Search This Blog

NILIPANGA NYUMBA MOJA NA MAJINI - 3

 





    Simulizi : Nilipanga Nyumba Moja Na Majini

    Sehemu Ya Tatu (3)





    Asubuhi, niliamka nikiwa nimechoka sana, lakini kabla sijatoka kitandani nilisikia nje ya mlango kukiwa na hali ya watu kutembeatembea tena kwa kasi, niliinua shingo ili nione kama nitasikia zaidi, lakini kukawa kimya.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Niliamka, nikatoka, nilikwenda sebuleni kwanza kuangalia kama kuko salama.

    Nilishangaa kukuta mezani kuna mfuko wa rambo uliojaa chipsi kuku kama nilivyonunua mimi, lakini zangu nilikula, sasa zile sikujua zilitoka wapi.

    Niliubeba ule mfuko nikatoka nao, nilifungua mlango mkubwa wa nje nikautupia pembeni kidogo, niliporudi, nikaenda chooni, mlango ulikuwa umefungwa kwa ndani kwani hata niliposhika kitasa na kukivuta kilikuwa kigumu.

     Hii iliashiria kwamba kuna mtu, kwa hiyo moyoni nilisema nisimame palepale nje ya mlango hadi atoke. Nilisimama eneo ambalo akitoka tu, uso kwa uso na mimi.

    “Tuone leo, wao si wajanja, leo nimemnasa mmoja wao,” nilisema moyoni.

    Dalili zote zilionesha kwamba mle chooni mlikuwa na mtu kwani niliweza kusikia hata kuhema kwake, mara mlio wa maji, mara alikohoa, tena kwenye kukohoa nikabaini mtu mwenyewe alikuwa ni mwanamke ndiye aliyekuwa mle.

    “We kohoa mpaka utapike, lakini mimi nipo hapa mpaka utoke,” nilisema moyoni.

    Nilikaa sana, ikafika mahali nikachoka, lakini moyoni nikasema siondoki hata iweje, lakini nilishtuka kitu, niligundua muda mrefu sijazisikia zile dalili kama maji au kuhema, nikafunguka akili.

    “Mh! Siyo kwamba ametoka?”

    Ile namalizia kusema ‘ametoka?’ nikasikia kicheko kutoka kwenye chumba chao. Vicheko vikubwa sana cha kike na kiume.

    Nilirudi chumbani mwili ukinisisimka, hapo ndipo niliamini mia kwa mia kwamba, nilikuwa nadili na watu wasiokuwa wa kawaida.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Niliingia chumbani, nikampigia simu dalali.

    “Haloo,” niliita.

    “Haloo. Halooo,” nilirudia lakini sikupokelewa.

    Nikiwa nimeachana na simu, mara iliita yenyewe, alikuwa ni dalali nikapokea.

    “Haloo,” niliita.

    “Haloo,” niliitikiwa lakini sauti haikuwa ya dalali.

    “Mzima bwana?” nilisalimia.

    “Tuone leo, wao si wajanja, leo nimemnasa mmoja wao.”

    Ha! Nilishtuka sana, nilisikia sauti yangu mwenyewe ikisema hivyo. Ikaendelea.

    “We kohoa mpaka utapike, lakini mimi nipo hapa mpaka utoke.”

    Nilikata simu, nilikuwa nahema sana, mapigo ya moyo yalikuwa yakienda kwa kasi ya ajabu huku nikishindwa kuona sawasawa.

    “Hii ni hatari sasa,” nilisema.

    ***

    Usiku wa siku hiyo sikulala kusema kweli kwani kila nilipofikiria maisha yale sikuona sababu ya kuendelea kuishi pale. Moyoni nilisema kwamba, ni afadhali ningeishi na watu ambao ni majambazi kuliko hawa, nafuu ningepanga nyumba moja na makahaba kuliko kupanga nyumba moja na majini.

    Nilichoamua, asubuhi nikifika kibaruani tu niombe ruksa kisha nianze kumsaka yule dalali na pia nitafute dalali mwingine ambaye atanitafutia vyumba kwingine na si maeneo yale tena kwani niliyaona yana nuksi.

    ***

    Asubuhi kulikucha salama kabisa, tena usiku wa siku hiyo sikuona mauzauza wala dalili zake. Nilikwenda kuoga bila kukagua mazingira, moyoni nilisema liwalo na liwe kwa maana kwamba, wawepo wasiwepo sawa tu.

    Bafuni niligundua wameshaoga kwani kulikuwa na majimaji ya muda mfupi uliopita. Nilipomaliza kuoga, nilijiandaa na kutoka. Nje nilikutana na mtu ana mkokoteni, akanisalimia.

    “Za asubuhi bwana mkubwa?”

    “Salama, karibu sana.”

    “Asante, kuna watu fulani wanaishi humu nina shida nao.”

    Aliposema hivyo nilishtuka sana, niliamini yeye ni mmoja wa wale ila amejigeuza kwa kujifanya ana shughuli za mkokoteni.

    “Unawajua kwa sura?” nilimuuliza huku nikiwa na wasiwasi maana alinikazia macho.

    “Siwajui.”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Sasa una shida nao kivipi watu usiowajua kwa sura?”

    Ni kwamba, kuna binti mmoja huwa wanamtuma niwaletee maji, nikifika hapa huyo binti anabeba madumu kupeleka ndani, sasa jana nilikutana na huyo binti nikamuuliza kuhusu malipo yangu ya mwezi sasa, akasema nije nifuatilie mwenyewe.”

    Nilishangaa sana kusikia hivyo. Nijuavyo mimi mle ndani mna watu wawili, mwanamke na mwanaume, sasa kama kuna binti hilo lilikuwa jipya kwangu, labda lakini.

    “Huyo binti naye anaishi humu au?” nilimuuliza.

    “Sidhani, inaonekana kama huwa wanamtuma tu.”

    “Kwa nini huamini kama anaishi humuhumu ndani? Hafanani na wao wenyewe?” hili swali niliuliza likiwa na mtego mkubwa sana, nilitaka nijue uhalisia wake.

    “Siwezi kusema hafanani wakati wao siwajui kwa sura.”

    Hapo ndipo nilipopataka, nilidhani atasema hafanani nao, ningejua ni walewale.

    “Oke, nadhani wameondoka kwenda kazini.”

    “Ah! Sasa mimi fedha zangu nitazipataje jamani?”

    “Subiri wakirudi jioni.”

    “Wewe utakuwepo?”

    Nililishangaa swali hilo, hakuwa akinidai mimi lakini anataka niwepo?

    “Unataka niwepo?”

    “Ee.”

    “Kwa nini?”

    “Naamini utanisaidia kuzipata fedha zangu.”

    “Uliwahi kuja wakagoma kukupa?”

    “Siyo hivyo, ila kila nikija, nikigonga mlango huwa hawafungui.”

    “Basi nitakuwepo.”

    “Asante kaka. Nije saa ngapi?”

    “Saa moja nitakuwa nimerudi.”

    Aligeuza mkokoteni na kuondoka zake huku akisema:

    “Muda huo nitakuwa nimefika kaka.”

    Niliondoka kwenda kazini kuomba ruksa. Lakini wakati naondoka, mfanyakazi mwenzangu mmoja aliniuliza nakwenda wapi, nikaamua kumsimulia kwa ufupi kisa changu.

    “Kha! Sasa hapo tatizo liko wapi, mbona dawa ipo rahisi sana.”

    “Rahisi! Ni ipi hiyo?”

    “Sikia, twende pembeni nikakusimulie,” aliniambia yule mfanyakazi mwenzangu huku akiangalia kulia na kushoto kama mabosi watatokea.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Tulikwenda kusimama pembeni, akaanza kuniambia:

    “Sikiliza, kama unaishi nyumba ya namna hiyo, unachotakiwa kufanya, kila siku asubuhi na jioni au usiku unapuliza bangi ndani ya nyumba, kama ni majini, mapepo sijui nini, utaona mambo poa kabisa.”

    Sikuamini maneno hayo, nikamuuliza mara mbilimbili kama ni kweli.

    “Khaa! Nina mjomba’ngu aliwahi kuishi kwenye nyumba ya hivyo, akaenda sehemu akaelekezwa dawa ni hiyo, akaitumia, mpaka sasa anaishi kwa raha hakuna cha majini wala mapepo,” alisema.

    Nilimsikiliza nikianza kuamini kwa mbali, lakini nilifika mahali nikamuuliza hiyo bangi mimi nitavuta au nitaiwasha ili itoe moshi yenyewe?

    “Ukishaiwasha, utaiweka mezani au popote ndani kwako, lakini angalia isizimike ili moshi wake usambae chumba kizima au sebule nzima.”

    “Hilo linawezekana,” nilimwambia nikimtumbulia macho.

    Kwa sababu nilikuwa nimeshaaga, ilibidi niondoke tu na kurudi baadaye. Nilikwenda mtaani, nilitafuta bangi nikapata maeneo ya Kariakoo, nikaitia mfukoni.

    Nilizurura sana siku hiyo, saa tisa kamili nilikuwa njiani narudi kazini. Nilipiga hesabu za kufika kazini na kuondoka, maana muda wa kazi ni saa tisa na nusu.

    Wakati napita pale Kituo cha Polisi Msimbazi, fujo zikazuka, kuna machinga wawili walikuwa wanapigana kwa sababu ya kugombea sehemu ya kufanyia biashara, katika ugomvi huo mimi nilibaini mmoja wao ndiyo mwenye kosa.

    Nikampa laivu kuwa yeye ndiye mwenye tatizo, alikuja juu, akachukua boksi lenye viatu na kunirushia, likanipata kwenye bega la kulia, sikukubali, nikaokota jiwe na kumrushia, likampata mkononi.

    Polisi walifika haraka sana, wakanikamata mimi, yeye na yule machinga niliyeona anaonewa, tukapelekwa Msimbazi polisi.

    Tulipofika pale, afande aliyetukamata alituamuru kuvua viatu, mikanda, simu kuweka pembeni. Halafu mmoja alianza kutusachi mifukoni. Wakati tendo hilo linaanza kwa wenzangu, ndipo nikakumbuka mimi mfukoni nina vipisi viwili vya bangi.

    Nilitaka kutoka mbio kituoni hapo, lakini sehemu tuliyokaa, ningesema nitoke, nisingefika nje au hata kama ningefika ningekamatwa au kupigwa risasi kama mhalifu, nilitetemeka, mwili uliisha nguvu.

    Ilipofika zamu yangu kusachiwa, askari mwenyewe alishangaa kuniona nachezesha miguu kama niliyebanwa na haja ndogo, akaniuliza:

    “We vipi, unaumwa?”

    Nikamjibu naumwa afande.

    “Unaumwa nini?”

    “Sijui, nadhani homa.”

    Hakunijibu, alianza kwa kutumbukiza mkono kwenye mfuko usiokuwa na kitu, akahamia wa nyuma ambao una waleti, akapeleka wa kulia kwangu ambao ndiyo wenye bangi, aliposhika, akakunja sura, alipotoa akashtuka sana na kusema:

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Haa! Hii bangi siyo?”

    Sikumjibu kwani niliamini ameshaijua, wenzake waliokuwa kaunta wakaacha mambo yao na kunigeukia mimi, nao wakashangaa sana. Mmoja alikuwa amekaa juu ya stuli, akashuka huku akiniangalia kwa kunikazia macho.

    “Unakuja kituo cha polisi na bangi, wewe unatutafuta nini sisi?” aliuliza yule aliyeshuka kwenye stuli.

    Niliambiwa nafunguliwa kesi ya pili, ya kwanza kupigana na kujeruhi ya pili kukutwa na bangi!

    Nilijitetea nikisema bangi ile si kwa ajili ya kuvuta bali nilikuwa nina shida nayo.

    “Wewe usitufanye sisi watoto wadogo, tunawajua ninyi raia,” alisema yule afande aliyenisachi.

    Lakini afande mmoja wa kike ambaye muda wote alikuwa akiangalia tu, akawaambia wenzake:

    “Lakini huyu kaka mbona hafanani na kuvuta bangi, muulizeni ana shida nayo gani?”

    Wale wenzake wakanigeukia na kuniuliza:

    “Haya, wewe mwananchi, raia kabisa, unaweza kuwa na shida gani na bangi mbali na kuvuta?”

    Niliwasimulia kila kitu, tena nilifika mahali nikawaambia kama kuna asiyeamini, tuongozane hadi nyumbani, Magomeni akaone maajabu ambayo hayahitaji kuelekezwa sana ili kuamini kama yapo au la!

    Palipita ukimya wa sekunde kadhaa, mmoja wao akaniuliza:

    “Kama ni kweli au tufanye ni kweli, ni kwa nini umemuumiza huyu?”

    Nilisema kilichotokea, yule chinga niliyemsaidia naye akanitetea kwa kusema hivyohivyo, lakini afande mmoja akasema nilijichukulia sheria mkononi ambapo ni kosa kisheria.

    Niliomba sana wanisamehe kwa yote, nikasingizia kwamba ni kwa sababu kichwa changu hakipo sawa kwa kuishi nyumba moja na majini.

    Namshukuru mmoja wao aliniambia niondoke lakini nihakikishe situmii bangi katika kujitibu kwani serikali haiamini kama bangi ni dawa.

    Nilipotoka, nilikwenda kununua nyingine, lakini akili iliingia hisia kwamba, huenda yule dada wa ajabu mle ndani ndiye anayecheza michezo ili kunikwamisha kwenda na bangi ndani ya nyumba, nikasema moyoni ngoja ninunue hii nione kitakachotokea, nikanunua tena misokoto miwili.

    Nilitembea kuelekea kituo cha daladala. Njiani nilimpigia simu yule mfanyakazi mwenzangu aliyenijulisha kuhusu dawa ya kutibu nyumba yenye majini, nikamwambia sitaweza kurudi kwani nilipata wakati mgumu kidogo njiani.

    Alinielewa, akaniuliza kama nimepata, nikamjibu kila kitu kimekwenda sawa, lakini sikumwambia kuhusu timbwili lililojitokeza.

    Nilipanda daladala nikashuka Magomeni, niliingia ATM kutoa fedha kidogo, kisha nikatoka. Wakati natafuta mwelekeo wa kwenda nyumbani, nilimkumbuka dalali, nikampigia simu.

    “Halo.”

    “Halo habari za kazi bwana?”

    “Nzuri, pole na kazi na wewe mwenzangu?”

    “Nimepoa. Bwana vipi kuhusu nyumba?” nilimuuliza.

    “Nyumba imefanyaje?”

    “Si nilikusimulia matatizo yake, umesahau?”

    “Kwani ulisema matatizo yake yakoje vile?”

    Nilimwelezea kwa kirefu, nikafika mahali nikamwambia hadi nilivyompigia simu halafu ikapokelewa na sauti ya ajabuajabu, alicheka sana.

    “Wewe bwana acha kunichekesha.

    “Kwa nini unasema hivyo?”

    “Yaani simu yangu mimi halafu apokee mtu mwenye sauti ya ajabuajabu, kwa nini sasa?”

    “Mimi pia sijui.”

    “We ulikosea namba.”

    “Labda bwana mi siwezi kukazania sana,” nilimjibu kwa kinyongo kwani namba yake niliisevu na ninapompigia huwa nasachi jina tu, sasa nilikosea kivipi?

    “Enhe, unasemaje bwana?” aliniuliza.

    “Nimeshakwambia bwana.”

    “Kwa hiyo unashauri nini?”

    “Nataka pesa zangu nikapange kwingine.”

    “Da! Hilo halitawezekana kirahisi bwana, maana mpaka nimpate mpangaji mwingine atoe fedha ndipo nikulipe wewe na mpangaji atakayekuwa tayari kutoa fedha lazima akute nyumba tupu, sasa wewe utalikubali hilo?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Naweza kulikubali, ila tuandikishiane.”

    “Kwamba?”

    “Kwamba unajikomiti nikiondoka, akiingia mpangaji mwingine tu unanilipa pesa zangu.”

    “Ngoja nitakupigia,” alisema dalali na kukata simu.

    Nilipokuwa nakaribia nyumbani, nikakutana na yule msukuma mkokoteni wa maji.

    “Kaka za kazi?”

    “Nzuri, vipi wewe?”

    “Niko sawa, ndiyo unarudi?”

    “Ndiyo.”

    “Najua jamaa hawajarudi, nitakuja muda uleule tuliopanga.”

    “Sawa, karibu sana.”

    “Asante sana.”

    Niliingiza funguo ili kufungua mlango, lakini nikagundua kwa ndani kulikuwa na funguo nyingine maana nilichungulia.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog