Search This Blog

TAFADHALI MAMA USIWAUE WATOTO WANGU - 3

 







    Simulizi : Tafadhali Mama Usiwaue Watoto Wangu

    Sehemu Ya Tatu (3)



    Ilikuwa ni saa kumi na mbili kasorobo na hapakuwa na mtu yeyote aliyekuwa ameingia ndani ya nyumba ya Anne asubuhi ile, alichofanya baada ya kuzinduka ni kukiokota kisu chake kilichokuwa pembeni na kujikongoja taratibu kuingia ndani ambako alizunguka akamtafuta bibi kizee yule lakini hakumuona mahali popote! Alishindwa kuelewa mahali alipokuwa lakini alihisi ni lazima aliondoka kichawi.

    Alipoingia katika chumba alicholala mama yake aliikuta maiti ikiwa imelala sakafuni ikiwa imezungukwa na damu nyingi iliyoganda, huruma ilimshika Anne! Alikuwa amemuua mama yake aliyemzaa.

    “Shauri yake si alinianza mwenyewe, kanitesa sana!” Alisema Anne kwa hasira huku akilia alijua wazi alilolifanya lilikuwa kosa.

    “Sikuwa tayari Nancy na Patrick wafe halafu mama aendelee kuishi! Ni heri mimi niendelee kuteseka na hii damu mpaka mwisho wa maisha yangu lakini mama afe na sijutii nilichokifanya!” Aliendelea kusema peke yake Anne.

    Ghafla kumbukumbu za tangu utoto wake zilimwijia, alikumbuka jinsi mama yake alivyompenda, alishindwa kuelewa ni kitu gani kilitokea kiasi cha kumfanya mama yake ampe mateso makubwa kiasi kile!Yaliyompata shuleni yalimuumiza zaidi moyo wake, alipokumbuka kifo cha Dio mvulana wa kwanza kumpenda hasira yake ilizidi kumpanda zaidi.

    “Kwa kweli aliyonifanyia mama ulistahili kifo! Hakuna mtu angeweza” Alipaza sauti Anne.

    Alitoka chumbani na kwenda moja kwa moja hadi chumba alicholala bibi kizee mwingine aliyemuua, hakuamini alipokuta maiti ya bibi kizee aliyemuua haipo! Alishindwa kuelewa ilikuwa wapi na ghafla alisikia sauti ikitoka darini lakini hakumuona mtu aliyekuwa akiongea, ilikuwa sauti nzito na ya kutisha.

    “Tunakuachia mzoga wa mama yako sisi tunaondoka zetu! Usingeweza kutuua kwani sisi si damu yako!”

    Baada ya sauti hiyo Anne alishuhudia kimbunga kikubwa kikiitingisha nyumba yake na paa la juu ya chumba alichokuwa amesimama liliezuliwa mabati kama matano yakatupwa pembeni Anne akauona mwanga kutoka nje.

    “Bahati yao!” Anne alitamka akijua bibi vizee wengine walikuwa wameondoka kichawi.

    Anne alikuwa amebaki na maiti ya mama yake, alianza kufikiria ni kitu gani angefanya na maiti hiyo na alikuwa na uhakika kabisa hapakuwa na mtu yeyote aliyefahamu nini kilichotokea ndani ya nyumba yake na hakutaka mtu yeyote aelewe.

    Alijua wazi kuwa hakuna mtu angekuwa kumsaidia kuzika mwili wa mama yake na alijua ni lazima watu wangehoji kilichomuua, akili ilimzunguka kichwani kwani hakutaka kubaki na maiti ndani kama ilivyotokea kwa watoto wake.

    “Nafunga mlango na ninatoka kwenda kwa mchungaji Aaron kuwanyonyesha watoto wangu, simwambii mtu yeyote juu ya jambo hili, nikirudi usiku nitaibeba maiti kwenda kuitupa barabarani halafu nitatangaza mama yangu amepotea!” aliwaza Anne.

    Alichofanya baada ya mawazo hayo ni kuingia ndani ya nyumba yake na kuvaa nguo safi, akachukua taulo nyingine nzito akaikunja na kuvaa katikati ya miguu yake ili kuzuia damu iliyokuwa ikitoka isimchafue zaidi.

    **********

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ali funga mlango wa nyumba yake na kuondoka taratibu kwenda nyumbani kwa mchungaji Aaron kunyonyesha watoto wake ndani ya moyo wake alijawa na huzuni, moyo wake ulikuwa mzito kupita kiasi kwa sababu ulibeba siri kubwa ya mauaji.

    Pamoja na kuua na maiti kuwa ndani Anne alikuwa ameamua kuonyesha ushujaa, hakutaka kuonyesha dalili yoyote juu ya mauaji aliyoyafanya.

    “Anne, una matatizo gani leo?” Mke wa mchungaji alimuuliza Anne baada ya kugundua tofauti katika tabia yake.

    “Hapana mama mchungaji najisikia kichwa kinauma sana, nafikiri ni sababu ya mawazo!”

    “Mh! Lakini nahisi kuna tatizo linalokusumbua!”

    “Hapana mama na lingekuwepo lazima ningekueleza!”

    Muda wote akiwanyonyesha watoto wake mawazo yake yalikuwa chumbani ilipolala maiti ya mama yake ni hicho ndicho kilifanya mke wa mchungaji agundue! Alipomaliza kuwanyonyesha watoto aliwakabidhi kwa mama mchungaji akawabusu usoni na kuaga kurudi nyumbani kwake.

    Njiani wazo jipya lilimwijia, hakuelewa wazo hilo lilianzia wapi, ghafla alijikuta akitamani kupita nyumbani kwa Delila ili aonane na Huggins! Aliogopa kwenda alipoyakumbuka mambo aliyofanyiwa na Huggins mara ya mwisho, kwa sababu moyoni mwake bado alijisikia kumpenda Huggins alijipa moyo na kuamua kupita tena ingawa moyo wake ulijaa hofu.

    Alijipa moyo na kuanza kutembea kuelekea nyumbani kwa Delila lakini alipokaribia akiwa umbali kama wa mita mia moja na hamsini alishangazwa na umati wa watu uliokuwepo, kulikuwa na magari mengi sana yaliyoegeshwa mbele ya nyumba ya Delila!

    Alipoangalia vizuri alilitambua gari la baba yake na Huggins! Moyo uliruka ghafla na ghafla aliona wanawake wengi wakijishughulisha na kusomba maji huku wengine wakipasua kuni.

    Anne alishindwa kuelewa kilichokuwa kimetokea nyumbani kwa Delila mpaka kuwa na idadi kubwa kiasi kile ya watu, wazo lililomwijia kwanza kichwani mwake lilikuwa ni harusi! Alihisi uwezekano wa Huggins kufunga ndoa na Delila kama njia ya kumkomoa na kumuumiza moyo.

    Alijaribu kusikiliza sauti ya muziki ambayo aliamini ingekuwa ishara ya harusi hakusikia lakini alipotulia zaidi alisikia sauti ya vilio vya watu! Moyo wake ulishituka ikabidi asogee karibu zaidi.

    Aliposimama katikati ya uwanja wa nyumba ya Delila kilio kiliongezeka, watu walizidi kulia kuliko hata mwanzo, maneno yenye kumuumiza yalitamkwa katikati ya vilio vya akina mama na alilisikia jina lake likitajwa akilalamikiwa kusababisha kifo cha Huggins.

    “Bila Anne kuwaua watoto wake Huggins asingeondoka nyumbani kwake kuja kwa huyu malaya na hivyo asingekufa!”

    Maneno hayo yalizidi kumchanganya akili Anne na alishindwa kuamini kama Huggins alikuwa amekufa! Afe vipi wakati alionekana mzima siku aliyomkimbiza na kumkata panga!

    “Haiwezekani! Huggins haweza kufa” alisema Anne akitembea kuelekea jikoni walikokuwa akina mama wengi alipowakaribia alishangaa kuona wanawake wote wakianza kusambaa na wengine kumkimbia, Anne alijisikia vibaya.

    Anne alikumbuka kilichokuwa kikiendelea watu waliogopa kuongea naye sababu ya vitu viwili, cha kwanza ni amri iliyotolewa na uongozi wa mtaa lakini cha pili kilikuwa ni mkosi aliomwagiwa na mama yake dirishani mara tu baada ya mazishi ya watoto wake!

    Alijaribu kuwasogelea akinamama lakini walizidi kumkimbia, kabla hajaondoka eneo hilo vijana watatu walimfuata wakamkatama na kuanza kumvuta kwa nguvu kumwondoa nyumbani pale.

    “Jamani mnieleze tu kimetokea nini?”

    “Mumeo Huggins amekufa!”

    “Haiwezekani amekufa vipi mume wangu wakati alikuwa mzima?”

    “Amenyweshwa sumu na Delila inaaminika alikuwa akimpa dawa ya mapenzi, hakujua kumbe ilikuwa sumu hivi sasa Delila ametoroka!”

    “Sasa kwanini mnanitoa kwenye msiba wa mume wangu?”

    “Haiwezekani wazee wamesema hawataki kukuona msibani sababu wewe ni mchawi!” Vijana wale walipomfikisha barabarani tu walimwacha na kuondoka zao kurudi nyumbani kwa Delila

    Anne alilala barabarani akilia alikuwa akimlilia Huggins, alimpenda na aliamini ni matatizo yake Anne ndiyo yaliyochangia sana kifo cha mumewe, alimlaumu mama yake kwa kila kitu.

    “Tena afadhali nimemuua !” alisema Anne huku akisimama, machozi yalikuwa yakimmwagika mfululizo.

    ****

    Muda mfupi baadaye akiwa amesimama barabarani alishuhudia sanduku likibebwa na kuingizwa katika moja ya magari, watu wengi walipanda kwenye magari na msafara mrefu ulianza kuondoka nyumbani kwa Delila.

    Ilivyoonekana ndugu wa Huggins walikwenda nyumbani kwa Delila kuichukua maiti ya Huggins kuirudisha nyumbani kwa baba yake kwa ajili ya mazishi!

    Gari lenye jeneza lilipopita karibu yake Anne alianza kulikimbilia jambo hilo lilionyesha ni kiasi gani Anne alimpenda mumewe pamoja na kutengana! Baadhi ya akina mama ndani ya gari walimuonea huruma na kumwomba dereva asimamishe gari ili Anne apande lakini dereva alikataa na kuendelea na safari, Anne aliendelea kulifukuza gari hilo bila kuchoka.

    “Hivi huyu dada ni kichaa?” Aliuliza mmoja wa wanawake aliyekuwa ndani ya moja ya magari.

    “Kichaa? Hapana huyu ni mke wa marehemu!”

    “Sasa ni kwanini hapandi kwenye gari badala yake anakimbia kwa miguu?”

    “ Ametengwa na kijiji baada ya kuua watoto wake wawili na ni yeye anayedaiwa kusababisha Huggins afe, wazazi wa marehemu hawataki hata kumwona kwenye mazishi!”

    Mbele zaidi Anne alichoka na kuanguka chini, magari yalipita yakimwacha amelala chini, hakuna aliyeonyesha kumjali baadaye alinyanyuka na kuanza kutembea taratibu kuelekea nyumbani kwao na Huggins, alipania kuhudhuria mazishi ingawa alijua asingeruhusiwa.

    Alipofika nyumbani kwao na Huggins alishangaa kukuta hakuna gari hata moja, ikabidi awaulize watu waliokuwepo na kuambiwa mwili wa Huggins ulisafirishwa kwenda Musoma kwa mazishi, Anne aliishiwa nguvu na kukaa chini na kuendelea kulia, hakuliona kosa lake mpaka azuiliwe kuuona mwili wa marehemu mume wake mara ya mwisho!Kwa mara nyingine tena alimlaumua marehemu mama yake.

    ****

    Alifika nyumbani kwake saa nne ya usiku akiwa na wazo moja tu la kuuchukua mwili wa marehemu mama yake na kwenda kuutupa njia panda ili kupoteza ushahidi kuwa ni yeye aliyefanya mauaji!



    Ilikuwa ni siku ya Februari 14, Siku ya Wapendano au Valentine Day kama ilivyojulikana na watu wengi, siku ambayo kabla ya Anne na Huggins kuingia katika migogoro yao ya ndoa, walisherehekea kushinda hata walivyofanya kwa Sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya.

    Ni siku waliyoonyeshana upendo mkubwa sana kati yao, walikwenda sehemu ambayo hawakuwahi kufika kabla na kula chakula pamoja, kucheza muziki na walipigana mabusu mbele ya watoto wao, ilikuwa ni siku nzuri na ya furaha kwa familia yao.

    Valentine ya siku hiyo ilikuwa tofauti sana na miaka ya nyuma, Huggins hakuwepo tena na si kuwepo nyumbani tu bali alikuwa amekufa, watoto wake wawili Frank na William nao pia walikuwa kaburini na Patrick na Nancy watoto wake waliobaki aliwahifadhi kwa mchungaji Aaron ili kuwaepusha na nguvu za kichawi.

    Anne alikuwa peke yake ndani ya nyumba kubwa ambayo awali aliishi na familia yake yenye furaha, ukubwa wa nyumba yake ndiyo uliifanya itishe zaidi na ilikuwa kimya, alitamani hali ingekuwa tofauti.

    Alikuwa amekaa mbele ya maiti ya mama yake mzazi akilia machozi, maisha yake yalikuwa yamebadilika tena na kumrudisha alikotokea, kwenye maumivu na mateso makali ya maisha, yote hayo kwa sababu ya mama yake.

    Anne alimlaumu mama yake aliyekuwa amemuua kwa mkono wake mwenyewe kwa yote yaliyotokea, kila alipoiona maiti ya mama yake mbele yake hasira ilizidi kuongezeka, alitamani achukue tena kisu achome mama yake ingawa tayari alishakufa, alihisi akili yake haikuwa sawa, alihisi kuchanganyikiwa na kuwa mwehu!

    “Ni lazima nitoe hii maiti hapa ndani nikaitupe barabarani, baadaye nitoe taarifa polisi nikijifanya mama yangu amepotea, polisi wakimtafuta lazima wataikuta maiti yake imetupwa hapo kila mtu ataamini mama ameuawa na majambazi!” Alisema Anne moyoni mwake.

    Moyoni mwake aliogopa na alihisi kutetemeka mwili lakini pamoja na hali hiyo hakuwa na la kufanya ili kujiepushia matatizo ilikuwa ni lazima aiondoe maiti ya mama yake ndani.

    “Vinginevyo kama ikikutwa humu ndani mambo yataniharibikia!” Aliwaza Anna.

    Alipoangalia saa yake ya ukutani ilimwonyesha tayari ilikuwa saa tano kasoro dakika kumi na sita! Anne alinyanyuka na kutembea kinyonge hadi chumbani kwake ambako aliwasha taa na kuchukua suruali na koti jeusi lililotumiwa na marehemu mume wake, Huggins na kuvaa wakati akitoka chumbani alipitia kofia kubwa nyeusi iliyokuwa ukutani nayo pia akaivaa, alisimama mbele ya kioo na kugundua ni kiasi gani alikuwa amebadilika.

    “I’m going for the last mission!”(ninakwenda kwa shughuli ya mwisho) Alijisemea mwenyewe moyoni mwake.

    Alinyoosha moja kwa moja hadi chumbani ilikokuwa maiti ya mama yake mama yake alikuwa mnene sana na Anne alijua maiti yake ingekuwa nzito lakini hakuhitaji msaada wa mtu mwingine, alijipa moyo na bila kujua zilikotokea nguvu nyingi mwilini mwake aliunyanyua mwili wa mama yake na kuuweka begani, akatoka nao nje ya nyumba yake ambako aliuweka chini na kukimbia nje kuangalia usalama kwani hakutaka mtu yeyote hasa majirani waigundue kazi aliyokuwa akiifanya usiku huo.

    Alipohakikisha hapakuwa na mtu yeyote akipita Anne alirudi mbio hadi uwani ambako aliubeba mwili wa mama yake begani kwa mara nyingine na kuanza kutoka nao nje, ambako aliingia katikati ya migomba na kuanza kutembea kuelekea darajani, hakutaka kutumia barabara kwa kuhofia angeweza kukutana na watu ambao wangetaka kujua nini alichobeba.

    Usiku ulikuwa wa giza nene na manyunyu ya mvua yaliendelea kudondoka taratibu, siku hiyo ya Valentine ilionekana ya kutisha sana lakini Anne hakuogopa alikuwa ameamua kutimiza kazi yake kikamilifu.

    Kutoka nyumbani kwake hadi darajani ulikuwa umbali wa mita kama mia tatu hivi, ulikuwa ni umbali mrefu sana kwa uzito wa mzigo ambao Anne alikuwa nao begani kwake ukizingatia alikuwa msichana, kwa mara mbili mfululizo alilazimika kuishusha chini maiti ya mama yake alipolemewa sana na uzito.

    Ghafla alishtukia radi ya ajabu ikianza kupiga katikati ya migomba, mwanga mkali ulionekana kila sehemu aliyopita, alijua ni nini kilitaka kutokea! Ni wazi ulikuwa uchawi wa mzimu wa Lutego, Anne aliogopa sana na kujikuta akishindwa kuendelea na safari yake na kuitupa maiti ya mama yake chini.

    Alianza kukimbia haraka kurudi alikotokea sauti nene na nzito ilimfuata nyuma yake, ilikuwa ni kama sauti ya binadamu lakini hakuwa binadamu wa kawaida!

    “Umemuua Malkia wetu ni lazima na wewe ufe, tena kifo cha mateso!” Iliendelea kusema sauti hiyo na kumtisha zaidi Anne.

    Radi ilizidi kupiga na muungurumo uliongezeka ghafla mvua kubwa tena ya mawe iliyoambatana na upepo ilianza kunyesha, Anne alishindwa kuelewa mvua ile ilitokea wapi kwa sababu hapakuwa na mawingu mazito na makubwa jioni ya siku hiyo, hakuwa na uhakika wa kufika salama nyumbani kwake.

    “Ni heri mniue mimi niliyewakosea kuliko kuwaua watoto wangu wasio na hatia!” Alipiga kelele Anne huku akikimbia katikati ya migomba, mawazo yake yote yakiwa kwa watoto wake, alijua ni lazima naye angekufa kabla ya kufika nyumbani, alijua yote yaliyokuwa yakitokea yalifanywa na bibi vizee waliotoroka mauaji yake.



    ****

    Gongo ilikuwa ni pombe haramu na ilipigwa vita kila siku iliyokwenda kwa Mungu, lakini pamoja na vita hiyo bado watu waliendelea kuitumia, ilionekana kama hapakuwa na njia yoyote ya kuwafanya wananchi wasinywe pombe hiyo.

    Bernard au Bernie Killer kama alivyojulikana na wengi maeneo ya Isamilo mjini Mwanza alikuwa ndiye mpikaji maarufu wa pombe hiyo na alishafungwa mara mbili mfululizo kwa kosa la kujishughulisha na pombe haramu ya gongo lakini hata alipotoka gerezani hakukoma, bado aliendelea kupika gongo kazi iliyomfanya aishi na hata kusomesha watoto wake!

    Alifanya kazi hiyo usiku wa manane wakati watu wote wamelala, alifanya hivyo ili kujiepusha na maaskari na alifanyia katikati ya migomba, alifanya kazi hiyo yeye na mke wake pamoja na vijana wengine wanne waliowaajiri.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Usiku wa siku hiyo ya Valentine, Bernard na mke wake pamoja na wafanyakazi wao walikuwa katikati ya migomba wakiendelea na kazi ya kupika gongo, walishangaa kuona mtu aliyevaa nguo nyeusi akitokea upande wa kulia katikati ya migomba! Wote walishtuka na kufikiri labda ni polisi waliokuwa katika msako wa wapika gongo, waliingiwa na hofu na kulala chini pembeni ya mtambo wao.

    Mtu huyo alionekana amebeba kitu mabegani kwake na alipita eneo walilokuwa bila kufanikiwa kuwaona, mbele aliutupa mzigo huo chini na kuanza kukimbia kurudi alikotoka na hapo hapo mvua kubwa ilianza kunyesha na radi ilitanda kila mahali, hali ilibadilika ghafla.

    “Sijui ametupa nini?”Bernard alimwambia mke wake.

    “Hata mimi sijui, isije kuwa ni pesa?”

    “Acha nikaangalie, vijana twendeni lisije kuwa bomu halafu linilipukie peke yangu!” Alisema Bernard huku akiwaita vibarua wake na wote waliongozana kwenda mahali ulipotupwa mzigo ule.

    “Mh! Huyu siyo mtu kweli?” Alisema Bernard!

    “Tumfunue mzee!”

    “Mfunueni!” Bernad aliwaruhusu vijana wake na kweli walifunua mwili ule na Bernard akaumulika kwa tochi.

    “Masikini huyu si ni mama yake na yule jirani yetu Anne, tena alikuja juzi tu kuhani msiba wake kimempata nini?” Alisema Bernard kwa sauti ya chinichini!

    “Ni yeye kweli au umemfananisha!”

    “Ni yeye namfahamu vizuri sana huyu mama ni mama mkwe wake na marehemu Huggins aliyefariki jana!”

    “Sasa tufanye nini?”

    “Hata mimi sijui ila najaribu kufikiria ni nani aliyemtupa hapa?” Alizidi kuuliza Bernard na baadaye kuanza kumulika pembeni ni huko ndiko alikokiona kiatu kimoja!

    “Mh! Hiki kiatu mbona ni cha Anne? Ina maana Anne ndiye ametupa maiti ya mama yake hapa, haiwezekani hii ni njama ya kumwigiza matatani binti wa watu, hebu tufungashe vifaa vyetu tuondoke eneo hili tayari limekwishaingiwa na gundu polisi wanaweza kufika hapa wakati wowote!”

    Walianza kufungua mitambo yao na kuifunga tayari kwa kuondoka kila mmoja wao alikuwa na hofu, lilikuwa tukio la kwanza katika historia ya kazi yao ya kupika gongo waliyoifanya kwa miaka kumi na tano.

    Kabla hawajaanza kuondoka eneo hilo walishtukia mtu akitokea katikati ya migomba huku akinyata, mtu huyo alikuwa na tochi yenye mwanga mkali mkononi mwake na alimulika kila mahali kuzunguka eneo ilipolala maiti.

    “Huyu si ndiye aliyekimbia au?” Alionong’ona Bernard akiongea na mmoja wa wafanyakazi wake.

    “Ni yeye alivaa nguo nyeusi hivihivi!”

    “Hebu tulieni mimi nimchunguze vizuri ni nani hasa?” Alisema Bernard na kuweka mizigo yake chini, akaanza kutembea kwa tumbo kuelekea nyuma ya mahali ilipolala maiti.

    “Masikini sijui kile kiatu kipo wapi jamani, kitaniponza ni lazima watajua ni mimi ndiye nimemuua mama!” Alisikika akisema mtu huyo, Bernard aliitambua sauti ile, haikuwa sauti ngeni masikioni mwake ingawa hakuweza kuitambua mara moja ni ya nani.

    “Hiki hapa!! Yes, afadhali, kisingepatikana ningefanya nini mie?” Sauti ile ilimfikia tena Bernard na kumpa jibu la uhakika, ilikuwa ni sauti ya Anne asilimia mia moja.

    Bila kugundua kuwa palikuwa na mtu akimchunguza Anne alianza kutimua mbio kwa kutumia tochi yake na kutokomea katikati ya migomba na kupotea.

    “Ni Anne amemuua mama yake!” Alisema Bernard mwili wake ukitetemeka.

    “Nani?” Mkewe aliuliza kwa mshangao.

    “Ni Anne!”

    “Kweli?”

    “Ndiyo na ni lazima suala hili niitaarifu polisi!” Alisema Bernard!

    *****

    Alipofika nyumbani kwake Anne aliingia moja kwa moja hadi ndani na kujitupa kitandani, nguo zake zote zililowa na maji lakini hakujali, alianguka hivyo hivyo na kuyalowanisha mashuka yote alikuwa amechoka kupita kiasi, kazi aliyokuwa amefanya ilikuwa ngumu sana.

    Aliendelea kuwa na uhakika hapakuwa mtu aliyemwona akitimiza azma yake, aliamini zoezi zima lilikuwa limekwenda kama alivyopanga! Kilichokuwa kimebaki mbele yake wakati huo ni kwenda kituo cha polisi na kutoa taarifa juu ya kupotea kwa mama yake mzazi.

    Hakutaka kupoteza muda zaidi, bila kuchelewa ingawa ilikuwa ni usiku wa manane alitoka na kuanza kutembea akielekea kituo cha polisi, Anne hakuogopa kitu kwani ilikuwa ni lazima atoe taarifa polisi ili kuficha ukweli wa tukio zima.

    Alipofika kituoni kabla hajaingia ndani, mlangoni alikutana na Bernard aliyeshuhudia Anne akilia na machozi.

    “Vipi jirani?”Bernard aliuliza.

    “Mama yangu amepotea tangu jana na nimemtafuta bila mafanikio au umemwona mahali?”

    “Hapana sijamwona, pole sana kwa hiyo umekuja kutoa taarifa siyo?” Alisema Bernard ingawa alifahamu kila kitu na alishatoa taarifa polisi!

    “Ndiyo!”

    “Sawa basi mimi naondoka polisi watakusaidia!”

    Alipoingia ndani kabla hajasema kitu chochote Anne alishtukia anapigwa pingu mikononi.

    “Vipi jamani mbona mnanifunga pingu?”

    “Muuaji mkubwa wee!”

    “Nimemuua nani?”

    “Umemuua mama yako halafu unajifanya mjanja!” Alisema Askari na kumpiga Anne kwa rungu kichwani damu ilianza kumtoka.

    “Mimi nimemuua mama yangu kwa makosa gani?”

    Alizidi kujitetea Anne lakini hakuna mtu aliyemsikiliza.

    “Mpakieni ndani ya gari mwende naye nyumbani kwake mkapekue haraka!” Mkuu wa kituo aliamuru na Anne alianza kuvutwa na kutupwa ndani ya gari, Anne alishindwa kuelewa ni nani aliiitoa taarifa hiyo polisi, aliamini kwa hali ilivyokuwa ndani ya nyumba yake hapakuwa na jinsi ya kujitetea juu ya mauaji ya mama yake kwani damu zilikuwa bado zimo vyumbani na alishindwa kuelewa ni maelezo gani angeyatoa juu ya damu hizo, ili aaminike kuwa hakumuua mtu.

    “Sijui niseme nilichinja kuku! Lakini pia hawataamini!” aliwaza Anne.

    Walipofika nyumbani kwake waliingia moja kwa moja hadi ndani na kuanza kupekua nyumba nzima, wote hawakuamini walipopambana na damu iliyogandamana sakafuni katika baadhi ya vyumba vya nyumba yake.

    “Hii damu ni ya nini?”

    “Kuku!”

    “Kuku? Unatufanya sisi watoto, hebu sema ukweli!”

    Alisema mmoja wa maaskari na kuanza kumshushia mvua ya virungu Anne kichwani mpaka akaanguka chini na kupoteza fahamu, alipozinduka damu nyingi zilikuwa zikimtoka mwili na baadaye aliendelea kupewa mateso makali sana ili aeleze ukweli.



    Anne alikuwa chini akiwa amepoteza fahamu kwa kipigo alichokipata lakini hakuna mtu aliyekuwa na muda wa kuchukua maji na kummwagia ili azinduke, polisi walimchukua hivyohivyo na kwa harakaharaka walimpakia ndani ya gari lao akiwa na pingu zake mkononi kwenda naye kituoni, walishakuwa na uhakika asilimia mia moja kuwa Anne ndiye alimuua mama yake mzazi na kwenda kumtupa porini.

    Alipofikishwa kituoni alipelekwa moja kwa moja hadi mahabusu ambako lango lilifunguliwa na kutupwa ndani na kuwaangukia mahabusu wengine waliokuwemo ndani.

    Alilala chini akiwa hajitambui lakini kwa ubaridi uliokuwepo sakafuni uliotokana na mikojo ya mahabusu Anne alirejewa na fahamu zake saa sita ya usiku na kujikuta yupo kwenye chumba kidogo chenye giza! Aliangalia huku na kule ndani ya chumba hicho na kushindwa kuelewa mahali alipokuwa.

    Alihisi yupo katikati ya watu na aliposikiliza vizuri alisikia watu wakihema na kukoroma pembeni yake, alizidi kuingiwa na hofu na kuchanganyikiwa alishindwa kuelewa ni mahali gani alipokuwa, moyo wake ulizidi kwenda mbio, hakuwa na kumbukumbu juu ya tukio lolote lililotokea mpaka kumfanya awe pale.

    Alipojigusa usoni juu ya jicho lake la kulia mkono wake ulikutana na uvimbe mkubwa! Ghafla kumbukumbu zilimiminika kichwani mwake juu ya kipigo kibaya alichokipata kutoka kwa polisi na pia aliyakumbuka mauaji ya mama yake aliyoyafanya siku hiyo.

    “Hivi hapa nipo wapi hasa? Au Nipo mochwari nini? Labda polisi walifikiri nimekufa wakaniweka chumba cha maiti?” Aliwaza Anne lakini sauti za watu wakikoroma zilimfanya aelewe mahali pale hapakuwa kama alivyopafikiria!

    Alipata nguvu na kunyanyuka akaanza kujikongoja kutembea mahali kulikoonekana kuwa na mwanga kidogo, alihisi kuwakanyaga watu waliolala sakafuni, alitembea hadi getini, ambako alimkuta mwanamke mmoja amesimama wima akiimba wimbo wa dini ulioonekana kuwa pambio.

    “Dada shikamoo!”

    “Marahaba mdogo wangu hujambo?”

    “Sijambo! Hivi hapa ni wapi?” Anne aliuliza.

    “Mdogo wangu hapa hupafahamu?”

    “Ndiyo dada!”

    “Hapa ni mahabusu!”

    “Dada nimeletwa hapa saa ngapi?”

    “Usiku lakini umefanya nini mdogo wangu?”

    “Sijafanya kitu dada wananionea!”

    “Hapana haiwezekani ukaletwa hapa hivihivi!”

    “Kwani wewe imekuwaje mpaka ukaingia humu?”

    “Nimeua watoto wangu mwenyewe!”

    “Umeua watoto wako? Kwanini?”

    “Kwa bahati mbaya nilikuwa napika mboga jikoni wakati huohuo nikawa napaka dawa ya kunguni kwenye magodoro sijui ile dawa iliingia vipi katika mboga watoto wangu watatu walipokula wote wakafa, ikagundulika ni sumu ndiyo iliwaua nikakamatwa ndiyo maana nipo hapa! Sasa niambie na wewe kitu gani kimekupata mdogo wangu?”

    “Dada ni siri nakueleza wewe tu, kwa kweli nimemuua mama yangu mzazi!”

    “Mdogo wangu kimetokea nini mpaka ukafikia hatua hiyo? Nini kilikuudhi?”

    “Mama yangu alinitesa sana tena kwa muda mrefu, aliwaua watoto wangu wawili, alisababisha kifo cha mume wangu na bado alitaka kuwaua watoto wangu wawili waliobaki! Nilipokataa akanipiga mimi na ugonjwa wa kupatwa na hedhi kila siku, nikawa nanuka na watu wakanitenga, hapakuwa na njia nyingine yoyote ya kumzuia asiendelee kunitesa zaidi ya kumuondoa duniani, sikufichi dada nimeua lakini mahakamani sitakubali jambo hilo, najua nitanyongwa! Kifo cha mama yangu hakinisikitishi hata kidogo mama alistahili kufa, kitu kimoja tu kinanitia huzuni nacho ni watoto wangu nimewaacha wakiwa na miaka miwili tu nani atawalea?” Alimaliza Anne na kuanza kulia.

    “Usilie pole sana mdogo wangu hebu nielezee umemuuaje mama yako?”

    “Anne alieleza kila kitu kilivyotokea, alimchoma mama yake kisu na kwenda kutupa mwili wake porini ambako hakuelewa ni nani alimwona na kutoa taarifa polisi hatimaye akakamatwa, alimweleza pia mateso mengine mengi yaliyompata maishani mwake ambayo yalisababishwa na mama yake.

    “Lakini kesi hiyo unaweza kushinda tena kirahisi kabisa!”

    “Inawezekanaje dada wakati mimi nimeua?”

    “Mimi ni mwanasheria, hakuna ushahidi wa kutosha kukubana!”

    “Mbona damu wameikuta ndani?”

    “Hiyo siyo sababu damu inaweza kuwa ya ng’ombe, mbuzi au hata kunguni!”

    “Nitashinda vipi kesi hii?”

    “Omba Mungu mimi nitoke hapa mahabusu, ndugu wananishughulikia nikitoka naweza kukusaidia bure ili ushinde!”

    “Kweli?”

    “Ndiyo wala usiwe na wasiwasi, hii siyo kesi kabisa, mimi pia nitashinda kwa sababu sikuua kwa kukusudia, nisingeweza kuua watoto wangu mwenyewe niliowapenda!”

    “Unaitwa nani?” Anne alimuuliza dada yule.

    “Mimi naitwa Lydia Ishengoma ni mwanasheria mashuhuri sana hapa mjini, wewe unaitwa nani?”

    “Mimi naitwa Anne nakuomba sana ukitoka hapa kabla yangu nisaidie dada yangu, watoto wangu! Watoto wangu nawapenda sana nimewaacha wadogo mno watateseka!” Anne alianza kulia tena.

    “Usilie binti utatoka tu ingawa inaweza kukuchukua muda mrefu kidogo lakini mwisho ni lazima uwe huru!”

    Waliongea mengi hadi mwanga wa asubuhi ulipoanza kuonekana na baadaye ndugu wengi walianza kuja kufuatilia masuala ya ndugu zao, maaskari waliwaita baadhi ya mahabusu mmoja baada ya mwingine wakawa wanatoka nje na wengine walipelekwa mahakamani, mahabusu wote walitoka wakabaki Anne na Lydia peke yao.

    “Nyie wauaji hamuwezi kutoka kaeni humo ndani msubiri kupelekwa Butimba!” Alisema askari mmoja wa kike.

    Mpaka saa nne asubuhi ilipotimu Anne na Lydia walikuwa bado wako mahabusu, wahalifu wengine zaidi walizidi kuongezwa katika chumba hicho kidogo. Ghafla Anne akiwa katikati ya mawazo alisikia sauti ya watoto wakilia na aliposikiliza vizuri aligundua zilikuwa ni sauti ya watoto wake! Alisimama wima na kuchungulia kaunta, huko aliwaona mchungaji Aaron na mkewe wakiwa wamewabeba Patrick na Nancy mikononi, watoto wakilia kwa sauti ya juu!

    “Jamani watoto wangu! Watoto wangu jamani” Anne alianza kupiga kelele, aliumia kuwaona watoto wake wakilia, alijua asingeishi nao tena maishani mwake alijua ilikuwa ni lazima anyongwe.

    “Kelele!” Askari mmoja aliongea kwa sauti akimuamuru Anne anyamaze.

    “Nawataka watoto wangu jamani, nataka niwaage kwa mara ya mwisho!” Alisema Anne.

    “Umeambiwa unakwenda kufa?” Alijibu askari

    “Ningejua nisingemuua mama, lakini kama nisingemuua ni lazima angewaua watoto wangu, ni heri mimi nikateseka gerezani lakini Patrick na Nancy wawe salama!” Anne aliwaza.

    Alipotupa tena macho yake kaunta aliwashuhudia polisi wakiwasukuma mchungaji Aaron na mkewe kuwatoa nje ya kituo, aliendelea kuwaona watoto wake wakilia na roho ilimuuma sana! Aliwahurumia watoto wake na alijua kwa yeye kupelekwa gerezani wangeishi kama yatima duniani kwa sababu baba yao alikuwa amekufa!

    *****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Muda mfupi baadaye Anne na Lydia walitolewa mahabusu na kuanza kusukumwa kwenda nje ambako gari lilikuwa tayari kuwapeleka gerezani Butimba, alipofika nje Anne alitupa macho kulia kwake na kuwaona mchungaji Aaron na mkewe wakiwa na watoto wake mikononi!

    Alishindwa kuvumilia na kujikuta akitimua mbio kuwafuata akiwa na pingu zake mikononi, askari aliyekuwa akiwalinda alifikiri Anne anatoroka, bila kuchelewa alilenga bunduki yake tayari kumfyatulia risasi, lakini kabla hajaachia hata risasi moja alimwona Anne akisimama mbele ya watu wawili wenye watoto.

    “Nisogezeeni watoto wangu niwabusu!” Anne alisema kwa sauti kubwa iliyomfikia askari aliyenyosha bundiki yake kwa lengo la kumpiga Anne.

    “Ana bahati vinginevyo ningemmalizia mbali!” Alisema askari huyo aliyeonekana si mwepesi kutumia bunduki.

    Watoto walisogezwa karibu yake na Anne alianza kuwamwagia mabusu kibao usoni kwao.

    “Watoto wangu Patrick na Nancy bakini salama nawapenda na nimemuua bibi yenu kwa sababu ya kuwalinda nyinyi,bibi yenu alitaka kuwaua bila hatia!” Alisema Anne na kuwafanya mchungaji na mke wake ambao hawakuwa na habari juu ya mauaji aliyoyafanya washangae.

    “Anne umemuua mama yako?” Mchungaji Aaron aliuliza kabla Anne hajajibu swali hilo maaskari walimvamia na kuanza kumpiga kwa virungu kichwani akaanguka chini tena.

    “Nyanyuka twende muuaji wewe!” Alifoka mmoja wa maaskari.

    “Mchungaji nitunzieni watoto wangu, ninajua sitatoka gerezani leo wala kesho, wafundisheni kumcha Mungu na mara kwa mara waelezeni kuwa mimi mama yao nipo ili wasinisahau, waleteni gerezani mara kwa mara kuniona!” Anne alisema maneno huku virungu vingi vikizidi kumwangukia chini alipolala.

    Baada ya kusema hayo alijikongoja na kunyanyuka ardhini alipoanguka ni kweli aliwatia huruma watu wote waliokuwepo kituoni, uso wake wote ulivimba, na nguo zake zote zilijaa damu, ilikuwa si rahisi hata kidogo kuamini kuwa mwanamke yule alikuwa Anne!

    ****

    Alivutwa na kupelekwa moja kwa moja hadi kwenye gari, ambako alitupwa sehemu ya nyuma na kumkuta wakili Lydia Ishengoma akiwa amekaa!

    “Anne tulia watakuumiza hawa hawana huruma!” Wakili alisema.

    Anne alinyanyuka na kuanza kuwapungia mchungaji na mke wake waliokuwa bado wamesimama mahali alipowaacha wakiwa watoto wakilia mikononi mwao, mlango wa gari kubwa aina ya Scania walilopanda ulifungwa baada ya kuingia askari mwenye bunduki mikononi.

    “Una bahati wewe! Pale nilishaamua kukumiminia risasi kwani nilijua unatoroka, mshukuru Mungu wako!” Askari yule alisema na gari lilianza kuondoka kutoka kituo cha polisi.

    Kutoka mjini Mwanza hadi gereza la Butimba ilikuwa ni mwendo wa kama kilometa kumi na tano lakini iliwachukua muda wa saa nzima kwa sababu ya ubovu wa barabara za Mwanza mjini! Walipofikishwa gerezani wote walishushwa na kuingizwa ndani ya gereza walipekuliwa na kuingizwa chumba maalum cha mahabusu wa mauaji ambako walikaa wawili tu.

    ****

    Miaka miwili tu baada ya kuingia gerezani wakili Lydia Ishengoma aliachiwa kutoka gerezani ilipogundulika hakuua kwa kukusudia, kazi yake ya kwanza kama alivyoahidi alipotoka gerezani ilikuwa ni kumtetea Anne! Akijua shida alizokuwa nazo gerezani hasa tatizo la upungufu wa damu ambalo Anne alilolipata mara kwa mara wakili Lyidia alianzisha harakati za kumtetea Anne mahakamani.

    Siku wakili Lydia aliyoondoka gerezani Anne alilia kama mtu aliyefiwa na ndugu yake kwa sababu hakuwa na rafiki mwingine yeyote zaidi yake, mahabusu wengine wote walimtenga kwa sababu ya harufu aliyotoa kutokana na hedhi ya kila siku, ni wakili Lydia peke yake katika gereza zima aliyemvumilia, alishindwa kuelewa maisha yake yangeendeleaje baada ya hapo, lilikuwa pigo kubwa!

    Huo ndio ukawa mwanzo wa Anne kuingia gerezani, ambako alikaa kwa muda wa miaka kumi akipelekwa mahakamani mara moja kila mwezi ambako kesi yake iliendelea kutajwa na baadaye kuanza kusikilizwa! Alishangaa siku aliyomkuta wakili Lydia amevaa mavazi ya Uwakili akimtetea mahakahami, Anne aliamini ipo siku angekuwa huru.

    Anne aliendelea kusota gerezani, nguo alizokuwa nazo zilichakaa damu ziliendelea kumtoka mfululizo, jambo hilo lilimkera sana, alinuka na inzi wengi walimfuata kila alikokwenda! Hali hiyo ilisababisha mahabusu wenzake wamfukuze katika kila chumba alichopangiwa kulala, mwisho akawa analala barazani kwenye baridi na mbu wengi.

    Yalikuwa ni mateso makali mno, lakini lawama zote hizo alimtupia mama yake mzazi aliyempa ugonjwa huo wa ajabu.

    “Mama alistahili kufa, na sijui ni kwanini alinizaa, inakuwaje mtoto umzae mwenyewe halafu umtese kiasi hiki? Na ninasema siku nikinyongwa huko kuzimu nikimkuta mama ni lazima nimuue tena!” Alilia Anne.

    ****

    Kama alivyowaomba mchungaji Aaron na mke wake walilazimika kuwapeleka Nancy na Patrick gerezani kumwona mama yao kila mwezi, walikuwa ni watoto wazuri waliokuwa na kulelewa katika familia ya Kikristo, walimpenda mama yao pamoja na kuwa alikuwa gerezani. Patrick alifanana sana na marehemu baba yake Huggins lakini Nancy alimfanana Anne kwa kila kitu.

    “Mama usijali ipo siku utatoka tu gerezani, tunakupenda mama, wewe ni mama yetu hata kama ni mfungwa!” Hayo ndiyo yalikuwa maneno ya watoto wake walipotimiza umri wa miaka minane.

    Katika umri huo walikwisha kuwa watoto wakubwa wenye kuyafahamu mema na mabaya, walikwenda mahakamani kila siku ya kesi ya mama yao ilipofika, ni kama walikulia mahakamani wazee wa mahakahama na Mahakimu wote waliwafahamu Patrick na Nancy!





    MIAKA KUMI BAADA YA KUINGIA GEREZANI



    Kesi ilikuwa imepamba moto wakili Lydia Ishegoma alikuwa amedhamiria kumtoa Anne gerezani, kila mara alimtembelea na kufanya naye mahojiano.

    “Haupo ushahidi wa kukufunga Anne!”

    “Lakini niliua mheshimiwa!”

    “Pamoja na hayo lakini nitahakikisha unatoka gerezani kwa sababu uliyofanyiwa na mama yako yalikuwa ya kukulazimisha ufanye ulichokifanya!”

    “Nitashukuru kama nitatoka gerezani naomba ujifahidi sana na Mungu atakusaidia, watoto wangu ndio wanaonifanya nihuzunike sana!”

    “Kwani kwa hivi sasa wanaishi na nani?”

    “Wanaishi na Mchungaji wa kanisa letu, niliwapeleka kwake kabla ya kukamatwa!”

    “Hebu nieleze vizuri, unafikiri kuna mtu yeyote aliyekuona wakati ukiibeba maiti ya mama yako kwenda kuitupa?”

    “Hapana ilikuwa ni usiku mno na watu wengi walikuwa wamelala isitoshe ilikuwepo dalili ya mvua kubwa kunyesha!”

    “Sasa nani aliwaeleza polisi?”

    “Hata mimi nashangaa!”

    “Kuna watu waliofahamu kuwa wewe na mama yako mlikuwa hamuelewani?”

    “Hapa mjini hapana, lakini kijijini kwetu Kome wapo watu wanaoelewa jambo hili!”

    “Je, kuna watu walielewa kuwa mama yako alikuja hapa mjini?”

    “Ndiyo lakini sio wengi!”

    “Baada ya kufanya kitendo hicho ulipiga kelele kuita watu kuwaeleza kuwa mama yako amepotea?”

    “Hapana ila nilikwenda moja kwa moja kituo cha polisi kutoa taarifa”

    “Na huko ndiko ulikamatwa?”

    “Ndiyo!”

    “Unahisi nani anaweza kuwa alitoa taarifa polisi?”

    “Kwa kweli sifahamu na si rahisi kuelewa na nilishangaa polisi walijuaje”

    “Uliushika maiti ya mama yako kwa mikono yako?”

    “Ndiyo, kwani vipi?”

    “Ilipopimwa haikuonyesha alama za vidole!”

    “Labda kwa sababu mvua ilinyesha sana usiku ule!”

    “Anne!” Aliita wakili Lydia.

    “Naam mheshimiwa!”

    “Nitahakikisha unashinda kesi hii!”

    “Nitashindaje mheshimiwa wakati niliua?”

    “Hiyo kazi niachie mimi! Wamepanga siku ya hukumu iwe Januari 21, leo ni tarehe ngapi?”

    “Ni tarehe 15, bado wiki moja tu ninyongwe! Dada Lydia utanisaidia kuwalea watoto wangu?”

    “Anne nimekuambia huwezi kunyongwa, kwani hakuna ushahidi wa kutosha kukutia hatiani, mtu mwingine yeyote angeweza kumuua mama yako na kwenda kumtupa porini!”

    ****

    Sifa ya Anne kuwa mwanamke muuaji ilisambaa kwa kasi mjini Mwanza na vitongoji vyake, kwa kitendo cha kumuua mama yake mzazi aliyemleta duniani Anne alionekana ni mwanamke mwenye roho mbaya pengine kuliko binadamu wote! Alilaaniwa na kila mtu na watu wote walitamani ahukumiwe kifo na kunyongwa!

    Ni kweli Anne aliua hata yeye hilo alilikubali lakini hakuwa na mtu hata mmoja aliyeufahamu ukweli ni kwanini alifikia uamuzi wa kumuua mama yake aliyemzaa. Alitamani kuueleza ukweli Ulimwengu mzima ili asafishe jina lake lakini hakuwa na nafasi ya kuongea na watu wote! Mtu pekee aliyeufahamu ukweli alikuwa ni wakili wake.

    Siku ya Januari 21, 1998 mamia ya watu walifurika mahakama kuu ya Mjini Mwanza kuisikiliza kesi ya Anne, alipoteremshwa tu kutoka katika gari lililombeba kutoka gerezani Butimba akiwa na mahabusu wengine, watu waliokuwa nje ya mahakama walianza kunong’onezana na wengine kusema kwa sauti bila hata uoga kuwa Anne alistahili kifo.

    “Mnyongeni tu! Hafai kuishi huyu kwanini amuue mama yake kinyama kiasi kile?” Alisema mama mmoja wakati Anne akipitishwa, maaskari waliokuwa wakimlinda walicheka lakini maneno yale yalimuumiza sana moyo Anne na kumfanya atokwe na machozi, alimhurumia mama yule kwa sababu hakuujua ukweli.

    Alitembea kwa shida akiwa amefungwa pingu mikononi na miguuni, nguo zake zilikuwa chafu kupita kiasi na mwili wake ulijaa ukurutu na ulikuwa mweusi kwa sababu ya kutokuoga, alionekana muuaji kuliko wauaji wengine wote waliotangulia.

    Anne alitupa macho yake pembeni na kuwaona watoto wawili wakilia huku wakijaribu kujitoa mikononi mwa mwanamke aliyewashikilia, Anne alipomwangalia mwanamke huyo alimkumbuka, alikuwa ni mdogo wake yaani mtoto wa baba yake mdogo, Suzzane na alipotupa macho yake kuwaangalia watoto hao aliwatambua, walikuwa ni Nancy na Patrick watoto wake.

    “Watoto wangu! Watoto wangu! Wale pale!” alipiga kelele Anne huku akijaribu kugeuka na kuanza kutembea kuelekea mahali walipokuwa Patrick na Nancy watoto wake mapacha waliobaki, waliosababisha amuue mama yake mzazi ili kuokoa maisha yao.

    “Mama! Mama! Mama! ninakupenda mama, pole mama!” Alisema Patrick.

    “Niachie! Niachie! Niachie niende kwa mama yangu!” Alilia Nancy huku akimuuma mama yake mdogo mkono ili amwachie lakini aliendelea kumshikilia kwa nguvu asimponyoke.

    Anne aliumia sana moyoni mwake kushuhudia kitendo kile cha watoto wake, alitamani kuwasogelea watoto wake lakini alishindwa kwani kabla hajasogea umbali mrefu maaskari walimshika na kumbeba juu akatupwa katika mahabusu ndogo iliyokuwepo karibu na mahakama hiyo, ilikuwa ni mahabusu chafu iliyonuka mikojo na kinyesi.

    “Ipo siku mama yangu atakuwa huru na nitamsaidia!” Alisema Patrick.

    Katika maisha yao Nancy na Patrick hawakuwahi kuishi na mama yao, kwani kwa mara ya kwanza alipokamatwa walikuwa na umri wa miaka miwili na mpaka siku hiyo alikuwa amekaa gerezani miaka kumi, tayari walikuwa na umri wa miaka kumi na mbili! Lakini pamoja na kutokuishi na mama yao bado walimpenda na waliamini siku moja angekuwa huru na kurejea tena kwao.

    ****

    Muda wa mahakama kuanza kazi uliwadia na watu walianza kuingia mahakamani na kuchukua viti vyao. Patrick, Nancy na mama yao mdogo nao waliingia na kuketi, wote walikuwa wakilia machozi ya uchungu ni kwa sababu walijua siku hiyo ndiyo ilikuwa siku ya hukumu ya mama yao na lolote lingeweza kutokea, kifo ama maisha.

    Watu wengi walishindwa kuingia mahakamani kwa sababu ya ufinyu wa nafasi iliyokuwepo na kusimama nje ya mahakama na wengine kukaa chini ya miti wakisubiri mahakama ianze. Mawakili wote walikuwa ndani.

    Kesi ya Anne ilipangwa kuwa ya kwanza, Anne alitolewa mahabusu na kuingizwa moja kwa moja hadi mahakamani, alipoingia tu hali ya hewa ndani ya chumba cha mahakama ilibadilika! Inzi waliongezeka na harufu mbaya ilitanda, watu walishindwa kuelewa hali hiyo ilitokana na nini lakini inzi walivyozidi kumfuata Anne wengi walianza kuhisi huenda alikuwa amejisaidia ndani ya nguo zake.

    Jaji Raphael Mpoki aliyekuwa maarufu kwa kuhukumu watu miaka mingi katika historia ya Tanzania tena bila huruma alipoketi kitini minong’ono yote iliyokuwepo ndani ya mahakama ilikwisha na mahakama ilianza bila kupoteza hata dakika moja.

    Karani wa mahakama alisimama na kuanza kutaja namba ya kesi na baadaye muendesha mashtaka alisimama na kusoma historia nzima ya kesi na baadaye kumwomba Jaji Mpoki amhuhuku Anne kwa sababu ulikuwepo ushahidi wa kutosha kuonyesha ni kweli alimuua mama yake kwa kumchoma visu.

    Anne alisimama kizimbani akilia akiwa amewaangalia watoto wake Patrick na Nancy ambao pia waliendelea kulia, roho yake ilimuuma sana kujua ni lazima angehukumiwa kifo na kuwaacha watoto wake wakiteseka peke yao duniani, kuna wakati alijilaumu ni kwanini alimuua mama yake lakini alipokumbuka kuwa mama yake alitaka kuwaua watoto wake alisita kujilaumu na kuona alichokifanya kilikuwa sahihi.

    Mahakama iliendelea kuwa kimya wakati mwendesha mashtaka akiendelea kumueleza Jaji Raphael Mpoki sababu za kuitaka mahakama imhukumu mshtakiwa kunyongwa.

    “Mheshimiwa Jaji ushahidi wa kutosha upo na hivyo naiomba mahakama yako Tukufu imhukumu mshtakiwa kifo ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hizo!”

    ****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Jaji Mpoki aliinamisha kichwa chake chini na kuanza kutafakari hiyo ndiyo ilikuwa kawaida yake kabla hajamhukumu mtu kifo! Watu wote walijua baada ya kunyanyuka pale ni lazima angemhukumu Anne kunyongwa.

    “Anne!” Jaji Mpoki aliita baada ya kunyanyua kichwa chake lakini Anne hakuitika aliendelea kulia machozi akiwa amewaangalia watoto wake waliokuwa wakilia kwa sauti na kusababisha kelele mahakamani.

    “Wanangu Patrick na Nancy leo nakufa kwa ajili yenu!” Badala ya kumwitikia hakimu Anne aliwaita watoto wake.

    “Hapana mama usife, bado tunakuhitaji sana usituache!” Patrick alipiga kelele mahakamani na kuchomoka mikononi mwa mama yake mdogo akakimbia na kumfuata mama yake lakini kabla hajakifikia kizimba alikamatwa mkono na askari na kuanza kuvutwa kupelekwa mahali alipokuwa amekaa.

    “Anne tafadhali nijibu nakuita!” Jaji Mpoki aliita tena

    “Na.a..am mhe...sh..i..mi..wa ja..ji!”

    “Sema Anne, sema usiogope unataka nikufanye nini? Kwani maisha yako hivi sasa yapo mikononi mwangu!” Aliuliza Jaji Mpoki, wakili Lydia Ishengoma alijua nini alichomaanisha Jaji Mpoki kwa kuuliza swali hilo kwani haikuwa kawaida yake kuuliza maswali wakati wa hukumu na ilipotokea akauliza swali hilo alikuwa ameingiwa na huruma na kulikuwa na uwezekano mkubwa wa kumwachia huru mshtakiwa.

    Wakili Lydia alitegemea Anne angeomba msamaha na alijua wazi angeachiwa huru! Moyoni alijawa na furaha kupindukia alijua ushindi ulikuwa umewadia, hakutaka kabisa Anne ahukumiwe kifo kwa sababu aliua kwa kulazimishwa na mazingira.

    “Mheshimiwa Jaji ninajua mimi ni muuaji na ninastahili kifo na siwezi kukataa ninakuruhusu unihukumu kifo nife lakini.....!” Anne alianza kuongea, mahakama nzima ilikuwa kimya kumsikiliza yeye, wakili Lydia alishangaa ni kwanini Anne alianza kujitetea kwa kauli hiyo lakini moyoni mwake alijua ingebadilika.

    Baadaye Anne aliendelea“.... ni kweli niliua lakini mheshimiwa Jaji naomba niseme maneno yafuatayo kwa watu waliokuwepo hapa mahakamani ili wapate kuelewa ni kwanini nifanya hivyo! Ni wengi wananyongwa na ni wengi wameua lakini kwa kweli hawakutakiwa kufanya hivyo, mimi si muuaji ila nililazimika kuua kwa sababu sikuwa na njia yoyote ya kuwalinda watoto wangu! Mama yangu aliyenizaa na kunileta duniani alitaka kuwaua wanangu ingawa tayari alikwishaua watoto wangu wengine wawili William na Henry”

    Mahakama ilikuwa kimya watu wote wakisikiliza maneno ya Anne aliyoyaongea huku akilia.

    “Nilipokataa kumpa watoto wangu alinipiga na ugonjwa wa kupata hedhi kila siku na hivi mnavyoniona hapa niliposimama nguo zangu zote zimelowa na nimekuwa katika hali hii kwa muda wa miaka kumi na moja!”

    Anne alieleza kila kitu na kila mtu mahakamani alishikwa na huzuni wengi walinong’ona taratibu wakidai hata wao wasingeweza kuvumilia mateso aliyofanyiwa Anne! Wengi walimwaga machozi na hata Jaji mwenyewe alishindwa kujizuia na kujikuta akilia mbele za watu.

    “Nimemaliza mheshimiwa naomba unihukumu kifo ili ninyongwe nimfuate huko mama huko aliko na nikimkuta ni lazima nimuue tena kwa sababu amenitesa sana na mara kwa mara najiuliza ni kwanini alinizaa!” Alimaliza Anne huku akilia.

    Watu wote walikaa kimya kumsubiri Jaji Mpoki atoe hukumu yake, walipomwangalia alikuwa akijifuta machozi kwa kitambaa chake na alipomaliza kufanya hivyo alimwangalia Anne kwa huruma.

    “Uta....kwenda jela mia...ka mitano!” Jaji Mpoki alijikuta akitoa hukumu ambayo hakuna mtu mahakamani aliitegemea na maaskari walimuongoza Anne kumtoa mahakamani, aliondoka huku akilia na alisindikizwa na vilio vya watoto wake.

    “Msiwe na wasiwasi muda si mrefu nitakuwa pamoja na nyinyi watoto wangu!” Anne aliwaaambia watoto wake kabla hajatolewa ndani ya mahakama.

    Wakili Lydia aliruka na kushangilia kwa furaha alijua miaka mitano haikuwa mingi na ilikuwa bora kuliko kunyongwa, aliwakumbatia Patrick na Nancy pamoja na mama yao mdogo, kila mtu alikuwa na furaha.

    “Masikini kumbe msichana huyu ameteseka kiasi hiki?”

    “Aisee kwa aliyofanyiwa alikuwa na haki ya kuua!” Walisikika wakiongea watu waliotoka mahakamani.

    Wakili Lydia,Patrick, Nancy na mama yao mdogo walisimama nje ya mahakama wakisubiri Anne atolewe na kupakiwa ndani ya gari kwa safari ya kwenda gerezani, machozi yalishapungua usoni na nyuso zao zilionyesha furaha.

    “Mnasoma?” Wakili aliuliza.

    “Ndiyo!” Patrick na Nancy waliitikia.

    “Darasa la ngapi?”

    “Darasa la sita!”

    “Mlishika nafasi ya ngapi darasani?”

    “Mimi nilishika nafasi ya pili dada yangu akashika nafasi ya kwanza!”

    “Ah! Hongereni sana, wewe unataka kuwa nani ukiwa mkubwa?” Wakili alimuuliza Patrick.

    “Ninataka kuwa Mchungaji! Lakini dada yangu anapenda kuwa mwanasheria!”

    “Kweli?” Wakili alimuuliza Nancy

    “Ndiyo mama!”

    Walikaa mahakamani mpaka saa saba mchana mahakama ilipokwisha na walishuhudia Anne akitolewa mahabusu na kupakiwa ndani ya lori kubwa lililokuwa maalum kwa ajili ya kubeba mahabusu kuwarudisha gerezani.

    Alikuwa amekonda sana na nguo kama sketi aliyovaa ilionekana kulowa kwa damu! Inzi wengi walimfuata, Patrick na Nancy waliumia mioyo yao kumwona mama yao katika hali hiyo na walitamani mambo yangekuwa tofauti.

    Pia mambo waliyoyasikia mahakamani siku hiyo yaliwaumiza moyo, waliumia kujua mama yao aliua lakini walifarijika kujua aliua kwa sababu ya kuwatetea wao! Huo ulikuwa upendo mkubwa mno kwa mama kuuonyesha, mama yao alikuwa amekubali kuteseka gerezani kwa sababu yao! Jambo hilo liliwafurahisha sana.

    “Tutaoanana watoto wangu! Miaka mitano si mingi kama nitabaki gereza la hapa Butimba tafadhali mje kunitembelea mara kwa mara lakini kama nikihamishwa basi tutaonana Mungu akipenda!”

    “Sawa mama, tunakupenda mama!”

    “Mchungaji Aaron na mkewe wako wapi? Na wewe Suzzane umekuja lini?”

    Alipouliza swali hilo Patrick na Nancy walianza kulia machozi tena.



    Miezi sita kabla ya hukumu hiyo mchungaji Aaron na mkewe walipata uhamisho kwenda nchini Kenya katika jiji la Nairobi ambako mchungaji Aaron alitegemea kuongezea elimu zaidi ya mambo ya dini, alitakiwa kusoma Digrii ya kwanza ya Teolojia katika chuo kikuu cha Nairobi Theological University

    Yalikuwa ni masomo ya miaka mitatu kamili, yeye na mke wake walisikitika sana kuwaacha Patrick na Nancy ambao tayari walishaanza kuwahesabu ni watoto wao, lakini kikubwa kilichowaumiza zaidi kilikuwa ni Anne aliyekuwa gerezani, hawakujua wangemwona tena lini kwani waliamini angehukumiwa kifo na si ajabu kunyongwa bila wao kuwepo.

    Taarifa za kwenda Nairobi zilikuja ghafla mno kiasi kwamba hawakupata kabisa nafasi ya kwenda gerezani kumuaga Anne! Kitu kikubwa walichokifanya ni kumtafuta Suzanne, msichana aliyekwenda nyumbani kwao mara kwa mara kuwaona Patrick na Nancy, akidai walikuwa ni watoto wa dada yake yaani yeye na Anne walikuwa watoto wa baba mkubwa na mdogo.

    Suzanne aliwaeleza kuwa alikuwa ameolewa hapohapo mjini Mwanza maeneo ya Capripoint, iliwachukua siku kama tatu kumtafuta Suzanne kwa sababu hakuwahi kuwaachia namba yake ya simu, siku ya nne wakiwa wamekata tamaa kabisa wakifikiria kuwapeleka Patrick na Nancy Ustawi wa Jamii, walifanikiwa kumpata baada ya kumuulizia kwa jina la mume wake Anorld aliyekuwa mfanyabiashara maarufu mjini Mwanza.

    Suzanne alikuwa ni miongoni mwa watu waliofanikiwa kimaisha kwani kulikuwa na nyumba kubwa na magari kadhaa ndani ya ngome yake! Nyumba yake ilipambwa vizuri na kila aina ya samani zilizofanya ivutie kupita kiasi. kifupi Suzanne na mumewe walikuwa na pesa!

    Tatizo pekee alilokuwa nalo Suzanne ni bahati mbaya ya kutozaa watoto! Akiwa kidato cha tatu bahati alipata ujauzito uliotaka kuhatarisha maisha na masomo yake, ilibidi yeye na mvulana aliyempa mimba washirikiane kutafuta mitaani daktari wa kuitoa, kazi hiyo ilifanyika lakini bahati mbaya haikufanyika vizuri kwani mabaki mengine ya mimba hiyo ya miezi mitatu hayakutoka, yalibaki ndani ya mfuko wa uzazi hivyo kusababisha mfuko wa uzazi kuoza.

    Ili kuokoa maisha ya Suzanne madaktari walilazimika kumfanyia operesheni na kuutoa mfuko wake wa uzazi uliooza! Suzanne akawa amepoteza uwezo wake wa kuzaa.

    Kwa uzuri wa sura Suzanne alikuwa ni mwanamke mzuri wa kumvutia kila mtu aliyemwangalia, alipata bahati ya kusoma hadi chuo kikuu na kuhitimu digrii mbili za uchumi, elimu hiyo ilimwezesha kupata kazi nzuri sana katika shirika lililojishughulisha na uchimbaji wa visima kanda ya ziwa, Hesawa na Suzanne ndiye alikuwa bosi katika shirika hilo lililofadhiliwa na wazungu.

    Ni kweli Suzanne na Anne walikuwa ndugu, baba zao walikuwa ni mtu na mdogo wake. Suzanne akiwa Mwanza alisikia habari za Anne na matatizo aliyoyapata, alisikitika sana kusikia alikuwa gerezani na alianza juhudi za kuwatafuta Patrick na Nancy ili aishi nao nyumbani kwake kwani alikuwa na kila kitu isipokuwa watoto!

    Mchungaji Aaron na mkewe hawakuwa tayari kwa jambo hilo, sababu hata wao waliwapenda sana watoto hao hivyo walimkatalia Suzanne kuwachukua, lakini walipotakiwa kwenda kusoma Nairobi hawakuwa na chaguo jingine zaidi ya kumtafuta tena Suzanne ili awachukue watoto na kuishi nao.

    “Ninakwenda kusoma kwa muda wa miaka mitatu!”

    “Wapi?”

    “Hapa jirani tu Kenya!”

    “Aisee hongera sana!”

    Suzanne alifurahi mno kukabidhiwa watoto, aliowatamani kuwa nao kila siku, kitu cha kwanza alichokifanya baada ya kuwachukua Patrick na Nancy ni kuwahamisha kutoka shule ya Nyakabungo waliyosoma na kuwapeleka shule ya kimataifa ya Green Garden iliyokuwa maarufu kwa watoto wa watu wenye uwezo, wakawa wanafuatwa asubuhi na gari la shule na kurudishwa nyumbani jioni na walipewa chakula cha kutumia na walinunuliwa nguo mpya!

    Hata mume wake Suzanne nae pia aliwapenda sana Patrick na Nancy na alitamani wangekuwa watoto wake! Alilifahamu tatizo la mke wake kutokuwa na uwezo wa kuzaa mtoto lakini alimpenda Suzanne na hakuwa tayari kumwacha Suzanne kwa sababu hiyo.

    Siku zote Anorld alitamani kuwa na mrithi wa mali zake na alimtamani sana Patrick, alitamani sana kuwa na mtoto kama yeye lakini alijua isingewezekana tena na hakutaka kabisa kuzaa nje ya ndoa yake, Anorld alikuwa mwanaume mwaminifu pengine kuliko wanaume wote mjini Mwanza ingawa alikuwa na mali nyingi.

    Nyumbani kwa Suzanne Patrick na Nancy walipewa kila kitu na mwisho wa wiki ilikuwa ni lazima wapelekwe kisiwa cha Saa nane kuogelea! Maisha yalibadilika na kuwa ya raha, pamoja na hayo bado hawakumsahau mama yao kila siku walimfikiria na kabla ya kwenda kulala ilikuwa ni lazima wapige magoti na kumuombea.

    Waliamini muda si mrefu mama yao angetoka gerezani na kuwachukua kwenda kuishi nao pamoja, walikuwa tayari kuacha kila kitu ili mradi wawe na mama yao hata kama wangetakiwa kulala chini na kulala bila kula kwao ilikuwa sawa kwa sababu walimpenda sana mama yao!

    Watu wengine ambao Patrick na Nancy hawakuwa tayari kabisa kuwasahau walikuwa ni mchungaji Aaron na mkewe, waliokuwa tayari chuoni Nairobi, kila siku waliukumbuka wema wao na walimweleza hata Suzanne na mumewe jinsi familia hiyo ilivyompenda Mungu! Walijaribu pia kumshauri Suzanne na mumewe wamgeukia Mungu na kumtegemea yeye katika maisha yao.

    *****

    Mchungaji Aaron na mkewe wako wapi na wewe Suzanne umekuja lini?”

    “Mimi dada? Mbona nipo hapa Mwanza muda mrefu tu shikamoo kwanza!”

    “Marahaba! Kweli?”

    “Ndiyo!”

    “Na hawa watoto wangu ulikutana nao wapi na vipi na Mchungaji Aaron na mkewe wako wapi?”

    “Mchungaji Aaron na mkewe hivi sasa hawapo wamekwenda Nairobi kimasomo, kabla ya kuondoka sababu nilishakwenda kwao kujitambulisha mimi ni nduguyo walikuja hapa kuniomba nikae na watoto mpaka utakapotoka gerezani,kwa hivi sasa ninao kwa miezi sita sasa, wanasoma vizuri na ninaishi nao kama watoto wa ndugu yangu!”

    “Ahsante sana hivi sasa una watoto wangapi Suzanne?”

    “Sijajaliwa bado!”

    “Kweli?”

    ‘Ndiyo!”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Usijali lakini! Watoto hutoka kwa Mungu!”

    “Mbona una hali hii Anne? Mbona nguo zako zimelowa sana?” Aliuliza Suzanne akimwangalia Anne kwenye sketi yake aliyovaa.

    “Ni mama!Ni mama aliyenifanyia kitu hiki kibaya kila siku ninapata hedhi, kwa muda wa miaka karibu kumi sasa!”

    “Mungu wangu kweli? Ulishakwenda hospitali?”

    “Ndiyo lakini siponi haya ni mambo ya Lutego, ili nipone ninahitaji kuombewa na mchungaji au mtumishi yeyote wa Mungu!”

    “Usijali mama Ipo siku utapona tu na sisi pia tutaendelea kukuombea!” Nancy alimwambia mama yake.

    “Suzanne nitunzie vizuri watoto wangu Mungu atakubariki!”

    “Mama usiwe na wasiwasi anti ni mtu mzuri sana anatupatia kila kitu!” Patrick aliongea kabla Suzanne hajasema neno

    “Nakushukuru sana Suz….!”Kabla Anne hajamaliza alivutwa kwa nyuma na kuanza kupelekwa moja kwa moja hadi kwenye gari la kupakia wafungwa kwenda mahabusu.

    “Kwaherini mwanangu, ninawapenda sana ipo siku tu tutakuwa pamoja!”

    “Hakuna shida tunakupenda mama na tunakuombea na tunasubiri urudi!”

    Baadaye wote walilishuhudia gari likipakia wafungwa na mahabusu likaanza safari ya kuondoka mahakamani kwenda gerezani Butimba, Patrick na Nancy walibaki wakilia machozi kwa ajili ya mama yao, walimpenda sana Anne na walitaka sana kuwa naye maishani mwao!

    Gari lilipopotea machoni pao, Suzanne alifungua mlango wa gari lake na Patrick na Nancy waliingia ndani safari ya kuelekea nyumbani ilianza!Njia nzima Patrick na Nancy walilia machozi wakilitaja jina la mama yao! Katika maisha yao hawakuwa na kumbukumbu za kuishi na mama yao kwani alipotiwa nguvuni walikuwa na umri wa miaka miwili.

    *****

    Jioni ya siku hiyo Patrick na Nancy wakiwa wamelala usingizi, maongezi mazito na ya hatari yaliendelea chumbani kwa Suzanne na mume wake maongezi ambayo hawakutaka kabisa watoto wayasikie.

    “Najua unataka sana watoto Anorld lakini mimi uwezo wa kuzaa sina, unataka sana mrithi wa mali zetu lakini sina la kufanya kusaidia!”

    “Sasa tutafanya nini mke wangu? Natamani kuwa na mtoto kama Patrick ili angalau nikifa aweze kurithi mali zetu!”

    “Lakini si Patrick yupo hapa na dada yake pia, hawa wanaweza kuwa watoto wetu au unaonaje?”

    “Mama yao je? Mimi nataka watoto wangu mwenyewe!”

    “Sasa tutawapate wapi?”

    Suala la watoto lilimsumbua sana Anorld, siku zote alikuwa mtu mwenye mawazo juu ya jambo hilo na alishindwa angelitatua vipi! Mara nyingi alimshawashi mke wake Suzanne angalau wanunue mtoto wa wizi na kujifanya ni wao lakini Suzanne aliukataa mpango huo.

    Usiku huo walivutana sana juu ya suala la watoto mpaka wakafikia mahali wakashindwa kuelewana, baada ya majadiliano walifikia uamuzi wa kuwachukua Patrick na Nancy moja kwa moja wawe kama watoto wao wa kuzaa.

    “Nauliza mama yao je?”Anorld aliuliza tena.

    “Mama yao pamoja na kuwa ni ndugu yangu,furaha katika ndoa yetu ni watoto, hivyo hakuna njia nyingine zaidi kama unakubali tuhakikishe Anne anafia huko huko gerezani, hatoki na haonani na watoto wake tena sisi ndio tutakuwa wazazi wao!”

    “Tutalifanyaje hilo?”

    “Tutamuua huko huko gerezani!”

    “Tutawezaje kumuua mtu gerezani na ulinzi wote ulipo kule?”

    Wote wawili walikaa kimya kwa muda wakijaribu kutafakari ni kipi kingefanyika ili kuhakikisha Anne anakufa gerezani, na Suzanne na Anorld wanawachukua watoto wake, Suzanne alikuwa ndugu kabisa wa Anne lakini alikuwa ameamua kumuua ndugu yake ili amnyang’anye watoto wake wazuri waliompenda.

    “Hilo la tutamuuaje hebu tuliache kwanza tulale kesho tutakuwa tumeshalifikiria vizuri!”

    *****

    Asubuhi kulipokucha Suzanne aliwaamsha watoto na kuwatayarisha kwa kwenda shule, hiyo ndiyo ilikuwa kawaida yake kila siku, hakuonyesha dalili yoyote ya maongezi yaliyofanyika kati yake na mumewe usiku, alikuwa na furaha na mapenzi kwa Patrick na Nancy kama kawaida na alizidi kuwatamani watoto wale maradufu.

    “Nimeshajua cha kufanya Anne atakufa kirahisi sana, tutatafuta msichana yeyote mteja wa madawa ya kulevya, tutampa pesa ili afanye kosa lolote na afungwe akiwa gerezani tutamwambia amtafute Anne mpaka ampate, akishampata tutampa sindano ya sumu ya ‘Heart stopper’amchome usiku akiwa amelala na kufa, hakuna mtu atakayegundua!”

    Aliwaza Suzanne bila kujali mtu aliyekuwa akipanga kumuua alikuwa ndugu yake kabisa.

    “Mimi sijali ni lazima afe na Anorld akija jioni nitamweleza mpango wangu!” Aliendelea kuwaza Suzanne.

    Jioni mumewe aliporudi kutoka kazini watoto wakiwa wamelala Suzanne alimweleza mpango wake aliokuwa ameupanga, Anorld alicheka sana.

    “Mbona unacheka?”

    “Nimeamini kweli wewe ni komandoo!”

    “Kwanini?”

    “Una mawazo kama yangu!”

    “Na wewe ulikuwa unawaza hivyo?”

    “Ndiyo na tayari nimeshampata msichana wa kufanya hiyo kazi, anaitwa Zena atafanya vurugu yoyote ile leo na akitiwa ndani tutapigiwa simu!”

    “Kweli?” Suzanne alieleza bila huruma.

    “Wewe subiri alisema baada ya vurugu zake kwenye ukumbi wa disko wa Deluxe kesho lazima atapelekwa polisi, atatupigia simu!”

    Waliongea mengi juu ya Patrick na Nancy lakini baadaye walipitiwa na usingizi na kulala fofofo! Walizinduka saa 12 asubuhi kengele ya simu pembeni mwa kitanda chao ilipoita, Anorld alinyoosha mkono akainyanyua na kuiweka sikioni.

    “Ndiyo! Anorld hapa, nani mwenzangu?”

    “Mh! Kituo cha polisi kati hapa?”

    “Kuna nini tena ndugu yangu?”

    “Kuna dada mmoja kakamatwa baada ya kupigana na polisi na kumchania shati lake Deluxe!”

    “Haya nakuja sasa hivi!” Alijibu Anorld alishafahamu msichana huyo ni nani na ni kwanini alikuwa akiitwa kituoni!

    “Suzanne! Suzanne! Suzanne!” Alimwita mkewe aliyeonekana kuwa katikati ya usingizi mzito.

    “Vi...pi?”

    “Tayari! Kazi imekwishaanza kutekelezeka!”

    “Kweli?Umejuaje?”

    “Nimepigiwa simu sasa hivi na polisi amka twende!”

    Wote wawili walijiandaa na kutoka nje ambako walichukua gari na kukimbia haraka hadi kituoni ambako walipata nafasi ya kuongea na Zena!

    “Naingia kazini hiyo milioni yangu niikute!”

    “Usiwe na wasiwasi tutakuwa tumekuja kukutembelea gerezani kila Jumapili, ukishampata tu utuambie tutatumia ujanja wetu wote kukuletea hiyo sindano ya kumchoma nayo! Sawa?”

    “Hakuna tatizo kabisa kaka Anorld kazi nitaifanya vizuri na kwa uangalifu!” Zena aliwaondolea wasiwasi.

    Baadaye waliondoka haraka kurudi nyumbani kwenda kuwatayarisha Patrick na Nancy kwenda shule! Watoto hawakuwa na habari kabisa juu ya mpango uliokuwa unaendelea juu ya kumuua mama yao! Walijua kila kitu kiliendelea vizuri.

    “Anti lini tutakwenda kumuona mama gerezani?”

    “Jumapili!” Alijibu Suzanne akijua ni siku hiyo ndiyo yeye na mumewe wangekwenda kumwona Zena gerezani Butimba!

    “Kweli?”

    “Ndiyo!”

    Gari la shule lilipokuja liliwachukua watoto na kuwapeleka shuleni, Suzanne na mumewe nao muda mfupi baadaye waliondoka kwenda kazini kwao.

    ****

    Kijua kilikuwa kikichoma hali ya Mwanza siku hiyo ya Jumapili ilikuwa ya joto kidogo, ilikuwa rahisi kuifanananisha na Morogoro, siku hiyo Anorld, Suzanne, Patrick na Nancy waliondoka kuelekea gerezani Butimba ndani ya gari dogo la Anorld aina ya Cadillac! Watoto waliamini walikuwa wakienda gerezani kumwona mama yao kumbe Anorld na mkewe walikuwa na mpango tofauti kabisa vichwani mwao, walikuwa wakienda kumwona Zena na kumuuliza kama alifanikiwa kumpata Anne gerezani ili wakamilishe mpango wa kumuua.

    Kitu cha kwanza kilichofanyika baada ya kufika gerezani Butimba kilichowashangaza pia watoto ni kuitwa kwa mwanamke mwingine badala ya mama yao ambaye hawakumtambua na Anorld kwenda kuongea naye pembeni kwa muda mrefu!

    “Anti mbona mama humwiti? Muda wa kuona ndugu si utakwisha?” Patrick alimuuliza Suzanne lakini hakujibiwa kitu.

    ****

    “Vipi Zena umefanikiwa kumpata?” Anorld alimuuliza Zena!

    “Hapana tangu niingie hapa nimemtafuta lakini sijampata , nimejaribu hata kuulizia jina lake lakini sijampata si anaitwa Anne?”

    “Aisee, basi subiri hapahapa kwani mwanamke atakayetoka sasa hivi kuongea na sisi ndiye huyo! Akija nitakuita nikutambulishe nikidai wewe ni dada yangu ili iwe rahisi wewe kuzoeana naye! Sitaongea na wewe tena ila Jumapili ijayo nitakuletea sindano ya sumu ndani ya ugali ambao hutatakiwa kuula kabisa! Cha kufanya kuanzia leo jaribu kumzoea sana ili nikileta sindano ukamilishe kazi!”

    “Hiyo wewe usijali nionyeshe kwanza huyo marehemu mtarajiwa mwenyewe! Alisema Zena aliyeonyesha sura ya mtumiaji halisi wa madawa ya kulevya na pombe kali!”

    Anorld aliondoka na kujiunga tena na familia yake, akamwacha Zena akiwa amesimama peke yake akisubiri kutambulishwa kwa Anne!’

    “Anko mbona mama hatoki?”

    “Subirini nilikuwa nasalimiana na anti yenu mwingine!”

    “Mbona na sisi hatusalimiani nae?” Watoto walizidi kudadisi.

    “Atakuja sasa hivi!” Alisema Anorld na kuondoka kwenda kuandikisha jina la Anne ili wamwone, haikuchukua muda Anne akatoka, watoto wake walimkimbilia na kumkumbatia kwa furaha! Kama ilivyokuwa kawaida yake Inzi wengi walikuwa nyuma yake na harufu mbaya ilisikika mara tu alipofika baadhi ya watu walianza kuhama eneo hilo!

    Nguo zake zote zililowa na kugandamana na damu! Anne alisikitisha, pamoja na hali hiyo watoto wake hawakudiriki kumwacha walimkumbatia mpaka wakaangushana naye chini! Watu wote walishangaa na Anne alicheka kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu!

    Hali ilipotulia waliketi chini na kusalimiana, Anne aliendelea kumshukuru sana Suzanne kwa wema aliokuwa akimfanyia kwa kuwalea watoto wake waliongea pia mengi juu ya maisha katika siku zilizopita kati yao!

    “Huyu ndiye shemeji yako anaitwa Anorld ni mfanyabiashara hapa mjini!”

    “Aisee nafurahi kukufahamu shemeji, huyu ni ndugu yangu kabisa ishi naye vizuri!”

    “Hakuna tatizo shemeji pole na matatizo yaliyokupata!”

    “Ulisema hujabarikiwa mtoto?” Anne aliuliza tena.

    “Bado lakini Patrick na Nancy wanatufariji sana, tunajisikia vizuri kuishi nao nyumbani kwetu na tunasubiri umalize muda wako ili tuungane wote nyumbani kwetu!”

    “Ahsanteni sana na kwa sababu kifungo kinahesabiwa usiku na mchana siku mbili tofauti nitakaa hapa kama miaka mitatu hivi!”

    “Siyo muda mrefu utatoka tu!” Patrick alimwambia mama yake, Anne alishangazwa na busara iliyokuwemo ndani ya mtoto wake! Alikuwa ni marehemu mume wake tupu.

    Waliongea kwa karibu saa nzima, wakamkabidhi zawadi walizomletea na kuondoka zao, Patrick na Nancy walisikitika kumwacha mama yao tena, lakini hivyo ndiyo ilivyokuwa.

    ****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Jumapili iliyofuata Anorld alinunua chupa ya sumu ya ‘heart stopper’ sumu kali ya kusimamisha moyo, aliinyonya na kuiweka ndani ya bomba la sindano, mkewe alipiga ugali mzuri na sindano hiyo ikazamishwa katikati ya ugali huo uliopozwa ili kuzuia bomba lisiyeyuke!

    Anorld aliwasha gari na kwenda moja kwa moja hadi gerezani ambako alifanya mpango getini na kutoa kitu kidogo kwa maaskari akamkabidhi Zena chakula kile bila kukaguliwa.

    “Humo ndani ndiyo ipo hiyo sindano baada ya kumchoma nayo, atakauka! Hapohapo usichelewe kimbia chooni ulitupe bomba la sindano! Si tayari mmeshazoeana?”

    “Tayari na tunalala pamoja!”

    “Fanya kweli basi!”

    “Usiwe na wasiwasi tayarisha pesa yangu tu!”



    “Utajiri bila watoto ni hasara, kumbe basi kipi bora? Watoto au mali?” Hilo ndilo swali alililojiuliza Anorld kila siku kichwani mwake! Alikuwa na kila kitu, mke mzuri mwenye mguu wa kuvutia, mwanya, rangi nzuri ya ngozi alikuwa mzuri pengine kuliko wanawake wote duniani.

    Anorld alipata kila starehe iliyopo chini ya jua, kila mwaka wakati wa sikukuu za Krismasi ilikuwa ni lazima yeye na mke wake waende Canada kupumzika na kurudi mwanzoni mwa mwaka mpya! Kwao safari za visiwa kama Shelisheli, Comoro, Zanzibar kwenda kupumzika lilikuwa jambo dogo na la kawaida! Waliweza kufanya hivyo mara tano au sita kwa mwaka! Pesa ilikuwepo kilichotakiwa ni namna gani itumike.

    Kifupi Suzanne na mume wake walikuwa na kila kitu kasoro kitu kimoja tu! Nacho ni mtoto, Suzanne kutokuwa na uwezo wa kuzaa ndio kuliwafanya wakose raha kidogo ya maisha katika ndoa yao pamoja na kuwa na kila kitu!

    Mrithi wa mali ndiye alikuwa tatizo sababu wote walifahamu ilikuwa ni lazima siku moja wafe! Nani angebaki mrithi wa mali yao? Hilo ndilo swali liliwaumiza vichwa vyao kila siku, hivyo kuja kwa Patrick na Nancy katika maisha yao kulionekana kutoa jibu la tatizo hilo!

    uzuri wa watoto hao uliwachanganya sana akili Suzanne na Anorld, Patrick na Nancy walikuwa watoto wazuri mno na hiyo ilitokana na mchanganyiko wa damu ya marehemu baba yao Huggins, walitamani watoto wale wawe wao! Roho ya dhuluma ilishawaingia mioyoni mwao, dhuluma ya watoto, viumbe hai, binadamu! Ilikuwa ni dhuluma kubwa lakini Suzanne na Anorld walikuwa wamedhamiria kuifanya bila uoga.

    Ilikuwa si rahisi kuwapata watoto hao kama mama yao angetoka gerezani baada ya miaka mitano! Hivyo ili wawapate njia pekee ilikuwa ni kumwondoa Anne duniani akiwa hukohuko gerezani, walifahamu pengine baada ya Anne kufa wazazi wa marehemu Huggins au ndugu zake wengine wangeweza kujitokeza na kudai kuwachukua watoto, ni hilo pekee ndilo liliwatia hofu lakini walijua jinsi ya kulishughulikia.

    “Pesa haishindwi kitu ni lazima watoto hawa wawe wetu, isitoshe sisi ni kama tumewasaidia katika maisha ni watoto wenye bahati kubwa sana hawa! Utajiri wote huu tuwaachie?’ Aliongea Anorld kwa uchungu!”

    “Kwa kweli tumewasaidia!” Suzanne aliitikia.

    Wakati maongezi hayo yakiendelea chumbani kwao Suzanne na Anorld waliaamini kabisa kuwa Patrick na Nancy walikuwa wamelala usingizi! Haikuwa hivyo kwani Patrick alikuwa macho akiendelea kumlilia mama yake, aliyoyaona gerezani siku hiyo yalimtia simanzi kubwa sana moyoni mwake.

    Hali ya mama yake ilivyokuwa, alivyotoa harufu, alivyofuatwa na Inzi wengi kila alikokwenda, alivyokonda ilimuumiza sana moyo na kumfanya akose kabisa usingizi!Dada yake Nancy alikuwa tayari usingizini lakini Patrick hakupata hata lepe la usingizi mawazo yalikuwa mengi mno kichwani mwake, alishindwa kuelewa ingekuwaje siku ambayo mama yake angetoka gerezani. Aliamini hiyo ndiyo ingekuwa siku ya furaha kuliko zote maishani mwake.

    Ghafla akiwa katika mawazo hayo alisikia maneno kutoka katika chumba cha Suzanne na Anorld hakuyaamini masikio yake ikabidi asikilize tena kwa makini zaidi lakini maongezi yaliendelea kubaki yaleyale!

    “Watoto hawa watakuwa wetu tu! Si Anne anakufa usiku huuhuu! Ile sindano atakayochomwa itamkausha kama samaki!”

    “Masikini Anne lakini inaniuma sana ndugu yangu kufa! Sina jinsi ya kuzuia hili lisitokee kwa sababu ninawataka sana Patrick na Nancy!”

    Moyo wa Patrick uliruka mapigo mawili mfululizo, alisikia kama moyo wake unataka kusimama kufanya kazi.

    “Ha! Mama yangu anakufa? Anakufa kwa nini?” Alijiuliza Patrick na kumwamsha dada yake aliyekuwa amelala fofofo!’

    “Nancy!Nancy!Nancy! Tafadhali amka upesi!” Aliongea taratibu huku akimtingisha dada yake.

    “Nini tena Patrick?”

    “Amka usikilize wanavyoongea anko na anti Suzanne!’

    “Wanaongea kitu gani?”

    “Wasikilize tu!” Patrick alimwambia dada yake.

    Wote wawili walisimama na kusogea dirishani na kuanza kusikiliza jinsi Anord na Suzanne walivyokuwa wakirufahia kifo cha Anne usiku huo, kifo cha sindano ya sumu aina ya Heartstopper ambayo Anne angechomwa na Zena usiku huo gerezani.

    Wote wawili walimkumbuka dada zena waliyemwana gerezani siku hiyo, Nancy alishindwa kujizuia na kuanza kulia machozi tena kwa sauti ya juu, sauti hiyo iliwafikia Anorld na Nancy chumbani kwao na kutoka mbio kukimbilia chumbani kwa akina Nancy.

    “Usithubutu kuwaonyesha kuwa tumeyasikia maongezi yao umenisikia?”Patrick alimwambia dada yake kabla hajafungua mlango kuruhusu Anorld na Suzanne waingie ndani.

    “Vipi watoto wangu?” Suzanne aliuliza.

    “Hakuna kitu ni Nancy alikuwa anaota ndoto ya kutisha!” Patrick alijibu wakati dada yake akiwa amelala kitandani na kujifunika na shuka hadi kichwani.

    “Nancy!Nancy!Nancy! Vipi mwanangu?”

    ‘Mh!Mh!” Nancy aliguna na kuendelea kulia machozi chini ya shuka hakutaka kujifunua, alitii alichoambiwa na kaka yake. Baadaye Anorld na Suzanne waliondoka kurejea chumbani kwao ambako waliingia kitandani na kulala.

    “Sijui wamesikia maongezi yetu hawa?” Anorld aliuliza.

    “Ah! Wapi, haiwezekani!”

    ****

    Nancy na Patrick hawakulala tena, waliendelea kulia wakimlilia mama yao! Walijua mama yao angekufa usiku huohuo kwa kuchomwa na sindano ya sumu, walijua wasingekuwa na mama tena duniani kuanzia asubuhi iliyofuata, walikuwa yatima tayari, walipoamka macho yao yalikuwa yamevimbiana kwa sababu ya kulia. Siku hiyo hawakujiweka tayari kwa shule kama ilivyokuwa kawaida yao jambo lililowapa Anorld na Suzanne wasiwasi kidogo.

    “Mbona macho yenu yamevimba kiasi hiki?”

    “Sababu ya kulia!”

    “Kwanini mlie sana watoto wangu wazuri?”

    “Kumbukumbu ya jana, mama alituumiza sana moyo!” Alijibu Patrick.

    “Vaeni basi mwende shule sasa hivi au?”

    “Mimi sijisikii hata kidogo kwenda shule anti, labda Nancy ajiandae!” Alijibu tena Patrick.

    Nancy alipoulizwa naye alikataa walishapanga kutokwenda shule siku hiyo,walitaka kutoroka kwenda gerezani kuangalia kama kweli mama yao alikuwa amekufa.

    “Haya chukueni hii pesa mtanununua soda mnywe sawa? Sisi tunakwenda kazini!” Alisema Suzanne na kuwakabidhi Patrick na Nancy noti ya shilingi 500.

    “Ahsante anti!’ Aliitikia Nancy baada ya kuipokea noti hiyo mkononi mwake.

    Suzanne na Anorld waliingia ndani ya gari na kuondoka kwenda kazini, nyuma Patrick na Nancy hawakutaka hata kupoteza dakika moja walichofanya ni kuvaa viatu na kuchomoka hadi nje ambako kabla ya kutoka mlinzi aliwauliza walikuwa wakienda wapi.

    “Tunakwenda dukani kununua miswaki!”

    “Ok! Nendeni basi lakini msichelewe kurudi!”

    “Sawa babu!” Patrick aliitikia.

    Walipofika nje walitembea hadi kituo cha daladala cha Nera ambako walipanda basi lililowapeleka hadi kitu cha mabasi ya kwenda Butimba karibu na kampuni ya Kauma, asubuhi hiyo walikuta basi moja likiwa limeegeshwa kituoni, wao ndio walikuwa abiria wa kwanza kupanda basi hilo na kusubiri abiria wengine walioanza kuingia mmoja baada ya mwingine mpaka likajaa na kuanza kuondoka.

    Njiani Patrick na Nancy waliendelea kulia machozi wakimlilia mama yao, waliamini kabisa kuwa tayari Anne alikuwa maiti! Kwa maongezi waliyoyasikia kutoka chumbani kwa suzanne na Anorld ilikuwa si rahi si kuamini kuwa mama yao angekuwa hai.

    “Sindano ya sumu! Yaani wamemuua mama yetu kwa sindano ya sumu? Huu ni unyama, kama walitutaka sisi ni kwanini wasingeongea tu na mama badala ya kumuua?’ Kwani mama angekataa kusema watuchukue, wakati hata uwezo wa kututunza kama mama angetoka gerezani hangekuwa nao?” Aliendelea kuwaza Patrick.

    Watu wote ndani ya basi walishangazwa na kitendo cha watoto hao wawili kuendelea kulia , mzee mmoja alitaka kufahamu nini kilikuwa chanzo.

    “watoto mbona mnalia tangu tuondoke kituoni?’

    “Mama yetu amekufa!”

    “Amekufa wapi?”

    “Gerezani Butimba?’

    “Nani amewapa taarifa hizo?”

    Patrick na Nancy walishindwa kujibu swali hilo na kujikuta wakiendelea kulia machozi tu.

    “Nielezeni basi?”Mzee yule aliendelea kuwabembeleza waseme lakini hawakufanya hivyo!

    Gari lilipofika gerezani Butimba Patrick na Nancy waliteremka na kunyoosha hadi gerezani lengo lao likiwa ni kufahamu kama kweli mama yao alikuwa amekufa au la! Watu wa kwanzakukutana nao walikuwa ni maaskari walinzi wa gereza.

    “Nyie watoto mnakwenda wapi asubuhi hii?’

    “Tumekuja kumwona mama yetu!”

    “Mama yenu nani?”

    “Anne!”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ni mfungwa wa mahabusu!”

    “Amefungwa miaka mitano!”

    “Leo siyo siku ya kuona wafungwa, njooni jumamosi au Jumapili siyo leo mnasikia?”

    “Hapana tunataka kumwona mama yetu, tunataka kujua yupo hai au amekufa!”

    “Kwani mmeambiwa amekufa?”

    “Ndiyo tunafahamu amechomwa sindano ya sumu!”

    “Sindano ya sumu nani kamchoma?”

    “Mfungwa mwenzake anaitwa Zena! ”

    “Nyie watoto mbona siwaelewi, mnaongea jambo kubwa sana hilo hebu jaribuni kunieleza vizuri!” Askari huyo aliwachukua na kuwapeleka pembeni ambako walianza kumsimulia kila kitu kilichotokea na jinsi walivyosikia sauti ya Suzanne na Anorld wakiongea, pia jinsi sindano hiyo ilivyoingizwa gerezani ndani ya ugali.

    “Mh! Jambo hilo linawezekana kweli?” Alihoji askari wakati bado akijaribu kutafakari jambo hilo lango la gereza lilifunguliwa na maiti ya mtu ikiwa imefungwa ndani ya shuka jeupe ilipitishwa mbele yao na kupakiwa ndani ya gari.

    “Haya maafande waliochanguliwa kwenda kuzika maiti hii pandeni haraka ndani ya gari tuondoke!” aliamuru askari magereza mmoja mwenye V tatu begani. Maaskari kama kumi hivi walipanda ndani ya garini haraka tayari kwa kuondoka.

    Tayari Patrick na Nancy walikuwa na uhakika kabisa kuwa maiti iliyopakiwa ndani ya gari ilikuwa ni mama yao,walianguka chini na kuanza kulia machozi, wakiliita jina la mama yao na kuwatupia lawama Suzanne na Anorld kwa kitendo chao cha kinyama!

    Kelele hizo ziliwafanya maaskari wangine zaidi washtuke na kulazimika kuwafuata Patrick na Nancy na kuwadadisi zaidi, maelezo yao yalitosha kuwafanya maaskari waamini kweli aliyekufa alikuwa ni mama yao.

    “Wapandisheni ndani ya gari wakalione kaburi la mama yao ili kama wakitaka kuwapeleka ndugu zao wawapeleke baadaye!” Alisema dereva.

    Patrick na Nancy walipandishwa ndani ya gari na safari ya kwenda eneo la Mkolani nje kidogo ya mji wa Mwanza kwa mazishi ilianza, njia nzima waliendelea kulia, katika maisha yao hawakuwahi kuishi na mama yao kwa muda mrefu lakini walimpenda na alikuwa kila kitu kwao.

    Walimtegemea baada ya miaka michache tu baadaye angekuwa huru pamoja nao lakini sasa maisha ya kipenzi chao yalikuwa yamekatishwa kinyama na Anorld na Suzanne sababu tu ya kutaka kumdhulumu watoto alizaa mwenyewe!

    “Huu ni ukatili na Mungu atawalipia anti na anko!” Nancy alisema kwa uchungu.

    “Na sitaki tena kurudi nyumbani kwao ninakwenda mwenyewe nitakako! Nitakuwa hata chokoraa lakini sipo tayari kurudi kwao tena wauaji wakubwa wale!” Alifoka Patrick.

    Walipofika makaburini shimo lilishachimbwa tayari na bila hata kuruhusiwa kutoa heshima zao za mwisho au kuiona sura ya mama yao kwa mara ya mwisho, maiti ilitupwa shimoni na kuanguka kama mzigo! Shimo likaanza kufukiwa na udongo, Patrick na dada yake walilia hadi sauti zao kukauka lakini hawakuubadili ukweli kuwa mama yao alikuwa amekufa.

    Baada ya mazishi walipakiwa ndani ya gari na safari ya kurudi gerezani ilianza tena ambako waliachiwa na kuingia mitaani, hawakurudi tena nyumbani kwa Anorld na Suzanne kama walivyokuwa wameamua, waliwaona ni wauaji ambao wangeweza kuwachinja hata wao wenyewe.

    ****

    Jioni ya siku hiyo Suzanne aliwahi kurudi kutoka kazini kabla ya Anorld na dakika kama ishirini tu tangu aingie ndani ya nyumba yake, maaskari watatu walibisha hodi mlangoni aliwakaribisha sebuleni lakini hawakukakaa sana kabla hawajamwambia shida yao.

    “Mama sisi ni maafisa wa polisi na hivi tunavyoongea na wewe upo chini ya ulinzi unahitajika kituoni mara moja!”

    “Nimefanya nini?” Aliuliza Suzanne.

    “utaelezwa hukohuko, mumeo yupo wapi?”

    “Yupo kazini bado hajarudi!”

    “Tutamfuata baadaye!”

    “Labda nimjulishe arudi upesi?”

    “Hapana!” Alijibu askari mmoja na kumpiga pingu za mikononi Suzanne akaanza kusukumwa kumtoa nje ya nyumba yake!

    Alipelekwa moja kwa moja hadi kituo cha polisi ambako alifahamishwa wazi kuwa yeye na mumewe walikuwa wakituhumiwa kuingiza sumu gerezani na kusababisha kifo cha mfungwa mmoja!

    Ndugu na marafiki waliofika baadaye polisi kutaka kujua sababu ya kukamatwa kwa Suzanne waliporudi majumbani kwao walimpigia simu Anorld ambaye alishapata taarifa na kujificha eneo la Nyamanoro kwa rafiki yake na kumjulisha sababu ya kukamatwa kwa mkewe na sababu iliyopelekea hilo!

    “Nendeni kwanza mkaangalie nyumbani kama wale watoto wapo?” Anorld alishauri.

    “Sawa!” Alijibu Jesca dada yake Anorld na bila kuchelewa alichukua gari la mama yake na kwenda nalo moja kwa moja hadi nyumbani kwa Anorld.

    Alipofika nyumbani kwa kaka yake ilikuwa tayari yapata saa sita na nusu ya usiku na kukutana na mlinzi wa nyumba hiyo.

    “Vipi babu akina Patrick na Nancy wamerudi?”

    “Hata mimi nashangaa sijui wapo wapi siyo kawaida yao hata siku moja kukaa nje hadi saa hizi za usiku, sijui nao wamekamatwa?” Alihoji mlinzi.

    “Hapana! Sijui mahali walipo! askari wamekuja tena?” Jesca aliuza.

    “Nafikiri kila baada ya dakika kumi hivi wanafika na ninaona ni heri uondoke sababu wakikukuta hapa halafu itakuwa taabu!”

    *****

    Jesca aliondoka kurejea nyumbani ambako alimpigia tena simu Anorld na kumtaarifu hali halisi ilivyokuwa.

    “Ninajua wazi hao ni Patrick na Nancy tu hakuna mwingine na nitawatafuta usiku huu huu hadi niwapate! Wamenichomea polisi watanitambua watoto hawa!” Alisema Anorld na baada ya kukata simu alimpigia msaidizi wake ambaye alitayarisha magari madogo kumi kwa ajili ya msako wa kuwatafuta watoto usiku huo.

    “Je kama wamelala nyumbani kwa mtu?”

    “Hawana ndugu yeyote hapa jijini na jua watakuwa wamelala sehemu fulani mitaani na ninafikiri maeneo ya hukohuko Butimba, mkikosa huko jaribuni kwenye makaburi ya Mkolani ambako wafungwa huzikwa kwa uchungu walionao ni lazima watakuwa wamelala juu ya kaburi la mama yao!”

    *****

    Usiku huohuo wa baridi kali huku manyunyu ya mvua yakidondoka, Patrick na Nancy walilala juu ya kaburi waliloamini ni la mama yao! Walikuwa bado wakimlilia mama yao kwa uchungu sana na kukilaani kitendo cha Suzanne na Anorld.

    Hawakuwa na ufahamu wa jambo lolote lililoendelea mjini Mwanza kwa wakati huo, wala hawakuwa na hisia za kusakwa ili wauawe.

    Patrick na Nancy wakiwa hawana hili wala lile mara ghafla walisikia muungurumo wa gari na kuona mwanga mkali wa taa za gari ukikatisha kutoka barabarani kuelekea makaburini kila mmoja wao alishtuka.

    “Mh!nini tena? Lakini hawa wanaweza kuwa majambazi au watu wamekuja kufanya uchawi wao makaburini!”

    “Sasa tufanye nini?” Nancy alimuuliza kaka yake wakati gari likizi kukaribia zaidi!

    “Njooni huku tujifiche!” Patrick alisema huku akimvuta dada yake kuelekea Kwenye nyasi ndefu zilizokuwepo jirani yao wakiwa katika nyasi hizo walishuhudia gari likiegeshwa na watu watano kushuka, pamoja na kuwa giza walipojaribu kuziangalia sura za watu wale waliitambua sura ya mtu mmoja na hata sauti ilikuwa ya Anorld!Moyo wa Patrick ulilipuka, watu wote walikuwa na bunduki mikononi!

    “Tafuteni kaburi la leo! Watakuwa wamelala hapohapo!” iliamrisha sauti ya Anorld.

    Tochi zilimulika kila mahali hatimaye wakalifikia kaburi la siku hiyo.

    “Hili hapa!” Alipiga kelele mtu mmoja!”

    “Wapo?”

    “Hawapo? Ila kuna miguu ya watoto hii hapa juu! Inavyoonekana walikuwa hapa muda si mrefu!”

    “Inaeelekea wapi?”

    “Porini!”

    “Fuatilieni huko huko porini na mkivipata hivyo vitoto ueni kabisa ili kupoteza ushahidi, maana hivyo vitajidai vishahidi maana ndivyo vilisikia maneno yangu!” Aliamuru Anorld.

    “Sawa bosi!”

    ****

    mauaji yalivyotokea gerezani:

    Usiku wa manane Anne akiwa amelala fofofo, Zena aliyekuwa pembeni yake alipohakikisha kuwa asingeweza kushtuka alinyanyuka na kwenda hadi chooni ambako alilificha sufuria lililokuwa na ugali darini, alilichukua na kushuka nalo hadi chini ambako alianza kuusambaza ugali na kulitoa bomba la sindano.

    “Yes! Kazi imekamilika mwisho wa maisha yake umefika! NI lazima nimuue nikachukue pesa yangu” alisema Zena.

    Aliliangalia bomba la sindano na kuona lilikuwa limejaa vizuri sumu ambayo ingeukausha mwili wa Anne kama alivyokuwa ameambiwa na Anorld.

    “Mimi sijali kuondoa maisha ya mende kama Anne ili mradi nimepewa pesa!” Alinong’ona Zena.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Je nini kiliendelea?

    Je Nancy na Patrick walipatikana?



    ITAENDELEA



0 comments:

Post a Comment

Blog