Search This Blog

NILITAFUNA MAITI YA MWANANGU NIWE TAJIRI - 2

 







    Simulizi : Nilitafuna Maiti Ya Mwanangu Niwe Tajiri

    Sehemu Ya  Pili (2)





    ILIPOISHIA...

    Damu zilikuwa zimetapakaa chumba kizima! Rita mke wangu kipenzi, alikuwa akigaragara kitandani!

    Nikashtuka sana!

    SASA ENDELEA...



    NILIKODOA macho pale kitandani nikiwa siamini kabisa nilichokuwa nakiona. Ni kweli Rita alikuwa amelala pale kitandani akionekana mchovu sana. Hana nguvu.

    Damu ndiyo zilinitisha zaidi, kitanda kizima kilikuwa chapachapa, achana na kitandani, damu nyingine ilikuwa inachuruzika chini. Nilihisi kizunguzungu.

    “Rita...” niliita kwa sauti nikisogea kitandani kwa hadhari sana.

    Hakuitika.

    “Rita...” nikaita tena.

    Bado hakuitika.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Moyo wangu ukapigwa na butwaa, nilihisi ganzi ikiushika moyo wangu. Nikasogea taratibu na kumtingisha, hakugeuka. Nikaamua kumgeuza mwenyewe.

    Hapo ndipo niliposhuhudia macho yake yakifumbuka kwa mbali, akinitazama kwa huruma. Nilijaribu



    kumuita lakini hakuitika. Alionekana kutaka kuzungumza lakini ulimi wake ulikuwa mzito sana.

    Nilishaanza kuhisi kilichotokea.

    “Jikaze mke wangu, hebu niambie unajisikiaje?” nikamwuliza.

    “Nakufa Galos, nakufa baba.”

    “Hufi mpenzi wangu, hutakufa niamini mimi.”

    “Kila mtu atakufa Galos, lakini muda wangu wa kufa umefika.”

    “Najua kila mtu atakufa, najua hata wewe utakufa, lakini namaanisha kwa sasa hutakufa mpenzi wangu. Utakufa siku uliyopangiwa na Mungu itakapofika, siyo katika tatizo hili,” nikamwambia.

    “Mimba imeharibika tena,” akasema.

    “Najua mpenzi, pole sana.”



    “Lakini Galos kwa nini inakuwa hivi? Kwa nini nakuwa kama vile nimetoa mimba? Sijawahi kufanya hivyo na wala sitafanya hivyo, kwa nini tumbo liniume sana halafu baadaye damu ziwe kama hivi?

    “Hali itaendelea hivi hadi lini? Lazima tutafute ufumbuzi wa hili jambo, hatuwezi kuacha mambo yakawa hivi kila siku,” akasema mke wangu.



    “Narudia tena kukuambia mama, niachie mimi. Hebu kwanza tuyaache yote, ngoja tujitayarishe twende hospitali,” nikamwambia.

    “Hospitali?” akang’aka.

    “Ndiyo, twende hospitali, kwani hujanisikia.”

    “Siendi.”

    “Kwa nini?”



    “Kwani kuna nini cha maana ninachokifuata huko? Mara zote nilizokwenda walinisaidia nini? Hakuna cha maana kabisa. Acha tu nipumzike. Chemsha maji unikande.”

    “Hapana, unahitajika kwenda hospitali mke wangu Rita, kwani hujionei huruma?”

    “Najionea huruma sana, nataka kwenda hospitali sana lakini kwanza una pesa?” Swali lake likaninyong’onyesha moyo wangu.



    Aliuliza swali la msingi sana ambalo kiukweli lilijaa ukweli mtupu. Sikuwa na fedha, hivyo kama nilitaka kweli kumpeleka hospitalini nilitakiwa kuwa na fedha.

    “Sina mke wangu lakini nitapata tu,” nikamwambia mke wangu.

    “Utapataje?”

    “Najua mwenyewe.”

    “Galos mume wangu, unanisikiliza lakini?”

    “Nakusikiliza mama.”



    “Nisaidie tu kubandika maji jikoni kisha unikande, nitapata nguvu,” akasema kwa sauti iliyojaa uchovu, akionekana kutokuwa na matumaini kabisa.

    “Jiko lina mafuta?” nikamwuliza.

    “Ndiyo...mafuta yapo kidogo, kwa kuchemsha maji tu, yanatosha sana.”

    “Sawa.”



    Haraka sana nikawasha jiko la mafuta, maarufu kama jiko la Mchina, nikamimina maji kwenye sufuria kisha nikabandika juu yake. Baada ya hapo, nikamgeuza mke wangu upande na kutoa lile shuka lenye damu.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nikakusanya sehemu moja, kisha nikadeki zile damu pale chini. Baada ya kuwa pasafi kabisa, maji nayo yalikuwa yameshachemka kabisa. Nikayaepua na kumimina kwenye ndoo ya plastiki.

    Nikachukua na mengine ya baridi kidogo, nikayachanganya ili kupunguza ule ukali. Nikamsaidia mke wangu kuteremka pale kitandani, nikamfunga kanga mbili, moja kiunoni na nyingine kifuani.



    Tukaongozana hadi bafuni, nikamkanda vizuri kisha nikamwogesha.

    Akajisikia nafuu kidogo. Nikamrudisha chumbani. Ilibidi nitandike kitanda kwanza ndipo apande. Nikampaka mafuta kisha nikamfunika na shuka, akapumzika.

    “Unajisikiaje sasa?” nikamwuliza.

    “Nguvu kidogo lakini njaa.”

    “Usijali mke wangu, nisubiri.”



    Nikatoka mbio kwenda kwa rafiki yangu Patrick. Bahati nzuri nilimkuta.

    “Vipi Galos,” akaniuliza.

    “Poa..”

    “Vipi? Mbona sikuelewi? Wale waliokuchukua ni akina nani na kwa nini ilikuwa vile?” akaniuliza akionekana kuwa na hofu.

    “Ilikuwaje?”



    “Wakati mimi nakuletea pesa uliyosema, nilishangaa kuwaona wale watu wakitaka kukuchukua mkukumkuku, nikajikuta narudi nyuma kiajabuajabu.”

    “Kivipi yaani,” nikamwuliza.



    “Nilishangaa nakosa nguvu ya kukufuata, kifupi nilijikuta narudi nyuma bila ridhaa yangu, lengo lilikuwa kuja kukusaidia lakini sijui nini kilitokea nini, kifupi nahisi kama ni nguvu za kishirikina.

    “Kwani wale ni akina nani na ilikuwaje wakakuchukua? Halafu walikupeleka wapi? Unajua sielewi kabisa,” akasema Patrick mfululizo kiasi cha kunifanya nishindwe kumjibu kwa haraka.



    “Kaka hebu tuachane na hayo kwanza, nimejia ile pesa kaka, bado nina matatizo makubwa sana ndugu yangu.”

    “Sawa lakini ilikuwaje?”



    “Kaka afya ya mke wangu kwa sasa ndiyo muhimu kuliko kitu kingine chochote, tafadhali nisaidie kwanza hiyo pesa niende nikamsaidie halafu mengine yatafuata baadaye,” nikamwambia.

    Patrick hakuzungumza kitu tena, alinikazia macho kwa sekunde kadhaa kisha akaingiza mkono mfukoni na kutoa noti moja ya shilingi 10,000, akanikabidhi.

    “Ahsante sana.”

    “Usijali kaka.”



    Nilitoka mbio hadi dukani, nikanunua unga wa sembe nusu kilo, kisha nikapitia kwa Mama Nishe, nikanunua chakula. Ilikuwa ni wali na samaki, nikawekewa kwenye mfuko mdogo wa Rambo.



    Nilipofika nyumbani, kwanza nikampikia mke wangu uji na kumsihi anywe, akajitahidi kunywa. Alipotosheka akarudi tena kulala.



    Nikatoa kile chakula kwenye mfuko wa nailoni na kuweka kwenye sahani, nami nikaanza kula. Nikiwa katikati ya mlo wangu, mawazo yakaanza kunisonga tena kuhusu kule Rukwa waliponipeleka wale akina Mango na Ngoma.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nikaanza kuwaza kuhusu marehemu baba yangu, mzee Matima Mtimandole. Niliumiza sana kichwa, lakini sikupata kiungio mahali popote kuwa baba yangu alikuwa mchawi.

