Search This Blog

BABA KIUMBE WA AJABU - 2

 





    Simulizi : Baba Kiumbe Wa Ajabu
    Sehemu Ya Pili (2)


    ILIPOISHIA


    “Nzuri sijui zako?”
    “Eti shemu dada Monika yupo wapi?”
    “Masalu swali gani hilo? Ina maana mtu akifa huwa anakwenda wapi?”
    “Una maana ni kweli dada Monika amekufa?”
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    “Masalu kioja gani unataka kunionesha, ina maana wakati Monika anakufa wewe ulikuwa wapi?”

    “Sasa kama amekufa maiti yake imezikwa wapi?”

    “Mimi nitajua wapi, wakati nilifukuzwa?”

    “Kama kazikwa mbona hakuna kaburi lake?”

    “Masalu upo sawa?”

    “Kwani wewe unanionaje?”

    “Nakuona haupo sawa.”

    “Nipo sawa na akili timamu.”

    “Kama kweli una akili timamu usingeniuliza suala la kifo cha Monika.”

    “Shemu kama dada alikufa mbona wewe mumewe haukuwepo msibani?”

    “Masalu, nilifukuzwa kama mbwa na kutishiwa maisha, kwanza nikionekana nimesimama na wewe nitajitafutia balaa.”

    “Shemu una uhakika Monika amekufa?”

    “Ndiyo.”

    “Ulimshuhudia kabisa amekufa?”

    “Monika amefia mikononi mwangu na kuna mengi alinieleza ya kukueleza lakini sikupata muda wa kuonana na wewe. Kama ni kweli aliyosema Monika basi familia yetu itakuwa ina hatari kubwa.”

    “Kuhusu utajiri?” Nijikuta naropoka.

    “Nalo hilo alilizungumzia, ila wamemtesa sana mke wangu mpaka kifo chake. Kibaya wamemuua hata mtoto wangu aliyekuwa tumboni bila kosa, yaani siamini familia yako kuna na roho mbaya kiasi hicho. Kama mtu kawapatia utajiri akisema amechoka na yeye anataka maisha yake kuna ubaya gani?” Maskini shemeji yangu alizungumza huku akitokwa na machozi, nilijikuta nikitokwa na mimi machozi bila kupenda.

    “Masalu familia yenu haifai, unafikiri maisha ya kuongozwa na nguvu za kishirikina mwisho wake nini? Haya sasa wamemuua Monika nani atafuata na kwa taarifa kidonda alichokikataa dada yako kitahamia kwako. Kabla ya kufa kaitaja familia yenu wote kuwa wanagombania roho yake kasoro wewe pake yako na kuonesha jinsi gani huhusiki na mateso ya mke wangu.”

    “Mungu wangu!”

    “Huo ndio ukweli wenyewe, hujiulizi kwa nini mama yako bado analima kama sio ushirikina, hivi baba yako hana pesa ya kuwapa watu walime na mama yako na utu uzima wake apumzike?”

    “Anaweza.”

    “Kama anaongeza majumba na magari kwa nini mama yako usipumzike, hebu angalia ndugu zako wakubwa. Nao wana roho ya tamaa ya mali kushindwa kumuonea huruma mama yenu. Nasikia ndani mwenu kuna chumba kisichofunguliwa, unajua kuna nini?”

    “Hata sijui!”

    “Kwa taarifa yako kuna maiti ya mtoto mchanga ambayo kila baada ya siku tatu hupakwa mafuta ili isiharibike.”

    “Shemuuuu! Umejuaje?” Nilishtuka kusikia habari zile, chumba alichokisema kweli kilikuwepo ambacho sikuwahi kukiona kikifunguliwa.

    “Dada yako Monika alikuwa na siri nzito moyoni mwake, nyingine alisema hawezi kuniambia labda ungekuwepo kabla ya kufa kwake.”

    “Sasa yeye alijuaje kama kuna maiti ya mtoto?”

    “Mara nyingi kazi ile aliifanya yeye, baba na mama yenu. Hakuna mtu mwingine aliyeruhusiwa kuifanya.”

    “Mmh! Maiti ya mtoto wa nani?”

    “Kama una kumbukumbu, nasikia mtoto wa kwanza wa dada yako ambaye ndiye aliye na pesa kuliko wote alimtoa mtoto wake kafara ili kuongeza utajiri.”

                                                                        *****

    Kauli ile ilinirudisha nyuma na kukumbuka miaka sita iliyopita dada mkubwa alifiwa na mwanaye lakini mazishi yake sikuyaelewa japo msiba ulikuwa nyumbani. Kingine kilichonifungua macho hakikuwa na tofauti na msiba wa Monika kilikuwa cha kifamilia tena ya ndani hata wanandugu hawakujulishwa. Taratibu nilianza kufunguka akili na kuamini kila lililosemwa na Monika lilikuwa na ukweli mkubwa.

    “Asante shemu kwa kunifumbua macho,” nilimshukuru ili tuagane, nilipotaka kuondoka aliniuliza kitu.

    “Masalu unataka kuniambia hukuwa na habari Monika amekufa au ulitaka kunitega akili?”

    “Shemu, huwezi kuamini kila dakika nimekuwa nikichanganyikiwa juu ya taarifa za msiba wa dada Monika. Kweli niliuona mwili ukiteremshwa kwenye gari. Lakini tokea hapo sikuweza kujua nini kilichoendelea mpaka leo hii.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Ulipouliza walikujibu nini?”

    “Sijauliza bali nilifanya upelelezi wangu, kila kona nilifika lakini sikupata kuona chochote.”

    “Ulichunguza nini?”

    “Sehemu za makaburi au kupata taarifa kama hajafa yupo wapi?”

    “Una uhakika Monika hakuzikwa?”

    “Nina uhakika.”



    “Basi kuna sehemu wamemuweka, isiwe naye wamemuweka kwenye hicho chumba  na kumpaka mafuta?”

    “Mmh! Sijui.”

    “Unaweza kuingia?”

    “Mmh! Nitajitahidi kuhakikisha napata ukweli.”

    “Basi utakachokipata usikose kunijulisha.”

    “Nakuahidi kukuletea kila kitu.”

    “Haya shemu kwaheri.”

    “Ya kuonana.”

    Niliagana na shemu na kurudi zangu nyumbani, nilizidi kuchanganyikiwa na maneno ya pande mbili juu ya ukweli juu ya kifo cha dada Monika. Moyoni niliapa nikipata muda lazima mama ataniambia ukweli.

    Siku zilikatika bila kujua taarifa za uhakika kuhusiana na habari tata juu ya kifo cha dada Monika ni kweli amekufa? Kitu ambacho moyo wangu haukukubaliana nacho. Uvumilivu ulinishinda, siku moja nilimfuata mama shambani kutaka kujua ukweli wa dada Monika. Kama kawaida yangu nilidanganya naumwa.                                                       

    *****

    Baada ya kuondoka na kuniacha nyumbani na mfanyakazi, majira saa nne asubuhi nilikwenda hadi shamba. Nilimkuta mama akipiga jembe kama hana akili nzuri. Moyoni nilimuonea huruma jinsi alivyohenyeka japo tuna pesa, kila dakika niliyakumbuka maneno ya dada Monika kuwa maisha yetu yanaongozwa na ushirikina.

    Nilimwita mama ambaye alishtuka kuniona, niliamini kabisa alijiandaa kutokana na kumuuliza maswali mazito siku ya kwanza.

    “Wee Masalu mbona huku si unaumwa?”

    “Kidogo nimepata nafuu.”

    “Haya ulikuwa unasemaje?”

    “Kuna kitu mama kinanisumbua kila siku naomba msaada wako kwani naweza kuwa chizi.”

    “Wee mwana mbona una mambo kuna nini tena?”

    Mama alisema huku akiweka jembe pembeni na kunifuata nilipokuwa nimesimama.

    “Masalu  kuna  nini tena?” Mama aliniuliza huku akifuta jasho kwenye paji la uso kwa mkono.

    “Mama toka kifo cha dada Monika kuna mambo yamekuwa yakinichanganya na kunifanya kila siku nisijielewe.”

    “Masalu mambo gani tena mwanangu kila siku huishi vioja?”

    “Kuhusu dada Monika.”

    “Monika kafanya nini tena?”

    “Mama ni kweli dada Monika amefariki?”

    ”Masalu wewe si mtoto mdogo sasa, kila mtu anajua Monika amefariki wewe ukiwemo.”

    “Mamaa, kama dada Monika amefariki mbona sikuona mazishi wala kaburi lake.”

    “Masalu uyaone hayo ili yakusaidie nini?”

    “Mama unajua majirani wanatusema vibaya toka taarifa za kifo cha dada Monika.”

    “Nani aliwaambia Monika amekufa?”

    “Mamaa, kwani kifo cha dada Monika kilikuwa cha siri?”

    “Hata kama sio cha siri sio lazima wajue.”

    “Hivi mama watu wakiniuliza dada Monika yupo wapi mimi niwajibu nini?”

    “Wanyamazie usiwajibu chochote.”

    “Lakini mama, kumbe hata yule shemeji aliyekuwa anakaa na dada Monika mlimfukuza asihudhurie mazishi?”

    “Ahudhurie ametoa kiasi gani cha pesa kwa dada yako, zaidi ya kutuchanganya kifamilia?”

    “Lakini mama tuachane na hayo, kaburi la babu na bibi nalifahamu, kaburi la kaka mkubwa nalifahamu. Makaburi yote yanayotuhusu nayafahamu na kila mwisho wa mwaka huenda kuyazuru familia yote na pia huenda kila mwezi kusafisha na kuyaweka katika hali ya usafi. Lakini kaburi la dada Monika lipo wapi, japo sikuhudhuria mazishi yake?”

    “Masalu, wee mtoto mdogo hujui lolote, elewa kuwa dada yako Monika amefariki.”

    “Mama, bado hayajaniingia akilini.”

    “Masalu hebu niondokee, nilifikiri jambo la maana kumbe ni upumbavu,” mama alisema huku akijiandaa kurudi shambani.

    “Mama unaniona mtoto lakini mambo yetu yote yapo hadharani.”

    “Mambo gani?” Mama alishtuka na kunigeukia ili kutaka kujua.

    “Dada Monika alinieleza mengi kuhusiana kifo chake alichotishiwa na baba kwa ajili ya kukikataa kidonda na kunitisha kidonda kile kitahamia kwangu.”

    “Masalu nikueleze mara ngapi kuwa dada yako Monika alikuwa muongo aliyetaka aonekane alichokifanya ni sahihi cha ukosefu wa adabu?”

    “Lakini mama mbona mengi aliyonieleza yanatokea? Uongo wake ni nini?”

    “Kama nini?”

    “Kuhusu wewe kuteseka na kilimo wakati familia ina uwezo mkubwa?”

    ”Kulima si kujitesa bali kujipa mazoezi.

    “Mama, juzi uligombana na baba akikulazimisha uje shamba wakati ulikuwa hujisikii vizuri hata juzi uliniambia hukulala kutokana na maumivu ya mgongo. Mama naona umejisahau pale uliponiambia kuwa baba atakuua kwa vitu vya kulazimishana, bado tu unasema mazoezi. Mama unaweza kuona mnafanya siri lakini kila kitu kipo wazi.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/“Unaweza kuona watu wapo kimya, lakini kuna maneno mengi sana juu ya kifo cha dada Monika, hakina tofauti na kifo cha mtoto wa dada Mihayo.”

    “Masalu! Hakina tofauti ya nini?”

    “Wanasema hata mtoto wa dada Mihayo alipokufa hakuzikwa.”

    “Hakuzikwa alifanywa nini?” Maskini mama aliniuliza huku macho yakimtoka pima na kijasho chembamba kilimvuja.

    “Eti wanasema kile chumba ambacho hakifunguliwi ndani kuna maiti ya mtoto ambayo huwa mnaipaka mafuta kila siku ndicho chanzo cha dada Mihayo kuwa na utajiri mkubwa kuliko wenzake.”

    “Wee mtoto, haya yote umeyasikia wapi?” Mama alishtuka.

    “Shemeji aliniambia kuwa kabla dada hajakata roho alimueleza mambo mengi juu ya ushirikina wa familia yetu kutumia kidonda chake kujipatia utajiri na hata alipotoka nyumbani kukataa kuendelea na kidonda ilisababisha kifo chake.”

    “Masalu! Alimueleza kuwa kwenye chumba hicho kuna maiti ya mtoto?”

    “Ndiyo, tena alimueleza kuwa watu waliokuwa wakiipaka maiti ile mafuta ni wewe baba na yeye dada Monika.”

    “Mungu wangu, kayasema hayo Monika?”

    “Na wasiwasi mwingine wanasema maiti ya dada Monika huenda nayo haikuzikwa imefichwa kwenye chumba kile cha siri.”

    “Ooh... Mungu wangu ...Ooh moyo wangu,” mama alisema huku akishikilia kifua na kuanguka chini. Nilipojaribu kumuamsha hakuamka, nilipiga kelele kwa majirani wa shamba la pili. Sauti yangu iliwakusanya watu ambao walifika na kumpa huduma ya kwanza mama aliyekuwa amepoteza fahamu.

    Alipopata fahamu aliwaomba wampe msaada wa kumrudisha nyumbani, jirani yetu mama Kusekwa alimsindikiza mama hadi nyumbani. Tulipofika alituacha na yeye kurudi shambani. Nilijawa na wasiwasi huku nikijilaumu kwa kumueleza mama mambo ambayo niliyaona mazito.

    Nikiwa pembeni ya mama aliyekuwa bado amejilaza kwenye zulia huku akipuliziwa na upepo wa feni aliniita:

    “Masalu.”

    “Naam mama.”

    “Kuna mtu aliuliza sababu ya kuanguka kwangu?”

    “Ndiyo mama.”

    “Uliwajibu nini?”

    “Niliwaeleza kuwa ulianguka ghafla.”

    “Hawakukuhoji zaidi?”

    “Hawakunihoji zaidi ya kukupa huduma ya haraka.”

    “Ooh, afadhali.”

    “Unajisikiaje kwa sasa?” Nilimuuliza mama kwa huruma.

    “Mmh, sijambo kidogo ila nakuomba tuliyozungumza yote usimwambie mtu.”

    “Sawa mama.”

    Nilimkubalia ili tu kuiacha siku ile ipite pia kutokana na hali yake, lakini bado sikupata jibu la dada Monika amekufa kweli, japo shemeji alinihakikishia amekufa. Na kama amekufa amezikwa wapi au ndiyo yaleyale niliyoelezwa kuwa mwili wake umefichwa ndani.

    Moyoni nilibakia njia panda kutaka kujua ukweli kuhusu dada Monika, nilipanga kama mama atashindwa kunieleza basi nitamvaa baba na ukali wake ili nijue amekufa au mzima na kama amekufa amezikwa wapi.

    Sikutaka kuliulizia jambo lile haraka kutokana na hali ya mama, niliamua kukaa kimya, lakini moyoni sikuwa na raha kutaka kujua ukweli wa kifo cha dada Monika. Siku moja asubuhi kabla ya kwenda shule mama alinifuata chumbani kwangu na kunieleza nisiende shule kuna sehemu anataka kunituma.

    Nilibadilisha nguo zangu za shule na kuvaa za nyumbani, wakati huo alikuwa akijiandaa kwenda shambani. Lakini siku ile hakuwahi kama ilivyo kawaida yake. Tuliondoka nyumbani pamoja kuelekea shambani, baada ya muda wa chai, kutoka  nyumbani mpaka shambani ni mwendo wa dakika 45. Tulikwenda huku tukizungumza, mama aliniulizia habari za shule, nilimuelezea maendeleo yangu japo hakuwahi hata siku moja kushika madaftari yangu kuyaangalia.

    Katika kumbukumbu zangu nilielezwa kuwa mama aliishia darasa la sita baada ya kupewa ujauzito na baba kisha kumtorosha. Taarifa hizo alinipa marehemu ambaye sina uhakika kama kweli amekufa au maiti yake imefungiwa katika chumba kisichofunguliwa.

    Dada Monika alinieleza kuwa mama yetu alitengwa na familia yake baada ya kubebeshwa ujauzito na baba na kutoroshwa. Kitendo kile ndicho kilichofanya mama aishi maisha ya peke yake bila ndugu, ndugu yake mkubwa alikuwa baba kitu kilichofanya amnyanyase kwa kujua hana pa kwenda.

    Sababu ile ndiyo iliyomfanya mama aishi kama mtumwa kwa vile kila alipofanya kosa baba alimtishia kumfukuza. Kwa kweli kitendo cha baba nilikiona cha kikatili sana, kila dakika nilijikuta nikimchukia baba kwa roho mbaya ya kuitesa familia yake kwa ajili ya mali.

    Niliamini  mateso ya muda mrefu na shuluba zote, baada ya kupata utajiri wa kushirikina, basi alitakiwa mama atulie na kufaidi matunda ya uchawi wao. Lakini imekuwa tofauti mama kila kukicha amekuwa mtu wa  kusurubika. Kilichonishangaza ni ndugu zangu kushindwa kumsimamia mama na kumpunguzia mateso ya kulima na kupasua kuni. Kila nilipomtazama mama yangu roho iliniuma na kujiapiza kama Mungu atanisaidia kupata kazi na kuwa na maisha mazuri basi nitamuondoa kwa baba.

    Moyoni nilijiapiza kutokubali kuishi maisha machafu ya ndugu zangu ya kutoa familia zao kwa ajili ya kafara ya hatari na kujiona kama wataishi milele. Nilijiuliza dada Mihayo atamwambia nini mwanaye mbele ya Mungu, aliyemtoa kafara kwa ajili ya utajiri na baadaye kuendelea kumtesa kwa kumlaza kwenye chumba?

                                                                 ****

    Kuna kitu alinieleza dada Monika juu ya mama na kuniomba nimchunguze, nakumbuka siku hiyo alinieleza:

    “Masalu, mama yetu anaishi maisha ya mateso makubwa sana, baba ni shetani asiyefaa mbele ya jamii. Nataka nikueleze kitu kimoja ambacho mimi wananikataza. Kwa taarifa yako nilikatazwa kulala na mwanaume lakini baba ana mwanamke kamjengea nyumba ya gharofa moja.”

    Dada Monika aliendelea kunieleza jinsi watu wanavyotumia pesa huku mama akiteseka, alinieleza:

    “Mdogo wangu familia yetu yote tutateketea kwa moto wa kiama, hebu ona maisha ya mama yanalingana na utajiri tulionao? Hata kama kuyumba hatuwezi kuishiwa kiasi cha kutisha, sawa na tembo kuugua maralia hawezi kukonda kama mbwa.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Masalu, sema tu mama mbishi, nilimueleza mapema tuondoke pamoja ili aepukane na maisha ya mateso, lakini mama kama amerogwa na baba haelewi hasikii. Hivi kweli mama yetu ni wakuvaa kandambili za kufunga na kamba?” Nakumbuka siku hiyo dada Monika alizungumza huku akibubujikwa machozi.

    Mama anateseka dada Mihayo anamhonga bwana wa pembeni gari, Masalu inauma lakini sina uwezo. Kama kidonda hiki angekuwa nacho mtu mwingine na mimi kuwa na uwezo wa dada Mihayo hata kwa kutoa kafara ya mtoto mama yangu angeishi kama malaika.

    Lakini sina uwezo, hata hiki kidogo ninachokipata nikimpelekea mama hatakitumia zaidi ya kugeuzwa ndondocha na baba.”                                                           

    Kila nilipoyakumbuka maneno ya dada nilijikuta nikitokwa na machozi. Nilikumbuka neno moja ambalo dada Monika alinieleza nilifanyie kazi, aliniambia:

    “Masalu, mchunguze mama muda mwingi akiwa peke yake mkono huwa shavuni, na kama utamfuatilia kwa muda baada ya kutoa mkono shavuni hutikisa kichwa na kufuta machozi. Katika maisha yetu toka tupate utajiri wa kishirikina furaha ya mama imetoweka, kutabasamu kumekuwa kama ajali lakini kulia kumekuwa kitu cha kawaida.

    Mara nyingi mama amekuwa kila akiwa peke yake kanga huwa mkononi ili kufuta machozi. Vitu vile nilivifanyia kazi na kumueleza dada Monika yote aliyonieleza ni kweli. Aliniuliza swali lingine:

    “Masalu umeshawahi kumuona mama akivaa nguo mpya?”

    “Hapana,” nilimjibu.

    “Hebu jifikirie mama yetu ni wa kuvaa nguo zilizoachwa na wanaye?”

    “Nilikuwa sijui.”

    “Kama hujui, hata macho yako hayaoni? Masalu sasa hivi wewe si mtoto unaona vitu ambavyo baadaye vinataka majibu kwa kile ulichokiona.”

    “Huwezi kuamini dada nilikuwa kama nimefungwa akili, unachonieleza sasa hivi ndiyo kama kwangu kunapambazuka baada ya kukaa gizani kwa muda mrefu. Kama usingenieleza haya ningekufa kibudu.”

    Niliamini kabisa kama dada Monika kweli amekufa, basi alikuwa amekufa na mengi moyoni sawa na samaki mwenye mengi ya kuzungumza lakini kila alipofumbua mdomo maji yalimjaa mdomoni. Kama alivyonieleza shemeji kabla ya kufa kutokana na maelezo yake mengi angenieleza mengi mazito.

                                                            ****

    Tulipofika shambani mama hakuonesha kama anataka kulima, aliniweka chini ya mti huku akionekana mwingi wa mawazo. Baada ya ukimya mfupi mama aliniita jina langu.

    “Masalu.”

    “Naam mama.”

    “Najua umesikia mengi juu ya maisha yetu, lakini hakuna ukweli kwa yote uliyosikia nakuomba uwapuuze, sawa baba.”

    “Lakini mama mbona yote niliyoelezwa yana ukweli.”

    “Ukweli upi?

    ”Mama kwanza naanza na wewe, toka nipate akili sijawahi kukuona ukifurahi, kila siku mtu wa masikitiko na kutokwa na machozi.”

    “Ha! Masalu umejuaje?”

    “Mama dada Monika kanieleza mambo mengi sana ambayo niliyafanyia kazi na kuupata ukweli juu yako.”

    “Ukweli gani?”

    “Kuhusu muda mwingi kuweka mkono shavuni na kutokwa na machozi, nilikufuatilia bila wewe kujijua na kuupata ukweli, pia uvaaji wako wa nguo mama toka nipate akili sijakuona ukivaa nguo mpya au nzuri, pia mama hebu angalia ndala zako. Kwa maisha tunayoishi wewe si wa kuvaa ndala za kufunga na waya.”

    Niliposema vile mama alijiangalia kama hakujua alichokivaa wakati wa kutoka nyumbani.

    “Mama najua yote haya yanatokea kwa ajili ya nini.”

    “Kwa ajili gani?”

    “Haya ni mateso anayokupa baba, baada ya kutengwa na ndugu zako, na chanzo cha yote ni yeye. Kutokuwa na ukaribu na familia yako, katumia ni fimbo ya kukuadhibia. Hivi mama hata wanao wengine wanajijali wao na kukusahau , bila wewe wangeijuaje dunia?

    “Mama maisha haya unayoishi siyo mazuri, nilisikia eti baba alikutishia maisha kama utataka mambo makubwa. Haya ndiyo aliyoyakataa dada Monika kidonda akitunze yeye wengine wale maisha mazuri. Matokeo yake mnaamua kumuua na kuificha maiti yake.”

    “Masalu nani kaificha maiti ya Monika?”

    “Ipo wapi?”

    “Masalu swali gani hilo, kila anayekufa si huzikwa?”

    “Mbona mtoto wa dada Mihayo hakuzikwa?”

    “Masalu una uhakika gani?”

    “Dada Monika hakunificha yote nisemayo ni yeye aliyeniambia ni mengi sana nayajua kuliko mtu mwingine.”

    “Masalu yote usemayo ni kweli, nakuomba usimwambie mtu yoyote habari hizi.”

    “Kama ni kweli naomba kuanzia leo kazi ya kulima aachiwe mtu mwingine, uvae nguo nzuri ili ulingane na utajiri wa familia yetu.”

    “Masalu hilo haliwezekani.”

    “Kwa nini?”

    “Baba  yako ataniua, naomba mwanangu yote unayoyaona yaache kama yalivyo, na ukizidi kumchokonoa anaweza kukuua.”

    “Kama alivyomuua dada Monika?”

    “Usiseme hivyo Masalu.”

    “Mama tunafichana nini? Hivi utajiri ndiyo unaotufanya tukose huruma kwa wenzetu?”

    “Masalu nakuomba usichimbe sana.”

    “Hapana mama, huwezi kujua sasa hivi tunaonekana vipi mbele ya macho ya watu, kwa taarifa yako inasemekana Monika hajazikwa amewekwa ndani kwa imani za kishirikina.”

    “Nani kasema?” CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Aliyekuwa akikaa na dada Monika ndiye anayeeneza habari hizi.”

    “Yeye kajuaje?”

    “Mama ina maana ninapozungumza na wewe unakuwa wapi? Nilikueleza kuwa kabla ya kufa dada Monika alimpa siri kubwa ya maisha yetu na sababu ya kifo chake. Pia alimueleza kuwa alikuwa na siri nzito ambayo asingemwambia mtu zaidi yangu mimi.”

     “Mmh, sasa huyo kijana kinamhusu nini kututangaza vibaya?”

    “Kinachomuuma ni kumuulia mtoto wake asiye na hatia.”

    “Hivi baba yako akijua kuwa ndiye anayetutangaza vibaya kwa watu kutakuwa na usalama kweli?”

    “Atamfanya nini?”

    “Masalu wee acha baba yako hana dogo, anaweza hata kumkata kichwa.”

    “Akimuua atapata faida gani? Si ndiyo atakuwa anaongeza chuki kwa watu?”

    “Masalu mwanangu, kwa umri wako hata nikueleza kitu hutanielewa, nakuomba kila ulilosikia liache lilivyo, wewe bado mtoto mdogo litakuchanganya.”

    “Sawa nimekuelewa, ila naomba ukweli wa jambo moja.”

    “Jambo gani?”

    ”Kuhusu ukweli wa dada Monika.”

    “Ukweli upi?”

    ”Ni kweli amekufa?”

    “Ndiyo.”

    “Amezikwa wapi?”

    “Mmh! Si makaburini.”

    “Makaburini gani?”

    “Kwa kweli siwezi kujua makaburi gani sikwenda kuzika.”

    “Mama kuna makaburi tofauti na tuliyoyazoea?”

    “Hakuna.”

    “Na misiba yote huanzia kanisani kisha kupelekwa kuzikwa?”

    “Ndiyo.”

    “Sasa msiba wa dada Monika mliupeleka kanisa gani?”

    “Masalu hata ukijua itakusaidia nini?  Aliyekufa amekufa huwezi kumfufua.”

    “Hata kama siwezi kumfufua, dada Monika ndiye kipenzi changu, kaburi lake kwangu ni kielelezo cha kumuona kipenzi changu.”

    “Masalu nakuomba suala hilo uachane nalo.”

    “Yote nitaachana nayo si la dada Monika.”

    “Masalu ukitaka kujua mengi utakosana na baba yako.”

    “Kwa hiyo ukweli dada Monika maiti yake haikuzikwa?”

    “Masalu nakuomba mwanangu chondechonde achana na hayo ili maisha yako yawe salama.”

    “Kwa hiyo nikitaka kujua baba ataniua?”

    “Hawezi kukuua ila utakuwa matatizoni.”

    “Mmh! Sawa mama,” nilikubali kwa shingo upande kutokana na kuonekana kumuweka mama katika wakati mgumu.

    Sikutaka kumsumbua sana mama yangu kutokana na maelezo ya dada Monika, kila nilipomtazama nilimuonea huruma. Nilimuahidi mama toka moyoni mwangu sitaulizia lolote kuhusiana na dada Monika wala kitu chochote kuhusiana na familia yetu.

    Kauli yangu ilimfurahisha mama na kuonekana hawezi kuamini nilichokisema.

    “Kweli Masalu.”

    “Kweli mama, nakupenda sana mama yangu.”

    “Asante Masalu, nakuomba kila unachokijua huenda hata mimi mama yako sivijui kwa vile baba yako alimpenda sana Monika hata siri zingine sizijui ambazo alikueleza wewe na pengine kabla ya kufa angekueleza,” maskini mama yangu alisema huku akitokwa na machozi, kitu kilichozidi kuniumiza nami machozi yalianza kunitoka kwa mbali.

    “Nimekuelewa mama yangu, nimekuelewa sina budi kukusikiliza.”

    “Asante Masalu, siku zote niliamini wewe na Monika ndiyo watoto wangu wanaonijali, endelea kunijali mwanangu wewe ndiye tegemeo langu, soma unikomboe.”

    “Nitafanya hivyo mama yangu, nakuahidi kuwa kimbilio lako.”

    “Asante mwanangu.”

    Baada ya mazungumzo marefu tulirudi nyumbani, lakini  bado aliniacha na maswali lukuki moyoni mwangu, nilijikuta nakubaliana na shemeji, bwana wa Monika kuwa mwili wa dada umefichwa ndani pamoja na mtoto wa dada Mihayo.

                                                    SIKU TATU BAADAYE

    Siku tatu baadaye nilipata taarifa za kusikitisha za kifo cha utata cha shemeji aliyekuwa bwana wa Monika. Taarifa zilizonitisha na kuamini mazungumzo yangu na mama juu ya taarifa zinazosambazwa na shemeji zilimfikia baba na kuamua kufanya umaruhuni wake.

    Ndugu walisema aliporudi nyumbani alianza kusema anasumbuliwa na kichwa huku akisema kama akifa atakuwa ni baba. Na usiku alipiga kelele akilitaja jina la baba, kitu kilichozidi kuaminisha kwamba anahusika moja kwa moja ili kumkomoa baada ya kusikia akitutangazia sifa mbaya familia yetu.

    Kifo kile kiliongeza sifa mbaya kufikia hatua familia ya aliyekuwa mpenzi wa marehemu dada Monika kuja kutushambulia kwa maneno ya kutuita wachawi. Siku hiyo nilikuwepo, mama wa marehemu alikuja nyumbani na kuanza kutoa shutuma nzito kwa sauti ya juu huku watu wakisikiliza.”

    “Mmeniulia mwanangu kwa imani zenu za kichawi ili muwe matajiri, kumuua mtoto wa Mihayo hamkuridhika mmemuua Monika na kumficha ndani bado tu mmeona haitoshi mmemuua mwanangu. Nawaambia damu ya mwanangu haiendi bure.”

    Taarifa zile zilipelekwa kwa baba ambaye aliita polisi na kumchukua yule mama na kumpeleka kituoni. Kwa kweli kilichoendelea sikujua zaidi ya kumsikia baba akitamba atamuonesha. Pamoja na yule mama kupelekwa polisi familia yetu ilitawaliwa na sifa mbaya ambazo wengi walizisikia na kuzisambaza kwa watu kuwa maisha yetu yametawaliwa na utajiri wa kishirikina ambao ulikuwa ukipitia kwenye kidonda cha marehemu dada. CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nilijikuta nikiishi maisha ya kukosa amani, hata tembea yangu ilikuwa ya mashaka kwa kuhofia maneno ya watu. Siku zilikatika walisema mchana, usiku wakalala. Walizungumza sana mwisho wakanyamaza na kusahaulika na maisha yakaendelea.

    Katika maisha yetu hakuna kilichobadilika, nilimaliza kidato cha nne kwa kupata matokeo mabaya. Niliamini kufanya vibaya kulitokana na migongano ya mawazo iliyotokana na kuchanganywa na mambo yote yaliyotokea yakihusu familia yetu, na taarifa nilizopewa na dada Monika juu ya kifo chake na matukio mengi ya kishirikina yaliyoilenga familia yetu.

    Wazo la kurudia mtihani wa kidato cha nne, lilipingwa na baba na kusema atanipatia shughuli nyingine. Roho iliniuma kwani ndoto zangu zilikuwa kusoma kwa bidii ili siku moja nimkomboe mama kwenye mateso ya kuwekwa kifungoni na baba.

    Miezi sita baada ya matokeo mabaya ya kidato cha nne, baba alionesha mapenzi makubwa kwangu tofauti na zamani. Alifikia hatua ya kuzunguka nami kila kona kwenye shughuli zake. Siku nyingine alinipa pesa za matumizi ambazo alinieleza ninunue kitu chochote nikitakacho.

    Kwa akili za kitoto nilianza kubadilika na kuyaona yote niliyoelezwa juu ya ukatili wa baba ni uongo. Baba alikuwa mtu mzuri kwa kuninunulia nguo za thamani, nilionekana kweli mtoto wa mtu mwenye pesa tofauti na  mwanzo nilivyokuwa nasoma shule.

    Baba siku zote alinisifia kuwa mimi ndiye mtoto anipendaye kuliko wote, kauli zile za baba zilinifanya nisahau hata wazo la kumuuliza juu ya dada Monika. Siku moja tulikuwa tumekaa kwenye moja ya hoteli ya baba huku akiniruhusu kula nikitakacho, baada ya chakula baba alinichukua na kuingia naye kwenye ofisi yake iliyokuwa ndani ya hoteli ile ambayo sikuwahi kuingia siku za nyuma.

    Baada ya kuingia ofisini baba aliendelea kunimwagia sifa.

    “Masalu unajua nakupenda sana kuliko watoto wangu wote.”

    “Najua baba.”

    “Hebu niambie unataka nini nikufanyie ili ujue napenda sana.”

    “Cha kwanza kunipa nafasi ya kurudia masomo niliyoanguka katika mtihani wangu ili nifanye vizuri, bado nina hamu ya kuendelea kusoma.”

    “Tofauti na hilo?”

    “Siwezi kusema kwa sasa mpaka nitakapofanya mtihani wangu wa marudio.”

    “Masalu, kusoma si muhimu sana kwako, kama pesa zipo nitakufungulia mradi wako ili uendeleze maisha yako.”

    “Lakini...”

    “Masalu hakuna haja ya kubishana, naomba ujiandae kuna duka moja nimelifungua na kuanza kazi wewe ndiye msimamizi mkubwa.“

    Nilijikuta nakosa cha kuzungumza na kukubaliana na baba japo nafsi yangu ilitaka kusoma ili nimkomboe mama yangu. Nilijua kukubali mradi ule japo utakuwa chini yangu bado utakuwa wa nguvu za kishirikina kwa kuhofia huenda siku za mbele baada ya kuoa na kupata mtoto akatolewa kafara.

    Baba alinitolea hati za kumiliki duka lile lenye jina langu na kunionesha sehemu ya kusaini. Nilisaini na kuniahidi kunifanyia mambo makubwa kuliko ndugu zangu wote. Baada ya kutoka pale aliniingiza kwenye gari lake na kunipeleka mjini Barabara ya Pamba kwenye duka langu.

    Nililikuta duka lipo wazi na watu wakiendelea na mauzo ya vitu, lilikuwa duka kubwa la kuuza vitu vya jumla na rejareja. Tulipofika dada mmoja ambaye alikuwa akinifahamu aliniuliza:

    “Leo Masalu ndiyo umeamua kuja?”

    “Alikuwa anamalizia masomo,” baba alijibu.

    “Karibu bosi.”

    “Asante.”

    Nilijibu huku nikiingia dukani na kwenda kukaa kwenye kiti changu kilichoandaliwa kwa ajili ya kukalia niwapo kazini. Baada ya kukagua duka lililokuwa likilingana na maduka ya  ndugu zangu, baba aliondoka na kuniacha nisimamie duka langu.

    Alinipitia jioni na kunirudisha nyumbani, nilipofika nyumbani nilimueleza mama kuwa nimepewa duka na baba. Ajabu mama badala ya kufurahi alitokwa na machozi, kwa vile tulikuwa peke yetu nilimuuliza:

    “Mama unalilia nini?”

    “Mmh, najua hukufurahi na unaweza usifurahi.”

    “Kwa nini mama?”

    “Ni vigumu kunielewa kwa sasa lakini tumuombe Mungu aepushe mbali.”

    “Mama mbona sikuelewi?”

    “Suala la shule limeishia wapi?”

    “Baba amekataa na kusema tayari ameishanifungulia duka, na leo ndiyo nimekabidhiwa rasmi.”

    “Mmh! Haya”

    “Kwani  kuna nini?”

    “Hakuna ubaya.”

    “Mama kuna kitu hutaki kuniambia.”

    “Hakuna kitu kikubwa zaidi ya kukatika kwa ndoto yako ya kusoma.”

    “Mama nitasoma tu.”

    “Kwa duka lako, si unawaona ndugu zako walivyo bize na maduka yao hata muda wa kunikumbuka hawana.”

    “Mama nitajipanga, siku hizi kuna masomo ya jioni.”

    Siku zilikatika, biashara nayo ilizidi kushika kasi, hata mwili wangu ulibadilika na kuonekana mtu mzima kutokana na kunenepa, hata sauti yangu ilibadilika. Lakini ilikuwa tofauti na wenzangu, mimi nilibakia nyumbani na mama pamoja na mfanyakazi mmoja, niliamua kumpumzisha mama kazi za shamba, lakini mama aling’ang’ania kwa kusema kama akiacha kwenda shamba atafukuzwa na baba.

    Nilipomuuliza baba naye alinijia juu na kunionya nisiingilie mambo yake, sikuwa na jinsi, nilimuacha mama aendelee kulima huku nikitumia vijana kumsaidia mama, ambaye alifanya kazi ndogondogo. Kingine ambacho sikukubaliana na baba ni kuhusu mavazi ya mama yaliyokuwa yamechoka.

    Hapo sikukubali hata kidogo na nilikuwa tayari kwa lolote.

    “Masalu unataka tubishane?” baba alinikaripia.

    “Kwa hili baba sikubaliani nawe hata kidogo.”

    “Umeanza kuvimba kichwa kwa vipesa unavyopata?”

    “Si kuvimba kichwa, nipo sahihi, kama mali zako chukua lakini nimechoka kuiona hali hii mpaka lini?”

    Sikuogopa chochote cha baba mpaka tulipokubaliana kumnunulia mama nguo mpya, pamoja na mzozano huo bado baba hakuonekana kukasirika sana. Mama alibadilika  na  kuanza kuvaa vitenge vya gharama, hata kandambili alivaa mpya.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ndugu zangu walipokuja nyumbani hawakuamini kumkuta mama yetu kapendeza. Walipomuuliza aliwaeleza ni kwa ajili yangu, walinifuata kutaka kujua nimewezaje kumbadili baba kukubali mama kuvaa nguo mpya. Niliwaeleza ni msimamo hakuna kitu kingine, maisha yaliendelea.

    Katika vitu ambavyo baba alinionya ni kutembea na wanawake, nilikumbuka kauli za dada Monika kuwa alianza kuelezwa asijihusishe na wanaume na mwisho alipata kidonda cha kichawi.

    Nilimkubalia kumridhisha tu, lakini niliendelea kuwa na uhusiano na binti mmoja ambaye ndiye tuliyepanga kuoana siku za mbeleni. Siku zote mambo yangu nilikuwa nayafanya kwa siri kubwa bila baba kujua kwa kuamini sina uhusiano wa kimapenzi na mwanamke.                                                     

                                                                               ****

    Siku moja nikiwa nimelala niliota kitu kama nyoka, lakini sikukielewa vizuri kikiniuma kwenye mguu wa kulia kwa ndani. Nilishtuka lakini hakukuwa na kitu chochote, niliendelea kulala. Kesho yake nilikwenda dukani kama kawaida na kuendelea na shughuli zangu.

    Wiki moja baadaye nilianza kusikia muwasho sehemu niliyoota nimeumwa na kitu kama nyoka. Nilimueleza mama asubuhi baada ya kujikuna mpaka kukaleta weusi sehemu iliyokuwa ikiniwasha. Mama alishtuka, jambo lililonitisha.

    ”Mama mbona umeshtuka?”

    “Baba yako alikueleza nini?”

    “Kuhusu nini?”

    “Huo muwasho wako?”

    “Hata, sijazungumza lolote.”

    “ Mmh!” Mama aliguna.

    “Unaguna nini?” nilimuuliza.

    “Hapana.”

    “Mbona kama unanitisha, unakuwa hauna tofauti na wa dada Monika?”

    “Ni kweli.”

    “Unataka kuniambia ndiyo huu?”

    “Ndiyo.”

    “Mungu wangu nimekwisha.”

    “Wala hujaisha, ukifuata masharti yake hauna tatizo.”

    “Kwa hiyo na mimi nitakuwa na kidonda kama dada Monika?”

    “Ndiyo lakini hakiumi.”

    “Na nikikosea nitakufa kama dada Monika?”

    “Monika kafa na yake.”

    “Mamaa, juzi tulizungumza nini, leo unanibadilikia?” Nilimuona mama akitaka kuficha mambo.

    “Masalu nakuomba suala hili muulize baba yako na usimueleze kuwa tumezungumza.”

    “Sawa mama.”

    Niliachana na mama huku mwili wote ukininyong’ea kwa kujua niliyoelezwa na dada Monika yametimia.

    Siku ile hata hamu ya kwenda kwenye duka langu sikuwa nayo, kwa kuamini nilikuwa nimeishaharibika. Nilishinda ndani huku nikilia lakini mama alitumia muda wake kunibembeleza kuwa sijaharibika kama ninavyo fikiria.

    “Masalu usilie mwanangu.”

    “Mama kwa nini mnanitendea unyama kama huu kosa langu nini?”

    “Huna kosa mwanangu, kidonda hiki humfuata yule aliyeteuliwa na mizimu.”

    “Wataniteua vipi wakati mimi sitaki?”

    “Huwezi kukataa.”

    “Mama nina malengo yangu wewe unajua.”

    “Ni kweli, lakini hakuna wa kumzuia baba yako uamuzi wake.”

    “Mama na mimi nitakufa kama dada Monika?”

    “Kwa nini?”

    ”Siwezi kufuata masharti ni magumu.”

    “Si magumu ukizingatia.”

    “Siwezi mama siwezi...,” nilikatwa kauli na sauti ya baba aliyekuwa akimwita mama. Nilimuona mama akishtuka na kuanza kutetemeka na kijasho chembamba kilimvuja.

    “Mama vipi?”

    “Naomba usimwambie baba yako niliyokueleza, ataniua.”

    “Siwezi kumwambia.”

    “Ng’wana Manoni.”

    “Lama,” mama aliitikia huku akitoka chumbani kwangu.

    “Vipi mbona unatoka chumbani kwa mtoto?”

    “Hajisikii vizuri.”CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Na shamba hujaenda?”

    “Baba Mihayo nimwache Masalu anaumwa niende shamba?”

    “Kwani anaumwa sana?”

    “Toka asubuhi analia tu.”

    “Kafanya nini?”

    “Mmh, nenda ndani ukamuone.”

    “Masalu,” baba aliniita.

    “Naam baba.”

    “Eti kuna nini?”



    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog