, lakini haikusaidia kitu aliendelea kulia. Alidhani huenda kuna ndugu yake.

    "Kijana kuna ndugu yako katika wale maiti?" Kusekwa alikataa kwa kutikisa kichwa.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    "Sasa nini kinakuliza?"

    "Hao ndiyo walitaka kuniua."

    "Kukuua?" mjumbe alishtuka.

    "Ndiyo."

    ;Kivipi?"

    Kusekwa ilibidi aanze kumhadithia maneno mazito ya tangu kuzaliwa kwake. Mjumbe aliona maneno yale hawezi kuyasikiliza peke yake akawaita wakuu wenzake na kumuweka chini.

    Kusekwa alielezea safari yake toka kuzaliwa mpaka siku ile aliyofika pale kijijini. Wote waliomsikiliza walishikwa na mshangao wasiamini alichokuwa akikisema.

    "Kumbe hawa ni watu wabaya, kwa vile maiti haina adui wazikwe kaburi moja," mjumbe alisema.

    Walikubaliana kuwazika Mr. Brown na vijana wake kaburi moja. Baada ya mazishi kikao cha kijiji kilikaa mara moja kupanga jinsi ya kumsaidia Kusekwa na kupeleka taarifa serikalini ili kukomesha mauaji ya walemavu wa ngozi na kufanya uchunguzi kwa taasisi zote zinazojitolea kuwasaidia wasiojiweza.

    Mzee mmoja alijitolea kumlea Kusekwa na kumsomesha mpaka mwisho wa elimu yake.

    Wakati huo Ng'wana Bupilipili baada ya kukimbia kwenye ile kambi alijikuta akifikia kwenye Kijiji cha Busesa alichopokelewa mwanaye Kusekwa.

    Baada ya kufika alipokelewa na mzee mmoja aliyekuwa mjane na kumchukua kama mkewe.

    Mpaka mwanaye Kusekwa anafika katika kijiji kile alikuwa na mtoto wa miaka mitatu na mimba juu, mmoja wa watoto wake watatu alikuwa albino.

    Siku moja alisikia taarifa za kuokotwa kwa mtoto albino mwenye mkono mmoja. Jina lake na taarifa zake zilimshtua, alipatwa na shauku ya kumjua huyo mtoto.

    Alikwenda hadi katika nyumba aliyokuwepo Kusekwa, akiwa na hamu ya kumuona huyo mtoto. Alipofika alimuona mtoto mwenye ulemavu wa ngozi akiwa amekaa akicheza na wenzake.

    Alipomuangalia sana mwili ulimsisimka na kuamini kuwa ndiye mwanaye wa kuzaa ambaye wakati huo alikuwa na mkono mmoja.

    Alijikuta akitamka kwa sauti.

    "Kusekwa."

    Kusekwa alishtuka na kugeuka bila kuitikia alimtazama aliyemwita, Ng'wana Bupilipili huku machozi yakimtoka alimwita huku akimfuata.

    "Kusekwa mwanangu."

    Kusekwa naye bila kujielewa alijikuta akinyanyuka na kwenda kumkumbatia mama yake. Ng'wana Bupilipili alijikuta akilia kwa uchungu hasa baada ya kumuona mwanaye akiwa na mkono mmoja. Watu hawakuamini historia iliyojirudia kwa watu waliopotezana kukutana tena.

    Baada ya Ng'wana Bupilipili kumpata mwanaye ambaye hakuwaza hata siku moja kama kuna siku wangeweza kuonana tena, alipiga magoti na kumshukuru Mungu.

    "Asante Mungu, umedhihirisha tena kuwa wewe unaweza kufanya kisichowezekana katika akili za kibinadamu. Huu muujiza ulionifanyia mbele yangu ni zaidi ya kumfufua aliyekufa, ni zaidi ya ngamia kupita kwenye tundu la sindano. Asante Mungu, asante baba, asante kwa kudhihirisha kuwa wewe ni mwanzo na mwisho."

    Baada ya kushukuru alimkumbatia mwanaye na kuwafanya watu wote waone muujiza ambao Mungu ameufanya kwa yeyote anayemuamini. Alimchukua na kurudi naye nyumbani kwake.

    ***

    Taarifa za kuwepo na migodi inayotumia nguvu za kishirikina kuua albino ili wapate mali nyingi zilipelekwa kwenye vyombo vya dola na kufuatia taarifa zile ambazo hata mkuu wa kambi aliyotoroka Kusekwa alikwisha peleka taarifa kwenye vyombo vya usalama.

    Msako mkali ulifanyika katika migodi mingi na watu wote wanaoishi pembezoni mwa machimbo. Wengi walikamatwa na viungo vya albino vilivyokuwa vipo tayari kuuzwa kwa wamiliki wa migodi wenye kuabudu nguvu za giza.

    Mgodi wa Mr. Brown ulitaifishwa na serikali na wote waliobakia katika mgodi huo walikamatwa na kufunguliwa kesi za mauaji. Baada ya operesheni iliyovumbua vitu vingi, serikali ilitoa tamko kwa watu wote kuwa makini na wageni wanaotumia njia za dini au uwezo wa fedha zao kuwasaidia watu huku wakifanya hujuma ya kuliteketeza taifa.

    Kuanzia siku ile ulinzi uliimarika kwa albino wote. Wageni wote waliwekwa chini ya uangalizi mkali na serikali.

    Kusekwa alifanikiwa kusoma akiwa na mkono mmoja na kujiunga cha chombo cha sheria cha kutetea watu wenye matatizo.

    Serikali ilimuongezea elimu, sasa hivi ndiye mkuu wa kitengo cha sheria na anapata mshahara mzuri unaomuwezesha kumlea mama yake na kuwasomesha

    wadogo zake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Huu ndiyo mwisho wa riwaya yetu ila lazima tuamini kila mwanadamu ana haki ya kuishi hakuna mtu aliyeumbwa kwa ajili ya kumpatia mwenzake utajiri kupitia damu yake. Imani potofu imesababisha maisha ya wenzetu wenye matatizo ya ngozi kuwa ya wasiwasi na wengine kuongezewa vilema vya maisha au kuuawa.

    Uhai wao unaonekana na waovu na kunukia kwa kila mpenda pesa. Kila apataye fedha kwa damu ya mtu huwa wakala wa Shetani ambaye ameamua kuwa mfuasi wakek wa kutenda dhambi kila siku.

    Tusifanye hivyo, kila mtu ana haki ya kuishi na kufurahia maisha, siri ya utajiri si kutoa damu ya mtu bali ni kufanya kazi kwa bidii.

    MWISHO.



0 comments:

Post a Comment

Blog