    “Yaani baba alikuwa mchawi? Kweli? Haiwezekani...” nikajisemea mwenyewe moyoni mwangu.

    “Inawezekana sana na wewe unatakiwa kulipa deni letu. Nimeshakuambia acha kiburi. Labda



    nikuambie, tayari usajili unaendelea. Ile juisi tuliyokunywa , haikuwa ya matunda kama ulivyodhani.

    “Ile ni juisi ya damu, tena damu mbichi kabisa. Damu iliyotoka kwenye mimba ya mkeo tuliyoiharibu. Leo jioni tunakuhitaji makao makuu haraka,” sauti hii iliyojaa muungurumo mkali niliisikia.



    Sikupata shida kugundua kuwa alikuwa ni mzee Mukulungu ambaye kule huitwa Mkuu. Nilibaki natetemeka, nisijue cha kufanya. Kwa kweli niliogopa sana!



    MAPIGO ya moyo wangu yalibadilika kabisa, yalikwenda kwa kasi kuliko kawaida. Niliangalia huku na huko, sikuona kitu. Nilibaki kama niliyepumbaa kwa muda ambao sikuujua.

    Nilitetemeka sana!

    “Nakuuliza, umenielewa?”

    “Sijaelewa. Kifupi sikuelewi? Kwa nini msiniache na maisha yangu?”

    “Hatuwezi kukuacha wakati kuna deni la baba yako. Hilo ndilo linalokutesa, vinginevyo tungekuacha huru.”

    Nikazidi kuchanganyikiwa, kila aliponiambia kuhusu baba yangu, akili yangu ilizubaa. Baba yangu anaingiliana vipi na mimi? Labda ni kweli alikuwa mchawi, maana sikuwahi kuona kiashiria chochote kutoka kwa mzee wangu, ambacho kilimkaribisha na mazingira ya uchawi.



    Hata kama ikiwa kweli, kwa nini mimi niingizwe kwenye mambo yao? Kwenye mikataba ambayo siifahamu na sijui makubaliano yao? Kwa nini?

    Kwa hakika nilichanganyikiwa sana!



    Nilitamani kuepukana na mkasa ule, lakini sikuwa na uwezo. Sikujua nilitakiwa kutoa jibu gani kwa yule mzee. Nilibaki kimya tu natetemeka, lakini cha ajabu, mke wangu Rita akiwa haonekani kugundua chochote.

    “Mimi na baba tunahusiana vipi?”

    “Swali la kipumbavu kabisa...hujui uhusiano wako na baba yako? Mnahusiana damu. Halafu hicho kiburi chako wewe, tulipaswa tuwe tumeshakuua, bahati yako ni mtoto wa mwisho.”

    “Niacheni jamani. Niacheni niendelee na haya maisha yangu kama yalivyo.”

    “Hatuwezi kuendelea kubishana, jioni utakuwa makao makuu, kwa heri.”



    Muungurumo mkali ukasikika, sauti kama radi ikafuatia kisha nikahisi kama upepo mkali sana ukivuma kwa kasi, kisha kukawa shwari!!!

    “Kwa nini mimi?” nikasema kwa sauti.

    Hapo ndipo Rita alipojitahidi kujigeuza na kuniangalia. Sauti ile aliisikia vyema, inamaana kuwa, muda wote ule hakusikia kitu chochote nilichozungumza...



    “Kuna nini mpenzi wangu?” akaniuliza akionekana kunionea huruma ya wazi kabisa.”

    “Acha tu mama.”

    “Usijali nitapona mke wangu, najua ni kwa kiasi gani unaumia. Najua ni kwa kiwango gani huna



    furaha kutokana na hali hii niliyonayo, lakini jipe moyo, nitakuwa sawa!”

    Hapo nikawa na uhakika zaidi kuwa, Rita hakuna alichokuwa akikijua. Sikutaka kumwambia chochote, isingekuwa sawa kumwambia kuwa mimba zake zilikuwa zinatoka kwa sababu ya kafara ya majini ambayo yalikuwa yanafanya kisasi.



    Sikutaka kabisa ajue jambo hilo, hiyo niliendelea kuifanya siri iliyokuwa katikati ya moyo wangu. Nilimsihi atulie, nikamwambia sikuwa na tatizo kubwa bali nilichanganywa na namna mimba zake zilivyokuwa zikiharibika kila mara.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/



    “Nataka sana watoto mpenzi, natamani kuona vurugu za watoto wetu humu ndani, ndiyo maana unaniona sina raha,” nikamwambia.

    “Hata mimi pia, ndani ya moyo wangu natamani sana jambo hilo, ndiyo haja ya moyo wangu



    mpenzi. Tutulie, muda ukifika mambo yatakuwa mazuri,” akasema Rita akiwa hajui kabisa kilicho kichwani mwangu.

    Nikajituliza kisha nikaendelea kula chakula changu. Sikuwa na raha kabisa. Nilipomaliza nilipanda kitandani, kisha nikajilaza, kichwa changu kikiangalia juu ya dari, mawazo tele yakiwa yamenisonga!

    ***



    “Galos! Galos! Galos...” kwa mbali nilisikia nikiitwa jina.

    Sikugeuka, nilihisi nilikuwa ndotoni. Ilikuwa usiku wa saa sita, nikiwa nimelala na mke wangu Rita ambaye wakati huo alikuwa akisema kuwa hali yake iliendelea vizuri.

    Nikapuuza!

    “Galos! Galos! We Galos...” sauti ile ikaendelea kuita.

    Nikatulia, nikatingisha mwili wangu kidogo ili kujihakikishia kuwa sikuwa ndotoni. Ni kweli sikuwa kwenye ndoto kama nilivyokuwa nikifikiria awali.

    “Galos!” sasa ikaita kwa sauti ya juu kidogo.

    “Nani?” nikauliza.



    Mtu huyo alikuwa akiniita kupitia dirishani. Pamoja na kumwuliza alikuwa ni nani, hakujibu kitu. Dakika ya kwanza ikakatika, ikafuata ya pili! Nikashindwa kuvumilia.

    “Wewe ni nani?”

    “Naitwa Ngoma.”

    “Ngoma?” nikauliza kwa mshtuko dhahiri.

    “Ndiyo ni Ngoma, nipo na rafiki yangu Mango.”

    “Naomba muondoke kwangu,” nikasema kwa hasira.



    “Wewe huna ubavu wa kutufukuza, nadhani ni vema kama ukitoka mwenyewe ndani tukaondoka.”

    “Kwenda wapi?”

    “Makao makuu.”

    “Haiwezekani.”



    “Itawezekana,” alijibu huku tayari akiwa ameshaingia ndani kwangu.

    Sikujua ni nani kati yao aliyeingia ndani, lakini niliona mtu mmoja tu. Alisimama mbele ya kitanda chetu, akaniangalia kwa macho yaliyoonekana kung’aa sana kwa mwanga mkali, kisha akapuliza dawa fulani ya unga iliyokuwa kwenye kiganja chake...

    Nikapoteza fahamu!

    ***



    Kwa harakaharaka niliwaona watu kama kumi wakiwa wamekaa kwenye zulia kwa mzunguko. Ulikuwa mduara mkubwa, halafu mimi nilikuwa nimekaa katikati. Mbele yangu kulikuwa na nyama mbichi, tena inayochuruzisha damu!



    Wale watu wote walikuwa wameinamisha vichwa vyao chini. Nikawaangalia, lakini hakuna aliyeniangalia hata mmoja. Cha kushangaza, sikuwaona Ngoma, Mango wala Mkuu.

    Muda kidogo, nikasikia vishindo, nikawaona watu wawili wakiingia. Nilipowaangalia nikagundua walikuwa ni Mango na Ngoma.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wale watu wakainua vichwa vyao juu mara moja na kuviinamisha tena. Kidogo, akaingia Mkuu akiwa amevaa joho linaloburuzika chini!

    “Mkuuu!” Mango na Ngoma walisema kwa wakati mmoja.

    Watu wote wakasimama wakati mkuu akiingia. Akaonyesha ishara kuwa wote waketi – wakafanya hivyo. Akabaki yeye mwenyewe akiwa amesimama. Tofauti pekee niliyoiona ni kwamba, wale watu waliokuwa wameinamisha vichwa vyao, sasa walikuwa wameviinua!

    Mkuu akaanza kuzungumza...



    “Nina furaha sana jioni ya leo. Tunakwenda kufanya tukio moja kubwa sana...kuna mgeni hapa kama mnavyoona na kama nilivyowapa taarifa zake. Anaitwa Galos. Jambo la kufurahisha ni kwamba ameshakunywa damu ya mwanaye. Zoezi lililobaki ni kula maiti ya mwanaye.



    “Zoezi hilo halitafanyika leo, kwa leo anatakiwa kusaini mkataba na kuanza kazi mara moja. Kuna mambo mawili tu, asaini maisha yake yabadilike yawe mazuri au asisaini, tumuue, mimi ninywe ubongo wake,” akasema Mkuu.

    “Sawa Mkuu,” wote wakaitikia wakiinamisha vichwa chini.

    “Galos...” Mkuu akaniita.

    Sikuitikia!

    Siyo kwamba nilionyesha kiburi, sikuweza kufanya hivyo!



    KAMA moyo ungekuwa unaweza kuonekana, naamini bila shaka yoyote moyo wangu ungeonekana ukiwa unatetemeka kwa hofu. Sikuwa na hili wala lile. Nilihisi kuchanganyikiwa.

    Niliinua uso wangu na kuwatazama wale watu waliokuwa wamenizunguka, nikawaona kama wananikodolea macho mimi wakinishangaa.



    Nikazidi kuchanganyikiwa. Kuna mambo matatu yalikuwa yakiuchanganya sana ubongo wangu. Kwanza kuhusu mkataba! Naweza kusaini mkataba wa kishetani?

    Naweza kuingia kwenye makubaliano nisiyoyaelewa? Inamaana mimi niwe mchawi? Niliwaza. Kwa mtu yeyote mwenye akili timamu lazima jambo hilo lingemchanganya kama ilivyokuwa kwangu.



    Pili ni kuhusu kunywa damu! Mimi nilikunywa damu ya mwanangu? Inawezekana vipi? Ni kweli nilipewa kitu kama juisi ambayo ladha yake sikuijua mara moja, lakini kwa nini niambiwe ilikuwa ni damu ya mwanangu?



    Damu ya mwanangu kivipi? Lingine kubwa kabisa lililoniumiza ni kuhusu kula maiti ya mwanangu. Nitaweza kumtafuna mwanangu? Kwa muda mrefu kiasi gani mimi na mke wangu tumehangaika kupata mtoto na mimba zinatoka!



    Leo iweje nije kula maiti ya mwanangu? Ni mambo ambayo yalizidi kunikoroga! Kwa namna fulani niliona ni bora kufa kuliko kula maiti ya mwanangu. Potelea mbali hata kama Rita atabaki katika mateso lakini hatanyanyasika tena maana atapata mwanaume mwingine ambaye atamzalia watoto.



    Mimi nisingeweza kumpa watoto kwa sababu tayari nilikuwa kama kafara la majini! Moyo wangu ulijaa huzuni sana, nikapata nguvu mpya na jeuri ya hali ya juu kunijaa moyoni. Nilimwangalia Mukulungu kwa hasira, sura yangu ikatangaza dharau ya wazi.

    Nilionekana waziwazi nilikuwa tayari kwa lolote!



    Ni kama nilikuwa nimejipanga sawasawa. Nikazidi kumkazia macho bila kuyapepesa kabisa. Naye akaniangalia kwa ukali. Muda uleule, nikaona kitu kama machozi yakidondoka machoni mwa Mukulungu. Nilipotazama vizuri, niligundua jambo jingine la kushangaza sana.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Macho ya Mukulungu yalikuwa yakidondosha damu! Tena ilikuwa damu mbichi kabisa!

    “Galos! Galos! Galos!” akaita kwa ukali.

    “Ukali wako haunitishi,” nikajikuta nimetamka kwa haraka nikiwa najiamini kuliko kawaida.

    Pamoja na woga niliokuwa nao tangu mtiririko wa tukio lile ulivyoanza, nilijishangaa sana kupata nguvu ya ajabu na ya ghafla sana mbele ya Mukulungu ambaye aliogopwa na kila mtu!



    “Unasemaje?”

    “Nipo tayari kwa lolote!”

    “Umeuuzunisha moyo wangu. Kwa hakika moyo wangu sasa unavuja damu....damu inachuruzika. Sasa nitakuuliza kwa mara ya mwisho kabla sijachukua hatua inayokustahili. Uko tayari kusaini mkataba au haupo tayari?” akauliza Mukulungu akinikazia macho.

    “Sipo tayari!”

    “Unasema?”

    “Sipo tayari.”

    “Galos, una hakika na kinachotoka kinywani mwako.”

    “Nasema sipo tayari kusaini ujinga!”



    “Paaaaa! Paaaaa! Paaaa!” ilikuwa ni mlio wa mikanda ikishuka mwilini mwangu.

    Sikuelewa ni nani aliyenipiga na alikuwa wapi. Nilihisi maumivu makali sana, mwili wangu ukaishiwa nguvu ghafla na nikahisi kutapika. Nilijilazimisha kutoa matapishi lakini haikuwezekana. Nikajitahidi tena na tena lakini haikuwezekana.



    “Mpelekeni kwenye hatua ya pili haraka! Huyu nitamalizana naye mwenyewe, hana ujanja huyu. Mpumbavu kabisa. Wa kumlaumu ni baba yako aliyeingia mkataba na sisi!” akasema Mukulungu.



    Wale watu haraka wakanivaa. Kila mmoja alikuwa akinisukuma huku akinipiga sehemu anayoona inamfaa. Ndani ya dakika kumi tu, tayari kila kiungo katika mwili wangu kilikuwa kimeshapigwa. Nililainika na nilipatwa na maumivu makali kuliko kawaida.



    Waliniburuza hadi kwenye chumba ambacho sikukielewa kilivyokuwa, lakini muda mfupi sana baadaye, nilipoteza fahamu kabisa! Sikujua chochote kilichoendelea.

    ***



    Nilihisi maumivu makali sana miguuni, mwili wangu ulikuwa una joto kali kuliko kawaida, baadaye nikagundua kuwa siyo joto tu, ni moto mkali ulikuwa unatembea mwilini mwangu. Nilipofumbua macho, nilishangaa kujiona nimening’inizwa, kichwa chini, miguu juu.



    Miguu yangu ilikuwa imefungwa kwa mnyororo juu ya kamba, mikono yangu ilikuwa chini lakini nayo ilikuwa imefungwa kwa mnyororo, chini kukiwa na moto ambao ulikuwa ukinielekea pale juu nilipokuwa nimefungwa!

    Nilikuwa nachomwa kama nyama!



    Ni eneo ambalo sikulijua ilikuwa ni wapi, lakini ilikuwa pembeni ya kitu kama ziwa au bahari, maana niliona nipo ufukweni. Nilipoangalia kando nikamuona Mukulungu akiwa na wenzake wawili wananitazama.



    Wote walikuwa wamekenua meno yao wakinicheka. Mukulungu ndiye aliyekuwa amebeba kitu kama faili lenye makaratasi. Akaacha kucheka na kusogea karibu yangu. Akanitazama kwa macho ya hasira sana. Alionekana kuwa na neno alilotaka kuzungumza...



    “Utakufa hapo mtini taratibu kama ng’ombe anavyobanikwa baada ya kuchomwa. Hili ni zoezi la mwisho kwako. Ni adhabu ya mwisho. Narudia tena hakuna adhabu nyingine, maana adhabu hii itakufikisha moja kwa moja kwenye kifo.



    “Sasa ni hiyari yako kusema, upo tayari kusaini mkataba uendelee na maisha yako na tukupe utajiri au ufe hapo mtini ukibanikwa kama nyama ya ng’ombe?” akasema Mukulungu akiniangalia kwa macho yanayosubiri majibu.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “SITASAINI UCHAFU WENU, KAMA KUFA NIPO TAYARI KUFA!”



    nikamjibu kwa kujiamini.

    Nilihisi maumivu makali sana lakini sikuwa tayari kabisa kujiunga na mambo nisiyoyajua wala sikuwahi kuyaota. Nilikuwa tayari kwa lolote! Mukulungu na wenzake wakaonekana kunishangaa sana!

    “Unasemaje wewe?” Mukulungu akauliza.

    “Nilivyosema ndiyo hivyohivyo!”

    “Ongeza moto tafadhali,” akasema Mukulungu.

    Muda huohuo, moto ukaongezeka ghafla. Nikahisi mwili mzima ukiungua.





    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog