Search This Blog

NILIPANGA NYUMBA MOJA NA MAJINI - 1

 





    IMEANDIKWA NA : GLOBAL PUBLISHERS





    *********************************************************************************



    Simulizi : Nilipanga Nyumba Moja Na Majini

    Sehemu Ya Kwanza (1)

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “KAMA kuna watu hawayajui haya nitakayoyaongea basi nawataka kuanzia sasa wajue kwamba, hapa Dar kuna mambo makubwa sana ambayo ukisimuliwa unaweza kusema si kweli, lakini wale wanaoyapata hayo mambo wanajua na wewe usiombe yakukute hata siku moja,” ndivyo alivyoanza kusimulia Bw. Humuli Samaki (43), mkazi wa Buguruni (kwa sasa) ambaye alipata mkasa mzito akidai alipanga nyumba moja na majini Magomeni, Dar es Salaam.

    “Si zamani sana mkasa huu uliponitokea, ilikuwa mwaka 2009 tu, kwa hiyo naweza kusema ni juzijuzi.  Kwa sasa naishi hapa Buguruni, baada ya kuhama kutoka Magomeni ambako nilipataka mkasa huo mzito na wa kuogopesha. Nilipanga nyumba moja na majini.”

    Awali nilikuwa nikiishi Mwanyamala Mwanjuma, jirani kabisa na Makao Makuu ya Bendi ya TOT, hata Kapteni John Komba nilizoeana naye kwa kuonanaonana pale CCM-Mwinjuma, ingawa jina langu najua hakuwa akilifahamu.

    Ile nyumba niliyokuwa nikiishi Mwananyamala iliingia kwenye mgogoro wa mirathi, familia ilifika mahakamani. Hukumu ilipotoka ikaamriwa iuzwe kisha ndugu wagawane fedha.

    Kwa maana hiyo, mimi na wapangaji wenzangu watano, tulipewa notisi ya kuhama baada ya mteja kupatikana. Huyu mteja anaitwa Masawe anafanya kazi Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) lakini sijui ofisi za wapi.

    Ilibidi mimi niangalie mwelekeo mwingine, niliamua nibadili upepo, nikaishi Magomeni. Kwa wakati huo nilikuwa sina familia. Sina mke wala mtoto, hata wa kusingiziwa, kwa hiyo nilikuwa naishi peke yangu. Ni mwaka jana ndiyo nimeoa mke wangu huyu.

    Rafiki yangu mmoja anaitwa Mohamed Kombe alinipa namba ya dalali kwani yeye anaishi Magomeni hata sasa. Nilimpigia simu dalali wake, anaitwa Yusuf Mwamba, akaniita Magomeni pale kwenye nyumba wanayosema aliwahi kuishi Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere.

    Nilikwenda mpaka pale, nilimkuta amesimama nje ya nyumba hiyo, tukasalimiana, akaniuliza nataka nyumba yenye sifa gani, nikamweleza.

    Akasema nyumba ya aina hiyo ipo moja mitaa ya katikati kama unatokea pale tulipokuwa kuelekea kwa Sheikh Yahya Hussein (marehemu).

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Tulikwenda kuiona hiyo nyumba. Wakati tukiwa tunaifikia, nilishangaa kuwaona majirani wakitukodolea macho, sikushangaa nikijua ni mambo ya mjini kitu kidogo tu watu kibao.

    Yule dalali alifungua mlango, tukaingia ndani. Tulipita sebuleni, tukaenda kwenye vyumba viwili, tukaelekea  jikoni, chooni na kumalizia na bafuni. Ni nyumba iliyojitegemea kwa maana kwamba, ilikuwa na ua wake na mtu akiwa uani hakuna aliyeweza kuona kwa nje. Mlango wa kuingilia ndani ni mmoja tu.

    Kulikuwa na vyumba vingine viwili ambavyo toka mwanzo alishaniambia kuna mtu anaishi na mkewe, kimoja wanalala, kingine wamekifanya sebuleni, lakini hawana watoto kama mimi.

    Nilijiridhisha kwamba ni pazuri, dalali akaniuliza kuhusu malipo, nikamwambia tuongozane nikachukue fedha Magomeni Mapipa kwenye benki ya Barclays, akasema wakati mimi nakwenda kutoa hizo fedha, yeye anakwenda Dawasco tawi la Magomeni.

    Tukiwa tunaelekea Magomeni Mapipa, nilimuuliza wenye vile vyumba wanafanya kazi wapi? Akajibu wafanyabishara, lakini hata yeye hajui ni wapi. Nilimuuliza imekuwaje ana funguo, wale wapangaji wengine wakirudi je, akajibu wana funguo yao na ile yeye alipewa na mwenye nyumba kwa ajili ya kutafutia mpangaji mwingine. Nilikubaliana naye.

    ***

    Baada ya nusu saa nilitoka benki nikiwa na fedha, nikampigia simu, akasema na yeye alishatoka Dawasco na wakati huo alikuwa anakunywa soda kwenye Hoteli ya Shibam, ipo palepale Mapipa. Nilimfuata pale, nikampa fedha, akatoa mkataba, nikajaza kwani yeye ndiye aliyepewa jukumu lote na mwenye nyumba.

    “Kwa hiyo upo huru kwenda kuhamia,” dalali aliniambia huku akinikabidhi funguo.

    “Sawa, nitahamia usiku wa leo.”

    Nilirudi nyumbani kwa awali na kupangapanga vitu tayari kwa usiku kuhamia makazi mapya, Magomeni. Niliwaambia wapangaji wenzangu wote, nao wakanitakia maisha mema huku wakisema tukumbukane kwani hata wao walikuwa kwenye mchakato wa kuhama kwenye nyumba ile.

    ***

    Saa mbili usiku nilikuwa juu ya lori tukipeleka mizigo makazi mapya, lakini moyoni nilikuwa na maswali mengi ambayo mpaka leo hii siyakumbuki na yalikosa majibu. Pia, nilijikuta nakosa amani ya moyo na sikujua ni kwa nini!

    Nje, nilikuta taa inawaka, ndani pia taa inawaka, lakini si sebuleni bali kwenye korido. Hii iliashiria kwamba, wale wapangaji wenzangu walisharudi kutoka kwenye biashara zao.

    Nilishusha vyombo kwa kusaidiwa na wasaidizi wa dereva wa lile lori, lakini nilishangaa sana kuona kila nikiingia na mizigo, wale wapangaji wenzangu wanacheka sana chumbani kwao. Maana yangu ni kwamba, kwa kawaida walitakiwa hata watoke na kunisalimia ili tufahamiane. Tena kwa wengine, mume angetoka na kunisaidia kubeba hata stuli tu.

    Ilifika mahali, wale vijana waliokuwa wakinisaidia waliniuliza:

    “Hivi hao majirani zako mbona hawatoki, wanacheka tu chumbani.”

    Niliwajibu mimi mwenyewe sijui, lakini sikumaindi sana. Akaja mama mmoja aliyesema anaishi nyumba ya pili, akasalimia na kuniuliza maswali.

    “Hamjambo wanangu?”

    Tuliitikia wote, akauliza nani anahamia pale kati ya sisi wote, tulikuwa watano mbali na dereva.

    “Ni mimi.”

    “Ooo, mzima baba?”

    “Mimi mzima mama.”

    “Unaitwa nani?”

    “Humuli Samaki.”

    “Unahamia peke yako au uko na mke na watoto?”

    “Peke yangu mama.”

    “Humuli Samaki ni mwenyeji wa wapi?”

    “Usukumani.”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Haya, naamini uliaga wakati unaondoka nyumbani.”

    “Hilo lilikuwa la kwanza mama.”

    “Haya, kila la kheri.”

    Tuliendelea na kazi ya kuingiza vyombo ndani hadi tukamaliza. Wale wenye gari wakaondoka, nikabaki mimi peke yangu.

    Nilijiwekea malengo kwamba, nihakikishe naweka sawa kila kitu ili kesho yake nisiwe na kazi hiyo zaidi ya kwenda kazini. Niliifanya kazi kwa muda wa saa tatu, mpaka kwenye saa saba na nusu usiku nikamaliza.

    Nilibadili nguo, nikavaa taulo na kwenda kuoga. Nilikuta bafu limetoka kutumika kama dakika kumi nyuma, sikushangaa kwani si kuna wapangaji wengine ambao tulitakuwa tunatumia bafu moja.

    Usiku kabla ya kuzima taa, nilizima taa, nikapanda kitandani. Kabla sijapata usingizi, niliwasikia wenzangu wakicheka sana na kuongea huku wameweka muziki. Lakini ule muziki haukuwa wa kiarabu, kizungu wala kiswahili.

    Hata maongezo yao, mimi nilisikia sauti tu lakini kusema walikuwa wanatumia lugha gani si rahisi. Kuna wakati kama walikuwa wakiongea kihindi, pia niliwasikia kama wanaongea kiarabu, nikajua ni watu wa namna hiyo.

    Lakini sikulala mpaka nikampigia simu dalali kumuuliza kama wale wapangaji wenzangu ni weupe au waswahili kama mimi, akasema hata yeye hajui kwani hakuwahi kuwaona hata siku moja.

    Basi, nililala. Asubuhi niliamka nikiwa nimechoka sana. Wakati nakwenda bafuni kuoga niligundua ni mimi peke yangu ndiye niliyekuwa nimetangulia kuamka, kwani bafuni hakukuwa na maji yaliyomwagika kwa muda huo.

    Baada ya kuoga nilirudi chumbani kwangu kujiandaa kwenda kazini. Wakati najiandaa, nilisikia mlango ukifunguliwa, nikajua ni wenzangu wanakwenda kuoga au chooni kama ilivyo kawaida kwa wanadamu wakiamka asubuhi.

    Niliamua kutumia nafasi hiyo kuwatambua. Nilivizia pale niliposikia mlio wa maji bafuni na mimi nikatoka kwenda kupiga mswaki kwa mara ya pili. Sehemu niliyosimama, mtu akitoka bafuni kwenda ndani ilikuwa lazima nimuone kwani ilikuwa kiasi cha kugeuka tu.

    Lakini cha kushangaza, nilikuwa sisikii maji kumwagika, nikageuka na kuona mlango wa bafuni upo wazi. Mbali na mlango kuwa wazi, pia chini nikaona alama za kandambili nne zikiwa zimekanyaga, nikajua wametoka.

    “Lakini wamepitaje hapa?” nilijiuliza.

    Nilirudi ndani, mlangoni kwao nilikuta kandambili pea mbili zikiwa bado na majimaji kwa mbali, jambo hili lilinifanya nijiulize sana.

    Nilijipa ujasiri na kuamua kuchungulia ndani ya chumba hicho kwa kutumia nafasi ya katikati ya mlango ambapo niliweza kuona hadi kitanda lakini sikumwona mtu mwingine.

    Niliingia kwangu, nikaweka mswaki, nikavaa vizuri na kuondoka zangu. Nilitegemea wenzangu nimewaacha ndani, kwani nilipofika mlangoni nilikuta umefunguliwa na upo wazi. Nilirudi ndani hadi kwenye mlango wao.

    “Wa ndugu,” niliita kwa sauti.

    “Jamani wa ndugu.”

    Ukimya ndiyo ulinifanya nibaini walishaondoka. Kwani kulikuwa kimya sana na kandambili zilikuwa pembeni ya mlango si pale pa kwanza.

    Nilifunga mlango mkubwa nikaondoka, mbele nilimwona yule mama aliyekuja usiku kuniuliza maswali. Alikuwa amesimama nje ya nyumba yake, aliponiona akashutuka na kuita majina mawili ya watu. Wakatoka watoto wake wawili, ni mabinti wenye miaka kama kumi na nane na ishirini na mbili hivi.

    “Hujambo kijana?” yule mama alinisalimia kwa furaha.

    “Sijambo mama, shikamoo.”

    “Marhaba.” Kisha akawaambia kitu wale watoto wake nao wakanikazia macho.

    “Mama umewaona majirani zangu hapa?”

    “Majirani zako akina nani?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Wapangaji wenzangu.”

    “Kijana, kua uyaone ya dunia. We si umeshakua, utayaona ya dunia.”

    Kauli hiyo iliniogopesha sana, nikashtuka na kumuuliza mama.

    “Mama una maana gani?”

    “Sisi hatutaki umbeya kijana.”

    “We si umeambiwa utayaona kwa hiyo subiri tu,” alidakia binti yake mkubwa.

    Miguu ilitetemeka, mwili uliisha nguvu, nikajikuta nataka kukaa, lakini sikuweza. Nilichoamua ni kuondoka huku nampigia simu yule dalali.

    “Vipi hujambo bwana?”

    “Mimi sijambo.”

    “Za makazi mapya.”

    “Si nzuri bwana.”

    “Kwa nini tena?”   

    “Sielewielewi.”

    “Kivipi?”

    “Kuna mambo kama si ya kawaida.”

    “Yapi hayo?”

    “Wale wapangaji wenzangu siwaelewi kabisa.”

    “Kivipi?”

    “Ah! Watu gani mimi mgeni nimehamia washindwe kutoka kunisalimia ili angalau tufahamiane?”

    Dalali alicheka sana kisha akasema:

    “Wale ndivyo walivyo bwana, si unajua tena malezi, mwingine kalelewa vile, mwingine hivi. Ila ulichokisema ni kweli, haiwezekani nyumba mnayoishi mpate mgeni halafu msitambuane, sasa mkikutana njiani je?”

    “Si ndiyo hapo sasa,” nilisema nikijifanya lawama zangu ni kwa ajili ya hilo tu, lakini kumbe nilikuwa na zaidi ya hapo.

    Kazini siku hiyo nilishinda sina amani, sina raha, mwili ulikuwa kama umetoka kufanya kazi nzito ambayo sijawahi kuifanya kwa siku nyingi, wenyeji wa Pwani wanaita mavune.

    Kwa upande mwingine nilitamani sana jioni ifike ili nikaone siku hiyo kitatokea kitu gani kipya kwenye nyumba ile. Jioni ilifika, nikaondoka kazini, sikutaka kupitia popote, dukuduku langu lilikuwa kwenda nyumbani tu.

    Nilichukua kama saa moja kutoka kazini hadi kufika nyumbani. Nje nilikuta mfuko wa rambo  mweusi, ndani yake ulionekana kuwa na kitu kwani ulikuwa umetuna sana. Niliinama kuipekenyua ili nijue ndani kulikuwa na nini, nilishangaa kuona ni vipande vya nyama za kuchoma tena vilikuwa vya moto.

    “Kha! Atakuwa nani ameweka?” nilijiuliza mwenyewe, nikauacha palepale, mimi nikapanda ngazi za kuingia ndani. Mlango ulikuwa wazi hali iliyoashiria kwamba, wenzangu walisharudi. Nilisukuma mlango, nikaingia. Nilikutana na harufu ya pafyumu, nikahisi walikuwa wakijiandaa kutoka.

    “Jamani za leo?” nilisalimia kwa sauti ya juu licha ya kwamba, mlango wao ulikuwa umefungwa, hakuna aliyeniitikia, hilo sikulijali sana kwani niliamini kwa kuwa walikuwa ndani, isingekuwa rahisi wasikie salamu yangu.

    Niliingia sebuleni kwangu, kisha nikaenda chumbani, kuna kitu kilinishangaza, nikasimama kwa mshtuko. Nilikuta sehemu nilipoweka kiberiti asubuhi siyo, nilikiacha juu ya meza, nikakikuta juu ya kitanda. Niliacha kioo na kitana juu ya kitanda, lakini nikavikuta kwenye stuli, niliguna!

    Nilikishika kioo na kukiangalia kwa umakini kama kina mabadiliko yoyote, lakini sikuona, nikashika kitana. Nilipokigaua sana pia sikuona kitu cha tofauti, nikaamua kuchania, nikahisi kuguswa na kitu kama nywele ndefu kama za mtu aliyefuga. Nilikiweka kitana juu usawa wa dirishani, nikaona nywelenywele nene, nyeusi, mwili wote ukasisimka.

    Ninavyojua mimi, mwanamke mwenye nywele nyingi akichania kitana, ndiyo huacha nywele, sasa mimi nilikuwa na nywele fupi sana zisingeweza kuacha nywele ndefu kwenye kitana.

    “Mh! Hapa kuna kinachoendelea,” nilisema moyoni huku nikikaa. Nilishtuka zaidi kuona soksi zikiwa kwenye msumari nyuma ya mlango wakati niliacha chini.

    “Huyu ni nani?” niliuliza kwa sauti ya ukali.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ghafla nikasikia kicheko kutoka chumbani kwa wale wenzangu.

    Nilikaa kwenye kochi, nikaanza kuangalia sehemu mbalimbali za mle ndani ambazo niliamini naweza kuona mabadiliko mengine mbali na yale ambayo nilishayaona, lakini sikubahatika.

    Nilitoka, nikaenda sebuleni ambako nako nilianza kuangalia kila kona ya sebule. Nilishangaa kuona glasi ya maji ya kunywa ambayo niliitumia asubuhi kisha nikaacha maji yamejaa, ikiwa haina hata tone la maji mbaya zaidi, iliwekwa juu ya kabati ambapo mimi niliiweka kwenye meza ya katikati ya sebule.

    “Mh! Hii kali sasa,” nilijikuta nikisema kwa sauti, mara nikasikia kicheko tena kutokea upande wa pili kule kwa wenzangu. Sasa nikaanza kama kuhisi kitu kuhusu watu hao. Ni kwa nini kila nilipoongea kwa sauti ndipo na wao waliangua kicheko?

    Niliamua kujaribu tena, nikasema kwa sauti:

    “Nitakuja kuua mtu, kweli tena.” Nikasikia kicheko tena, safari hii kilidumu kwa muda.

    Moyoni nikasema naanza kufanyia kazi uhusiano wa maneno yangu na vicheko vya wale majirani. Nilitoka kurudi chumbani, wakati napita kwenye korido, nilisimama jirani na mlango wao. Walikuwa wakiongea, lakini niliposimama mimi, kukawa kimya ghafla kama hakuna watu.

    Nilipozama chumbani, nyuma wakaanza kuongea tena. Sikufunga mlango ili niweze kusikia wanachokiongea, lakini jamani kwa kusema ule ukweli wa Mungu, sikujua walikuwa wakitumia lugha gani katika kuwasiliana hata pale nilipojitahidi kutega masikio kwa umakini wa hali ya juu sana.

    Kuna wakati utadhani wanatumia sana neno dotikom, lakini ukisema usikilize zaidi unasikia wakisema sana kotoko au kiburate, wakati mwingine sauti ya kike ilisema kaunto, ya kiume ikarudia hivyohivyo, kaunto.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog