Search This Blog

TAFADHALI MAMA USIWAUE WATOTO WANGU - 4

 







    Simulizi : Tafadhali Mama Usiwaue Watoto Wangu

    Sehemu Ya Nne (4)



    Kama ilivyo kawaida ya gereza lolote chakula huwa kidogo na mara nyingi hakifai wala hakiwezi kulinganishwa na chakula cha nyumbani na kwa kawaida wafungwa hula mara moja kwa siku, hivyo siku zote huwa ni watu wenye njaa!

    Akiwa na bomba la sindano mkononi Zena alianza kupiga hatua kuelekea mahali alipolala Anne, alikuwa amedhamiria kuyakatisha maisha yake kwa sababu ya pesa! Hatua kama tano mbele aliikumbuka sufuria la ugali aliloliacha chini, aligeuka kuliangalia na kukuta liko palepale.

    “Hili sufuria na ugali wake litaniletea taabu wacha nilirudishe kwanza darini ndiyo nije niendelee na kazi yangu!” Aliwaza Zena na kumwangalia Anne aliyekuwa amelala sakafuni akiendelea kukoroma taratibu.

    Bila kuchelewa wala kusita Zena alikata kona akiwa na bomba lake mkononi kulifuata sufuria la ugali, alilibeba na kuanza kutembea kuelekea nalo chooni! Mbele kidogo hisia za ajabu zilimwijia, mate yakaanza kumdondoka! Alijisikia njaa ya ajabu, hakuwa kusikia njaa namna hiyo katika maisha yake, aliutamani ugali aliokuwa ameubeba na kujikuta akiyapuuzia maneno aliyoambiwa na Anorld kuwa asiutie mdomoni ugali huo.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Aliuangalia ugali ule na kuzidi kuutamani mdomo wake ulitaka sana aule lakini akili yake ilishindana sana na mawazo hayo. Zena alijikuta njia panda bila kujua la kufanya, ghafla alijikuta akiliweka bomba la sindano chini na pamoja na kuwepo harufu kali chooni alianza kuula ugali huo kwa juujuu bila kuingia ndani ambako bomba la sindano lilifukiwa kabla hajalitoa.

    “Hata kama ni sumu huku juu haiwezi kuwa imefika ni lazima itakuwa humohumo ndani lilipokuwa bomba!” Alijipa moyo Zena na kuendelea kula ugali huo lakini dakika tano baadaye alianza kusikia kizunguzungu na baadaye macho yake yalianza kuona kiza, misuli ikaanza kukamaa na kubana kama ambavyo hutokea kwa mcheza mpira, maumivu ya misuli yalikuwa makali mno kabla hajaanza kulia alianguka chini na kupoteza fahamu hakujua tena kilichoendelea.

    Saa kumi na moja alfajiri Anne alizinduka usingizini na kuanza kumwamsha mfungwa aliyelala jirani yake akidhani ni Zena.

    “Mimi sio Zena!”

    “Zena yuko wapi?”

    “Aliondoka usiku wakati wewe umelala na hakurudi tena sijui yuko wapi?”

    Kabla hawajaendelea sana na maongezi yao mara walisikia kelele za mtu kutoka chooni, wote wawili walishtuka wakanyanyuka na kukaa.

    “Jamani!Jamani!Jamani! Mtu kafia chooni!” Alipiga kelele mtu huyo akikimbia kutoka chooni kwenda katika ukumbi waliolala wafungwa.

    Baada ya kusikia kelele hiyo wafungwa wote walinyanyuka sakafuni walikokuwa wamelala na kuanza kumfuata mwanamke aliyekuwa akipiga kelele ili kumuuliza vizuri juu ya jambo alilokuwa akilisema.

    “Yuko wapi huyo mtu aliyekufa?” Anne aliuliza hakuwa na wasiwasi kuwa mtu huyo angeweza kuwa Zena.

    “Yupo chooni ingieni wenyewe mkaone!”

    Anne aliongoza kundi la wafungwa kuingia ndani ya choo, hakuyaamini macho yake kukuta aliyenguka chini ni Zena!

    Bomba la sindano na sufuria la ugali vikiwa pembeni mwake, hakuamini kama alikuwa amekufa palepale alipiga magoti chini na kuanza kumtingisha akimwita jina lakini Zena hakushtuka alipogusa moyo wake pia ulikuwa umesimama kabisa ni hapo ndipo alipoamini Zena alikuwa amekufa!

    Kila mfungwa alihisi Zena alikuwa amejiua mwenyewe kwa kujichoma sindano ya madawa ya kulevya lakini walipoliangalia bomba la sindano lilikuwa limejaa dawa mpaka juu jambo lililoonyesha wazi kuwa alikuwa bado hajajichoma kwa sindano ile.

    Anne aliangua kilio, alilia mpaka akaanguka chini na kuzimia! Ikabidi wafugwa wenzake wamtoe nje na kummwagia maji ndipo akazinduka tena, alikuwa akimlilia rafiki yake mpendwa Zena waliyekutana naye hapohapo gerezani.

    Hakuwa na habari hata kidogo juu ya jambo ambalo Zena alipanga kumfanyia usiku wa siku hiyo, bila Zena kuula ugali ni lazima yeye Anne ndiye angekuwa marehemu wakati huo! Aliendelea kumlilia Zena mpaka mkuu wa gereza alipokuja na kuamuru mwili wa Zena uondolewe chooni na kupelekwa zahanati ambako ulihifadhiwa.

    Pia ugali na bomba la sindano vilivyokutwa pembeni kwa Zena viliondolewa na kuhifadhiwa kwa uchunguzi asubuhi ya siku hiyo, kila mtu alichanganyikiwa na kifo cha Zena, mkuu wa gereza na daktari wa gereza walishindwa kuelewa ni dawa gani iliyokuwa ndani ya bomba la sindano alilokutwa nalo Zena na walishindwa kuelewa alilipata wapi akiwa kama mfungwa.

    Kulipokucha asubuhi bomba la sindano pamoja na ugali vilichukuliwa na kupelekwa moja kwa moja hadi hospitali ya Bugando ambako vyote vilifanyiwa uchunguzi na kugundulika kuwa bomba la sindano pamoja na ugali vilikuwa na sumu aina ya ‘Heartstopper’ ambayo kazi yake ni kuusimamisha moyo kufanya kazi!

    Kila mtu aliamini Zena alikuwa ameamua kujiua mwenyewe kwa sumu hiyo mbaya, hakuna mtu hata mmoja aliyehisi kuwa sumu ile iliingizwa gerezani kwa lengo la kumuua Anne na si Zena.

    Nani aliingiza sumu ile gerezani ndilo lilibaki kuwa swali la kila mtu, mkuu wa gereza alichanganyikiwa na kuamuru kufuatilia ni nani aliyeingia ugali ule ndani ya gereza. Kwa sababu ya umaarufu wa Anorld haikuchukua muda mrefu kugundua kuwa ni yeye ndiye aliyeleta chakula hicho.

    Mkuu wa gereza alitoa taarifa hiyo polisi ambao bila kuchelewa walianza msako wa kumtafuta Anorld kama mtuhumiwa namba moja wa mauaji hayo! Polisi walipokwenda kwake hawakumkuta na kulazimika kumkamata mke wake Suzanne na kumweka mahabusu wakati msako wa kumtafuta Anorld ukiendelea.

    Mipango ya mazishi kwa taratibu za gereza ilianza kuandaliwa ili mwili wa Zena uzikwe lakini mara tu baada ya maiti yake kupakiwa ndani ya gari watoto wawili mapacha Patrick na Nancy waliwasili gerezani, habari waliyoitoa kuwa waliwasikia Anorld na mkewe wakipanga jinsi ya kumuua mama yao ili wamdhulumu watoto wake ilizidi kuwahakikishia kuwa ni Anorld na Suzanne ndiyo waliofanya mauaji hayo.

    *****

    Msako wa Patrick na Nancy porini:



    “Fuatilieni hukohuko porini na mkivipata hivyo vitoto viueni kabisa ili kupoteza ushahidi, maana hivyo ndivyo vitajidai ni mashahidi mahakamani sababu ndivyo vilisikia maneno yangu!” Aliamuru Anorld.

    Maneno hayo yalimfikia Patrick moja kwa moja mahali alipokuwa amejificha, hofu kubwa ilimwingia moyoni mwake alijua mwisho wao ulikuwa umefika kama tu wangeingia mikononi mwa watu waliokuwa wakiwatafuta. Alishindwa kuelewa ni kwanini Anorld na mama yao mdogo Suzanne walikuwa wameamua kuwageuka kiasi hicho.

    Hawakuwa na mahali pa kukimbilia walijua kwa vyovyote vile wangekamatwa tu! Kwani miale ya kurunzi za majambazi ilimulika kila mahali, mahali walipolala katikati ya nyasi hapakuwa mbali sana na makaburi na kama wangejaribu kusimama wima ni lazima wangeonekana.

    Nancy alijua pia kuwa yeye na kaka yake walikuwa katikati ya hatari, walikuwa katikati ya kifo na maisha! Kama mtoto wa kike hakuna alichokijua zaidi ya kulia na kuzidi kumkumbatia kaka yake akimuuliza kipi wangefanya ili kujiokoa.

    “Patrick! Patrick!Patrick!” Aliita lakini kaka yake hakumwitikia.

    Alianza kumtingisha lakini Patrick hakuonekana kushtuka wala kujibu kitu chochote!Alikuwa kimya kabisa na mwili wake ulikuwa wa baridi kupita kiasi, Nancy alishindwa kuelewa ni nini kilimpata kaka yake, alishindwa kuyazuia machozi yalianza kumiminika huku tochi zikimulika kuelekea mahali walipokuwa wamejificha.

    “Patrick!Patrick!Amka twende, mbona umekaa kimya?” Alizidi kusema Nancy lakini Patrick hakushtuka wala kuongea kitu chochote alionekana kama mtu aliyekufa na Nancy alishindwa kuelewa alikuwa hai au la!

    “Patrick usife kaka yangu! Usiniache peke yangu ninakuhitaji tutoroke pamoja! Bila baba, bila mama, bila wewe nitaishije mimi?” Alisema Nancy huku akibubujikwa na machozi.

    Tochi zilizidi kumulika katikati ya nyasi walipojificha, hofu ilizidi kumwingia Nancy na mwili wake ulikufa ganzi kabisa, alijikuta akiwa tayari kwa kifo au lolote ambalo lingetokea.

    “Nasikia minong’ono sehemu hizi sijui viko wapi? Mara mbili nimesikia sauti ikiita Patrick!Patrick sijui tuko wapi hutu tutoto!” Alisema mmoja wa majambazi.

    “Mulika sehemu ambako umesikia minong’ono inatokea! Ni lazima hawa watoto wauawe!” Anorld alizidi kuamuru na majambazi walizidi kuzikanyaga nyasi ndefu katika kuwatafuta Patrick na Nancy.

    Patrick aliendelea kuwa kimya na Nancy aliendelea kutetemeka mwili mzima, dakika chache baadaye wazo lilimwijia kichwani mwake akaamua kusogea mbele, kwa sababu hakuwa na uwezo wa kumbeba kaka yake aliamua kumvuta katikati ya nyasi ni kelele za nyasi zilizowashtua majambazi mpaka wakagundua mahali walipokuwa wamejificha.

    “Hivi huku!” Alipiga kelele mmoja wa majambazi baada ya kusikia mlio wa kitu kikivutwa katikati ya nyasi na majambazi wote walikimbia kuelekea eneo hilo na tochi zao.

    *****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ilikuwa ni saa tisa alasiri siku hiyo baada ya kazi ya kupasua kuni, Anne na wafungwa wenzake walikaa ndani ya gereza wengine wakiimba nyimbo za kumsifu Mungu, mpaka wakati huo Anne alikuwa bado akilia machozi sababu ya kifo cha Zena, alikuwa bado hajauelewa ukweli, mara ghafla askari magereza wa kike alisimama mlangoni.

    “Kuna mfungwa anaitwa Anne humu ndani?” Aliuliza askari huyo.

    “Ndiyo! Ni mimi afande!” Anne aliitikia.

    “Unaitwa ofisini kwa mkuu wa gereza mara moja!”

    Anne alisimama na kuanza kukimbia kutoka nje ya gereza na kwenda moja kwa moja hadi ofisini kwa mkuu wa gereza. Mkuu wa gereza alikuwa mzee wa makamo kati ya miaka 45-50, mweusi na kichwa chake kilijaa mvi nyingi, alikuwa ni mwenyeji wa Kigoma na sura yake ilitisha kidogo.

    Hakuna mtu aliyemuogopesha Anne katika maisha yake kama mkuu huyo wa gereza! Hakutaka hata kumwona na kwa kuitwa kwake ofisini siku hiyo alijua wazi kulikuwa na tatizo kubwa sana ambalo kwa vyovyote lingepelekea kuongezwa kifungo, ilikuwa si kawaida kwa mfungwa kuitwa ofisini kwa mkuu wa gereza.

    “Sijui nimekosa nini tena mie? Sijui wamebadilisha tena kifungo changu?” Anne alijiuliza maswali mengi kabla hajafika ofisini kwa mkuu wa gereza.

    “Unaitwa nani?”

    “Mimi?”

    “Wewe ndiyo!”

    “Ninaitwa Anne!”

    “Unatakiwa kuhama gereza hili na utapelekwa gereza la Keko jijini Dar es Salaam! Hivyo utaondoka hapa Butimba kesho asubuhi!” Mkuu wa gereza alisema.

    Anne alikaa chini na kuanza kulia machozi akimwomba Mkuu wa gereza abadilishe uamuzi huo kwa sababu alikuwa na watoto ambao wangependa kumwona mara kwa mara.

    “Mungu wangu watoto wangu watanionaje huko Dar es Salaam baba? Nihurumie tafadhali” Alisema Anne, hakujua jambo lolote lililokuwa likiendelea nje ya gereza juu ya watoto wake.



    Suzanne aliwekwa maabusu kwa karibu masaa mawili akihojiwa mahali alipokuwa mumewe Anorld, mahojiano hayo yaliambatana na mateso makali akilazimishwa kusema ukweli, Alivumilia kwa muda lakini baadae alishindwa na kutoboa mahali ambako alifikiri mumewe angeweza kuwa amejificha.

    Kilichofanywa na polisi ni kumchukua ndani ya gari hadi nyumbani kwa dada yake ambako waliwachukua watu watatu akiwemo dada yake na Anorld na kwenda kufanya nao mahojiano kituoni, nao waliteswa sana mpaka kufikia mpaka wakataja kila kitu kilichoendelea.

    “Wamekwenda kuwatafuta wale watoto ili wawaue kwa sababu wanaamini ni wao ndio waliowaeleza nyinyi juu ya mpango wa kumuua mama yao!” Dada yake Anorld aliyasema maneno hayo mbele ya Suzanne baada ya kubanwa mikono na koleo!

    “Wewe uliufahamu vipi mpango huo?”

    “Nilimsikia kaka akisema kwa hasira baada ya kusikia mmemkamata mke wake, alisema ni lazima Patrick na Nancy wafe kwani ndio waliotoboa siri hiyo nilipomuuliza juu ya siri hiyo alinieleza kila kitu!”

    “Kwa hiyo wamekwenda kuwatafuta wapi?”

    “Taarifa nilizonazo wamekwenda katika makundi mawili, moja linazunguka mitaani na jingine limekwenda makaburini ambako mwili wa marehemu umezikwa wanaamini watoto hao watakuwa huko!”

    “Yeye Anorld amekwenda na kundi gani?”

    “Amekwenda na kundi lililokwenda makaburini!”

    “Ok ahsante!” Alijibu mkuu wa kituo na kuwaamuru maaskari waliokuwa karibu kuwaweka Suzanne na watu wengine waliowakamata mahabusu!

    “Tunaondoka kwenda makaburini Sawa, fanyeni hivyo haraka!” Aliendelea kusema Mkuu wa kituo cha Polisi cha kati mjini Mwanza.

    “Sawa Afande!” Waliitikia Maaskari wote.

    Mkuu wa kituo na Maaskari wengine kumi na tano waliingia ndani ya magari matatu ya polisi na safari ya kwenda makaburini kumsaka Anorld na kundi lake lilianza.

    Walipolikaribia eneo la makaburini Mkuu wa kituo alisimamisha gari lake na kushuka.

    “Vijana tumekaribia eneo lenyewe, tafadhali wekeni silaha zenu tayari na taa za magari yote zizimwe!”

    “Sawa afande!”

    “Si mnayafahamu makaburi yenyewe?”

    “Ndiyo tunayafahamu!”

    “Ok!”

    Baada ya kusema maneno hayo safari iliendelea kuelekea makaburini, taa za magari zikiwa zimezimwa na magari yakiendeshwa kwa mwendo wa taratibu ili sauti ya miungurumo yake isisikike, mita kama mia nne hivi kutoka makaburini magari yote yalisimamishwa na maaskari wote wakashuka na bunduki zao mikononi.

    “Magari yote yabaki hapa na maaskari watano wazunguke upande huu na wengine watano wapite upande huu na tutakaobaki twende moja kwa moja, nafikiri kama wapo hapa tutawakamata sababu tutakuwa tumewaweka kati!”

    “Ni lazima tuwakamate kabla hawajawaua watoto! Askari mwingine aliitikia na wote walisonga mbele.

    ******

    Makaburini



    Tochi zilizidi kumulika kila upande wa msitu wa nyasi ambamo Patrick na Nancy walijificha, majambazi waliwatafuta ili wawaue watoto wale wasio na hatia, Anorld huku akitetemeka kwa hasira alizidi kuamrisha juhudi za kuwatafuta ziongezeke! Nancy aliisikia sauti ya Anorld na kuzidi kuogopa, alizidi kulala juu ya mwili wa kaka yake bila kujua la kufanya.

    Alijua ni lazima wangekamatwa na kwa uhakika hata yeye angekufa kama alivyokuwa kaka yake! Aliamini asilimia mia moja Patrick hakuwa hai! Roho ilimuuma sana na kujikuta akitokwa machozi ya huzuni.

    Alishindwa kuelewa kama Anorld aliyewatunza na kuwalea akiwapa kila kitu ndiye aliyekuwa akiwatafuta ili awaue, lilikuwa si rahisi kulikubali na mpaka wakati huo Nancy alikuwa haamini juu ya mambo yaliyomtokea, alifikiri ilikuwa ni ndoto.

    Patrick alikuwa bado amelala akiwa kimya kabisa kama mfu. Nancy alijua tayari kaka yake alikuwa maiti, hivyo alikuwa amebaki peke yake duniani ilikuwa ni lazima apambane na maisha mwenyewe na akujua angeyaanza vipi mapambano hayo! Alipoliwaza hilo ndio alizidi kububujikwa na machozi zaidi, hakujua maisha yangeendeleaje baada ya siku hiyo bila kaka yake na pacha wake Patrick.

    Hakuwa na mama, hakuwa na baba na kwa historia aliyopewa ndugu zake wawili walifariki dunia katika mazingira ya kutatanisha ni bibi yao aliyedaiwa kufanya uchawi kuwaua na alipotaka kuwaua wao Patrick na Nancy kwa uchawi huo huo mama yao Anne aliamua kumuua kabla hajatekeleza nia yake ni jambo hilo ndilo lilimfanya aingie gerezani.

    Wakati akiyawaza hayo huku akilia, tochi zilizidi kuelekea mahali alipokuwa, mwili wake wote ulikufa ganzi na hakujua angefanya nini kuokoa maisha yake kwa sababu ndugu yake tayari alishakufa!

    “Vitoto hivi vipo wapi jamani?” Aliuliza mmoja wa majambazi

    “Vipo maeneo haya haya tu!” jambazi mwingine alijibu.

    Ghafla lilimwijia wazo kichwani mwake akiwa katika kutafuta kujiokoa, alianza kumvuta kaka yake katikati ya nyasi kutafuta mahali pengine pa kujificha, ni kelele ya nyasi ndiyo iiyowashtua majambazi na kujikuta mmoja wao akipiga kelele.

    “Jamani wale watoto hawa hapa!” Alipiga kelele mmoja wa majambazi na kelele hiyo ilisababisha majambazi wengine wote wakimbilie eneo hilo, kwa hofu bila kufikiria mara mbili Nancy alijikuta akinyanyuka na kuanza kukimbia katikati ya nyasi akiwa ameinama.

    Risasi kama tano hivi zilimfuata nyuma yake lakini bahati ya Mungu zote zilimkosa! Akazidi kutokomea katikati ya nyasi, ni milio hiyo ya risasi ndiyo iliyowafanya maaskari waliokuwa karibu na eneo hilo waweke tayari silaha zao, ilikuwa ni milio ya bunduki aina ya SMG wakati wao walikuwa na bunduki aina ya RPG! Walijua wazi kuwa milio ile haikuwa ya bunduki za zao.

    Majambazi wakiongozana na Anold walizidi kumkimbiza Nancy porini, lakini mbele kidogo Nancy alijikuta akitumbukia ndani ya shimo refu lililoonekana kuwa ni kaburi ambalo halikutumika, shimo hilo lilikuwa katikati ya nyasi nyingi kiasi kwamba majambazi hawakufanikiwa kumwona alipotumbukia.

    “Kakimbilia wapi?”

    “Sijui!”

    “Lakini si vilikuwa vitoto viwili?”

    “Ndiyo lakini kitafuteni tu ndiyo hicho kimoja kimalizeni kwanza halafu tukitafute kingine, sawa?” Anorld aliendelea kutoa amri.

    “Hakionekani tena!” Alijibu mmoja wa majambazi.

    Nancy aliyasikia maneno hayo akiwa ndani ya shimo lenye urefu kama futi 5 hivi yalizidi kumuogofya. Alitetemeka sababu ya hofu na baridi kali iliyokuwepo, alizidi kulia machozi na hali ya kukata tamaa iliutawala moyo wake, hakujua ni kitu gani kingeendelea dakika chake baadae! Kwa mara nyingine alimkumbuka mama yake

    Alipomfikiria Patrick na mahali alipomwacha roho ndiyo ilizidi kumuuma zaidi, alitamani kutoka shimoni ili nae auawe kama alivyokufa kaka yake, lakini alishindwa kutoka shimoni kwa sababu hapakuwa na mahali popote pa kushika kama msaada wa yeye kutoka nje.

    Kilichofuata Nancy akiwa shimoni ni milio mingi ya risasi, alishindwa kuelewa ni kitu gani kilikuwa kikiendelea. Alisikia sauti za watu wakilia na vishindo vya watu wakikimbia huku na kule vilisikika, Nancy hakupata jibu la kilichokuwa kikiendelea juu ya shimo hilo! Alihisi kulikuwa na mapigano makali sana yakiendelea.

    Dakika kama arobaini na tano hivi baadae hali ilitulia kukawa na ukimya wa ajabu, alisikia kitu kama mizigo ikiburuzwa juu ya ardhi na watu ikivutwa na watu waliokuwa wakinong’ona .

    “Tumewamaliza na kama Anorld asingenyoosha mikono juu naye tungemmaliza pia!” Nancy aliwasikia watu hao wakiongea.



    ******

    Mapigano kati ya polisi na majambazi aliokuwa nao Anorld yalikuwa makali kupita kiasi, majambazi wote isipokuwa Anorld walipigwa risasi na kufa papo hapo, kilichomuokoa Anorld ni kujisalimisha mbele ya polisi, maiti za majambazi aliokuwa nao zilichukuliwa na polisi kupelekwa chumba cha maiti cha Bugando ambako ziihifadhiwa .

    Hakuna askari hata mmoja aliyepoteza maisha yake katika mapambano hayo, maaskari waliuona huo kama ushindi mkubwa na hakuna askari hata mmoja aliyekumbuka kuwepo kwa watu wengine zaidi ya majambazi katika makaburi hayo, wote walisahau kuwa majambazi waliwafuata Patrick na Nancy.

    *****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Asubuhi kulipokucha taarifa za kuuawa kwa Anorld zilishasambaa mji mzima wa Mwanza, redio na televisheni zilitangaza juu ya mauaji hayo yaliyounganishwa na mauaji yaliyotokea gerezani Butimba ambayo Anorld alihusishwa nayo moja kwa moja!

    Majira ya saa mbili hivi asubuhi Nancy kwa msaada mzizi uliokuwemo ndani ya shimo hilo alifanikiwa kutoka hadi nje, alishangazwa na hali iliyokuwepo juu, nyasi zililala na damu ilitapakaa sehemu mbalimbali katika nyasi.

    Kitu cha kwanza alichofanya Nancy baada ya kusimama juu ya ardhi ni kwenda moja kwa moja hadi mahali alipouacha mwili wa kaka yake ukiwa umelala. Hakuyaamini macho yake alipokuta mwili huo haupo! Alianguka chini na kuanza kulia alijua majambazi waliuchukua na kuondoka nao, ilikuwa huzuni kubwa kwa Nancy.

    *****

    Milio mengi ya risasi iliyotawala makaburini ndiyo iliyomzindua Patrick kutoka katika hali ya kuzimia aliyoipata sababu ya hofu! Kwanza hakukumbuka mahali alipokuwa lakini muda mfupi baadae fahamu zake zilimrejea akamkumbuka kila kitu kilichotokea na pia dada yake Nancy!

    Aliangaza huku na kule lakini hakumwona dada yake mahali popote, kwa jinsi risasi zilivyolitawala anga Patrick alijua kwa vyovyote majambazi walishamuua! Naye alianza kulia akimlilia dada yake.

    Hali ilipozidi kuwa mbaya zaidi makaburini aliamua kuokoa maisha yake bila kujali kitu gani kingempata, alinyanyuka na kuanza kukimbia mbio kuelekea kwenye nyasi ndefu zaidi, alifanikiwa kutokomea bila kuonekana mbele aliendelea kutembea kwenda mbali zaidi.

    Alitembea usiku mzima kulipokucha alikuwa barabarani eneo la Usagara, njia panda ya kwenda Bukumbi! Mwili wake wote ulikuwa ukimwasha kwa sababu ya kupita kwenye nyasi zilizowasha! Mawazo yake yote yalikuwa kwa dada yake Nancy! Mpaka wakati huo hakuelewa alikokuwa na kama alikuwa hai au alikuwa amekufa!

    “Jamani Nancy dada yangu umekufa kweli?” Patrick aliongea peke yake huku akilia.

    Alijiona mtu asiye na thamani yoyote duniani bila dada yake! Hakuwa na mama, baba wala mtu yeyote aliyemfahamu kama ndugu, mtu pekee aliyemtegemea alikuwa Anti Suzanne lakini nae tayari alishawasaliti na kuamua kumuua mama yao na sasa alikuwa akitaka kuwaua wao.

    “Naondoka sirudi tena Mwanza hata shule kusoma tena sitaki mie! Nitakwenda mahali popote hata kama nikifa hukohuko sawa!” Alisema Patrick kwa uchungu.

    Siku hiyo nzima alishinda hapo hapo Usagara akifikiria akifikiria mahali pa kwenda tena bila kuwa na pesa yoyote mfukoni mwake, mchana aliosha vyombo kwa mama ntilie na kupewa ukoko akala! Watu wengi waliomuona walishangaa ni kwa nini alikuwa akilia muda wote, walipomuuliza hakuwa tayari kueleza kila kitu kwa kila mtu! Lakini alifanya hivyo kwa mzee mmoja wa Kisomali aliyemkuta ndani ya Hoteli iliyoitwa Bismillah, mzee huyo alimnunulia Patrick chakula cha usiku baada ya kumwona akilia nje ya hoteli hiyo.

    “Kwa hiyo lengo lako ni kuondoka mkoa wa Mwanza siyo?”

    “Ndiyo, nisipoondoka wataniua!”

    “Unataka kwenda wapi?”

    “Mimi?”

    “Ndiyo”

    “Nataka kwenda Dar es Salaam! Nataka nipotee kabisa sitaki kubaki Mwanza, sitaki kuona vitu vitakavyonikumbusha mama na ndugu zangu hasa dada yangu Nancy nilimpenda mno!”

    “Mimi ni dereva wa lile gari aina ya Fiat pale nje ninasafiri kwenda Dar es Salaam, leo ninalala hapa kesho alfajiri naendelea na safari yangu, nitakusaidia kufika huko Dar es Salaam, lakini una ndugu yeyote katika jiji hilo?”

    “Yupo shangazi yangu!” Patrick alimdanganya ili yule mzee azidi kumwamini zaidi.

    Mzee yule ambaye baadae Patrick aligundua aliitwa Bashir alimchukulia chumba katika hoteli aliyopanga yeye akalala, alfajiri saa 11 siku iliyofuata alimwamsha tayari kwa safari kuelekea Dar es Salaam iliyotegemewa kuwachukua karibu siku nne.

    Siku hiyo hiyo jioni walifika Nzega walichukuwa vyumba na kulala tayari kwa safari tena siku iliyofuata! Mawazo na akili yote ya Patrick ilikuwa kwa dada yake Nancy! Hakuwa na uhakika kama alikuwa hai mpaka wakati huo, safari yote hadi Nzega aliimaliza akilia.

    Dereva na utingo walijaribu kila waliloweza kumfariji lakini haikuwezekana , alinyamaza dakika thelathini na kulia masaa mawili na kila alivyolia alilitaja jina la Nancy!



    ******

    Pamoja na Anne kulia machozi akiomba abaki gerezani Butimba kumalizia kifungo chake, alishindwa kumshawishi mkuu wa gereza kukubaliana naye hivyo jioni ya siku iliyofuata alipakiwa ndani ya treni la abiria kutoka Mwanza kuelekea Dar es Salaam.

    Muda wote alilia watoto wake, alishindwa kuelewa angewaona vipi maishani mwake, alikuwa na uhakika kabisa kuwa halikuwa jambo rahisi kwa watoto wake kupata nauli za kuwafikisha Dar es Salaam, moyo wake uliumia sana.

    Aliondoka gereza la Butimba bila kuelewa ni kitu gani hasa kilichompelekea rafiki yake Zena kujiua kwa kujidunga sindano, hakuwa na ufahamu wowote juu ya kuhusika kwa ndugu yake Suzanne na mume wake Anorld katika jambo hilo na hakujua ni yeye aliyetakiwa kufa badala ya Zena !

    Aliendelea kulia akililia watoto wake pamoja na rafiki yake Zena.

    Nasikitikia sana uamuzi wa wa Zena kujiua, nilikaa nae muda mfupi sana nikamzoea!” Aliwaza Anne akiwa ndani ya treni akilindwa na maaskari jela watatu.

    Miongoni mwa watu waliopanda treni ya abiria siku hiyo ni Nancy tena bila tiketi, alikuwa ameamua kutoroka ili kuokoa maisha yake, alikuwa na uhakika asilimia mia moja kuwa kama angeendelea kukaa Mwanza ni lazima angeuawa kama alivyokuwa imepangwa! Akiwa ndani ya treni daraja la tatu alijificha chini ya kiti ili asionekane.





    Tofauti na wengi walivyoamini baada ya vyombo vya habari kutangaza kuwa Anorld alikufa katika mapigano makali kati ya majambazi na polisi makaburini, Anorld alikuwa hai na kutiwa nguvuni na polisi na yeye na mke wake Suzanne walifikishwa mahakamani wakishitakiwa kwa makosa ya mauaji ya Zena ndani ya gereza kwa kumpa chakula chenye sumu na pia mauaji ya watu wengine waliouwawa makaburini.

    Watu wengi waliomfahamu Anorld walisikitika sana kusikia Anorld alishiriki katika kitendo hicho na wengi hawakuamini, Anorld aliaminiwa sana na watu kwa sababu ya utoaji wake wa misaada kwa wasiojiweza.

    Mahakamani hawakutakiwa kujibu kitu chochote na walipelekwa mahabusu gerezani Butimba.

    Suzanne alifika gerezani akilia na kichwani mwake alifikiria kitu kimoja tu nacho ni kumuomba Anne msamaha kwa mabaya yote aliyoyafanya! Alijua wazi kitendo cha kuamua kumuua ili awachukue watoto wake hakikuwa chema na alijua bila Mungu kuepusha Anne angekuwa marehemu!

    Tayari mambo yalishawaharibikia Anorld na mke wake, yote hayo sababu ya tamaa ya kupata watoto! Wakiwa ndani ya gari la kuelekea gerezani wakiangaliana na hawakusema lolote, kila mtu alimuonea aibu na huruma mwenzake.

    Walipofika gerezani kila mmoja alishuka na kuongozwa kuelekea gerezani, Anorld alipelekwa upande wa wanaume na Suzanne alipelekwa upande wa wanawake.

    Kitu cha kwanza alichokifanya Anne baada ya kuingia gerezani ni kuanza kumtafuta Anne, alikuwa akijuta moyoni mwake kwa kitu alichokifanya! Aliulizia kwa muda mrefu bila kufanikiwa kumpata. Jioni ya siku hiyo hiyo alikutana na mama mmoja na kumuulizia yeye alionekana kumfahamu Anne vizuri!

    “Si yule rafiki yake na marehemu Zena?”

    “Ndiyo!”

    “Amehamishiwa gereza la Segerea Dar es Salaam na aliondoka jana tu hapa gerezani”

    “Eh ungu wangu eh! Nitamwona wapi Anne? Sitaki kufa bila kumuona ninajua nitafungwa lakini kabla ya hilo nataka kwanza nikutane na Anne!” Alisema Suzanne huku akilia.

    “Kwani kuna nini?” Mama aliuliza.

    “Nimemkosea sana!”

    “Umemkosea nini?”

    “Mama hayo tuyaache ila ahsante sana kwa kunisaidia” Alisema Anne na kuanza kuondoka sehemu hiyo huku akilia na kumwacha mama huyo akishangaa!

    Siku hiyo pia kama siku mbili zilizopita alilala safarini, aliumwa na kunguni na kupigwa na baridi kali! Suzanne aliumia sana moyoni na kujutia uamuzi ambao yeye na mume wake waliufikia.

    “Pesa tulikuwa nayo tungeweza hata kuzaa watoto wa kwenye chupa! Sasa maisha yetu yameishia gerezani hata Patrick na Nancy wenyewe hatukuwapata!”

    ****************************

    Lori aina ya Fiat lililoendeshwa na dereva Kisomali lilikuwa likiingia mjini Dodoma, Patrick akiwa amechoka hoi bin taban, ilikuwa ni mara ya kwanza kwake kusafiri safari ndefu kiasi hicho, njiani alishalia machozi mengi yakakauka na hatimaye kuyaona yote yaliyotokea kuwa ni sehemu ya maisha!

    Ilikuwa ni mara yake ya kwanza kuingia Dodoma usiku huo, alishangazwa na wingi wa taa alizozifananisha kabisa na mji wa Mwanza aliotoka! Zilimkumbusha mengi kuhusu nyumbani, zilimkumbusha marehemu mama yake, zilimkumbusha mengi kuhusu Mchungaji Aron na mke wake na Patrick alijua bila wao kuondoka kwenda Nairobi kisha yeye na dada yake kuhamia nyumbani kwa Suzanne yaliyotokea yasingetokea!

    Patrick alikuwa ameyaacha maisha yake yote nyuma yake, alikuwa akienda katika nchi ya ugeni ambako hakumjua mtu yeyote, hofu ilimuingia moyoni kila alipolifikiria jiji la Dar es Salaam na sifa alizopewa juu yake! Madawa ya kulevya, machangudoa, vibaka, majambazi kwa upande mwingine aliamini alikokuwa amekwenda alikuwa anafuata matatizo kama si kifo chake mwenyewe.

    Siku hiyo walilala Dodoma kama ilivyokuwa kawaida yake hakuacha kusali kabla ya kulala, dereva aliwaacha yeye na Tingo na kwenda kulala hotelini ingawa alilala kwa tabu kubwa alipata usingizi na katika usingizi wake siku hiyo aliota ndoto aliyomrejeshea faraja zake, katika ndoto hiyo alikuwa na mama yake pamoja na dada yake Nancy lakini hawakuwa watoto tena, mama yao alikuwa mzee sana na Nancy alikuwa mwanamke tajiri na yeye Patrick alikuwa mtumishi wa Mungu!

    Alifurahi sana lakini alipozinduka na kukuta ilikuwa ni ndoto aliumia na kujikuta akilia machozi.

    Hakulala tena mpaka asubuhi akilia na dereva alipokuja saa kumi na mbili asubuhi, waliendelea na safari yao kuelekea Dar es Salaam.

    “Hivi kutoka hapa mpaka Dar es Salaam ni kama kilometa ngapi?”

    “Ni kama kilometa 450 hivi, tumebakiza miji ya Morogoro, Mlandizi, Chalinze, Kibaha na Dar es Salaam yenyewe, leo hii hii saa mbili ama saa tatu usiku tutakuwa tayari tupo Dar!”

    “Mtakaa muda gani Dar es Salaam?”

    “Hatukai sana tukifika tutateremsha mzigo huu na kupakia mwingine kwenda Congo Braziville!”

    Jibu hilo lilimtisha sana Patrick aliyetegemea dereva na utingo wangebaki Dar es Salaam angalau kwa siku kadhaa wakati akijaribu kutafuta utaratibu wowote wa kuishi! Lakini yote hayo alimwachia Mungu.

    “Si ulisema kuna shangazi yako Dar?”

    “Ndiyo!”

    “Una namba zake za simu ili tukifika tumpigie aje kukuchukua?”

    “Namba zake?”

    “Ndiyo!”

    “Hapa sina ila nikizifikiria vizuri naweza kuzikumbuka!” Alisema Patrick na kujifanya kufumba macho kama mtu aliyekuwa akikumbuka kitu fulani wakati hakuwa na namba yoyote ya kukumbuka wala huyo shangazi yake pia hakuwepo!

    “Aisee mzee sikumbuki kabisa!”

    “Sasa utafanyaje maana sisi tunaweza kuondoka usiku wa leo hii hii kwenda Congo!”

    “Hiyo usijali mtaniacha tu hapo hapo Dar es Salaam nitajua la kufanya ili asubuhi niende kutafuta shangazi yangu!”

    “Anafanya kazi wapi?”

    “Anafanyakazi uhimbili hospitali” Patrick alitaja jina lililokuwa karibu yake.

    *****************************

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Tatizo la Anne kutokwa na hedhi kila siku lilikuwa bado linaendelea na yeye kama mfungwa hakuweza kujitunza vizuri, ndani ya behewa alilokaa hapakukalika abiria wote waliokuwa katika viti vya karibu na kiti alichokikalia Anne walivikimbia viti vyao! Hali ya hewa iliwashinda maafande wa magereza tu ndiyo walibaki walishindwa kuondoka kwa sababu ilikuwa kazi yao lakini hata kwao pia yalikuwa mateso.

    Anne alikaa kwenye kiti chake akilia machozi ya uchungu wa mateso aliyokuwa akiyapata, pia aliwalilia watoto wake na hakujua angekutana nao vipi! Mikono yake ilifungwa pingu! Aliyafikiria maisha yake tangu utotoni na kugundua yalijaa maumivu na machozi, hakuwahi kupata furaha yoyote katika maisha yake!

    Mume wake alikufa! Watoto wake wawili nao pia na bado mapacha wake Patrick na Nancy aliobakiza pia alikuwa ametenganishwa nao na alikuwa akisota kifungoni na ugonjwa wa ajabu uliomfanya atengwe na watu kwa sababu ya harufu aliyotoa! Alimlaumu mama yake kwa yote haya na muzimu wa uchawi aliokuwa nao!

    “Kweli mama alistahili kufa! Ni heri nilimuua!” Aliwaza Anne huku akilia.

    Wakati akiwaza hayo tayari treni ilikuwa ikiingia stesheni ya Saranda, watu wengi waliteremka na kwenda chini kununua pilau na wali na vyakula vingine vilivyouzwa stesheni hapo! Anne alibaki ndani ya treni akilalamika njaa, askari aliteremka na kwenda chini kununua chakula kwa ajili ya Anne!

    Aliporudi askari alikuwa na sahani ya pilau na glasi ya maziwa, walimfungua na kuzifunga miguuni kisha akamkabidhi sahani ya chakula alikifakamia chakula hicho na kukila kwa fujo.

    “Wamepika pilau nzuri sana hawa watu! Utafikiri ya nyumbani!” Alisema Anne na baada ya kumaliza kula alichukua glasi ya maziwa na kuimimina mdomoni na akajisikia vizuri, ni mara ya kwanza alikunywa maziwa katika muda wa miaka karibu kumi na tatu aliyokaa gerezani.



    *****************************

    Nancy chini ya kiti:

    Kwa siku mbili mfululizo Nancy alijificha chini ya kiti cha treni akiogopa kugunduliwa na wakaguzi wa tiketi kwa sababu hakuwa nayo, hakuna mtu aliyegundua kulikuwa na mtu chini ya kiti, hata abiria waliokikalia kiti hawakugundua kuwa kulikuwa na mtu chini ya kiti chao, Nancy alijibana vizuri katikati ya maboksi mawili na kulala kimya!

    Njaa ilimsumbua kupita kiasi lakini hakuwa na la kufanya ilibidi avumilie, alikuwa amedhamiria kujificha chini ya kiti hicho mpaka treni ifike Dar es Salaam! Hakuwahi kufikiria Dar es Salaam ilikuwa ni umbali mrefu kiasi gani kwa treni, alikuwa amesafiri kwa muda mrefu sana lakini bado hawakufika, mwisho alichoshwa na maumivu ya njaa kali aliyokuwa nayo!

    Mpaka treni lilipofika stesheni ya Saranda, Nancy alikuwa akilia kwa njaa kali chini ya kiti na alishindwa kuvumilia zaidi hasa alipoanza kusikia harufu ya wali kutoka kwa abiria wengine! Aliamua kujitokeza na kupambana na sura za watu mbalimbali waliomwangalia na kumshangaa!

    “Wewe binti umekaa hapo chini ya kiti tangu saa ngapi mbona hatujakuona?”

    “Tangu mwanzo wa safari!”

    “Mh! Kwanini lakini? Una matatizo gani?”

    “Nina njaa! Nisaidieni chakula kwanza!” Nancy alisema bila woga.

    “Chakula? Mbona nimemaliza hebu njoo huku!” Mama yule alijibu huku akiondoka na Nancy.

    Walishuka hadi chini ambako mama huyo alimnunulia Nancy chakula akaanza kula, kasi yake ya kula ilimshangaza sana, alionekana kuwa na njaa kali kupita kiasi.

    Kabla hata Nancy hajamaliza chakula chake vizuri katika sahani, treni lilipiga honi.

    “Malizieni tu hiyo ni honi ya kwanza!”

    “Kweli?” mama aliyemnunulia Nancy chakula aliuliza.

    “Ndiyo” Mama muuza aliitikia.

    Baadae treni ilianza kusogea mbele taratibu na Nancy aliendelea kula chakula na hiyo ilikuwa ni sahani ya pili ! Baada ya chakula wote wawili walipanda ndani ya treni kwa haraka kabla halijazidisha mwendo.

    “Lo kumbe walikuwa wanatudanganya!” Alisema mama yule wakati wakikaa vitini, Nancy alianza kujikunja ili aingie tena chini ya kiti!

    “Hapana kaa tu hapa juu ili unieleze wewe ni nani na umetoka wapi?”

    “Sina tiketi nitakamatwa!”

    “Wee kaa tu usiwe na shaka, wakikukamata sisi tutalipa!”

    Nancy alikaa kitini na kuanza kumsimulia mama huyo kila kitu kilichotokea maishani mwake, alimweleza ni kwanini alikuwa akisafiri kwenda Dar es Salaam, mama yule alisikitika sana na machozi yalimtoka bila kutegemea, hakudhani Nancy angekuwa na matatizo makubwa kiasi hicho! Kila mtu aliyesikia habari hiyo alisikitika.

    “Hiyo habari niliisoma magazetini na ilidaiwa wewe na kaka yako mlikuwa mmekufa!”

    “Hapana mimi sikufa ila kaka yangu ndiye amefariki dunia!”

    “Pole sana”

    “Ahsante!”

    “Usiwe na shaka tutakusaidia tutafika Dar es salaam mimi na mume wangu tunafanyakazi chuo kikuu cha Dar es Salaam tunatoka nyumbani Bukoba, huko ndiko nyumbani kwetu na hawa wawili ni watoto wetu Lilian na Rugarabamu” Alisema mama huyo na kumtambulisha Nancy kwa mume wake!

    **********************************

    Usiku wa saa sita treni lilingia Kilosa mkoani Morogoro, lakini hali ya Nancy haikuwa nzuri, tumbo lake lilikuwa linauma sana na hakuwa yeye tu aliyeumwa na tumbo ni pamoja na mama aliyemnunulia chakula na watoto wake pia waliumwa sana na matumbo, kila mtu alikitilia shaka chakula walichokula!

    Kabla hawajaondoka Kilosa wote walianza kuharisha na baadae kutapika! Waliharisha maji meupe sana kama maji ya mchele na kuchafua behewa! Minong’ono kuwa walikuwa na kipindupindu ilianza kujitokeza, taarifa zilitolewa kwa kiongozi wa treni na Nancy, mama Isabela, Rugarabamu na mume wake walichukuliwa na kupelekwa zahanati iliyomo ndani ya treni ambako daktari alithibitisha kuwa wote walikuwa na kipindupindu!

    Hakuwa na maji ya kutosha kuwawekea katika mishipa yao, aliwawekea chupa moja moja lakini haikusaidia kitu hali zao zilizidi kudhoofika, waliharisha na kutapika maji mengi mno! Watoto wa yule mama katika muda wa masaa mawili wakawa hawawezi hata kuongea.

    Wakati wanaingia Morogoro watoto wote wawili wa mama yule walishafariki na hali ya Nancy ilikuwa mbaya mno! Walikimbizwa haraka hospitali ya mkoa wa Morogoro ambako walilazwa na kutundikiwa dripu za maji ili kuyarejesha maji yote yaliyopotea na walipewa madawa aina ya tetracycline!

    Hali ya Nancy ilikuwa mbaya mno na hakuna mtu aliyekuwa na matumaini kuwa angepona kwa hali aliyokuwa nayo.

    Alilazwa kitanda cha kwanza kabisa katika chumba alichopewa na mama Isabela na mume wake waliwekwa chumba cha pili, ingawa hali yake ilikuwa mbaya sana Isabela akiwa katika chumba hicho alimwona mgonjwa mwingine akiingizwa yeye naye hali yake ilikuwa mbaya mno na pamoja na kuwa hoi mgonjwa huyo alikuwa na pingu mkononi na nyuma yake walikuwepo maaskari magereza watatu.

    “Huyu ni nani?” Muuguzi aliuliza.

    “Ni mfungwa amehamishwa gereza la Segerea kutoka Butimba baada ya kutoka Kilosa ghafla alianza kuharisha nafikiri ni chakula alichokula Saranda!” Alijibu askari magereza mmoja.

    Macho ya Nancy yalikuwa yamelegea na midomo ilikuwa mizito kupita kiasi, giza lilishaanza kuyaingilia macho yake, alijua huo ndio ulikuwa mwisho wake, lakini aliposikia kwa mbali maneno ya askari Magereza juu ya mgonjwa aliyeingizwa ndani ya chumba alijitahidi kufumbua macho yake ili amuone mgonjwa mwenzake! Hakuyaamini macho yake alipokuta ni mama yake na kujikuta akitamka kwa shida.

    “Ma....ma!” Aliita kwa taabu kama mara tatu lakini alizidi kuishiwa nguvu na kulegea, hakusema neno tena.

    Anne alisikia sauti ikiita mama, ingawa haikusikika vizuri lakini sauti hiyo aliifananisha na sauti aliyozoea kuisikia kabla, ilifanana na ya Nancy! Ingawa hakuwa na uhakika sana wa jambo hilo Anne aligeuza macho yake na kuangalia pembeni, alimwona mwanae Nancy katika hali mbaya.

    “Ja...ma...ni mwa...na...ngu!” Alisema Anne kwa shida na kunyoosha mkono wake, Nancy nae alinyoosha wa kwake mpaka wakashikana waliamini huo ulikuwa ndiyo mwisho wao baada ya hapo walianza kuharisha mfululizo bila kusitisha!

    “Patr..ic...yupo wa...pi!?” Aliuliza Anne kwa shida huku akiendelea kuharisha.

    “Ali...ku...fa!”

    Ingawa alikuwa mgonjwa taabani aliposikia Patrick alikufa Anne alimwaga machozi! Lakini alishukuru Mungu kukutana na mwanae angalau mmoja.





    Global outreach Mission lilikuwa ni shirika la kidini lililohubiri dini Duniani kote na liliongozwa na Mwijilisti wa Kimataifa Karl Heinz Schroden, Mjerumani mwenye mwenye umri usiopungua miaka hamsini hivi!

    Mwinjilisti huyu alizunguka dunia nzima akihubiri Injili, na kazi yake watu wengi waliokoka na kumrejea Mungu! Lengo lake lilikuwa ni kuwafikia watu milioni 200 katika muda wa miaka thelathini. Alikuwa amefanya kazi hiyo kwa miaka karibu ishirini bila kurudi nyumbani kwao Ujerumani.

    Heinz hakuwa na mke wala mtoto wala familia iliyomtegemea, kwa sababu hiyo aliamua kutumia kila alichokuwa nacho kuikamilisha kazi ya Mungu kabla ya kulala mauti.

    Watu wengi walidai Mwinjilisti Heinz alikuwa na kasoro kimaumbile ndiyo maana aliweza kuifanya kazi hiyo kwa muda mrefu bila kukumbwa na kashfa yoyote! Yeye Heinz alilikanusha sana jambo hilo kwa kudai aliitwa na Bwana kwa ajili ya kazi ya Mungu na ni yeye Mungu aliyemwezesha kufanya yote aliyoyafanya.

    Shirika lake lilikuwa kwa kasi ya ajabu, katika miaka mitano ya kuwepo kwake lilikua na kuwa shirika kubwa la Kidini kuliko mashirika mengine ya dini duniani! Mikutano aliyofanya ilijaza maelfu kwa maelfu ya watu na hapakuwa na utaratibu wa kukusanya sadaka bali ni yeye aliyegawa nguo na msaada kwa wasiojiweza waliofika mkutanoni.

    Heinz alifungua Makanisa katika kila nchi aliyokwenda, nayo pia yalikua kwa kasi kubwa! Alimiliki ndege tatu, magari ambayo hata yeye hakujua idadi yake, meli za kusafiria, kifupi Heinz alikuwa Mwinjilisti tajiri kuliko wafanyabiashara wengi na watu walishindwa kuelewa alipata wapi utajiri huo.

    Mwinjilisti Heinz aliingia Tanzania akitokea Kenya baada ya kuhubiri katika nchi za Msumbiji,Zambia, Zimbabwe, Botswana na Afrika ya Kusini, matangazo ya kuingia kwake Tanzania yalianza miezi mitatu kabla, Redio na vituo mbalimbali vya televisheni vilijipatia mamilioni ya shilingi kwa matangazo yake peke yake!

    Vituo vingine vilifikiria hata kubadili vipindi vya taarifa za habari ili kutangaza matangazo ya Mwinjilisti Heinz kwa sababu yalilipiwa pesa nyingi zaidi.

    Msafara alioingia nao nchini kupitia Namanga uliwashangaza watu wengi, alikuwa na magari aina ya Scania ya tani ishirini yasiyopungua thelathini ambayo yalibeba mizigo yake, alikuwa na magari mengine madogo ishirini yaliyobeba wafanyakazi wa shirika lake na waimbaji wa Kwaya mbalimbali alizotembea nazo kila alikokwenda duniani.

    Hiyo peke yake ilikuwa haitoshi kwani ndege mbili zilimfuata katika kila nchi aliyoingia zikileta mizigo yake mingine, mizigo hiyo iliyodaiwa kuwa misaada iliteremshwa usiku na kwa uangalizi na usiri mkubwa! Hakuna mtu hata mmoja katika watu waliosafiri nao aliyebahatika kujua mizigo hiyo ilikuwa nini na mara nyingi usiku huohuo baada ya kupakuliwa ilipakiwa ndani ya magari madogomadogo na kupelekwa kusikojulikana.

    Kila Mwinjilisti alipoulizwa jibu lake lilikuwa moja kuwa “Ilikuwa misaada kwa wenye shida!” ambalo lilitosha kuwafanya wafuasi wake waamini na kutohoji tena.

    Siku alipoingia Arusha na msafara wake hoteli zilikodiwa na shirika lake, wageni walioingia Arusha siku hiyo walilala stendi za mabasi na wengine walilazimika kwenda kulala mjini Moshi! Sifa za Mwinjilisti Heinz zilisambaa Arusha nzima katika muda wa masaa mawili!

    Alifanya mikutano kwa wiki nzima mjini Arusha akaondoka na kuelekea Moshi ambako alifanya tena mkutano kwa wiki nzima na baadaye kuingia Dar es Salaam, katika mikutano yake watu walipokea miujiza ya ajabu na aliwashangaza watu kwa uwezo wake wa kuwagusa puani kwa mikono yake wakaanguka chini na kupoteza fahamu na kusikia raha ya ajabu mioyoni mwao.

    Kilichowashangaza wengi baada ya baada ya kuguswa puani siku iliyofuata walitaka kuguswa tena na walipoguswa walisikia raha ileile kama waliyosikia siku moja kabla hatimaye wengi wakawa hawawezi chochote mpaka wameguswa puani na Mwinjilisti Heinz! Wengi waliamini hiyo ilikuwa nguvu ya Roho Mtakatifu!

    Ni siku hiyohiyo aliyoingia Dar es Salaam ndiyo pia Patrick aliingia ndani ya jiji hilo la maraha akitokea Bara, gari alilokuja nalo kwa msaada wa dereva wa Kisomali liliteremsha mizigo usiku huohuo likapakia mizigo mingine na kuondoka kuelekea Kongo kupitia Tunduma! Patrick alisikitika sana lakini alimshukuru sana dereva wa gari hilo kwa msaada wake!

    Ingawa alikuwa mgeni jijini usiku wa siku hiyo Patrick alilazimika kutembea hadi ufukweni ambako alilala ndani ya mtumbwi mbovu huku akiumwa na mbu na kupigwa na baridi kali! Usiku mzima Patrick hakupata usingizi akijaribu kuyafikiria maisha yake tangu utotoni na mateso aliyoyapata!

    Alipomkumbuka mama yake Anne pamoja na dada yake Nancy alishindwa kujizuia na kujikuta akilia machozi! Mpaka wakati huo Patrick hakujua kuwa aliyekufa gerezani hakuwa mama yake bali Zena, aliamini mama na dada yake hawakuwa hai na alikuwa peke yake duniani!

    Mawazo hayo yalimfanya Patrick aumie sana moyoni mwake na kuona alikuwa ni mtu asiye na thamani duniani, aliichukia Tanzania na kuwaona watu wote hawafai.

    “Hakuna ninaloweza kufanya hapa duniani zaidi ya kumfuata Yesu Kristo peke yake! Ni yeye ndiye anayeweza kuwa mfariji na rafiki yangu wa kweli, sina mwingine wa kurejesha furaha yangu isipokuwa yeye!’ Aliwaza Patrick huku akilia.

    *****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Asubuhi ya kwanza jijini

    Dar es Salaam:

    Kulipokucha asubuhi Patrick alitoka ndani ya mtumbwi mchafu aliolala na kuamua kuingia mitaani kutafuta lolote! Ilikuwa ni mara ya kwanza kwake kuwa katika mji mkubwa kama Dar es Salaam alishangaa karibu kila kitu alichokiona hasa maghorofa marefu yaliyokuwepo maeneo ya posta!

    Hakujua mtu yeyote ndani ya jiji hilo na hakujua aanzie wapi kwa sababu kila sehemu zilifanana! Asubuhi hakuwa na uhakika wa kufungua kinywa chake lakini bado aliamini asingeweza kufa katika nchi ambayo watu walikula na kusaza, alijua lazima ilikuwepo njia ya yeye kuishi ambayo Mungu pekee aliijua!

    Ilipofika saa saba ya mchana alikuwa maeneo ya Kariakoo, kila kitu kilishamchanganya hakuelewa ni wapi kulikuwa Mashariki,Magharibi, Kaskazini wala Kusini! Hakuelewa alikokuwa akitoka wala alikokuwa akielekea! Alikwenda tu kama kitu kilichosukumwa na upepo.

    Baada ya kuzunguka sana ghalfa alijikuta amesimama kwenye mnara wa askari, Patrick aliiangalia sanamu ya askari yule kwa muda mrefu na hakuona taabu wala aibu kwa jinsi watu ndani ya magari yaliyopita kwenye mzunguko wa mnara huo walivyomshangaa kwani aliamini alikuwa akijaribu kulizoea jiji la Dar es Salaam taratibu!

    Huku njaa ikimuuma alipotoka kwenye mnara wa askari alinyoosha moja kwa moja kupitia barabara za Azikiwe na Maktaba na kujikuta kwenye makutano ya barabara ya Maktaba na Bibi Titi, kwa muda aliyashangaa mataa ya kuongozea magari yaliyokuwepo katika makutano ya barabara hizo lakini baadaye alikata kushoto na kuelekea Akiba!

    Alipofika kwenye makutano ya barabara ya Bibi Titi na Morogoro alisimama chini ya mti mkubwa nje ya chuo cha Ufundi Dar es Salaam na kuanza kuwaza ni wapi angepata chakula cha mchana huo kwani njaa ilikuwa ikimsumbua kupita kiasi!

    “Nitajikaza sababu mimi ni mwanaume isitoshe riziki ya mbwa ipo miguuni mwake!” Patrick alijisemea moyoni na kusonga mbele kufuata barabara ya Morogoro akielekea kituo cha mabasi cha Faya!

    “Hivi hapa ndipo kwenye ofisi ya umoja wa vijana? Hapa kumbe ndipo zilipo ofisi za Nchimbi? Nikishindwa kabisa nitamtafuta hata yeye anisaidie hela ya kula! Ingawa hanifahamu, nitajieleza kwake nafikiri hataninyima hata mia mbili!” Patrick alijisemea moyoni mwake wakati akilipita jengo la Umoja wa vijana kulia kwake.

    Alipofika kituo cha Faya alikuta watu wengi wakisubiri usafiri wa daladala kuwarudisha majumbani kwao!

    “Haya, Sinza, Sinza! Sinza wahi gari!” Mpiga debe alipiga kelele kuwaita abiria wakati gari lake likiegeshwa.

    “Ndiyo niliwahi kusikia hapa Dar es Salaam kuna Sinza tena na yule mwanamuziki Remmy anakaa hukohuko!” Aliwaza Patrick na hakusimama kituoni hapo alizidi kusonga mbele na kuzipita taa za kuongozea magari za Faya.

    Mbele alishangaa kuona makundi makubwa ya watu wakitembea kwa miguu kuelekea bondeni wengi wakiwa akinamama na watoto!

    “Masikini sijui hawa wamekosa nauli?” Aliwaza Patrick lakini alipowaangalia mikononi mwao aliwaona wakiwa na Biblia.

    “Nafikiri wanakwenda kanisani, lakini leo mbona siyo Jumapili?” Alijiuliza Patrick.

    Ghafla mawazo yake hayo yaliingiliwa na sauti ya kipaza sauti kikiongea kwa sauti ya juu! Alisikia sauti za watu wakiimba nyimbo za kumsifu Mungu!

    “Njoo kwa Kristo, Kristo anaokoa!” Patrick aliyasikia maneno hayo ndani ya wimbo ulioimbwa.

    “Namshukuru Mungu hiki ndicho kitu nilichokuwa nakitaka!” Patrick alisema na bila hata kusita alianza kuwafuata watu waliotembea katika makundi kuelekea bondeni.

    “Karibuni katika viwanja vya Jangwani mmsikilize mtumishi wa Mungu Karl Heinz kutoka Ujerumani, leo yupo hapa! Njooni nyote mpokee uponyaji yaleteni matatizo yenu yote kwa Bwana!” Sauti ilisikika kwenye kipaza sauti.

    Bila hata kutegemea Patrick alisikia furaha ya ajabu moyoni mwake alitembea na kujichanganya katikati ya watu na kusogea mbele zaidi ingawa ilikuwa ni kwa taabu kubwa! Aliimba nyimbo za mapambio na kurukaruka pamoja nao.Siku hiyo alijisikia kuutua mzigo uliokuwa kifuani mwake.

    Baadaye Mwinjilisti Karl Heinz alisimama na kulihubiri neno la Mungu, karibu kila alichokiongea katika mahubiri yake kiliyagusa maisha ya Patrick moja kwa moja na alipoongea juu ya kifo na mauti Patrick alijikuta akiwakumbuka mama na dada yake.

    Patrick alipiga magoti chini na kusali huku akilia machozi, akiwaombea mama na dada yake kwa Mungu ili awaweke mahali pema mpaka siku ambayo angekutana nao tena!

    Ilikuwa ni huzuni kubwa sana kwa Patrick lakini alipokumbuka kuwa tayari alikuwa ndani ya Kristo alijisikia amani na furaha ikirejea kubwa moyoni mwake.

    Mkutano ulipokwisha Patrick alisikia msukumo wa kutaka kumwona Mwinjilisti Karl Heinz, ingawa alijua ilikuwa kazi ngumu lakini aliamini kama angefanikiwa ni lazima angemwonyesha ni kwa jinsi gani angeweza kuwa mtumishi wa Mungu jambo alilotamani kulifanya!

    “Nitamwona tu!” Alisema Patrick na kuanza kujongea mbele kuzunguka nyuma ya jukwaa ambako alikutana na mmoja wa shemasi waliohudumia katika mkutano huo.

    “Bwana asifiwe mpendwa?” Patrick alimsalimia shemasi huyo.

    “Ameeeni! hujambo mpendwa?”

    “Sijambo!”

    “Unauonaje mkutano huu?”

    “Kwa kweli nimebarikiwa sana na ninatamani kuonana na mtumishi wa Mungu Heinz kwani ameyagusa sana maisha yangu!”

    “Kweli?”

    “Ndiyo!”

    “Basi subiri, ingawa najua ni shida sana kumwona, hivi sasa bado anafanya maombi kwa wagonjwa!”

    “Una kalamu na karatasi hapo mpendwa?” Partick aliuliza.

    “Ndiyo!”

    Shemasi alinyoosha mkono na kumpatia Patrick kalamu na karatasi pamoja na Biblia kugandamizia, akaanza kuandika ujumbe wa Kiingereza kwa mwinjilisti Karl Heinz.

    “Ninaitwa Patrick Huggins, ni kijana mdogo na Mungu amesema na mimi jambo ambalo ni muhimu sana niongee na wewe!

    Ni mimi.

    Patrick

    Patrick alimaliza kuandika barua hiyo na kumkabidhi shemasi.

    “Tafadhali mpendwa mkabidhi tu barua hiyo mimi nasubiri huku nyuma!”

    “Sawa!”

    Shemasi aliondoka kwenda jukwaani ambako aliikabidhi barua hiyo kwa mchungaji mwenyeji wa mkutano ambaye alikaa nayo mkononi akisubiri Mwinjilisti Heinz amalize kuombea wagonjwa ndipo akamkabidhi barua akaanza kuisoma!

    “Where is this boy?”(Mvulana huyu yupo wapi?)

    “Behind the Platform!”(Nyuma ya jukwaa)

    “Bring him forward I want to talk to him!”(Mleteni mbele, nataka kuongea naye)

    Mchungaji mwenyeji aliteremka akikimbia na kwenda nyuma ya jukwaa kumwangalia Patrick.

    “Wewe ndiyo Patrick?”

    “Ndiyo!”

    “Tafadhali njoo mtumishi wa Mungu anataka kuongea na wewe!”

    Patrick hakuamini ingekuwa rahisi kiasi hicho kuonana na mhubiri mkubwa kama Kart Heinz.

    Patrick alipandishwa jukwaani na kupewa kiti akakaa na kusubiri Mwijilisti Karl Heinz amalize kuhubiri, njaa yote aliyokuwa nayo Patrick iliyeyuka alijisikia kushiba bila kujua chakula kilitokea wapi!

    “Are you Patrick?”(Wewe ni Patrick?) Mtumishi wa mungu Kart Heinz alimuuliza Patrick alipomfikia.

    “Yes I’m, I cant believe I’m talking to the great servant of God!”(Ndiyo ni mimi na siamini kama ninaongea na wewe mtumishi wa Mungu!)

    “ Can we talk here?Or you need more Privacy?”(Unataka tuongee hapa au unahitaji faragha zaidi?)

    “I need to talk to you alone!”(Nataka kuongea na wewe peke yako)

    “Sure!”(Hakika?)

    “Yes!”Ndiyo)

    “Then come inside with me!”(Basi nifuate ndani) Kart Heinz alimwambia Patrick na wote wawili waliteremka jukwaani na kwenda moja kwa moja ndani ya hema moja lililokuwa na kila kitu kilifanya liitwe ofisi.

    “This is my temporally office!”(Hii ni ofisi yangu ya muda)

    “Oh it is very nice office!”(Oh! Ni ofisi nzuri)

    “Sure?Thanks God!(Hakika? Ninamshukuru Mungu)

    Baada ya kujitambulisha kwa Mwijilisti Patrick alianza kumsimulia kila kitu kilichotokea maishani mwake, kufiwa na wazazi wake ndugu zake na baadaye dada yake mpendwa Nancy! Na alieleza nia yake ya kutaka kumtumikia Mungu na kuokoa roho za watu wengi waliopotea, alimwomba Mwijilisti Heinz amsaidie kutimiza ndoto yake.

    “I’m very poor, but I always wanted to be an Evangelist and save people’s lives! Please help me!”(Mimi ni masikini lakini siku zote nimetaka kuwa Mwijilisti nihubiri neno la Mungu na kuokoa maisha ya waliopotea, tafadhali nisaidie kutimiza ndoto hiyo) Alisema Patrick Mwijilisti Kart Heinz alitokwa na machozi.

    “So you are an orphan?”(Kwa hiyo wewe ni yatima?)

    “In the world I’m an orphan, but in Heaven I’m not because I have Jesus Christ!”(Hapa duniani mimi kweli ni yatima lakini mbinguni mimi si yatima kwa sababu ninaye Yesu Kristo)

    “So where do you stay in the city?”(kwa hiyo hapa jijini unaishi wapi?)

    “I have no where to stay! I arrived yesterday and slept at the beach in a decaying boat!”(Sina mahali pa kuishi hapa jijini, niliingia jijini jana na nililala ufukweni kwenye moja ya boti inayooza)

    Mwijilisti Karl Heinz alichukua kitambaa chake na kufuta machozi yaliyokuwa yakimtoka na kulowanisha usoni, alikuwa ameumizwa sana na habari ya Patrick! Aliguswa sana na kujisikia kumsaidia Patrick.

    “Patrick I will help you fulfil you dream! will make sure you have a Passiport,and will be travelling with you wherever I go” (Patrick nitakusaidia kutimiza ndoto zako, nitashughulikia hati yako ya kusafiria na tangu sasa nitasafiri na wewe kila ninakokwenda)

    “Thanks! Thanks!Thanks!”(Ahsante! Ahsante! Ahsante!) Patrick alisema huku akilia kwa furaha.

    *****

    Anne, Nancy hospitalini:

    Hali za wagonjwa zilikuwa bado mbaya,Anne na Nancy walikuwa bado wakiharisha na kutapika sababu ya kipindupindu! Dawa za kutibu ugonjwa huo zilikuwa zimekwisha hospitali ya Mkoa wa Morogoro na ziliagizwa kutoka jijini Dar es Salaam na kuwaacha Anne na Nancy katika hali mbaya na bila dawa, walilala vitanda jirani mikono yao ikiwa imeshikana na kung’ang’aniana! Hakuna aliyeongea kati yao wote walijua kifo chao kilikuwa kimefika.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ngozi zao zilikuwa nyembamba na zilichukua muda mrefu sana kurudi zilipominywa wauguzi, nyama zao zilikakamaa mwilini kupita kiasi.

    “Wapo dehydrated mno na sijui tutaokoaje maisha yao sababu kila tunapowapatia ORS wanatapika!” Alisema muuguzi akimwambia mwenzake aliyekuwa jirani alimaanisha kila walipowapa maji ya chumvi walitapika.

    “Waliofuata dripu Dar es Salaam nao wamechelewa mno sijui kifanyike kitu gani kuokoa maisha ya wagonjwa hawa!”

    “Tunahitaji dripu zenye sodium chloride ziingie katika mishipa yao hapo watapona kama wangekuwa na pesa tungekwenda kuwanunulia kwenye duka la dawa wakati tukisubiri dawa zetu zifike bila hivyo watakufa tu!” Muuguzi mwingine alijibu.

    “Kwani wale wenzao wawili mtu na mke wake wako wapi?”

    “Si unaamanisha yule mama aliyekuwa akiongea kihaya?”

    “Ndiyo!”

    “Amefariki muda mfupi uliopita!”

    “Kwa hiyo wote wamefariki maana watoto wao pia walifariki hapahapa hospitalini muda mfupi baada ya kufika!”

    Nancy aliyasikia maongezi hayo ya wauguzi kwa mbali sana, mwili wake haukuwa na nguvu kabisa na macho yake yalifunikwa na giza nene, kitu pekee alichokikumbuka kilikuwa ni mkono wake wa kushoto uliokuwa umekamatana na mkono wa mama yake wote walikuwa katika hali ya kufa!

    Mwili wa Nancy ulikuwa umelegea kupita kiasi, alishindwa hata kujigeuza kitandani akisubiri dakika yake ya mwisho ifike! Aliamini hapakuwa na njia ya kuyaokoa maisha yake na mama yake hasa aliposikia kuwa mama Rugarabamu na mumewe tayari nao walishafariki dunia!

    Alitamani sana kupona ili ajue ni kitu gani kilitokea mpaka mama yake akawa hai wakati hata kaburi lake waliliona, lakini haikuwepo tena nafasi ya kulijua jambo hilo kwani alitakiwa kufa wakati wowote

    “Mimi na mama tunamfuata Patrick, familia yetu yote imekwisha duniani!” Aliwaza Nancy.

    *****

    Mafia Drug Traffikers:



    Lilikuwa kundi maarufu la uuzaji wa madawa ya kulevya na mauaji duniani, lilianzishwa miaka ya 1900 huko Mirano, Italia. Lilikuwa na matawi sehemu nyingi sana duniani ikiwemo Ujerumani, Uingereza, Marekani, Nigeria, Tunisia, Brazil, Chile na katika nchi hizo walichaguliwa wawakilishi walioitwa Presdento! Ni hao ndio waliohakikisha madawa yanaingia katika nchi zao na kuyasambaza kisirisiri bila mtu yoyote kugundua, Mapresdento wa nchi nyingine walikuwa ni viongozi kama Mawaziri, Makatibu wakuu na hata Maraisi wa nchi zao.

    Biashara ya madawa ya kulevya ilikuwa ni biashara haramu iliyopigwa vita karibu kila pembe ya dunia, katika nchi za Kiarabu watu wote waliofanya biashara hiyo walipigwa risasi ama kuchinjwa hadharani walipokamatwa lakini pamoja na hali hiyo watu hawakuacha kuifanya biashara hiyo ingawa kila siku walikamatwa na kupigwa risasi hiyo yote ilikuwa ni kazi ya kundi la Mafia drug Traffikers.



    Heinz Luminie, Berlin 1947



    Heinz Luminie alikuwa Presdento wa Mafia nchini Ujerumani, baada ya njia nyingi za kusafirishia madawa kugundulika na wafuasi wengi kukamatwa, kufungwa na wengine kuuawa Heinz alibuni mpango wa kuyasafirisha madawa haya kupitia mkondo wa kofia ya dini! Alielewa mizigo ya Wamisionari haikukaguliwa bandarini au katika viwanja vya ndege na wala haikutozwa ushuru.

    Ulikuwa ni mpango wa muda mrefu sana kuutekeleza lakini ilikuwa ni lazima afanyike baada ya miaka mingi. Heinz alikuwa baba wa watoto wawili wa kike na mwingine wa kiume, wa kike aliitwa Patricia na wa kiume aliitwa Karl ni huyo ndiye aliyetegemewa kuja kuwa mrithi wa maliz zote za Heinz Luminie.

    “Nitahakikisha siku moja Karl anakuwa mfanyabiashara wa madawa kwa kupitia kofia ya dini!” Aliwaeleza wanachama wa Mafia katika mikutano yao.

    “Utalifanyaje hilo?”

    “Nitamlea katika mzingira ya kidini, nitampeleka katika shule za Biblia ili aje kuwa mhubiri maarufu duniani ni yeye atayesafirisha mizigo yetu yote kokote duniani na hakuna mtu atakayegundua jambo hilo!” Aliongea kwa uhakika Heinz.

    “Inawezekana fanya basi!”

    ****

    Katika umri wa miaka 12 tu Karl alipelekwa katika chuo cha Berlin Theological Institute kusomea mambo ya dini, yote hayo yalifanyika kumwandaa kuja kuwa mwinjilisti wa kimataifa. Karl aliwashangaza walimu wake kwa uwezo aliokuwa nao darasani, alisoma kwa bidii kubwa na kufanya vizuri sana katika masomo yake yote.

    Pamoja na hayo Karl hakupenda kuwa Mwinjilisti, katika maisha yake alitaka sana kuwa Mwanasheria au daktari lakini sababu baba yake alimlazimisha kusoma masomo ya Uinjilisti hakuwa na la kufanya zaidi ya kukubali na kila siku aliyakumbuka maneno ya baba yake.

    “Unasoma Uinjilisti si kuwa Mwinjilisti bali kutimiza kazi fulani ambayo nitakuja kukupatia baadaye maishani, kazi ambayo siku zote itakufanya kuwa tajiri kuliko binadamu yeyote!”

    “Sawa baba lakini kazi gani hiyo?”

    “Siwezi kukuambia sasa hivi soma kwanza na ni lazima uifanye vinginevyo utauawa!”

    “Nitauawa? Kazi gani hiyo baba mimi napaswa kuifahamu!”

    “Haiwezekani kuifahamu sasa hivi!”

    Maongezi hayo kila siku yalimsumbua Karl akilini mwake na kwa sababu ya kuogopa kuuawa alisoma kwa bidii.

    ****

    Akiwa na umri wa miaka 23 Karl alifanikiwa kumaliza masomo yake ya teolojia na kupata digrii zake tatu, jina lake likabadilika akawa Dr Karl Heinz!

    Ilikuwa ni furaha kubwa mno kwa baba yake, alijua mtoto wake kumaliza masomo hayo kulimaanisha kazi yake kukamilika, alikuwa na uhakika dawa za kulevya aina ya Cocaine, Heroine na Mandrax ambazo kundi la Mafia lilisambaza zingefika mbali sana duniani bila mtu kukamatwa au kutiliwa mashaka na hivyo wangetajirika kupita kiasi.

    ****

    Ulikuwa ni wakati wa kiangazi katika jiji la Berlin, jua la kawaida lilitawala angani na kuufanya mji kutokuwa na baridi hata kidogo, hali hiyo ilimfurahisha karibu kila mkazi wa jiji hilo lenye baridi. Jioni hiyo Karl alikaa na baba yake ndani ya chumba kidogo chenye mwanga duni, walikuwa wawili tu ndani ya chumba hicho! Dada yake Patricia alikuwa shuleni na mama yake alishafariki miaka kumi kabla ya siku hiyo kwa kuzama na boti baharini alikokwenda kuogelea wakati wa Sikukuu ya pasaka.

    Mzee Heinz alimwita mtoto wake ili kumweleza ni kwanini alimlazimisha kwenda kusomea Uinjilisti! Karl pia alikuwa na nia sana ya kulifahamu jambo hilo kwani kwa muda mrefu alimuuliza baba yake lakini hakupewa jibu hiyo ilikuwa siku aliyoisubiri kwa hamu kubwa!

    “Mwanangu Karl!” Alianza mzee Heinz na maongezi yao yalifanyika katika lugha Kijerumani.

    “Ndiyo baba!”

    “Leo nataka nikueleze kitu ambacho hukuwahi kukisikia na kama ulishakisikia basi haukuwa na uhakika, nataka nikueleze ni kwanini niliamua usomee Uinjilisti!!”

    “Nakusikia baba!” Karl Aliendelea kumwitikia baba yake.

    “Tafadhali niahidi kuwa siri nitayaokueleza hapa hautaisema mahali popote!”

    “Nakuahidi baba!”

    ”Mwanangu mimi ni mwanachama wa Mafia na biashara yangu ni madawa ya kulevya!”

    Moyo wa Karl ulipasuka paa na mapigo kubadilika, alianza kuhisi jasho likimtoka kwani hakuwahi hata siku moja kufikiri kuwa baba yake aliyeonekana mpenda dini angeweza kuwa mwanachama wa kundi hilo hatari la wauaji.

    “Baba unasema kweli?”

    “Ndiyo mwanangu na hutakiwi kusema kwa mtu yoyote ukisema tu utauawa wanachama wenzangu watakunywa damu yako!”

    “Ndiyo nimekusikia baba sasa ni kwanini ulinipeleka kusoma Uinjilisti?”

    “Nilitaka uje kufanya hii kazi ninayoifanya!”

    ‘Kazi ya kuuza madawa?”

    “Ndiyo!”

    “Siwezi baba mimi sasa namfahamu Mungu siwezi kufanya biashara hiyo!”

    “Karl!Karl! Karl! Unakaidi maagizo yangu?” Alisema mzee Heinz akiwa amepandisha hasira yake kupita kiasi.

    “Siyo hivyo baba nasema ukweli wangu!”

    Hapakuwa na maelewano kati yao na walitoka chumbani bila kufikia muafaka. Jioni ya siku iliyofuata Karl akitembea mjini alikamatwa na watu wasiojulikana akafungwa kitambaa machoni na kupelekwa mahali kusikojulikana ambako alipewa mateso ya kutikiswa na umeme kwa usiku mzima na kulipokucha asubuhi baba yake alifika na kuongea naye tena, Karl alikubali kuifanya kazi hiyo.

    Wiki mbili baadaye shirika la Global Outreach Mission lilianzishwa nchini Ujerumani, mwinjilisti kijana Karl Heinz mwenye umri wa miaka 23 akawa kiongozi wake, kwa siri kubwa shirika hilo lilifadhiliwa kila kitu na kundi la mafia! Lengo la kundi hili kwa nje lilikuwa ni kuzunguka dunia nzima kuhubiri dini lakini kwa ndani lilikuwa shirika la kusambaza madawa ya kulevya duniani.

    Ratiba za safari za shirika hilo zilipangwa na kundi la Mafia, Karl Heinz alisafiri kwenda katika nchi ambazo Mafia walitaka kupeleka madawa yao. Hakuipenda kazi hiyo lakini ilibidi aifanye kwa sababu aliogopa kuuawa! Alifundishwa jinsi ya kuushika unga wa Cocaine katika mikono na kuwagusa watu puani wakati wa maombi ili walewe madawa na kuamini alikuwa na miujiza ya Mungu.

    Alifundishwa pia kuchukua kitambaa na kukipaka unga wa dawa aina ya Heroine kalina alipompiga mtu na kitambaa hicho usoni alilewa na kuanguka chini na aliponyanyuka alikuwa na furaha isiyo kifani sababu ya madawa hayo kulevya.

    Mambo hayo yalimpa sifa kubwa Mwinjilisti kijana Dr.Karl Heinz na kufahamika dunia nzima, kila alikokwenda kuhubiri maelfu ya watu walikusanyika kumsikiliza, katika kila nchi aliyokwenda ilikuwa ni lazima ndege mbili za madawa ya kulevya zimfuate na kushusha mizigo usiku, hakuna mtu aliyetilia mashaka wala kufuatiliwa wengi waliamii ilikuwa ni misaada aliyogawa kwa wasiojiweza.

    Karl Heinz aliheshimiwa mpaka na viongozi wa serikali katika nchi nyingi duniani, alikaribishwa Ikulu katika kila nchi aliyokwenda na kula chakula na Marais, aliwapa viongozi wa Afrika pesa nyingi kwa ajili ya maendeleo lakini hakuna mtu aliyeijua siri ya utajiri wake.

    Kilichowashangaza watu waliosafiri naye ni kitendo cha kila mtu aliyeteuliwa kuwa msaidizi wake kuchanganyikiwa na kuwa mwehu baada ya kufanya kazi kwa kipindi kirefu na baadaye kukutwa amekufa! Hapakuwepo na maelezo ya kutosha kuhusu vifo vyao, wasaidizi karibu wanne walishakufa kwa mtindo huohuo na Patrick ndiye msaidizi wake wa tano!

    Siri ya vifo hivyo vya wasaidizi hao hakuna aliyeielewa isipokuwa Mwinjilisti Karl Heinz mwenyewe, ukweli ni kwamba aliwaua baada ya kuigundua siri yake ya madawa na kuanza kuhoji! Aliwapulizia dawa aina ya Pedraxone iliyowachaganya akili na kuwatia wehu na baada ya hapo aliwatilia sumu katika chakula na kuwaua! Karl Heinz hakutaka hata siku moja siri yake igundulike.

    *****

    “Nimefurahi sana kukutana na wewe mtumishi wa Mungu!” Alisema Patrick huku akitabasamu na alisema hayo kwa kutokujua ubaya wa Dr Karl Heinz, alikuwa mnyama na mkatili lakini dunia haikuelewa na haikuwa rahisi hata siku moja kulifahamu jambo hilo kwa sababu Mwinjilisti Karl alijificha chini ya mwavuli wa dini!

    “Unaweza kutunza siri lakini kijana?”

    “Naweza mtumishi wa Mungu!”

    “Tafadhali kumbuka hutakiwi kusema chochote cha ajabu utakachokiona sawa?”

    “Sawa mtumishi wa Mungu!” Aliitikia Patrick.

    *****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wodini:

    “Blandina hivi hauna pesa kidogo tukanunue angalau chupa kadhaa za dripu wakati tunasubiri dawa zetu zifike?” Muuguzi alimuuliza mwenzake.

    “Ninayo shingili 5000 na tunaweza kuitumia tu!”

    “Basi acha mimi nikaongee na daktari ili tununue maji kwenye duka la dawa vinginevyo hata hawa nao watakufa!’

    Baada ya kusema maneno hayo muuguzi alitoka mbio kuelekea ofisini kwa daktari lakini kabla hajafika alikutana na wauguzi wengine wakikimbia kuelekea katika chumba alichotoka muuguzi huyo.

    “Vipi hali za wagonjwa?”

    “Ni mbaya sana sista, nilikuwa nakwenda kumwomba daktari tukanunue angalau maji ya dripu kwenye duka la dawa!”

    ‘Hapana twende tu wodini dawa zimeshakuja!”

    Walisaidiana na kuanza kutembea kwa haraka kurudi tena wodini ambako walimkuta Nancy na Anne katika hali mbaya kupita kiasi, walitundika chupa za maji na kuzichomeka katika mshipa yao ya damu zikaanza kutiririka kwa kasi kubwa ili kufifia maji yaliyopotea miilini mwao.

    Kila chupa ilipoisha ilibadilishwa na dawa walizopewa kwa mdomo na kuzitapika zilianza kupitishwa katika mishipa ya damu, kwa masaa arobaini na nane ya kutumia maji na dawa hali zao zilianza kubadilika na kuwa nzuri, ngozi zao zilianza kupendeza na kujaa badala ya kusinyaa! Fahamu zilianza kuwarejea akilini.

    Siku ya tatu Nancy alipopata nguvu vizuri alijigeuza na kuagalia upande wa pili wa kitanda chake, alikutanisha macho na sura ya mama yake akimwangalia na kutabasamu!”

    “Nancy mwanangu!”

    “Naam mama!”

    “Tumenusurika na kifo kwa uwezo wa Mungu!”

    “Kweli mama, wenzetu wote wamekufa!”

    “Umejuaje?”

    “Nilisikia kwa mbali manesi wakiongea!”

    Hawakuweza kuongea sana siku hiyo sababu miili yao haikuwa na nguvu za kutosha lakini siku ya tano wakiwa wodini walikuwa wazima kabisa, hawakuharisha wala kutapika tena, kila mtu hospitali alishangazwa na muujiza uliotokea.

    *****

    Mama ilikuwaje ukawa mzima wakati hata kaburi lako tuliliona nani alikufa?”

    “ Sikufa mimi alikufa rafiki yangu Zena, alijichoma sindano ya sumu!”

    Pamoja na kuwa Anne kufurahi sana kutana na Nancy, bado alitaka kufahamu ni wapi alikokuwa mtoto wake wa kiume Patrick, alipojibiwa kuwa Patrick alikufa, alidondosha machozi ya huzuni.

    ******

    Siku ya sita maaskari wa magereza walimfunga Anne pingu zake mikononi na safari ya kuelekea gereza la Segerea iliendelea, Nancy ilibidi aungane nao katika safari moja. Walipoingia Dar es Salaam Anne alipelekewa moja kwa moja gerezani Segerea, ambako alipokelewa kama mfungwa lakini kote huko Nancy alifuata kwa nyuma.

    “Mwanangu Nancy utakwenda wapi sasa?”

    “Sitaki kuondoka nataka nikae na wewe mama!” Alisema Nancy huku akilia machozi.

    “Huwezi kukaa na wewe mimi gerezani mwanangu!” Alijibu Anne na kuanza kuvutwa na maaskari kuingizwa gerezani.

    “Mama!Mama! Mama!” Aliita Nancy.

    Nancy alikaa chini na kuanza kulia hakujua aende wapi baada ya kutoka gerezani, alitembea hadi barabarani ambako alisimama na kuanza kulia machozi, njaa ilimuuma kupita kiasi na hakujua angepata wapi chakula cha mchana huo.

    Ghafla aliona gari dogo aina ya Pickup likija mbele yake, Nancy alisogea hadi katikati ya barabara na kuanza kulisimamisha,gari hilo.

    “Shikamoo dada!” Nancy alimwamkia mwanamke aliyekuwa akiendesha gari hilo liliposimama na baadaye alimwamkia mwanaume aliyekaa upande wake wa kushoto!

    “Naomba shilingi mia nikale nina njaa dada!”

    “Baba Teddy una mia tano hapo?” Mama huyo alimuuliza mwanaume aliyeonekana kuwa mumewe aliyekaa pembeni akisoma gazeti la Amani.

    “Sina darling nina kubwakubwa tu!”

    “Ingia kwenye gari twende pale mbele ukale hotelini!” Mama yule alisema na Nancy alianza kupanda nyuma ya gari hilo.

    “Hapana njoo ukae huku mbele!” alisema mwanaume huyo na kufungua mlango, Nancy akaingia na kukaa katikati yao.

    “Mimi naitwa mama Teddy na huyu ni mume wangu anaitwa Kidubo wewe unaitwa nani binti!”

    “Ninaitwa Nancy!”

    “Jina zuri sana unakaa wapi hapa Segerea?”

    “Mimi ni mgeni!”

    “Mgeni kutokea wapi?”

    Alipoulizwa swali hilo Nancy alianza kulia machozi na baadaye kusimulia kila kitu kilichotokea katika maisha yake, hakusahau kueleza juu ya mama yake aliyeingia siku hiyo hiyo gerezani Segerea.

    “Pole sana, je umeokoka?”

    “Hapana ila natamani sana kuwa hivyo!”

    “Twende basi ukale tutakusubiri twende kwenye mkutano wa dini, kuna mhubiri mmoja anaitwa Karl Heinz kutoka Ujerumani anahubiri vizuri na tukitoka huko tutakuja nyumbani kwetu utaishi na sisi sawa?”

    “Sawa dada!”

    Walimpeleka hotelini akala na baadaye wakaondoka kwenda jangwani kwenye mkutano, watu walikuwa wengi sana siku hiyo kwa sababu ndiyo ilikuwa siku ya mwisho ya mkutano! Mama Teddy, Kidubo na Nancy walisimama nyuma kabisa na haikuwepo nafasi ya kusogea mbele zaidi! Walianza kusikiliza mkutano hadi mwisho mambo yote yalioongelewa katika mkutano huo yalimgusa Nancy na alilia karibu muda wote wa mahubiri hayo.

    “We have only three minutes to be in Dar es Salam, let me introduce to you my new tour assistant, I met this boy here yesterday and I’m going to be travelling with him wherever I go, his name is Patrick!”(Tuna dakika tatu tu za kuwa hapa Dar es Salaam, acha nimtambulishe kwenu msaidizi wangu mpya wa safari, ni kijana niliyekutana naye hapa jana na nitasafiri naye kila niendako jina lake anaitwa Patrick!)

    Patrick alipunga mkono wake hewani na sekunde chache baadaye wote walianza kuteremka jukwaani na kuingia katika magari tayari kwa safari ya kuelekea Zambia.

    Nancy aliposikia jina Patrick alishtuka na kuacha kulia, alipoangalia mbele yake jukwaani, hakuamini macho yake alipomwona Patrick akipunga mkono hewani.

    “PATRIIIIIIIICK!” Alipiga kelele na kuchomoka akaanza kukimbia kwenda mbele akipita katikati ya watu lakini alipofika kwa Anne magari tayari yalishaanza kuondoka, alipaza sauti akiita jina la Patrick huku akiyakimbiza magari hayo!





    “Patrick! Patrick! Patrick!” Nancy aliendelea kuita huku akiukimbiza msururu wa magari ulizidi kusogea mbele kuingia barabara ya Morogoro kutoka viwanja vya Jangwani, alilipita kila gari akiita jina la kaka yake lakini hakuitikiwa! Nancy alichanganyikiwa na kushindwa kuelewa ni wapi Patrick alikokuwa.

    “Dada vipi mbona unahangaika?”

    “Mimi?”

    “Ndiyo!”

    “Namtafuta kaka yangu Patrick!”

    “Patrick gani?”

    “Aliyetangazwa jukwaani kama msaidizi wa Mwinjilisti Heinz! Nimepotezana naye siku nyingi na niliamini alishakufa!”

    “Unamwongelea kijana aliyetambulishwa na Mwinjilisti?”

    “Ndiyo!”

    “Njoo nikuonyesha gari alilipanda!” Kijana huyo alimshika Nancy mkono na kuanza kumvuta kuelekea mbele ulikoelekea msafara wa magari.

    Walipokaribia mwanzo wa msafara huo, kijana alijishika kichwani na kuonyesha masikitiko makubwa huku akimwangalia Nancy usoni.

    “Nini?” Nancy aliuliza.

    “Gari lenyewe ndiyo lile linaloingia barabarani!” Alisema kijana huyo baada ya kuliona gari aina ya Landcruiser Vx likiingia barabara ya Morogoro na kuongeza kasi.

    “Una uhakika Patrick kapanda gari hilo kaka?”

    “Ndiyo na si yeye tu bali hata mtumishi wa Mungu Heinz!”

    “Kweli?”Nancy aliuliza tena.

    “Ndiyo!”

    “Asilimia mia moja?”

    “Ahsante kaka kwa msaada wako Mungu akubariki sana!”

    Alisema Nancy na kuondoka mbio akikimbia kwenda mbele, hakufuata barabara ya lami bali alikimbilia bondeni kwenye nyasi akijaribu kuliwahi gari ambalo Patrick alidaiwa kupanda. Mwisho wa bonde aliingia barabarani na kuyaona magari yote yamesimama na alipoangalia mbele yake aliona taa nyekundu zikiwaka!

    “Hizi nafikiri ndio taa za kuzuia magari ambazo huwa nazisikia, lazima gari lililombeba Patrick litakuwa miongoni mwa gari haya !” Aliwaza Nancy na kuanza kupepesa macho yake kuangalia magari yote yaliyokuwa katika mstari yakisubiri taa ziruhusu.

    Ghafla aliliona gari alililoonyeshwa likiwa kama hatua thelathini hivi kutoka mahali aliposimama! Furaha kubwa ilijaa moyoni mwake akawa na uhakika wa kumpata kaka yake Patrick.Watu waliokuwa ndani ya magari mengine walimwona kama mtu aliyechanganyikiwa, Nancy hakujali wala kuona aibu aliendelea kuliita jina la nduguye huku akikimbia kulielekea gari!

    Alipokaribia gari hilo alizisoma namba zake na kuona ndio lenyewe, akawa na uhakika zaidi ya kumpata pacha wake! Akaongeza mbio zaidi lakini hatua kama tatu hivi kabla hajaligusa gari hilo taa nyekundu zilibadilika na kuwa kijani magari yote yakaanza kuondoka kwa kasi.

    “Patrick! Patrick! Patrick! Mimi dada yako niko hapa!” Alipaza sauti Nancy lakini sauti yake yake haikusikika sababu gari hilo lilifungwa vioo vyote!

    Nguvu zilimwishia Nancy miguuni na kwa sababu ya kukimbia sana alijisikia mvurugiko wa tumbo na kuanza kutapika! Hakutaka kupoteza muda aliendelea kukimbia huku akitapika kuufuata msururu wa magari uliokuwa ukienda kwa kasi kubwa.

    “KUUUUUUUUUU!” Ulikuwa ni mlio wa magari yaliyogonana ghafla.

    “Wee mshamba utaua watu!” Kelele zilisikika kutoka ndani ya magari yaliyokuwa jirani na eneo hilo, Nancy alikuwa amekatisha barabara ghafla akikimbia, kidogo tu agongwe vibaya kama dereva asingemkwepa! Lakini katika kufanya hivyo gari lake lilikutana uso kwa uso na daladala lililokuwa likitoka upande wa pili!

    Kwa hofu ya kupigwa Nancy hakusimama alizidi kukimbia mbio kwenda mbele zaidi, dereva wa daladala alichomoka kwenye usukani na kuanza kumkimbiza, hasira kali ilimshika sababu ya kuharibiwa gari lake kwa uzembe wa Nancy, hatua chache tu mbele alimtia Nancy mkononi na kuanza kumzaba vibao usoni.

    “Nisamehe kaka ....mimi ni mgeni hapa mjini!” Alisema Nancy huku machozi yakimtoka.

    “Ukiwa mgeni ndiyo ukatishe barabara vibaya kiasi hicho, ungekufa wewe!”

    “Ahsante kwa kuokoa maisha yangu kaka, nisamehe na Mungu atakulipia gari lako!”

    Dereva alimmshushia Nancy ngumi mzito usoni, iliyomfanya avimbe juu ya jicho lake, alinguka chini na kusikia kizunguzungu lakini sababu alikuwa akilikimbiza gari lililombeba Patrick alijitahidi na kunyanyuka ardhini akiwa na maumivu yake na kuendelea mbele! Watu ndani ya magari walimcheka na kumzomea, roho yake iliuma lakini hakuwa na la kufanya.

    Mbele kidogo alikuta magari yote yakiwa yamesimam kama ilivyokuwa nyuma na alipotupa macho yake mbele aliyaona mataa mengine yakiwaka kwa rangi nyekundu! Alijua gari lililombeba Patrick lilikuwa miongoni mwa magari hayo, Nancy aliongeza mbio jicho lake lilimuuma lakini hakujali, alipotupa macho mbele zaidi aliliona gari lililombeba l Patrick likiwa mbele ya magari yote, akaongeza mwendo zaidi lakini kabla hajalifikia taa za kijani ziliwaka na kuyaruhusu magari kuendelea na safari.

    Aliendelea kuliita jina la Patrick wakati akikimbiza gari hilo, almanusura agongwe na lori lililobeba mchanga! Roho ya Nancy ilizidi kuuma akajikuta akilia machozi zaidi.

    Hakukata tamaa alizidi kulifukuza gari hilo kwa nyuma, alikuwa amechoka kukimbia lakini aliendelea kwani alipania mno kukutana na kaka yake na pacha wake Patrick na alitaka kufanya kila linalowezekana kuhakikisha kuwa anazuia safari yake ya kwenda nchi za nje na Mwinjilisti Heinz ! Alijua wazi Patrick alichukua uamuzi huo baada ya kuona hakuwa na ndugu tena Tanzania.

    Mbele kidogo kwenye mataa ya Lumumba na barabara ya Morogoro Nancy aliyaona magari yakisimama, alikimbia zaidi lakini hakuyawahi kwani kabla hajayafikia taa ziliruhusu na magari yakaanza kuondoka kwa kasi, Nancy alichoka na kuamua kutembea taratibu hadi kwenye makutano ya barabara za Morogoro na bibi Titi ambako aliyaona magari hayo yakikata kushoto kwa mwendo wa kasi.

    Hakuweza kukimbia zaidi ikabidi atembee taratibu, mbele aliingia barabara ya Bibi Titi Mohamed, giza lilishanzaa kuingia na taa ziliwaka kila mahali, kwa msaada wa taa alifanikiwa kusoma mabango ya ofisi mbalimbali kushoto kwake, aliona bango la ofisi za Tritel na mbele kidogo kwenye mataa ya Bibi Titi na barabara ya Azikiwe aliona bango jingine lililosomeka “Maktaba ya Taifa”!

    “Sasa sijui magari hayo yaliekea upande gani? Sijui yalinyoosha au yalikata kulia?” Alijiuliza Nancy baada ya kuchanganikiwa juu ya upande yalikoelekea magari ya msafara wa mwinjilisti Heinz! Baada ya kufikiri kwa muda hatimaye aliamua kukata kulia kuingia barabara ya maktaba na kunyoosha moja kwa moja hadi Posta mpya lakini hakuona dalili yoyote ya kuliona tena gari lililombeba Patrick wala magari mengine ya msafara wa Mwinjilisti Heinz!

    ****************

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alipofika maeneo ya Posta alishangazwa na umati wa watu wengi wakisubiri magari ya kuwarudisha majumbani kwao, alizunguka hapo kwa muda bila kuelewa aelekee wapi au amuulize nani! Ghafla alipomwona msichana mmoja akipita jirani yake, msichana huyo alikuwa na biblia mkononi mwake, Nancy alijua huo ndio ulikuwa msaada pekee kwake wakati huo alimkimbilia na kumshika bega!

    “Dada yangu samahani sana kwanza shikamoo!”

    “Marahaba mdogo wangu, vipi mbona unalia?’

    “Mimi?”

    “Ndiyo!”

    “Ninamtafuta kaka yangu!”

    “Wewe ni mgeni hapa?”

    “Ndiyo!”

    “Unatoka wapi?”

    “Mwanza!”

    “Huyo kaka yako anafanya kazi wapi?”

    “Hafanyi kazi ila yupo na Mwinjilisti Heinz aliyekuwa akihubiri kwenye viwanja vya!……….vya!……..vya! Vya Jangwani!”

    “Aha! Yule kafikia hoteli ya Sheraton!”

    “Ipo wapi hiyo dada?”

    “Pitia hapa!” Alimwonyesha barabara iliyoshuka chini kupitia makao makuu ya wizara ya mambo ya ndani na makao makuu ya posta nchini Tanzania!

    “Sawa!”

    “Pale mbele utakutana na barabara nyingine inayokatisha, hiyo ni mtaa wa Ohio! Hapo kata kushoto mbele utaona jumba refu mkono wa kulia si unajua kusoma?”

    “Ndiyo!”

    “Basi hapo utaona bango lililoandikwa Sheraton, kuna magari mengi sana utayakuta, ukifika ulizia tu watakuonyesha chumba cha huyo Mwinjilisti!”

    “Ahsante sana dada yangu sina namna ya kukushukuru!” Alisema Nancy na kuanza kuondoka eneo hilo mbele kidogo aliona kibao kilichoandikwa ‘Ohio street’ alikata kushoto kama alivyoelekezwa na kusonga mbele, aliliona ghorofa refu zaidi mkono wake wa kulia na kukata kona kuingia hotelini hapo.

    Alishangazwa na uzuri wa hoteli hiyo na kwa jinsi alivyovaa nguo chafu alihisi asingeruhusiwa kabisa kuingia ndani ya hoteli hiyo, alijipa moyo na kusonga mbele!

    “Mimi sijali hata kidogo ili mradi tu nimwone Patrick!” Alijisemea Nancy akielekea geti la hoteli hiyo.

    Tayari ilishatimua saa tatu ya usiku, Nancy alitembea bila kujiamini alipolifikia lango la kuingilia hotelini askari wa ulinzi alimsimamisha.

    “wee changu unakwenda wapi?”

    “Mh! Unasemaje kaka yangu?”

    “Nakuuliza unakwenda wapi saa hizi?”

    “Humu hotelini!”

    “Hapana! Utawala wa hoteli umezuia kabisa nyinyi msiingie humu ndani wateja wenu wawakute hukohuko mtaani!” Alisema askari na kuanza kumsukuma Nancy kumtoa nje ya hoteli hiyo.

    “Kaka sikuelewi?”

    “Kama hunielewi basi shauri yako kafanyie umalaya wako nje!”

    “Umalaya? Kwa umri huu mdogo niwe malaya, tafadhali nisikilize kaka yangu nikusimulie shida yangu!”

    “Hakuna! Sitakii! Toka nje!” Alisema askari huyo akimsukuma Nancy kumtoa nje na kulifunga lango nyuma yake.

    Nje Nancy aliendelea kulia akiligonga lango hilo, ilikuwa si rahisi kuamini kuwa kaka yake na pacha wake Patrick alikuwa ndani ya hoteli hiyo lakini alizuiliwa kumwona, alilia kwa uchungu na kuendelea kuligonga lango!

    “Nifungulieni jamani! Nifungulieni, nimwone kaka yangu!”

    “Kaka yako gani malaya wewe, toka hapa na nikitoka huko nje utanitambua!”

    Nancy hakusikia onyo hilo la askari aliendelea kulia akibisha hodi mlangoni, mlinzi alitafsiri hiyo kama dharau na kuamua kutoka hadi nje ambako alimkuta Nancy na kumbeba juu juu hadi barabarani ambako alimbwaga chini na kurudi ndani ya hoteli.

    Muda mfupi akiwa chini kundi la wasichana waliovaa nguo fupi na wengine wakiwa na chupi peke yake walimvamia, Nancy alitetemeka akifikiri labda wasichana wale walikuwa wachawi!

    “Mdogo wetu vipi, umetoa huduma wamekudhulumu nini? Maana hapa kuna wazungu wadhulumati ile mbaya!”

    Nancy alizidi kuwaangalia kwa mshangao hakuelewa kitu walichokua wakimweleza, aliendelea kulia machozi, kabla hajawaeleza kilichotokea walishtukia magari mawili aina ya Landrover yakiegesha pembeni yao, wasichana wengine wote walitimukia porini na kuwaacha Nancy na msichana mwingine mmoja ambao walijikuta mikononi mwa polisi, walifungwa pingu na kutupwa nyuma ya gari ambako walikutana na askari mwenye virungu, aliyekitumia vizuri kirungu chake juu ya vichwa vyao! Nancy alilia kupita kiasi.

    “Nyie malaya tumeshawaeleza msikae mtaa huu wanapita viongozi hamsikii siyo?” Askari alisema huku akiendelea kuwagonga na virungu vichwani, kama wewe mtoto mdogo kabisa unafanya umalaya.

    “Mimi siyo……!” Nancy alijaribu kujieleza lakini kabla sentensi yake haijafikia mwisho kirungu kilitua juu ya pua yake na damu zilianza kutoka puani.

    “Kimya! Funga domo lako changu wee unafikiri mimi nataka mapenzi hapa?” Alifoka askari huyo.

    Kwa upande wake Nancy aliamini kama angepewa nafasi ya kujieleza askari huyu angeweza kumwachia huru lakini nafasi hiyo haikuwepo.

    Walipofikishwa kituoni walitupwa mahabusu bila hata kutoa maelezo, kila mtu aliwaita malaya wazururaji, majina hayo yalimuuma sana Nancy ukizingatia katika maisha yake hakuwahi hata mara moja kukutana na mwanaume kimapenzi.

    “Ninaitwa Lwina! Sijui mwenzangu unaitwa nani?” Changudoa waliyekamatwa nae alimuuliza, Nancy hakujibu aliendelea kulia machozi ya uchungu mambo yalikuwa yakitokea katika maisha yake yalimsikitisha kupita kiasi, hata siku moja katika maisha yake hakuwahi kufikiria kuwa angeweza kuitwa malaya!

    “Unaitwa nani?”msichana yule aliuliza tena.

    “Mimi naitwa N….a..n…cy!” Alijibu huku akilia machozi.

    “Jina lako zuri sana wewe huwa unasimama kiwanja gani? Sababu kiwanja cha Ohio ndio kwanza nimekuona leo? Huwa upo Kinondoni au Las Vegas nini?”

    “Hapana!”

    “Oysterbay?”

    “Viwanja vya nini dada?”

    ************

    Kidubo na mke wake mama Teddy walimtafuta Nancy kwenye mkutano bila mafanikio, walishaamua kuishi naye nyumbani kwao mpaka mama yake amalize kifungo cha miaka mitano, walijua Nancy alikuwa na matatizo na alihitaji msaada mkubwa na waliamini msaada huu ulikuwa mikononi mwao.

    Watu wote kwenye mkutano walisambaa bila Nancy kuonekana, ndipo walipoamua kuzunguka huku na kule jijini wakimtafuta bila mafanikio mwisho walikata tamaa na kuamua kuondoka kurejea nyumbani kwao Segerea.

    “Si ajabu amekutana na kaka yake na kuamua kuondoka naye!” Kidubo alimwambia mke wake.

    “Inawezekana!” Mkewe aliitikia.

    “Basi tena Mungu anajua!”

    Walirejea nyumbani wakiwa na masikitiko makubwa mno kumpoteza Nancy Moyoni mwao walishampenda sana Nancy na walitaka kumsaidia!

    ****************

    Mpaka usiku wa manane ndani ya hoteli ya Sheraton wakiwa wamelala chumba kimoja na Mwinjilisti Heinz, Patrick alikuwa bado hajapata usingizi akiyafikiria maisha yake! Hakuamini yote yaliyomtokea katika maisha yake, kukutana na mzungu na kukubali kumsaidia hakikuwa kitu alichowahi kukifikiria maishani mwake.

    Pamoja na mawazo hayo yote bado aliendelea kuwafikiria mama na dada yake Nancy ambao aliamini walikuwa wafu! Hakuwa na taarifa yoyote kuwa usiku huo Nancy alishakuja hadi nje ya hoteli ya Sheraton akimtafuta! Mawazo juu ya mama na dada yake yalimfanya atokwe na machozi.

    Ghafla alishtukia akimwona Mwinjilisti Heinz akinyanyuka kitandani kwake na kwenda kwenye moja ya masanduku yake na kulifungua akatoa kitu kama bomba la sindano na chupa ya dawa fulani! Alitupa macho yake kuangalia kwenye kitanda cha Patrick, Patrick aliamua kujifanya amelala ili ajue ni kitu gani kilichotaka kutokea, Mwinjilisti alisogea hadi karibu kabisa na kitanda cha Patrick na kumchunguza usoni.

    “He is fully asleep!”(amelala fofofo)Mwinjilisti alisema peke yake na kuondoka.

    Patrick alishuhudia kila kitu kutoka kwenye kona ya jicho lake la kushoto alimwona Mwinjilisti akihangaika kujifunga na mpira wa plastiki na kujipigapiga, alionekana kama mtu aliyekuwa akitafuta mishipa wa damu mikononi mwake. Alionekana kutofanikiwa ndipo alipochukua mpira huo na kuufunga sehemu za siri kwenye uume wake! Kwa macho yake yote mawili Patrick alishuhudia Mwinjilisti akichoma sindano ndani ya uume wake! Alilegea na kuanza kulala hapohapo sakafuni.

    Patrick aliogopa na kunyanyuka kitandani kwake kumkimbilia Mwinjilisti, akidhani labda madawa aliyojichoma yalimzidi.

    “Mtumishi! Mtumishi! Mtumishi wa Mungu Heinz!” Patrick aliita lakini Mwinjilisti hakuitikia aliendelea kukoroma na kudondosha udelele mdomoni kwake.

    Patrick alimnyanyua na kumpandisha Mwinjilisti kitandani huku akitetemeka, alifikiria kupiga simu mapokezi ili waje wampe msaada!

    Patrick ameshuhudia mambo ya Mwinjilisti Heinz ambayo ni siri kubwa na Mwinjilisti humuua mtu yeyote agunduaye siri hiyo!

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Je nini kitampata Patrick?

    Nancy yupo mahabusu akidhaniwa ni changudoa!

    Je nini kinafuata?



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog