Search This Blog

NILIPANGA NYUMBA MOJA NA MAJINI - 2

 





    Simulizi : Nilipanga Nyumba Moja Na Majini

    Sehemu Ya Pili (2)





    Nia yangu kubwa ilikuwa kuwaona kwa sura na kufahamu kama ni ngozi nyeusi au nyeupe. Hilo peke yake lingenipa mwanga ni watu wa aina gani naishi nao pale ndani ya nyumba.

    Nilisikia mlango wa chumbani kwao ukifunguliwa na mimi nikatoka haraka sana, cha ajabu sikuona mtu akitoka lakini mlangoni kulikuwa na kandambili pea moja tu wakati zilikuwa pea mbili.

    Hilo lilimaanisha kwamba, mmoja wao alitoka kwenda chooni, nilichofanya ni kuamua kusimama katikati ya mlango wangu ili huyo aliyekwenda chooni akirudi nimuone. Ni kweli mmoja wao alikwenda chooni kwani nilisikia mlio wa maji.!!CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    NilijiTahidi kusimama mlangoni kwangu kumsubiria. Kwa ramani ya nyumba ile ilivyo, asingeweza kutoka chooni bila mimi kumwona hata kama angekuwa anataka kutoka kwenda nje au uani.

    Mlio wa maji ulikosa kusikika, nikawa natumbulia macho kule huku moyoni nikisema:

    “Leo ndiyo leo, asemaye kesho mwongo, hata afanyaje, hawezi kunichenga hapa hata kidogo,” nilisema moyoni, ingawa wakati huo mapigo ya moyo yalikuwa yakinienda kwa kasi.

    Nilipoanza kuhisi muda unakwenda na hakuna mtu aliyetoka, nikampa dakika tatu kwamba lazima atakuwa anavaa ndiyo maana anachelewa:

    “Labda alikuwa anajisaidia haja kubwa, maana wengine huwa wanavua nguo zote, lakini mimi nipo, siendi kokote,” nilisema moyoni nikiwa bado nimesimama mlangoni kwangu.

    Baada ya muda, nikasikia watu wakiongea chumbani kwao, nikashtuka, nilijikuta nikisema:

    “Haa!”

    Haraka sana nilitupa macho mlangoni kuangalia kandambili, nikazikuta pea mbili, nikashangaa:

    “Ina maana amenipita hapahapa au? Haiwezekani, asingeweza kunipita hata kama ingekuwaje?” niliwaza. Nilitoka kuelekea chooni, nikakuta mlango uko wazi, nikachungulia ndani, hakukuwa na mtu, nikanyoosha mikoni, nikarudi ndani.

    Nilifikia kwenye kochi sebuleni, nikahema kwa nguvu kwani niliamini nimo ndani ya miujiza mikubwa ya ndani ya nyumba ile.

    “Hivi ni kwa nini dalali alinidanganya hivi?” nilijiuliza mwenyewe nikiamini kwamba, dalali aliyenipangisha nyumba ile alijua mchezo mzima ila alitaka kupata fedha tu ndiyo maana alinipangisha bila kunipa tahadhari.

    Nilitoka sebuleni, nikaenda chumbani, kitandani nikakuta ‘toilet paper’ ikiwa imekatwa sehemu. Mimi niliicha pembeni ya dirisha, lakini ikaonesha kuna mtu aliichukua na kunyofoa kidogo kisha badala ya kuirudishia palepale, yeye aliiacha kitandani.

    Mbali na ‘toilet paper’ pia kuna kikopo chenye vijiti vyenye pamba za masikio kilikuwa kwenye stuli jirani na kitanda, lakini kwa muda huo kilikuwa kimeanguka chini halafu vijiti vimebaki kama vitatu tu kwa maana kwamba, aliyeingia kuchukua ‘toilet paper’ ndiye huyohuyo aliyechota vijiti vya pamba.

    Nilianza kuhisi kuwa sikuwa kwenye nyumba salama, lakini kwa uthibitisho upi? Moyoni nikasema nitajua tu, mimi ndiyo mimi.

    ***

    Nilikaa ndani kwangu hadi usiku ulipoingia, nikasema nibadili nguo kwa kuvaa bukta na singilendi halafu nitoke kwenda kula gengeni kwani siku hiyo sikuwa najisikia kupika chochote. Ni mara nyingi nilipenda kula gengeni.

    Nilitoka, nikasimama mlangoni ili nifunge mlango wa chumbani, nilipoangalia chini, upande wa wenzangu nilikuta nje ya mlango wao pana vijiti vya pamba za masikioni vikiwa vimetumika, nikiwa katika mshango, mbele nikaona tishu ikiwa imefutiwa majimaji yenye rangi nyekundu kama damu.

    Nilitembea kwa wasiwasi, nikatoka nje, sikufunga mlango kwa funguo, lakini niliubamiza tu, funguo nilikuwa nazo, nikaenda gengeni kula.

    Pale kwenye genge ambapo si mbali sana na nyumbani, alikuja yule mama aliyeniuliza mimi ni mtu wa wapi, nilimsalimia, lakini kabla hajaitikia alishtuka kuniona.

    “Upo kijana wangu?”

    “Nipo mama, nimetoka kazini nimekuja kupata kidogo.”

    “Pole sana, uoe sasa.”

    “Huo ndiyo mpango wangu mama.”

    “Ee, uoe halafu mimi nitakupa vyumba viwili pale kwangu, nakuahidi.”

    “Nashukuru sana mama. Naanza kujipanga.”

    “Sawa, vipi wenzako lakini?”

    Nilisita kumjibu, nikabaki namwangalia tu, naye alibaini kwamba nimepata mshtuko na swali lake.

    “Vipi wapangaji wenzako, naamini utakuwa hujaonana nao?”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ni kweli mama, tena hebu nakuomba kidogo,” nilisema nikienda pembeni kidogo ili na yeye anifuate tukaongee.

    “Niambie,” alianza kusema.

    Nilimuuliza kama kuna anachokijua chochote kile kuhusu wale wapangaji wenzangu. Alianza kwa kusema:

    “Kusema ule ukweli sina kwa undani, ila napenda kukwambia kwamba, unaishi na watu ambao unahitajika moyo wa ziada ili uweze kuendelea kuishi nao.

    “Pale mbali na wewe, pameshakaa wapangaji wengine saba, tena wote kama wewe, hawajaoa. Lakini kinachoshangaza ni kwamba, wanaondoka baada ya wiki mbili, mmoja aliondoka baada ya siku tatu tu.”

    “Kwa hiyo hakuna hata mmoja aliyewahi kukwambia ameona nini kule ndani?”

    “Hakuna.”

    “Lo! Mimi mama mambo ninayoyaona yanatisha.”

    “Kama mambo yapi, nisimulie kidogo.”

    Nilipotaka kuanza kumsimulia huyu mwanamke, ghafla alitokea msichana mmoja, mweupe, mrefu kiasi, amejazia sehemu mbalimbali za mwili, akaguna na kusema:

    “Kaka Humuli mambo vipi, za siku?”

    Nilipata kigugumizi kikubwa kumjibu mambo poa kwani sikumjua na sikuwa nakumbuka chochote kuhusu yeye, sura yake ilikataa kichwani mwangu.

    “Wewe ni nani kwani?” nilimuuliza.

    Akaachia tabasamu kwa mbali, uzuri wake ukaongezeka.

    “Ha! Humuli, hunikumbuki mimi, kweli?”

    “Sikukumbuki hata kidogo.”

    “Sasa we binti, kama wewe ndiyo unamkumbuka si umkumbushe mlionana wapi?” yule mwanamke alisema kwa sauti ya mshangao.

    Lakini yule msichana mrembo alimwangalia yule mwanamke kwa macho yaliyojaa hasira…

    “Mama uhusiki.”

    “Najua, lakini unapoteza muda kwa kuzungushazungusha wakati kumbe wewe unamkumbuka, yeye umeshajua hakukumbuki na amekwambia tayari.”

    Nilishangaa kumwona yule msichana akibetua kichwa kama aliyekuwa akiweka vizuri nywele zake, ghafla yule mwanamke niliyekuwa naye akajishika kichwa na kulalamika kinamuuma sana.

    “Jamani kichwa! Kichwa jamani, daa!”

    “Vipi mama, imekuwaje kwani?” nilimuuliza.

    “Kichwa Humuli, kinavuta ghafla! Uwiii.”



    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nilianza kuogopa, nilihisi naangukiwa na msala maana akifa pale na watu waliona nikienda naye pembeni si nitahojiwa mimi?

    “Kwani mama una kawaida ya kuumwa kichwa?” nilimuuliza nikimsogelea ambapo yeye sasa alikuwa ameinama.

    “Sina, ndiyo nashangaa hapa.”

    Niliona hakuna dawa nyingine zaidi ya kumpeleka kwake ili nikaungane na familia yake kumpeleka hospitali. Lakini kabla ya kufanya hivyo niliinua macho ili nimwambie yule dada anisaidie na kama anataka kunikumbusha, hayo yangefanyika baadaye.

    Ile naanaza kusema anti huku nikiwa nimeinua macho, nilishangaa kutomwona yule msichana pale.

    “Khaa!” nilijikuta nikisema hivyo.

    “Mama twende nyumbani ili tukupeleke hospitali na watoto wako.”

    “Ha! Mbona kimeachia,” alisema akionekana kushangaa na kuniangalia, alikuwa amepanua kinywa.

    “Kweli?”

    “Eee, niko mzima kabisa.”

    “Au?” nilitaka kusema neno lakini zikulimaliza, nikahisi ulimi unakuwa mzito si kwa kushikwa bali kwa matakwa yangu.

    “Humuli.”

    “Naam.”

    “Ni kweli yule binti humjui?”

    “Simjui mama.”

    “Kuna mawili hapo, humjui au humkumbuki.”

    “Vyote mama, simkumbuki na pia simjui.”

    “Lakini wewe si alikutaja kwa jina?”

    “Mwenyewe nilishangaa sana.”

    “Basi Humuli nimeshaelewa, kwaheri, nimeelawa ni kwa nini nimeugua kichwa na yule ni nani, pole sana wewe kijana,” alisema yule mwanamke huku akiondoka zake kuelekea kwake.

    Nilimtazama, lakini baadaye nilirudi kwenye kibanda cha chipsi.

    “Mzee nakuona na miss jini,” muuza chipsi mmoja alisema.

    “Yupi, yule mwanamke?”

    “Hapana, yule msichana.”

    “Mi simjui, kwani anaishi wapi? Maana kasema ananijua, ameniita na jina.”

     “Khaa! Kumbe wewe kama sisi. Huyu dada anaishi mitaa hiihii, lakini hakuna hata mmoja anayejua nyumba anayoishi!

    “Kuna jamaa mmoja anaitwa Maleke, Maleke aliwahi kumfuatilia kwa nyuma lakini alishindwa kujua aliingia nyumba gani!”

    “Mh! Au jini?” niliuliza kwa mshtuko mkubwa.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ndivyo watu wanavyosema, sasa alipokuja kusimama na wewe, tukawa tunabishana, wengine wanasema ni miss jini, wengine siye, lakini alipokuwa anaondoka tukagundua ni miss jini.”

    Basi, tuliishia hapo, nikachukua chipsi zangu na kwenda nazo nyumbani, niliamua kwenda kulia kule.

    Nilifika, nikasukuma mlango mkubwa nikazama ndani kwangu. Lakini wakati napita kwenye usawa wa chumba cha wale wenzangu nikasikia vicheko, tena vicheko kwelikweli.

    Sikuwajali, nikaingia sebuleni kwangu, nikafunga mlango kwa ndani, nikaweka chipsi juu ya meza, nikaenda pembeni ya chumba ambako kuna ndoo ya maji ili nichote ya kunawa.

    Wakati naanza kula nilihisi na kugundua kitu. Niligundua mabakimabaki ya chipsi na kuku juu ya meza yangu wakati ukweli ni kwamba, tangu nimehamia pale sikuwahi kula chipsi wala kuku.

    “Humu ndani kuna mtu anaingia kufanya mambo yake, lini mimi nimekula chipsi na kuku humu ndani?” nilijiuliza, nikasikia kicheko kutoka kwa wenzangu.

    “Haa! Haaa! Ha! Haaaa…aaaa.”

    Niliinua macho kuangalia juu kwenye ‘silingbodi’ kama vile niliyekuwa nimeona kitu, akili yangu ikawaza kitu cha dakika chache nyuma, nacho ni hiki:

    “Humuli.”

    “Naam.”

    “Ni kweli yule binti humjui?”

    “Simjui mama.”

    “Kuna mawili hapo, humjui au humkumbuki.”

    “Vyote mama, simkumbuki na pia simjui.”

    “Lakini wewe si alikutaja kwa jina?”

    “Mwenyewe nilishangaa sana.”

    “Basi Humuli nimeshaelewa, kwaheri, nimeelawa ni kwa nini nimeugua kichwa na yule ni nani, pole sana wewe kijana.”

    Nilianza kuamini kwamba, kuna uhusiano mkubwa kati ya yule msichana na wale wapangaji wa pale ndani nilipo, inawezekana alinijua jina kwa sababu naishi nao na wana uwezo wa kujua jina la mtu kulingana na mazingira yao.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Pia niliwaza kwamba, kuna uwezekano mkubwa yule msichana alitokea baada ya maono yao kuniona mimi na yule mama wa jirani tukitaka kuwazungumzia wao kama wapangaji wenye maajabu hivyo hawakupenda iwe hivyo ndiyo maana msichana akaibuka na kusababisha mvurugano.

    “Itakuwa kweli, ndiyo maana yule mama naye alisema ameshajua ni kwa nini aliugua kichwa ghafla, alijua yule msichana ni nani na kwa nini yeye kasikia maumivu ya ghafla vile.”

    “Lakini pia kuna wale wauza chipsi, nao niliwakumbuka hasa yule mmoja aliyesema yule msichana wanamjua, anaishi mtaani, lakini hawajawahi kubaini anaishi nyumba gani na kwa mzee nani wala anajishughulisha na nini,” hayo yote niliyawaza mimi.

    Nilisimama, nikachukua sabuni ya kuogea ambayo haijafunguliwa, nikaipiga chini kwenye kapeti  kwa hasira huku nikisonya, nikasema kwa sauti ya chini:

    “Humu ndani naishi na majini.”

    Kule chumbani nikasikia wakicheka.

    “Si unaona, nimesema mimi, lazima naishi nao humu ndani, da! Najuta sana,” nilisema. Kicheko kikasikika tena, safari hii kilikuwa cha juu zaidi kuliko kile cha awali.

    Moyo ulijaa mawazo, akili ilihisi uchungu wa maisha, niliwaza fedha nilizozilipa kwa ajili ya kupanga mle ndani, nikamkumbuka dalili, niligundua alichofanya ni kunitapeli na hakuna lingine wala hakuwa msaada kwangu.

    “Mimi ni mwanaume, kama niliweza kupata fedha za kupanga hapa, sishindwi kupata nyingine za kupanga sehemu nyingine tena mbali na hapa,” nilisema kwa moyoni.

    ***

    Usiku nikiwa nimelala, nilichelewa sana kupata usingizi, ghafla nikaona taswira za watu ukutani, wawili tena wakiwa wamesimama, ni mwanamke na mwanaume. Niliogopa sana, nikainua kichwa polepole kuwaangalia kwa umakini, japo kulikuwa na giza, lakini niliweza kuona vizuri lakini si kwa uwazi mkubwa kama ambavyo taa ingekuwa inawaka.

    Ni kweli walikuwa watu wawili kama nilivyoona, tena weupe nikimaanisha si watu weusi. Walikuwa wakionesha vitendo vya kucheka huku wakijinyonganyonga.

    Kuna wakati walitembea mpaka jirani na kitanda changu kisha wakageuza na kurudi pale ukutani. Nilipeleka mkono hadi kwenye swichi ya kitanda (bed switch), nikawasha, cha ajabu sikumwona mtu wala dalili pale ukutani.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Niliamka nikiwa nahema kwa kasi mpaka nikajishika kifuani, nikafungua mlango na kutoka nje ili nijifanye nakwenda chooni lengo langu lilikuwa kupata picha kwa wenzangu kukoje maana niliwashuku wao na wale walioonekana chumbani kwangu.

    Kwa wenzangu niliwasikia wakikoroma kwa zamu. Nikajiuliza ina maana si wao waliokuja chumbani kwangu? Niliona ni utani wa hali ya juu.

    Niliamua kurudi chumbani na kukatisha safari ya kwenda chooni, nikafunga mlango wangu kwa funguo na kupanda kitandani, nilizima taa ili nione kama yale mauzauza yatatokea tena.

    Ukimya ulitawala kwa muda bila kujitokeza chochote, nikaanza kupitiwa na usingizi kwa kusinziasinzia, ghafla ukutani nikawaona tena wale watu wawili.

    Safari hii walikuja hadi kitandani, wakakaa, wakasimama, wakaenda kwenye kabati, wakafungua, wakatoa mashuka na kujifunika, wakayarudisha, wakaenda nyuma ya mlango, wakatungua mashati yangu mawili, wakagawana na kuyavaa kisha wakayavua, mmoja mwanaume akaenda sehemu yenye redio, akapeleka mkono, nikajua anataka kuiwasha, lakini hakufanya hivyo.

    Nilichoamua kukifanya akilini ni kuwasha taa kwa ghafla na kuwavamia na nilipanga kumvamia mwanamke nikiamini ndiye aliyekuja kule kwenye chipsi. Polepole nilipeleka mkono hadi kwenye swichi, nikawasha taa kwa ghafla huku macho yangu yakiwa kwao, lakini sikumwona hata mmoja! Kwangu haikuwa mapambano bali nilichukulia kama changamoto za maisha.

    ***



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog