Search This Blog

NILIJIUNGA NA DINI YA SHETANI - 1

 





    IMEANDIKWA NA : AZIZ HASHIM



    *********************************************************************************



    Simulizi : Nilijiunga Na Dini Ya Shetani

    Sehemu Ya Kwanza (1)

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Jina langu naitwa Mkanwa Sebastian au Saba kama wengi walivyozoea kuniita, mkazi wa Itete, Tukuyu wilayani Rungwe, Mbeya. Baba yangu mzazi, Sebastian Mwambenja alikuwa ni mchungaji wa Kanisa la Wokovu lililokuwa kwenye kijiji nilichozaliwa huku mama yangu akiwa ni muuguzi katika Zahanati ya Lufingo iliyokuwa kijiji cha pili kutoka pale tulipokuwa tunaishi.



    Mimi nilikuwa ni mtoto wa mwisho kuzaliwa katika familia yetu iliyokuwa na watoto saba. Baba yangu alikuwa akitokea kwenye ukoo wa kichifu wa Mzee Mwambenja ingawa baada ya babu yetu kufariki, aliamua kuokoka na ndipo alipoupata uchungaji wa kanisa hilo.



    Tangu nikiwa mdogo, wazazi wangu walinilea katika misingi ya kumuabudu na kumtukuza Mungu huku mara kwa mara wakinieleza kuwa Yesu alikufa msalabani kwa ajili ya dhambi zangu. Kila Jumapili nilikuwa nikiongozana na wazazi wangu kuelekea kanisani na baba alikuwa akitaka nikae mbele kabisa, jirani na madhabahu ambayo alikuwa akiyatumia kutangazia Injili na kuhubiri Neno la Mungu.



    Mara kwa mara alikuwa akiniambia kuwa imani ndiyokitu pekee kinachoweza kumkomboa mwanadamu kutoka kwenye kifungo cha mateso ya dunia.

    Watu wengi walikuwa wakimheshimu sana baba, kila alipokuwa anapita alikuwa akiitwa baba mchungaji, mama yeye akawa anaitwa mama mchungaji huku mimi nikiitwa mtoto wa mchungaji.



    Nakumbuka wakati baba anaanza kushika cheo cha mchungaji, nilikuwa na umri wa kati ya miaka sita au saba. Katika siku za mwanzo, hakuwa na uwezo wowote wa kufanya miujiza na kanisa lake halikuwa na waumini wengi zaidi ya ndugu zetu wa karibu na majirani ambao walikuwa wakijumuika nasi kila muda wa ibada ulipofika.



    Mimi kazi yangu ilikuwa ni kumbebea baba Biblia, sadaka na vifaa vingine vilivyokuwa vinatumika kwenye sala na wakati mwingine nilikuwa nikibeba zawadi ndogondogo alizokuwa anapewa na waumini wake.



    Kwa kadiri siku zilivyokuwa zinazidi kusonga mbele na mimi kuwa mkubwa, baba alianza kubadilika kwa vitu vingi, nilianza kumshuhudia akiwa na uwezo wa kufanya miujiza na mambo ambayo katika hali ya kawaida ni vigumu kuyaelezea. Kila Jumapili, alikuwa akifanya miujiza ya kuwaponya watu wenye matatizo mbalimbali yakiwemo magonjwa sugu, kuwaombea watu wenye shida mbalimbali na kutoa huduma ya kiroho.



    Kila nilipokuwa nikimuuliza anapata wapi nguvu za kufanya miujiza kama ile ambayo awali nilizoea kuiangalia kwenye mkanda wa video wa Yesu, aliniambia kuwa alikuwa amefikia hatua ya ukomavu wa kiimani na ndiyo maana alikuwa na uwezo wa kufanya chochote na kikatokea kweli kama alivyotaka.



    “Sasa baba, kama una uwezo wa kufanya chochote, kwa nini usiombee familia yetu tukawa matajiri na kumiliki mashamba makubwa ya migomba na magari ya kusafirishia mizigo kama baba yake Angenile?” nilimuuliza siku moja, akanitazama usoni kisha akanijibu kuwa umri wangu ulikuwa mdogo kuuliza maswali kama yale, akaniambia nikikua nitayaona mwenyewe.



    Sikuridhika na majibu yake, nikaona njia pekee inayoweza kuniridhisha nafsi yangu ni kuutafuta ukweli mimi mwenyewe. Siku ziliendelea kusonga mbele, kanisa la baba likawa linazidi kuwa maarufu pale kijijini, vijiji vya jirani na wilaya nzima ya Rungwe.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ilifika mahali watukutoka Tukuyu Mjini, Ushirika, Katumba, Kiwira na sehemu nyingine wakawa wanakuja kijijini kwetu na kujaa kwenyekanisa la baba. Kwa kuwa awali kanisa lilikuwa dogo na lisilo na ubora wowote, baada ya waumini kuanza kuongezeka, nilimsikia baba akijadiliana na watu fulani kwenye simu, akawaomba wamjengee kanisa kubwa na la kisasa.



    Baadaye baba aliniambia kuwa wale ni Wamisionari waliokuwa wanaishi Ulaya ambao alifahamiana nao katikakazi yake ya kutangaza injili.



    Siku iliyofuatia, tukamtafuta mpiga picha ambaye alilipiga picha lile kanisa la zamani na maeneo ya kuzunguka eneo hilo, tukasafairi na baba hadi Tukuyu mjini ambapo nilimsaidia kuzituma zile picha kwa njia ya mtandao kwenda kwa Wamisionari hao wa nchini Denmark.



    Wiki kadhaa baadaye, wale wamisionari walimpigia simu baba na kumweleza kuwa fedha zilikuwa tayari, tukaenda tena mjini kufungua akaunti benki kisha tukasubiri baada ya siku tatu, fedha nyingi zikaingia kwenyeakaunti hiyo.

    Baada ya hapo, baba alisaidiana na wazee wa kanisa pamoja na wauminji wengine kupanga namna kanisa jipya litakavyokuwa.



    Baada ya mipango kukamilika, kanisa zuri la kisasa lilijengwa pembeni kidogo ya lile la zamani. Watu wengi wakavutiwa nalo, hali iliyosababisha waumini wazidi kuongezeka.



    Kila baada ya misa kumalizika, kama kawaida yangu ya siku zote, nilikuwa nikibeba boksi lenye sadaka na kulipeleka nyumbani. Safari hii sadaka ziliongezeka kuliko kawaida, kila Jumapili watu wakawa wanamtolea Mungu wao kwa sana, noti za shilingi elfu kumikumi zikawa zinatolewa kwa wingi, tofauti na zamani ambapo waumini wa kiwango cha juu walikuwa wakitoa shilingi mia tano au elfu moja.



    Maisha yetu nayo yalizidi kubadilika kila siku, tukaachana na kula mbalaga (ndizi zinazopikwa na kupondwa), sasa tukawa tunakula vyakula vizuri huku tukibadilisha milo kila siku.

    Mama naye alianza kuvaa vitenge vya wax na kupaka mafuta yanayonukia vizuri.



    Miezi sita baada ya ujenzi wa kanisa jipya, niliwasikia baba na mama wakijadiliana kwenda kununua nyumba Tukuyu mjini nakuhama kule kijijini. Nikawasikia wakisema kuwa kule tutakuwa tunaenda kila Jumapili kwa ajili ya ibada tu kisha baada ya hapo tutarudi mjini.



    Nilifurahi sana kwani hata mimi sikuwa nikiyapenda maisha ya kijijini, baba akatuita wanaye wote na kutueleza juu ya mpango ule wa kuhama Itete na kwenda kuishi Tukuyu.



    “Baba kwani tayari umeshajenga nyumba nyingine?”

    “Hapana hatujengi bali tutanunua nyumba ambayo tayari imeshajengwa. Kuna madalali wanaendelea na kazi hiyo.”

    “Itakuwa nzuri kama kanisa lako?”

    “Ndiyo, tena nataka iwe nzuri zaidi,” tulikuwa tukizungumza na baba. Kila mmoja alikuwa na furaha.



    Siku kadhaa baadaye, kweli nyumba ilipatikana katika Mtaa wa Msasani, Tukuyu, jirani na chuo cha ualimu. Ilikuwa ni nyumba nzuri yenye kila kitu, taratibu za kuhamia makazi mapya zikaanza mara moja. Wakati zoezi la kuhamisha vitu likiendelea, niliona kitu kilichonishtua mno.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wakati nikikusanya vitu chumbani kwa baba na kuvipeleka kwenye gari lililokuwa nje, niliona vitu kama ndumba, hirizi, shanga, mapembe, fuvu la mtu, mifupa na vifaa vingine vya kishirikina vikiwa chini ya kitanda ya baba. Nilishtuka sana kwani sikuwahi kudhani kama baba anashiriki katika imani za kichawi.

    Nikiwa bado nimeduwaa, nilimsikia baba akifungua mlango, akanibamba nikiwa nimeinama mahali palipokuwa na vitu vile.



    “Unafanya nini?” aliniuliza kwa ukali. Nilishindwa cha kumjibu, nikabaki nimeduwaa.

    “Nakuuliza unafanya nini? Wewe si nimekwambia kasaidiane na wenzako kuhamisha vitu kwenye chumba chenu?”



    “Samahani baba,” nilisema huku nikiwa natetemeka, akanipokonya vile vitu nilivyovishika na kunitishia kuwa nikimwambia mtu yeyote kuhusu kile nilichokiona, atanifunza adabu. Harakaharaka nikatoka na kwenda kuungana na wenzangu na kuendelea kuhamisha vitu na kuvipakiza kwenye gari, tayari kwa safari ya kuhamia Tukuyu mjini.



    Nikiwa naendelea nakazi ya kuhamisha vitu na wenzangu, bado tukio la kile nilichokiona chini ya kitanda cha baba kilikuwa kikiendelea kunisumbua.

    Nilijiuliza maswali mengi ambayo yote yalikosa majibu.



    Kwa kifupi nilikosa raha kabisa, nikawa najiuliza kama baba anafanya miujiza kanisani kwa kutumia nguvu za Mungu au giza kama nilivyokuwa nikisikia kwa watu kuwa kuna watumishi wa Mungu wana kamchezo hako.



    “Mbona unaonekana una mawazo mwanangu, hujafurahia kuhama huku kijijini na kwenda mjini?” aliniuliza mama wakati tukiendelea na kazi ile, sikumjibu kitu zaidi ya kujichekelesha na kumuonesha kuwa sikuwa na chochote kichwani mwangu.



    Kazi iliendelea mpaka jioni, hatimaye tukamaliza na kuanza kuondoka. Baba na mama walipanda mbele ya lile gari, mimi na ndugu zangu wengine tukapanda nyuma na kushikilia vyombo, safari kutoka Itete kwenda Tukuyu Mjini ikaanza.



    Tukasafiri kwenye barabara ya vumbi kwa karibu kilometa kumi,tukafika njia panda ambapo dereva alikata kona na kuingia kwenye barabara ya lami ya Mbeya- Tukuyu. Bado niliendelea kufikiria mambo mengi ndani ya kichwa changu kuhusu kile nilichokiona.



    Kule mbele baba na mama walipokuwa wamekaa, kulikuwa na kifurushi kidogo kilichokuwa kimefungwa kwa ustadi mkubwa, nikatambua kuwa lazima vile vitu vya baba vilikuwa ndani ya kifurushi kile, nikajiapiza kuwa tukifika na kuanza kushusha vyombo, nitamfuatilia baba kwa makini ili nijue ataenda kuviweka wapi.



    Safari iliendelea, cha ajabu tulipofika sehemu inayoitwa Katumba, njia panda ya kuelekea Mwakaleli, baba aliteremka kwenye gari akiwa na kile kifurushi, akatuambia sisi tutangulie nay eye atafuata baada ya muda si mrefu. Kwa kuwamama alikuwa akipafahamu tunapohamia, tulikuwa na uhakika wa kufika salama.



    Nikamtazama baba ambaye tayari alikuwa ameteremsha kile kifurushi chini, macho yake na yangu yakagongana, nikamuona akinipa ishara kama ya kunitisha kuwa endapo nitasema nilichokiona, atanifanya kitu kibaya.



    Dereva akawasha gari na safari ikaendelea. Niliendelea kumsindikiza baba kwa macho, nikamuona akizamia kwenye migomba mingi iliyokuwa kando ya barabara, hakuna aliyeelewa anakwenda wapi. Baada ya dakika kadhaa, tuliwasili Tukuyu, mama akamuelekeza dereva njia ya makazi mapya.



    Tulienda mpaka kwenye jumba kubwa la kifahari lililokuwa limeezekwa kwa vigae vyekundu. Mama akatuambia kua pale ndiyo tutakapokuwa tukiishi, sote tukapigwa na butwaa kutokana na uzuri wa nyumba ile.



    Tulianza kuteremsha vyombo kwenye gari kwa kusaidiana na vijana tuliowakuta pale nje ya nyumba ile ya kifahari. Wakati tukiendelea na kazi ile, nilikuwa makini kumuangalia baba kama atatokea lakini haikuwa hivyo. Kikubwa nilichokuwa nataka kukiona, ni mahali anapoenda kuhifadhi ule mzigo wake aliokuwa ameushika

    mkononi.



    Tuliendelea na kazi mpaka tukamaliza kushusha vyombo vyote, mama akamlipa dereva na utingo wake gharama walizokubaliana, wakawasha gari na kuondoka. Wale vijana waliotusaidia kushusha vyombo pia walipewa kifuta jasho, wakaondoka na

    kutuacha mimi, ndugu zangu na mama tukiendelea kupanga vitu.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kikubwa nilichokibaini ni kuwa vyombo vyetu tulivyotoka navyo kule kijijini havikuwa na hadhi ya kuwekwa kwenye nyumba ile ya kisasa. Viti vichakavu, vitanda na samani nyingine kuukuu tulizokuwa nazo, zilionekana kuwa za hadhi ya chini sana

    ukilinganisha na thamani ya ile nyumba ambayo sakafu yote ilikuwa imewekwa marumaru za kisasa.



    Tuliendelea kuishangaa ile nyumba na mazingira yake ya nje, kila mmoja alikuwa na furaha kubwa ya kuhamia mjini, tena kwenye jumba la kifahari kama lile. Wakati ndugu zangu wakiendelea kufurahia, mimi bado nilikuwa najiuliza maswali ambayo sikupata majibu kirahisi.

    Niliendelea kushangaa iweje baba awe anajihusisha na mambo yakishirikina wakati yeye ni mchungaji anayeaminiwa na waumini wengi, tena akiwa na uwezo wa kufanya miujiza kama kuponya wagonjwa, kukemea mapepo na mambo mengine mengi ambayo katika hali ya kawaida ni ngumu kufanywanamtu asiye na upako.



    “Ina maana baba anamuabudu shetani? Lakini mbona anakemea mapepo kwa kutumia jina la Mungu? Mbona sielewi kinachoendelea?” nilijiuliza lakini hakukuwa na wa kujibu maswali yangu.



    “Mbona mwenzetu unaonekana kuwa mbali kimawazo? Au hujafurahia kuhamia kwenye jumba la kifahari kama hili?” mama aliniuliza, safari hii akiwa amenikazia macho. Nilijaribu kumdanganya kwa kujichekesha lakini alinibana na kuniambia kuwa

    amegundua tofauti tangu wakati tukihamisha vyombo, akanitaka nimweleze ukweli.



    “Mimi ndiyo mama’ako, kama utashindwa kuniambia ukweli unafikiri utamwambia nani? Niambie mwanangu.”



    “Mama kuna kitu nimekiona wakati tunahamisha vitu kule nyumbani kimenikosesha raha kabisa.”

    “Kitu gani mwanangu? Naona kweli umekosa raha.”

    “Nimeona vitu kama vifaa vya kichawi vikiwa chini ya kitanda chenu na baba, nikiwa naviangalia baba akanikuta na kunitishia, akaniambia kuwa nisimwambie mtu yeyote.”

    “Hicho ndicho kilichokuchanganya?”



    “Ndiyo mama, kwani baba si mtumishi wa Mungu, kwa nini anakaa na vitu vya kichawi ndani? Waumini wake wakijua itakuwaje?”



    “Mwanangu haya mambo we yaache kama yalivyo, mimi mwenyewe nimekorofishana sana na baba yako kuhusu hilo suala lakini baadaye nikaamua kunyamaza, kama

    alivyokwambia, na mimi nakuomba uitunze siri hii kwani watu wengine wakijua itakuwa hatari sana.”



    Mama aliendelea kuniambia mambo mengi ambayo sikuwa nayajua hapo awali, akanisisitiza kuitunza siri ile huku akiahidi kuendelea kuzungumza na baba ili atambue makosa anayoyafanya. Tukiwa tunaendelea kuzungumza, tulisikia mtu akigonga mlango, mama akatoka kwenda kumfungulia. Alikuwa ni baba.



    Baada ya kuingia, baba alitupa pole kwa kazi ya kushusha mizigo na kupanga vitu vizuri mle ndani, akatuahidi kuwa kesho yake atatupa zawadi nzuri, pia akaahidi kuwa

    tutaenda kununua samani mpya kama masofa ya kisasa, makabati na vitu vingine vinavyoendana na hadhi ya ile nyumba tuliyokuwa tunaishi.



    Wakati akizungumza hayo, akili yangu nilikuwa nimeielekeza kwenye mkoba wa ngozi aliokuwa ameubeba baba. Mama alipotaka kumpokea, alikataa na kuendelea kuubeba vilevile, nikajua kuwa lazima vile vitu vya kichawi atakuwa ameviweka mle na ndiyo maana aliteremka kwenye gari tukiwa njiani kuhamia makazi mapya.



    Baada ya muda, aliondoka na kuelekea chumbani huku ule mkoba akiwa ameubeba vilevile. Kwa kuwa nilikuwa na shauku kubwa ya kutaka kuona mahali anapoenda kuuhifadhi mkoba ule, alipoinuka kuelekea chumbani, na mimi nilisimama na

    kujifanya nataka kwenda chooni.



    Harakaharaka nilitoka nje na kuzunguka upande kulipokuwa na dirisha la chumba chao. Kwa kuwa bado tulikuwa hatujaweka mapazia, niliweza kuona ndani bila shida, nikatulia na kuanza kuangalia kilichokuwa kinaendelea ndani.



    Nilimuona baba akiwa amepiga magoti na kuweka mikono kama mtu anayesali, huku ule mkoba wake akiwa ameuweka mbele yake, akakaa katika hali ile kwa zaidi ya dakika kumi, kisha nikamuona akiinuka na kufungua begi kubwa la nguo, akatoa joho lake la kichungaji na kulivaa juu ya nguo alizokuwa amezivaa.



    Kwa uangalifu mkubwa akaanza kufungua ule mkoba, akatoa vitu vyote vilimokuwemo, kibuyu kikubwa kilichokuwa kimefungwa shanga nyeupe, nyeusi na nyekundu upande wa juu, fuvu la kichwa, pembe kubwa la mnyama ambaye sikumtambua, dawa kibao za mitishamba na vikorokoro vingine vya kutisha.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Akavipanga sakafuni, akakaa akiwa amevaa lile joho lake na kuanza kuzungumza na kile kibuyu kwa lugha ambayo sikuielewa. Mara kile kibuyu kikaanza kutoa moshi mweupe, nikajikuta nikipiga kelele huku nikitetemeka mwili mzima.



    Baba alishtuka sana kusikia sauti ya mtu pale dirishani, akaacha kila alichokuwa

    anakifanya na kusimama kwa jazba, akageukia pale dirishani nilipokuwa nimejificha.



    Kwa kasi ya ajabu niliinama chini na kutimua mbio kukwepa baba asije akaniona, nikafanikiwa kuingia ndani bila mtu yeyote kugundua kuwa nilikuwa nimetoka nje, nikapitiliza moja kwa moja chooni na kujifungia.



    Nikawa nahema kama mwanariadha wa Marathoni. Kwa mbali nikamsikia baba akifungua mlango wa chumbani kwake na kutoka kwa hasira hadi sebuleni.

    “Saba yuko wapi?” aliuliza kwa jazba, nikamsikia mama akimjibu kuwa nimeenda chooni. Hakutaka kuamini, akaja mpaka chooni ambapo alijaribu kuusukuma mlango kwa nguvu ili ahakikishe kama kweli nilikuwa chooni.



    “Kuna mtu,” nilijibu huku nikijifanya sihafamu chochote kinachoendelea.



    “Ni wewe Saba!”

    “Ndiyo baba, tumbo la kuendesha linanisumbua,” nilimjibu bila kufungua

    mlango, nikamsikia akitembea harakaharaka kuelekea nje. Alifungua mlango na kuubamiza, akazunguka nyuma ya nyumba yetu huku akionekana kuwa na hasira kupita kiasi.



    Nilimshukuru Mungu kwa akili niliyoitumia kwani kama angenikuta kule nje, sijui hata angenifanya nini.

    “Kwani kuna nini mume wangu,” mama aliuliza mama huku naye akionekana kushtushwa na hali aliyokuwa nayo baba.”



    “Kuna vibaka wanachungulia madirishani, hawa vijana wa hapa Tukuyu

    wahuni sana,” alisema huku akimulika huku na kule kwa kutumia tochi kubwa. Licha ya kuzunguka karibu nyumba nzima, baba hakumuona mtu yeyote, akarudi ndani huku akiwa amefura kwa hasira.



    Kwa muda huo na mimi nilikuwa tayari nimeshatoka chooni, nikaenda kukaa

    sebuleni na ndugu zangu. Baba alirudi ndani huku mama akiwa anamfuata nyuma, akapitiliza hadi chumbani kwake na kujifungia tena mlango, sisi tukabaki na mama ambaye aliendelea kutusimulia hadithi na mambo mbalimbali ya kufurahisha.



    Ilipofika saa tano za usiku, mama alituaga na kutuambia kila mmoja aende kulala, na yeye akainuka na kuelekea kwenye kile chumba alichokuwemo baba. Tulienda kulala lakini kichwa changu bado kiliendelea kutawaliwa na mawazo mengi, nikawa najiuliza maswali ambayo sikuyapatia majibu. Baadaye usingizi ulinipitia.



    Kulipopambazuka, nilikuwa wa kwanza kuamka. Muda mfupi baadaye mama naye aliamka, tukawa tunasaidiana kufanya usafi wa nyumba na mazingira ya nje. Wakati tukiendelea kufanya usafi, mama aliniita na kuniuliza jambo.



    “Wewe ndiyo ulikuwa unamchungulia baba yako jana?”

    “Hapana mama, siyo mimi!”

    “Acha uongo we mtoto, hizi nyayo za miguu mbona zinafanana na za kwako? Unataka nikamwambie baba yako?”



    “Basi mama usimwambie baba, ni kweli mimi ndiyo nilikuwa namchungulia,” nilimwambia mama kwa sauti ya chini huku nikimsihi asimwambie baba. Kutokana na jinsi mama alivyokuwa ananipenda, alikubali kunifichia siri ile, tukasaidiana kufuta

    nyayo za miguu yangu ambazo zilikuwa zimejichora ardhini kwenye matope, ikabaki kuwa siri yetu.



    “Mama kusema ukweli nimeanza kumuogopa sana baba, mambo niliyoyaona jana yalinitisha sana, sitaki kuamini kama kweli baba anashiriki kwenye ushirikina wakati ni mchungaji.”



    “Kwani uliona nini mwanangu?” mama aliniuliza huku akiacha kila alichokuwa anakifanya, akanisogelea na kuanza kunipapasa mgongoni kwa upendo. Nilimwambia kila nilichokiona, akaniambia nisiwe na wasiwasi kwani ushirikina wa baba haukuwa kwa ajili ya kutudhuru sisi bali kwa ajili ya kazi yake.



    Aliendelea kunibembeleza na kunisihi nisimwambie mtu yeyote juu ya kile nilichokiona, akaniuliza kama sikuwa nayafurahia mabadiliko ya kimaisha tuliyokuwa tunapitia, kutoka ufukara uliopindukia hadi utajiri tulioanza kuupata. Nilimjibu kuwa nafurahia lakini naogopa hatua watakayochukua waumini wake siku wakiujua ukweli

    kuwa baba huwa anatumia nguvu za giza.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mama alinihakikishia kuwa kamwe hawataweza kugundua chochote, tukaendelea kufanya usafi. Tulipomaliza, mama aliandaa chai kisha tukawaamsha baba na ndugu zangu wengine, tukajumuika pamoja kupata kifungua kinywa. Wakati tukiendelea

    kupata kifungua kinywa, baba alikuwa akinitazama kwa jicho kali kama anayesema ‘ole wako umwambie mtu juu ya ulichokiona’.



    Kila macho yetu yalipokuwa yakikutana, nilikuwa nikiyakwepesha ya kwangu na kutazama chini, tukaendelea kupata kifungua kinywa mpaka tulipotosheka. Baada ya muda, nilimuaga mama kuwa nakwenda stendi kutafuta magazeti kwani nilikuwa napenda sana kusoma Gazeti la The Bongo Sun.



    Aliniruhusu na kunipa shilingi elfu moja, akaniambia niwe makini barabarani. Nilitoka na kuanza kuelekea kwenye stendi ya mabasi ya Tukuyu. Nilipandisha kilima kidogo kutoka kule tulikokuwa tunaishi kwani Mji wa Tukuyu umejawa na milima na mabonde, muda mfupi baadaye nikafika stendi na kwenda kwenye meza ya kuuzia magazeti .



    Nikanunua Gazeti la The Bongo Sun lakini pale juu ya meza ya magazeti, niliona kitu kingine ambacho kilinivutia sana. Kilikuwa ni kitabu kilichokuwa na picha ya fuvu na maandishi makubwa yaliyoandikwa Uchawi; Unavyofanya kazi na jinsi ya kujikinga kilichoandikwa na mwandishi mahiri na mtaaalamu wa elimu ya utambuzi, Munga Tehenan.

    Nikajikuta navutiwa nacho sana, nikauliza bei. Aliponitajia, niliondoka haraka na

    kurudi nyumbani kwa lengo la kwenda kumuomba mama fedha ili nikakinunue.



    Niliporudi nyumbani, sikumkuta mama, ikabidi nikae kumsubiri. Baada ya takribani saa mbili kupita, mama alirudi ambapo kitu cha kwanza nilichokifanya ilikuwa ni kumueleza shida yangu.

    “Ukanunue kitabu? Kitabu gani?”

    “Ni kitabu cha masomo shuleni, naamini nikikipata kitanisaidia sana.”

    “Yaani nitoe shilingi elfu saba kwa ajili ya kitabu? Mimi sina fedha, kamuombe baba yako,” alijibu mama huku akionekana kutokuwa na imani na mimi.



    Alihisi huenda nataka kumtapeli fedha zake. Aliponiambia nikamuombe baba, nilikataa katakata, nikaendelea kumbembeleza mpaka akakubali. Akatoa noti ya shilingi elfu kumi na kuniambia nimrudishie chenji yake.



    Harakaharaka nilitoka na kurudi stendi, mahali nilipokiona kile kitabu, nikampa yule muuza magazeti fedha yake, akanipa chenji na kile kitabu. Nikakificha kwenye shati nililokuwa nimevaa na kurudi nyumbani haraka, sikutaka mtu yeyote akione. Nilienda kumpa mama chenji yake kisha nikaingia chumbani na kujifungia.



    “Hicho kitabu chenyewe kipo wapi?” nilimsikia mama akiniuliza lakini nilijifanya kama simsikii. Sikutaka ajue ni kitabu gani nilichokuwa nimekinunua. Nilianza kukitazama vizuri kile kitabu kuanzia ukurasa wa kwanza hadi wa mwisho. Ama kwa hakika kilikuwa na mada zilizonivutia sana.



    Bila kupoteza muda nikaanza kusoma mada motomoto zilizokuwa ndani ya kitabu kile, kuanzia ile ya kwanza iliyokuwa inauliza wewe ni nini? Nilisoma kwa makini lakini cha ajabu, kila nilichokuwa nakisoma kilikuwa ni kama kinanichanganya kwani sikuwahi kukisikia sehemu yoyote wala kukiwaza.



    Naikumbuka vizuri mada ya kwanza kuhusu utu na thamani ya binadamu ambapo mwandishi alifafanua kwa kina tafsiri ya mtu, akili na roho. Nikajikuta narudiarudia mada moja zaidi ya mara tatu ili niweze kuelewa.



    “Wewe ni nini? Ni mwili wako, akili zako, uzuri wako, mali au elimu yako? Kwa nini mtu akifa tunasema tunaenda kuuzika mwili wa fulani, huyo anayeumiliki mwili ni nani?” hayo yalikuwa baadhi ya maswali magumu ambayo ama kwa hakika yalinifanya nijikune kichwa. Uelewa wangu ukaanza kufunguka.



    Niliendelea kusoma juu ya umuhimu wa kila mtu kujitambua na kufahamu thamani yake na malengo yaliyomleta duniani. Nikasoma kuhusu nguvu zinazozalishwa na watu bila ya wao wenyewe kujua kuanzia kwenye kauli, mawazo na matendo.



    Mwandishi akafafanua kwa kina namna watu wanavyoshindwa kuzitumia nguvu walizojaaliwa ndani ya akili zao na kujikuta wakiishia kuishi maisha ya kifukara mpaka wanakufa. Akaeleza kwa nini watu wengine wanaishi maisha ya kifukara, mlo wa siku moja ukiwa ni tatizo kubwa kwao ilhali kuna wanaoishi kifahari, wakila, kunywa na kusaza.



    “Wewe ndiyo uliyechagua aina ya maisha unayotaka kuishi, ukiamua kuwa tajiri, bila shaka utakuwa tajiri kwa sababu akili na mawazo yako vinazalisha nguvu kubwa ambayo inaweza kuyafanya yale uliyokuwa unayafikiria yatokee katika maisha halisi,” ilisomeka sehemu ya kitabu kile.



    Niliendelea kushangaa kwani kila neno nililokuwa nalisoma kwenye kitabu kile, lilikuwa likiniamsha ari ndani ya nafsi yangu kutaka kufahamu kwa undani kilichokuwa kinazungumziwa. Mwandishi aliendelea kutoa mifano jinsi binadamu alivyojaliwa uwezo mkubwa wa kufikiri na kufanya kila analofikiri litokee.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Alitolea mfano watu wenye uwezo wa kupindisha vitu kama kijiko au chuma chochote kwa kukitazama tu, akazungumzia pia watu wenye uwezo wa kupasua glasi kwa kuitazama au kuhamisha kitu kimoja kwenda sehemu nyingine. Nilijiuliza kile kilichokuwa kinazungumziwa ni uchawi au nguvu za mawazo? Mwandishi alinijibu katika ufafanuzi kuwa hakuna uchawi katika suala lile na kila mmoja anaweza kufanya akifundishwa.



    Nilipoendelea kusoma, kuna sehemu mwandishi alitoa mfano kwa kila msomaji kujaribu kujipima kama ana nguvu za mawazo kiasi gani. Na mimi nikajaribu.

    Nilikaa sakafuni na kutulia, nikawa navuta pumzi ndefu na kuzitoa taratibu kupitia mdomo huku nikiwa nimeweka uzingativu wa kutosha akilini mwangu. Nikiwa katika hali ile, nilishangaa nikijihisi kitu tofauti kabisa kwenye mwili wangu. Nikawa ni kama nimehama kwenye ulimwengu wa kawaida na kwenda mahali nisipopajua.



    Nilishtuka kwa nguvu hadi nikaanguka sakafuni, nikawa nafikicha macho ili kuhakikisha kama sikuwa kwenye ndoto. Nilikaa vizuri kisha nikaendelea kukisoma kile kitabu, safari hii nikiwa naelewa na kuamini kila nilichokuwa nakisoma kwani nilihakikisha mwenyewe kuwa kile kilichokuwa kinaelezewa hakikuwa porojo bali ukweli mtupu.



    Nikiwa naendelea kukisoma kile kitabu, kumbe baba alikuwa amezunguka nyuma ya nyumba na kuja mpaka kwenye dirisha la chumba changu, akawa ananiangalia nafanya nini kwani nilikuwa nimetulia kwa muda mrefu.

    “Unafanya nini? Aliniuliza kwa sauti ya ukali.”



    “Najisomea baba, mitihani imekaribia,” nilimjibu huku nikijitahidi kukificha kile kitabu ili asikione.

    “Hebu lete hicho kitabu,” aliniambia, nikawa nasita kama nimpe au la lakini kwa jinsi alivyokuwa ananitazama kwa ukali, ikabidi nifanye kama alivyoniambia. Nikampa kile kitabu huku nikitetemeka kuliko kawaida.



    “Haaa! Unasoma kitabu cha kichawi? Unataka kujiunga na jamii za siri na dini ya shetani siyo? Hujui kama mimi baba yako ni mtumishi wa Mungu? Kwa nini unataka kunitia aibu?” alisema baba huku akiendelea kufunua kurasa za kile kitabu. Sikumjibu kitu, nikawa naendelea kutetemeka kwa hofu.



    Akiwa na hasira za hali ya juu, nilimshuhudia akikichanachana kile kitabu, akatupatupa karatasi huku na kule huku akinitolea macho ya ukali. Kwa kuwa alikuwa upande wa nje, aliniambia nisitoke mle chumbani nimsubiri, nikajua anataka kuja kuniadhibu vikali, nikawa nafikiria namna ya kumkimbia.



    Nilipata akili ya kukimbia haraka kabla baba hajaingia ndani na kuja kuniadhibu, nikatoka na kuingia chumba kingine, nikajifungia mlango kwa ndani. Nilimsikia baba akiingia ndani na kusukuma mlango kwa nguvu, nikawa natetetema kwa hofu.

    “Yuko wapi?” nilimsikia baba akiuliza kwa jazba. Nilijibanza kwenye kabati la nguo la ukutani na kujifungia, nikawa namuomba Mungu asinione kwani kwa jinsi nilivyokuwa namfahamu, angeniadhibu vikali.

    “Kwani kuna nini tena?”

    “Huyu mwanao mshenzi sana, yaani anajifunza mambo ya dini ya shetani ndani ya nyumba yangu, leo atanikoma.”

    “Mambo ya dini ya shetani? Ndiyo mambo gani hayo,” mama aliuliza huku akiwa haelewi kinachoendelea. Nilimsikia baba akimfafanulia kuwa amenikuta nikiwa nasoma na kujifunza mambo ya kichawi kwenye kitabu.



    Mama alimuuliza yeye amejuaje kama nilichokuwa nakisoma kinahusu dini ya shetani? Nikawasikia wakianza kufokeana wenyewe kwa wenyewe. Nilishukuru sana mama kuingilia ugomvi ule kwani hiyo ndiyo ilikuwa ahueni yangu. Wakaendelea kujibizana, baba akatoka na kwenda kukusanya karatasi za kile kitabu changu alichokichanachana.

    Akarudi ndani na kumuonesha mama, akawa anaziangalia huku na yeye akishangaa. Baadaye nilisikia wakianza kuzungumza vizuri, nikajua wameshapatana, hasira za baba zikawa zimepungua, nikatoka mafichoni na kufungua mlango.

    “Njoo hapa,” nilimsikia baba akisema. Kumbe wakati nafungua mlango alikuwa ameshaniona, nikawa sina ujanja zaidi ya kujipeleka mwenyewe kwake. Mkononi alikuwa ameshika fimbo mbili ngumu, nikasogea huku nikiendelea kuomba kimoyomoyo.

    Tofauti na nilivyotegemea, baba hakunipiga bali aliutumia muda ule kuzungumza na mimi kwa busara. Akaniambia nimshukuru mama kwani bila yeye kuingilia kati na kuniombea msamaha, ningekiona cha mtema kuni. Aliendelea kuzungumza na mimi kwa kirefu, akaniambia sitakiwi kujifunza au kushiriki kwa namna yoyote mambo yanayohusu imani ya dini ya shetani.

    Kiukweli sikumuelewa anamaanisha nini kwani kile nilichokuwa nikikisoma kwenye kile kitabu alichokichana, hakikuwa na matatizo yoyote ukilinganisha na matendo yake aliyokuwa anayafanya gizani.

    Hata hivyo, sikutaka kubishana naye kwa chochote, nikawa namsikiliza mpaka alipomaliza kuongea. Alipomaliza aliniambia niondoke ili waendelee kuzungumza na mama.

    Kiukweli nilichukizwa sana na kitendo chake cha kunichania kitabu changu, nikajiwekea nadhiri kuwa lazima nitaenda kununua kingine. CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Siku iliyokuwa inafuatia ilikuwa ni Jumapili, baba akatuambia tuvae vizuri kwa sababu ataenda kututambulisha rasmi kwenye kanisa jipya mbele ya waumini wengi zaidi tofauti na kule kijijini Itete.

    Wenzangu walifurahia sana lakini kwangu mimi ilikuwa tofauti. Baada ya kugundua mambo aliyokuwa anayafanya baba, nilikosa imani naye kabisa, nikawa nachukizwa na tabia yake ya kuwadanganya watu, tena wengine wakiwa wamemzidi umri.

    Jumapili ilipofika, kama baba alivyokuwa ametuambia, wote tulivaa suti mpya tulizokuwa tumenunuliwa, mama akavaa gauni lake jipya na kujifunga kilemba kama wafanyavyo wanawake wa Kinigeria, tukaondoka mpaka kanisani.

    Baba alinipa Biblia yake nimshikie, akaniambia nisiende kukaa upande waliokuwa wamekaa waumini wengine pamoja na ndugu zangu, akaniambia nitakaa nyuma ya madhabahu. Sikuelewa kwa nini aliniambia vile lakini nilitii, nikawekewa kiti nyuma ya madhabahu na baba akaanza kuongoza ibada akitumia Biblia nyingine tofauti na ile.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog