Search This Blog

NYAYO ZA DAMU - 2

 







    Simulizi : Nyayo Za Damu

    Sehemu Ya Pili (2)



    Wakati huo daladala iliyokuwa na watu wachache ilisimama kituoni, yule mwanamke aliyejitambulisha kwa jina la Nasra alikimbilia ndani ya gari na kuwahi siti mbili moja yake na nyingine ya mke wa Sule. Lakini mke wa Sule miguu ilikuwa mizito kuingia kwenye gari lile.

    Yule mwanamke aliyewahi kwenye gari alimwita ili akae kwenye siti iliyomshikia.

    “Shoga mbona umeganda kama sanamu, njoo nimekushikia siti.”



    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/


    “Tangulia shoga kuna mtu namsubiri.”
    Daladala ile iliondoka na kumuacha mke wa Sule kituoni, baada ya kuondoka alijikuta akijawa na mawazo juu ya yule mwanamke ambaye amekuwa akigeuka kila dakika mara Nargis mara mwanamke mwingine mara jina la Nargis mara Nasra.
    Japo magari yaliongezeka wazo la kwenda tena Bagamoyo alilifuta kwa siku ile, aliamua kurudi nyumbani kufanya shughuli zingine. Alirudi nyumbani taratibu hadi karibia na kwao, alipofika alishangaa kuwaona Thabit na Nargis wakitoka kuoga.
    Kwa vile aliwaona yeye kabla hawajamuona, aligeuza kwa kuamini yule mwanamke hakuwa Nargis bali wasi wasi wake. Lakini hakufanya kosa kwa vile asingeweza kuongozana naye Lugaro hospital sehemu ambayo haikuwa kusudio lake.
    Kwa haraka aligeuka na kurudi kituoni ili awahi safari yake ya Bagamoyo kwa mganga Kigobile. Alipofika kituoni kwa haraka alipanda daladala lililokuwa limejaa na kusimama hadi Mwenge. Alipofika Mwenge aliingia kwenye daladala ya kuelekea Bagamoyo.
    Alitulia kitini kwa vile siti zilikuwa zimebakia chache gari haikuchelewa, baada ya kuenea abiria kwenye siti iliondoka kituo cha Mwenge na kuelekea Bagamoyo. Moyoni mke wa Sule alimuomba Mungu amfikishe salama na mganga amkute. 
    Safari iliendelea huku akiwa amejituliza kwenye siti yake, gari lilivuka Tegeta huku likishusha abiria wa safari fupi na kupandisha waliokuwa wakienda Bagamoyo. Gari lilipofika Bunju mke wa Sule alishtuka kumuona mtu kama Nargis akitelemka katika gari alilokuwa amepanda na kushangaa mbona hakumuona muda wote mpaka wakati wa kushuka.
    Bado aliamini ni moyo wa wasi wasi wa kumuhofia Nargis, gari nalo liliendelea na safari yake kwa kushusha na kupandisha watu njiani. Alishangaa wote walitozwa nauri lakini yeye hakuguswa. Alijiuliza ina maana konda amemsahau au vipi.
    Gari lilisimama kituoni Bagamoyo, watu walitelemka, kwa vile alikuwa amekaa nyuma alikuwa wa mwisho kutelemka. Hakutaka kuondoka bila kulipa alifungua pochi yake alipe nauli.
    “Umeisha lipiwa dada yangu,” konda alimweleza mke wa Sule.
    “Na nani?” 
    “Na dada mmoja mrembo mwenye asili ya Kisomali.”
    “Mmh, dada mmoja alinijuaje?”
    “Mimi nitajuaje aliniambia na dada huyo hapo nyuma alikuonesha wewe.”
    “Mungu wangu, dada huyo alipandia wapi?”
    “Mlikuwa ameongozana kwa wewe kuwahi kuingia na kukaa siti ya nyuma na yeye alikaa ya mbele nyuma ya dereva.”
    “Mmh, alitelemkia wapi?”
    “Kwani vipi nakuona umejaa wasiwasi.”
    “Kaka yangu huu si muda wa maswali zaidi ya kusubiri jibu.”
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/


    “Dada yule aliteremkia Bunju”
    “Mungu wangu nimekwisha,” mke wa Sule alisema huku akishika kichwa.


    “Kwani vipi, mbona sikuelewi.”
    “Kaka yangu weee tuyaache.”
    “Kwani kuna ubaya dada yule alipokulipia?”
    “Hakuna tatizo, alitaja jina lake?”
    “Sikumuuliza jina lake kwa vile alikuwa na shida naye, ila alikuwa na mkufu mmoja wa Dhahabu wenye kidani kilichoandikwa jina la Nargis.”
    “Eti nani?” Mke wa Sule alishtuka kusikia jina lile.
    “Nargis”


    “Mungu wangu nimekwisha amenifuata mpaka huku.”
    “Kwani yule dada ana ubaya gani mbona anaonekana mstaarabu kama angekuwa adui yako asingekulipia.”
    “Mmh, makubwa.”
    “Kwani vipi dada?”Konda wa daladala alizidi kumshangaa.
    Mke wa Sule aliona anapoteza muda kwani hata kama angemueleza yule konda asinge msaidia chochote.


    “Hayana muhimu sana kuyajua,” 
    alisema huku akiondoka kuelekea maeneo ya mganga ambayo yalikuwa nyuma ya uwanja mkongwe wa mpira pale Bagamoyo wa Mwana Kalenge. Alitembea mwendo mdogo mdogo kuelekea kwa mganga huku moyo wake ukiwa mzito kwa kuamini huenda kila kona aliyopita lazima Nargis atakuwa yupo pembeni yake.
    Baada ya mwendo mfupi mke wa Sule alisimama ili aamue moja kurudi au aendelee na safari yake. Wazo moja lilikuwa arudi Dar japo ameisha fika Bagamoyo, lakini moyo mwingine ulimueleza aende kwa mganga huenda maeneo yale akaogopa kujitokeza.


    Aliamua bora aende kwa mganga kwani aliamini Nargis alikuwa akimhofia na ndiyo maana alikuta akimtolea vitisho.
    Alikwenda hadi kwa mganga bila kizuizi chochote na kuingia ndani ya uzio wa nyumba ya mganga, kulikuwa na watu wachache kama kumi. Naye alijisogeza kwenye foleni ya watu baada ya kusalimilia alikaa pembeni na kusubiri zamu yake.
    Ajabu ilipita zaidi ya saa nzima bila mtu aliyeingia ndani kutoka, ilibidi watu waanze kuzungumza juu ya mgonjwa huyo kuchelewa kutoka kwani alichukua muda mrefu. Baada ya muda pazia ilifunguliwa na mgonjwa aliyeingia kuonana na mganga alitoka.


    Mke wa Sule hakuamini alichokiona mbele yake, mgonjwa aliyetoka ndani kwa mganga alikuwa Nargis, hakukubaliana na macho yake aliyapikicha ili kuondoa wazo la kufikirika. Kabla hajapata ufahamu wa kitu alichokiona Nargis alimsamilia.
    “Ha! Mpenzi na wewe huku unafika?”
    Mke wa Sule mdomo ulikuwa mzito kwa kuamini bado kile alichokiona ni kiini macho.


    “Basi mimi natangulia tutakutana nyumbani.”
    Baada ya kusema vile bila kusubiri majibu ya mke wa Sule, Nargis aliondoka.
    Wakati huo wagonjwa wengine waliendelea kuingia. Japo alikuwa akisogea aliamini siri yake yote ipo nje hata akienda kwa mganga huenda alichokidhamiria kisitimia.
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Lakini alipiga moyo konde na kujisemea: “Liwalo na liwe.”
    Ilipofika zamu yake aliingia kwa mganga huku akiwa na mawazo lukuki kichwani juu ya kumueleza mganga kilichompeleka, akikiri adanganye na kuacha kukisema kilichompeleka huko Bagamoyo.
    Aliingia ndani kwa mganga na kukaribishwa kwenye mkeka.
    “Karibu mama yangu,” mzee Kigobile alimkaribisha.
    “Asante babu.”
    “Karibu uketi mjukuu wangu.”


    Mke wa Sule aliketi kwenye mkeka na kutulia kumsikiliza mzee Kigobile aliyekuwa akiweka vizuri dawa zake zilizokuwa zimedondoka chini kwenye kapu dogo lililokuwa pembeni yake. 
    “MH! Mjukuu wangu una shida gani?” alimuuliza bila kumtazama.
    “Babu mimi naitwa Mariamu Musa natokea Dar maeneo ya Buguruni...,” alitulia kidogo na kuendelea kusema.
    “Babu nina tatizo moja linanisumbua.”
    “Tatizo gani hilo?”
    “Mh!” Alijikuta akishindwa aanzie wapi hasa baada ya kumuona Nargis akitoka ndani, alishindwa kuelewa kule kwa mganga alifuata nini.


    “Vipi mama mbona upo mbali una tatizo gani?” Mzee Kigobile alimshtua katikati ya dimbwi la mawazo.
    “Eti mzee yule mwanamke alikuja kufanya nini?”
    “Mwanamke gani? Sina tabia ya kutoa siri za wateja wangu kwa vile kila mtu anayekuja hapa ana matatizo yake ambayo ni siri yake.”
    “Mh! Basi wacha tu nirudi nina imani huwezi kunisaidia.”
    “Mbona sikuelewi, huyo mwanamke unayemsema anahusiana vipi na matatizo yako?”


    “Ndiye aliyenifanya nifunge safari kuja huku.”
    “Mh! Una matatizo naye?”
    “Tena makubwa.”
    “Mwanamke gani huyo?”
    “Kuna mwanamke mrembo shombe wa Kiarabu.”
    “Shombe wa Kiarabu?” Mganga alionesha kushtuka.
    “Ndiyo tena alichelewa sana kutoka.”


    “Si kweli leo sijahudumia mteja kama huyo.”
    “Babu una siri gani na huyo mwanamke au babu siku hizi huwezi kutusaidia sisi wateja tusio na uwezo?”
    ”Binti mbona sikuelewi, akili yako ipo sawa?” Kauli ile ilimshtua mke wa Sule na kuamini huenda alichokizungumza sicho. Alikumbuka hata Msamvu Morogoro alipofika kwa miguu watu walimuuliza swali hilo hilo.


    Alituliza akili yake akiamini huenda hofu ndiyo iliyomtawala kufikia hatua ya kuchanganyikiwa na kufikia hatua ambapo kila apitaye mbele yake alimfananisha na Nargis.
    Baada ya kutulia kwa muda aliamini kabisa yote yanayomtokea ni viinimacho, lakini alikumbuka Morogoro alipotokea na haikuwa kiini macho bali wa ukweli. 


    Hapo alizidi kuwa njiapanda, lakini aliamini akifika kwa mganga ambaye anafahamika kuwa kiboko ya majini basi atakuwa salama zaidi.
    Alijikuta akiamua kusema ukweli huku akirudia kauli yake ya awali ya liwalo na liwe. Alijitengeneza vizuri na kuanza kumweleza kilichompeleka pale.
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Babu,” alianza kwa sauti ya chini kumwita mganga.
    “Rabeka.”
    “Nina tatizo.”
    “Tatizo gani?”
    “Kuna kitu kinanisumbua na kutishia uhai wangu.”
    “Kitu gani hicho mama?”
    “Kuna jini linanisumbua.”
    “Jini?”


    “Ee..ee.ee..ha.ha.a.pana,” mke wa Sule alipatwa na kigugumizi cha ghafla baada ya kumuona aliyekuwa akizungumza naye si mzee Kigobile bali jini Nargis. 
    “Eeh, unasema nani anakusumbua?”
    Mke wa Sule alituliza macho yake kuhakikisha kama alichokuwa anakiona mbele yake kilikuwa au kilikuwa kiinimacho.
    Aliyekuwa mbele yake hakuwa mganga Kigobile bali Nargis aliyekuwa amevaa kama mganga na kujifunga rubega na kiremba chekundu. Mwili wake alionekana wazi uliokuwa mweupe usio na doa.


    Mke wa Sule alifikicha macho tena asiamini aliyekuwa mbele yake ni Nargis kweli au amechanganyikiwa. Aliamini kama kweli ni Nargis basi adhabu yake ni kubwa ambazo alishindwa kuifananisha na kitu chochote.
    “Vipi mbona umepigwa na mshangao wa ghafla?” Sauti ya mganga Kigobile ilimshtua mke wa Sule ambaye alikuwa kama mtu aliyerukwa na ufahamu.


    Alipoangalia vizuri bado alibakia njia panda asipate jibu la kile alichokiona mbele yake, kilikuwa kweli au ni mauzauza ya dunia. Aliyekuwa mbele yake alikuwa mganga Kigobile na si Nargis.


    “Binti mbona sikuelewi tulikuwa tunzazungumza vizuri mbona umebadirika ghafla?”
    “Aaa..aa..babu,” mke wa sule alipatwa na kigagaziko.
    “Una tatizo gani?”


    Kabla ya kujibu alijiangalia kwa kujikagua kama ni yeye au mwingine, alipepesa macho kukiangalia chumba cha mganga ambacho hakikubadilika chochote na aliyekuwa mbele yake ni mzee Kigobile. Alivuta pumzi ndefu na kuzishusha alijipa moyo na kujisema kwa sauti ya ndani kuwa liwalo na liwe hata mbele ya sura yake asimame nani atasema shida yake.
    “Mmhu, binti mbona unaonekana haupo sawa?”


    “Ni kweli babu kuna mwanaharamu mmoja anataka kunichezea akili yangu, nahitaji msaada wako.”
    “Msaada upi maana nilipokuuliza ulichokisema ulishtuka na kukuona ukinishangaa kama nimegeuka simba.”
    “Ni hivi babu nyumba ninayo ishi kuna mpangaji mwenzangu tuna wasiwasi mpenzi aliyenae ni Jini.”


    “Kwa nini unasema hivyo?”
    ”Toka ameanza mahusiano kumekuwa na mambo ya miujiza ambayo si ya kibinadamu,” mke wa Sule alielezea yote aliyokutananayo toka alipoanza kumfuatilia Nargis na onyo alilopewa.”


    Mzee Kigobile baada ya maelezo yale alitoa simbi kwenye kikopo na kuzitazama kisha alizitupa juu ya msala wake. Aliziangalia kwa kuma huku akisoma moja baada ya nyingine kisha alinyanyua uso wake na kusema.
    “Binti.”
    “Abee babu.”


    “Ni kweli kabisa huyo mwanamke ni Jini, tena jini hilo lipo chini ya miamba bahari, lakini jini huyu ni mwenye huruma sana tofauti na majini mengine ni jini asiyependa kuua. Jini huyu anaitwa Nargis ambaye ana dada yake aitwae Hailati.
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Jini huyu alitokea kumpenda Thabit na kumlinda na kifo siku ambayo Thabit aliona miujiza pale kituo cha basi cha Mwenge. Aliweza kumshawishi Thabit na kukubali kwenda chini ya bahati kulala bila kujijua. Hata Thabit alikuwa na wasiwasi na mpenzi wake ambaye aliogopa kujitambulisha kwa kuhofia familia yake kumuua Thabit. 
    Jini Nargis alijikuta anaingia katika kazi ya kuua si kwa hiyari yake bali kwa shinikizo la dada yake. Kutokana na matatizo yaliyompata kutokana kutendwa na wanadamu basi wamekuwa maadui zao wakubwa.


    Nargis amekuwa akikutisha ili uache kumfuatilia lakini umekuwa mbishi, 
    tena kichwa ngumu.”
    “Sasa mganga maelezo hayo hayanisaidii utanisaidia vipi?” 


    “Nitakupa dawa za kufukiza na kuoga ili kumfanya asikufuate.”
    “Lakini shida yangu kubwa ni kummaliza kabisa.”
    “Kwa nini ummalize wakati yeye hakutaka kukumaliza.”


    “Siwezi kuishi kwa raha kama ataendelea kuwepo.”
    “Mmh, sawa nitakupa dawa hiyo ambayo inatakiwa ujasiri kaichimbie kwenye mlango wa Thabit akiiruka na mchezo unaishia palepale.”


    “Ndiyo ninayoitaka.”
    Mzee Kigobile alimpa mke wa Sule dawa ambayo alielezwa aifanye pindi afikapo nyumbani kwa kuanza kuichoma na kufukuza vitu vibaya majini na wachawi.


    Baada ya kulipa pesa aliaga na kuondoka, akiwa na furaha moyoni kwani aliamini amepata dawa ya kumkomesha adui yake. Alipofika kituoni alipanda daladala ambayo ilikuwa imebakiza siti chache, alibahatika kupata siti ya mbele alikaa kwenye siti yake kusubiri gari liondoke kituoni. 


    Baada ya daladala kujaa safari ya kurudi Dar iliwadia, alitulia kitini huku akiomba Mungu gari lifike salama ili akamuonesha Nargis kuwa yeye ni nani kama alimtembeza kwa miguu kwa siku tatu basi yeye atampoteza katika ramani ya dunia .


    Gari lilikwenda huku dereva akitembeza gari kwa kasi kutokana na barabara kuruhusu, mke wa Sule naye alikuwa akiimba taratibu nyimbo ya taarabu iliyokuwa ikiimbwa kwenye gari ile kwa kuifuatiliza.


    Gari liliondoka Bagamoyo na kuanza kuitafuta Bunju, dereva nae alizidi kukanyaga mafuta, gari lilopokuwa linateremsha mtelemko uliokuwa karibu ya daraja wote waliokuwa mbele walishangaa kuona mti mkubwa uliokuwa katikati ya barabara ambao ilikuwa vigumu kuukwepa na kasi ile.


    Dereva alijitahidi kwa uwezo wake wote kuukwepa ule mti mkubwa ulikuwa katikati ya barabara na gari kuhama njia na kuangukia chini ya daraja. 




    Abiria wote walipiga kelele za kuhofia maisha yao
    Gari liliangukia bondeni na kufanya watu wote wapate majeraha hata hivyo hakuna abiria aliyekufa, wasamaria wema walijitokeza kuwasaidia majeruhi hao. Mke wa Sule aliyekuwa amebanwa sehemu za kifua alibebwa na mtu mmoja aliyemuweka mbali na gari lililokuwa limepinduka.
    Dereva naye hakuamini baada ya gari kupinduka mti mkubwa aliouona awali hakuuona tena barabarani. Alipomuangalia mtu aliyekuwa akimsaidia mke wa Sule kwa kumnyoosha viungo vilivyokuwa vikimuuma, ghafla alihisi mapigo ya moyo nayanaenda kasi na kupata mshtuko uliosababisha apoteze fahamu. 
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Baada ya kupata ufahamu alijikuta kwenye miamba ambayo hakujua kule ni wapi pia kulikuwa na harufu kali, alisikia kama mawimbi yakipiga kwa nje kuonesha ni karibu na bahari akiwa peke yake amelala juu ya mwamba wenye baridi. Alisimama na kujiuliza yupo maeneo gani na alifikaje huko, kwani alikumbuka kwa mara ya mwisho alikuwa katika majeruhi waliopata ajali ya gari baada ya dereva kuukwepa mti hewa na kulifanya gari kupinduka.
    Kilichomshtua ni harufu ya mafuta ambayo hupendwa kutumiwa na adui yake Nargis.


    “Mariamu mwanamke katili,” sauti aliyoizoea iliisikia.
    Hakujibu bali mapigo ya moyo yalimwenda mbio na kujua siku zake za kuishi duniani zilikuwa zimefika kikomo. 
    Alipogeuka alikutana uso kwa uso na Nargis akiwa katika uso wa tabasamu tofauti na siku zote anapokasirika uso wake hugeuka kama wa mzee. Alihisi tumbo la kuhara likimshika kwa hofu, lakini Nargis aliendelea kutabasamu huku akipiga hatua taratibu kumsogelea.
    “Mariamu,” alisema huku akipiga makofi ya dharau, mke wa Sule alibakia kimya.
    “Mariamu nakuita sitaki kiburi, nimekusamehe sana huu ni wakati wa mimi kukuonesha ni nani, nina uwezo gani na nilichokuahidi nitakitimiza.”
    “Sa...sa...mahani Nargis,” mke wa Sule alipiga magoti mbele ya Nargis.


    “Niite Jini si Nargis.”
    “Ha...ha...pana wewe si Jini.”
    “Mariamu nimefanya kila hila uachane na nyendo zangu imeshindikana, kwa mdomo wako umedhamiria kuniangamiza. Mariamu nimekufanyia nini kibaya ambacho kimekufanya uwe adui yangu?
    Nimejitokeza kwa kila aina ili ujue kila ukifanyacho mimi nipo jirani yako, lakini inaonesha jinsi gani ulivyo na roho ngumu, Mariamu una masikio ya kenge husikii mpaka utoke damu na sasa muda wako umefika.


    Sina nia ya kukuua bali kukutesa japo wewe ulidhamiria kuniua, nimeipindua gari makusudi ili niweze kukupata baada ya kuipata dawa ambayo kweli ingeniangamiza. Baada ya kupinduka gari dawa zile zimepotea na kunipa nguvu za kukupata.
    Ni kweli wewe ni mwanamke jasiri ambaye hakika ulikuwa umefanikiwa kuniangamiza kwani baada ya kufika nyumbani nisingekuweza tena. Na kwa vile dawa ya mlangoni nisingeiona basi nilikuwa naangamia bila kujua.
    Mariamu hebu leo nielezee nilichokukosea mpaka kufikia hatua ya wewe kunitafuta usiku na mchana ili uniangamize?” Swali lile hakujibu alibakia kama bubu.
    “Mariamu usiniudhi nitakufanya kitu kibaya ambacho hujafanyiwa toka uzaliwe.” Uso wa Nargis ulibadilika na kuweka makunjanzi.
    “Kabla sijakujibu nieleze huku wapi na nimefikaje?” Mke wa Sule aliuliza kwa ujasiri huku moyoni akijisemea liwalo na liwe.
    “Huku ni chini ya mwamba bahari ambako huwafunga majini na wanadamu wenye kiburi, juu yetu kuna bahari kama unavyosikia mawimbi yake.” 


    “Haya nieleze shida yako nini kwangu?”
    “Sina shida na wewe ila nataka nitimize ahadi niliyokuahidi, nitakugeuza nguruwe na kwenda kukutia kwenye banda la nguruwe la jirani yenu na mwisho wa wiki utakuwa mmoja wa nguruwe watakaochinjwa.”
    “Eti?” Mke wa sule alishtuka.
    “Eeh, nilitaka kukutesa kama nilivyokuahidi lakini kila nitakapo kuona moyo wangu utakosa amani, lakini nawe ukipotea katika sura ya dunia itamaliza malumbano yasiyo ya msingi.”
    “Usinitishe fanya lolote huna uwezo wa kuniua ila Mungu pekee.”
    “Napenda viumbe wenye kiburi kama wewe.” 
    Baada ya kusema vile Nargis alimnyooshea kidole mke wa Sule na kumuamuru ageuke nguruwe.
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Kuanzia sasa maisha yako yatakuwa katika umbile la nguruwe.”
    Baada ya kusema vile pale pale mke wa Sule aligeuka nguruwe, lakini mke wa Sule kwake hakuona mabadiliko yoyote zaidi ya kujiona yupo kawaida.
    “Mbona sijabadilika?” Aliuliza kwa kiburi.
    “Mh! Sogea pale kwenye jiwe linalong’aa kama kioo ujione.”
    Mke wa Sule aliona utani kwa kuamini Nargis alikuwa akimuogopa na kuamua kumtisha kila kukicha. Aliposogea kwenye jile lile lililokuwa kama kioo alishangaa kuona mbele ya jiwe lile kuna nguruwe.


    Hakuamini alijaribu kuchezesha mikono nguruwe aliyembele yake alifanya vile, aliinamisha kichwa vile vile nguruwe yule alifanya vile. Kila alichokifanya nguruwe yule alifanya na kumfanya aamini kabisa yule nguruwe ni yeye.
    Lakini bado hakuamini alijua ni kiini macho tu Nargis cha kuendelea kumtisha ili aachane naye. 
    Akiwa bado anajiangalia asijimalize kama kweli yeye ndiye anayeonekana katika umbile la nguruwe Nargis alisogea karibu yake na kumsemesha.
    “Najua bado huamini ila mwisho wa wiki utaamini ukiwa mmoja wa nguruwe watakao chinjwa.”
    “Nargis usinitishe hiki ni kiini macho tu huwezi kunigeuza nguruwe wewe si Mungu,” Licha ya vituko vya Nargis, mke wa Sule hakutetereka.


    “Nitakuacha huku na usiku nitakufuata na kukupeleka kwenye banda la nguruwe wenzako.”
    Baada ya kusema vile Nargis aliondoka na kumuacha mke wa Sule chini ya miamba bahari. Hakumfunga kamba alimuacha huru na kumfanya mke wa Sule azunguke kila kona ya miamba ile bila mafanikio.
    Majira ya usiku Nargis alimchukua mke wa Sule aliyekuwa katika umbile la nguruwe na kwenda kumuweka katika banda la nguruwe kisha aliondoka na kumuacha mule. Kwa mara ya kwanza toka atoke tumboni kwa mama yake mke wa Sule alikumbana na adhabu kali.


    Ndani ya jumba lile kulikuwa na uchafu na harufu kali ambayo haivumiliki kwa mtu kukaa mule kwa muda mrefu, mwanzo alikuwa akijitahidi kuwakimbia wale nguruwe wasimsogelee kwani alijiamini kabisa yeye ni mwanadamu na wale ni nguruwe.
    Kwa kuwa alikuwa na muonekano wa nguruwe jike, nguruwe dume walimsumbua sana kumtaka kimapenzi kitu kilichomfanya akimbie bandani lakini hakuweza kutoka nje. Harufu kali ya nguruwe waliokuwa wakimsogelea kwa kuamini ni nguruwe mwenzao ilimkera sana.
    Siku hiyo alilala na njaa baada kushindwa kula uchafu waliokuwa wakila nguruwe, alitamani kufa kuliko mateso yale na kama Nargis angetokea mbele yake, angempigia magoti na kumuomba amuue au amsamehe.


    Njaa na kiu ilikuwa kali hakukuwa na maji zaidi ya maji ya tope ambayo nguruwe halisi waliokuwemo bandani walikuwa wakiogelea na kunywa. Alisogea pembeni ya banda na kuanza kulia kilio kilichokuwa kikitoa mlio wa nguruwe. 


    Muda ulivyozidi kwenda ndivyo kiu na njaa kali vilivyokuwa vikimshika, alihisi kizunguzungu huku nguruwe watoto wakimsogelea kutafuta kunyonya. Aliwasukuma kwa miguu na kuwapiga vikumbo vilivyowafanya waanguke chini na kumuacha. Mke wa Sule alimuomba Mungu amuue kuliko adha ile ya kuteseka kukaa na viumbe ambavyo ni haramu na najisi hasa yeye akiwa muislamu. 


    Kiu kilipokuwa kikali alijaribu kunywa maji yenye mchanganyiko na matope lakini alipofikisha pua yake maji yalimshinda kutokana na harufu kali yaliyokuwa yakinuka. Alijuta kumfuatilia Nargis kiumbe ambaye hakuwa na ubaya na yeye zaidi ya kumuonya asimfuatilie nyendo zake.
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Alijilaumu kwa kushindwa kuwa msikivu na matokeo yake kuishi kama nguruwe tena kwenye banda chafu lisilostahili mwanadamu kuishi. Alijiuliza ataishi vile mpaka lini na kukumbuka kauli ya Nargis ya yeye kuchinjwa mwishoni mwa wiki akichanganywa na nguruwe wengine.


    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog