Search This Blog

SAFARI YANGU YA KWANZA KUZIMU - 5

 





    Simulizi : Safari Yangu Ya Kwanza Kuzimu

    Sehemu Ya Tano (5)

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hakukuwa na kupoteza muda mahali hapo, ilikuwa ni lazima kuondoka na kuendelea na safari mpaka kuhakikisha wanafika juu kabisa alipokuwa akikaa Lusifa. Japokuwa mzee Hamisi alikuwa akilia pale huku akiwa amelishika kapu lile, mzee Hamadi hakutaka kumuacha, geti lile lilipojifungua akamnyanyua na kuanza kuelekea naye ndani.

    “Inaniuma sana,” alisema mzee Hamisi huku akijifuta machozi yake.

    “Kumuona mkuu ni lazima ujiandae, kumuona Mungu kuna ugumu, mpaka utende mema mengi, na hata kumuona mkuu wetu ni hivyohivyo, haonekani kirahisi, ni lazima umwage damu nyingi” alisema mzee Hamadi.

    “Hivi kweli nimemuua mama yangu?”

    “Ndiyo! Umemuaa lakini kwa faida sana kwani hata usingemuua, bado angekufa siku nyingine,” alisema mzee Hamadi.

    Walikuwa wamesimama sehemu wakizungumza, mzee Hamisi aliumia sana moyoni mwake lakini muda huo haukuwa wa kujuta na kujiuliza juu ya kile kilichokuwa kimetokea, walitakiwa kusonga mbele kwenda upande mwingine kabisa.

    Wakati wamepandisha ngazi ndefu, wakalifikia geti jingine, hili lilikuwa kubwa na jekundu ambalo liliandikwa BARDHAZ tena kwa maandishi makubwa. Walipofika hapo, mzee Hamadi akamwambia mzee Hamisi asimame na afanye kile atakachokwenda kufanya.

    “Kuna nini?” aliuliza mzee Hamadi.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Tunaingia kwa waziri mkuu wa huku,” alijibu mzee Hamadi.

    “Kwa hiyo?”

    “Inamisha kichwa chako chini kama ishara ya kuabudu,” alisema mzee Hamadi na mzee Hamisi kufanya hivyo.

    Geti lile likajifungua, wa kwanza kutoka lilikuwa jitu kubwa lenye umbo mithili ya tembo mkubwa. Kichwa chake kilikuwa ni cha nyani, alikuwa na mapembe huku tumboni akiwa na manyoya mengi kama kondoo.

    Meno yake yalifanana na ngiri huku masikio yake yakiwa makubwa kama sahani ya kuwekea chakula. Lilipofika hapo nje, likaanza kuwaangalia wazee hao kwa macho yaliyojaa chuki. Aliwaangalia kwa makini kisha kuwaruhusu kuingia ndani.

    Hawakutakiwa kuingia kama kawaida, walichoambiwa ni kugeuka na kuingia kinyumenyume, wakafanya hivyo na kuingia ndani. Ndani ya chumba hicho kikubwa wakakutana na viumbe wengi ambao walikuwa kama yule waliyekutana naye mlangoni.

    Hawakusalimia, kila mmoja akaonekana kuwa bize akifanya yake. Waliendelea kupiga hatua mpaka kufika katika sehemu iliyokuwa na ngazi fupi ambazo hazikupanda juu sana, mbele kabisa ya ngazi zile kulikuwa na kiti kimoja kikubwa kilichokuwa na mafuvu ya binadamu pembeni.

    “Inamisheni vichwa vyenu,” ilisikika sauti, hawakujua ilikuwa ni sauti ya nani na ilitokea wapi ila walichokifanya ni kutii kile walichokuwa wameambiwa, wakainamisha vichwa vyao kama ishara ya kuabudu.

    Mara wakaanza kusikia vishindo kutoka kule kulipokuwa na kiti, hawakujua ni nani lakini baada ya vishindo hivyo kuacha, wakaambiwa wanyanyue nyuso zao. Kiumbe mmoja mkubwa, mwenye umbo kubwa alikuwa amekalia kiti kile huku akiwa na mabawa yaliyoonekana kuharibiwa mno, sehemu nyingine yalikuwa yamechanikachanika sana.

    “Mnataka nini?” aliuliza yule kiumbe wa kutisha.

    “Tumekuja kumuona mkuu,” alijibu mzee Hamadi.

    “Mna shida gani?”

    “Ndugu yangu anataka kuwa na nguvu, awamiliki wengine wenye nguvu,” alijibu mzee Hamadi.

    Hapohapo kikaanza kusikika kicheko kikubwa kutoka kwa kile kiumbe, alionekana kama amechkeshwa kwa kile alichokuwa ameambiwa. Akatoka pale kitini alipokuwa amekaa na kuanza kipga hatua kuwafuata wazee wale pale walipokuwa.

    “Mbona mmekuja kunichekesha?” aliuliza kiumbe kile.

    “Hapana mkuu! Anahitaji nguvu.”

    “Huyu wa kulialia?”

    “Ndiyo mkuu!”

    “Nguvu hapewi mtu mwenye moyo wa kike, nguvu anapewa mtu mwenye moyo wa kishujaa na si kama yeye,” alisema kiumbe yule huku akimwangalia mzee Hamisi aliyekuwa akiogopa mno kwani sura ya kiumbe kile, kuiangalia ilitaka moyo mno.

    “Mkuu! Naomba umsaidie,” alisema mzee Hamadi.

    “Ni muoga, hawezi kufanya maamuzi!”

    “Natumaini hatokuwa muoga tena, natumaini hilo.”

    “Una uhakika?”

    “Ndiyo mkuu!” alisema mzee Hamadi.

    Alichokifanya kiumbe yule ni kurudi kule kulipokuwa na kiti chake na kisha kuchukua kisu kisha kuwarudia pale walipokuwa na kumkabidhi mzee Hamisi kisu kile.

    “Ninataka niuone ujasiri ambao mwenzako ameusema juu yako,” alisema jitu lile.

    “Ujasiri gani?”

    “Ninataka umuue mtoto wako mahali hapa. Wakati unamuua, sitaki ulie wala kuhuzunika, ukifanikiwa katika hilo, nitakupa ruhusa ya kumuona mkuu, tena mageti mengine hautopita kama wengine,” alisema kiumbe lile na kisha hapohapo katika hali isiyotegemewa, picha ya binti yake mmoja ikatokea, hakukuwa na kioo, ilitokea kwa mbele na kutakiwa kumchoma kisu mpaka afe.

    Alipomwangalia binti yake, moyo wake uliumia mno lakini hakuwa na cha kufanya, alimuua mama yake, hapo, tayari aliandaliwa kwa ajili ya kumuua mtoto wake, ilimuuma mno lakini hakuwa na cha kufanya.

    “Yaani ninafanya yote haya kwa ajili ya Ramadhani?” aliujiuliza moyoni pasipo kupata jibu lolote lile.

    “Haina jinsi. Nitalipiza kisasi kwa Ramadhani,” alisema na kisha kuchoma pale kulipokuwa na taswira ya binti yake, hapohapo akamuona akianguka chini, akianza kurusha miguu yake huku na kule, damu zikaanza kumtoka puani na mdomoni, watu wote waliokuwa pembeni ya binti yake wakashtuka, hata kabla hawajafanya chochote, palepale akakauka.

    Kumbuka.....hakutakiwa kulia wala kuhuzunika, akapokonywa kisu kile.

    ****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Moyo wake ulimuuma lakini hakuwa na cha kufanya, hakuruhusiwa kuhuzunika hivyo maumivu yale aliyoyapata, yalikuwa moyoni mwake tu. Alipopokonywa kisu kile, wakaambiwa waende katika mlango mmoja wa chumba, huo ulikuwa na jina kubwa lililosomeka Lusifa mlangoni.

    Walipofika, mlango ukajifungua na kisha kuingia ndani. Sehemu hiyo ilionekana kuwa tofauti na vyumba vingine, pale kulikuwa na uwanja mkubwa zaidi ya wa mpira wa miguu, mbele kabisa kulikuwa na jumba moja kubwa na la kifahari.

    Sehemu hiyo ilikuwa na msisimko wa ajabu, hawakuona kitu chochote kile cha kutisha lakini kila walipokuwa wakilisogelea jumba lile, walikuwa wakisisimka mno. Mbele kabisa wakakutana na watu wengi warefu, urefu wao unaweza kufikia ule wa twiga, walikuwa na mapembe kama ya ng’ombe, chini walikuwa na kwato za kondoo.

    Walikuwa wakitisha sana, walipowaangalia vizuri wakagundua kwamba hao walikuwa majini, yale yaliyokuwa yakija duniani huku wakiwa na maumbo hayo na kuwatisha watu.

    Hawakuonekana kujali, wakazidi kupiga hatua kuelekea mbele zaidi, huko, wakakutana na sehemu iliyokuwa na bwawa kubwa kama haya yaliyokuwepo duniani (swimming pool), bwawa lile halikuwa la maji bali lilikuwa ni la damu tu.

    Pembeni ya bwana hilo kulikuwa na mabomba makubwa kadhaa, mabomba hayo yalikuwa na kazi ya kumimina damu ndani ya bwawa lile. Katika mabomba yale kulikuwa na maneno yaliyokuwa yameandikwa, moja liliandikwa magari, hilo lilikuwa bomba pekee lililokuwa na kazi ya kukusanya damu kutoka kwa watu waliopata ajali za magari duniani.

    Huku duniani watu wanapopata ajali, na kama ile ajali ni ya kishetani, basi zile damu zao zinakwenda katika bwana lile kupitia bomba lile. Mbali na bomba hilo, pia kulikuwa na bomba jingine lililoandikwa ndege, hilo nalo lilikuwa na kazi hiyohiyo.

    Haikuishia hapo, kulikuwa na megine yameandikwa treni, meli na pikipiki, yote hayo yalikuwa yakipitisha damu kuelekea katika bwana hilo. Mbali na mabomba yote hayo, kulikuwa na bomba jingine ambalo liliandikwa mhanga.

    Hili lilikuwa bomba pekee ambalo lilipitisha damu za watu waliokuwa wakifariki duniani mara mtu fulani anapojitoa mhanga na kuwaua watu kadhaa katika mkusanyiko wa watu anapokwenda kujitolea mhanga.

    Hapa ningependa niseme kitu ili watu wanielewe. Mtu unapomuona anakwenda sehemu fulani kujitoa mhanga, huwa anapewa elimu ya chuki. Anaweza akaambiwa bwana Waafrika ni watu wabaya mno, nenda kawaue kwani usipowaua, watakuua wewe na kukuolea dada yako.

    Maneno yale hayaendi hivihivi, bali mtu yule huanza kupandikizwa chuki kali na watu waliokuwa na uwezo wa juu wa kupandikiza majini mioyoni mwa watu wale, na wanapoondoka pale, yale majini yanawatia nguvu na kuwaambia kweli Waafrika ni watu wabaya, kawaue, hawafai kabisa, watakuja kukuolea dada zako, yule mtu anakwenda na kujitoa mhanga na hatimaye watu wanaokufa, damu zinachukuliwa na kuingia ndani ya bwawa lile.

    “Mmmh!”

    “Usigune, huku kuna utajiri wa damu,” alisema mzee Hamadi, hapohapo damu zikaanza kumwagikia ndani ya bwawa lile kupitia katika bomba kubwa lililoandikwa magari kuonyesha kwamba tayari huko duniani kulikuwa na ajali mbaya ilitokea na watu kufariki.

    Walikwenda mbele mpaka walipoanza kuziona ngazi na kuanza kupandisha, huko, wakakutana na umati mkubwa wa watu waliokuwa wamevaa mavazi makubwa kama madela, yalikuwa na rangi nyeusi na juu yao kulikuwa na vitu kama vikofia ambavyo viliunganishwa kupitia mavazi yale.

    Watu wale walikuwa wamepiga magoti katika jengo kubwa, walionekana kama kusubiria kitu fulani, hivyo mzee Hamadi na Hamisi wakaanza kupiga hatua kuelekea kule kwani nao walihitaji kushiriki hata kabla huyo kiongozi hajafika.

    “Mnakwenda wapi?” walizuiwa na kuulizwa, yule aliyewazuia alikuwa kiumbe wa ajabu pia.

    “Tunakwenda kuabudu, tunakwenda kumuabudu mkuu!”

    “Na huyu ni nani?”

    “Ni mgeni.”

    “Mara yake ya kwanza kufika hapa?”

    “Ndiyo!”

    “Nendeni kule mkajiandae, hamtakiwi kuingia pale hivihivi,” alisema kiumbe kile cha ajabu huku akiwaonyesha sehemu iliyokuwa na damu nyingi.

    Wakaelekea hapo, hawakuwa peke yao, kulikuwa na kundi la watu kama kumi na tano hivi waliokuwa wakinywa damu zilizokuwa kwenye bakuli kubwa, walionekana kufurahia uwepo wao mahali hapo.

    Nilipokuwa nikiwaangalia watu wale, niliwaona watu maarufu nao wakiwa mahali pale, walikuwepo wanamuziki wakubwa duniani, wanasiasa, matajiri na watu wengine wengi ambao nisingependa kuwataja mahali hapa.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nao wakaungana nao na kuanza kunywa zile damu, hayo ndiyo yalikuwa matakaso hata kabla ya kwenda kuonana na shetani ambaye alipenda kuitwa kwa jina la Lusifa.

    Walipokunywa damu zile, nao wakapewa mavazi meusi kama waliyovaa watu wale na kisha kusogea kule walipokuwa wale watu wanaoabudu, walipofika, nao wakapiga magoti chini na kuinamisha vichwa vyao.

    Ni ndani ya dakika chache tu wakaanza kusikia vishindo vya mtu akija mahali hapo, alikuwa shetani mwenyewe, hawakutaka kuviinua vichwa vyao, walitakiwa kuvituliza vilevile kama walivyokuwa, shetani huyo akakifuata kiti, akakikalia na kuwaambia watu wote wainue vichwa, kile alichokiona mzee Hamisi, ilikuwa bado kidogo tu azimie.



    Aliyesimama mbele yao alionekana kuwa kiumbe wa ajabu kuliko viumbe vyote alivyowahi kuviona tangu waingie huko kuzimu. Kiumbe huyu mwenye mwili mkubwa alikuwa na sura ya paka, alikuwa na masikio makubwa, ngozi yake haikuwa ya kawaida, kuna sehemu ilikuwa na mabakamabaka kama chura lakini sehemu nyingine alikuwa na manyoya mengi kama kondoo.

    Ukiachana na hayo, miguu yake ilikuwa ni kwato za ng’ombe, nyuma alikuwa na mkia mkubwa uliokuwa na ncha kali kama mshale kwa kule mwisho. Alikuwa akitembea kwa kupiga hatua ndefu, alitisha sana kwani hata macho yake yalikuwa menkundu mithili ya moto mkali uliokuwa ukiwaka.

    “Karibuni sana,” ilisikika sauti ya kiumbe hicho, alikuwa Lusifa mwenyewe.

    Sauti yake ilikuwa na utetemeshi mkubwa, aliposema hivyo tu, mara ghafla miale kama ya radi ikaanza kuonekana mahali hapo. Ardhi ikaanza kutetemeka, kwa kifupi shetani alikuwa na utisho, kila sehemu alijaribu kujifananisha na Mungu.

    Watu wote walikuwa kimya, walikuwa wakimsikiliza tu, kitu cha kwanza alichokisema ni kuwapongeza watu wale kwa kuwa kazi yao inaendelea vizuri duniani kwa kuwa idadi kubwa ya watu hawaendi makanisani wala misikitini, walikuwa wamemsahau Mungu kwa kuwa walisimama imara kuhakikisha Mungu haabudiwi kwa chochote kile.

    Kwa watu waliokuwa matajiri, aliwapongeza kwa kuwa kupitia fedha zile alizowapa, watu wengi walishawishika na hivyo kuzitumia fedha hizo kwa kuwa tayari walizibania fedha nyingine zisiweze kupatikana kwa urahisi ili waendelee kuitawala dunia.

    Hakuishia hapo, akawashukuru na wanasiasa ambao kila siku walihakikisha jina lake linakuwa juu, akawashukuru wanamuziki kwa kazi kubwa waliyokuwa wakiifanya kwa kuweka alama zake katika video zao zote walizokuwa wakizitoa kitu kilichoonyesha kwamba walikuwa wakifanya kazi kwa juhudi kubwa.

    Akawashukuru na wachungaji waliokuwa wakitumia nguvu zake katika kuponya magonjwa, aliwasifia kwa sababu walikusanya washirika wengi kwa kile kilichokuwa kikitokea na hivyo kuwapotosha watu kumfahamu Mungu wa kweli, akaendelea kuwasisitiza kwamba wasihubiri kuhusu kuacha dhambi bali makanisa yao yahubiri kuhusu mafanikio tu na baraka tu ili waendelee kuyapenda.

    Akawashukuru mashehe wote ambao nao walihakikisha misikiti haisimami kama inavyotakiwa kwa kuanzia ugomvi wa hapa na pale. Huko kote, alikuwa ameweka watu wake waliokuwa wakiaminika kwa asilimia mia moja.

    Siku hiyo ilikuwa ni siku ya shangwe mno, damu ikaletwa na kisha kila mtu kuanza kugaiwa na kuanza kunywa. Kitendo cha kunywa damu ile tu, shetani akabadilika, akawa na muonekano kama wa malaika japokuwa hakuwa mweupe, yeye alikuwa malaika mweusi tii mwenye macho mekundu.

    Mabawa yake nayo yalikuwa yamechanikachanika kama yule kiumbe waliyekutana naye kule walipotoka. Mzee Hamisi akatamani kuuliza lakini akashindwa kufanya hivyo.

    “Nahisi kuna mtu ana swali,” alisema Lusifa huku akiwaangalia.

    “Nitakwenda kuwajibu. Hapo zamani kulikuwa na vita kati yangu, wenzangu na bwana mkubwa, katika vita ile, tulionekana kushinda kwa asilimia kubwa lakini hatujui ni wapi tulijichanganya, tukashtuka tukipigwa na kisha kushushwa huku tulipo. Ile moto waliyokuwa wakiitumia ndiyo iliyoyafanya mbawa zetu kuwa kama hivi mnavyoona,” alisema Lusifa huku jina bwana mkubwa akimaanisha MUNGU!

    “Nitakwenda kuwapa nguvu.”

    Aliposema hivyo, miale ya mwanga ya rangi ikaongezeka na kisha kujikusanya sehemu moja na kuingia ndani ya chungu kimoja kikubwa, alichokifanya baada ya kuona hivyo ni kukifuata na kisha kuingiza mkono wake ulikuwa na vidole vyenye kucha ndefu na kutoa kitu fulani ambacho kilifanana na usinga ila hicho kilikuwa kikubwa na kisha kuanza kukipiga kuelekea kwa watu watu.

    “Hiyo ndiyo nguvu yenu,” alisema Lusifa huku akiendelea na kazi ile.

    Watu walikula na kunywa, katika kipindi chote hicho hawakutakiwa kuongea, ni Lusifa peke yake ndiye aliyetakiwa kuzungumza mahali hapo, wote walifanya vitu kwa ishara tu, hata kama utakuwa unahitaji kikombe cha damu, ulitakiwa kuonyesha ishara na kisha kukabidhiwa.

    Hicho ndicho kilichoendelea kule kuzimu, watu walisherehekea kwa kuwa kila kitu kule duniani kilikwenda kama kilivyotakiwa. Baada ya sherehe hiyo fupi kumalizika ndipo watu walipopewa ruhusa ya kuzungumza na kuulizwa kile walichotaka kufanyiwa.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ninataka utajiri wangu uongezeke.”

    “Ninataka niwe na nguvu kubwa zaidi.”

    “Ninataka niwe na heshima kubwa.”

    “Ninataka niogopwe.”

    “Ninataka umaarufu wangu uongezeke.”

    Kila mmoja alizungumza lake, na kila alilolisema mahali hapo, alipewa nguvu ya kupokea. Zamu ya mzee Hamisi ilipofika, akaweka wazi kwamba alihitaji nguvu zaidi, na pia alitaka kuongezewa majini mengi, yenye nguvu kwa ajili ya kupambana na wabaya wake,.

    Watu wote waliokuwa mahali hapo wakaangua vicheko, hata Lusifa mwenyewe akaanza kucheka. Mzee Hamisi akashangaa juu ya vicheko vya watu wale kwani hata mzee Hamadi naye alikuwa akicheka.



    Hakujua sababu iliyowafanya watu wote mahali hapo kuanza kucheka na wakati alijiona ameomba kitu cha msingi mno. Akabaki akiwa ameduwaa tu asijue la kufanya. Lusifa aliendelea kumwangalia huku akiendelea kucheka, kicheko kilichowafanya hata wale wengine kucheka zaidi.

    “Mbona mnacheka?” aliuliza mzee Hamisi huku akionekana kushangaa.

    “Hakuna anayeweza kuomba kitu kama hicho! Hicho ni kitu ambacho kinakuja moja kwa moja, umefikiria nini mpaka kuomba kitu kama hicho?” aliuliza kiumbe mmoja, alikuwa akimshangaa mzee Hamisi.

    “Ninataka niwe na nguvu.”

    “Kwa hiyo unataka uwe na nguvu au unataka kuwa na majini?”

    “Nataka kuwa na vyotevyote,” alisema mzee Hamisi.

    “Hahaha! Hakuna mtu mwenye majini duniani.”

    “Unasemaje?”

    “Hakuna mtu mwenye majini duniani, majini yote makazi yao ni kuzimu, duniani hakuna majini yanayofugwa na mtu,” alisema kiumbe yule, kidogo vicheko vikaanza kupungtua.

    “Na wale wanaosema wana majini?”

    “Hakuna mwenye majini, binadamu hawezi kufuga majini, hakuna mwanadamu mwenye nguvu kama majini,” alisema kiumbe yule.

    “Nifafanulie juu ya hili.”

    “Hakuna ufafanuzi, jua kwamba hakuna mwanadamu mwenye majini.”

    “Na yale niliyokuwa nayo nyumbani.”

    “Huna majini.”

    “Wale ni wakina nani?”

    “Nguvu zako!”

    “Nguvu zangu?”

    “Ndiyo!”

    “Sijaelewa.”

    “Utakwenda kuelewa tu, njoo hapa mbele tukupe nguvu ambazo unaamini ni majini,” alisema kiumbe yule.

    Mzee Hamisi akaanza kupiga hatua kwenda pale mbele, ghafla akajikuta akianza kupata nguvu za ajabu ambazo hakuwahi kuzipata kabla. Hakujua kitu gani kilikuwa kinaendelea, mpaka alipofika pale mbele na kuambiwa kupiga magoti, akajisi kuwa mtu mpya kabisa.

    Kiumbe yule akachukua kikombe kilichojaa damu, alimwambia kwamba hiyo ilikuwa damu yenye mchanganyiko wa watu tofauti, alimaanisha Wazungu, watu weusi, Wachina na wale wenye ulemavu wa ngozi, akampa kikombe kile na kumtaka kunywa.

    Alipomaliza kunywa damu ile, akahisi akiongezeka nguvu fulani mwilini mwake, watu wote waliokuwa mahali pale wakapiga makofi ya shangwe kwani walijua kwamba kwa siku hiyo tayari aliongezeka mtu mwingine.

    Kuanzia siku hiyo, mzee Hamisi akawa moto wa kuotea mbali, hakumuogopa kabisa Ramadhani kwa kuona kwamba tayari alikuwa na nguvu nyingi hivyo angeweza kumsambaratisha kwa dakika moja tu.

    Aliporudi nyumbani, alikuta kukiwa kumetundikwa turubai na alipouliza kitu gani kilikuwa kikiendelea, aliambiwa kwamba binti yake alifariki dunia ghafla na alipoplekwa hospitalini majibu yalionyesha kwamba alikufa kwa shinikizo la damu.

    Moyoni aliumia lakini hakuwa na jinsi kwani alijua kila kitu kilichokuwa kimetokea. Alihuzunika na majirani zake na maiti haikulala siku nyingi kwani kesho yake mazishi yakafanyika na kwenda kumzika.

    Hawakukaa sana baada ya mazishi, taarifa zikaletwa na kusema kwamba mama yake alikuwa amefariki dunia. Mzee Hamisi aliumia zaidi lakini hakuwa na jinsi kwani yeye ndiye alihusika kwa kila kitu hivyo alijua kile kilichokuwa kikienda kutokea.

    Familia nzima ililia, kilikuwa kipindi kigumu kuliko vyote ambavyo viliwahi kutokea katika familia hiyo, kuwapoteza watu wawili kwa mpigo kuliwaumiza mno. Hawakuwa na jinsi kwani kwa mawazo yao walijua kwamba Mungu ndiye aliamua hayo yote yatokee.

    “Haya yote amesababisha Ramadhani,” alisema pasipo kujua kwamba pembeni alikuwa amekaa mtu.

    “Unasemaje?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hapana! Hakuna kitu.”

    Hasira zake zikawa kwa Ramadhani tu kwani bila yeye asingekwenda kule kuzimu na kusababisha mama yake na mtoto wake kufariki dunia. Moyoni alikuwa na hasira mno, hakutaka kuona kile kilichotokea kinakwenda hivihivi tu, alichokuwa akikitaka ni kumuua Ramdahani kama kisasi.

    “Huyu atakuwa Ramadhani tu,” alimwambia mke wake.

    “Kwa nini?”

    “Yeye si ndiyo mwenye ugomvi na mimi!”

    “Mume wangu! Usifikirie hivyo!”

    “Hivi kweli kupoteza watu wawili kwa siku mbili tu, hapana, kuna kitu,” alisema mzee Hamisi.

    “Usifikirie hivyo mume wangu!”

    “Hapana! Hapa kuna kitu. Haiwezekani, leo namfuata na kumuondoa duniani, siwezi kukubali,” alisema mzee Hamisi huku akionekana kuumia mno. Akapanga usiku huo ndiyo aanze kupambana na Ramdahani, hivyo akajipanga.

    *****

    Usiku wa siku hiyo ndiyo ulikuwa usiku wa kazi, mzee Hamisi alimchukia mno Ramadhani, na hakupenda hata kidogo. Aliamini kwamba mtu huyo ndiye aliyesababisha vyote vilivyotokea katika maisha yake vikiwemo vifo vya watu aliowapenda mno maishani mwake.

    Usiku wa siku hiyo alitulia chumbani kwake, hakutaka kuwasha taa yenye mwanga mkali, ilikuwa ni taa iliyokuwa na mwanga hafifu sana wa rangi nyekundu, alijifunika shuka jeusi tii huku ndani yake akiwa na karatasi iliyokuwa na maneno ambayo aliweza kuyatamka yeye tu kwa kuyasoma.

    Chumba kizima kilinukia udi tu, sauti yake ilikuwa ikisikika kwa chini sana. Ulikuwa ni usiku wa manane ambapo alitaka kufanya kazi yake ili kummaliza Ramadhani aliyeonekana kuwa nuksi kwa kile akitu alichokuwa akikifanya.

    Kelele zikaanza kusikika ndani ya chumba hicho, hakutaka kunyamaza aliendelea kuyazungumza maneno yale mpaka akajiona akianza kupaa juu chumbani mule na kuelea angani kitu ambacho hakikuwahi kutokea kabla.

    Harufu ya udi ule ikaongezeka zaidi, akaongeza kasi ya kuzungumza maneno yale, mara zile tunguli zilizokuwa ndani ya chumba kile zikaanza kuvunjikavunjika kuonyesha kwamba yale aliyokuwa akiyafanya chumbani mule yalikuwa na nguvu zaidi.

    Ghafla, akajikuta akipotea, alipokuja kuibuka, akajikuta ndani ya chumba cha Ramadhani, wakabaki wakiangaliana tu kwani naye Ramadhani alijua kwamba mtu huyo angefika nyumbani hapo usiku huo.

    Hakukuwa na mtu aliyeongea kitu chochote kile, kilichofuata ni kuanza kupimana nguvu za kichawi. Walibaki wakiangalia huku kila mmoja akianza kuzungumza maneno yake yenye nguvu tena kwa haraka mno kwani ndiyo yalikuwa maneno yenye nguvu ambayo mara nyingi huyatumia.

    Ghafla, taa iliyokuwa ikiwaka, ikapasuka, vyombo vilivyokuwa kabatini vikaanza kuanguka kutokana na tetemeka la ardhi lililotokea ndani ya chumba hicho tu. Hawakuacha kuzungumza maneno hayo ya ajabu, ghafla, Ramadhani akaanza kuzidiwa, akaanza kuzunguka huku na kule chumbani mule.

    Mzee Hamisi hakutaka kunyamaza, tayari aliona kwamba huo ulikuwa nusu ya ushindi wake na alitaka kupambana mpaka pale atakapouona ushindi wenyewe.

    Alizidi kuyatamka maneno yale, alipoona kwamba hayatoshi tu, akaanza kuchukua karatasi zenye maneno yale, akachukua na unga fulani kisha kuuweka katika karatasi ile na kuanza kumpulizia Ramadhani kitu kilichomchanganya vilivyo, hapohapo akaanguka chini na mapovu kuanza kumtoka mdomoni na puani.

    Huo ulikuwa ushindi mkubwa ambao hakutarajia kuupata kabla, mtu ambaye alimsumbua kwa kipindi klirefu, leo hii, tena usiku huu alikuwa hoi pale chini. Kwake, hiyo iliendelea kuwa furaha, kubwa, alichokifanya ni kupotea, na ghafla akaibukia katika uwanja wa wachawi wenzake, wote waliomuona, wakaanza kutetemeka akiwemo mkubwa wao.

    Nguvu alizokuja nazo mzee Hamisi zilikuwa kubwa mno, uwanjani hapo walikuwa na kiongozi wao lakini alipomuona mzee Hamisi akiingia, naye akajikuta akitetemeka, hofu ikamjaa na mwisho wa siku, wote kwa pamoja akiwemo yeye kiongozi wakapiga magoti chini kama ishara ya kumpa heshima.

    Huo nao ukawa ushindi mkubwa, kule kuzimu alipokuwa amekwenda, alipewa nguvu za ajabu ambazo hakuamini kama angeweza kuzipata katika maisha yake.

    Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kila kitu, mzee Hamisi alikuwa kiongozi wa wachawi lakini huyohuyo ndiye alikuwa hakosi msikitini. Alikuwa mtu wa swala tano, aliheshimika mno pasipo watu kujua kwamba mtu huyo alikuwa mkubwa wa wachawi na alikuwa na nguvu mno za kichawi.

    Hiyo ndiyo stori ya mzee Hamisi niliyotaka kukupa, alikuwa miongoni mwa watu niliokutana nao kule kuzimu. Walikuwa watu wengi sana, wote hao walikuwa wakimuabudu shetani ambaye alikuwa mbele yao.

    Ukiachana na mzee Hamisi, yule mchungaji na mwanasiasa ambao wote niliwapeni sifa zao, kulikuwa na msichana mmoja hivi, msichana mrembo kwa kumwangalia, aliyekuwa na figa matata sana, naye huo alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa humo.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kwa kumwangalia, mwanaume yeyote aliye rijali asingeweza kumuacha, alivutia, alikuwa na umbo namba nane, sura nyembamba na kifuani alionekana kama msichana aliyetoka kuvunja ungo siku si nyingi.

    Sikuwa nikimfahamu, sikuwahi kumuona kabla lakini Yusnath aliniambia kwamba msichana huyo aliitwa Esta.

    Naweza kusema kwamba nchi ya Tanzania ilikuwa ikifanya mashindano ya walimbwende kila mwaka, niliwahi kuwaona wengi wakiwemo Wema Sepetu, Irena Uwoya na wengine wengi lakini kwa uzuri aliokuwa nao Esta ilikuwa ni balaa.

    “Huyu msichana ni nani?” nilimuuliza Yusnath.

    “Anaitwa Esta.”

    “Anakaa wapi?”

    “Anaishi Ilala.”

    “Naye anaabudu hapa?”

    “Ndiyo!”

    “Yupo kitengo gani?”

    “Huyu ni kwa ajili ya kuua tu na kuwalaghai watu. Huyu ni msichana mbaya sana ambaye ombea kukutana na simba lakini si msichana huyu,” alisema Yusnath.

    “Mmmh!”

    “Ndiyo hivyo!”

    “Ooppss!”

    “Nikwambie kingine?”

    “Kipi?”

    “Huyu msichana si binadamu!”

    “Unasemaje?”

    “Ni jini!”

    “Hebu niambie vizuri kwanza,” nilimwambia Yusnath.

    “Usijali, kuna mengi nitakwambia kuhusu Esta na namna anavyofanya kazi zake,” aliniambia Yusnath.

    “Sawa. Ningependa kusikia mengi.”

    “Usihofu! Ushawahi kusikia kuhusu jini Maimuna?”

    “Ndiyo! Nasikia ni msichana mzuri mno!”

    “Basi ndiye huyu!”

    “Ndiye yule tuliyekutana naye kule mwanzo?”

    “Unaposikia jini Maimuna, hayupo mmoja, wapo wengi, tena wote warembo!”

    “Duuh! Hebu niambie kuhusu Maimuna, ningependa kusikia mengi sana!”

    Wala usijali! Njoo huku,” aliniambia na kunipeleka pembeni, kulikuwa na viti kadhaa, nikatulia hapo, baadae akaniambia twende kwenye ule mlima mkubwa, tukapaa mpaka tulipofika huko. Kama kawaida ile televisheni kubwa ikawashwa, nilikuwa hapo kwa ajili ya kuona yale yaliyokuwa yakimhusu jini Maimuna tu. Akaanza kazi.



    Nilimuona msichana akiwa amesimama barabarani, ilikuwa usiku sana, kama saa nane hivi. Alikuwa msichana mrembo, alivalia kiheshima sana, alivutia mno, nywele zake ndefu zilifika mgongoni, alipendeza mno, kadiri nilivyokuwa nikimwangalia, hata mimi nilimpenda sana.

    Uso wake ulijawa na tabasamu kila wakati, hakuwa mswahili, alikuwa msichana mwenye mchanganyiko wa rangi ambaye ningeweza kumuita Chotara. Sikujua msichana huyu alikuwa nani, alikuwa akifanya nini mahali pale, ila kila nilipomwangalia, hakika nikajisemea kwamba hakukuwa na mwanamke mrembo kama alivyokuwa.

    Mwanzo nilifikiri alikuwa akijiuza barabarani pale, lakini haikuwa hivyo, sidhani kama kungekuwa na mwanamke aliyekuwa akijiuza huku akiwa amevalia gauni refu, lililofika unyayoni kama alivyovaa msichana yule.

    Magari yalipita, kila aliyepita na gari lake, alipokaribia mahali aliposimama msichana yule, alipunguza kasi ya gari lake na kisha kumtupia macho. Msichana yule aliendelea kusimama mpaka nilipomuona jamaa mmoja akienda upande ule aliokuwa msichana yule, kwanza akampita huku akimwangalia, alipofika kama hatua nne mbele, akaona haiwezekani, akaanza kupiga hatua kumfuata.

    Kumbuka haya yote nilikuwa nikiyaona kwenye ile televisheni kubwa ya kichawi, baada ya kumuona msichana huyu kule kuzimu huku akiitwa kwa jina la Maimuna, hapo ndipo nilipoanza kuonyeshewa maisha yake, yaani kwetu sisi hujulikana kama Jini Maimuna, yaani jini ambaye hutumia sana mvuto wake kukamata wanaume.

    Kabla ya kuzungumza chochote kile, mwanaume yule akaupamba uso wake kwa tabasamu pana, alijitahidi kuonyesha uchangamfu usoni mwake lakini msichana yule akabaki akimshangaa, mshangao uliomfanya aonekane mzuri zaidi.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Mambo vipi mrembo!” alisalimia jamaa yule.

    “Salama.”

    “Mbona upo hapa usikuusiku, huogopi vibaka na wabakaji?’ aliuliza jamaa yule.

    “Niogope nini sasa?”

    “Au mfanyabiashara tufanye biashara ya chapchap?”

    “Wewe kaka, umeniona mimi malaya?”

    “Hapana. Ila nimeuliza tu, ila kama haupo kama ninavyofikiria, naomba unisamehe,” alisema jamaa yule.

    Msichana yule hakuongea chochote, alibaki kimya huku akipiga hatua kwenda nyuma zaidi. Kumuacha msichana yule ilihitaji roho ngumu mno, jamaa yule hakutaka kukubali, mvuto wa msichana yule ulimpagawisha sana, hivyo akaona iwe isiwe ilikuwa ni lazima kumchukua usiku huo.

    Jamaa alijielezeaelezea wee, mwisho wa siku msichana yule akakubaliana naye, ila kwa sharti moja tu kwamba hakuwa tayari kwenda nyumbani kwa mwanaume huyo au gesti, kama alitaka, basi usiku huohuo, sehemu yoyote isipokuwa zile sehemu alizozitaja, na baada ya hapo, wasijuane, jamaa akakubaliana naye.

    Wakasogea pembeni kidogo, kutokana na usiku kuwa mkubwa, hakukuwa na watu kabisa, ni magari tu ndiyo yaliyokuwa yakipita. Walisogea nyumba mpaka walipofika sehemu iliyokuwa na mitimiti, hapo ndipo walipoamua kumalizia haja zao.

    Kuwa na Chotara, mrembo, anayevutia, kulimpagawisha sana jamaa yule, akachojoa nguo zake harakaharka mithili ya mtu aliyetaka kwenda sehemu fulani, baada ya hapo, akalipandisha gauni la msichana yule, akaishusha nguo ya ndani na kisha kumlaza chini na kwenda juu yake.

    Ni sauti za mahaba tu ndizo zilizokuwa zikisikika, wala hazikupita hata dakika mbili, ghafla nikamuona jamaa yule akianza kukakamaa mwili wake, akaanza kutokwa na mapovu mdomoni yaliyochanganyikana na damu, baada ya hapo, akatulia palepale kifuani.

    Msichana yule akasimama, macho yake yalikuwa mekundu mno, meno yake yakabadilika na kuwa kama ya ngiri, akamwangalia kijana yule, mwili wake ukakauka, baada ya kuona kwamba amekufa, akanyoosha mikono juu kisha kupotea.

    *****

    “Dada! Una kampani yoyote?”

    “Kampani ya nini?”

    “Utakaporudi nyumbani!”

    “Hapana! Kwani nini?”

    “Wewe unaishi wapi?”

    “Naishi Ilala!”

    “Waooo! Mimi naishi Magomeni Mikumi. Naweza japo kukupa lifti manake nipo alone tu, nina usafiri mzuri tu.”

    Sawa! Ila mpaka muziki uishe!”

    “Haina noma.”

    Yalikuwa ni mazungumzo ya watu wawili, alikuwa kijana mmoja aliyeonekana mstaarabu sana lakini uso wake ungekufanya kugundua kwamba alikuwa mlevi, alikuwa akizungumza na msichana mmoja mrembo sana katika klabu ya Usiku ya Maisha.

    Kulikuwa na disko, watu walijazana mno, kila aliyecheza, alijitahidi kuonyesha umahiri mkubwa, msichana huyo ambaye alikaa peke yake, alikuwa kimya. Wanaume wengi walikuwa wakimmezea mate msichana yule mrembo, kila mtu alikuwa na shauku ya kutaka kuzungumza naye lakini hakukuwa na aliyemsogelea zaidi ya kijana huyo tu.

    “Mimi naondoka!”

    “Poa! Twende tu!

    Wakachukuana na kisha kuelekea garini. Mwanaume yule alijiona kupata lakini ukweli ni kwamba alipatikana yeye. Alionekana kuwa mchangamfu mno, kuopoa msichana mzuri kama yule klabu, kulimfurahisha na kujiona mtu mwenye bahati sana.

    Gari likawashwa na kisha kuanza safari ya kuelekea huko Ilala. Njiani, walizungumza mengi. Kijana yule alionekana kuwa na presha kubwa, alijiona kama angemkosa msichana yule au ule ndiyo ungekuwa mwisho wa kuonana naye, hivyo akaanza kutupia ndoano yake.

    Kweli ikanasa, walipofika karibu na Mkwajuni, Kinondoni, jamaa akaegesha gari pembeni, akahamia kiti cha nyuma na kisha kumvuta msichana yule kulekule. Hakukuwa kilichoendelea zaidi ya kuanza kushikana hapa na pale na mwisho wa siku wote kujikuta wakiwa watupu, kilichofauata ni kuanza kufanya ngono.

    Kama ilivhyokuwa kwa jamaa yule wa jana ndivyo ilivyotokea hata kwa huyu, akiwa kifuani mwa msichana yule, akaanza kukakamaa mwili wake, mapovu yaliyochanganyikana na damu yakaanza kumtoka mdomoni mwake, kilichofuata, akafariki dunia na kisha yule Jini Maimuna kupotea mulemule garini.

    *****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Tetesi zikaanza kusikika ndani ya jiji la Dar es Salaam kwamba kulikuwa na mwanamke aliyekuwa akiua watu nyakati za usiku, alikuwa msichana mrembo kwa kumwangalia lakini urembo wake ule ndiyo uliowamaliza wanaume wengi.

    Watu wengi walipuuzia na hivyo kuendelea kupukutika mitaani. Wengi waliogopa lakini hakukuwa na mtu aliyethubutu kuacha kumchukua msichana mrembo kama alivyokuwa Maimuna ambaye kazi yake kubwa ilikuwa ni kupeleka damu kule kuzimu.

    Ndani ya miezi miwili, tayari wanaume kumi na nne walikuwa wameuawa na miili yao kukutwa ikiwa imekakamaa.

    Miongoni mwa majini yote yaliyokuwa na roho mbaya, Maimuna alikuwa na roho ya kikatili, hakuwa na huruma hata kidogo kitu kilichompelekea kukusanya kiasi kikubwa cha damu na kukipeleka kuzimu.

    Ndugu yangu! Unaposikia kuhusu majini, usitegemee kila jini atakuja huku akiwa kwenye utisho mkubwa, kwa hapa Tanzania, hasa mitaani kuna majini wengi mno wanaokatiza huku wakiwa katika maumbo ya kibinadamu, ni vigumu kuwajua.

    Niliendelea kubaki kuzimu kwa muda zaidi, mpaka hapo nilionyeshwa watu watatu au wanne ambao walikuwa na kazi kubwa ya kuhakikisha kazi ya Mungu aiendi sawa huku duniani na kwa kiasi kikubwa walikuwa wamefanikiwa kwani kama alivyotaka shetani ndivyo kile kilichokuwa kikiendelea kilivyofanyika.

    “Tunataka kuondoka,” aliniambia Yusnath.

    “Kwenda wapi?”

    “Kwako!”

    “Wapi?”

    “Duniani!”

    “Kwani tushamaliza?”

    “Ndiyo! Sikutaka kukuonyeshea mengi kwa huyu Maimuna kwani bado anaendelea na kazi kubwa huko duniani, cha msingi, kuwa makini na wasichana warembo wa usiku wa manane,” aliniambia Yusnath.

    “Sawa. Ila hukuniambia lengo la kunileta huku usiku huu.”

    “Nilitaka kukuonyeshea haya, upate kuwaambia na wenzako wawe makini.”

    “Mmmh!”

    “Nini?”

    “Wewe ni jini au binadamu?”

    “Unanionaje?”

    “Sijui nijibu nini, ila unaonekana kuwasaidia wanadamu, unanishangaza,” nilimwambia Yusnath ambaye alicheka sana, naweza kusema kwamba kicheko chake kilikuwa cha ajabu mno, kilinishtua sana, hapohapo akapotea, na mimi kujikuta nikiwa nimelala kitandani, yaani usiku uleule aliokuwa amenichukua, nikajiuliza sasa mbona siku haikubadilika na wakati nilitumia siku nyingi? Sikupata jibu.

    Asubuhi nilipoamka, nikayabadilisha maisha yangu, kwanza sikutaka kumuamini mtu yeyote, leo hii ninapowasikia wachungaji wakijisifia sana kwamba wanatenda miujiza, huwa ninawachukia kwa kuamini miujiza anafanya Mungu peke yake na si binadamu.

    Ninaposikia kwamba maalbino wanauawa, najua wanasiasa wenye roho mbaya wapo kazini wakifanya mambo yao ya kikatili.

    Ndugu yangu! Katika ulimwengu huu kuna mambo mengi sana hutokea, mengine yanaweza kuonekana kwa macho ya kibinadamu ila mengine ni vigumu sana. Tunachotakiwa ni kuishi katika misingi ya Mungu, wale wa kwenda kanisani, waende, na wale wa kwenda msikitini pia waende japokuwa hatutakiwi kuwaamini hata viongozi wetu kwani wengi wao huchukua nguvu kutoka kuzimu.

    Hiyo ilikuwa safari yangu ya kwanza na ya mwisho kwenda kuzimu, ni miaka ishirini imepita, sikuwahi kuchukuliwa tena na kupelekwa huko mpaka leo hii ambapo nimemkabidhi Mungu maisha yangu na kuwa mchungaji katika Kanisa la Praise And Worship.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Yusnath hakunitokea tena, na sikutaka kusikia kitu chochote kile kutoka kwake. Nilichokuwa najaribu kukwambia ni kwamba shetani yupo kazini, unapojikwaa tu, anatokea kwa ajili ya kukuchukua na kukutumikisha maisha yako yote.

    Sisi kama watoto wa Mungu! Yatupasa tumwangalie Baba yetu ambaye ni Mungu na kuachana na uovu wote wa dunia hii.



    MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog