Search This Blog

BABA KIUMBE WA AJABU - 5

 





    Simulizi : Baba Kiumbe Wa Ajabu
    Sehemu Ya Tano (5)


    Pamoja na kujua ubaya wao kwangu, bado sikutakiwa kuua nikijua kabisa chanzo cha kifo kinatokana na nini. Tulilala kila mtu na kitanda chake kwa kuzima taa. Katikati ya usiku niliota ndoto moja baba amegeuka kiumbe cha ajabu chenye manyoya na meno marefu. Nilimuona mama na ndugu zangu wakilia. Kilichonishangaza zaidi alionekana kama kiumbe kisicho na uhai.
    Nilishtuka usingizini na kukaa kitako huku nikijiuliza ndoto ile ina maana gani, Nilijikuta nikishindwa kuelewa ndoto ile ina maana gani na kwa nini baba ageuke kiumbe cha ajabu chenye kutisha? Sauti za kilio nilizozisikia  ilionesha wazi msiba ule ni wa baba. Niliamini ndoto ile iliashilia kifo cha baba lakini kubadilika kwa umbile la ajabu lilikuwa likiashiria nini?
    Lakini sikutaka kuamini moja kwa moja kutokana na kauli ya mganga kuwa baba yangu atakufa kama nikikutana kimwili na mpenzi wangu na sharti lile nililitekeleza.  Niliamini huenda ile ni ndoto ya kawaida tu wala haihusiani na ukweli wowote, kutokana na kutoelezwa chochote na mganga juu ya kupata ndoto yenye kiashirio.
    “Vipi Masalu?” Sauti ya mpenzi wangu ilinishtua nikiwa katikati ya dimbwi la mawazo.
    “Aah… safi tu,” nilijibu huku nikijitahidi kuficha kilicho moyoni mwangu.
    “Safi, mbona umeamka na kukuona ukitupa mikono kama unazungumza na mtu kuna kitu gani kimekusibu?”
    “Mmh! Kweli nimeona ndoto moja imenitisha sana.”
    “Ndoto gani?”
    “Nimeota nyumbani ndugu zangu wanalia baba akiwa amelala kitandani, lakini kitu cha ajabu amegeuka kiumbe cha ajabu chenye kutisha.”
    “Sasa wasiwasi wako nini? hiyo si ndoto tu?”
    “Huenda baba amekufa.”
    “Masalu si ulielezwa atakufa kama tukikutana kimwili?”
    “Ndiyo, hata mimi nashangaa.”
    “Kwani mganga alikueleza nini juu ya njozi utakayoota?”
    “Hakunieleza chochote.”
    “Sasa wasiwasi wako nini?”
    “Kwa vile baba hali yake ilikuwa mbaya, ndoto hii imenitisha sana.”
    “Masalu acha kujitia presha bure, maisha ya baba yako yako mikononi mwako.”
    “Mmh! Sawa, lakini niliingiwa na wasiwasi mkubwa.”
    “Lala mpenzi.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Nashukuru kwa kunipa moyo.”
    “Nipo hapa kwa ajili hiyo.”
    “Asante mpenzi wangu kwa kunijali sina cha kukulipa.”
    “Cha kunilipa baada ya kupona ni ndoa tu.”
    “Omba jingine hilo umepata. ”
    Niliagana na mpenzi wangu kila mmoja alilala, usingizi haukuchelewa kunichukua, haikuchukua muda mrefu njozi ilijirudia, tena safari hii niliwasikia wakilia huku wakitupia shutuma zao kwangu kuwa mimi ndiye chanzo cha kifo cha baba.
    Nilishtuka tena kitandani na kuwasha taa, mpenzi wangu naye alishtuka na kuhoji kwa nini nimeamka tena.
    “Masalu, vipi mpenzi wangu?”
    “Mmh!” niliguna tu.
    “Mbona sikuelewi?”
    “Mmh! Ndoto bado inaning’ang’ania.”
    “Umeota nini tena?”
    “Bado kifo cha baba kinaendelea na safari hii nimewasikia mama na ndugu zangu wakinishutumu ndiye niliyesababisha.”
    “Lakini bado itakuwa ni njozi tu kwa vile mawazo yako yote umeyahamishia huko.”
    “Kwa hiyo nifanyeje?”
    “Hebu iache njozi iishe wala usiamke.”
    “Mmh! Ngoja nijaribu.”
    Nilirudi kulala tena, ajabu nililala mpaka asubuhi bila kuota tena, mpenzi wangu ndiye aliyeniamsha.
    “Masalu.”
    “Naam.”
    “Vipi upo sawa?” 
    “Nipo sawa, vipi?” 
    “Naona leo umelala sana.”
    “Kwa muda huu ni saa ngapi?”
    “Mmh! Ni saa tatu na nusu.”
    “Ooh! Leo nimelala sana.”
    “Inawezekana ni kutokana na kuamkaamka usiku kutokana na njozi ulizoota.”
    “Na kweli.”
    “Vipi uliota tena?”
    “Sikuota, nimelala vizuri.”
    “Unaona wasiwasi wako tu, njozi zingine hutokana  na mawazo ya mtu.”
    “Ni kweli, lakini ziliniweka kwenye hali mbaya kwa vile kama kweli baba atakufa ndugu zangu hawatanielewa.”
    “Wasikuelewe vipi?”
    “Si nitaonekana mimi ndiye niliyemuua.”
    “Masalu acha kujitoa akili, ulikwenda sehemu gani kumroga baba yako?”
    “Sijaenda popote.”
    “Sasa?”
    “Si inaonesha kuwa uchawi umewarudia.”
    “Hukuwaroga?”
    “Ndiyo.”
    “Sasa wewe unaogopa nini?”
    “Mmh! Suala la kuua si la kawaida.”
    “Wangekuua wewe lingekuwa la kawaida au umefurahia kuuawa kwa dada yako Monika?”
    “Swali gani hilo, hujui nilivyoumizwa na kifo cha dada yangu?”
    “Sasa inakuwaje unaogopa vifo vya watu mnajua kabisa hawana nia nzuri na wewe?”
    “Basi tuachane na hayo, tuoge tukapate chai.”
    Niliamka kitandani na kwenda kuoga, baada ya kuoga tulikwenda kupata kifungua kinywa kilichokuwa mlemle kwenye hoteli tuliyokuwa tumepanga. 
    Wiki ilikatika tukiwa tumejificha na mpenzi wangu, hata simu niliamua kuizima ili kuondoa usumbufu wa ndugu zangu. Siku moja asubuhi tukiwa mgahawani tukipata kifungua kinywa niliamua kuwasha simu. Utafikiri kuna mtu alikuwa akisubiri kwa hamu nilipowasha tu simu iliingia. Kuangalia ilionesha namba ya kaka yangu, niliiangalia kwa muda bila kupokea mpaka ikakatika. Haikupita muda simu iliita tena alikuwa dada nayo niliiangalia bila kuipokea.
    “Masalu mbona hupokei simu?”
    “Achana nao.”
    “Kina nani?”
    “Si hawa wapuuzi.”


    “Ndugu zako?”
    “Ndiyo.”
    “Hebu pokea uwasikilize kwa vile hujui wanataka nini?”
    “Achana nao najua wanataka kunijua nilivyo.”
    “Masalu si umeambiwa kuwa sasa hivi mtu hakusogelei, wasiwasi wako nini?”
    “Sina wasiwasi ila sipendi kuwasikiliza kwa vile hakuna jipya la kuniambia.”
    “Wasikilize.”
    “Sitaki, wale sio watu siwezi kuwasikiliza watu wabaya kama wale.”
    Mara simu ya mpenzi wangu iliita aliipokea na kuzungumza.
    “Eeeh...Ndiyo...Shikamoo mama...Ndiyo...Hapana...Lini?..... Leo...Sawa nitamwambia....nitakujulisha....Hapana tupo Mwanza...Sawa mama nitamwambia....Haya mama.”
    Baada ya kukata simu alinigeukia na kunitazama kwa muda.
    “Vipi kuna usalama?”
    “Kiasi.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Kuna tatizo nyumbani kwenu?”
    “Hapana, kwenu.”
    “Kwetu kuna tatizo gani?” nilishtuka.
    “Ndoto yako imekuwa na ukweli.”
    “Ina maana baba amefariki?”
    “Ndiyo, inaonekana hata ndugu zako walikuwa wakikutafuta kukupa taarifa.”
    “Mmh! Sasa itakuwaje?”
    “Mmh! Kazi ipo nataka nikueleze kitu kimoja kabla ya kufanya lolote turudi kwanza kwa mganga.”
    “Kweli hilo wazo zuri. “
    “Vipi mbona unanyanyuka?”
    “Mambo yameharibika, japo alinitenda vibaya lakini kifo cha baba yangu kimeniuma sana.”
    “Utafanyaje imeshatokea!”
    “Lakini mganga si alisema mpaka tukikutana kimwili! Sasa imekuwaje?”
    “Ndiyo maana nikasema twende kwanza tukamuulize kabla hatujafanya lolote.”
    “Naona tusipoteze wakati.”
    “Subiri basi tumalize kunywa chai.”
    “Chai haipandi tena,” nilisema huku nikinyanyuka kwenye kiti.
    “Pole mpenzi wangu.”
    “Bado sijapoa, kifo cha baba kimeniuma sana,” nilijikuta nikidondokwa na machozi.
    “Pole mpenzi,“ mpenzi wangu alinisogelea na kunibembeleza, kitu kile kiliniongeza uchungu moyoni na kuangua kilio cha sauti kilichowashangaza waliokuwepo hotelini. Ilibidi mpenzi wangu anipeleke chumbani.  
                                                                   *****
    Nilipofika hotelini niliendelea kulia kwa sauti ya chini huku mpenzi wangu akiendelea kunibembeleza. Pamoja na yote niliyotendewa na baba, lakini kifo chake kiliniuma sana. Niliweka pembeni ubaya wake na kuyakumbuka mapenzi yake kwangu kipindi chote cha kukua kwangu.
    Nilijua kilichomponza baba yangu ni tamaa ya mali ambayo masharti yake yaliiathiri familia yetu. Nikiwa bado nimeinama nikiendelea kumlilia baba yangu, mpenzi wangu aliniuliza:
    “Kwa hiyo utakwenda kwenye msiba?”
    “Hata sijui nifanye nini?”
    “Lakini jambo hili ni zito si la kukurupuka.”
    “Ni kweli, najua kabisa kifo cha baba ndugu zangu wanajua mimi ndiye mhusika mkuu. Unafikiri nikienda itakuwaje kama siyo kutiana aibu msibani?”
    “Lakini kwa nini tusirudi kwa mganga ili atueleze tufanye nini?”
    “Lakini si mganga alisema mpaka tukutane kimwili, sasa nini kilichomuua baba yangu?”
    “Masalu swali hilo mimi siwezi kukujibu.”
    “Basi twende kwa huyo mganga.”
    Tulikubaliana kwenda kwa mganga kumpa taarifa ya kifo cha baba, tulipofika tulikuta watu wengi, hivyo ilitupasa kusubiri zamu yetu japo niliamini itatuchukua muda mrefu kuonana na mganga. Hatukuwa na budi kusubiri, lakini mganga alipita na mgonjwa akienda naye nyuma ya nyumba, nilijua anakwenda kumfanyia matibabu.
    Baada ya dakika kama ishirini alirudi peke yake na kuniona, alionesha ishara ya kuniita. Nilinyanyuka na kumfuata ndani ya kilinge cha kutibia, baada ya kukaa alisema:
    “Vipi, mbona umerudi mapema?”
    “Baba amefariki jana.”
    “Sasa tatizo nini?”
     Swali la mganga lilinishangaza, baba yangu amefariki yeye haoni tatizo.                 
    “Si ulisema mpaka tukutane kimwili ndipo baba angefariki, au hata kulala chumba kimoja?”
    “Masalu sijakueleza hivyo kuwa muelewa, nilikueleza mpaka mkutane kimwili si kulala chumba kimoja.”
    “Sasa kifo cha baba yangu kinatokana na nini?”
    “Kwa amri ya Mungu.”
    “Si ulisema mpaka tukutane kimwili?”
    “Eeh, lakini na Mungu ana nafasi yake, huamini kuna kifo?”
    “Naamini.”
    “Sasa?”
    “Lakini ndugu zangu waliniomba niokoe hali ya baba, kama amekufa bila mimi kufika si nitaonekana ndiye niliyechangia.”
    “Huo ni wasiwasi wako, baba yako amejiua mwenyewe kwa msaada wa ndugu zako.”
    “Una maana gani kusema hivyo?”
    “Baada ya kushindwa kukudhuru walijaribu uchawi mmoja ambao ni mbaya kuliko kitu chochote. Ule ukifanyiwa huchukui muda lazima ufe, baada ya kuonekana hujali na unajiamini waliamua jambo moja, kukufutilia mbali. Kama si kinga niliyokufanyia sasa hivi ungebaki jina.”
    “Ni uchawi gani?” Kauli ya mganga ilinitisha.
    “Kweli ndugu zako wamekupania vibaya, uchawi uliofanywa ni wa kinyonga, anakamatwa kinyonga mzima anapasuliwa na kuchunwa ngozi. Kisha ngozi yake inawambwa na kupakwa dawa huku likinuizwa jina lako. Ngozi ikikauka na wewe uhai huna.”
    “Du!” Nilishtuka.
    “Ndiyo walivyofanya, kazi hiyo ilifanywa saa sita usiku ili asubuhi ukiamka ukutwe umekufa. Baada ya kutega uchawi wao walikwenda kulala huku mganga akiwahakikishia kuwa asubuhi wakiamka watasikia habari za kifo chako.
    “Lakini ilikuwa tofauti na walivyo fikiria, kinga niliyokuwekea ilifanya kazi, nilikueleza kila watakachokufanyia kitawarudia. Uchawi uliotaka kukuua ndiyo uliomuua baba yako. Ndio maana nilikuambia kifo cha baba yako alijitakia mwenyewe akishirikiana na ndugu zako.”
    “Unataka kuniambia bila kinga nisingeiona leo?”
    “Hilo ni jibu uliza swali.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Kuhusu kwenda msibani itakuwaje?”
    “Ukitaka nenda hawawezi kukufanya lolote.”
    “Hatuwezi kutiana aibu kuwa mimi ndiye niliyemuua baba?”
    “Wataanzia wapi, kwa kitendo walichokitenda jana usiku na leo kukuona hai wamezidi kuchanganyikiwa. Kama wangejua kama ni mimi ndiye niliyekukinga, basi wangenipa pesa nyingi ili wakupoteze.”
    “Kuna umuhimu wa kuongeza kinga mwilini maana kama kinyonga kashindwa lazima wataendelea kutafuta kitu kingine,” nilijikuta nikijihami baada ya kuona vita iliyopo mbele na ndugu zangu ni nzito.
    “Kijana kama kinyonga ameshindwa hakuna kitu chochote kitaweza japo kwa dawa yangu walikuwa wakijisumbua, uchawi ule ni mbaya sana.”
    “Kwa hiyo unaniambiaje?”
    “Ondoa wasiwasi, chochote kitakachokupata si mkono wa mtu bali amri ya Mungu.”
    “Nashukuru mzee wangu.”
    “Basi ondoa hofu hakuna chochote kitakachokukuta, kila atakayekugusa kitamrudia.”
    Niliagana na mganga kisha nilimpitia mpenzi wangu na kurudi hotelini kujiandaa na kwenda msibani. Tukiwa njiani simu ya dada iliita, nilitaka kuacha kuipokea lakini niliipokea ili nijue ana shida gani.
    “Haloo,” nilipokea.
    “Asante Masalu, asante sana.. njoo umle nyama baba,” dada alisema kwa sauti iliyoonesha analia.
    “Tena wewe ndiye ninayekutafuta mchawi mkubwa, nakuapia sitakusamehe wewe na wote hata marehemu baba  mpaka nakufa. Vitendo vyote mlivyonitendea hamkuridhika mpaka mnaitaka roho yangu kwa nguvu? Hivi nikifa mtafaidika nini?”
    “Nani anataka kukuua?”
    “Kitendo mlichofanya wiki moja iliyopita sitawasamehe mpaka nakufa, mnanilaumu nahusika na kifo cha baba. Hebu niambieni mimi nimefanya nini kuchangia ugonjwa mpaka kifo cha baba. Kinyonga mliyemtumia ili mniue ndiye aliyemmaliza baba kwa taarifa yenu.”
    “Ha! Umejuaje?” Dada alishtuka.
    “Nakuapia nilikuwa nina mpango wa kuwasamehe, lakini kwa kitendo mlichokitenda jana saa sita usiku sitawasamehe milele na mimi nitajua cha kuwafanya, endeleeni kuroga nami sasa naingia vitani tuona nani zaidi.”
    Kauli yangu ya vitisho japo sikuwa na nia hiyo ilimfanya dada akate simu.
    “Masalu vipi mbona sikuelewi?” Mpenzi wangu aliniuliza.
    “Wee waache tu.”
    “Nani huyo?”
    “Dada.”
    “Mbona mnatishana?”
    “Namtisha namwambia ukweli!”
    “Kwa nini umewaambia mapema?”
    “Lazima waujue ubaya wao na tena nawafuata msibani wanieleze kisa na mkasa cha kuyatafuta maisha yangu,” nilijikuta nikipandwa na hasira.
    “Punguza hasira tukifika hotelini tutalizungumza, umeshawajua wabaya wako kwa nini uchanganyikiwe?”
    Nilikubaliana na mpenzi wangu kurudi hotelini, tulipofika nilikuwa bado na hasira kwa kauli za dada kuwa nitamla nyama baba yangu aliyefariki kwa ajili yao wenyewe. Nilijikuta njia panda katika maamuzi yangu ya kwenda kwenye msiba wa baba. Nilijikuta nikipata ujasiri wa kwenda kwenye msiba wa baba.
    “Aisee wacha niende kwenye msiba wa baba,” nilimwambia mpenzi wangu.
    “Masalu nakuomba usiende.”
    “Hapana lazima niende.”
    “Panaweza kutokea ugomvi.”
    “Na utokee, tena nakwenda kuwapa makavu.”
    “ Nakuomba usiende mtatiana aibu.”
    “Nisipokwenda watu hawatanielewa.”
    “Bora wasikuelewe kuliko aibu itakayowakuta.”
    “Hakuna aibu, mganga amesema hawatafunua midomo yao kusema lolote kwa kuiogopa aibu.”
    “Mmh! Lakini ningekuwa mimi nisingeenda.”
    “Lazima niende na leo watanitambua, siwezi kuishi na maadui zangu na kuwachekea.”
    ”Hayo ndiyo ninayokukataza, kama huwezi kuzuia hasira zako hakuna haja ya kwenda.”
    “Nitajitahidi lakini moyo unaniuma baada ya kujua ubaya waliotaka kunifanyia usiku wa kuamkia leo.”
    “Lakini si umepata kinga?”
    “Ni kweli, lakini kama nisingepata ingekuwaje?”
    “Ungepotea, lakini nakuomba ulimalize jambo hili kwa busara.”
    “Nimekuelewa.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Nilijiandaa na baadaye tuliondoka na mpenzi wangu ambaye nilimuacha nyumbani kwao na mimi kwenda kwetu. Nilipofika nilikuwa watu wengi wamekusanyika nje ya nyumba yetu wakiwepo wafanyabiashara wenzetu.
    Sehemu kubwa ilikuwa imejaa magari ya watu, nilipoteremka kwenye teksi na kutembea kwenda ndani, kila aliyenitazama alinishangaa. Wengi walinipa pole ya kifo cha baba, niliwaitikia na kuingia ndani. Nilipofika ndani ndugu zangu walishtuka kuniona.
    Sikujali hali ile, niliingia chumba alichokuwa mama, aliponiona aliacha kulia na kunitazama kama kiumbe cha ajabu. Kwa vile kila kitu nilikuwa nakijua sikuijali hali ile na kumsalimia.
    “Shikamoo mama.”
    “Marahaba.”
    “Poleni.”
    “Asante.”
    “Mnazika saa ngapi?”
    “Sijajua mipango yote wanafanya ndugu zako.”
    “Kwani Masalu ulikuwa wapi?” Mama wa jirani aliniuliza.
    “Nilikuwa safari.”
    “Ooh! Pole sana kwa kumpoteza kipenzi baba yako, najua kiasi gani alivyokuwa akikupenda.”
    “Ni mapenzi ya Mungu.”
    “Na kweli, ni yeye aliyetoa na ndiye aliyetwaa.”
    “Kila neno litatimia.”
    “Masalu,” sauti kali ya dada iliniita.
    “Unasemaje?”
    “Njoo nje.”
    “Kufanya nini?”
    “Nimekwambia njoo au nitakutoa kwa nguvu.”
    “Jeuri hiyo huna.”
    “Salome hebu zungumzeni kwa ustaarabu hamjui hapa ni msibani?” Mama aliingilia kati.
    “Kafuata nini? Namuuliza kafuata nini, aliyotaka yamekuwa anataka nini tena?”
    “Tena wewe malaya wa kike funga domo lako,” Kwa mara ya kwanza nilimvunjia heshima dada yangu.
    “Jamani mama Salome ni maneno gani hayo?” Jirani alitushangaa.
    “Samahani jirani naomba utupishe mara moja,” mama alimtoa nje jirani baada ya kuona tunataka kumwaga mtama kwenye kuku wengi.                                            
    Baada ya jirani kutoka nje, tulibakia watatu ndani, mama alisema kwa sauti ya kilio:
    “Salome unafanya nini?”
    “Mama hujui aliyofanya mwanao, kamuua baba kisingizio eti tulitaka kumuua jana.”
    “Una uhakika gani nimemuua baba?” Nilimuuliza.
    “Kumbuka ulipokuja kumuona baba alisema tukuondoe kwa vile unataka kumuua.”
    “Sikiliza wee malaya,” nilimnyooshea kidole dada.
    “Ha! We niliyekushika kinyesi chako unanivunjia heshima?”
    “Tena shetani wa kike, yaani nakuapieni yote mliyoyafanya juu yangu hamkuridhika, mkaamua jana kunifutilia mbali kwa uchawi wa kinyonga? Mama nisikilize vizuri tena kwa makini. Sitaisamehe familia yako mpaka naingia kaburini.”
    “Usitutishe mchawi mkubwa.”
    “Nafahamu kila kitu mnakijua hata mama niliyekuwa nakuamini kwa ajili ya mali unakubali wanao tuishe kwa ajili ya tamaa ya wachache. Nilikuwa na huruma na ndugu zangu na kukubali kuteseka kwa ajili yao, lakini hili la kutaka kuniua sitawasamehe milele.”
    “Muongo mkubwa, wewe ndiye uliyemuua baba.”
    “Mama nimemuua vipi baba?”
    Mama hakujibu alitazama chini kwa aibu, niliendelea kusema kwa hasira lakini sauti ilikuwa ya chini.
    “Dada Salome unajua kila kitu wewe ndiye uliyempa dawa mpenzi wangu anipake ili kuua nguvu zangu za kiume mlifanikiwa. Lakini mlisahau mimi si mzimu wa familia nilijua mlitaka kunitoa kafara kama dada Monika lakini mambo hayakwenda hivyo.
    “Niliweza kupita chini juu na kuweza kuidhibiti hali hiyo, baada ya hapo hamkuridhika mkataka kunigeuza ndondocha mkashindwa na mwisho mkataka kuniua matokeo yake mmemuua baba. Mnakosa haya kunishtumu, hivi uchawi wenu wa kinyonga ungefanikiwa mimi ningekuwa wapi?
    “Nasema hivi naondoka si hamnitaki, naondoka ila nawatahadharisha mkiendelea na mchezo wenu mtapukutika wote kama mlivyomtanguliza baba. Mimi si Monika ni Masalu,” nilisema nikiwa nimebadilika, sikuwa Masalu wa kuonewa tena.
    “Masalu,” Dada Monika alitaka kusema kitu.
    “Kwanza kabla sijaondoka nataka niione maiti ya baba yangu kwa mara ya mwisho.”
    “Hapana Masalu baba huwezi kumuona,” dada Monika aliweka ngumu.
    “Unajua nawastahi sana, najua kila kitu, kama mnataka siri yote nikaitoe kwa watu nje nikatazeni,” nilipiga mkwara mzito.
    “Maiti ya baba yako imeharibika,” mama alisema kwa sauti ya upole.
    “Hata kama iweje ni baba yangu nina haki ya kumuona.”
    “Masalu acha tu baba yako azikwe, ameharibika sana,” mama aliendelea kunibembeleza.
    “Mama mimi si mtoto wako?”
    “Mtoto wangu.”
    “Aliyekufa si baba yangu?”
    “Baba yako.”
    “Basi nipeleke nikamuone.”
    Walitazamana kwa muda kisha mama alisema kwa sauti ya chini.
    “Salome mpeleke mdogo wako akamuone baba yake.”
    “Mama tulizungumza nini?”
    “Salome sitaki ubishi hebu maliza hili kwa nini tuwafaidishe watu?”
    Nilipelekwa chumba ulicholazwa mwili wa baba, nilikuta amefunikwa shuka, niliifungua upande wa kichwani. Kidogo nikimbie baada ya kukuta kiumbe cha ajabu kilichokuwa kama mnyama chenye manyoya na meno ya kutisha. Nililivuta shuka lote, sikuamini nilichokiona. Baba alikuwa amebadilika na kuwa kiumbe wa ajabu, mwili mzima akiwa na manyoya kama mnyama.
    Nilimgeukia dada Salome.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Baba yupo wapi?”
    “Si huyo mbele yako.”
    “Hapana huyu si baba yangu, naomba unioneshe baba yangu,” nilijikuta nikipandwa na hasira.
    “Masalu huyu ndiye baba, tangu alipoanguka kila siku alikuwa akibadilika na kuwa kiumbe cha ajabu mpaka mauti yalipomkuta,” dada Salome alinipa maelezo ya sababu ya hali ya baba kuwa vile.
    “Jamani mmeona mwisho wa ubaya aibu kama hii.”
    Mara mlango ulifunguliwa na kuingia kaka zangu walioonekana wanatoka kunywa.
    Jamani huyu mchawi amefuata nini?”
    “Mama ndiye kampokea,” dada Salome alijibu.
    “Toka nje, hebu kalete panga amfuate baba.”
    “Kama jana mlishindwa kuniua kwa uchawi wa kinyonga na matokeo yake mkamuua baba, hamtaweza kuniua kamwe. Nitaondoka kwa kupenda si kwa kulazimishwa na familia ya wanga.”   
    Baada ya kusema vile niligeuka na kutoka nje, bila kuzungumza na mtu niliwapita watu ambao hawakuelewa kinachoendelea. Nilielekea barabarani na kukodi teksi iliyonipeleka nyumbani. Nilimpigia simu mpenzi wangu anifuate nyumbani. Alishangaa na kuniuliza:
    “Vipi mbona unasema upo nyumbani kwako wapi, msibani?”
    “Noo, kwangu kabisa.”
    “Utani huo, si ulikwenda msibani au baba yako hakufa?”
    “Amekufa.”
    “Sasa mbona upo nyumbani?”
    “Ni hadithi ndefu njoo mara moja nyumbani.”
    “Nakuja.”
    Nilikata simu na kujilaza kwenye kochi nikiwa bado hasira imenijaa moyoni. Baada ya muda mpenzi wangu alifika nyumbani na kunikuta katika dimbwi la mawazo. Hata alipoingia sikumuona alinishtua kwa kuniita.
    “Masalu....Masalu.”
    “Ee..eeh.”
    “Jamani mbona hivyo?”
    “Aah, umekuja saa ngapi?”
    “Ndiyo naingia, mbona umerudi mapema  mmeshazika?”
    “Bado.”
    “Sasa mbona umerudi?”
    “Wee acha tu.”
    “Kuna nini tena?” Aliniuliza kwa mshtuko kidogo.
    “Wee acha tu.”
    “Niache nini Masalu! Hebu nieleze kuna nini?”
    Sikuwa na budi kumueleza niliyokutana nayo msibani, mpenzi wangu aliniangalia kwa huruma na kusema:
    “Lakini Masalu we mbishi sana, si nilikueleza usiende ukabisha.”
    “Ilikuwa lazima niende kwenye msiba wa baba yangu kwa vile unanihusu.”
    “Japo unakuhusu lakini mazingira yake hayakuwa mazuri.” 
    “Yawe mazuri vipi ikiwa aliyekufa ni mzazi wangu?”
    “Sawa mzazi wako lakini unajua kifo chake kilitokana na nini, Na dada yako  baada ya kifo cha baba yenu maneno aliyokuambia, sasa nini kigeni kwako?”
    “Nimekuelewa, lakini watanitambua.”


    “Lakini Masalu we mbishi sana, si nilikueleza usiende ukabisha.”
    “Ilikuwa lazima niende kwenye msiba wa baba yangu kwa vile unanihusu.”
    “Japo unakuhusu lakini mazingira yake hayakuwa mazuri.” 
    “Yawe mazuri vipi ikiwa aliyekufa ni mzazi wangu?”
    “Sawa mzazi wako lakini unajua kifo chake kilitokana na nini, Na dada yako  baada ya kifo cha baba yenu maneno aliyokuambia, sasa nini kigeni kwako?”
    “Nimekuelewa, lakini watanitambua.”
    “Masalu jambo hili linahitaji utulivu, nakuomba tuondoke hapa twende sehemu yoyote ili upate utulivu wa moyo.”
    “Nashukuru kwa kunipa moyo na kuwa mtu wangu muhimu.”
    “Najua upo katika kipindi kigumu hivyo nahitaji kuwa karibu yako na kuhakikisha hupati mawazo mabaya. Nina imani utavuka kipindi hiki kigumu.”
    “Nashukuru sana, sasa tutakwenda wapi?”
    “Twende Musoma au Shinyanga.”
    “Mi nafikiri Musoma panafaa.”
    “Vipi kuhusu duka linaendelea?”
    “Hata najua.”
    Kwa kweli nilijibu nikiwa sijui nini kinaendelea, muda mwingi nilifikiria maisha yangu kuliko biashara kilichokuwa kikinisaidia ni pesa kidogo zilizokuwa kwenye akiba yangu pia mpenzi wangu naye alichangia kwa kiasi kikubwa kutokana na uwezo wa familia yake.
    “Nakuomba kitu kimoja, funga duka kisha tuondoke, na msiba ukiisha usifanye biashara yoyote bila kumshirikisha yule babu. Si alikuambia biashara zenu zinaendeshwa na kidonda chako na maiti ya dada na mtoto wa dada yako?”




    “Na kweli basi nitampigia simu anayetunza funguo za duka ili asilifungue tena.”
    “Sio alifungue anaweza kuombwa funguo na dada zako na kufanya jambo lolote dukani kwako wale sasa si ndugu bali maadui  zako.”
    “Na kweli wacha nimwambie aniletee funguo kabisa.”
    “Hilo ndilo jambo muhimu.”
    Nilimpigia simu anayetunza funguo za duka ili asifungue pia aniletee funguo. Alikubali ataniletea baada ya kutoka msibani, lakini nilimuomba aniletee muda ule, alikubali na kuniahidi kuniletea baada ya muda mfupi. Tulikubaliana na mwenzangu baada ya kupata funguo za duka tuondoke mchana ule kwenda Musoma.
    Kwa vile safari ilikuwa ya kuchukua hata wiki mpenzi wangu alirudi kwao kuchukua nguo za kuvaa na kuniacha nikijiandaa. Muuzaji wangu aliniletea  funguo na kushangaa kuniona nipo nyumbani badala ya msibani.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Bosi mbona haupo msibani?”
    “Nitakuja baadaye.”
    “Sawa lakini nimeacha maandalizi ya mwisho kwenda kuzika.”
    “Nakuja muda si mrefu.”
    “Haya wacha niwahi.”
    Tuliagana na kuniacha nikimsubiri mpenzi wangu ambaye alikuja baada muda si mrefu. Tuliongozana hadi Buzuruga na kukata tiketi ya basi la Musoma, tulifika Musoma jioni na kupanga tatika Hoteli ya Orange Tree iliyokuwa ipo katika hali nzuri, tulipanga pale kwa wiki nzima nikiwa nimezima simu ili kujiepusha na maneno ya ndugu zangu.
    Kwa mara ya kwanza baada ya kipindi kirefu kuogopa kufanya mapenzi na mpenzi wangu nikihofia kusababisha kifo cha baba tuliweza kufanya mapenzi bila hofu ya kila kitu huku mpenzi wangu akifurahia starehe ya siku ile huku akiniahidi nifanye haraka kumuoa.
    Nilimuahidi kufanya vile baada ya matatizo kutulia kwa kuonesha mapenzi ya dhati kwangu kipindi chote cha matatizo. Kipindi nilichopitia kama mwanamke asiye na mapenzi ya dhati lazima angenikimbia lakini wa kwangu hakunikimbia zaidi ya kunipa moyo.
    Baada ya wiki tulirudi Mwanza na kwenda moja kwa moja kwa mganga, baada ya kuniona alinieleza hali ilivyokuwa juu ya mipango ya ndugu zangu.
    “Kijana japo ndugu zako walijaribu kutaka kukuangamiza lakini matokeo yao ni kufilisika kwa kasi ya ajabu, aibu itakayowakuta juu yako watakuja kukuomba msamaha. Ulichokifanya ni kitu cha busara sana kama ulivyonieleza mawazo yote kakupa mpenzi wako nina imani hiki ni kipindi cha kukaa pamoja na kupanga maisha yenu.
    “Kuhusu duka nilitalifanyia zindiko kuhakikisha ndagu ya familia haikupati, na kazi hii itafanyika usiku huu. Tutaondoka pamoja hadi kwenye duka lako tutaingia ndani na kuua uchawi ambao ungeweza kupoteza mali yako yote iliyo humo ndani.”
    Nilikubaliana na mganga usiku nimfuate na gari, nilimueleza mwenzangu na kurudi kwenye hoteli yetu. Majira ya saa tano usiku tulimfuata na kwenda moja kwa moja kwenye duka, alifanya zindiko lake kisha tulifungua duka, alifanya dawa zake kisha tulimrudisha na sisi kurudi hotelini kulala mpaka siku ya pili.
    Tangu siku ile niliendelea na biashara zangu kama kawaida huku sehemu kubwa ya mambo yangu nikiwashirikisha marafiki zangu na upande wa mpenzi wangu ambao waliahidi kunisimamia katika mambo yangu yote.
    Nilishukuru Mungu biashara zangu zilikwenda vizuri tofauti na ndugu zangu ambao walianguka anguko la aibu. Sikuwaonea huruma kwa vile hawakuwa watu wema kwangu. Pamoja na ubaya wao wote  taarifa za kufilisika kwa haraka sikuzifurahia.
    Dada mkubwa alianza kuchanganyikiwa na kutembea akizungumza peke yake, watu wa karibu waliniomba niinusuru aibu ya familia. Katika mtu aliyeniuma alikuwa mama yangu mzazi ambaye siku zote aliona aibu kwa niliyotendewa na baba na ndugu zangu na yeye kukaa kimya.
    Nilijiuliza nikimfuata nyumbani na kuwakuta na ndugu zangu ambao walinigeuza mchawi itakuwaje? Taarifa za kusikitisha zilisema sehemu kubwa za maduka zimefilisika na wafanyakazi wengine wamekimbia na  pesa baada ya malimbikizo ya mshahara.
                                                                ****
    Hali ilizidi kuwa mbaya zaidi baada ya kushindwa kulipa mikopo mikubwa ya benki kufikia hatua ya kufilisiwa vitu vyao kwa kupigwa mnada zikiwemo nyumba na magari. Ilibidi ndugu zangu warudi kuishi nyumba ya wazazi ambayo siku zote haikufanyiwa ukarabati. Kila aliyenielezea anguko la familia yangu huku wakiishi maisha ya kubahatisha aliniomba niinusuru kutokana na maisha yangu kuwa na uafadhali mkubwa.
    Taarifa za utajiri wa ndagu zilisambaa kila kona kama moto kwenye majani makavu ambao uliipaka matope mazito familia yetu. Kilichowashangaza watu wengi ni anguko la familia yangu lakini upande wangu mambo yaliendelea kuninyookea.
    Niliamua kumchukua mama yangu na kukaa naye, kila tulipokuwa wawili mama alitumia muda mwingi kuniomba msamaha kutokana na yote waliyonitendea. Nilimueleza mama sitaweza kumlaumu ila sitawasamehe ndugu zangu.
    “Mwanangu Masalu nakuomba nipo chini ya miguu yako wasamehe ndugu zako, hali yao ni mbaya sana.”
    “Mama siwezi kuwasamehe mpaka nakufa.”
    “Nakuomba nipo chini ya miguu yako tunaadhirika.”
    “Mama kama ningekufa angewasamehe nani?”
    “Ni kweli walikuwa na dhamira mbaya kwako lakini ilikuwa ni shinikizo la baba yako.”
    Pamoja na mama kunibembeleza sikuwa tayari kuwasamehe ndugu zangu, muda ulikatika huku nikiendelea na maisha yangu huku nikiishi nyumba moja na mpenzi wangu Mary, baada ya mama kuwepo pale nilipanga mipango ya ndoa kwa kuamini msimamizi yupo.
    Siku moja nikiwa mjini nilishtuka kumuona dada yangu akiwa nusu uchi huku akiomba kwa watu, muonekano wake alionekana mtu aliyerukwa na akili. Nilipatwa na mshtuko wa ajabu na moyo kuniuma, nilibakia nikimtazama kwa muda huku machozi yakinitoka.
    Kwa vile nilikuwa ndani ya gari nililipaki gari pembeni na kujikuta nikilia kwa uchungu huku nikisikia sauti ya mama kuwa niwasamehe ndugu zangu. Taratibu donge la kisasi liliyeyuka  moyoni mwangu na kuamua kusikiliza kilio cha mama yangu  juu ya ndugu zangu. Lakini sikuwa na jibu la moja kwa moja, niligeuza gari na kwenda kwa mganga Pasiansi kuulizia kama nitaweza kuwasaidia ndugu zangu.
    Nilipofika kwa mganga nilikuta watu wengi kama kawaida, aliponiona pamoja na kuwa na watu wengi kwa vile alinizoea alinipa upendeleo. Nilipofika aliniuliza:
    “Vipi una shida gani?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Nilimweleza ombi la mama kuwasamehe ndugu zangu na hali ya dada yangu, baada ya kunisikiliza kwa kina mganga alisema:
    “Nimekuelewa, hakuna tatizo lolote kama wewe utakubali kuwasamehe ndugu zako.”
    “Na kuhusu dada yangu?”
    “Alichotaka kukufanyia ndicho kilichomrudia lakini kama umemsamehe kazi ya kumtibu si ngumu.”
    “Nimemsamehe kwa vile kisu kimegusa mfupa.”
    “Basi mleteni hapa apate tiba.”
    Baada ya makubaliano na mganga nilirudi nyumbani na kumueleza mama kuwa nipo tayari kuwasamehe ndugu zangu na kumtibu dada, mama alifurahi sana. Niliwatuma watu wamkamate dada ambaye nilimpeleka kwa mganga, kutokana na tatizo lake alikaa wiki moja na kurudi katika hali ya kawaida. Baada ya kupona mama alimueleza kuwa mimi ndiye niliyemsaidia baada ya kuugua wendawazimu.
    Nilimueleza mama akimtoa kwa mganga amrudishe nyumbani kwangu, jioni niliporudi nyumbani nilimkuta na mama wamekaa sebuleni wakitazama runinga. Aliponiona naingia alinikimbilia na kunipigia magoti kuniomba msamaha.
    Nilimuwahi kumnyanyua na kumweleza yaliyopita yamepita ni wakati mwingine wa kujipanga upya na kujenga familia iliyo imara. Maneno yangu yalimliza dada yangu na kujikuta akisema:
    “Sasa tungekuuwa tungepata faida gani, nani angetusaidia kama hivi?”
    “Dada yamekwisha naomba ya zamani tuyasahau.”
    ”Ni kweli kaka lakini ulichonifanyia Mungu pekee atakulipa.”
    “Amina.”
    Baada ya kumrudisha dada nilifanya utaratibu wa kuwakusanya ndugu zangu, baada kuwakusanya. Tulikaa kikao cha kifamilia kuondoa tofauti zetu huku ndugu zangu wakitokwa na machozi kwa yote waliyoyafanya. Nilimshukuru Mungu kuturudisha katika mapenzi ya awali nami niliwaheshimu kama ndugu zangu japo hawakuwa na kitu. Nilijitahidi kuhakikisha kila ndugu yangu anakuwa na maisha mazuri baada ya Mungu kuniangazia mafanikio.
    Leo hii ninavyomalizia kutoa ushuhuda huu, kila ndugu yangu ana duka lake japo si kubwa kama enzi za baba la kutumia ndagu ya kidonda. Lakini maisha yaliendelea huku tukimalizia siku zote za maisha kurudi kwa Mungu ili atuongoze na kutuepusha na maisha machafu.
    Maisha sasa hivi ni mazuri huku Mary akiwa mke wangu wa ndoa, japo inauma baada ya mama yangu kufariki miezi minne baada ya ndoa yangu. Nitaendelea kumuombea mama yangu kipenzi Mungu ampe mapumziko ya milele. Pia baba yangu japo alikuwa chanzo cha matatizo kwenye familia.
    Naamini Mungu ni mwenye huruma hivyo atamsamehe kwa kujua udhaifu wa sisi wanadamu. Namalizia kwa kuwaomba wote tumtangulize Mungu kwa kila kitu ili tusiishi maisha ya mashaka kwa kuwategemea miungu watu. Mungu anatupenda tumtegemee yeye siku zote.


    MWISHO


0 comments:

Post a Comment

Blog