Search This Blog

SAFARI YANGU YA KWANZA KUZIMU - 4

 





    Simulizi : Safari Yangu Ya Kwanza Kuzimu

    Sehemu Ya Nne (4)



    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hofu zilizidi kuongezeka mioyoni mwao, hawakuamini kile kilichokuwa kikija mbele yao, mawimbi makubwa mithili ya ghorofa nne yalikuwa yakiwafuata kule walipokuwa, hawakutaka kusubiri, wakaanza kutimua mbio kurudi nyuma.

    Walikimbia kwa kasi kubwa lakini kila walivyogeuka nyuma, mawimbi yalikuwa yakija kwa kasi. Mbio zile ziliendelea kwa umbali fulani na ndipo waliposimama baada ya kusikia ukimya mkubwa nyuma yao, walipogeuka, hakukuwa na kitu chochote zaidi ya lile pori walilokuwa wakilifuata.

    Hawakujua ni kitu gani walitakiwa kufanya zaidi ya kuondoka huku wakihesabia kwamba walishindwa kwa kile walichotaka kukifanya. Hawakuwa na sehemu nyingine ya kwenda zaidi ya kurudi nyumbani huku kila mmoja akionekana kuwa na mawazo.

    “Umefikiria nini?” aliuliza mzee Hamisi, alionekana kuchanganyikiwa.

    “Inabidi tuondoke hapa.”

    “Kwenda wapi?”

    “Tongoni.”

    “Mmmh!”

    “Usigune, huko ndiyo nuksi, hakuna sehemu iliyokuwa na wataalamu wa kuroga kama huko, ni balaa,” alisema mzee Majoka.

    “Ila nasikia ni mbali, tutaweza kufika leoleo?”

    “Haitowezekana, hapa kitu cha msingi tuondoke kesho asubuhi na mapema kwenda huko,” alisema mzee Majoka.

    Hawakuwa na jinsi, kwa kuwa walikwenda Tanga kwa ajili ya kazi moja tu, hawakukubali kurudi kirahisi pasipo kukamilisha kile walichokuwa wakitaka kukamilisha. Usiku wa siku hiyo, walikuwa wakizungumza namna ya kukabiliana na Ramadhani ambaye alionekana kuwa moto wa kuotea mbali.

    “Huyu kijana ni balaa,” alisema mzee Hamisi.

    “Kwani ilikuwajekuwaje mpaka ukataka kupambana naye?” aliuliza mzee Majoka na mzee Hamisi kuanza kuhadithia kile kilichokuwa kimetokea.

    “Kuna watu balaa, usipende kuwaingilia kichwakichwa, utauawa,” alionya mzee Majoka.

    Hakukuwa na mtu aliyelala mapema siku hiyo, kwa kuwa alikuwa amepata ugeni, mzee Majoka hakuondoka usiku kwenda kuwanga, walibaki mpaka saa nane ya usiku ndipo wakalala.

    Siku iliyofuata asubuhi na mapema wakaamka na kujiandaa kwa safari ya kuelekea Tongoni. Huko hakukuwa karibu, kutoka hapo Handeni mpaka huko ilikuwa ni zaidi ya masaa matano kwa gari la kawaida na kutokana na ubovu wa barabara, walitarajia kutumia masaa nane njiani.

    Wakabeba mizigo yao, wakaikabidhi safari yao kwa majini yao na kisha kwenda huko Tongoni kwa mzee aliyekuwa nuksi kuliko wote, huyo alitwa mzee Hamadi, mzee aliyekuwa na mguu mbovu, akichechemea lakini kwenye suala zima la uchawi, hakuwa mtu wa kuchezewa.

    Tongo kilikuwa moja ya vijiji vilivyojaa wachawi kuliko sehemu zote nchini Tanzania, huko kulikuwa na uchawi wa kila namna, watu wengi waliokuwa wakitafuta utajiri walikwenda huko na hata wale waliokuwa wakitaka kuwatoa watu kafara ya damu, sehemu ya kwanza kwenda ilikuwa Tongoni.

    Uchawi wa Tongoni ulikuwa tofauti na uchawi wa sehemu nyingine, huko, kila mtu alionekana kuwa mtaalamu wa kuroga jambo lililowafanya uchawi wao mwingi kwenda kufanyia nje ya kijiji hicho.

    Kutokana na umbali wa sehemu yenyewe, walichukua masaa saba mpaka kufika Tongoni ambapo huko wakapokelewa kwa ukarimu mkubwa kwani mzee Majoka alijulikana sana kutokana na uchawi aliokuwa akiufanya kutetemesha Handeni yote.

    “Mnacheza na mtu hatari sana,.” Alisema mzee Hamadi hata kabla wageni wake hawajaelezea kile kilichokuwa kimewaleta.

    “Umejuaje?”

    “Huyo mtu ni hatari sana, ni mkuu wa uchawi kule Magharibi, ana nguvu mno na anaweza kukuueni siku yoyote ile na mahali popote,” alisema mzee Hamadi.

    “Ramadhani ni mkubwa wa wachawi Magharibi?”

    “Ndiyo! Ni mtu wa kukaa mbali sana kwani anatisha.”

    “Sawa. Ila sisi tumekuja utufanyie mambo, tunataka tumuondoe,” alisema mzee Hamisi.

    “Jamani! Hivi nilivyowaambieni kuhusu yeye, mnafikiri mimi nitamuweza kweli?” aliuliza mzee Hamadi huku akiwashangaa.

    “Kwa hiyo unashindwa?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ndiyo!”

    “Na hakuna njia ya kumpoteza?”

    “Ipo.”

    “Ipi hiyo?”

    “Ni lazima ufuge majini,” alijibu mzee Hamadi.

    “Nifuge majini? Mbona ninayo mengi tu!” alisema mzee Hamisi.

    “Hayo majini ni machache sana, halafu majini yako hayana nguvu ya kutosha, mwenzako huyu ana majini yale makubwa ambayo yana roho mbaya na muda wote yapo yanamlinda, cha kufanya na wewe ni kutafuta majini makubwa na yenye nguvu ambayo yataweza kupambana na majini ya huyu,” alisema mzee Hamadi.

    “Hayo majini nitayapata wapi?”

    “Nyumbani.”

    “Wapi?”

    “Kuzimu. Huko ndipo utakapoyapata hayo majini mengine.”

    “Kwa hiyo natakiwa kwenda huko? Nitakwendaje? Sijawahi kwenda huko kwani nasikia wote wanaokwenda huko huwa na vibali maalumu,” alisema mzee Hamadi.

    “Nitakupeleka!”

    “Nitashukuru sana.”

    Kidogo moyo wa mzee Hamisi ukapoa, hakuamini kama naye angefanikiwa kwenda kuzimu. Ngoja niwaambie kitu kimoja. Katika suala la kwenda kuzimu halikuwa la kawaida hata kidogo, kwa kila mchawi alikuwa akitamani kwenda huko lakini si kila mtu aliyewwahi kufika.

    Kuna mtu mwingine anakuwa mchawi tangu akiwa mdogo lakini mpaka anazeeka na kufariki, hajawahi kukanyaga huko. Hiyo ni sawa na mawaziri wetu. Unaweza kuwa waziri lakini katika miaka yote kumi, unaweza usikanyage ikulu, hivyo ndivyo ilivyokuwa hata kwa wachawi kuingia kuzimu.

    Alipoambiwa hivyo, mzee Hamisi alifurahi sana, ni kweli alihitaji kwenda huko na ndiyo maana aliambiwa kwamba alipaswa kujiandaa na hakukuwa sehemu ya mchezomchezo. Hilo wala halikuwa tatizo, ilipofika usiku, akaambiwa kwamba safari hiyo ingefanyika baharini, hivyo walitakiwa kupanda ungo na kwenda huko sehemu ambayo ndiyo yalikuwa makazi makuu ya shetani. Safari ikaanza.

    Mzee Hamisi alikuwa na hamu kubwa ya kufika kuzimu, kitu alichokuwa akikifikiria kwa wakati huo ni kufuga majini tu, tena yale yenye nguvu kubwa ambayo aliambiwa kwamba ndiyo yangeweza kumuua Ramadhani kama alivyokuwa akitaka.

    Usiku huohuo wakachukua ungo, ndani yake kulikuwa na tunguli nyingi na walikuwa wakienda kwa mwendo wa kasi mno. Kwa wakati huo, safari yao ilikuwa ni kuelekea katika Bahari ya Hindi ambapo huko ndipo wangepita na kuelekea kuzimu.

    Hawakuchukua muda mrefu, wakafika ufukweni ambapo moja kwa moja wakateremka na mzee Hamadi kuchukua mayai mawili na kuyatupa mule baharini kisha kumwambia mzee Hamisi waingie ndani ya yale maji.

    Mara ya kwanza mzee huyo alikuwa akiogopa, alipopiga hatua ndani ya maji na kusogea mbele, aliona kwamba angeweza kuzama hivyo akaanza kwenye kwa machale sana. Kwa muonekano aliokuwa nao tu mahali hapo, ulitosha kukwambia kwama alikuwa na hofu kubwa ya kukumbana na kitu kibaya, alichokifikiria zaidi ni kuzama tu.

    “Hatutoweza kuzama?” aliuliza huku akionekana kuwa na hofu.

    “Hatuwezi, huku ndipo makao makuu, huku ndipo ilipo ikulu yetu,” alisema mzee Hamadi.

    Tayari maji yaliwafikia vifuani, mzee Hamisi aliendelea kuogopa zaidi lakini baada ya maji kuwafikia machoni, ghafla wakajikuta wakiwa katika ulimwengu mwingine kabisa, kulipokuwa na mji mwingine, kwa muonekano tungesema dunia nyingine kabisa.

    Mzee Hamisi akabaki akiangalia huku na kule, kuzimu kulikuwa kama duniani, kama ambavyo huku tuna serikali yetu basi napo kule kuna serikali yao pia, kama huku watoto walikuwa wakielekea shuleni kusoma basi hata kule ilikuwa hivyohivyo.

    Hakukuwa na mabadiliko makubwa japokuwa kule hakukuwa na binadamu, kulikuwa na viumbe vya ajabuajabu ambavyo kama ungekuwa nje ya ulimwengu ule ilikuwa ni lazima kuogopa sana.

    Wakaanza kupiga hatua kuelekea sehemu iliyokuwa na njia nyembamba ambayo ilizungukwa na majani mengi. Moyo wa mzee Hamisi ulikuwa na mengi ya kuuliza lakini aliamua kukaa kimya mpaka pale ambapo angeruhusiwa kuuliza kitu chochote kile.

    Wakafika katika nyumba moja, ilikuwa kubwa mno, nje ya nyumba ile kulikuwa na miti miwili iliyokuwa imesimikwa chini, juu ya miti ile kulikuwa na mafuvu ya watu yaliyoonekana kukauka mno. Wakaanza kupanda ngazi kueleka katika jumba lile.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ni wapi hapa?” aliuliza mzee Hamisi kwa sauti ya chini.

    “Hapa ni kwa mkuu wa mkoa!”

    “Mkuu wa mkoa?”

    “Ndiyo!”

    “Kivipi tena? Mbona unanichanganya?”

    “Huku pia kuna serikali kama ilivyo duniani, kuna balozi wa nyumba kumi, wakuu wa wilaya, mikoa, bunge, mawaziri na hata rais,” alisema mzee Hamadi.

    “Huwa nao wanazungumzia bajeti na mambo mengine?”

    “Hapana! Huku watu wapo bize kuzungumzia mambo mengi kuhusu kuiteka dunia, watu wasiweze kwenda makanisani wala misikitini, hicho ndicho wanachokizungumzia sana huku, kuiangusha dunia,” alijibu mzee Hamadi.

    Tayari walikuwa wamefika katika mlango wa kuingilia ndani ya jumba lile kubwa hasa mara baada ya kupandisha ngazi kadhaa. Wala hawakugonga mlango, wakaona ukijifungua na kuingia ndani.

    Mandhari yaliyokuwa ndani, mzee Hamisi akajikuta akitamani japokuwa baadhi ya vitu havikuwa kama duniani. Kulikuwa na televisheni kubwa ikiwa imepachikwa ukutani, ilikuwa na ukubwa wa inchi 40.

    Mbali na televisheni ile, pia kulikuwa na makochi makubwa, yalikuwa na rangi nyekundu na alipouliza, aliambiwa kwamba makochi yale hayakutengenezwa kwa kutumia vitambaa bali yalitengenezwa kwa kutumia ngozi za binadamu ambazo kule zilikuwa dili mno.

    Juu ya meza ya kioo kulikuwa na birika moja kubwa na pembeni yake kulikuwa na jagi la jeupe. Mzee Hamisi alipoliangalia vizuri jagi lile, akagundua kwamba ndani yake kulikuwa na damu kwani ilikuwa nyekundu mno.

    “Kuna kitu nataka nikuonyeshee,” alisema mzee Hamadi.

    “Kitu gani?”

    “Nataka nikuonyeshee maiti mbalimbali.”

    “Maiti zipi?”

    “Kila wiki zinaletwa maiti humu.”

    “Kazi yake nini?”

    “Kwa ajili ya nyama tu.”

    Wakati wanazunguka ndani ya nyumba hiyo kubwa na ya kifahari, hawakuwa peke yao bali walikuwa wakipishana na viumbe vya ajabu ambavyo kwa kuviangalia tu, mzee Hamisi alijawa na hofu kubwa, wakati mwingine alitamani kukimbia, akajikuta akifumba macho tu.

    Wakafika katika mlango mmoja ambao uliandikwa maneno ambayo wala hakuyaelewa, mzee Hamadi akagonga hodi na baada ya sekunde kadhaa, mlango ukafunguliwa na mwanamke mmoja mrembo wa sura, alimvutia hadi mzee Hamisi.

    Alikuwa msichana mrefu, mweupe, nywele zake zilifika kiunoni, alipendeza kumwangalia na kila alipokuwa akitabasamu, uzuri wake uliongezeka zaidi.

    “Usitabasamu,” alisema mzee Hemedi, alikuwa akimwambia mzee Hamisi.

    “Kwa nini? Yeye si ndiye aliyeanza kutabasamu?”

    “Hata kama! Ukitabasamu kama alivyotabasamu, huwa anakasirika sana,” alisema mzee Hamadi.

    “Kwa nini? Kwani yule nani?”

    “Unamjua jini Maimuna?”

    “Namsikiasikia tu, si yule wa mapenzi?”

    “Ndiyo!”

    “Huwa ninamsikia tu.”

    “Ndiye yule aliyetufungulia mlango!”

    “Kumbe ni mzuri vile!”

    “Ndiyo! Twende mbele kwanza, kuna mengi ya kukuonyesha.”

    Wakaendelea kusonga mbele mpaka kwenye mlango mmoja mkubwa uliokuwa na rangi nyeusi, walipouangalia mlango ule, ulionekana kuwa tofauti na milango mingine. Mlangoni kulikuwa kumeandikwa maneno makubwa yaliyosomeka SONYITO, maneno ambayo mzee Hamisi hakuyaelewa kabisa.

    “Sonyito ndiyo nini?”

    “Maiti zinazozungumza.”

    “Mmmh!”

    “Ngoja tuingie, utaziona tu,” alisema mzee Hamadi na kisha kuanza kuugonga mlango ule, kwanza kwa mbali, wakaanza kusikia sauti ya vilio kutoka ndani ya chumba kile, mzee Hamisi akaanza kuogopa, alitamani kumwambia mzee Hamadi warudi walipotoka.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mwili ukaanza kumtetemeka na kijasho chembamba kumtoka. Mlango ukafunguliwa, huyo aliyeufungua, hakuonekana kuwa jini wa kawaida, alikuwa ni wa tofauti sana na majini wengine.

    “Mama yangu!” alijikuta akijisemea mzee Hamisi huku mapigo yake ya moyo yakianza kudunda kwa kasi. Hofu ikamjaa.

    Aliyesimama mbele yao alikuwa jini makata, jini mkorofi aliyekuwa na kazi moja ya kuwatesa watu kule kuzimu. Ngoja nikwambie kitu kimoja, unapofika kuzimu huwa kunakuwa na yale majini ambayo yalipewa kazi ya kufanya lakini kwa bahati mbaya yakajikuta yakishindwa. Kule kuzimu hakuna kitu kinachoitwa kushindwa hivyo uadhibiwa.

    Mbali na majini hayo, huwa kunakuwa na zile maiti za watu waliokufa lakini makazi yao huwa ni ya kuzimu milele. Maiti zile huwa zinachukuliwa na kupelekwa huko ambapo hupewa roho chafu na kisha kuanza kuadhibiwa kwani roho ile yenyewe inakuwa imekwishakwenda kwenye hukumu.

    Huyo ndiye alikuwa jini makata, alitisha, alikuwa na kichwa kama cha paka, alikuwa na nywele nyingi kama simba, kila alipoongea, meno yake yaliyochongeka yalionekana vizuri. Kuna kipindi kingine hasa anapokuwa na hasira kali, kila anapoongea huwa anatoa cheche mdomoni mwake.

    Jini yule alipowaona watu hao, hakuzungumza kitu chochote, aliwaruhusu kuingia ndani na kuona jinsi maiti zile zilivyokuwa zikiteswa kule kuzimu. Yalikuwa mateso makubwa na zilipiga kelele mno lakini hakuonekana kujali chochote kile, aliendelea kuzitesa kama kawaida yake.

    Alichukua mikuki mikubwa iliyokuwa na ncha kali ambayo iliwekwa kwenye moto na kuwa nyekundu mno kisha kuanza kuzchoma kana kwamba alizichoma na miti ya mishikaki na kisha kuanza kuzipiga huku na kule.

    Alipoona hiyo haitoshi, alikuwa akichukua rungu moja kubwa na kuanza kuzipiga kwa zamu. Hiyo ilikuwa ni kazi yake ya kila siku na wala hakuchoka kabisa. Yalikuwa ni mateso makali lakini hakuacha, hizo zilikuwa adhabu kwa kuwa walishindwa kufanya kile walichotaka kukifanya.

    Mzee Hamisi alikuwa na hofu kubwa, ni kweli alifuga majini lakini hakuwahi kuona jini aliyekuwa na sura mbaya kama aliyokuwa nayo jini makata. Alitisha sana lakini akashindwa kukimbia.

    Walizunguka ndani ya kile chumba kwa dakika kadhaa kisha kuondoka na kuelekea katika jumba jingine kabisa, huko ndipo alipoambiwa kwamba rais wa kuzimu, shetani alipokuwa akiishi.

    Aliwahi kuzisikia hadithi nyingi kuhusu shetani, siku hiyo alikuwa mahali hapo kwa ajili ya kumuona huyo shetani mwenyewe ambaye kila siku aliifanya kazi zake kama mfuasi wake duniani.

    Walipiolifikia jumba hilo, wakaanza kupandisha ngazi na kuona kibao fulani kikubwa kilichoandikwa LUCIFER PARADISE. Hapo, akatakiwa kuinamisha kichwa chake kama kutoa ishara ya kumuabudu na kisha kuruhusiwa kuingia ndani ya jumba hilo kubwa.

    “Hapa ndipo kwa mkuu wetu,” alisema mzee Hamadi.

    “Umesemaje?”

    “Hapa ndipo kwa mkuu wetu, chochote nitakachofanya, fanya,” alisema mzee Hamadi.

    “Sawa mkuu.”

    Mzee Hamisi alionekana kutokujiamini, hata hatua zake zikaanza kubadilika mahali pale, hakuamini kama katika maisha yake angeweza kumuona shetani ambaye kila siku alimuabudu kwa vitu vya kishirikina alivyokuwa akivifanya.

    Kabla ya kumuona shetani, kulikuwa na mageti saba ambayo ulitakiwa kuvuka. Naomba niseme kitu kwamba hata naye shetani alijifanya Mungu. Kama ambavyo watu wanaposema kulikuwa na mbingu saba mpaka kufika kwa Mungu basi naye shetani alijiwekea mipaka kwamba ulitakiwa uvuke mageti saba ndiyo umfikie yeye.

    Geti la kwanza kabisa ambalo walikutana nalo kulikuwa na mwanamke mmoja aliyeonekana kuwa mzee sana, alitia huruma kwa kumwangalia tu, ni kama alikuwa akihitaji msaada wa fedha.

    Alionekana kuwa na uhitaji mkubwa sana, mzee Hamisi na Hamadi walipofika getini hapo na kumwangalia mwanamke yule, walimuonea huruma sana, hasa mzee Hamisi ambaye hakutarajia kukutana na mwanamke aliyekuwa akitia huruma kama yule.

    Huyo ndiye aliyekuwa ufunguo wa kuingilia geti la kwanza kabisa, ili uweze kuvuka hapo ulitakiwa kumuua tu. Haukutakiwa kumuonea huruma, ili uweze kupita kwa urahisi ilikuwa ni lazima kumuua.

    Wengi waliotaka kwenda huko walishindwa mahali hapo. Kwa jinsi mwanamke yule alivyotia huruma, lilikuwa jambo gumu sana kumuua. Pembeni mwa mwanamke yule kulikuwa na panga moja kubwa lenye makali pande zote mbili.

    “Huyu mwanamke anafanya nini hapa?” aliuliza mzee Hamisi.

    “Amekaa tu.”

    “Kwa nini aondoki?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hawezi kuondoka kwani yeye ndiye ufunguo wa kusonga mbele,” alijibu mzee Hamadi.

    “Unamaanisha nini?”

    “Unatakiwa umuue ili uvuke geti la kwanza.”

    “Nimuue huyu mwanamke?”

    “Ndiyo!”

    “Acha utani!”

    “Basi turudi.”

    “Turudi kabla ya kufanya kilichotuleta?”

    “Sasa tutafikaje kama hutaki tuchukue ufunguo.”

    “Kwa maana hiyo mwanamke huyu ndiye ufunguo?”

    “Haswaaaa.”

    Mzee Hamadi alivyoongea hivyo, mwanamke yule alizidi kutia huruma zaidi kiasi kwamba mzee Hamisi akajikuta akilengwa na machozi na baada ya sekunde chache machozi kuanza kumbubujika mashavuni mwake.

    Ni kweli alikutana na ombaomba wengi mitaani lakini siku hiyo, mwanamke yule alitia huruma kuliko ombaomba wote aliowahi kukutana nao mitaani. Alimwangalia vizuri mwanamke yule, alijiona akishindwa kabisa kuchukua lile panga na kumuua.

    “Basi turudi.”

    “Ningependa niendelee mbele mpaka huko alipo lucifa,” alisema mzee Hamisi.

    “Basi fanya kama nilivyokwambia,” alisema mzee Hamadi.

    Mzee Hamisi hakujua afanye nini kwani kila alipomwangalia mwanamke yule, alizidi kutia huruma mno.



    Moyo wake ulikuwa na hofu tele, uso wa mwanamke yule mzee bado uliendelea kumtia huruma kubwa kiasi kwamba aliona kulikuwa na ugumu mkubwa wa kuweza kufanya kile alichokuwa ameambiwa.

    “Muue haraka mlango ufunguke,” alisema mzee Hamadi kwa sauti kubwa.

    Kwa mzee Hamisi, lile likaonekana kuwa jambo gumu, kilichompa ugumu wa kumuua mwanamke yule ni sura ya kipole aliyokuwa nayo. Hakuwa radhi kuona akimuua mwanamke huyo na wakati hata muonekano wake ulionyesha kwamba alikuwa na shida mno katika maisha yake.

    Pamoja na kukataa huko lakini bado mzee Hamadi alikuwa akimsisitiza kwamba alitakiwa kumuua ili waendelee mbele kwani mlango ule wa kwanza usingeweza kufunguka pasipo kumuua mwanamke yule.

    “Kama hautaki sema turudi na usimuone Lusifa,” alisema mzee Hamisi.

    Kitendo cha kulitaja jina la Lusifa tu, mzee Hamisi akajikuta moyo wake ukipata nguvu, huruma aliyokuwa nayo ikaanza kupungua, akajikuta akichukua panga lile lililokuwa pembeni na kisha bila kumwangalia usoni mwanamke yule akaanza kumshambulia na panga lile, alikuwa akimkatakata kichwani na maeneo mengine ya mwili wake.

    Damu zilitapakaa sehemu hiyo yote, japokuwa sauti ya mwanamke yule ilisikika masikioni mwake akiomba msamaha lakini mzee Hamisi hakujali hilo, alichokifanya ni kuendelea kumkatakata na panga lile mpaka pale alipokufa, hapohapo geti lile kubwa likafunguka.

    “Tuondoke. Hongera sana, umefanikiwa,” alisema mzee Hamadi huku akionekana kurufahia.

    Wakaingia ndani, wakaanza kupiga hatua na kuelekea sehemu ambayo aliambiwa kwamba kulikuwa na geti la pili.

    Walitembea kwa harakaharaka, hakukuwa na mtu yeyote ambaye walipishana naye njiani lakini kwa hali halisi ni kwamba walipishana na majini pasipo kufahamu hilo. Walitembea mpaka walipofika katika geti moja kubwa ambalo hilo lilikuwa ni geti la pili kuelekea kule kwa Lusifa, hivyo walitakiwa kupita.

    Walichokifanya ni kulifuata geti hilo na kutaka kulifungua, kama lilivyokuwa lile la mwanzo, hata hilo lilikuwa gumu kufunguka. Huku wakijifikiria nini cha kufanya, mara kukatokea mwanamke mmoja akiwa mjauzito, alionekana kuwa kwenye nyakati za mwisho kujifungua na alipowaona tu, alihitaji msaada wa kusaidiwa kwani hakukuwa na watu wengine wa kuwaomba msaada zaidi yao.

    “Kwanza tungemsaidia huyu mwanamke,” alisema mzee Hamisi.

    “Hakuna kumsaidia.”

    “Kwa nini na wakati anahitaji msaada?” aliuliza mzee Hamisi.

    “Ukimsaidia, unakufa wewe.”

    “Unasemaje?”

    “Ndiyo hivyo!”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hapana! Mimi nataka nimsaidie, ni mwanamke mjauzito, anahitaji sana msaada,” alisema mzee Hamisi huku akimwangalia mwanamke yule kwa macho yaliyojaa huruma tele.

    “Hamisi! Nisikilize kwa makini. Nikwambie.”

    “Kitu gani.”

    “Unataka kumuona Lusifa?”

    “Ndiyo! Tena nina hamu kubwa.”

    “Basi muue huyu mwanamke!”

    “Unasemaje?”

    “Muue huyu mwanamke kwa kumpiga ngumi za tumbo, tena mfululizo,” alisema mzee Hamadi huku akimaanisha kile alichokuwa akikisema.

    Mwanamke yule mjauzito ambaye alikuwa akiomba msaada ndiye aliyekuwa ufunguo wa geti lile la pilii kuelekea kwa Lusifa. Hilo lilionekana kuwa gumu mno kwa mzee Hamisi kwani kila alipokuwa akimwangalia mwanamke yule, hakika alitia huruma sana.

    Alipoambiwa kwamba ndiye aliyekuwa ufunguo wa geti lile, kwanza akabisha kwani muonekano wa mwanamke yule ulionyesha kwamba alihitaji msaada wa hali na mali.

    “Ukimsaidia utakufa,” yalijirudia maneno yale aliyosema mzee Hamdai, maneno ambayo yalimfanya kuwa na hofu kubwa moyoni mwake.

    “Muue haraka tuendelee na safari,” alisema mzee Hamadi.

    Hiyo ndiyo ilikuwa njia ya kuweza kupita katika geti lile, mwanamke yule hakunyamaza, bado aliendelea kulia huku akiomba msaada wa kusaidiwa pale alipokuwa kwani alionekana kuwa katika kipindi cha kutaka kujifungua.

    Huku wakiendelea kumwangalia, mara damu zikaanza kumtoka mwanamke yule sehemu za siri, alionekana kuzidiwa na kama asingepewa msaada mahali pale basi angeweza kufariki dunia. Kama walivyokuwa binadamu wengine, mzee Hamisi alishikwa na huruma ya kiwango cha juu kabisa, kile kilichokuwa kikitokea, alihisi isingekuwa roho nzuri kama angemwacha mwanamke yule akiendelea kuteseka.

    “Anakaribia kujifungua, fanya haraka, mpige ngumi, mtoto akitoka tu tutakufa,” alisema mzee Hamadi huku akimshikashika mzee Hamisi kama kumsisitiza juu ya kile alichotakiwa kukifanya mahali pale.

    Hakukuwa na la kufanya, kwa kuwa ndiyo ilikuwa moja ya masharti aliyokuwa amepewa ya kufungua geti lile, hapohapo akaanza kumpiga mwanamke yule ngumi za tumbo. Moyo ulimuuma mno, alijiona kuwa mtu katili lakini hakutaka kuona akishindwa kumuona Lusifa na wakati kumuona huko aliamini kwamba angepata nguvu kubwa na hata kumiliki majini yaliyokuwa na uwezo mkubwa.

    Ngumi zile zikampeleka mwanamke yule chini, alikuwa akiugulia kwa maumivu makali, damu ziliendelea kumtoka huku mtoto akianza kutoka katika njia ya kujifungulia.

    “Nimeua...” alisema mzee Hamisi, machozi yalikuwa yakimtoka.

    “Usijali! Ni sehemu ya kumuona mkuu wetu, tuondoke,” alisema mzee Hamadi.

    Mzee Hamisi hakutaka kuondoka, kwanza akapiga magoti chini na kumwangalia mwanamke yule, machozi yalikuwa yakimbubujika tu. Hapohapo, mwanamke yule na mtoto wake, wakafariki dunia. Geti likafunguka.



    “Tuondoke!” alisema mzee Hamadi.

    “Inaniuma sana,” alisema mzee Hamisi huku akiwa pale chini akiiangalia maiti ya yule mwanamke.

    “Tuondoke geti litafunga,” aliendelea kusisitiza mzee Hamadi ambapo hapohapo mzee Hamisi akanyanyuka na kuanza kuondoka mahali hapo.

    Moyo wake bado uliendelea kuwa kwenye maumivu makali, hakuamini vile vilivyokuwa vikitokea kule kuzimu, vilimtisha, vilimhuzunisha na kumpa huzuni kubwa moyoni mwake, katika kila geti alilotakiwa kupita, ilikuwa ni lazima afanye mauaji, tena kwa mkono wake mwenyewe.

    “Wewe mbona hutaki kuua?” aliuliza mzee Hamisi.

    “Siwezi kuua kwa sababu nimeshaua sana nilipokuja kwa mara ya kwanza, huku nimekuleta wewe, unatakiwa kuwa makini sana, wakati mwingine unaweza kufa wewe,” alisema mzee Hamadi.

    Wakati huo walikuwa wakipiga hatua kuelekea mbele zaidi, walikuwa wakilifuata geti jingine la tatu. Mzee Hamisi alikuwa akijifikiria juu ya geti la tatu, hakujua ni kitu gani ambacho angekikuta huko, akabaki kimya, hakutaka kujifikiria sana kwani aliamini kwamba angejisumbua tu.

    Walipita katika jumba hilo, walikuwa wakielekea juu kabisa. Walipofika katika korido moja kubwa iliyokuwa na sakafu nyeusi, wakaingia katika chumba kimoja ambacho mzee Hamadi alimwambia kwamba kilikuwa chumba cha mapumziko, huko wangekula na kunywa.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ndani ya chumba kile kulikuwa na meza kubwa, kuangalia juu yake, kulikuwa na chupa moja kubwa, ilikuwa ni kama ya soda, ndani kulikuwa na maji mekundu ambayo kwa harakaharaka mzee Hamisi akagundua kwamba ile ilikuwa damu.

    Mbali na chupa ile, pia kulikuwa na mabakuli makubwa yaliyosheheni nyama iliyokuwa ikinukia vizuri kabisa. Wakaanza kupiga hatua kuifuata meza ile ndefu iliyozungukwa na viti zaidi ya ishirini na kisha kuchukua vikombe na kuanza kuimimina damu ile na kuanza kunywa.

    Mzee Hamisi alikuwa mchawi, hiyo haikuwa mara yake ya kwanza kunywa damu, alikwishawahi kunywa walipokuwa katika uwanja wa kichawi hivyo ile ilikuwa ni kama kujikumbushia tu.

    Nyamza zile zilizokuwa zikionekana katika mabakuli hazikuwa nyama za ng’ombe au mbuzi, zilikuwa ni nyama za binadamu zilizokatwa vipandevipande, hapohapo wakaanza kuchukua na kuanza kula.

    “Usiniangushe rafiki yangu,” alisema mzee Hamadi.

    “Sitoweza kukuangusha.”

    “Sasa kwa nini umekuwa na moyo wa huruma hivyo?”

    “Huwa inatokea, ila nakuahidi kwamba sitokuangusha tena,” alisema mzee Hamisi huku akionekana kumaanisha alichokuwa akikizungumza.

    “Kama ni hivyo, sawa, tuendelee na safari,” alisema mzee Hamadi na safari kuanza tena.

    Walitembea kwa mwendo wa harakaharaka kama watu wanaowahi sehemu fulani. Hawakuzungumza kitu chochote kile mpaka walipofika sehemu iliyokuwa na geti jingine la kuingilia sehemu ya upande wa pili, kama yalivyokuwa mageti mengine yaliyopita, hata lile geti la tatu nalo lilikuwa limefungwa.

    “Tunafanyaje? Ufunguo upo wapi?” aliuliza mzee Hamisi.

    “Subiri kwanza.”

    Mzee Hamisi ndiye aliyeonekana kuwa na presha sana kana kwamba hilo lilikuwa geti la mwisho ambapo baada ya kulifungua angekutana na shetani. Kila wakati alikuwa akimuuliza mzee Hamadi juu ya ufunguo wa kufungulia geti lile lakini mzee Hamadi hakusema kitu zaidi ya kumwambia kwamba anapaswa kusubiri.

    “Hakuna kitu.”

    “Subiri kwanza, wala usijali.”

    Hawakukaa sana, ni ndani ya dakika chache tu, ghafla likatokea giza kubwa mahali hapo kiasi cha kutoweza kuonana. Mzee Hamisi aliogopa mno, alikuwa akiweweseka huku akihisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wao.

    Akaanza kupapasa huku na kule ili hata aweze kumgusa mzee Hamadi lakini hakuweza kufahamu mahali alipokuwa hali iliyomfanya kuwa na hofu kubwa moyoni mwake kiasi cha kutetemeka mwili huku kijasho chembamba kikimtoka.

    “Hamadi! Upo wapi?” aliita mzee Hamisi.

    “Nipo hapa.”

    “Wapi?”

    “Hapana niliposimama.”

    “Kuna nini tena? Mbona giza sana?” aliuliza mzee Hamisi huku akiwa na hofu kubwa.

    “Ufunguo unakuja.”

    “Upo wapi?”

    “Nisikilize kwa makini. Nakupa maelekezo juu ya unachotakiwa kukifanya,” alisema mzee Hamadi.

    “Sawa. Nipe maelekezo.”

    “Hapo mbele yako kuna vikapu vitatu vyenye majina ya watu watatu.”

    “Ndiyo!”

    “Kikapu kimoja kina jina la mtoto wako wa mwisho, yule unayempenda sana, kikapu cha pili kina jina la mke wako na kikapu cha tatu kina jina la mama yako,” alisema mzee Hamadi.

    “Nifanye nini sasa na hivyo vikapu?”

    “Unatakiwa kuchagua kikapu kimoja, utakachokigusa, mtu mwenye jina lake ndani ya kikapu hicho atakufa muda huohuo,” alisema mzee Hamadi.

    “Unasemaje?”

    “Ndiyo hivyo. Sogea mbele, kuna mwanga utatokea na vikapu hivyo kuonekana mbele yako. Chaguakimoja tu, kisha mlango utajifungua,” alisema mzee Hamadi.

    “Kwa nini yote yanatokea?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ni kwa sababu huwezi kumuona Lusifa pasipo kutoa sadaka ya damu,” alisema mzee Hamadi.

    Mzee Hamisi hakuwa na jinsi, kama ni maji, tayari aliyavulia nguo na wakati huo alitakiwa kuyaoga, alichokifanya ni kuanza kupiga hatua kwenda mbele, alipofika karibu na mlango ule, vikapu vitatu vikaonekana mbele yake na ndani vilikuwa na majina ya watu watatu ambao alikuwa akiwapenda sana.

    Hakujua ni kikapu gani kilikuwa na jina gani, alichotakiwa ni kuchagua tu kikapu pasipo kujua ndani kulikuwa na jina gani. Mapigo yake ya moyo yakaanza kudunda, alikuwa kwenye mtihani mgumu mno.

    Watu wote watatu ambao alitajiwa alikuwa akiwapenda mno, ila hakuwa na jinsi kwa wakati huo, alitakiwa kuchagua kapu moja na mtu mmoja kufariki dunia, hivyo alitakiwa kufanya hivyo ili geti lifunguke.

    Akakishika kikapu kimoja ambacho hakujua kulikuwa na jina gani, ghafla akahisi akianza kububujikwa na machozi ya uchungu, alipochungulia ndani, akakutana na jina la mama yake. Akajikuta akipiga magoti na kuanza kukipiga kifua chake kwa maumivu makali.

    “Uwiiiiiiiiiiii.....” alijikuta akianza kulia kwa sauti kubwa.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog