Search This Blog

NILIJIUNGA NA DINI YA SHETANI - 2

 







    Simulizi : Nilijiunga Na Dini Ya Shetani

    Sehemu Ya Pili (2)

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Baba alinipa Biblia yake nimshikie, akaniambia nisiende kukaa upande waliokuwa wamekaa waumini wengine pamoja na ndugu zangu, akaniambia nitakaa nyuma ya madhabahu. Sikuelewa kwa nini aliniambia vile lakini nilitii, nikawekewa kiti nyuma ya madhabahu na baba akaanza kuongoza ibada akitumia Biblia nyingine tofauti na ile.

    Ulipofika muda wa kuwaombea wagonjwa na watu wenye shida mbalimbali, baba alishuka madhabahuni na kuja pale nilipokuwa nimekaa, akachukua ile Biblia niliyokuwa nimeishika, akarudi kwenye madhabahu na kuanza kufanya maombezi.

    Wagonjwa na wenye shida mbalimbali walijitokeza kwa wingi lakini miongoni mwao, kuna mmoja alinishangaza sana. Jina lake alikuwa anaitwa Sinai na wakati tukiishi kijijini Itete, alikuwa akija nyumbani mara mojamoja na kuzungumza na baba. Kilichonishangaza ni kwamba alikuwa akitembelea magongo huku miguu yake ikiwa kama mtu mwenye ulemavu.



    Nilishangaa sana Sinai amepata ulemavu lini na ilikuwaje kwani mara mwisho kumuona, hata miezi sita haikuwa imeisha. Nikanyamaza ili nijionee kitakachotokea. Baba aliteremka kwenye madhabahu na kusogea pale mbele wagonjwa walipokuwa wamesimama.



    Nikamuona akiwapita wale wengine na kwenda moja kwa moja kwa Sinai, akaanza kumhoji maswali huku akimuwekea kipaza sauti mdomoni, watu wote waliokuwa kanisani wakawa wanasikia alichokuwa anakisema.



    “Nilizaliwa nikiwa mlemavu, mama yangu alirogwa akiwa na mimba yangu, naomba uniombee nipone,” alisema Sinai, nikazidi kupigwa na butwaa kwani nilikuwa nikimfahamu vizuri na hakuwahi kuwa mlemavu.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Baba alimuwekea mikono kichwani, akaanza kumuombea huku akinena kwa lugha, nikaona Sinai ameanza kuongea hovyo kama mtu aliyepandwa na mapepo, kisha akaanguka chini. Baba akamshika miguu aliyodai ina ulemavu, akaendelea kuomba kwa nguvu.



    Muda mfupi baadaye Sinai alijifanya amezinduka, akamshikilia baba mwilini na kujaribu kusimama, eti akaanza kusema miguu yake iliyokuwa na ulemavu wa kuzaliwa nao imepata nguvu baada ya kuombewa, akatupa magongo na kuanza kurukaruka kwa furaha.



    Waumini wengine walishangilia sana wakiamini Mungu ametenda miujiza wakati haikuwa kweli. Nilimuona mama naye akishangilia japokuwa alikuwa akimfahamu vizuri Sinai kuwa hakuwa mlemavu na siyo kweli kwamba baba ndiyo amemponya. Watu wakatoa sadaka kwa wingi, nikapewa mimi nizishike.



    Kwa kuwa nilikuwa nahitaji fedha kwa ajili ya kwenda kununulia kitabu kingine baada ya kile cha awali kuchanwa na baba, nilichomoa noti moja ya shilingi elfu kumi kwenye kapu la sadaka lililokuwa limejaa na kuificha kwenye mfuko wa koti.

    Baada ya kumuombea Sinai, baba aliendelea kuwaombea wagonjwa wengine hasa wale waliokuwa na matatizo madogomadogo ambapo kila aliyeombewa, muda mfupi baadaye alitoa ushuhuda kuwa amepona na anajisikia vizuri. Kanisa liliendelea kulipuka kwa shangwe na vigelegele mpaka muda wa kumaliza misa ulipofika.



    Japokuwa kapu la sadaka nililopewa na baba kushika lilikuwa kubwa, lilijaa noti walizotoa waumini kama sadaka. Nafikiri muujiza feki wa Sinai ulisaidia sana kuwafanya waumini watoe sadaka kwa wingi.



    “Tangulia na huo mzigo kwenye taxi aliyokodi mama yako, ipo hapo nje inakusubiri, pitia mlango wa huku nyuma watu wasikuone,” baba aliniambia kwa sauti ya chini, akanionesha mlango wa kutokea ambapo niliinuka na lile kapu la sadaka, nikatoka nje ambapo nilimkuta mama akiwa na dereva taxi wananisubiri. Tukaondoka na kueleka nyumbani huku baba akiendelea kuagana na waumini wake.



    Baada ya muda, baba alirejea akiwa kwenye teksi nyingine, akiwa na dereva na mtu mwingine ambaye sikumtambua haraka kwani hakushuka garini. Baba aliingia ndani na moja kwa moja akapitiliza mpaka sebuleni tulipokuwa tumekaa na mama tukiangalia runinga.

    “Ule mzigo umeuweka wapi?” baba aliniuliza akimaanisha kapu la sadaka. Mama alimjibu kuwa lipo chumbani kwao, akaingia ndani kisha mama naye akamfuata. Niliutumia muda huo kutoka hadi nje, nikaenda kumuangalia yule mtu wa tatu aliyekuwa ameongozana na baba.

    “Haa! Kumbe ni Sinai,” nilishtuka baada ya kugundua kuwa kumbe baba alikuwa amekuja na yule mtu aliyejifanya alizaliwa na ulemavu ambao uliisha muda mfupi uliopita baada ya kuombewa na baba.

    Nilitamani kwenda kumuuliza ni kwa nini ametoa ushuhuda wa uongo ndani ya nyumba ya Mungu lakini nikaogopa anaweza kumwambia baba na kuanzisha matatizo mengine ambayo hayakuwa ya lazima.

    Nilijibanza nikitaka kuona baba alikuwa amefuata kitu gani ndani. Baada ya muda nikamuona akitoka akiwa amebeba bahasha ya kaki mkononi iliyokuwa imetuna, nikajua kuwa lazima zilikuwa ni fedha. Alitembea harakaharaka hadi kwenye gari, akafungua mlango wa nyuma na kumpa Sinai ile bahasha.

    Akamfuata dereva na kumpa maelekezo fulani kisha lile gari likaondoka pale nyumbani. Harakaharaka nilitoka pale nilipokuwa nimejificha na kurudi sebuleni, baba alipoingia ndani, alinikuta nikiwa nimekaa hivyo hakuhisi chochote.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Umefanya kazi nzuri sana leo kanisani, chochote ulichokiona kibakie kuwa siri yako, sawa mwanangu kipenzi,” baba aliniambia huku akiwa amekaa jirani kabisa na pale nilipokuwa nimekaa. Nilishangaa kwa jinsi alivyokuwa anazungumza na mimi kwa upole. Nikaitikia na kumwambia sitamwambia mtu yeyote. Nilimridhisha tu lakini kiukweli nilikuwa nachukizwa sana na matendo yake.

    Baada ya kula chakula cha mchana, nilitoka bila kumuaga mtu yeyote, nikaenda moja kwa moja mpaka stendi kununua kitabu kama kile ambacho baba alikichana. Nilipofika nilitoa noti ya shilingi elfu kumi niliyoiiba kwenye sadaka za baba, nikampa yule muuzaji ambapo alinipa kitabu kama kilekile.

    Ili kuzuia baba au mama wasigundue kilichokuwa kinaendelea, nilinunua kitabu kingine cha hadithi kiitwacho Usilie Tena Geneviv, nikachana kava lake na kumuomba yule muuzaji gundi, aliponipa nilibandika kava lile juu ya kitabu changu. Kwa harakaharaka kikawa kinaonekana kama kitabu cha hadithi nzuri za kusisimua kumbe haikuwa hivyo.

    Nilipohakikisha kipo sawa, nilirudi nyumbani na kwenda kukificha chumbani kwangu. Nilipohakikisha hakuna mtu aliyenishtukia, niliingia chumbani kwangu na kujifungia, nikaanza kusoma kuanzia pale nilipokuwa nimeishia kabla baba hajanifuma.

    Bado niliendelea kushangazwa na mada zilizokuwa ndani ya kitabu kile kwani kila nilichokuwa nakisoma kilikuwa kigeni kwangu lakini chenye manufaa makubwa.

    Kutokana na uzito wa mada zenyewe, nililazimika kutafuta ‘ki-notebook’ kingine kidogo, nikawa naandika mambo ya muhimu niliyokuwa najifunza. Niliendelea kusoma hadi nikafika kwenye kipengele cha tahajudi (meditation).



    Mwandishi alifafanua maana ya tahajudi na kueleza kuwa ni kitendo cha mtu kukaa katika hali ya utulivu na kutafuta usawaziko wa kimwili na kiakili. Akafafanua kuwa mtu anayetaka kufanya tahajudi, anatakiwa kukaa sehemu tulivu na kutulia huku mikono yake akiwa ameiweka kwa namna ya utulivu kabisa, kisha kuanza kuikabili akili yake.

    Nilimuelewa mwandishi vizuri kuhusu namna ya kufanya tahajudi, akazidi kueleza kuwa mtu anapofanya meditation, anachofanya ni kuiruhusu akili yake kurudi katika hali ya asili ambapo uzingativu, usikivu, utulivu na uvumilivu huwa ni wa kiwango cha juu. Katika hali hii ya utulivu, mwandishi alieleza kuwa unaweza kuiamuru akili yako ifanye kile unachokitaka na kweli matokeo yakaonekana.

    Akaendelea kueleza kuwa wakati mwingine, tahajudi huambatana na matumizi ya maneno fulani (mantra) kwa kuyataja na kuyarudiarudia mara nyingi ambapo kile kinachotamkwa au kunuiwa, hutokea ndani ya muda mfupi. Akaeleza kuwa hata wachawi wanapotaka kumroga au kumdhuru mtu, hutumia tahajudi.

    “Mtu akitaka kukuroga, lazima awe anakujua jina lako ambapo hutafuta sehemu tulivu na kuanza kulitaja jina lako mara nyingi na kunuia kile anachotaka kitokee.

    Kama anayelengwa si mtu anayejitambua, nguvu zinazorushwa humpata kirahisi na hapo ndiyo tunasema fulani amerogwa,” ilisomeka sehemu ya kitabu kile. Nikapigia mstari kwa kutumia penseli kwenye kipengele hicho.

    Zikaelezwa faida za tahajudi ambapo niligundua kuwa ni kitendo chenye faida nyingi sana kwenye mwili na akili ya binadamu.



    Baada ya kuhakikisha nimeelewa vizuri, nilikaa sakafuni kwa utulivu kabisa, nikawa navuta hewa kwa kutumia pua na kuitoa kupitia mdomo huku nikiwa nimefumba macho yangu. Nilijiachananisha na mawazo yote yaliyokuwa yananikabili, nikawa nafanya tahajudi.



    Baada ya dakika chache, nilijikuta nikitokewa na hali ambayo sikuwahi kuihisi tangu nizaliwe.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nilijihisi naelea angani, sehemu ambapo hakukuwa na mtu mwingine yeyote zaidi yangu. Nikawa naendelea kupumua kwa uhuru, nikivuta hewa kwa pua na kutoa kwa mdomo. Nilifurahia hali ile kwani kwa mara ya kwanza, nilijihisi nikiwa sina mawazo yoyote kichwani, sikuwa nikifikiria wala kuona chochote zaidi ya taswira yangu mwenyewe, nikiwa naelea kwenye giza.



    Sikujua nimekaa kwenye hali ile kwa muda gani lakini nilikuja kurejewa na fahamu zangu za kawaida na kugundua kuwa kumbe baba alikuwa ameingia chumbani kwangu na kusimama kwa muda mrefu akinitazama.



    Nilishtuka na kujifikicha macho nikiwa siamini nilichokuwa nakiona mbele yangu. Sikujua baba alisimama pale kwa muda gani kwani hata wakati anaingia sikumsikia wala sikuhisi kitu chochote.

    “Umeanza kuwa mchawi siyo? Kwa nini unawanga ndani ya nyumba yangu?”

    “Baba mimi siyo mchawi, nilikuwa nafanya ‘meditation’, tumejifunza shuleni kuwa inasaidia kutuliza akili na kuijengea akili ya kufanya maamuzi sahihi na kufanya chochote tunachokiwaza kitokee.”

    “Hakuna, usijifanye unajua kugeuzageuza maneno, haiwezekani nisimame kwa zaidi ya dakika ishirini hapa mbele yako bila kugundua kuwa kuna mtu anakutazama, ulikuwa unawanga na leo nitakufunza adabu,” alisema baba huku uso wake ukiwa umefura kwa hasira, alininyanyua kutoka pale sakafuni nilipokuwa nimekaa, akanibeba juujuu mpaka sebuleni.

    Alinishika mikono yote miwili kwa kutumia mkono wake mmoja, nikamuona akifungua mkanda wa ngozi aliokuwa amevalia suruali yake, akaanza kunicharaza mwili mzima bila huruma.

    Nililia kwa uchungu sana kwani niliona ananionea, sikuona kama kuna kosa lolote mimi kujifunza kufanya meditation kwani nilisoma kwenye kila kitabu kuwa huko ulaya elimu ile hufundishwa kwenye madarasa rasmi tofauti na hapa Tanzania.

    Wakati anaendelea kunichapa, ili kujitetea nilimtishia kuwa akiendelea kuniadhibu nitatoa siri ya nilichokiona siku wakati tunahama kutoka kule kijijini Itete, nilivyomfuma akiwa na zana za kiganga chumbani kwake na jinsi alivyowadanganya watu kuwa amemponya Sinai ulemavu wakati tangu awali hakuwa na tatizo lolote.

    Niliposema vile, baba aliniachia na kunipiga teke kwa nguvu, nikaenda kujigonga ukutani na kuanguka chini, nikasimama na kukimbilia nje huku nikichechemea mguu mmoja. Nililia sana siku ile mpaka macho yakabadilika rangi na kuwa mekundu kama nimemwagiwa pilipili.

    Mama aliyekuwa ameenda sokoni kutafuta mboga, alirudi na kunikuta nikiwa nimekaa karibu na barabara ya kuingilia pale nyumbani, huku nikiwa naendelea kulia kwa kwikwi, mwilini nikiwa na alama nyingi za mikanda niliyochapwa na baba.

    “Hee! Umepatwa na nini mwanangu,” aliniuliza mama huku akionekana kushtuka kutokana na hali aliyonikuta nayo. Sikumjibu kitu, kitendo cha kuniuliza kikawa ni kama kimeniongezea hasira na uchungu ndani ya moyo wangu, nikawa nalia kwa kwikwi huku nikijitoa kwenye mikono ya mama.

    Alinibembeleza na kunikumbatia kwa upendo, akanishika mkono na kuelekea ndani, tukamkuta baba akiwa amesimama mlangoni.

    “Huyo mwanao siku hizi anajifunza uchawi, nimemfuma kwa macho yangu akiwanga ndani ya chumba chake ndiyo nimemuadhibu,” alisema baba huku akionekana bado ana hasira na mimi.

    “Muongo, yeye ndiyo mchawi,” nilisema huku nikiendelea kulia kwa kwikwi, baba akawa anataka kuja kuniongeza lakini mama alimzuia, wakaanza kujibizana wenyewe kwa wenyewe.

    “Hata kama amefanya makosa ndiyo uniumizea mwanangu kiasi hiki? Cheki alivyovimba! Kwa nini unakuwa mkatili kiasi hicho mume wangu,” alisema mama huku na yeye akianza kulengwalenga na machozi.

    Baba alishindwa cha kujibu, akaingia ndani na kutuacha tukiwa pale mlangoni na mama.

    “Kwani baba yako amekukuta ukiwa unafanya nini?”

    “Nilikuwa nafanya ‘meditation’,” nilimjibu mama, akanitazama kwa macho ya udadisi.

    “Meditation ndiyo nini? Wewe nani kakufundisha?” aliniuliza, nikaanza kumfafanulia. Mama alionesha kutoridhishwa na majibu yangu, akaniambia nikitulia nitamueleza kwa kina. Akapasha maji ya moto na kuanza kunikanda mwili mzima. Nilikuwa nikisikia maumivu makali sana.



    “Huyu mtoto tukiendelea kukaa naye hapa atatuletea matatizo makubwa sana, inabidi tumhamishie kwa baba yake mkubwa jijini Dar es Salaam.”

    “Hapana mume wangu, huko ndiyo atazidi kuharibika, inabidi tubaki naye hapahapa ili tumdhibiti vizuri.”

    “Hapana, nimeshasema lazima tumhamishie Dar, kwanza ameanza kutishia kuwa atatoa siri kwa waumini wangu kuhusu huduma hii ya maombezi na uponyaji.”

    “Mh! Makubwa, lakini na wewe unazidi kuwa mkali kwa watoto mpaka inafikia hatua wanakuogopa kama simba, jirekebishe mume wangu, hawa wameshakuwa wakubwa sasa,” mama alikuwa akijadiliana na baba chumbani kwao.

    Nilikuwa nimelala kwenye kochi huku nikiendelea kuugulia maumivu makali niliyokuwa nayahisi, nikawa nasikia kila kitu walichokuwa wanakizungumza.

    Japokuwa mama alikuwa akipinga suala la mimi kupelekwa Dar, kimoyomoyo nilifurahi sana kwani ndani ya kile kitabu, kuna sehemu nilisomakuwa kuna vituo vingi jijini Dar es Salaam vinavyofundisha elimu ya utambuzi, nikaona hiyo ndiyo fursa pekee ya kujua mambo mengi niliyokuwa na hamu ya kuyajua.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Walijadilianakwa muda mrefu sana, baadaye nikamsikia mama akikubaliana na wazo la mimi kuhamishiwa jijini Dar kwenda kuishi na baba mkubwa ambaye alizaliwa tumbo moja na baba, akiwa ni mfanyakazi wa Mamlaka ya Bandari. Niliwahi kumsikia mama akisema kuwa baba mkubwa anaishi Kimara Kona, karibu na ofisi za FAJI (Familia ya Jitambue).



    Nikiwa kule chumbani, niliamka na kuanza kurukaruka kwa furaha baada ya kupata uhakika kuwa siku chache zijazo nitahamia jijini Dar es Salaam. Pamoja na ujanja wangu wote, sikuwahi kufika Dar hata siku moja, nikaona huo ndiyo wakati muafaka wa kujifuta matongotongo kwenye macho yangu.



    Kulipopambazuka, mama aliwahi kuja chumbani kwangu kunijulia hali kwani nililala nikiwa na maumivu makali baada ya kuadhibiwa vikali na baba.

    “Umeamkaje baba,” aliniuliza mama huku akinishika shavuni kwa upole.

    “Nimeamka salama mama, leo najisikia ahueni, siyo kama jana.”



    “Pole mwanangu, utapona kabisa wala usijali, enhee niambie vizuri kuhusu ile sijui nini huko uliyokutwa unaifanya na baba yako jana.”

    “Meditation?”

    “Eeeh, hiyohiyo,” alisema mama huku akikaa vizuri kitandani kwangu, akawa ananipapasa kwenye majeraha yangu niliyoyapata baada ya kupigwa na mama.

    Nilichompendea mama yangu, tofauti na baba, alikuwa akituonesha upendo wa dhati kiasi kwamba mambo yetu mengi tulikuwa tukimwambia yeye. Alikuwa mpole, mkarimu na msikivu kwetu ndiyo maana hata aliponihoji kuhusu meditation, sikuona ubaya wowote kumueleza.



    “Kwa Kiswahili inaitwa tahajudi, ni kitendo kinacholeta usawaziko kati ya mwili, akili na roho. Huyafanya mawazo yatulie kabisa na hivyo kutoa nafasi kwa mwili usioonekana au roho kuinuka na kupaa kwenda kwenye ukamilifu wa kibinadamu,” nilimwambia mama.



    “We mtoto, hayo mambo umeyajulia wapi? Mbona unajua vitu vikubwa kuliko umri wako? Mimi pamoja na umri wangu mkubwa ndiyo kwanza hayo mambo nayasikia kwa mara ya kwanza kutoka kwako,” alisema mama huku akikaa vizuri. Maelezo yangu kuhusu meditation yalimshangaza sana.

    “Nimejifunza mwenyewe mama, kile kitabu ambacho baba alikichana ndiyo kilikuwa na mambo yote hayo.”

    “Sasa baba yako na yeye angekuwa anayajua mambo haya si yangemsaidia sana kwenye kazi zake za uchungaji kuliko kutumia tunguri?” alisema mama, nikaendelea kumuelezea faida za tahajudi kama nilivyozisoma kwenye kile kitabu. Baada ya kuongea kwa muda mrefu na mama, aliniomba na yeye nimfundishe namna ya kufanya meditation.

    Niliamka pale kitandani na kuchukua jamvi, nikatandika chini na kumwambia mama akae kama mimi nilivyokuwa nimekaa. Akakunja miguu na kukaa kama wafanyavyo waumini wanapokuwa kwenye ibada, mkao ambao wengine huuita ‘atahiyatu’.

    Nilimwambia aiunganishe mikono yake kwa kupishanisha vidole vya mkono wa kushoto na wa kulia, nikamwelekeza kuyatuliza mawazo yake na kuhakikisha akili yake inafikiria jambo moja tu, pumzi alizokuwa anazivuta na kuzitoa. Alinielewa haraka kuliko nilivyofikiria, tukatulia kimya, muda mfupi baadaye kila mmoja akawa ameshachukuliwa kiakili na meditation.

    Mimi ndiyo nilikuwa wa kwanza kurejewa na fahamu, nikasimama na kujinyoosha miguu ambayo ilikuwa inauma kutokana na kukaa kwa muda mrefu. Nikamtingisha mama taratibu, na yeye akazinduka lakini tofauti yake, yeye alishtuka sana wakati akirejewa na fahamu zake. Almanusra aanguke, nikawahi kumshika na kumkalisha vizuri.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Heee! We mtoto mbona una miujiza kiasi hiki? Yaani nilikuwa naelea angani kama nyota au mwezi, sijawahi kuihisi hali kama hii tangu nizaliwe. Nilikuwa sijielewi kama nipo macho au nimelala, nimeshindwa kutofautisha kama hizi zilikuwa ni ndoto au maono, mbona maajabu?” alisema mama huku akisimama na kujinyoosha miguu.

    Nikaendelea kumfafanulia kuwa ukiwa katika hali ile, roho ndiyo inayochukua nafasi ya mwili, nikamwambia kuwa hata vitabu vya dini vinaeleza kuwa mtu anapokufa, roho huwa inauacha mwili kama ilivyotokea tukiwa kwenye meditation.

    “Lakini mwanangu, mbona nasikia kuwa haya mambo yanahusiana na dini ya shetani?”

    “Mimi pia nimewahi kusikia hivyo kabla sijaamua kuutafuta ukweli lakini naona kama mambo ni tofauti. Hakuna cha dini ya shetani wala nini.”

    “Unataka kusema duniani hakuna dini ya shetani?”

    “Dini zote zinaamini kuhusu uwepo wa Mungu mmoja, hata jamii ya wajenzi huru nao wanaamini katika Mungu mmoja na siyo shetani kama watu wanavyoaminishwa uongo.”

    “Mh! Mungu gani anayeruhusu watu kuwatoa wengine kafara? Mbona nasikia wajenzi huru huwa wanatoa kafara za damu?”

    “Hakuna kitu kama hicho, hizo ni propaganda zilizopandikizwa na watu waliokuwa na masilahi yao binafsi, sijasoma sehemu yoyote inayoonesha kuwa wajenzi huru huwa wanatoa kafara za binadamu, ila kwenye Kitabu cha Mwanzo kwenye Biblia kuna sehemu inasema Ibrahim, baba wa imani aliambiwa na Mungu amtoe kafara mwanaye Isaka, sasa sijui uhusiano wake ni upi?”

    “Biblia inatufundisha kuwa watu wa zamani walikuwa wanatoa kafara kwa Mungu kama ishara ya shukrani na kipimo cha imani lakini tangu kuja kwa mwana wa Adam, mambo yote yamebadilika kwani yeye alifunua mapazia ya mbingu na kumfanya binadamu awe na mawasiliano ya moja kwa moja na muumba wake.”

    “Sasa mama, hivi…” nilitaka kumuuliza mama swali lakini akanikatisha.

    “Sitaki maswali yako magumu, ngoja nikaandae chai, baba yako akirudi atataka akute kila kitu kipo tayari. Halafu nilitaka kusahau, wiki ijayo tutakusafirisha kwenda Dar kwa baba yako mkubwa, utasoma hukohuko mpaka umalize darasa la saba,” alisema mama na kufungua mlango, akatoka na kuniacha nikichekacheka mwenyewe kama mwendawazimu.



    Hamu ya safari ilizidi kunijaa kiasi kwamba niliona siku haziendi haraka. Kila siku nilikuwa nikiwaza juu ya kufika Dar es Salaam, jiji ambalo nilikuwa nikizisikia sifa zake. Niliendelea kufanya maandalizi madogomadogo kama kufua nguo zangu na kuzinyoosha kisha kuzihifadhi kwenye begi.

    Siku zilizidi kusonga mbele na hatimaye safari ikawadia. Japokuwa sikuwahi kufika Dar es Salaam kabla, baba aliniambia nitasafiri peke yangu na nikifika Ubungo, nitamkuta baba mkubwa ananisubiri. Aliniandikia namba zake za simu kwenye kikaratasi na kunipa maelekezo muhimu. Alfajiri na mapema wakanisindikiza mpaka stendi.

    “Kuwa makini mwanangu, ukifika utulie na umsikilize baba yako mkubwa na mkewe, usithubutu kuonesha dharau wala utundu wa aina yoyote, sawa mwanangu?”

    “Sawa mama, nimekusikia na nakuahidi kuwa mtiifu kwa siku zote.”

    “Na tabia zako za kishetanishetani uziache, nitakuwa nampigia simu baba yako mkubwa mara kwa mara, kama hutaacha mambo yako nitajua cha kukufanya,” alidakia baba na kuingilia mazungumzo yangu na mama. Ilibidi tunyamaze kimya, baba akaendelea kuongea huku akiweka msisitizo juu ya mimi kuachana kabisa na kile alichokiita dini ya shetani.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kimoyomoyo nilijisemea kuwa lazima nifahamu mambo mengi kuhusu elimu ya utambuzi na kuutafuta ukweli kama hicho kinachoitwa dini ya shetani kinahusiana na shetani kweli au ni propaganda za kuwachanganya watu akili.



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog