Search This Blog

BABA KIUMBE WA AJABU - 4

 





    Simulizi : Baba Kiumbe Wa Ajabu
    Sehemu Ya Nne (4)


    ILIPOISHIA


    Baada ya kusema yale aliondoka kipande cha mti wa mnyaa sikioni na kuutupia kwenye kapu la dawa lililokuwa pembeni yake.
    “Umesikia?”
    “Ndiyo.”
    “Yaliyozungumzwa yana ukweli?”
    “Ndiyo.”
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Unajijua kuwa wewe ni maiti?”
    “Maiti?” Kauli ya mganga ilinishtua sana.
    “Hujijui?”
    “Sijijui.”
    “Mpaka sasa hivi upo sawa kama nduguzo?”
    “Kivipi?”
    “Viungo vyako vipo sawa?”
    “Vipo sawa.”
    “Kipi kilichokuleta hapa?”
    “Mambo mengi.”
    “Moja wapo?”
    “Ni mengi ila kubwa ni hii hali iliyojitokeza hivi karibuni ya kufa nguvu za kiume.”
    “Hujui sababu zake?”
    “Najua.”
    “Sasa nini kimekuleta huku?”
    “Mwenzangu alinieleza unaweza kunisaidia.”
    “Nikusaidie nini?”
    ”Kuitoa hali hii?”
    “Kidonda umeridhika nacho?”
    “Nasikia nikikitoa panaweza kutokea matatizo katika familia yetu.”
    “Kama unajua hivyo kwa nini unataka dawa ya nguvu za kiume?” 
    “Kama utajiri ni wao lakini mapenzi ni haki yangu ya msingi.”
    “Sikiliza kijana usijitoe akili,  kwa jinsi alivyokuelekeza dada yako mkubwa juu ya kupona nguvu zako za kiume, nini kitampata baba yako?”
    “Kwa hiyo nibaki na hali hii milele?”
    “Ni uamuzi wako, kupona upoteze watu au uendelee kuwa maiti inayotembea ili kuiokoa familia yako. Na hiyo mosi familia yako sasa hivi itakutuliza ndani kwa kupooza miguu, utakuwa wa kula na kulala wao wanaponda maisha.”
    “Eti?”
    “Ukweli ndiyo huo mpango huo utatekelezwa mara moja baada ya kuonekana umekuwa mkaidi.”
    “Sikubali.”
    “Kama hukubali utafanya nini?”
    ”Nitatibiwa kila kitu nihakikishe napona na litakalowatokea watajijua wenyewe.”
    “Usiseme kwa hasira, upo tayari kuisambaratisha familia yako?”
    “Nipo tayari.”
    “Kwa kukupa mfano mdogo, dawa utakayokunywa itarudisha nguvu zako za kiume, lakini ukirudi nyumbani utamkuta baba yako yupo hoi kitandani.”
    “Kitakachofuata?”
    “Siku ukifanya mapenzi ndiyo siku ya kifo chake.”
    “Mmh!” Niliguna.
    “Ukweli ndiyo huo, chagua kusuka ama kunyoa?”
    Nilibakia kimya kwa muda nikiwaza nitakachokifanya na matatizo ambayo yangeikuta familia yangu. Nilikuwa radhi kuendelea na kidonda changu na kukosa nguvu za kiume. Lakini maelezo ya mganga kuwa wanataka kunigeuza msukule kwa ajili ya kuendeleza mali kilinichanganya sana. 
    Kufikia pale nilijikuta nikichanganyikiwa na kushindwa niegemee upande gani, lakini niliamini maisha yangu ni muhimu kuliko kitu chochote chini ya jua. Vilevile  sikuwa tayari kumhurumia mtu aliyepanga kuniangamiza kwa ajili ya tamaa zake za mali.
    Uamuzi nilioamua ni kujitengeneza mimi na lolote litakalotokea kila mmoja ataubeba msalaba wake.
    Baada ya kukaa kimya kwa muda mrefu mganga alinishtua.
    “Vipi umeamua nini maana naona umekaa kimya?”
    “Mzee wangu mambo ni mazito kila ninalofikiria naliona zito.”
    “Kwa hiyo tuache kama ilivyo?”
    “Mzee wangu huna ufumbuzi mwingine usio na madhara?”
    “Sikiliza kijana wewe unajua matatizo ya familia yenu kuliko mimi, hebu nisaidie nifanye nini?”
    “Wewe si ndiye mtaalamu ninayekutegemea?”
    “Hutaki kunisikiliza, kwani mimi napenda kuona matatizo, lakini mambo yenyewe yamekaa vibaya.”
    “Kwa hiyo?”
    “Nimekueleza yote una uamuzi wako mwenyewe wala siwezi kukuingilia lakini ukweli ndiyo huo.”
    “Basi fanya unavyoweza.”
    “Vipi?”
    “Utakaloliona linafaa.”
    “Kijana acha kujitoa akili, mimi sipo hapa kwa ajili ya kuwachagulia wateja jinsi ya kufanya.”
    “Mzee wangu kwa vile mpango wao ni mbaya kwangu naomba unisaidie mimi.”
    “Kwa hiyo upo tayari kwa lolote litakalotokea?”
    “Nipo tayari.” 
    Leo nitaanza kukupa dawa ya kurudisha nguvu za kiume, lakini usishtuke kusikia taarifa zitakazokufikia ambazo zitajenga uadui mkubwa kati yako na nduguzo.”
    “Siwezi kushtuka kwa viumbe wasio na huruma na mimi, wewe nipe hiyo dawa kila mtu ataubeba mzigo wake mwenyewe.”
    “Haya nisubiri.”
    Mganga alinyanyuka na kutoka nje, akiniacha na uamuzi mmoja ambao nilikuwa tayari kwa lolote. Baada ya muda aliniita nje, nilitoka na kuelezwa nisubiri kwenye kigoda. Baada ya muda nilimuona mpenzi wangu akiwa amebeba ndoo kutoka kwenye kisima kilichokuwa pembeni ya nyumba ya mganga.
    Alipofika, mganga alimueleza ayapeleke nyuma ya nyumba na kuyaweka kwenye beseni. Alifanya vile, aliporudi mganga alizunguka nyuma na baada ya muda aliniita. Nilimfuata na kukuta kuna beseni lililokuwa na maji yaliyochanganywa na dawa ya unga na majani mabichi kama ya mnyonyo.
    “Oga haya maji, kisha haya majani utajisugua sehemu zako zisizofanya kazi, sawa?”
    “Sawa.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Haya, ukimaliza kuoga vitu vyote viache hukuhuku.”
    “Hakuna tatizo mzee.”
    Mganga aliondoka na kuniacha nikivua nguo na kuanza kujimwagia maji kwa mikono huku nikijisugua kwa majani yale mabichi sehemu zangu za siri zilizokwisha nguvu. Baada ya kumaliza kuoga nilirudi kwa mganga, alinielekeza nikae kwenye kigoda kisha alizunguka nyuma ya nyumba, sikujua anakwenda kufanya nini, mara alirudi akiwa ameshikilia majani niliyojisugulia na kuingia kwenye kilinge chake. Baada ya muda aliniita.
    Niliingia kibandani na kuketi kwenye ngozi ya ng’ombe, baada ya kuketi mganga alinipa maji yaliyokuwa kwenye kikombe cha plastiki. Nilikunywa maji yale kisha nilimrudishia kikombe, baada ya kukipokea alisema:
    “Sasa nafikiri kazi tumemaliza, weka hapo kwenye kikapu kiasi chochote kama sadaka kwa mizimu.”
    Nilichomoa pochi na kuweka elfu hamsini, baada ya kuweka mganga alisema:
    “Mpaka sasa kwenu kuna hali ya sintofahamu, inaonesha hapa baba yako ameanguka dukani na anarudishwa nyumba. Ukitaka kumuua haraka baba yako ukikutana na mpenzi wako haimkopeshi, salamu utasikia.”
    “Sasa mganga kama ni hivyo kuna faida gani ya kuja kwako?”
    “Nilikuwa nakujulisha tu, litakalotokea usishangae, kesho asubuhi njoo haraka maana kuna vita nzito itakayotokea. Itakuwa mara mbili ya leo, ningeweza kukutengenezea zindiko lakini siwezi kufanya kazi mbili kubwa kwa wakati mmoja.”
    “Hakuna tatizo.”
    “Basi wewe nenda nyumbani, kama unaweza usionane nao watakutafuta sana ili kuhakikisha baba yenu anarudi katika hali ya kawaida. Na kurudi kwa afya ya baba yako, huchukui muda unakuwa msukule wa familia wa kuwaingizia pesa.” 
    “Siwezi kukubali, kama nimepona nitaendelea na mpenzi wangu kwa vile bila yeye nisingeweza kupona.”
    “Pia kuna kitu cha ajabu kitamtokea baba yake, sumu ya uchawi itamgeuza kiumbe cha kutisha.”
    “Vyovyote atakavyokuwa mimi hainihusu, yule sasa ni adui yangu na si mzazi wangu,” pamoja na maneno yale kuwa ya kutisha sikuingiwa huruma kwa vile wao walitafuta uhai wangu. 
    “Hiyo ni juu yako kwa vile yote nimekueleza bila kuacha kitu.”
                                                           *****
    Baada ya maelezo ya mganga, nilitoka na kumpitia mpenzi wangu na kuondoka, tulipofika Pasiansi tulitafuta sehemu kupata chakula kutokana na njaa iliyokuwa ikituchonyota. 
    Wakati wa kula nilijikuta mtu mwenye mawazo mengi, kitu kilichomshtua mpenzi wangu na kutaka kujua kulikoni. 
    “Masalu kuna nini mbona unaoneka una mawazo mengi?”
    “Ni kweli, nina mtihani mzito.”
    “Upi huo?”
    “Kuhusiana na hali yangu, kama nilivyokueleza, kuna mambo mazito yamejitokeza.”
    Sikuwa na jinsi nilimueleza kila kitu, sikutaka kumficha kwa vile msaada wake ndiyo uliofichua yote. Baada ya kunisikiliza alishtuka sana.
    “He!”
    “Ndiyo hivyo nikubali ili nigeuzwe ndondocha au niokoe maisha ya baba  na familia kukutwa na matatizo mazito.”
    “Mmh! Huo mtihani, lakini maisha yako ni muhimu kuliko kitu chochote.”
    “Nami ndiyo nimefanya hivyo, ila mganga ameniomba leo nisionane nao ili kesho turudi mapema kwake.”
    “Hakuna haja ya kuhangaika, tutafute gesti yoyote nzuri hapahapa Pasiansi ili kesho turudi kwa mganga mapema.”
    “Kweli wazo zuri, basi tufanye hivyo.”
    Nilikubaliana na mpenzi, wangu baada ya chakula tulitafuta nyumba ya wageni yenye hadhi na kupanga pale.
    Siku ile tulishinda na kulala pale, majira ya saa tano za usiku dada alinipigia simu, nilitaka kuacha kuipokea lakini niliamua kuipokea.
    “Haloo.”
    “Haloo Masalu.”
    “Shikamoo”
    “Marahaba.”
    “Unasemaje?”
    “Masalu upo wapi?”
    “Una shinda gani?”
    “Masalu umefanya nini?”
    “Kuhusu nini?”
    “Unataka kumuua baba?”
    “Kumuua kivipi?”
    “Masalu baba akifa utamla nyama.”
    “Kama mlivyo mla nyama dada Monika?”
    “Nini?”
    “Umenisikia vizuri.”
    “Wee fanya mzaha, lakini ole wako baba afe.” 
    “Na wewe ole wako siku ukisogeza pua yako kwangu utanitambua mimi ni nani mwanga mkubwa we, kwanza nilikuwa nakuchekea sasa hivi sikupendi nakuchukia ni adui yangu namba moja na taarifa zako nazipeleka polisi.”
    “Polisi! Utawaambia nini?”
    “Kwamba wewe na wenzako ni wauaji.”
    “Tumemuua nani?”
    “Dada Monika na mtoto wako na ushahidi wa sehemu ulipoziweka hizo maiti ninao na lazima mtanyongwa mwaka huu.”
    “Masalu usifike huko hali ya baba ni mbaya sana, hebu rudi nyumbani tujue tufanye nini,” ilibidi arudishe sauti chini.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Nirudi mnimalize.”
    “Tukumalize?” Alijifanya kushtuka.
    “Eeh, baada ya kuniua nguvu za kiume sasa mnataka kunigeuza msukule.”
    “Ha! Masalu nani kakudanyanya hivyo?”
    “Dada hakuna siri duniani, yaani pamoja na kunipa kidonda hamkuridhika pamoja na utajiri na maisha mazuri kupitia mwili wangu. Mkaamua kuniua nguvu za kiume ili nisiwe na thamani yoyote dunia. Haitoshi mmeniandalia pigo zito la kunimaliza kabisa la kunigeuza msukule ili tu muwe na maisha mazuri.
    “Ninyi ni viumbe gani mnaojali fedha kuliko utu wa mtu, mmemtoa kafara dada Monika kwa tamaa zenu, hamkuridhika umemtoa mtoto wako ili uwe na pesa nyingi vile vile hamkuridhika mmenigeukia mimi. Kwa vile hakuna mtu mwingine wa kumpa kidonda hiki mmeamua mnigeuze ndondocha wa familia.”
    “Masalu umejuaje?”
    “Si kujuaje, kwa nini umeamua kunifanya hivyo?”
    “Si kweli,” dada alijifanya kushtuka.
    “Sawa si kweli, basi baba anakufa.”
    “Umeamua kuuana?”
    “Masalu bila wewe baba atakufa, unakubali baba yetu afe kweli?”
    “Mimi na ninyi nani kaamua kumuua mwenzake?”
    “Masalu kumbuka baba yetu ni huyuhuyu, akifa hatutampata mwingine.”
    “Kwani kuna mbadala wa dada Monika, baba ni huyo huyo, dada Monika mwingine yupo wapi?”
    “Masalu makosa yamekwisha fanyika rudisha moyo uokoe maisha ya baba.”
    “Kwanza mnaniambia hivyo mimi nimemfanya nini baba?” niliwauliza swali gumu.
    “Inaonekana umekwenda kwa mganga kurudisha nguvu zako za kiume.”
    “Mlitaka niwe hivihivi milele kwa raha zenu, mbona ninyi mna watoto na wanaume?”
    “Kwani Masalu upo wapi?”
    “Tokea lini mlinitafuta?”
    “Basi zungumza na mama,” baada ya muda nilimsikia mama akiniita.
    “Masalu.”
    “Naam mama, shikamoo.”
    “Marahaba mwanangu upo wapi? hali ya baba yako ni mbaya sana.”
    “Anaumwa nini?”
    “Ameanguka kwenye mishughuliko yake, kama ni kweli umefanya wewe njoo umsaidie baba yako, hali inatisha hajitambui anakoroma tu.”
    “Mama sihusiani na lolote kuhusiana na matatizo ya baba, naomba mumpeleke hospitali.”
    “Ugonjwa huu si wa hospitali.”
    “Kwa hiyo mimi ndiye niliyemroga?”
    “Hapana Masalu, ila inawezekana ulichokifanya ndicho kilichomuathiri baba yako.”
    “Kipi hicho?”
    “Unakijua Masalu, hebu rudi haraka nyumbani.”
    “Mama ni nani kwako?”
    “Mtoto.”
    “Nina haki gani kama mmoja wa watoto wako?”
    “Haki zote kama walizonazo wenzako.”
    “Sasa kama kila mtu ana haki hiyo kwa nini unataka kushiriki katika kunigeuza ndondocha wa familia?”
    “Masalu! Wakugeuze kivipi?” mama alishtuka.
    “Mama, unajua vizuri sana si suala la siri, mpango wenu wa kunimaliza nimeugundua lakini nawahakikishia kila atakayenigusa nitampoteza.”
    “Upo tayari baba yako afe?”
    “Mimi situnzi uhai wake bali Mungu aliyetuumba wote, kama wakati wake umefika basi atakufa, kama alivyokufa mtoto wa dada na dada Monika.”
    “Kwa nini umekosa huruma?”
    “Kwa vile ninyi mnanionea huruma eeeh.”
    “Kama ulivyosikia hali ya baba yako ni mbaya kifo chake kitakuhusu.”
    “Sishangai hata wewe mama niliyekuwa nakutegemea ni mmoja wapo. Asante sana nashukuru, Mungu yupo atanilinda.”
    “Masalu...Masa..,” nilikata simu na kuizima kabisa.
                                                       ******
    Baada ya mazungumzo nilijikuta nikilia peke yangu jinsi familia yangu ilivyokuwa ikijijali yenyewe na kuwa tayari kupoteza uhai wa mtu ili tu ipate mali. 
    “Masalu nyamaza mpenzi wangu,” mpenzi wangu alinibembeleza, kipindi kile yeye ndiye aliyekuwa mfariji wangu.
    “Inaniuma.”
    “Kweli inauma, lakini kwa nini umekubali kuzungumza nao? Ungezima simu yote haya yasingetokea.”
    “Ilikuwa lazima nizungumze nao ili wajue kuwa naelewa kila kitu, pia hata kujua kama kweli hali ya baba ikoje.”
    “Kwa hiyo utakwenda kumuona baba yako?”
    “Nikitoka kwa mganga nitakwenda.”
    “Pole sana inasikitisha, familia yako ina dhambi kubwa.”
    “Wee waache sijui kwa Mungu watasema nini?”
    “Ulisema wewe ndiye chanzo cha utajiri kilichoachwa na marehemu dada yako Monika, ukipona itakuwaje?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Sijui, watajua wenyewe, mimi nitaangalia afya yangu.”
    “Mmh! Pole sana mpenzi wangu, kupona lazima uwe na roho ngumu ili umeze mfupa.”
    “Nimekwisha umeza lolote na liwe, siwapendi mashetani wale.”
    Kwa vile muda ulikuwa umekwenda tulipanda kitandani kulala, usiku nilijikuta nikipatwa na hamu ya mapenzi. Lakini nilikumbuka kauli ya mganga kuwa nikikutana kimwili na mwenzangu ndiyo kifo cha baba, hawezi kuomba hata maji.
    Pamoja na hasira kutokana na roho mbaya ya familia yangu juu ya mambo waliyotaka kunifanyia nilijikuta nikiingiwa na imani ya kutofanya tendo lile kuokoa maisha ya baba. Tulilala mpaka asubuhi bila kufanya tendo la ndoa, asubuhi tuliamkia kwa mganga.
    Hatukuchelewa kufika kwa vile hapakuwa  mbali kutoka tulipokuwa tumepanga, ulikuwa mwendo wa dakika ishrini. Ilionesha sisi ndiyo tulikuwa wateja wa kwanza toka nje kufika pale kwa siku ile, tuliowakuta pale ni wale waliokuwa wakitibiwa na kulala palepale.
    Mganga alitukaribisha, kama kawaida niliingia ndani peke yangu na mpenzi wangu alibakia nje. Nilipofika hakunisemesha lolote, aliendelea na kutoa chupa za dawa kwenye kikapu na kuziweka juu ya ngozi kisha alichukua karatasi ya kaki na kuanza kumiminia unga wa dawa kidogo kidogo kutoka katika kila chupa.
    Zilikuwa chupa zaidi ya tano, baada ya kuukusanya unga wa dawa katika karatasi moja, alichukua chupa iliyokuwa na mafuta kama sikosei ya ng’ombe, yalikuwa meupe na mazito. Aliyamiminia yale mafuta na kuyachanganya na mchanganyiko wa dawa kisha alitoka nje.
    Baada ya muda alirudi na kunionesha kwa ishara nimfuate, nilimfuata mpaka kwenye kichuguu kimoja ambacho alinielekeza. Kabla ya kupanda juu ya kichuguu alinielekeza kwa ishara nivue shati. Nami nilifanya kama alivyonielekeza.
    Baada ya kupanda juu ya kichuguu kifua wazi, alipanda na yeye na kuanza kunichanja kila kona ya mwili huku akinipaka ile dawa aliyochanganya na mafuta mazito. Alipomaliza tuliteremka na kurudi hadi ndani ya kilinge, ndipo aliponisemesha.
    ”Habari za toka jana?”
    “Nzuri mzee wangu, shikamoo.”
    “Marahaba, kuna habari gani mpya?”
    “Jana walinipigia simu usiku na kuniomba ninusuru maisha ya baba.”
    “Uliwajibu nini?”
    “Niliwaambia siwezi kujiteketeza mwenyewe.”
    “Wao walisemaje?”
    “Walinitishia kama baba akifa nitamla nyama.”
    “Akawajibu nini?”
    “Niliwaeleza kama walivyokula nyama ya dada Monika.”
    “Wakasemaje?”
    “Walishtuka na kunieleza kuwa habari nimezijulia wapi?”
    “Mh, ukawajibu nini?”
    “Niliwambia nitawapeleka polisi na kuwafungulia mashtaka ya uuaji na kukaa na maiti za watu ndani?”
    “Enhee! Wakasemaje?”
    “Walishtuka na kuniomba ninusuru maisha ya baba.”
    “Ukawajibu nini?”
    “Niliwaeleza sipo tayari.”
    ”Wakasemaje?”
    “Waliendelea kunibembeleza niende kwa vile uliniahidi nikitoka hapa nitakuwa kamili, nimewaeleza nitakwenda leo.”
    “Wakasemaje?”
    “Tumekubaliana, nikitoka hapa niende.”
    “Sikiliza, una bahati kama usingekuja hapa na kujipendekeza jana ukaenda ungekwisha palepale.”
    “He!” Nilishtuka kusikia vile.
    “Unashtuka, kama nilivyokueleza familia yako haina mapenzi na wewe kwa ajili ya mali.”
    “Mmh! Sasa nikienda leo itakuwaje?”
    “Leo usiende, nenda keshokutwa ila kuna kitu kitatokea si cha kawaida, kuwa tayari kukabiliana nacho.”
    “Kitu gani hicho?”
    “Wee nenda, ila majibu utayapata kujua kinga niliyokukinga inafanya kazi kiasi gani.”
    “Niambie ili nijue ikiwezekana nisiende.”
    “Lazima uende ili kuwaumbua wabaya wako.”
    “Mmh! Sawa.”
    “Baada ya kesho kwenda rudi tumalizie tiba, kwa vile hawatakubali kuona umewashinda.”
    “Sawa nimekuelewa.”
    “Nilitaka kusahau kitu kimoja, leo usioge wala kukutana na mwanamke kimwili ikiwezekana leo kila mmoja alale chumba chake au kitanda chake.”
    “Sawa nimekuelewa.”
    “Ndoto utakayoiota ndilo jibu la safari yako.”
    “Nashukuru kwa msaada wako.”
                                                  ******
    Baada ya mazungumzo, tulirudi hoteli tuliyokuwa tumepanga kwa ajili ya mapumziko, siku ile sikukaa kutokana na kuwa na alama nyeusi za kuchanjwa na mganga.
    Kwa vile hatukuruhusiwa kulala pamoja, tulichukua chumba cha vitanda viwili na kila mtu alilala kitanda chake. Usiku niliota ndoto nafukuzwa na kichaa mmoja ambaye katika kunifukuza aligongwa na gari, hapohapo nilishtuka usingizini na kujiuliza kichaa yule ni nani na ndoto ile inaashiria kitu gani.
    Siku ya pili nilimueleza mpenzi wangu ambaye alinishauri heri nisiende nyumbani ili kuepusha nilichokiota.
    “Masalu kama mganga alikuambia utakachokiota ndicho kitakachotokea, kwa nini uende?”
    “Hilo wazo hata mimi nilikuwa nalo lakini mganga alisema lazima niende, ili nirudi na kupata dawa ya mwisho.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Kwa nini asikupe hiyo dawa?”
    “Alisema lazima niende ili kuonesha uwezo wa kile alichokifanya jana.”
    “Mmh! Mtihani mzito kweli.”
    “Lakini kwetu hatuna kichaa.”
    “Basi inawezekana utakutana naye njiani.”
    “Kama ni hivyo bora nikodi gari mpaka mlangoni.”
    “Bora ufanye hivyo.”
    “Sawa, basi tuongozane, wewe uende kwenu najua wamekutafuta sana.”
    “Hata wakinitafuta mimi mtu mzima, kuna mdogo wangu anajua kila kitu sidhani kama watasumbuka sana. Mbona tuliishasafiri zaidi ya wiki hakuna kilichoharibika?”
    “Si uliaga?”
    “Basi taarifa zangu watazipata kwa mdogo wangu na leo nikifika watapata jibu.”
    “Mmh! Haya.”
    Niliongozana na mpenzi wangu hadi kwao, nilimteresha na mimi kuendelea na safari yangu. Nilikwenda na gari hadi mlangoni na kuteremka, wote waliokuwepo walishtuka. Baba aliyekuwa amelazwa sebuleni aliponiona alipiga kelele.
    “Mtoeni...mtoeni  ataniua...ataniua.”
    “Baba siwezi kukuua, utajiua mwenyewe,” nilimjibu baba.
    “Jamani mtoeni ataniua,” baba alizidi kupiga kelele.
    “Masalu hebu toka nje,” dada alinifokea.
    Niligeuka kutoka nje, kaka yangu alikuja kwa nyuma na kunishika kisogoni, mara alianza kupiga kelele kama mtu aliyepagawa, akachukua jembe na kutaka kunipiga nalo, alinikosakosa mara mbili, nilipoona hatanii nilitimua mbio, alinikimbiza mpaka barabarani huku akidhamiria kuniumiza.
    Ilinibidi nivuke barabara bila kuangalia baada ya kuona nakufa najiona, baada ya kuvuka nilisikia kishindo nyuma yangu na kelele za watu. Nilipogeuka nilimuona kaka yangu akiwa chini akivuja damu kichwani.
    Japo ajali ile ilifanya moyo uume na kupatwa na huruma, lakini sikutaka kurudi kuangalia, wakati huo watu walikuwa wakijaa kwenye tukio la ajali na kumzunguka kaka. Nilikodi teksi iliyokuwa ikipita kuwahi nyumbani. Nilipofika nyumbani nilimpigia simu mpenzi wangu.
    “Vipi Masalu mbona kama kuna tatizo?”
    “Ndiyo.”
    “Tatizo gani?”
    “Si la kulizungumzia kwenye simu.”
    “Upo wapi?”
    “Nyumbani.”
    “Nakuja sasa hivi.”
    Baada ya kukata simu nilibaki nimejilaza kwenye kochi nilijiuliza vita nzito niliyoelezwa na mganga ndani ya familia yangu nini hatima yake. Nilijiuliza kaka yangu bila kugongwa na gari alitaka kunifanya nini. Au alikusudia kuniua?
    Njozi ile baada ya kuuona ukweli nilijuliza nini kitafuata.
    Niliamini kama vita ya nguvu za giza itashindikana basi watatumia nguvu za kawaida ili kunitokomeza duniani. Nilijiuliza kama itakuwa hivyo nitawezaje kuwaepuka? Nilipanga kuukimbia Mji wa Mwanza ili kuokoa maisha yangu kwa kuliuza duka langu.
    Wazo lile nilitaka nishauriane na mwenzangu kabla ya kutoa uamuzi, nilipanga akija nitamgusia suala lile ambalo kwa upande wangu lilichukua sura mpya ya kutishia maisha yangu. Wakati nikiwa kwenye dimbwi la mawazo mpenzi wangu aliingia kwa hali aliyonikuta nayo ya kujilaza mikono kichwani ilimshtua sana. 
    “Vipi?”
    “Masalu?”
    “Mambo mazito.”
    “Kivipi?”
    Nilimueleza niliyokutana nayo nyumbani, alibakia mdomo wazi asiamini nilichomueleza.
    “Sasa bila kugongwa na gari ingekuwaje?”
    “Hata sijui.”
    “Sasa kwa nini mganga hakukuambia?”
    “Aniambie nini wakati aliniambia nitakayoyaota ndotoni ndiyo nitakutana nayo?”
    “Sawa, lakini alitakiwa akupe tahadhari.”
    “Mganga hawezi kukuambia kitu kijacho kabla ya kutokea ili usije sema uongo.”
    “Pole sana mpenzi wangu sasa tutafanya nini?”
    Mara simu yangu iliita nilipoangalia nilikuta ni dada, niliitazama bila kupokea kitu kilichomfanya mpenzi wangu kuuliza.
    “Mbona hupokei ni nani?”
    “Dada”
    “Anataka nini si alikufukuza?”
    “Hata mimi nashangaa.”
    “Usipokee.”
    Kweli sikuipokea, iliita mpaka ikakatika, baada ya kukatika haukupita muda iliita tena. Vilevile sikuipokea, ikaita mpaka ikakatika. Nilitaka kuizima lakini mpenzi wangu alikataa kwa kuniambia:
    “Simu za ndugu zako usipokee, lakini zingine ziache ziingie.”
    “Kutokana na vita hii nzito nilikuwa nimepanga kuuza duka langu niondoke Mwanza, ulikuwa na wazo gani?”
    “Mmh! Ni haraka sana kwa nini tusirudi kwa mganga tumsikilize atasema nini?”
    “Mganga kazi yake ni kunizindika ili nisidhurike na nguvu za wachawi, lakini si kuwazuia kunidhuru kwa silaha za kawaida.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Sawa, lakini kabla ya kufanya hayo tukamsikilize mganga, si alikuambia urudi.”
    “Mmh! Kweli, kuna umuhimu wa kwenda muda huu.”
    “Hakuna tatizo ni muda mzuri.”
    Nilikubaliana na mwenzangu kurudi kwa mganga, tuliongozana hadi kwa mganga, tulimkuta akihudumia wagonjwa. Ilitupasa kusuburi kwa zaidi ya saa nne. Ilipofika zamu yangu niliingia kwa mganga, aliponiona alitabasamu na kusema:
    “Umeona?”
    “Ndiyo.”
    “Sasa ule ndiyo ubaya uliokuwa umekuzunguka, bila kupitia hapa alipokushika ungeanguka chini na kupooza, kuanzia muda ule ungewekwa kwenye chumba chenye mwanga hafifu na hayo ndiyo yangekuwa maisha yako mpaka unakufa.”
    “Mmh! Na kaka yangu aliyegongwa na gari hakufa?”
    “Hakufa.”
    “Atapona?”
    “Atapona, lakini itachukua muda mrefu sana kupona, alipogongwa hakuumia. Lile halikuwa gari la ukweli kama ulivyodhania ni kinga yako mwilini hakuna wa kukuchezea. Atakayetaka kukuchezea atapatwa na mazito kuliko yaliyompata kaka yako.
    “Kila tatizo litakalokutokea utaliota usingizini kabla ya kukutokea.”
    “Kwa hilo nashukuru, lakini wakitumia silaha?”
    “Zindiko nililokuwekea hawawezi kukudhuru kwa kitu chochote.”
    “Nilikuwa na wazo la kuuza duka ili nitoroke.”
    “Wala usiende popote, hakuna wa kukugusa, watakuogopa kama ukoma, ila inabidi duka lako lifanyiwe zindiko bila hivyo mali zako zote zitamomonyoka na kukufanya ubaki kuwa maskini wa kutupwa.”
    “Na ndugu zangu?”
    “Nao wana wakati mgumu, si muda mrefu watakuwa na maisha magumu, labda wahangaike tena la sivyo kwa kutegemea ndagu ya kidonda wataadhirika.” 
    “Kwa hiyo unataka kuniambia kaka hakupata ajali?”
    “Hakupata ajali ila amepata kichaa baada ya kutaka kukudhuru na kumrudia mwenyewe.”
    “Lile gari na watu waliokuja walitokea wapi?”
    Kile ni kiini macho tu lakini ile ndiyo kinga inayokulinda, baada ya kumzuia ulipata nafasi ya kukimbia na kurudi kwako.”
    “Na hali ya baba?”
    “Mmh! Hali ya baba yako ndiyo hivyo imeshikiliwa na uhai wako, kubali uteseke baba yako apone.”
    “Sipo tayari wacha afe, siwezi kuwaonea huruma tena ni watu wabaya wasionitakia mema.”
    “Basi leo nitamalizia kazi yangu, ukitoka hapa fanya mambo yako bila hofu, atakayekugusa atapotea.”
    Mganga baada ya kusema vile alichukua dawa nyeusi iliyokuwa kwenye chupa na kuichanganya na asali kisha alisema niachame mdomo, akanichanja kwenye ulimi na kunipaka dawa kwa kutumia simbi. Chale zingine alinichanja katikati ya utosi, kifuani na mgongoni na sehemu zote za maungio ya mwili kisha alinipa ruhusa ya kurudi nyumbani na kunipa masharti yaleyale ya kutolala na mwanamke kwa siku ile. 
    “Kijana kazi imekwisha, unaweza kuendelea na shughuli zako kama kawaida.”
    “Asante, na kuhusu hali ya baba?”
    “Yangu nimemaliza, utaamua mwenyewe.”
    “Hawezi kupona tena?”
    “Akipona ujue unakufa wewe.”
    “Hata akipelekwa kwa mtaalamu mwingine?”
    “Kwangu nimemaliza na kazi yangu naiamini haijawahi kutokea kama itatokea basi ujue ndiyo kifo chako.”
    “Na asipopona?”
    “Utakufa.”
    “Sasa itakuwaje, ndugu si watajua mimi ndiye niliyemuua?”
    “Kijana niondolee upumbavu, niambie unataka nifanye nini, ufe baba yako apone au afe baba yako wewe upone?” Mganga alikasirishwa na maswali yangu. 
    “Basi mzee nisamehe,” niliomba msamaha baada ya kuona nimemuudhi mganga.
    “Sjawahi kuona mtu mpumbavu kama wewe, unanipotezea wakati wangu nakuomba uondoke,” mganga alikuja juu na kunifukuza.
    “Samahani mzee wangu,” nilijikuta nikichanganyikiwa baada ya kumuudhi mamba kabla sijavuka mto.
    “Samahani nini, nilikuita hapa nikutibu?”
    “Hapana.”
    “Nilikuomba nikusaidie?”
    “Hapana.”
    “Sasa kwa nini unanitia ujinga kwa kazi nzito niliyoifanya ya kuokoa maisha yako?”
    “Nisamehe mzee wangu nipo chini ya miguu yako sitakuuliza tena swali lolote kuhusiana na familia yangu.”
    “Kazi nimemaliza nipe changu kilichobaki kisha uende zako utaamua chochote kwenda kwa mganga yeyote akusaidie. Ila ukiondoa mguu wako hapa usije tena.”
    “Mzee wangu najua nimekukosea naomba usifike huko,” nilizidi kumuomba msamaha mganga baada ya kubaini kosa langu.
    “Lazima nifike nimekufafanulia mangapi yaliyotaka kukupata na leo umepata jibu bado unajitoa akili nikufanye nini? Wewe mtoto?”
    “Hapana, nimekosa mzee wangu nipe adhabu yoyoye lakini usinikataze kuja hapa,” nilipiga magoti mbele ya mganga kuomba msamaha.
    “Nimekuelewa kijana lakini usirudie tena kuingilia kazi za watu.”
    “Nashukuru mzee wangu.”
                                                       ******
    Baada ya kusamehewa na mganga, tuliagana na kunieleza ninapotokewa na tatizo niende kwake bila tatizo.  Baada ya kutoka pale sikutaka kurudi nyumbani ambako niliamini lazima ndugu zangu watanitafuta. 
    Kama  kawaida tulirudi kwenye hoteli yetu tuliyolala jana yake, tulilala pale mpaka siku ya pili. Usiku wa siku ile mpenzi wangu alitaka kujua nini hatima ya maisha yangu baada ya kutoka kwa mganga.
    “Mh, Masalu mganga amesemaje juu ya uamuzi wako wa kukimbia mji?”
    “Amesema hakuna kitakachonitokea nikae hapahapa.”
    “Na kuhusu ile ajali?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Anasema haikuwa ajali bali kinga aliyoniwekea ndiyo iliyonilinda nisidhuliwe na kaka.”
    “Masalu! Unataka kuniambia kaka yako hakugongwa na gari?”
    “Mganga ndivyo alivyonieleza.”
    “Mmh! Makubwa, lakini mganga huyu kiboko, sifa zake ni kubwa.”
    “Lakini alitaka kunitimua.”
    “He! Kivipi?”
    “Nilitaka kumuulizia hatima ya hali ya baba yangu.”
    “Akakujibu nini?”
    “Wewe, kumbe niliwasha moto wacha anifukuze kama mbwa aliyeiba mayai.”
    “Ehe! Ikawaje?”
    “Mmh! Ilibidi nimuombe msamaha huku ninalia.”
    “Mkaishiaje?”
    “Alinisamehe na kunionya nisirudie tena kuuliza maswali ya kijinga.”
    “Lakini nawe umeyataka, unamuombea dhamana mtu uliyemfunga mwenyewe?”
    “Pamoja na hayo, lakini yule ni mzazi wangu.”
    “Haya sasa, chagua mzazi apone uumie wewe.”
    “Japo inaniuma lakini kisu kimegusa mfupa, kungekuwa na njia mbadala nisingekubali kuona baba yangu anateseka kwa ajili yangu.”
    “Lakini ningekuwa ni mimi nisingekuwa na huruma na mtu anayenitoa kafara kwa tamaa zake. Tena ningemuulia mbali hata kwa sumu.”
    “Lakini kumbuka pamoja na yote ni mzazi wako.”
    “Siwezi kumuonea huruma mzazi mwenye nia mbaya na mimi, akitaka kuniua nikigundua na mimi namfanyia kitu kibaya.”
    “Lakini si kila baya lazima ulipe baya kuna lingine  unatakiwa kulisamehe.”
    “Kwa upande wako utasamehe vipi, ili kupona lazima mtu aumie, kibaya zaidi pamoja na yote waliyokufanyia bado wanataka kukupoteza kwenye sura ya dunia bado watu kama hao unawaonea huruma?”
    “Kwa kweli nimechanganyikiwa.”
    “Sikiliza Masalu, unapofanya kitu kibaya kisha ukaona huruma basi lazima litakurudia na halitapata tiba mpaka unakufa.”
    “Wewe nani kakwambia?”
    “Masalu mpaka nakupeleka kwa yule mganga  nayajua mengi kwa hiyo jiepushe kukingia kifua unayoyafanya, bora ungeacha kabisa kuliko kuingilia kazi ya mganga hasa wakikusaidia katika matatizo yako.”
    “Kwa hiyo nikiendelea kusikitika itakuwaje?”
    “Usishangae ugonjwa wa baba yako ukakurudia.” 
    “Lakini sasa hivi si nimeachana nao.”
    “Basi ndiyo hivyo, siku zote usioneshe huruma pale unapoamua kutenda jambo zito, huruma yako hugeuka sumu na kukurudia mwenyewe.”
    “Nimekuelewa.”
    Kwa vile muda ulikuwa umekwenda tulikubaliana tulale ili mengine tuzungumze kesho yake kwa vile bado tulipanga kuendelea kuwa pale  kwa siku moja zaidi. Kila mtu alilala kitanda chake kama tulivyoelezwa na mganga, ilionesha wazi kabisa mpenzi wangu alikuwa akiumia kutokana na kumnyima haki yake ya msingi.
    Lakini bado sikuwa tayari kumuua baba yangu kwa kulifanya tendo lile, hata hali aliyokuwa nayo ilitokana na kuyaokoa maisha yangu yaliyofikia hatua mbaya. Pia hakukuwa na njia mbadala ya kuweza mimi kupona bila  baba yangu kuguswa.
    Japo mpenzi wangu alionekana hana huruma na familia yangu na kuwa tayari kuiona inapotea baada ya kugundua walikuwa na mpango mbaya kwangu lakini nilijitahidi kutafuta njia ya kumueleza kwa makini ili anielewe, sikupenda hata siku moja kifo cha baba yangu kitokane na mimi kwa kufanya tendo la ndoa nikijua kabisa ndilo litakalomaliza uhai wake.
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog