Search This Blog

SAFARI YANGU YA KWANZA KUZIMU - 2

 





    Simulizi : Safari Yangu Ya Kwanza Kuzimu

    Sehemu Ya Pili (2)



    Uchawi upo ndugu yangu, tena umejaa sana katika nyumba za ibada. Kwa kile nilichokiona kwa mchungaji yule kiliyafumbua macho yangu na kuona kwamba hakukuwa na mtu aliyetakiwa kuaminika katika dunia hii.

    Niliyoyaona yalitosha sana na hivyo kumwambia Yusnath kwamba alitakiwa kunitoa mahali pale na kunipeleka kule tulipotoka ili niweze kuwaona watu wengine, hilo halikuwa tatizo, akaniambia nifumbe macho, nikafanya hivyo na nilipofumbua tu, tayari tulikuwa tumefika.

    Kwenye kundi lile la watu waliokuwa wamepiga magoti akiwemo mchungaji yule aliyependa kujiita mtume, kulikuwa na mtu mwingine ambaye nilimfahamu sana, alikuwa mwanasiasa mkubwa ambaye alipendwa na watu wengi.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nilimwangalia, sikuamini kama na yeye alikuwa mahali pale, uso wangu ulionyesha kutokukubaliana na kile nilichokuwa nikikiona hivyo nikamuuliza Yusnath kama yule niliyekuwa nikimuona ndiye yule niliyekuwa nikimfahamu au macho yangu yalichanganya? Akaniambia ndiye mwenyewe.

    Huyu alikuwa mwanasiasa mmoja mkubwa anayejulikana kwa jina la Abuzael John. Alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wakitikisa sana Tanzania kutokana na umahiri wake katika kuteka akili za watu mara anaposimama jukwaani na kuzungumza.

    Huyu naye alikuwa kule kuzimu akimuabudu shetani kitu kilichonishangaza sana. Yusnath alijua jinsi nilivyochanganyikiwa mara baada ya kumuona mtu huyo mahali hapo, hivyo alivyotaka kukifanya ni kunionyeshea maisha ya huyo mtu.

    “Nataka nikuonyeshee maisha ya huyu mwanasiasa,” aliniambia.

    “Sawa, hakuna tatizo.”

    Kama kawaida akaniambia nifumbe macho, nilipofumbua baada ya sekunde kadhaa, tulitokea katika ule mlima wa kutisha ambapo mbele yetu kulikuwa na televisheni kubwa, ikawashwa na kuanza kumuona Abuzael akiwa ofisini kwake.

    “Unataka kuona nini?” aliniuliza Yusnath.

    “Nione jinsi anavyofanya kazi zake za kishirikina,” nilimjibu.

    “Hakuna tatizo. Subiri.”

    Yusnath akayafumba macho, sikujua alikuwa akifanya nini kwani alikaa kimya kwa muda fulani kisha kuyafumbua macho yake, nilipoyapeleka macho yangu katika televisheni ile, nikaona Abuzael akiwa sehemu moja iliyokuwa na msitu mnene sana.

    Hapohapo Yusnath akanichukua na kuwa kule alipokuwa mwanasiasa yule yaani kila kitu alichokuwa akikifanya ni kama nilikuwa pembeni yake. Nilimuona akitembea huku akionekana kuwa na mawazo mno, alionekana kutokuwa na furaha hata mara moja.

    Alikuwa akitembea kwa mwendo wa taratibu sana, alipokuwa akielekea, sikuwa nikipafahamu. Alizidi kupiga hatua mpaka katika kijumba fulani kidogo, kilikuwa kimetengenezwa kwa udongo na nje ya nyumba ile kulikuwa na fimbo kubwa iliyokuwa imesimikwa.

    Alichokifanya Abuzael ni kugeuka nyuma, akavua suruali yake na kuyaacha makalio nje kisha kuingia ndani ya nyumba ile kinyumenyume. Mpaka hapo nikapata jibu kwamba pale alipokuwa kulikuwa kwa mganga, hivyo na mimi nikaingia huku nikitaka kujua alikwenda kufanya nini.

    Kilio chake kikubwa kwa mganga yule kilikuwa ni kupata ubunge Aliongea huku akilalamika kwamba hakuwa akipendwa na watu wa jimboni kwake, wengi walimchukia na kumuahidi kwamba iwe isiwe asingeweza kurudi tena bungeni, yaani kipindi kile cha karibia na uchaguzi ndiyo ungekuwa wakati wake wa mwisho kuingia bungeni kule.

    Alionekana kuhitaji sana msaada kwani hata uongeaji wake ulionyesha hilo. Mganga yule alibaki akimwangalia tu, kwa mtazamo alioutumia kipindi kile, ulionyesha kumuonea huruma mno.

    “Ninataka ulete mkono wa albino,” alisema mganga yule huku akimkazia macho.

    “Unasemaje?”

    “Nadhani umenisikia, ukifanikiwa, utapata ubunge,” alisema mganga yule.

    Abuzael alionekana kuwa na mawazo mno, hitaji alilopewa lilionekana kubwa sana lakini hakuwa na jinsi, alitakiwa kufanya kama alivyoambiwa afanye. Alionekana kumuamini sana mganga yule, nahisi ndiye aliyekuwa akimfanyia kazi zake katika kipindi alichokuwa akigombania kila mwaka na ndiyo maana alidumu sana katika ngazi ya ubunge.

    Baada ya kuambiwa hivyo, mganga akamwambia kwamba ainuke na amfuate kule alipotaka kwenda, akamchukua na kuelekea naye porini zaidi. Walitembea huku kila mmoja akiwa kimya, kwa Abuzael alionekana kuwa mwingi wa mawazo, bado kichwa chake kilikuwa kikifikiria ni kwa namna gani angeweza kupata nafasi ile ambayo alikuwa akiililia kila siku.

    Walitembea mpaka walipofika katika mti mmoja mkubwa. Katika mti ule, kulikuwa na tunguli nne zilizokuwa zimefungwa vitambaa vyekundu huku kukiwa na kitambaa kikubwa kilichokuwa na rangi nyeusi, kilifanana na kaniki.

    “Subiri tuite nguvu zaidi ili upewe dawa ya kufanya kutokugundulika,” alimwambia mganga yule na kuanza kuzungumza maneno yasiyoeleweka.

    Katika kila kitu kilichokuwa kikiendelea, niligundua kwamba watu walikuwa radhi kufanya jambo lolote lile lakini mwisho wa siku wafanikiwe maishani mwao. Mbunge huyu alionekana kuwa na uchu wa madaraka, hakutaka kuwa mwananchi wa kawaida.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alichekwa sana jimboni kwake, watu walisema hafai hata kidogo hivyo kuamua kumfuata mganga huyo aliyempa sharti kubwa ambalo kwangu lilionekana kuwa kubwa ila kwake, halikuwa kubwa sana. Aliendelea kubaki kimya huku mganga yule kiendelea kuzungumza maneno yasiyoeleweka, ghafla nikaanza kuona moshi mkubwa na mzito ukifuka kutoka katika kitambaa kile. Nikaogopa.

    *****

    Sikujua ni kitu gani kilikuwa kinaendelea mahali pale kwani kufuka moshi kwa kitambaa kile kulizidi kuniongezea hofu zaidi. Niliendelea kumwangalia mzee yule huku macho yangu wakati mwingine yakikiangalia kitambaa kile.

    Hapohapo huku moshi ukiendelea kufuka, ghafla nikaona kitu kama sura za watu zikitokea katika kitambaa kile. Mganga yule aliendelea kuzungumza maneno yasiyoeleweka na baada ya dakika chache sana, nikaona kitu kama kisu kikitokea chini ya mti ule mkubwa, kilikuwa kisu chenye makali pande zote na kilifungwa kwa kitambaa cheusi.

    “Chukua hicho kisu,” alisema na hivyo mzee yule kuchukua kisu kile.

    “Unachotakiwa ni kutumia kukatia viungo vya albino kwa kisu hiki,” alimwambia.

    “Ooppss...!”

    “Pia nitakupa dawa ambayo utawaambia watu wote watakaohusika kuwateka albino wasionekana kirahisi, yaani wawe wanapoteapotea machoni mwa watu. Na kazi yote itakayofanyika, ni lazima uwepo,” alisema mganga yule.

    Mzee yule ambaye alikuwa mwanasiasa akapewa maelekezo yote ambayo alitakiwa kufanya mara baada ya kutoka mahali pale. Nilibaki nikimwangalia, watu walimchukulia kuwa mtu mpole na mara nyingi vyombo vya habari vilikuwa vikimpamba kwamba tangu nchi ipate uhuru hakukuwa na mtu aliyekuwa mpole bungeni kama yeye.

    Nyuma ya pazia mzee huyo alikuwa mbaya mno, ilikuwa ni afadhali kumuamini tapeli kwa kumpa fedha zako akufikishie nyumbani lakini si kumwamini mzee huyu. Mara baada ya kukabidhiwa kila kitu, akaondoka mahali hapo.

    Hatukuishia hapo, Yusnath akaanza kunionyeshea mambo mengine ya huyu mzee, tayari alikuwa amewaita vijana wake na kuwapa maagizo kwamba alikuwa akihitajika albino kwa ajili ya kumkata kiungo chochote kwa ajili ya kazi maalumu hivyo vijana wale wakaondoka kwa ajili ya kufanya kazi.

    Ikaonyesha upande mwingine kwamba tayari vijana wale walikuwa mitaani, walikuwa katika mishemishe yao ya kumvizia mtoto mmoja wa kiukme ambaye alikuwa albino kwa ajili ya kufanya kile walichokuwa wameagizwa kukifanya.

    Walikuwa wakijipitisha sana katika nyumba aliyokuwa akiishi albino huyo mtoto, baada ya dakika kadhaa alipotoka nje, wakajipaka unga maalumu ambao walipewa na yule mzee na kisha mmoja wao kumfuata kijana yule.

    “We mtoto njoo,” alisema jamaa mmoja.

    “Shikamoo kaka,” alisalimia mtoto yule.

    “Marahabaaa....hujambo?”

    “Sijambo.”

    “Hebu twende huku,” alisema mwanaume yule.

    Ndugu yangu, kila kitu kilichokuwa kikitokea nilikuwa nakifuatilia kwa macho yangu. Ule unga ambao alikuwa ameupaka kijana yule na wenzake ulikuwa na mvuto fulani wa kichawi ambapo hata mtu gani angeambiwa amfuate, asingeweza kukataa.

    Mbali na hivyo, hata nyie watu mliokaa pembeni mlipokuwa mkimuona mtu huyo akiondoka na mtoto wala msingeshtukia kitu chochote kile, yaani mngechukulia kawaida sana.

    Walimchukua mtoto yule na kuanza kuondoka naye. Hakuonekana kuwa na wasiwasi hata kidogo, uchawi aliokuwa amefanyiwa ulimfanya kuwaona watu wote kuwa ndugu zake kama walivyokuwa watu wengine, hivyo akaanza kutangulizana nao.

    Walikwenda mpaka kwenye moja ya magari waliyokuja nayo na kuondoka naye. Moyoni nilihuzunika sana lakini Yusnath akaniambia kwamba nisihuzunike kwani kama ningefanya hivyo basi asingeendelea kunionyeshea mambo mengi zaidi.

    “Usihuzunike...” aliniambia.

    “Sasa nifanye nini kama naumia?”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Fanya vyovyote lakini usihuzunike, kuna mengi nitakuonyeshea,” aliniambia Yusnath.

    Kabla ya kuona kile kilichokuwa kikitokea mara albino walipokuwa wakichukuliwa, nilikuwa nawalalamikia polisi kwamba ilikuwaje mpaka hao watu wasikamatwe? Siku hiyo ndiyo nikagundua kwamba ushirikina unatumika sana.

    Waliondoka na yule mtoto mpaka katika mkoa aliokuwa akitokea yule mzee na huko ndipo walipomwambia kwamba mzigo aliokuwa akiutaka tayari ulikuwa umekwishaletwa mahali hapo.

    “Hakuna cha zaidi, fanyeni kazi,” alisema.

    “Lakini na wewe si utakuwepo au?”

    ‘Ndiyo! Ni lazima nishuhudie,” alisema na kisha kuelekea huko.

    Ndugu yangu, naweza kukwambia kwamba katika dunia hii tuna watu wenye roho mbaya mno. Madaraka yanatafutwa kwa nguvu sana, watu wanauawa kinyama kwa sababu ya fedha na vyeo. Ninachokuhadithia hapa, si kwamba nimeahadithiwa bali ninakwambia kile kitu kilichokuwa kikitokea na nilikishuhudia kwa macho yangu.

    Mpaka katika kipindi hicho, tayari niliwaona watu wawili, mchungaji na mwanasiasa. Yusnath aliniambia kulikuwa na watu wa aina mbalimbali ambao duniani waliheshimika sana, hivyo sikutakiwa kuwa na haraka kwani angeniambia mmoja baada ya mwingine.

    Baada ya kwenda kule alipokuwa yule mtoto, wakaanza kumkata mkono kitu kilichousisimua sana mwili wangu. Mtoto yule ambaye alifungwa kitambaa machoni kwa ajili ya kutomuona mzee yule aliyekuwa akijulikana sana, alikuwa akilia lakini hakukuwa na mtu aliyejali chochote kile, walichokuwa wakikitaka ni kukamilisha kazi zao.

    Niliyashuhudia yote hayo kwa macho yangu mawili na wala sikuhadithiwa. Baada ya kuukata mkono ule huku damu zikiendelea kumtoka huku akilia kwa maumivu makali mno, wakamuacha kwanza apumzike.

    “Kuna chochote kinahitajika?” aliuliza kijana mmoja.

    “Ndiyo! Tunahitaji miguu pia, unajua hawa watu ni mali sana, nikipata viungo vyote, nitavuiuza kwa wenzangu wengine,” alisema mzee yule na hivyo kuanza kuikata miguu ya mtoto yule. Kila nilivyokuwa nikiangalia, mwili ulinisismka mno. Hayo ndiyo maagizo aliyokuwa amepewa na mganga kwamba viungo vya albino vilikuwa vikihitajika kwa hali na mali.



    Niliyoyaona, yalitosha kabisa, sikutaka kuendelea kuona zaidi kuhusu maisha ya mwanasiasa huyu bali kitu nilichokifahamu kwa wakati huo ni kwamba mwanasiasa huyo alikuwa mtu mbaya sana na hakutakiwa kupendwa hata mara moja.

    Walimkata viungo vilivyobakia kitu kilichopelekea kifo cha yule mtoto, moyo wangu uliumia sana lakini sikuwa na jinsi, sikujua ni kwa jinsi gani ningeweza kumsaidia kwani nilichokuwa nikikiona pale hakikuwa kitu kilichokuwa kikitokea wakati huo, ni kama kilirekodiwa.

    Nilimwambia Yusnath kwamba ninahitaji anitoe hapo na kama kulikuwa na mtu mwingine wa kumuona basi afanye hivyo, basi akanichukua na kunirudisha kulekule kuzimu, mtu ambaye alitaka kunionyeshea ambaye alikuwa mahali hapo ni mwanaume mmoja mwenye ndevu nyingi nyeupe, kwa kumwangalia usoni, hakuonekana kuwa mpole sana lakini inawezekana alikuwa mkali hasa wakati wa kuongea. Nilimwangalia mzee yule, hakuonekana kuwa mgeni machoni mwangu, kila nilipomwangalia, nilihisi kwamba niliwahi kumuona mahali fulani japokuwa sikupakumbuka.

    “Huyu ni mtu mwenye heshima kubwa, unamfahamu?”

    “Hapana! Ila sura yake si ngeni machoni mwangu.”

    “Anaishi Manzese Midizini,” aliniambia Yusnath.

    Hapo ndipo nilipata kumbukumbu juu ya mtu huyu aliyekuwa amesimama mbele yangu. Niliweza kumgundua kwamba alikuwa Muislamu mkubwa ambaye alipewa cheo kikubwa na msikiti mmoja maeneo ya Manzese. Kama ilivyokuwa kwa mchungaji yule aliyepita, hata huyu shekhe naye alikuwa kule kuzimu.

    Nilihuzunika sana, viongozi hawa wa dini hizi mbili walipewa majukumu makubwa ya kuwafanya watu kwenda peponi lakini mwisho wa siku, nao walikuwa kule kuzimu wakiendelea kumuabudu yule shetani.

    Mzee huyu, kila siku ya Ijumaa alisimama mbele ya waumini wa dini hiyo na kuwasisitizia watu kwamba walitakiwa kumswalia Mungu. Ndugu zangu, kila nilichokiona kule kuzimu kilinisikitisha sana na kuona kwamba dunia ilipokuwa ikielekea si pazuri kabisa.

    Sikutaka kujali sana, nilimwambia Yusnath kwamba nilitaka kuangalia maisha ya mzee huyo kama nilivyoyaona maisha ya mchungaji na mwanasiasa yule, hapo ndipo aliponichukua na kunipeleka kule kulipokuwa na televisheni.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Huko, nilimuona mzee yule akiwa amesimama sehemu moja iliyokuwa na giza totoro, alikuwa amevalia kanzu yake kubwa na macho yake aliyapeleka juu huku akiongea maneno yasiyoeleweka. Nilijaribu kumwangalia mikononi nikagundua kwamba alikuwa na hirizi moja kubwa iliyofungwa na kitambaa chekundu.

    Muda, ilikuwa ni saa nane na nusu usiku. Yusnath akaniambia kwamba alikuwa akijiandaa kwa ajili ya kwenda kuswalisha. Alikaa katika hali ile kwa dakika kadhaa, ghafla nikaanza kusikia sauti za miungurumo, ilifanana na miungurumo ya radi.

    Huku nikiendelea kuangalia kila kitu kilichokuwa kikitokea, ghafla nikamuona mwanamke mmoja akija mbele yake. Alikuwa mwanamke mzuri sana, naweza kusema kwamba sikuwahi kumuona mwanamke mwenye sura nzuri kama aliyokuwa nayo huyo.

    Alimsogelea mzee yule aliyekuwa ameyapeleka macho yake juu na kisha kumshika ndevu zake. Ghafla, nikaanza kuona vitu kama shotishoti vikiiingia mwilini mwake kupitia ndevu zake zile.

    “Ndiyo nini ile?” niliuliza.

    “Anaingiziwa nguvu ili aendee kuwapoteza watu wengi zaidi duniani,” alinijibu Yusnath.

    Sikiliza ndugu yangu, nilipelekwa kuzimu kwa kuwa kulikuwa na baadhi ya vitu nilitakiwa kuonyeshwa, nilitaka kufahamu mengi sana hivyo akaanza kuniambia mambo mengine kuhusu huyu mzee.

    Heshima kubwa aliyokuwa nayo duniani ilionekana si lolote lile, alikuwa akisifiwa kutokana na ukarimu wake mkubwa lakini ukweli ni kwamba huyu mzee hakuwa lolote lile. Watu wengi walimheshimu, walimuita katika sherehe za Maulidi mbalimbali huku akipewa sifa kubwa lakini mzee huyo hakuwa kama watu walivyomfikiria.

    Alikuwa mtu hatari sana ambaye kazi yake kubwa ilikuwa ni kuviua vyuo vya madrasa vingi kama moja ya njia zake za kuweza kusimamisha kazi zao.

    Hiyo ndiyo ilikuwa kazi yake ambayo aliifanya mara kwa mara. Vyuo hivyo viliongezeka lakini hakukuwa na maendeleo yoyote yale. Ukiachana na hivyo, kulikuwa na misikiti mingi ambayo ilikuwa na kusudio la kuendelea zaidi lakini shehe huyu alikuwa na kazi moja ya kuhakikisha misikiti haikui zaidi.

    Alisababisha roho chafu kwa watu wengine misikitini, unapoona watu wanagombana wenyewe kwa wenyewe, ilikuwa ni kazi ya huyu mtu. Hapo ndipo nilipoamini kwamba shetani alikuwa bize kuhakikisha kwamba kila kitu kinaokwenda sawa kwa upande wake.

    Migogoro mingi, majivuno na vitu vingine misikitini vilisababishwa na huyu mzee. Fedha zake zilitumika kujenga matabaka na kufanya vitu vingine.

    Alipomaliza kupewa nguvu na mwanamke yule mrembo, nikamuona mzee yule akiondoka mahali hapo, kuja kuonyeshwa, nilimuona akiwa amesimama katika uwanja mmoja mkubwa wa wazi, ulikuwa ni uwanja wa mpira wa miguu lakini sikujua ulikuwa maeneo gani.

    Mzee yule alisimama akiwa mtupu huku mkononi akiwa na tunguli moja kubwa iliyofungwa kitambaa chekundu. Alikuwa akizungumza maneno ya ajabuajabu, mbali na ule mkono aliokuwa ameshika tunguli, mkono mwingine ulikuwa umeshika kuku mwekundu ambaye akamuweka chini kuanza kumchinja.

    “Kwa nini anachinja kuku mahali hapa? Naye anahitaji kunywa damu?” nilimuuliza Yusnath.

    “Hapana.”

    “Sasa kwa nini anafanya hivyo?”

    “Anatafuta nguvu ya ziada ya kusonga mbele.”

    “Sasa kupitia kuku!”

    “Ngoja nikwambie kitu, hakuna kitu chenye nguvu duniani kama kutoa kafara ya damu. Kitu kinapowekwa kwa kutumia damu huwa na nguvu sana. Mtu anapotaka kuua kwa kutumia damu, kazi hufanyika kwa haraka sana, mtu anapotaka mafanikio kwa kutumia damu, hufanyika kwa haraka zaidi ya kitu chochote kile,” aliniambia Yusnath.

    Niliwahi kusikia hilo kipindi cha nyuma kwamba kafara ya damu huwa na nguvu na hata Yusnath alivyokuwa akiniambia, nilikubaliana naye kwa asilimia mia moja kwamba huo ndiyo ulikuwa ukweli wenyewe.

    Mbali na hayo aliyokuwa akiyafanya, mzee huyu alikuwa mfuga majini nyumbani kwake. Mambo mengi aliyokuwa akiyafanya, alielekezwa na majini ambayo yalikuwa ndani ya nyumba yake.

    Hakuwa mzee wa kuchezewa, alichokifanya Yusnath alitaka kunionyeshea roho mbaya ya huyu mzee. Nilimuona akiwa amesimama nje ya nyumba yake, alionekana kuangalia kitu ambacho wala sikukiona, uso wake ulikunjwa kwa hasira na hakutoa tabasamu hata mara moja.

    Sikujua aliangalia nini lakini alionekana kuchukizwa na kitu fulani hivi. Huku nikimwangalia kwa makini, ghafla nikamuona mwanaume mmoja akija kwa kasi kule alipokuwa, alionekana kukasirika sana. Kijana huyo alikuwa na panga mkononi.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Wewe mzee nitakuua,” alisema kijana huyo huku akisimama na akionekana kuwa na hasira mno. Kila alipokuwa akiongea, alimnyooshea panga lile.

    “Na wewe nitakuua, tena kuwa makini kijana,” alisema mzee yule, hakuonekana kuogopa kitu chochote kile.

    Kwa kuwa walikuwa wakiongea kwa sauti kubwa, watu waliokuwa pembeni waliposikia wakaanza kusogea kule walipokuwa wale watu na hatimaye vita vya maneno kuanza kuzuka mahali hapo, kila mtu aliyekuwa akimwambia mwenzake, walipeana vitisho vya kuua tu pasipo kujua tatizo lolote lile. Ghafla mzee yule akazidi kupandwa na hasira, nikajua kuna kitu kingetokea mahali hapo.



    Watu walizidi kukusanyika mahali pale wakiwasikiliza watu hao waliokuwa wakipeana vitisho kwamba yeyote angeweza kumuua mwenzake. Hakukuwa na mtu aliyeingilia, labda kwa sababu wengi waliyafahamu maisha ya huyu mzee huyu aliyeitwa Hamisi tena huku wengine wakimsonta kidole kijana yule aachane naye lakini hakutaka kuacha, aliendelea kumwambia kwamba angeweza kumuua.

    “Kijana anatafuta balaa, huyu mgeni nini?” aliuliza mzee mmoja.

    “Si mgeni, ni mwenyeji kabisa.”

    “Sasa kwa nini anampiga mkwara huyu mzee, hamjui nini?”

    “Anamjua sana, si unajua hivi visifa vya vijana wetu,” alisema mzee mwingine.

    Mzee Hamisi hakutaka kuzungumza kitu, alichokifanya ni kuondoka mahali hapo na kuingia ndani huku akiwa amefura kwa hasira. Kijana yule hakutaka kuondoka, alijiona kuwa bingwa na kuona mpinzani wake ameshindwa.

    Alitukana na kutukana huku mikwara ikiendelea kusikika mdomoni mwake lakini mzee Hamisi hakurudi nje, aliendelea kubaki mulemule ndani kwake. Nakumbuka kijana yule alichukua zaidi ya dakika tano zaidi kutukana na kisha kuondoka.

    Usiku ulipoingia, nikaanza kumuona mzee Hamisi akiwa kwenye mti mmoja mkubwa uliokuwa katikati ya uwanja mmoja mkubwa wa mpira. Mahali hapo alisimama peke yake na baada ya dakika kadhaa, kulikuwa na idadi kubwa ya watu waliofika uwanjani hapo.

    Kila mtu alikuwa mtupu, haikujalisha kama ni mtu mzima, mtoto au kijana, uwe mwanaume au mwanamke, unapokuwa hapo ulitakiwa kuwa mtupu. Niliwaona wanawake wawili wakiwa wamebeba chungu kimoja kikubwa na kukipeleka mbele kabisa kisha mwanamke mmoja aliyeonekana kuwa mtu mzima kusogea karibu na kile chungu.

    “Leo ni siku ya kuleta mahitaji yenu na kufanyiwa kazi,” alisema mwanamke yule, sauti yake ni kama ililazimishwa iwe ya kutisha.

    Ngoja nikwambie kitu. Miongoni mwa mambo mengi niliyoambiwa na Yusnath ni kuhusu siku maalumu ambayo hutumika kwa ajili ya kupeleka mahitaji yao kwa ajili ya kufanyiwa kazi. Wachawi hutenga siku maalumu kwa ajili ya kufanyia kazi matatizo yao.

    Siku hiyo, kama kulikuwa na mtu aliyekuwa akiwasumbua, labda kuna mtu ambaye hakuwa akirogeka kirahisi basi siku hiyo jina lake lingetumbukizwa ndani ya chungu kile na kisha kufanyiwa kazi.

    Kama mtu huyo hakuwa na nguvu zozote zile basi angepata kile walichokuwa wakitaka akipate, labda ugonjwa wa kudumu na mambo mengine mabaya ambayo mchawi anataka mtu huyo ayapate.

    Baada ya kuambiwa hivyo, nikamuona mzee Hamisi akisogea karibu na chungu kile kisha kusimama huku akiwaangalia wachawi wengine waliokusanyika uwanjani hapo. Alionekana kuwa na hasira, alikuwa kama mtu aliyepagawa hivi, kila mtu akabaki kimya akimsikiliza.

    “Nimekasirishwa sana mkuu,” alisema mzee Hamisi huku akiwa ameyageuzia macho yake kwa mwanamke yule aliyeonekana kuwa kiongozi mahali hapo.

    “Sema chochote kile, tutalifanyia kazi,” alisema kiongozi.

    “Kuna kijana amenikera sana,” alisema mzee Hamisi.

    “Unataka tumfanye nini?”

    “Awe kichaa tu ili iwe fundisho kwa kila mtu mtaani,” alisema mzee Hamisi.

    “Anaitwa nani?”

    “Ramadhani.”

    “Sawa. Ombi lako limekubaliwa. Weka jina lake katika chungu hicho.”

    Alichokifanya mzee Hamisi ni kukiingiza kikaratasi kilichokuwa na jina la kijana yule, Ramadhani katika chungu kile kilichokuwa kikitoa moshi mkubwa kisha kwenda kusimama na wenzake.

    Siku hiyo ilitumiwa vilivyo, kila mmoja alikuwa na kazi ya kuchukua kikaratasi kilichokuwa na jina la mtu aliyekuwa akitaka kumfanyia jambo na kukiweka katika chungu kile. Ndugu yangu, asikwambie mtu kwamba unapokuwa mchawi basi utakuwa na maisha yenye uhakika kwamba kila kitu utakachokitaka basi kitafanikiwa.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kuna wachawi wanakutana na vitu vya kutisha mno, kuna wengine kazi zao zinashindwa na hivyo kujikuta wakikamatwa. Mchawi yeyote yule anayekamatwa kwa uzembe wake basi ni lazima apewe adhabu kule kuzimu.

    Hii ndiyo sababu inayowafanya wengi kupeleka majina ya wabaya wao. Kulikuwa na watu wagumu kurogeka, kuna wengine wana kinga kali, mchawi anaposhindwa kumroga, basi huenda kwenye uwanja wao wa makutanio na kueleza kile kilichotokea.

    Anachokifanya mchawi mkuu ni kuchukua lile jina na kuliweka kwenye kile chungu kisha kumpa mtu huyo nguvu na kurudi. Anaporudi, huwa na nguvu ya ziada, atakaposhindwa kwa mara nyingine, hapo ndipo wanapoongeza nguvu, yaani haendi mmoja, wanakwenda na wengine hata watano, wanaposhindwa hapo ndipo wanapotafuta njia nyingine.

    Kuna wachawi wengine huwa wanakufa kazini, wengine wanapata misukosuko mingi, yote hiyo wanaita ajali kazini na mara nyingi hutokea kwani si kila mtu huwa rahisi kurogeka.

    Mara baada ya mzee Hamisi kuliweka lile jina katika chungu kile, akawa na uhakika kwamba kile alichokuwa akikitaka ni lazima kingefanyika tu kwani aliamini kwamba kijana yule hakuwa na nguvu kubwa, hata kama alijiamini kwa kumpiga mikwara, bado alijiona kuweza kumfanya kijana yule kuwa kichaa.

    Uchawi ukatumwa!

    *****

    Niliuona uchawi ukianza safari kumfuata kijana yule aliyeitwa kwa jina la Ramadhani ili uweze kumdhuru na kuwa kichaa. Katika upande wa pili nilimuona Ramadhani akiwa amekaa chumbani kwake, alionekana kuwa na mawazo mno, alionekana kama mtu aliyekata tamaa kwa jambo fulani.

    Nikauona ule uchawi unaingia ndani. Ndugu yangu, huwezi kuuona huu uchawi kama hauna nguvu fulani. Sikuwa kwenye ulimwengu wa kibinadamu bali nilikuwa kwenye ulimwengu wa kijini. Ule uchawi ulipofika mlangoni, ukaingia ndani kwa ajili ya kumvaa kijana yule.

    Sikujua nini kilitokea, nilimuona Ramadhani akishtuka, akasimama harakaharaka na kukunja ngumi mikono yake, kitu cha kushangaza, uchawi ule nao ukasimama. Sijajua kama Ramadhani alikuwa akiuona au la, alichokifanya ni kufungua droo yake ndogo ya kitanda na kuchukua kikaratasi kimoja kilichoandikwa maneno mengi kwa Lugha ya Kiarabu na kisha kuanza kukisoma kwa harakaharaka.

    Ule uchawi ukamfuata na kumvamia, nikasikia sauti kubwa ya radi ikipiga, ule uchawi nikauona ukishindwa kumuingia na hapohapo kupotea katika mazingira ya kutatanisha.

    “Mmmh!” nilijikuta nikiguna.”

    Usiku huohuo nikauona uchawi ule ukirudi mpaka kule ulipotumwa. Hakukuwa na hali ya kawaida, kila mtu alipouona ukija, akakimbia mahali pale na kusimama pembeni kabisa ya uwanja ule, ule uchawi, kutokana na nguvu kubwa iliyokuwa nao, ukakivunja kile chungu hivyo wachawi wote kujua kwamba ule uchawi ulikuwa umeshindwa.

    “Ni lazima tuungane, mtu mmoja hawezi kututisha,” nilimsikia mzee mmoja akizungumza maneno hayo, alikuwa mbali kabisa na aliogopa kusogea kule kilipokuwa chungu kile.

    Baada ya dakika tano tena walipoona hali imetulia, walichokifanya ni kusogea mpaka pale kulipokuwa na chungu kile kilichokuwa kimevunjika na kuanza kuangalia kwa ndani, hakukuwa na kitu chochote zaidi ya manyoya ya kuku tu.

    Kila mmoja akashangaa, japokuwa walijua kwamba kulikuwa na wakati wachawi walikuwa wakishindwa kufanya jambo fulani, lakini kwao hawakuwahi kushindwa hata mara moja, hiyo ilikuwa ni mara ya kwanza.

    Mzee Hamisi alikosa la kuongea, kila wakati alikuwa ameuachamisha mdomo wake, hakuonekana kuamini juu ya kile kilichokuwa kimetokea. Kijana yule, Ramadhani alionekana kuwa na nguvu mno na hakuwa mtu wa kumchezea hata mara moja, alikuwa mwenye uwezo mkubwa kichawi hivyo hata kama kufuatwa, alitakiwa kufuatwa kimakini zaidi.

    “Haiwezekani! Haiwezekani!” nilimsikia mzee Hamisi akisema kwa sauti kubwa.

    “Huyu mtu ana kinga kubwa sana,” alisema kiongozi wao.

    “Tufanye nini? Tuongeze nguvu kumfuata?” aliuliza mchawi mwingine.

    “Hatuwezi kwenda kwa kukurupuka, ni lazima tujipange, vinginevyo tutaumbuka,” alisema kiongozi yule.

    Hapohapo wakapangwa watu waliotakiwa kwenda kwa Ramadhani kwa ajili ya kuhakikisha kwamba kijana yule anamalizwa haraka iwezekanavyo kwani waliamini kwamba hakukuwa na mtu aliyekuwa na uchawi mkubwa zaidi yao.

    Wachawi wengine waliochaguliwa kwa ajili ya kwenda huko, walionekana kuwa na wasiwasi mno, hawakupenda kwenda kwa kuwa walijua kwamba kazi huwa ngumu sana na hivyo wanaweza kushindwa na hata mwisho wa siku kukamatwa.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Nitawapeni maelekezo juu ya nini cha kufanya,” alisema kiongozi yule na kuanza kuwapa maelekezo.

    Hakuchukua muda mrefu kuwaelekeza nini cha kufanya, baada ya kumaliza, akawapa unga fulani na kuwataka kujipaka nyusoni mwao kisha kupotea, ghafla nikawaona wakiwa juu ya nyungo zao huku kiongozi wao akiwa mbele kabisa akiwaelekeza nini cha kufanya.

    Nilikuwa nikiyaona yote, mzee Hamisi alikuwa ametulia kwenye ungo wake uliojaa tunguli nyingi, mkoni alikuwa ameshika usinga mmoja mkubwa na alikuwa akiupepea kila ungo wake ulipokwenda kwa umbali fulani.

    Hawakuchukua muda mrefu wakawa wamefika katika nyumba waliyotaka kuingia. Ilikuwa ni usiku sana, katika mtaa huo waliokuwepo, kulikuwa na watu wengine, hasa vijana ambao walikuwa wakinywa pombe na hata kucheza drafti lakini hakukuwa na yeyote aliyewaona mahali hapo.

    “Nani anaanza kuingia?” aliuliza mchawi mmoja.

    Kiongozi wao ndiye aliyekuwa akiamua ni nani wa kuingia na nani wa kubaki nje, alichokifanya ni kuwachagua wachawi wawili, walikuwa mabinti wadogo, kwa kuwaangalia kwa harakaharaka ungeweza kugundua kwamba walikuwa wakijifunza mambo ya kishirikina.

    “Kwa nini waende wao?” aliuliza mwanamke mmoja, nahisi alikuwa mzazi wa watoto hao.

    “Ni lazima wajifunze mengi, bila hivyo, hawatokua,” alijibu kiongozi.

    Ngoja nikwambie kitu kimoja, kwenye suala zima la kuingia ndani ya nyumba ya mtu aliyeshindikana kichawi huwa linaogopwa sana, hakuna mtu anayependa kuingia humo kwani wengi wanaoingia hunaswa na mwisho wa siku kukutwa mpaka asubuhi wakiwa hapohapo wamenasa na mbaya zaidi, wakati mwingine hufariki dunia.

    Kila mmoja aliogopa hivyo kuwasakizia wale mabinti ili waingie ndani. Mama yao alijua kwamba hiyo ilikuwa ni moja ya hatua kubwa na ngumu sana na ndiyo maana alilazimisha sana mabinti zake wasiingie ndani.

    “Lakini ndiyo wanajifunza,” alisema mama yao.

    “Hata kama! Ndiyo wajifunze jinsi ya kuroga watu kama hawa,” alisema kiongozi

    Mwanamke yule hakuwa na jinsi, japokuwa alikuwa na mapenzi makubwa kwa mabinti zake lakini akakubaliana na kiongozi wake kwamba awaache mabinti zake waingie ndani kwa ajili ya kumroga Ramadhani.

    Kilichofanyika ni kuupuruzia dawa mlango wa nyumba ile na pembe zote kisha mabinti wale wakaambiwa waingie ndani. Ghafla wakapotea na kuwaona wakiwa kwenye pembe moja ya nyumba ile na kuanza kuingia ndani.

    Nilibaki kimya, nilikuwa nikifuatilia kila ktu tena kwa ukaribu, nilitaka kuona ni kitu gani kingetokea mahali hapo. Pale nje walipobaki, wale wachawi walikuwa wakiendelea kufanya mambo yao, walikuwa wakicheza utupu huku wakiendelea kupulizia unga fulani katika nyumba ile.

    Huku kila mmoja akiwa bize, ghafla ukasikika uyowe mmoja mkubwa kutoka ndani. Kila mmoja akashtuka! Hawakujua nini kilitokea ndani.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog